KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, April 30, 2013

YANGA KUANZA KUSHEREHEKEA UBINGWA KESHO, KUKIPIGA NA COASTAL UNION DAR

Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inaendelea katika raundi yake ya 25 kesho (Mei Mosi) kwa mechi tano zitakazochezwa katika miji ya Dar es Salaam, Turiani, Morogoro na Mlandizi.

Licha ya kuwa tayari Yanga imetawazwa kuwa mabingwa wa VPL msimu huu (2012/2013), mechi dhidi ya Coastal Union itakayochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ni moja kati ya zitakazovuta macho na masikio ya washabiki wa mpira wa miguu nchini.

Mechi hiyo namba 172 itachezeshwa na mwamuzi Simon Mberwa kutoka Pwani akisaidiwa na Said Mnonga na Charles Chambea wote wa Mtwara wakati mwamuzi wa mezani atakiwa Hashim Abdallah wa Dar es Salaam. Kamishna wa mechi hiyo ni David Lugenge kutoka Iringa.

Viingilio katik mechi hiyo itakayoanza saa 10.15 jioni ni sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya bluu na kijani, sh. 8,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, sh. 15,000 kwa VIP C na B wakati VIP A itakuwa sh. 20,000. Tiketi zitauzwa uwanjani siku ya mchezo.

Mtibwa Sugar itakuwa mwenyeji wa African Lyon katika mechi namba 170 itakayochezeshwa na mwamuzi Dominic Nyamisana wa Dodoma kwenye Uwanja wa Manungu ulioko Turiani mkoani Morogoro. Nayo Kagera Sugar iliyo katika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi hiyo itakuwa mgeni wa Polisi Morogoro kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.

Uwanja wa Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam na wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 7,000 uko tayari kwa mechi kati ya JKT Ruvu na Tanzania Prisons. Nayo Ruvu Shooting itakuwa nyumbani kwenye uwanja wake Mabatini ulioko Mlandizi, Pwani kuikabili Oljoro JKT kutoka Arusha.

MTANZANIA APEWA ITC KUCHEZA MSUMBIJI



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limetoa Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) kwa mchezaji Yusuf Kunasa kucheza nchini Msumbiji.

Shirikisho la Mpira wa Miguu cha Msumbiji (FMF) lilituma maombi TFF kumuombea hati hiyo Kunasa anayekwenda kujiunga na timu ya Estrela Vermelha da Beira inayocheza Ligi Kuu nchini humo.

Kunasa ambaye msimu huu hakuwa na timu (free agent) amejiunga na timu hiyo akiwa mchezaji wa ridhaa (amateur). Zaidi ya wachezaji kumi kutoka Tanzania hivi sasa wanacheza katika klabu mbalimbali nchini Msumbiji.

SIMBA, POLISI ZAINGIZA MIL 18/-

Mechi namba 163 ya Ligi Kuu ya Vodacom iliyochezwa juzi (Aprili 28 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kumalizika kwa Simba kuibuka ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Polisi Morogoro imeingiza sh. 18,014,000.

Watazamaji 3,145 walikata tiketi kushuhudia mechi hiyo ambayo viingilio vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 3,564,252.45 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 2,747,898.31.

Kiingilio cha sh. 5,000 ndicho kilichovutia watazamaji wengi ambapo waliokata tiketi hizo walikuwa 2,841 na kuingiza sh. 14,205,000 wakati idadi ndogo ya washabiki ilikuwa ya kiingilio cha sh. 20,000 kilichovutia washabiki 36 na kuingiza sh. 720,000.

Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 1,812,331.75, tiketi sh. 3,183,890, gharama za mechi sh. 1,087,399.05, Kamati ya Ligi sh. 1,087,399.05, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 543,699.53 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 422,877.41.

Monday, April 29, 2013

HAYA NDO MAMBO YA EXTRA BONGO NDANI YA MAEDA


Mkurugenzi wa Extra bongo Ally Choki akiimba mbele ya mashabiki wake (hawapo pichani) ndani ya ukumbi wa Meeda, Sinza, Dar es Salaam jana usiku wakati bendi yake ilipokuwa ikiburudisha pande hizo
Kushoto ni mwimbaji mahiri wa bendi ya Extra Bongo, Athanas akiwa na mwimbaji pekee wa kike wa bendi hiyo, Khadija Mnoga a.k.a 'Kimobitel', ambaye anatamba kwa sasa na wimbo wake wa 'Mgeni' wakishoo luv mbele ya kamera yetu ndani ya ukumbi wa Meeda ,Sinza, Dar es Salaam jana usiku.
Kushoto ni mmoja wa marapa bora wa muziki wa dansi nchini, Totoo Ze Bingwa akirap ndani ya Meeda Sinza, Dar es Salaam wakati bendi anayopigia mzigo, Extra Bongo ilipokuwa ikitumbuiza pande hizo. Kulia ni Banza Stone a.k.a Generale akimpa big up.
Maua ya Extra Bongo mzigoni
Wakata nyonga maarufu kwa sasa wa Extra Bongo wakiongozwa na Super Nyamwela wakiwapagawisha mashabiki waliohudhuria shoo hiyo ndani ya Meeda  jana usiku
Waimbji bora wa Extra bongo kulia ni Rogert Hega a.k.a Katapila wakiimba ndani ya Meeda Sinza jana usiku
Rapa bora wa Extra bongo Kabatano (Kulia) akigani moja ya jimbo zao bora huku akipewa sapoti na nguli wa muziki wa dansi Banza Stone mwana masanja wakati bendi hiyo ilipokuwa ikitumbuiza maeneo ya Sinza katika ukumbi wa Meeda jana usiku.

MNYAMA AUA POLISI



SIMBA jana ilijiweka kwenye nafazi nzuri ya kushika nafasi ya tatu katika msimamo wa ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kuichapa Polisi Morogoro mabao 2-1 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Ushindi huo ulikuwa wa kulipiza kisasi kwa Simba kufuatia kufungwa idadi hiyo ya mabao na Polisi katika mechi ya mzunguko wa kwanza iliyochezwa mjini Morogoro.

Kutokana na ushindi huo, Simba sasa imefikisha pointi 39 kutokana na mechi 23 ilizocheza, ikiwa bado nafasi ya nne wakati Kagera Sugar niya tatu ikiwa na pointi 40.

Polisi ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 10 lililofungwa na Bantu Admini kwa shuti kali baada ya beki Miraji Juma na kipa Juma Kaseja wa Simba kuchanganyana.

Dakika tano baadaye, Haruna Chanongo aligongeana vizuri na Ramadhani Singano 'Messi', lakini shuti la Messi lilitoka nje sentimita chache.

Chanongo, ambaye alikuwa mwiba kwa mabeki wa Polisi, aliwainua vitini mashabiki wa Simba dakika ya 33 baada ya kuifungia bao la kusawazisha. Alifunga bao hilo baada ya kupokea pasi kutoka kwa Amri Kiemba. Timu hizo zilikwenda mapumziko zikiwa sare ya bao 1-1.

Mrisho Ngasa aliiongezea Simba bao la pili dakika ya 47 kwa shuti lililogonga mwamba wa juu wa goli na mpira kutinga wavuni.

Saturday, April 27, 2013

HANSPOPE AREJEA SIMBA


MWENYEKITI wa Simba, Ismail Aden Rage, amemshukuru aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya klabu, Zacharia Hans Poppe, kwa kukubali kurejea kushikilia nyadhifa zake zote.


Poppe alitangaza kujiuzulu nyadhifa zake za uongozi ndani ya Simba Machi 7 mwaka huu, kutokana na hali ya migogoro iliyokuwapo wakati huo.

Hata hivyo, Rage alikataa kujiuzulu huko kwa Poppe na akasema atamshawishi abadili maamuzi kwa manufaa ya Simba.

“Napenda kutumia nafasi hii kuwaarifu wana Simba popote walipo kwamba Poppe amerejea na yuko tayari kuitumikia Simba kama Mjumbe wa Kamati ya Utendaji na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba,” alisema Rage.

Kwa upande wake, Poppe alisema amerejea Simba kutokana na utulivu ulioanza kujitokeza klabuni na kwamba nia yake ni kuhakikisha klabu inafanya usajili mzuri na wa kiwango kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu.

SIMBA YAIPA SOMO TFF


UONGOZI wa Simba umekubaliana na hatua ya serikali kuzuia kuchezwa kwa mchezo uliopangwa kuchezwa leo wa Ligi Kuu ya Tanzania baina ya Wekundu wa Msimbazi na Ruvu Shooting Stars.

Hata hivyo, uongozi wa Simba haujafurahishwa na namna uzuiaji huo ulivyofanyika. Taarifa imetolewa leo kwenye siku ya mechi yenyewe wakati maandalizi yote yakiwa yamefanyika na hivyo kusababisha matatizo katika sehemu kubwa tatu.

Mosi, uongozi wa Simba umeingia gharama kubwa ya kuweka timu kambini na kujiandaa na mechi. Pili, benchi la ufundi na wachezaji walikuwa tayari wamejiandaa na mechi kimwili na kiakili na kuahirishwa huku kwa mechi kumesaidia tu kuvuruga programu. Tatu, wapenzi na washabiki wa Simba wamepata usumbufu wa kwenda uwanjani na kukuta hakuna mechi.

Uongozi wa Simba unapenda kutumia nafasi hii, katika namna ya kipekee kabisa, kuwaomba radhi wapenzi na wanachama wake ambao walifika Uwanja wa Taifa kutazama mechi ambayo haikuwapo.

Washabiki ndiyo wanaoifanya Simba na mchezo wa mpira wa miguu nchini uwe na umaarufu ulionao na bila wao ligi yetu inaweza kupoteza nguvu na ushindani ilionao.

Simba SC inapenda kuwe na utaratibu unaojulikana wa kuahirisha mechi wa walau saa 48 kabla ya siku ya mechi. Hii itasaidia pande zote zinazohusika. Kama mechi imeshindikana kwa sababu za nje ya uwezo wa kibinadamau (Force de Majeure) kama vile mafuriko, tetemeko la ardhi na vimbunga, mechi inaweza kuahirishwa ghafla lakini si kwa mechi ambayo uwepo wake ulifahamika miezi kadhaa nyuma.

Tunashauri pia kwamba siku za mechi ambapo Ligi Kuu inachezwa (match days), inatakiwa kuwa zinafahamika na isiwe kila siku mechi zinachezwa. Simba ilikuwa na mechi wikiendi iliyopita na Ruvu ilikuwa na mechi Mbeya zaidi ya wiki moja iliyopita na hivyo mechi hii ingeweza kuchezwa hata jana (Jumatano) ambayo ni siku ya kawaida kwa mechi kuchezwa badala ya leo Alhamisi.

Ni matumaini yetu kwamba kuahirishwa kwa mechi hii kutakuwa fundisho kubwa katika upangaji wa ratiba na uahirishaji wa mechi ambao una faida kwa pande zote husika.

YANGA BINGWA 2013/2014

HATIMAYE Yanga jana ilitawazwa kuwa mabingwa wapya wa ligi kuu ya Tanzania Bara msimu wa 2012-2013 baada ya Azam kulazimishwa sare ya bao 1-1 na Coastal Union katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

Sare hiyo imeifanya Azam, iliyokuwa ikipambana na Yanga kuwania ubingwa, isiwe na uwezo wa kufikisha pointi 56, ambazo tayari Wana-Jangwani wameshaziweka kibindoni. Iwapo Azam itashinda mechi zake zilizosalia, itakuwa na uwezo wa kufikisha pointi 54.

Mshambuliaji Danny Lyanga ndiye aliyezima matumaini ya Azam kutwaa taji hilo baada ya kuifungia Coastal Union bao la kusawazisha dakika ya 72. Danny alifunga bao hilo dakika chache baada ya kuingia uwanjani kuchukua nafasi ya Suleiman Kassim Selembe.

Azam ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 60 lililofungwa kwa njia ya penalti na beki Aggrey Morris baada ya Gaudence Mwaikimba kuangushwa ndani ya eneo la hatari na beki Yussuf Chuma wa Coastal Union.

MABINGWA WA JUMLA LIGI KUU:
1965 : Sunderland (Dar es Salaam)
1966 : Sunderland (Dar es Salaam)
1967 : Cosmopolitans (Dar es Salaam)
1968 : Yanga
1969 : Yanga
1970 : Yanga
1971 : Yanga
1972 : Yanga
1973 : Simba
1974 : Yanga
1975 : Mseto SC (Morogoro)
1976 : Simba
1977 : Simba
1978 : Simba
1979 : Simba
1980 : Simba
1981 : Yanga
1982 : Pan African
1983 : Yanga
1984 : Simba
1985 : Yanga
1986 : Tukuyu Stars (Mbeya)
1987 : Yanga
1988 : Coastal Union (Dar es Salaam)
1989 : Yanga
1990 : Simba
1991 : Yanga
1992 : Yanga
1993 : Yanga
1994 : Simba
1995 : Simba
1996 : Yanga
1997 : Yanga
1998 : Yanga
1999 : Mtibwa Sugar (Morogoro)
2000 : Mtibwa Sugar (Morogoro)
2001 : Simba
2002 : Yanga
2003 : Simba
2004 : Simba
2005 : Yanga
2006 : Yanga
2007 : Simba (Ligi Ndogo)
2008 : Yanga
2009: Yanga
2010: Simba SC
2011: Yanga SC
2012: Simba SC
2013: Yanga SC

Thursday, April 25, 2013

SIMBA, RUVU SHOOTING SASA KUCHEZA MEI 5




Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya Ruvu Shooting na Simba iliyokuwa ichezwe leo (Aprili 25 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam sasa itafanyika Mei 5 mwaka huu kwenye uwanja huo huo.

Mabadiliko hayo yametokana na Serikali kuutumia uwanja kwa ajili ya maandalizi ya sherehe za Muungano ambazo kitaifa zitafanyika kesho (Aprili 26 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linawaomba radhi washabiki kwa usumbufu uliojitokeza kutokana na mabadiliko hayo na ghafla. Ratiba ya mechi nyingine za VPL zinabaki kama zilivyo.

Ligi hiyo inaendelea kesho (Aprili 26 mwaka huu) kwa mechi kati ya Coastal Union na Azam itakayochezwa Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga wakati Jumapili (Aprili 28 mwaka huu) itakuwa katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ni Simba dhidi ya Polisi Morogoro.

SIMBA, RUVU SHOOTING KAZI IPO LEO


TIMU kongwe ya soka ya Simba inatarajiwa kushuka dimbani leo kumenyana na Ruvu Shooting katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Pambano hilo lina umuhimu mkubwa kwa Simba kwa vile iwapo itashinda, itajiweka katika nafasi nzuri ya kumaliza ligi ikiwa nafasi ya tatu.

Simba inashika nafasi ya tatu katika msimamo wa ligi hiyo, ikiwa na pointi 36 baada ya kucheza mechi 22, sawa na Mtibwa Sugar, lakini zinatofautiana kwa mabao ya kufunga na kufungwa.

Yanga yenye matumaini makubwa ya kutwaa ubingwa wa ligi hiyo, bado inaongoza ikiwa na pointi 56 baada ya kucheza mechi 24, ikifuatiwa na Azam yenye pointi 47 na Kagera Sugar yenye pointi 40.

Kaimu Makamu Mwenyekiti wa Simba, Joseph Itangale, maarufu kwa jina la Kinesi, alisema jana kuwa, timu hiyo imeshaingia kambini kwa ajili ya kujiandaa kwa pambano hilo.

Kinesi alisema lengo kubwa walilonalo ni kushinda mechi zote nne zilizosalia ili waweze kumaliza ligi wakiwa kwenye nafasi ya tatu.

Baada ya mechi ya leo, Simba inatarajiwa kushuka tena dimbani Aprili 28 kumenyana na Polisi Moro kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kabla ya kuvaana na Mgambo JKT Mei 8 mwaka huu kwenye uwanja huo.

Mabingwa hao wa mwaka jana wa ligi hiyo, watahitimisha mechi zao za ligi Mei 18 mwaka huu kwa kumenyana na watani wao wa jadi, Yanga.

Kwa mujibu wa Kinesi, katika mechi zote hizo, Simba itaendelea kuwatumia wachezaji wake wa kikosi cha pili, ambao wameonyesha kiwango cha juu.

TAIFA STARS YAALIKWA KOMBE LA COSAFA



Timu ya soka ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) imealikwa kushiriki katika michuano ya Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Kusini mwa Afrika (COSAFA) itakayofanyika Julai mwaka huu nchini Zambia.

Taifa Stars itashiriki katika michuano hiyo ya nchi wanachama wa COSAFA ikiwa timu mwalikwa. Nchi wanachama wa COSAFA ni Afrika Kusini, Angola, Botswana, Comoro, Lesotho, Madagascar, Malawi, Mauritius, Msumbiji, Namibia, Shelisheli, Swaziland, Zambia na Zimbabwe.

Michuano hiyo itafanyika kuanzia Julai 6 hadi 21 mwaka huu katika miji ya Lusaka, Ndola na Kabwe. Ratiba ya makundi ya michuano hiyo itapangwa Mei 3 mwaka huu jijini Lusaka.

Mara ya mwisho michuano hiyo ilifanyika miaka mitatu iliyopita. Hii itakuwa mara ya pili kwa Tanzania kushiriki michuano hiyo baada ya kucheza ya kwanza iliyofanyika mwaka 1996 nchini Zimbabwe.

Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager, inatarajia kuingia kambini mwishoni mwa mwezi ujao kujiandaa kwa mechi ya Kombe la Dunia dhidi ya Morocco itakayochezwa Juni 8 mwaka huu jijini Marrakech.

Juni 16 mwaka huu, Taifa Stars itacheza na Ivory Coast jijini Dar es Salaam katika mechi nyingine ya mchujo ya Kombe la Dunia wakati Juni mwishoni na Julai mwanzoni itacheza mechi ya Kombe la Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) dhidi ya Uganda.

Wakati huo huo, waandishi wa habari wanaotaka kuripoti michuano hiyo wanatakiwa kuwasilisha majina yao TFF kabla ya Aprili 27 mwaka huu ili maombi yao yatumwe COSAFA kwa ajili ya kupatiwa vitambulisho (Accreditation).

RAGE ATUNISHA MISULI, APELEKA SUALA LA OKWI FIFA



MWENYEKITI wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage ameendelea kusisitiza msimamo wake wa kutojiuzulu uongozi wa klabu hiyo kwa tuhuma za kutafuna fedha za mauzo ya mshambuliaji Emmanuel Okwi.

Rage, ambaye ni mbunge wa Tabora Mjini (CCM) amesema, ataendelea kubaki madarakani hadi kipindi chake cha uongozi cha miaka minne kitakapomalizika mwakani.

Mwenyekiti huyo wa Simba alitoa kauli hiyo jana wakati wa kipindi cha Jambo Tanzania kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha TBC 1.

Alisema watu wanaomtaka ajiuzulu, hawana uwezo wa kumng'oa kwa sababu alichaguliwa kuiongoza klabu hiyo kikatiba.

"Hawa wamedandia hoja kama vile UDA. Mimi niko Simba kwa mujibu wa katiba, hivyo siwezi kujiuzulu kwa sababu sioni kosa langu. Kama ni fedha za mchezaji (Emmanuel Okwi) hazijalipwa," alisema Rage.

Alisisitiza kuwa, Simba imemuuza Okwi kwa dola 300,000 (sh. milioni 480) kwenda klabu ya Etoile du Sahel ya Tunisia, lakini fedha hizo bado hazijatua mikononi mwa uongozi.

Mwenyekiti huyo alisema Simba ilimuuza nyota huyo wa zamani wa SC Villa ya Uganda kwa nia njema ya kupata fedha na pia kumfanya mchezaji huyo anufaike kutokana na kazi yake.

"Fedha za Okwi hazijafika, kama zingefika, watu wote wangejua kupitia mfumo wa Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), ambao mchezaji anapouzwa, mauzo yake yanaonekana, lakini kwetu bado inasomeka sifiri," alisema Rage.

Aliongeza kuwa, kwa sasa, suala la mauzo ya Okwi liko chini ya uangalizi wa Mario Demento wa FIFA, ambaye anashughulia fedha hizo ili klabu ya Simba izipate haraka iwezekanavyo.

YANGA WAMUOMBA JK KUICHANGIA


KLABU ya Yanga inatarajia kuandaa hafla ya kuchangisha michango kwa ajili ya ujenzi wa uwanja wake mpya wa kisasa maeneo ya mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam.

Habari kutoka ndani ya klabu hiyo zimeeleza kuwa, mgeni rasmi katika hafla hiyo anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano Jakaya Kikwete.

Kwa mujibu wa habari hizo, uamuzi wa kuandaa hafla hiyo ulifikiwa katika kikao cha kamati ya utendaji ya klabu hiyo kilichofanyika hivi karibuni mjini Dar es Salaam.

"Kamati ya utendaji iliyokutana hivi karibuni ilikubaliana kuandaa hafla kubwa ya kuchangisha mamilioni ya pesa kwa ajili ya ujenzi wa uwanja huo,"alisema mmoja wa viongozi wa kamati hiyo, ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini.

Mbali ya kuandaa hafla hiyo, kamati hiyo imeshapendekeza ramani ya uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 40,000, ambao ujenzi wake unatarajiwa kugharimu dola milioni 50 za Marekani

Chanzo hicho cha habari kilieleza kuwa, uwanja huo ndio chaguo la kwanza katika ramani zilizochorwa na kuwasilishwa kwa uongozi wa Yanga na Kampuni ya Beijing Construction Engineering tawi la Tanzania.

Kiliongeza kuwa, chaguo la pili ni uwanja ambao ujenzi wake utagharimu dola milioni 40 na wa tatu ujenzi wake utagharimu dola milioni 30.

Alipoulizwa kuhusu taarifa hizo, Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako alisema, anachojua ni kwamba mchakato wa ujenzi wa uwanja huo bado unaendelea.

"Mambo yatakakapokamilika, uongozi utaweka wazi kila kitu kwani muda si mrefu, ndoto ya klabu yetu kumiliki uwanja wa kisasa itakamilika,"alisema.

Mwezi uliopita, Kampuni ya Beijing Construction Engineering tawi la Tanzania, kupitia Meneja Msaidizi wake, Zhang Chengwei alisema, ujenzi wa uwanja huo utaanza mara baada ya uongozi wa Yanga kupata fedha.

Chengwei alisema uwanja huo utakuwa na sehemu ya maduka, hoteli, migahawa, 'super market', sehemu ya maegesho ya magari na uwanja mdogo wa mazoezi.

Alisema iwapo Yanga itakuwa na fedha za kutosha, watajenga uwanja huo kwa kipindi cha mwaka mmoja na utafanana na uwanja uliojengwa na kampuni hiyo nchini Afrika Kusini.

Kampuni hiyo ndiyo iliyojenga Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Uwanja wa Uhuru, jengo la maonyesho la Chuo Kikuu cha Elimu (DUCE), uwanja wa ndege wa Zanzibar, jengo la mapumziko la wageni mashuhuri katika uwanja wa Mwalimu Julius Nyerere na ofisi za Mamlaka ya Usafiri wa Anga (TCAA).

YANGA: UBINGWA HAUNA RAHA BILA KUMUUA MNYAMA




MAKAMU Mwenyekiti wa Klabu ya Yanga, Clement Sanga amesema japokuwa timu yake inayo nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa wa ligi kuu ya Tanzania Bara msimu huu, hautakuwa na raha bila kuwafunga watani wao wa jadi Simba.

Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Sanga alisema watakuwa na raha ya kuwa mabingwa wa Bara iwapo wataifunga Simba katika mechi yao ya mwisho.

Simba na Yanga zinatarajiwa kushuka dimbani Mei 18 mwaka huu katika moja ya mechi saba za mwisho za ligi hiyo itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Katika mechi ya kwanza iliyochezwa Oktoba 3 mwaka jana kwenye uwanja huo, timu hizo zilishindwa kutambiana baada ya kutoka sare ya bao 1-1.

Yanga huenda ikatawazwa kuwa mabingwa wapya wa ligi iwapo itaishinda Coastal Union katika mechi itakayopigwa Mei Mosi mwaka huu.

Yanga inaongoza ligi hiyo kwa kuwa na pointi 56 baada ya kucheza mechi 24, ikifuatiwa na Azam yenye pointi 47 na Kagera Sugar yenye pointi 40.

Iwapo Yanga itatoka sare ama kuishinda Coastal, itatwaa ubingwa kabla ya ligi kumalizika na pambano lake dhidi ya Simba litakuwa la kukamilisha ratiba.

"Ni kweli nafasi ya Yanga kutwaa ubingwa ni kubwa kwa vile tunahitaji pointi moja tu katika mechi yetu na Coastal Union. Ni kama vile tumeshatwaa ubingwa,"alisema Sanga.

"Lakini sintakuwana na raha hadi pale tutakapotoa kipigo kwa wapinzani wetu Simba. Lazima tuwafunge, tena kwa idadi kubwa ya mabao,"aliongeza.

Sanga alisema wamejipanga vyema kuhakikisha kuwa, wanashinda mechi zote mbili zilizosalia ili kuufanya ubingwa huo uwe na ladha iliyokamilika.

Kwa mujibu wa Sanga, wamepania kuishinda Simba kwa idadi kubwa ya mabao kwa lengo la kulipa kisasi cha kufungwa mabao 5-0 katika ligi ya msimu wa 2011/2012.

DEO MUNISHI 'DIDA': INAUMA SANA



UONGOZI wa timu ya soka ya Azam hivi karibuni uliamua kuwarejesha kikosini wachezaji wake wanne, akiwemo kipa Deo Munishi 'Dida', waliokuwa wakikabiliwa na tuhuma za kupokea rushwa kutoka kwa timu pinzani. Katika makala hii ya ana kwa ana iliyoandikwa na Mwandishi Wetu ATHANAS KAZIGE, kipa huyo anasimulia mkasa huo na masuala mengine kuhusu maisha yake kisoka.

SWALI: Ulijisikiaje wakati uongozi wa Azam ulipotangaza kukusimamisha wewe na wachezaji wenzako watatu kwa tuhuma za kupokea rushwa kutoka kwa timu pinzani baada ya timu yako kufungwa mabao 3-1 na Simba katika mechi ya ligi?

JIBU: Kwanza kabisa ninapenda kumshukuru Mungu baada ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kutusafisha kwa vile hali ilikuwa mbaya sana. Haya mambo omba yatokee kwa mtu mwingine, lakini yanapotokea kwako, utajuta.

Tuhuma hizo zilitunyima raha na kutufanya tukose amani. Kila tulipokuwa tukikatiza, tulionekana kama vile watu wa ajabu mbele ya jamii.

Binafsi tuhuma hizi zilinikera sana kwa sababu hazikuwa na ukweli wowote. Ndio sababu siku niliposikia TAKUKURU ikitoa taarifa ya kutusafisha, nilifurahi sana na kujiona kama vile nimekuwa mtu huru baada ya kutoka kifungoni.

SWALI: Ni kitu gani hasa kilichokuwa kikikufanya ukose raha?

JIBU: Kila nilipokuwa nikipita kwenye mkusanyiko wa watu wengi, baadhi yao walikuwa wakinong'onezana na wengine kunisema vibaya. Nilikuwa naonekana kama vile ni mhalifu.

Unajua inapofika hatua hata watoto wadogo wanajua nini kimetokea na kukushangaa wakati kitu chenyewe sio cha kweli, inauma sana. Nashukuru kwamba mambo haya yamemalizika salama na nimeamua kumshtakia Mungu.

Napenda kuweka wazi kwamba, kamwe sijawahi kupokea rushwa katika maisha yangu kutoka kwa kiongozi wa timu yoyote. Mimi ni muumini mzuri wa kanisa katoliki na kila Jumapili nasali kwenye kanisa la Chang'ombe.

SWALI: Familia yako, ndugu zako na rafiki zao alizipokeaje taarifa za wewe kusimamishwa Azam kwa tuhuma za kupokea rushwa?

JIBU: Familia yangu ilishangazwa sana na taarifa hizi kwa vile inanifahamu vyema. Baadhi ya ndugu zangu walinishauri niwaache viongozi wa Azam wajiridhishe wakiamini kwamba ipo siku ukweli utadhihirika na kweli hilo limefanyika.

SWALI: Je, umepanga kuchukua hatua zozote kwa uongozi wa Azam kutokana na kukupakazia tuhuma hizo?

JIBU: Kwa kweli sitarajii kufanya lolote kwa uongozi wa Azam kwa sababu umeshatangaza kuturejesha kwenye timu na tumeshaanza mazoezi na wenzetu. Waswahili wanasema, yaliyopita si ndwele, tugange yajayo. Kwangu hayo sasa yameshapita, najipanga upya kutafuta namba kwenye kikosi cha kwanza.

SWALI: Athari zipi nyingine ulizozipata kutokana na kusimamishwa na uongozi wa Azam?

JIBU: Athari zipo nyingi tu. Nyingine zilikuwa ni kutosajiliwa katika michuano ya Kombe la Shirikisho na hivyo kukosa pesa nyingi za posho za safari.

Michuano hii ilikuwa sehemu nzuri kwetu kuonyesha uwezo na vipaji vyetu na pengine kupata nafasi ya kucheza soka ya kulipwa nje. Nilijikuta nikigeuka kuwa mtazamaji wa Azam katika mechi za michuano hiyo badala ya mchezaji.

Ninachopenda kusisitiza ni kwamba, sina kinyongo na mtu yeyote, nimeamua kumuachia Mungu. Ninaendelea na kazi yangu ya kuichezea Azam bila ya kuwa na hofu yoyote. Nawaomba viongozi wa Azam waendelee kuniamini kwa vile kucheza soka ndio kazi yangu.

SWALI: Unauelezeaje ushindani wa namba kwenye kikosi cha Azam kwa sasa, hasa ya ukipa?

JIBU: Ninachoweza kusema ni kwamba, Azam imebahatika kuwa na makipa wazuri. Yupo Mwadini Ally na Aishi Manura, wote ni wazuri na wapo kwenye kiwango cha juu. Nitakachokifanya ni kupambana nao kuwania namba. Mwamuzi wa mwisho ni kocha Stewart Hall.

Lakini nitakuwa na kazi ngumu kwa sababu nimekuwa nje ya uwanja kwa muda mrefu. Nitalazimika kufanya mazoezi kwa bidii ili niwe fiti. Naamini mazoezi binafsi niliyokuwa nikiyafanya wakati tumesimamishwa, yatanisaidia kuwa fiti.

SWALI: Nini matarajio yako kwenye kikosi cha Taifa Stars?

JIBU: Hakuna kitu ambacho nimekuwa nikikipa kipaumbele kama kuichezea Taifa Stars. Nitafanya kila ninaloweza ili niitwe kwenye kikosi hicho.

SWALI: Umejifunza nini katika maisha yako ya soka hadi sasa?

JIBU: Nashukuru kwa swali lako zuri. Nimejifunza mambo mengi katika maisha yangu, lakini kubwa ni kwamba usimuamini kila mtu kwenye ulimwengu huu kwa vile unaweza kuzuliwa jambo, likakuangamiza ama kukuletea matatizo.

Kuanzia sasa nitakuwa makini sana na watu wangu wa karibu. Sitakuwa karibu na watu wenye tabia za majungu kwa sababu wanaweza kunizulia mambo mengine nikapata matatizo. Waliyonifanyia yanatosha. Nimepoteza vitu vingi sana.

Funzo lililonipata litaendelea kudumu ndani ya moyo wangu. Lakini daima nitabaki kuwa mtu mwenye nidhamu na upendo kwa wenzangu. Nataka kuishi maisha ya amani.

REDDS MISS TANZANIA AANZA KUSAKWA



Warembo wanaoshiriki katika shindano la kumtafuta  Redd's Miss Dar Indian Ocean wakiwa katika semina fupi Kutoka kwa kamati ya Miss TZ. Anayeendesha  semina hiyo ni Mkurugeni wa Kampuni ya Lino Agency International, Hashim Lundenga.


HATUA za awali za kumsaka Redd’s Miss Tanzania sasa zinaanza kushika kasi, wakati wiki hii kutakapokuwa na kinyang’anyiro katika vitongoji kadhaa vya kusaka warembo wao.

Kazi kubwa itaanza Morogoro, wakati atakaposakwa Redd’s Miss High Learning atakayeuwakilisha mkoa huo katika kumpata mrembo kutoka Vyuo vya Elimu ya Juu, shindano litakalofanyika kwenye Ukumbi wa Sirvoy.

Wakati Morogoro Miss High Learning akipatikana kesho, shughuli pevu ipo keshokutwa (Jumamosi) pale kutakapokuwa na shindano la kumsaka Redd’s Miss UDOM, litakalofanyika katika Ukumbi wa Kilimani, Dodoma.

Siku hiyo pia atapatikana mwakilishi wa vyuo vya elimu ya juu kutoka Kagera na Mwanza, shindano ambalo litafanyika Yacht Club, Mwanza.

Akizungumzia kuhusu Redd’s Miss Morogoro High Learning, mratibu wa shindano hilo, Verdian Kamugisha alisema kila kitu kimekamilika na kutakuwa na burudani za kufa mtu.

“Tumekamilisha kila kitu na warembo wote wako katika hali nzuri na kutakuwa na burudani za kumwaga, wakazi wa Morogo wanatakiwa kuja kwa wingi kushuhudia kile kitakachotukia,” alisema.

Mratibu wa Shindano la Redd’s Miss UDOM, Rachel Matina naye alisema kila kitu kwao kipo tayari na watu wanatakiwa kufika kwa wingi kushuhudia jinsi warembo kutoka Chuo Kikuu Dodoma, walivyopania kulitwaa taji la Redd’s Miss Tanzania mwaka huu.

Joseph Rwebangira wa anayeratibu shindano la wanafunzi wa Vyuo vya Elimu ya Juu kwa mikoa ya Kagera na Mwanza naye alikiri kukamilika kwa maandalizi yote na kutakuwa na burudani za kila aina siku ya onyesho.

Upande wa kanda ya kaskazini mwa nchi kutakuwa na shindano la kumsaka mrembo wa kitongoji cha Hai ambapo shindano hilo linatarajiwa kufanyikia katika ukumbi wa Hotel ya Snow View na mkoani Mara katika kitongoji cha Tarime shindano litakuwa katika ukumbi wa JJ Club na maandalizi kwa sehemu zote husika yameshakamilika kwa kiwango kikubwa.

Redd’s Miss Tanzania kwa sasa inadhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia kinywaji chake cha Redd’s Original.

JIM IYKE, NADIA BUHARI WATOKA KWA SIRI



LAGOS, Nigeria
HATIMAYE imebainika kuwa, mcheza filamu machachari wa Nigeria, Jim Iyke ana uhusiano wa kimapenzi na mwigizaji wa Ghana, Nadia Buari.

Chanzo cha habari kimedai kuwa, Jim na Nadia wamekuwa wakiufanya uhusiano wao huo kuwa siri ili kuepuka kuandamwa na vyombo vya habari.

Kwa mujibu wa chanzo hicho cha habari, Jim na Nadia wamekuwa wakikutana kwa siri na hivi karibuni walionekana wakiwa pamoja nchini Uganda.

Wacheza filamu hao pia walionekana pamoja wakati wa ndoa ya mwanamuziki 2 Face Idibia wa Nigeria iliyofanyika hivi karibuni mjini Dubai, Falme za Kiarabu.

Sehemu zingine, ambazo Jim na Nadia wamekuwa wakionekana pamoja ni Uingereza na Afrika Kusini.

"Jim Iyke amekuwa akiichukulia Ghana kama sehemu yake ya pili ya kuishi na amekuwa akisafiri mara kwa mara kwenda Accra kumuona Nadia,"kilisema chanzo cha habari.

Imeelezwa pia kuwa, safari za Nadia kwenda Lagos hazihesabiki na hivi karibuni alikwenda mapumziko nchini Marekani, ambako alionekana akiwa na Jim.

MONALISA AJUTA KUACHWA NA MUMEWE



LAGOS, Nigeria
MCHEZA filamu nyota wa Nigeria, Monalisa Chinda amesema moja ya mambo anayoyajutia katika maisha yake ni kuachika kwa mumewe.

Monalisa amesema yeye ni binti wa kwanza katika familia yao na anatoka kwenye familia ya kitajiri na haijawahi kutokea kwa mtoto wa kwanza kuachika.

"Lakini lilikuwa ni suala la maisha na kifo, vinginevyo, ningeweza kurejea kwa mume wangu na kuifanya ndoa yangu idumu. Nilijaribu kuifanya iwe hivyo, lakini haikuwezekana,"alisema.

Monalisa alisema hicho ndicho pekee anachokijutia katika maisha yake, kumtunza na kumkuza mwanaye bila kuwa na baba.

"Inauma sana. Lakini ninapaswa kuizoea hali hii,"alisema Monalisa.

Pamoja na kuachika, Monalisa alisema bado anaamini yapo mapenzi ya kweli na ndiyo yanayowafanya binadamu kuendelea kuwepo duniani.

Monalisa alisema angependa kuolewa kwa mara ya pili kwa vile hafurahii kuishi maisha ya upweke.

"Lakini kwa vile sina mtu kwa sasa, napaswa kuyazoea maisha haya,"alisema.

Monalisa alisema ni vigumu kwa sasa kusema ni lini anatarajia kufunga tena ndoa, lakini alisisitiza kuwa, anapendwa na anapenda kuwamo katika mapenzi.

HUYU NDIYE BINTI WA GENEVIEVE



LAGOS, Nigeria
KAMA kuna mcheza filamu wa Kinigeria, anayestahili kupewa tuzo kutoka na usiri, basi ni mwingine zaidi ya Genevieve Nnaji.

Genevieve, ambaye ni miongoni mwa wacheza filamu maarufu na tajiri nchini Nigeria, amekuwa akiyafanya siri kubwa maisha ya binti yake mwenye umri wa miaka 18 pamoja na baba wa mtoto huyo.

Kuna utata mkubwa kuhusu mwanaume anayedaiwa kuzaa na Genevieve na kamwe hajawahi kumtaja hadharani.

Na hii ni kutokana na mazingira, ambayo Genevieve alipata uja uzito. Inadaiwa kuwa, alipata uja uzito wa binti huyo, anayejulikana kwa jina la Chimebuka akiwa na umri wa miaka 15.

Gazeti la National Enquirer, ambalo lilikuwa la kwanza kuchapisha picha ya mtoto wa Genevieve, liliripoti hivi karibuni kuwa, mwanaume aliyezaa na mwanadada huyo anajulikana kwa jina la Acura.

Acura alilieleza gazeti hilo kwamba, baada ya kumpa uja uzito Genevieve, hakubeba jukumu la kumtunza kutokana na mazingira ya dini zao. Dini ya Genevieve (Mkatoliki) hairuhusu msichana kupata uja uzito nje ya ndoa.

Juhudi za gazeti hilo kumtafuta Genevieve ili athibitishe madai hayo, hazikuweza kufanikiwa.

Kwa sasa, Chimebuka anaishi nje ya Nigeria na hivi karibuni alikubali kupigwa picha akiwa kwenye ufukwe wa bahari, ndani ya gari na akiwa na rafiki zake hotelini.

Tuesday, April 23, 2013

CHIPUKIZI WA SIMBA, AZAM WAMKUNA POULSEN, AWAITA TAIFA STARS B




Kocha wa Taifa Stars, Kim Poulsen ametangaza timu ya pili ya Taifa (Young Taifa Stars) atakayoitumia kuangalia wachezaji ambao baadaye anaweza kuwajumuisha kwenye timu ya wakubwa.

Akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam leo (Aprili 23 mwaka huu) kabla ya kutaja kikosi hicho, Kim amesema timu hiyo ni sehemu ya Mpango wa Maendeleo wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) uliozinduliwa Aprili 4 mwaka huu ukilenga kuendeleza wachezaji.

Amesema timu hiyo inajumuisha wachezaji ambao wamepita umri wa kuchezea timu ya Taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 20 (Ngorongoro Heroes) na wakubwa ambao hawajapata fursa ya kuingia Taifa Stars, lakini atatumia Young Taifa Stars kuangalia uwezo wao.

“Timu hii ni kiungo kati ya vijana na wakubwa. Wengi wa wachezaji watakuwa vijana, lakini wakubwa wachache watapata fursa ya kuwemo ili kuangalia uwezo wao hata kama uko nyuma waliwahi kuchezea Taifa Stars. Lakini timu hii vilevile ni changamoto wa wachezaji wa Taifa Stars kuwa wapo wanaosubiri wazembee ili wachukue nafasi zao,” amesema.

Young Taifa Stars yenye wachezaji 30 itakuwa na kambi ya siku tano jijini Dar es Salaam kuanzia Mei 2 hadi 6 mwaka huu.

Wachezaji walioitwa ni Aishi Manula (Azam), Hussein Shariff (Mtibwa Sugar) na Ali Mustapha (Yanga) ambao ni makipa. Mabeki ni Kessy Hassan (Mtibwa Sugar), Kennan Ngoma (Barnsley FC, Uingereza), Himid Mao (Azam), Ismail Gambo (Azam), David Mwantika (Azam), Miraji Adam (Simba), Mohamed Hussein (Kagera Sugar), Waziri Salum (Azam), Samih Nuhu (Azam) na Emily Mgeta (Simba).

Viungo ni Haruna Chanongo (Simba), Edward Christopher (Simba), Mudathiri Yahya (Azam), William Lucian (Simba), Jonas Mkude (Simba), Hassan Dilunga (Ruvu Shooting), Jimmy Shoji (JKT Ruvu), Abdallah Seseme (Simba), Ramadhan Singano (Simba), Farid Mussa (Azam) na Vicent Barnabas (Mtibwa Sugar).

Washambuliaji ni Hussein Javu (Mtibwa Sugar), Jerome Lambele (Ashanti United), Zahoro Pazi (JKT Ruvu), Twaha Hussein (Coastal Union), Abdallah Karihe (Azam) na Juma Luizio (Mtibwa Sugar).

AFRICAN LYON, JKT RUVU KUUMANA CHAMAZI
Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inaendelea kesho (Aprili 24 mwaka huu) kwa mechi moja kati ya wenyeji African Lyon na JKT Ruvu.

Mechi hiyo namba 165 itachezwa Uwanja wa Azam Chamazi, Dar es Salaam chini ya usimamizi wa Kamishna Hamisi Kisiwa wa Dar es Salaam. Waamuzi wa mechi hiyo itakayoanza saa 10 kamili jioni ni Hashim Abdallah, Omari Kambangwa, Abdallah Selega na Said Ndege wote wa Dar es Salaam.

Monday, April 22, 2013

TENGA AMWAGA MIPIRA YA MAMILIONI KWA VYAMA NA SHULE ZA SOKA




Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga ametoa mipira zaidi ya 1,200 yenye thamani ya dola 30,000 za Marekani kwa vyama vya mpira wa miguu vya mikoa ya Tanzania Bara na vituo 21 vilivyo hai vya kuendeleza vijana (academies).

Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) lilimpa Rais Tenga fedha hizo ikiwa ni shukrani kwake kwa kushughulikia mgogoro wa uongozi wa mpira wa miguu nchini Kenya uliodumu kwa miaka miwili; ambapo nchi hiyo kutokana na mgogoro huo ilikuwa na vyama viwili (KFF na FKL).

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi mipira hiyo kwenye ofisi za TFF, Dar es Salaam leo (Aprili 22 mwaka huu), Rais Tenga amesema amefanya hivyo kwa vile anaamini kuwa mipira ndiyo kitu muhimu katika kuinua mchezo huo mahali popote.

“Dhamira yangi si kushukuru kwa hafla hii, bali kutoa sababu kwa nini nimefanya hivi. Ninaamini kwa kuanzia mipira ndiyo muhimu, pili kwa kufanya hivi itaonekana kweli mipira imegawiwa,” amesema Rais Tenga.

Amesema amesema mpira wa miguu kwa Tanzania unahitaji sana watu wa kujitolea, na yeye amefanya hivyo kwa kujitolea kutokana na ukweli shughuli anazotumwa na FIFA ni za kujitolea.

Rais Tenga ambaye pia alitumwa na FIFA kutatua matatizo ya uongozi wa mpira wa miguu katika nchi za Uganda, Zambia na Sudan Kusini amesema anaamini anapata fursa hizo kutokana na kuwa kiongozi wa TFF, na kwa kuwakumbuka waliomchagua ndiyo maana hakusita kupeleka fedha hizo kwenye mipira.

Amesema moja ya ndoto zake wakati anaingia kuongoza TFF mwaka 2004 ameshindwa kutimiza ni kusaidia mipira, kwani uwezo wa kununua mipira kwa wanaocheza katika ngazi ya chini hasa watoto haupo.

“Hizi kelele zote za maendeleo ya mpira wa miguu ni kwa sababu shuleni hakuna vifaa. Nia yangu ilikuwa shule zote zipate mipira, lakini hiyo ni moja ya ndoto nilizoshindwa kutekeleza. Vipaji haziwezi kupatikana kama watoto hawachezi.

“Tunashukuru sana kwa Serikali kurejesha mpira shuleni. Hata nitakapoondoka madarakani nikipata nafasi nitaendelea kuomba mipira kwa ajili ya shule,” amesema Rais Tenga.

Vyama vya mikoa ambavyo jumla ni 32 (Tanzania Bara na Zanzibar) kila kimoja kimekabidhiwa mipira 25 (kumi saizi namba tano, 15 saizi namba nne kwa ajili ya vijana). Kwa academies ambazo ni 21 kila moja imepewa mipira 25 (minane saizi namba tano, na 15 saizi namba nne).

Viongozi waliohudhuria hafla hiyo ni Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) Almasi Kasongo, Katibu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Mwanza (MZFA) Nassib Mabrouk na Katibu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA) Riziki Majala.

Kwa upande wa shule alikuwa Kanali mstaafu Idd Kipingu ambaye ni mmiliki wa shule ya Lord Baden ya Bagamoyo mkoani Pwani.

AZAM, COASTAL UNION KUCHEZA SIKU YA MUUNGANO


Timu za Coastal Union ya Tanga na Azam zitapambana Aprili 26 mwaka huu katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) itakayofanyika kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.

Awali mechi hiyo namba 168 ilikuwa ichezwe Aprili 27 mwaka huu, lakini imerudishwa nyuma kwa siku moja ili kuipa fursa Azam kujiandaa kwa mechi ya marudiano ya raundi ya pili ya Kombe la Shirikisho dhidi ya AS FAR Rabat ya Morocco.

Mechi hiyo itachezeshwa na Andrew Shamba kutoka mkoani Pwani akisaidiwa na Abdallah Mkomwa (Pwani), Vicent Mlabu (Morogoro) wakati mwamuzi wa mezani atakuwa Mohamed Mkono wa Tanga. Charles Komba wa Dodoma ndiye atakayekuwa Kamishna wa mechi hiyo ya raundi ya 24.

Baada ya mechi ya Tanga, Azam itarejea Dar es Salaam siku inayofuata tayari kwa safari ya kwenda Rabat itakayofanyika Aprili 28 mwaka huu. Mechi hiyo itachezwa wikiendi ya Mei 3, 4 au 5 mwaka huu.

Keshokutwa (Aprili 24 mwaka huu) kutakuwa na mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya African Lyon na JKT Ruvu itakayochezwa Uwanja wa Azam Chamazi, Dar es Salaam.

Iwapo Azam itafanikiwa kusonga mbele katika michuano ya Kombe la Shirikisho kutakuwa na marekebisho ya ratiba ya VPL. Hiyo ni kutokana na raundi inayofuata ya Kombe la Shrikisho kuchezwa wikiendi ya Mei 17, 18 na 19 mwaka huu ambapo bado haijajulikana Azam itaanzia wapi (nyumbani au ugenini) iwapo itavuka.

Mechi nyingine za VPL mwezi ni Aprili 25 (Ruvu Shooting vs Simba- Uwanja wa Taifa), na Aprili 28 (Simba vs Polisi Morogoro- Uwanja wa Taifa).


MKUTANO WA WAANDISHI WA HABARI
Kocha Mkuu wa Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager, Kim Poulsen atakuwa na mkutano na waandishi wa habari kesho (Aprili 23 mwaka huu).

Mkutano huo utafanyika saa 5 kamili asubuhi kwenye ukumbi wa mikutano wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

WAMOROCCO WA AZAM WAINGIZA MIL. 50/-, YANGA, JKT RUVU ZAINGIZA MIL 66/-



Mechi ya kwanza ya raundi ya pili ya Kombe la Shirikisho kati ya Azam na AS FAR Rabat ya Morocco iliyochezwa juzi (Aprili 20 mwaka huu) imeingiza sh. 50,850,000.

Fedha hizo katika mechi hiyo iliyochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kumalizika kwa timu hizo kutoka suluhu zimetokana na watazamaji 8,268 waliokata tiketi.

Viingilio vilikuwa sh. 5,000, sh. 10,000, sh. 10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000 ambacho kilikuwa kiingilio cha juu kwa jukwaa la VIP A. Kiingilio cha sh. 5,000 ndicho kilichovutia watazamaji wengi ambapo walikuwa 7,354.

Mgawo ulikuwa kama ifuatavyo; gharama za tiketi sh. 5,575,500, asilimia 15 ya uwanja sh. 6,791,175, asilimia 10 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh. 4,527,450 na asilimia 75 iliyokwenda kwa klabu ya Azam ni sh. 33,955,875.

Mechi iliyopita ya Azam katika michuano hiyo dhidi ya Barrack Young Controllers II ya Liberia iliingiza sh. 44,229,000 kutokana na watazamaji 17,128 waliokata tiketi. Viingilio vilikuwa sh. 2,000, sh. 5,000, sh. 10,000 na sh. 20,000 ambacho kilikuwa kiingilio cha juu kwa jukwaa la VIP A.

Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya JKT Ruvu na Yanga iliyochezwa jana (Aprili 21 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 66,568,000 kutokana na watazamaji 11,864.

Viingilio katika mechi hiyo namba 106 iliyomalizika kwa Yanga kutoa dozi ya 3-0 kwa wenyeji wao vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 15,702,752.45 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 10,154,440.68.

Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 7,984,450.40, tiketi sh. 3,183,890, gharama za mechi sh. 4,790,670.24, Kamati ya Ligi sh. 4,790,670.24, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 2,395,335.12, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA) sh. 931,519.21 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 931,519.21.

Sunday, April 21, 2013

ANNA KIBIRA MWENYEKITI MPYA CHANETA



KATIBU Mkuu wa zamani wa Chama cha Netiboli nchini (CHANETA), Anna
Kibira mwishoni mwa wiki iliyopita alichaguliwa kuwa mwenyekiti
mpya wa chama hicho.

Katika uchaguzi huo uliofanyika mkoani Dodoma, Anna aliibuka
mshindi baada ya kupata kura 61 na kumbwaga mpinzani wake, Shyrose
Banji aliyepata kura 21.

Nafasi ya makamu mwenyekiti ilichukuliwa na Zainabu Mbiro baada ya
kupata kura 57 wakati Agness Hatibu alichaguliwa kuwa mweka hazina
baada ya kupata kura 84.

Waliochaguliwa kuunda kamati ya utendaji ya chama hicho ni
Fortunata Kabeja, Asha Sapi, Judith Ilunda, Yasinta Sylvester,
Hilder Makatobe na Penina Igwe.

Akifungua mkutano mkuu wa chama hicho, Mkuu wa mkoa wa Dodoma,
Rehema Nchimbi aliitaka CHANETA kuhakikisha mchezo wa netiboli
unakuwa sehemu ya watoto wa kike.

TASWA YAAHIDIWA MAKUBWA NA AIPS




CHAMA cha Kimataifa cha Waandishi wa Habari za Michezo (AIPS),
kimeahidi kusaidia masuala mbalimbali yahusiyo mafunzo kwa
waandishi wa habari za michezo wa Tanzania.

Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi za Michezo Tanzania (TASWA), Juma
Pinto amesema kwamba rais wa AIPS, Gianni Merlo raia wa Italia
aliwapa fursa viongozi wa vyama vya waandishi wa habari za michezo
wa Afrika kuwasilisha changamoto mbalimbali zinazovikabili vyama
vyao, lakini kati ya hizo changamoto waitaje moja ambayo wanataka
AIPS isaidie kuwapa msaada.

Pinto amesema anashukuru Merlo kwanza alivutiwa sana na namna TASWA
inavyofanya kazi zake na ushiriki wake wa mikutano ya Dunia mara
kwa mara, hali ambayo aliahidi yeye binafsi kusaidia chama chetu
kuboresha masuala ya kimsingi.

Amesema kubwa ambalo AIPS baada ya kuelezwa imesema italipangia
utaratibu ni suala la mafunzo kwa waandishi wa habari chipukizi na
wanawake kwani hayo ni baadhi ya mambo ambayo wenyewe wanayatilia
mkazo na hasa baada ya kujulishwa kuwa kuna wanahabari zaidi ya 50
wanawake hapa nchini wanaofanya kazi kwenye masuala ya michezo.

Hata hivyo, Pinto amesema ingawa TASWA iliomba isaidiwe mafunzo kwa
wanachama wake wote kwa kupatiwa wataalamu hasa wakati huu ambao
kuna changamoto kubwa ya teknolojia ya habari na mawasiliano,
lakini AIPS imesema kwa mwaka huu uwezo wake ni kwa waandishi wa
habari za michezo chipukizi kupitia programu inayoandaliwa na AIPS.

Lakini Rais wa AIPS aliutaka ujumbe wa Tanzania utakapokuwa umerudi
nyumbani umuandalie mikakati hiyo kwa mafunzo ya wanawake ili
ikiwekezekana yafanyike kwa awamu katika kipindi cha miezi 18
kutegemea na idadi ya wahusika na pia gharama zenyewe.

Nchi wanachama 103 duniani zikiwemo nchi 24 za Afrika zilihudhuria
mkutano huo uliomalizika juzi Sochi, Urusi, ambapo pia ulifanyika
uchaguzi wa viongozi wa AIPS watakaokuwa madarakani kwa miaka minne
ijayo, ambapo Merlo alipita bila kupingwa.

Mkutano Mkuu wa AIPS ambao ni wa 76 ulimalizika juzi, ambapo
kulikuwa na kikao cha makatibu wakuu wa kila nchi kilichoendeshwa
na Katibu Mkuu wa AIPS, Roslyn Morris ambapo Tanzania iliwakilishwa
na Katibu Mkuu wa TASWA, Amir Mhando na huko pia suala la tuzo
mbalimbali zinazotolewa na wanahabari zilizungumzwa kwa kina.

Pia kulifanyika kikao cha marais wa AIPS wa mabara na baadhi ya
viongozi wa vyama vya wanahabari wa michezo wa Afrika kilichokuwa
chini ya Merlo, ambapo Mwenyekiti wa TASWA, Pinto alidhuria na
ajenda kubwa ilikuwa suala la rushwa kwenye michezo na mambo ya
upangaji wa matokeo wa mechi mbalimbali.

Baada ya mkutano huo, wakati ujumbe wa Tanzania ukiwa njiani
kurejea nyumbani ulipitia jijini Moscow, Urusi na kuzungumza
masuala mbalimbali na Balozi wa Tanzania nchini Urusi, Jaka Mwambi.

“Kwa ujumla mkutano ulikuwa na manufaa makubwa kwa Tanzania na
Afrika kwa ujumla, ambapo masuala mengine mengi yaliyojitokeza
kwenye mkutano huo ikiwemo namna ya mafunzo hayo yatakavyofanyika
tutayazungumza Jumatano ijayo kwenye mkutano na wanahabari
utakaofanyika ukumbi wa City Sports Lounge, Dar es Salaam saa tano
asubuhi,”alisema Pinto.

TASWA ni mwanachama hai wa AIPS yenye makao yake makuu Lausanne,
Uswisi, ndiyo sababu kila mwaka tumekuwa tukishiriki mikutano hiyo
tangu tulipoingia madarakani mwaka 2010.

Mwaka 2011 tulishiriki Mkutano Mkuu wa AIPS uliofanyika Seoul
Korea, Korea Kusini na tuliwakilishwa na Makamu Mwenyekiti, Maulid
Kitenge na Katibu Msaidizi, George John. Pia ilishiriki Mkutano Mkuu wa AIPS uliofanyika Innsbruck, Austria Januari mwaka jana, ambako Katibu Mkuu, Amir Mhando alihudhuria.

AZAM YAJIWEKA PABAYA, YALAZIMISHWA SARE NA WAMOROCCO


AZAM jana ilijiweka kwenye nafasi ngumu ya kusonga mbele katika
michuano ya soka ya Kombe la Shirikisho baada ya kulazimishwa
kutoka suluhu na FAR Rabat ya Morocco.

Katika mechi hiyo ya raundi ya pili iliyochezwa kwenye Uwanja wa
Taifa, Dar es Salaam, Azam ilipata nafasi kadhaa nzuri za kufunga
mabao, lakini ilishindwa kuzitumia vyema kutokana na washambuliaji
wake kuwa na papara ama kupiga mashuti bila malengo.

Kutokana na matokeo hayo, Azam sasa inahitaji ushindi ama sare
yoyote ya mabao ili iweze kusonga mbele wakati timu hizo
zitakaporudiana wiki mbili zijazo mjini Rabat.

Kimsingi, Azam ilicheza vizuri katika safu yake ya ulinzi na
kiungo, lakini tatizo kubwa lilikuwa katika safu yake ya
ushambuliaji, ambayo ilishindwa kucheza kwa malengo.

Kosa lingine kubwa lililofanywa na Azam katika mechi hiyo ni kujaza
wachezaji wengi wa kiungo katikati na hivyo kushindwa kujulikana ni
mchezaji yupi aliyekuwa akicheza namba 10. Pia ilimtegemea zaidi
mshambuliaji mmoja katika kufunga mabao.

Wachezaji waliocheza nafasi ya kiungo ni Humprey Mieno, Kipre
Balou, Salum Abubakar wakati Kipre Tchetche, Khamis Mcha na John
Bocco walicheza safi ya ushambuliaji.

Akizungumza baada ya mechi hiyo, Kocha Mkuu wa Azam, Stewart Hall
alisema, pamoja na kulazimishwa kutoka sare nyumbani, bado wanayo
matumaini ya kusonga mbele.

Thursday, April 18, 2013

SIMBA: HATUIBEBI YANGA NG'O


UONGOZI wa klabu ya Simba umesema kamwe hauna mpango wa kuwabeba watani wao wa jadi Yanga katika mechi yao ya mwisho ya ligi kuu ya Tanzania Bara, itakayochezwa Mei 18 mwaka huu mjini Dar es Salaam.

Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema mjini Dar es Salaam juzi kuwa, habari hizo zinazosambazwa kwa kutumia meseji kupitia simu za mkononi hazina ukweli wowote.

"Kuna ujumbe mfupi wa maneno umeenezwa kwenye baadhi ya simu za mkononi za wapenzi wa Simba ukidai kwamba washabiki wa Yanga waliokuwa wakiishangilia timu yetu tulipocheza na Azam walifanya hivyo kwa sababu klabu hizi mbili zimeingia katika mahusiano," alisema Kamwaga.

"Ujumbe huo ukadai kwamba lengo la mahusiano hayo mapya baina ya Simba na Yanga ni kuhakikisha kwamba Simba inafungwa kwa idadi kubwa ya mabao kwenye mechi ya watani wa jadi Mei 18 mwaka huu.

Ujumbe huo ukaenda mbali zaidi kwa kudai kwamba hata kambi ya Simba ya Bamba Beach imefadhiliwa na Yanga. Ujumbe huo wa simu ni wa kuchekesha sana,"aliongeza.

"Uongozi wa Simba unakana kuwepo kwa mahusiano yoyote ya kuhujumu timu baina ya viongozi wa klabu na Yanga. Kitendo cha kushangiliwa kwa timu pinzani si kigeni kwani kimewahi pia kutokea katika nchi kadhaa duniani.

"Ikumbukwe kwamba kimsingi, sio kosa la jinai au mwiko kwa shabiki wa Yanga kuishangilia Simba. Kama washabiki wa wapinzani wetu wa jadi walivutiwa na kiwango chetu na kuamua kutushangilia, hiyo haikuwa dhambi.

"Uongozi unapenda kuwaomba wanachama wa Simba kuwa na imani na uongozi wao na kufahamu kwamba unafanya kila unaloweza kulinda na kuhifadhi hadhi na heshima ya klabu,"alisisitiza Kamwaga.

Wakati huo huo, Kamwaga alisema kikosi cha timu hiyo kilianza mazoezi jana kwa ajili ya maandalizi ya mechi zake zijazo za ligi kuu.

Kamwaga alisema wachezaji wa timu hiyo walikuwa wamepewa mapumziko ya siku mbili baada ya kucheza mechi yao dhidi ya Azam mwishoni mwa wiki iliyopita na kutoka nayo sare ya mabao 2-2.

Wednesday, April 17, 2013

YANGA CHUPUCHUPU KWA MGAMBO JKT


Na Sophia Wakati, Tanga

BAO lililofungwa na mshambuliaji Simon Msuva jana liliinusuru Yanga isiadhirike kwa Mgambo JKT baada ya timu hizo kutoka sare ya bao 1-1 katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara iliyochezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani mjini hapa.

Msuva alifunga bao hilo dakika tano kabla ya mchezo kumalizika, baada ya kutokea piga nikupige kwenye lango la Mgambo JKT na mabeki wa Maafande hao kujichanganya.

Mgambo JKT ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 43 lililofungwa na Issa Kandulu baada ya kumalizia pasi kati yake, Nassoro Gumbo na Sammy Mlima.

Sare hiyo imepunguza kasi ya Yanga kutangaza ubingwa wa ligi hiyo mapema, lakini bado inaendelea kuongoza ikiwa na pointi 53 baada ya kucheza mechi 23, ikifuatiwa na Azam yenye pointi 47. Timu hizo zinatofautiana kwa pointi sita.

Mgambo JKT ililianza pambano hilo kwa kasi na kupata nafasi mbili nzuri za kufunga mabao dakika za mwanzo, lakini umaliziaji mbovu wa washambuliaji wake, Nassoro Gumbo na Sammy Mlima ulikuwa kikwazo.

Yanga ilijibu mashambulizi hayo dakika ya 10 na 15, lakini washambuliaji wake, Simon Msuva na Hamisi Kiiza walikosa umakini na kupoteza nafasi za kufunga mabao.

Pambano hilo liliingia doa dakika ya 44 baada ya Simon Msuva kuangushwa ndani ya eneo la hatari na beki Bakari Mtama wa Mgambo JKT , lakini mwamuzi Athumani Lazi kutoka Morogoro aliamua kupeta.

Kufuatia mwamuzi kutotoa adhabu yoyote, mashabiki wa Yanga waliamua kurusha chupa ndani ya uwanja, lakini hakuna mchezaji aliyejeruhiwa. Ilibidi pambano lisimame kwa dakika mbili kabla ya kuendelea. Timu hizo zilikwenda mapumziko Mgambo ikiwa mbele kwa bao 1-0.

Pambano hilo liliingia tena doa dakika ya 56 baada ya mashabiki wa Yanga kurusha chupa uwanjani, wakipinga kitendo cha mwamuzi kumwonyesha kadi ya njano Nadir Haroub 'Cannavaro' aliyemlalamikia baada ya Kevin Yondan kupigwa kiwiko na mchezaji mmoja wa Mgambo JKT.

Katika kipindi cha pili, Yanga iliwapumzisha Hamisi Kiiza na Frank Dumayo, ambao nafasi zao zilichukuliwa na Saidi Bahanuzi na Nurdin Bakari.

Pamoja na kufanya mabadiliko hayo, Yanga ilishindwa kusawazisha kutokana na washambuliaji wake kukosa umakini kila walipofika kwenye lango la Mgambo JKT.

NGASA AITABIRIA MAKUBWA SIMBA MSIMU UJAO


MSHAMBULIAJI Mrisho Ngasa wa Simba amesema wachezaji chipukizi wa timu hiyo ni wazuri, lakini bado wanahitaji muda zaidi ili kuzoea mikikimikiki ya ligi kuu ya Tanzania Bara.

Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Ngasa alisema chipukizi hao wanacheza soka ya kiwango cha juu na ya kuvutia, lakini kutokana na kukosa uzoefu, wamekuwa wakifanya makosa ya kizembe.

Akitoa mfano, Ngasa alisema katika mechi yao dhidi ya Azam iliyochezwa Jumapili iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, chipukizi hao walionyesha kiwango cha juu kuliko wapinzani wao.

"Tatizo lililosababisha wapinzani wetu wasawazishe ni makosa madogo madogo yaliyofanywa na vijana wetu. Vinginevyo, Simba itakuwa na timu nzuri sana mwakani,"alisema.

Ngasa amewataka mashabiki na wanachama wa Simba wawe na subira kwa sababu vijana hao wanahitaji muda zaidi ili waweze kuzoea mikikimikiki ya ligi hiyo.

Katika mechi hiyo, Simba na Azam zilishindwa kutambiana baada ya kutoka sare ya mabao 2-2. Simba ilikuwa ya kwanza kupata mabao kupitia kwa mshambuliaji wake chipukizi, Ramadhani Singano, aliyetengenezwa vyumba safi na Ngasa.

Azam ilisawazisha kwa bao la penalti lililofungwa na Kipre Tchetche baada ya beki Miraji Juma kumchezea vibaya Khamis Mcha ndani ya eneo la hatari. Bao la kusawazisha lilifungwa na Humphrey Mieno.

Tayari Simba imeshavuliwa ubingwa wa ligi hiyo na kupoteza mwelekeo wa kushika nafasi ya pili baada ya kuvurunda katika mechi zake za hivi karibuni, ikiwa ni pamoja na kuchapwa bao 1-0 na Kagera Sugar na kulazimishwa sare ya mabao 2-2 na Toto African.

BARTHEZ AMPIKU KASEJA KWA UBORA

KIPA Ally Mustapha 'Barthez' wa klabu ya Yanga amewapiku kwa ubora makipa Juma Kaseja wa Simba na Mwadini Ally wa Azam.

Barthez amewapiku kwa ubora makipa hao wawili wa timu ya Taifa, Taifa Stars kutokana na kufungwa mabao machache katika michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara inayoendelea.

Takwimu zinaonyesha kuwa, kabla ya mechi ya jana kati ya Yanga na Mgambo JKT iliyotarajiwa kuchezwa mjini Tanga, Barthez alikuwa amefungwa mabao 12 katika mechi 22.

Kwa mujibu wa takwimu hizo, Mwadini alikuwa akishika nafasi ya tatu kwa kufungwa mabao 19 wakati Kaseja amesharuhusu nyavu za timu yake kutikisika mara 21.

Kabla ya mechi za jana, mabao 327 yalikuwa yameshatinga wavuni, Azam ikiongoza kwa kufunga mabao 41, ikifuatiwa na Yanga iliyofunga mabao 40.

Simba ilikuwa ikishika nafasi ya tatu kwa kufunga mabao 32, ikifuatiwa na Mtibwa Sugar iliyofunga mabao 26, Kagera Sugar imefunga mabao 24, Coastal Union imefunga mabao 23 wakati JKT Oljoro na Toto African zimefunga mabao 22 kila moja.

African Lyon inaongoza kwa kufungwa mabao mengi baada ya kuruhusu nyavu zake kutikisika mabar 35, ikifuatiwa na JKT Ruvu iliyofungwa mabao 34 na Toto African iliyofungwa mabao 33.

Yanga inaongoza ligi kwa kuwa na pointi 52 (kabla ya mechi ya jana), ikifuatiwa na Azam yenye pointi 47, Kagera Sugar yenye pointi 37 na Simba yenye pointi 36.

SERIKALI BADO HAIJAWASAIDIA WASANII-PROFESA JAY

LICHA ya serikali kuanza kutoza kodi kazi za wasanii kwa lengo la kudhibiti wizi wa sanaa, msanii Joseph Haule amesema bado haijaweza kuwakwamua kimaendeleo.

Haule, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Profesa Jay, alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, bado kilio cha wasanii wa Tanzania ni kuibwa kwa kazi zao na kwamba serikali haijachukua hatua madhubuti kupambana na tatizo hilo.

"Serikali ingejaribu kuangalia jinsi gani ya kuwasaidia wasanii wa Tanzania katika kazi zao, kama vile milio ya simu na katika sheria, jinsi gani msanii anaweza kunufaika na kazi zake anazozifanya,"alisema.

"Hivi sasa kuna stika za TRA, lakini haziwezi kusaidia kitu, stika zitakuwepo, lakini tatizo sugu tumeliacha, tatizo ni wizi wa kazi za wasanii," aliongeza msanii huyo mkongwe.

Mbali na kuilaumu serikali, Profesa Jay pia aliwaponda baadhi ya wasanii wa muziki wa kizazi kipya nchini kwa kukosa ubunifu na kuimba nyimbo zisizoeleweka na kudumu kwa muda mrefu.

Profesa Jay alisema wakati umefika kwa wasanii wa Tanzania kuamka na kutazama wapi wanakopaswa kwenda na pia kutumia vyema fursa ya lugha ya kiswahili kuwa ya kimataifa.

"Hivi sasa kila mmoja anamtupia lawama mwenzake. Jambo la muhimu ni kwamba tukae kama wasanii tunaotaka kuupeleka muziki wetu mahali fulani,"alisisitiza.

Msanii huyo mkongwe alisema muziki wa Tanzania unaharibiwa na wasanii wenyewe kutokana na kuandika mashairi yasiyoeleweka na pia kufanya maonyesho yasiyo na mvuto.

Profesa Jay pia alivilaumu vyombo vya habari nchini, hasa redio na televisheni kwa kupiga nyimbo zinazokiuka maadili na hivyo kutosaidia katika kuutangaza muziki wa Tanzania kimataifa.

JUMA NATURE AFUNGUKA


BAADA ya ukimya wa muda mrefu, msanii nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Juma Kassim 'Nature' ameamua kutoka kivingine kwa kuwashirikisha wasanii wasiokuwa na majina kurekodi nyimbo zake.

Nature alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, ameamua kushirikiana na baadhi ya wasanii wanaokubalika katika jamii ili kuzifanya nyimbo zake ziwe na mvuto zaidi.

Kwa kuanzia, Nature alisema amemshirikisha Tunda Man katika wimbo wake mpya wa Haipotei kutokana na uimbaji wake na sauti yenye mvuto.

Aliwataja wasanii wengine anaotarajia kuwashirikisha katika nyimbo zake kuwa ni pamoja na Kitale, Kingwendu, Stoppa na Dogo Lila.

Nature alisema kwa sasa hatarajii kutoa albamu kutokana na soko la muziki huo kuyumba.

Mbali na kufyatua kibao cha Haipotei, Nature pia amezindua fulana mpya zenye jina la wimbo huo.

Nature alisema mwanzo alikuwa akizigawa bure fulana hizo kwa mashabiki wake, lakini kwa sasa ameamua kuziuza.

Alisema fulana hizo zinapatikana nyumbani kwake Mbagala Zakhem na kuongeza kuwa, fulana moja inauzwa kwa sh. 16,000.

KEISHA AISIMULIA NDIMU



BAADA ya ukimya mrefu, msanii nyota wa kike wa muziki wa kizazi kipya, Khadija Shaaban ameibuka na kibao kipya kinachokwenda kwa jina la Ndimu.

Khadija, maarufu zaidi kwa jina la Keisha, amerekodi kibao hicho kwenye studio za AM Records chini ya prodyuza maneke.

Katika kibao hicho, Keisha amemfananisha mwanaume kuwa sawa na ndimu, ikiwemo kwenye chakula inatengeneza ladha nzuri.

Mbali na kutengeneza ladha nzuri kwenye chakula, Keisha ameimba kwenye kibao hicho akisema, hata isipokuwepo, haimaanishi kwamba haiwezekani chakula kuliwa.

Nyota huyo, ambaye alifunika vilivyo kwenye wimbo wa ‘Bado tunapanda’ wa kundi la Tip Top Connection lenye maskani yake Manzese jijini Dar alisema, mwaka jana alijifungua mtoto wa kiume.

Pamoja na kupata mtoto, Keisha alisema bado ataendelea na kazi yake ya kukonga nyoyo za mashabiki.

Keisha alijiengua katika kundi hilo mwishoni mwa mwaka jana baada ya kutokea hali ya kutokuelewana kati yake na uongozi. Kwa sasa, Keisha anapiga muziki kwa kujitegemea.

D0GO JANJA: SIKUFELI MITIHANI SABABU YA KUENDEKEZA STAREHE



MSANII machachari wa muziki wa kizazi kipya nchini, Abubakar Chende 'Dogo Janja' amesema si kweli kwamba amefeli mitihani ya kidato cha nne kutokana na kuendekeza starehe.

Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii Dogo Janja alisema, kufeli kwake kulitokana na bahati mbaya na ni mambo ya kawaida katika mitihani kwa wanafunzi.

Dogo Janja alisema madai yaliyotolewa hivi karibuni na kiongozi wake wa zamani wa kundi la Tip Top Connections, Hamad Ally 'Madee' kwamba amefeli kutokana na kuendekeza sana starehe, yamelenga kumchafua.

"Nashangaa sana kwa nini Madee anaendelea kunifuatafuata. Wakati nikiwa Afrika Kusini, nilipigiwa simu na mtangazaji mmoja wa redio akiniambia kwamba, Madee ameniponda kwa kusema nimefeli tena kwa sababu ya kuendekekeza starehe.

"Madai haya hayana ukweli wowote. Mimi na yeye tulishamaliza tofauti zetu na kuamua kusameheana. Namheshimu kama mtu aliyenitoa na kunifikisha hapa nilipo, lakini sipendi tabia yake ya kunifuatafuata,"alisema.

Ofisa Taaluma katika shule ya sekondari ya Makongo, Alfred Mbaula alikaririwa akisema kuwa, mahudhurio ya Dogo Janja darasani yalikuwa mazuri na alikuwa akishirikiana vyema na wenzake.

Mbaula alisema Dogo Janja alifeli mitihani yake kwa wastani mdogo, ambao usingemruhusu kuendelea na kidato cha tatu, hivyo atalazimika kurudia kidato cha pili.

Alipoulizwa iwapo uongozi wa shule ulikuwa na taarifa ya safari ya Dongo Janja nchini Afrika Kusini, ofisa huyo alisema hakuwa ameomba ruhusa.

"Sio kweli kwamba aliomba ruhua na wala ofisi haina taarifa, japokuwa shule haina tatizo, akitoa taarifa hata katikati ya masomo iwapo anatakiwa kufanya shughuli za muziki kwa sababu Makongo ni shule ya vipaji,"alisema.

KATHRYN BERNARDO, MWIGIZAJI ALIYEINADHIFISHA TAMTHILIA YA MARA CLARA





KWA mashabiki wanaofuatilia tamthilia ya Mara Clara, inayoonyeshwa na kituo cha televisheni cha Star TV kila siku za Jumanne, Ijumaa, Jumamosi na Jumapili usiku, jina la Mara si geni kwao. Ni mmoja wa wasanii walioinadhifisha tamthilia hiyo kutokana na uigizaji wake mzuri na wa kuvutia.

Mara Clara ni tamthilia ya Kifilipino, ambayo ilionyeshwa kwa mara ya kwanza na kituo cha ABS-CBN kuanzia Agosti 17, 1992 hadi Februari 14, 1997. Ni tamthilia inayotokana na kitabu cha Mara Clara kilichoandikwa na Emil Cruz Jr.

Katika tamthilia hiyo, Mara ambaye jina lake halisi ni Kathryn Bernardo, ameigiza na Julia Montes, anayetumia jina la Clara.

Mabinti hawa wawili walibadilishwa na Karlo mara baada ya kuzaliwa bila ya wazazi wao kujijua. Mara aliishi maisha ya kimaskini akiwa na wanandoa, Susan na Gary wakati binti yao halisi, Clara aliishi katika familia ya matajiri ya Amante na Alvira del Valle.

Lengo la Karlo kuwabadilisha watoto hao wawili baada ya kulizaliwa, lilikuwa kumwezesha Clara kuishi maisha ya kifahari na kupata elimu nzuri kwa vile baba yake halisi, Gary alikuwa jela.

Karlo, ambaye alikuwa mtumishi wa hospitali na ndugu wa Gary, aliamua kuandika kumbukumbu ya tukio hilo kwenye kitabu chake maalumu na ndicho kilichowezesha ukweli kubainika hata baada ya kufa kwake.

Kuna wakati, familia ya Del Valle ilimchukulia Mara kama mtumishi wa ndani na kuamua kumgharamia kimasomo bila kujua ndiye mtoto wao halisi. Clara, ambaye ni mtoto halisi wa Gary, alisababisha maisha ya Mara yawe magumu.

Hasira za Clara kwa Mara zilitokasana na sababu nyingi. Ya kwanza ilikuwa Mara alimzidi Clara kimasomo. Ya pili ilikuwa uhusiano wa karibu aliokuwa nao Mara kwa Cristian, ambaye Clara alikuwa akimpenda.

Hata hivyo, kadri maisha yalivyosonga mbele, ukweli ukaja kubainika kwamba Mara ndiye mtoto halisi wa familia ya Del Valle wakati Clara ni mtoto halisi wa familia ya Gary.

Unazuka uhasama mkubwa kati ya familia hizo mbili, ambapo Gary analazimika kufanya kila linalowezekana kumfanya Clara amkubali kwamba ndiye baba yake halisi, ikiwa ni pamoja na kumteka Mara na Clara kwa lengo la kuishinikiza familia ya Del Valle ilipe pesa kwa ajili ya kuwagomboa.

Licha ya Gary kufanikiwa kupata mamilioni ya pesa kutoka kwa familia ya Del Valle, anaandaa mpango wa kumuangamiza Mara kwa milipuko ya mabomu huku Clara akifanikiwa kujiokoa. Kifo cha Mara kinawasikitisha wazazi wake, ambao wanaapa lazima wawapate wauaji na kuwafikisha kwenye vyombo vya dola.

Hata hivyo, inakuja kubainika baadaye kwamba, Mara hakuwa amekufa kwenye mlipuko uliotokea kwenye jumba alimofungiwa na Clara. Aliokolewa na mmoja wa vikaragosi wa Gary kabla ya kupelekwa mafichoni na Cristian.

Mama yake Gary ndiye anayefanikiwa kufichua mpango mzima wa mauaji ya kupanga ya Mara baada ya kukuta mamilioni ya pesa chumbani kwa mtoto wake huyo na pia kumfuatilia na kumuona akiingia kwenye nyumba alimomuhifadhi Cristine, ambaye alikuwa akitafutwa na polisi.

Hatimaye Gary na Cristine wanatiwa mbaroni na polisi na wakati huo huo, Mara anaibuka kutoka mafichoni na kuibua furaha kwa familia yake.

Mara alizaliwa Machi 26, 1996 katika mji wa Cabanatuan , Philippines. Ni mmoja wa waigizaji wa kike wenye mvuto nchini humo, akiwa amejipatia umaarufu mkubwa baada ya kucheza filamu ya Mara Clara.

Kwa sasa, Mara ni msanii mwenye mkataba na vituo vya televisheni vya Star Magic na ABS-CBN na hivi karibuni alishiriki kuigiza tamthilia ya Way Back Home akiwa anatumia jina la Ana Bartolome. Tamthilia hiyo iliandaliwa 2011.

Binti huyo mwenye sura jamali, pia amecheza tamthilia ya Princess and I akiwa anatumia jina la Mikay. Mara ni swahiba mkubwa wa Clara na mara nyingi hupenda kutembea pamoja.

Mara ni mwanafunzi wa chuo cha Angelicum na amewahi kushinda tuzo mbalimbali kutokana na tamthilia ya Mara Clara.

Mara alianza kucheza filamu tangu 2004 alipoigiza filamu ya Gagamboy, lakini alianza kupata umaarufu baada ya kucheza filamu ya Way Back Home akishirikiana na Julia Montes.

Filamu hiyo iliongozwa kwa kutazamwa na watu milioni 18 katika wiki yake ya kwanza na kuzipiku filamu za kizungu zilizokuwa zikionyeshwa nchini humo katika wiki hiyo kama vile The Smurfs na Conan the Barnarian.

Mbali na kucheza filamu na tamthilia, Mara pia ni mwanamitindo na amekuwa akitumika kutangaza bidhaa mbalimbali kama vile Bench and Coca-Cola. Pia ni mwanamuziki na mwaka jana alirekodi kibao cha Mula Noon Hanggang Ngayon.

MOO KUONGOZA KAMATI YA TAIFA STARS



Kama mnavyofahamu, hivi sasa Timu ya Taifa ya mpira wa Miguu kwa Wanaume (Taifa Stars) ipo kwenye michuano ya kufuzu kushiriki Fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika nchini Brazil mwaka 2014.

Katika Afrika, Tanzania (Taifa Stars) imepangwa kundi C kati ya makundi 10. Kundi C linajumuisha timu za Ivory Coast, Morocco, Gambia na Tanzania.

Kwa sasa katika kundi C, Taifa Stars inashika nafasi ya pili ikiwa na alama sita (6), nyuma ya Ivory Coast yenye alama saba (7), Morocco ina alama mbili (2) na Gambia ina alama moja(1).

Kwa mara nyingine Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo inapenda kuwapongeza Taifa Stars, kwa kazi nzuri ambayo wameishaifanya ikiwemo ushindi wa Bao Tatu kwa Moja dhidi ya Morocco. Watanzania wote na Wadau wa Soka nchini wamefurahishwa sana na mafanikio yaliyofikiwa na Taifa Stars na yenye kutupa matumaini katika kuitayarisha Taifa Stars kufuzu kucheza Fainali za Kombe la Dunia kwa mwaka 2014 nchini Brazil.

Kwa hali ilivyo hivi sasa, Taifa Stars ipo katika nafasi nzuri ya kufuzu. Ili Tanzania tuweze kufuzu, Taifa Stars inatakiwa ishinde mechi zote tatu (3) na kuongoza kundi C na baadae iingie katika Timu kumi (10) bora na kisha zipatikane Timu tano (5) kutoka Afrika ambazo zitakuwa zimefuzu kwenda Brazil katika Fainali za Kombe la Dunia kwa mwaka 2014. Tunaamini hili linawezekana.

Sasa kwa kuzingatia uzito wa jukumu lililo mbele yetu na kwa Taifa Stars kwa ujumla; Serikali imeunda Kamati ya Ushindi ya Taifa Stars.

Jukumu la msingi la Kamati tunayoiunda ni kuhakikisha Taifa Stars inawezeshwa na kuandaliwa ipasavyo ikiwa ni pamoja na kuunda kikundi cha kuishangilia timu ya Taifa ndani na nje ya nchi. Wajumbe wa Kamati ya Taifa Stars Stars itakayoongozwa na Mhe. Mohamed Dewji ni hawa wafuatao:-

1. Mhe Mohamed Dewji - Mbunge
2. Bi. Teddy Mapunda - Montage
3. Dkt. Ramadhani Dau - Mkurugenzi Mtendaji NSSF
4. Bw. Dioniz Malinzi - Mwenyekiti BMT
5. Bw. Abji Shabir - New Africa Hotel
6. Bw. George Kavishe - TBL
7. Mhe. Mohamed Raza - Zanzibar
8. Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
9. Bw. Joseph Kusaga - Clouds
10. Mhe. Kapt. John Komba - Mbunge
11. Mhe. Zitto Kabwe - Mbunge

Kamati hii iliyoteuliwa leo, naomba ianze kazi mara moja. Hadidu za rejea zitakazowaongoza kutekeleza majukumu yao chini ya Kamati hii watazipata kutoka Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo. Kamati itashirikisha wadau mbalimbali kadri itakavyoona inafaa.

Serikali inaahidi kutoa ushirikiano utakaohitajika katika kuhakikisha Kamati hii inafanya kazi vizuri ili kuiwezesha Taifa Stars kushinda Mechi zote zilizombele yetu.

Aidha nichukue fursa hii kutoa wito kwa Watanzania wote, kuiunga mkono Taifa Stars na Kamati ya Ushindi ya Taifa Stars kwa hali na mali katika kuhakikisha timu yetu inafuzu kucheza Fainali za Kombe la Dunia.

Kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri Mkuu naomba niwasilishe salaam zao za kuwapongeza Vijana wetu wa Taifa Stars, pamoja na benchi la ufundi likiongozwa na Kocha Mkuu Kim Poulsen. Kwa pamoja wanaomba Taifa Stars iendelee kujipanga kwa mechi zijazo. Nawahakikishia kuwa Serikali, Watanzania na wadau wa Soka nchini wapo nyuma yao.

Mungu Ibariki Taifa Stars. Mungu Ibariki Tanzania.

Dkt. Fenella Mukangara (Mb)
WAZIRI WA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO
16 Aprili, 2013

Monday, April 15, 2013

SIMBA, AZAM ZAINGIZA MILIONI 66

Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Azam na Simba iliyochezwa jana (Aprili 14 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 66,855,000 kutokana na watazamaji 11,458.

Viingilio katika mechi hiyo namba 155 iliyomalizika kwa timu hizo kutoka sare ya mabao 2-2 vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 15,587,177.45 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 10,198,220.34.

Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 7,925,683.45, tiketi sh. 3,818,890, gharama za mechi sh. 4,755,410.07, Kamati ya Ligi sh. 4,755,410.07, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 2,377,705.03 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 1,849,326.14.

WATAZAMAJI 11,021 WAZISHUHUDIA YANGA, OLJORO
Watazamaji 11,021 walikata tiketi kushuhudia mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Yanga na Oljoro JKT iliyochezwa juzi (Aprili 13 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kuingiza sh. 63,170,000.

Viingilio katika mechi hiyo namba 156 iliyomalizika kwa Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 14,853,252.45 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 9,636,101.69.

Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 7,552,501.25, tiketi sh. 3,183,890, gharama za mechi sh. 4,531,500.75, Kamati ya Ligi sh. 4,531,500.75, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 2,265,750.37 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 1,762,250.29.

Sunday, April 14, 2013

MBAGA, MSAIDIZI WAKE WAIBEBA AZAM KWA BAO LA MKONO, CHIPUKIZI WA SIMBA USIPIME



MWAMUZI Oden Mbaga leo alionekana dhahiri kuibeba Azam baada ya kuruhusu bao lake la kusawazisha lililofungwa na Humphrey Mieno baada ya kuushika mpira kwa mkono kwa makusudi.

Mieno alifunga bao hilo katika kipindi cha pili baada ya mpira wa krosi uliopigwa na Khamis Mcha kutoka pembeni kidogo ya uwanja.

Awali, mwamuzi msaidizi namba mbili alinyoosha kibendera hewani kuashiria kwamba kuna mashambi yalitendeka, lakini baada ya kumuona Mbaga akielekea kati, aliamua kukishusha mara moja na kuungana naye.

Kipa Abbel Dhaira wa Simba hakuwa amefanya jitihada yoyote ya kuokoa mpira uliopigwa na Mieno kwa sababu aliushika mpira kwa mkono mbele yake na pia alimuona mwamuzi msaidizi akinyoosha kibendera hewani.

Kutokana na utata huo, wachezaji wa Simba walimzonga Mbaga na msaidizi wake, wakilalamikia bao hilo, lakini hakuna aliyebadili msimamo.

Baadhi ya mashabiki waliohudhuria pambano hilo, wamekielezea kitendo hicho cha Mbaga kuwa ni cha fedheha kwa mwamuzi mwenye beji ya Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA), anayetakiwa kuchezesha mechi za michuano ya kimataifa.

Katika pambano hilo, Simba ambayo ilichezesha wachezaji wengi chipukizi, ilionyesha kiwango cha juu na kuwafanya mashabiki wake wawashangilie kwa furaha kubwa. Pia mashabiki wa Yanga leo walikuwa wakiishangilia Simba ili iifunge Azam.

Kwa matokeo hayo, Simba imeendelea kushika nafasi ya nne katika msimamo wa ligi hiyo, ikiwa na pointi 36 wakati Azam ni ya pili ikiwa na pointi 47.

Mshambuliaji Ramadhani Singano aliibuka shujaa wa Simba baada ya kuifungia mabao yote mawili dakika ya 10 na 14 baada ya kupokea pasi kutoka kwa Mrisho Ngasa.

Azam ilipata bao lake la kwanza kwa njia ya penalti kupitia kwa Kipre Tchetche baada ya beki wa pembeni, Miraji Juma kumkwatua ndani ya eneo la hatari kabla ya Mieno kufunga bao la utata.

Simba: Abbel Dhaira, Nassor Masoud ‘Chollo’, Miraj Adam, Mussa Mudde, Shomary Kapombe, Amri Kiemba, Haroun Chanongo/Edward Christopher, Abdallah Seseme, William Lucian/Mwinyi Kazimoto, Ramadhani Singano na Mrisho Ngassa/Fliex Sunzu.

Azam :Mwadini Ally, Himid Mao, Waziri Salum, David Mwantika, Joackins Atudo, Kipre Balou, Luckson Kakolaki/Khamis Mcha ‘Vialli’ dk, Salum Abubakar, John Bocco/Abdi Kassim, Humphrey Mieno/Jabir Aziz na Kipre Tchetche

YANGA YAMTENDEA HAKI MANJI, LEO NI SIMBA NA AZAM



YANGA jana iliendelea kuchanua katika michuano ya soka ya ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kuibugiza JKT Oljoro mabao 3-0 katika mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Ushindi huo mnono wa Yanga umekuja siku chache baada ya Mwenyekiti wa klabu hiyo, Yussuf Manji kukilalamikia kikosi chake kwa kuibuka na ushindi kiduchu wa bao 1-0 katika mechi zake zilizopita za ligi hiyo.

Katika kikao chake na wachezaji, Manji alisema anataka kuiona timu yake ikitoka uwanjani na ushindi mkubwa wa mabao na kuahidi kuwazawadia sh. milioni 100 iwapo watafanikiwa kutwaa ubingwa msimu huu.

Kutokana na ushindi huo, Yanga sasa imefikisha pointi 52 baada ya kucheza mechi 22, ikifuatiwa na Azam yenye pointi 46. Azam inatarajiwa kushuka dimbani leo kwenye uwanja huo kumenyana na mabingwa watetezi, Simba.

Katika mechi hiyo, Yanga ilijipatia mabao yake yote matatu kupitia kwa Nadir Haroub 'Cannavaro, Simon Msuva na Hamisi Kiiza.

Cannavaro alifunga bao la kwanza baada ya kutokea piga nikupige kwenye lango la JKT Oljoro, kufuatia mpira wa kona uliopigwa na Haruna Niyonzima.

Msuva aliongeza bao la pili baada ya kupokea pasi kutoka kwa David Luhende, akawatoka mabeki kadhaa wa Oljoro kabla ya kufumua shuti kali lililotinga moja kwa moja wavuni.

Bao la tatu lilifungwa na Kiiza baada ya kupokea pasi kutoka kwa Niyonzima na kumpiga chenga kipa wa Oljoro kabla ya kuutumbukiza mpira wavuni.

Saturday, April 13, 2013

AMRI IBRAHIM, MKONGWE WA SOKA ANAYEWASIKITIKIA VIONGOZI WA SASA WA MCHEZO HUO




WIKI iliyopita, mwanasoka mkongwe nchini, Amri Ibrahim alielezea mambo mbalimbali yanayomkera katika uendeshaji wa mchezo huo hivi sasa hapa nchini na kupendekeza hatua mbalimbali zinazofaa kuchukuliwa na kuinua kiwango cha soka. Katika sehemu hii ya pili na ya mwisho, mkongwe huyo anaelezea historia yake na matukio mbalimbali anayoyakumbuka.


Amri alisema kama klabu inaye mfadhili, anapaswa kuheshimu nafasi za viongozi na makocha, vivyo hivyo vongozi, ambao alisema nao wanapaswa kuheshimu nafasi za wafadhili na makocha.

Aliipongeza TFF kwa hatua, ambazo imekuwa ikichukua kukomesha vitendo vya vurugu kwenye viwanja vya soka kwa kuwaadhibu wachezaji, waamuzi na viongozi wanaohusika kuchochea vitendo hivyo.

"Nidhamu ni muhimu sana katika soka, na ilikuwa imeshuka sana katika miaka ya nyuma. Mashabiki walifikia hatua ya kuweka mikojo kwenye chupa za maji na kuwarushi waamuzi na wachezaji uwanjani. Huu ulikuwa uhuni," alisema kiungo huyo wa zamani wa Pamba na Simba.

Aliitaka TFF kuweka wazi programu zake za kuendesha soka nchini ili wadau wa mchezo huo waweze kuzisoma, kuzielewa na kuchangia mawazo yao. Alisema ni vyema programu hizo ziwe zikisambazwa katika vyama vya soka vya wilaya ya mikoa yote nchini.

Amri alizaliwa 1959 kijiji cha Gungu kilichopo Kigoma Mjini. Alisoma elimu ya msingi mkoani Kigoma na katika mikoa ya Mwanza na Mara.

Alianza kucheza soka tangu alipokuwa mdogo kwa kutumia chandimu. Alichezea timu za mitaani na za shule alizosoma kabla ya kujiunga na Gungu Heroes na baadaye Lake Stars.

Alianza kupata umaarufu kisoka 1973 alipokuwa akichezea Lake Stars katika michuano ya kuwania ubingwa wa wilaya na mkoa. Timu hiyo ilifanikiwa kucheza fainali ya ubingwa wa Taifa na kufungwa mabao 2-0 na Simba.

Amri alijiunga na Pamba ya Shinyanga 1975 na kuichezea kwa muda mfupi kabla ya kuhamishiwa Pamba ya Mwanza. Aliichezea Pamba ya Mwanza kwa mara ya kwanza ilipomenyana na Luo Union ya Kenya katika mechi ya kirafiki iliyochezwa kwenye uwanja wa Nyamagana na kuibuka na ushindi wa bao 1-0.

Katika mechi hiyo, Amri aliingizwa uwanjani kipindi cha pili na kutoa pasi kwa Ibrahim Posi, aliyefunga bao hilo na pekee na la ushindi kwa kichwa.

Wakati Amri alipojiunga na Pamba ya Mwanza, kikosi cha timu hiyo kilikuwa kinaundwa na baadhi ya wachezaji waliokuwa nyota wakati huo kama vile Joram Mwakatika, Tabu Mwakatika, Titus Bandawe, Khalid Bitebo, Hamisi Bilali, James Ng'ong'a na Makinga Shabani.

Mechi ya pili ya kimataifa kwa Amri kuichezea Pamba ilikuwa dhidi ya Galacia ya Brazil. Mechi hiyo pia ilichezwa kwenye uwanja wa Nyamagana na Pamba ilichapwa mabao 2-1.

Amri amemwelezea mwenyekiti wa zamani wa Pamba, marehemu Shabani Mwakayugwa kuwa alichangia kwa kiasi kikubwa kuinua maendeleo ya soka mkoani Mwanza kutokana na kuzialika timu mbalimbali za kigeni kucheza na Pamba.

Amri alihamishiwa mkoa wa Mara kikazi 1976, ambako alijiunga na Mara Stars. Timu hiyo ilikuwa ikiongozwa na Suleiman Kigera.

Mwaka uliofuata, alirejeshwa Mwanza na kuitwa katika timu ya Taifa, Taifa Stars ilipokuwa ikijiandaa kwenda Malawi kucheza na timu ya taifa ya nchi hiyo katika mechi ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Afrika.

Hata hivyo, Amri hakuweza kusafiri na timu hiyo kwenda Malawi kutokana na kuumia mguu. Alisikitika kwa kupoteza nafasi hiyo, ambayo alisema kwa kawaida huwa ni ndoto ya kila mwanasoka katika maisha yake.

Baada ya kuzidi kung'ara katika kikosi cha Pamba, hatimaye Amri alinaswa na klabu ya Simba 1980. Binafsi anakiri kwamba, alikuwa na mapenzi na klabu hiyo tangu akiwa mdogo, hivyo ilipomuhitaji, hakujiuliza mara mbili.

"Viongozi wa Simba waliniona nina uwezo, maana wakati huo nilikuwa natisha katika namba zote mbili za kiungo na ushambuliaji. Nilikuwa na uwezo wa kucheza namba sita, nane, saba hadi 11,"alisema Amri, ambaye kwa kawaida ni mcheshi.

Mechi ya kwanza kuichezea Simba ilikuwa ya kirafiki dhidi ya Power Dynamos ya Russia. Katika mechi hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Simba ilichapwa mabao 3-2.

Wakati alipojiunga na Simba, kikosi cha timu hiyo kilikuwa kikiundwa na wachezaji tishio kama vile marehemu Jumanne Hassan 'Masimenti', marehemu Adam Sabu, Thuweni Ally, marehemu Athumani Mambosasa, George Kulagwa, Rahim Rumelezi, Nico Njohole, Abbas Kuka.

Amri alikuwa mmoja wa wachezaji walioiwezesha Simba kutwaa ubingwa wa Bra 1984. Alisema katika kipindi cha miaka saba alichoichezea Simba, mwaka huo pekee ndio ambao hakukuwepo migogoro ya uongozi.

"Niliichezea Simba katika kipindi ambacho ilikuwa ikikabiliwa na migogoro mingi. Mgogoro wa kwanza mkubwa ulizuka 1980 wakati huo, mwenyekiti alikuwa, marehemu Alfred Sanga. Baadaye akaingia David Ngonya. Mgogoro mkubwa zaidi ulizuka 1985 na kusababisha timu isambaratike,"alisema.

Anaikumba zaidi mechi ya ligi kati ya Simba na Yana iliyochezwa 1985 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, ambapo timu hizo zilitoka sare ya bao 1-1. Kinachomfanya aikumbuke mechi hiyo ni wachezaji wa timu zote mbili kucheza kwa kukamiana.

Kwa mujibu wa Amri, katika mechi hiyo, kipa Hamisi Kinye wa Yanga aliwachezea rafu mbaya washambuliaji Zamoyoni Mogella na Zuberi Magowa wa Simba na kuwasababishia maumivu makubwa.

Amri aliwahi kuwa kocha wa timu ya daraja la tatu ya Rhino ya Morogoro, ambayo aliiwezesha kufuzu kucheza ligi daraja la pili ngazi ya kanda.

Hata hivyo, aliamua kuacha kuifundisha timu hiyo kwa kile alichodai kuwa, kukatishwa tamaa na mfumo mpya wa ligi uliotangazwa na TFF, ambapo ligi za soka zitaanza kuchezwa katika ngazi ya wilaya, mkoa na Taifa.

"Nilikata tamaa. Niliiwezesha Rhino kupanda hadi daraja la pili ngazi ya taifa, lakini baada ya kutangazwa kwa mfumo huo, nimeona jitihada zangu ni sawa na kazi ya bure,"alisema.

"Unajua klabu zetu nyingi ni za mitaani, hazina vyanzo vya uhakika vya mapato, zinategemea michango ya wanachama, sasa sisi tulishalipa ada ya kucheza ligi daraja la pili, leo hii TFF inasema ligi zote zimefutwa. Nani angeturejeshea fedha zetu za ada ya ligi." alihoji.