KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, January 4, 2013

TAIFA STARS KUJIPIMA UBAVU NA ETHIOPIA JAN 11

Timu ya Taifa (Taifa Stars) itacheza mechi ya kujipima nguvu dhidi ya Ethiopia. Mechi hiyo itachezwa Januari 11 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Addis Ababa, Ethiopia.

Stars chini ya Kocha Mkuu Kim Poulsen inatarajia kuingia kambini jijini Dar es Salaam keshokutwa (Januari 6 mwaka huu) kujiandaa kwa mechi hiyo.

 Mechi hiyo itakuwa kipimo cha mwisho kwa Ethiopia kabla ya kwenda Afrika Kusini kwenye fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) zitakazoanza Januari 19 mwaka huu.

Ethiopia iko kundi C pamoja na mabingwa watetezi Zambia, Nigeria na Burkina Faso. Ethiopia itacheza mechi yake ya kwanza Januari 21 mwaka huu dhidi ya Zambia.

Katika mechi yake ya mwisho, Taifa Stars iliifunga Zambia bao 1-0 katika mchezo wa kirafiki uliofanyika Desemba 22 mwaka jana Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mechi hiyo ya kirafiki dhidi ya Ethiopia ni sehemu ya maandalizi ya mechi ya mchujo dhidi ya Morocco kuwania tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia 2014. Mechi hiyo itachezwa Machi mwaka huu.

Wachezaji wanaotakiwa kambini ni Juma Kaseja kutoka Simba ambaye pia ndiye nahodha wa Stars, Aishi Manula na Mwadini Ally wote kutoka Azam.

Mabeki ni Aggrey Morris (Azam), Amir Maftah (Simba), Erasto Nyoni (Azam), Issa Rashid (Mtibwa Sugar), Kelvin Yondani (Yanga), Nadir Haroub (Yanga) na Shomari Kapombe (Simba).

Viungo ni Salum Abubakar (Azam), Athuman Idd (Yanga), Amri Kiemba (Simba), Khamis Mcha (Azam), Frank Domayo (Yanga), Mwinyi Kazimoto (Simba) na Shabani Nditi (Mtibwa Sugar).

Washambuliaji ni John Bocco (Azam), Mbwana Samata (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC), Mrisho Ngasa (Simba), Simon Msuva (Yanga), na Thomas Ulimwengu wa TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC).

Benchi la Ufundi linaundwa na  Kim, Sylvester Marsh (Kocha Msaidizi), Juma Pondamali (Kocha wa makipa), Leopold Tasso (Meneja), Dk. Mwanandi Mwankemwa (Daktari wa timu), Frank Mhonda (Mtaalamu wa tibamaungo) na Alfred Chimela (Mtunza vifaa).

UCHAGUZI KWA WANACHAMA WA TFF

Kamati ya Uchaguzi ya TFF inatarajia kukutana leo mchana (Januari 4 mwaka huu) ambapo pamoja na mambo mengine itapitia maendeleo ya uchaguzi kwa wanachama wa TFF ikiwemo Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board).

Wanachama wa TFF (vyama vya mikoa) wote wameshafanya uchaguzi ukiondoa mikoa ya Rukwa na Katavi inayotarajiwa kufanya uchaguzi baadaye mwezi huu.

Kwa upande wa vyama shiriki ambavyo bado havijafanya uchaguzi ni Makocha (TAFCA), Wachezaji (SPUTANZA), Waamuzi (FRAT) na Tiba ya Michezo (TASMA).

Vilevile Kamati ya Uchaguzi ya TFF baada ya kikao hicho huenda ikatangaza rasmi mchakato wa uchaguzi wa TFF unaotarajiwa kufanyika Februari 24 mwaka huu.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

No comments:

Post a Comment