KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, January 28, 2015

SIMBA YAPIGWA MWELEKA NA MBEYA CITY



TIMU ya soka ya Simba jana ilikwaa kisiki katika michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kukubali kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Mbeya City.

Katika mechi hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Simba ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 23 lililofungwa na mshambuliaji chipukizi Ibrahim Ajibu. Bao hilo lilidumu hadi mapumziko.

Mbeya City ilisawazisha bao hilo dakika ya 76 kupitiakwa Paul Nonga baada ya kufanyika kwa shambulizi kali kwenye lango la Simba.

Bao la pili na la ushindi la Mbeya City lilifungwa kwa njia ya penalti na Yussuf Abdalla baada ya kipa Manyika Peter wa Simba kudaka mguu wa Raphael Alfa ndani ya mita 18 badala ya mpira.


Tuesday, January 27, 2015

NSSF, REAL MADRID KUZALISHA VIPAJI VYA SOKA TANZANIA

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Dkt. Ramadhani Dau  akifafanua jambo kwa wageni waliohudhuria hafla fupi ya kusaini mkataba  kati ya shirika hilo na timu ya mpira wa miguu ya Real Madrid wa kuanzishwa kwa kituo cha michezo (sports academy) katika eneo la Kigamboni jijini Dar es Salaam. Dk. Dau alisema katika uendeshaji wa kituo hicho, Real Madrid itakua na dhamana ya kushughulikia masuala yote ya ufundi, kuwatambua wachezaji, chakula, wataalamu wa saikolojia na wataalamu wa viungo na kwamba wajibu wa shirika lake utakuwa kwenye kujenga tu.
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Dkt. Ramadhani Dau (aliyekaa kushoto) na Mkurugenzi wa Ufundi wa timu ya mpira wa miguu ya Real Madrid, Bw. Ruben De la Red Gutierrez (aliyekaa kulia) kwa pamoja wakisaini mkataba wa kuanzishwa kwa kituo cha michezo (sports academy) katika eneo la Kigamboni jijini Dar es Salaam. Wakishuhudia ni wawakilishi kutoka pande hizo mbili. Kituo hicho kitakua na uwezo wa kupokea wanafunzi 108 kwa wakati mmoja.
  
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Dkt. Ramadhani Dau (kushoto) na Mkurugenzi wa Ufundi wa timu ya mpira wa miguu ya Real Madrid, Bw. Ruben De la Red Gutierrez (kulia) wakibadilishana mikataba ya kuanzishwa kwa kituo cha michezo (sports academy) katika eneo la Kigamboni jijini Dar es Salaam. Wakishuhudia ni wawakilishi kutoka pande hizo mbili. Kituo hicho kitakua na uwezo wa kupokea wanafunzi 108 kwa wakati mmoja.

Mkurugenzi wa Ufundi wa timu ya mpira wa miguu ya Real Madrid, Bw. Ruben De la Red Gutierrez akifafanua jambo kwa wageni waliohudhuria hafla fupi ya kusaini mkataba  kati ya timu yake  na Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF) wa kuanzishwa kwa kituo cha michezo (sports academy) katika eneo la Kigamboni jijini Dar es Salaam. Kituo hicho kitahusisha wanafunzi 108 watakaogawanywa kwenye timu za chini ya umri wa miaka 13, 15, 17, 19, kikosi cha pili na timu ya wakubwa.


Na Mwandishi wetu

SHIRIKA la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) limeingia mkataba na klabu maarufu duniani ya Real Madrid ya Hispania wa kujenga kituo cha michezo kwa ajili ya kuzalisha vipaji.

Akizungumza katika hafla ya kusaini mkataba huo wa miaka 18, Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Dk Ramadhani Dau alisema ujenzi huo utagharimu Sh bilioni 16 na unatarajiwa kuanza kujengwa Mei mwaka huu na kwamba utakamilika baada ya miezi 18.

Dk Dau alisema kituo hicho ambacho kitajengwa kwenye kijiji cha michezo cha shirika hilo (NSSF Sports City), kitakuwa eneo la Mwasoga, Kigamboni, Dar es Salaam.

“Tuna eneo la zaidi ya ekari 400 ambapo tutajenga viwanja, shule ya michezo, nyumba za kuishi na maduka. Lengo letu tuzalishe na kuuza wachezaji. Tunakusudia kuwa na timu ya vijana chini ya umri wa miaka 13, 18, 20, timu B na timu ya wakubwa,” alisema Dk Dau.

Alisema utekelezaji wa kituo hicho utaanza hivi karibuni kwa kutumia majengo ya kukodi wakati wakisubiri ujenzi kukamilika.

“Hivi hapa baada ya kusaini mkataba, utekelezaji utaanza kwa kutumia majengo ya kukodi ambayo tunadhani yatakuwa maeneo ya Temeke na tutakuwa tukitumia viwanja vya Karume na Uhuru,” alisema.

Mkurugenzi Mkuu huyo wa NSSF alisema katika kuendesha kituo hicho, kila kitu kitafanywa na Real Madrid kuanzia masuala yote ya ufundi, kuwatambua wachezaji, chakula, wataalamu wa saikolojia na wataalamu wa viungo na kwamba wajibu wa shirika lake utakuwa kwenye kujenga tu.

“Sisi tunachukulia huu mradi ni uwekezaji na hatufanyi hisani, itazingatia misingi ya biashara na faida kubwa ni kwamba NSSF itaongeza kipato, lakini pia kituo kitatumika kuitangaza Tanzania kwa sababu yatakayofanyika yataoneshwa kwenye televisheni ya Real Madrid,” alifafanua Dk Dau.

“Lakini pia wakati umefika sasa kwa Tanzania kushiriki Kombe la Dunia Qatar 2022, kama unaandaa vizuri vijana wa miaka 13 sasa mpaka mwaka 2020 wanaweza kuwakilisha vizuri kwenye mechi za kufuzu na mwaka 2022 wakashiriki Kombe la Dunia, wakikosa la Qatar, basi hata hizo zinazokuja, hiyo pia ni moja ya madhumuni ya kituo hicho.”

Akizungumzia namna walivyofikia uamuzi wa kujenga kituo, Dk Dau alisema wazo hilo lilipatikana Agosti mwaka jana na kisha likapelekwa kwenye Mkutano wa Wanachama uliofanyika Arusha ambako waliazimia NSSF iwekeze rasmi kwenye michezo kabla ya kuwasilishwa kwenye bodi na utekelezaji kuanza kufanyika.

“Tulitembelea sehemu nyingi kuona wenzetu wanafanyaje. Binafsi nilitembelea nchi kadhaa za Ulaya, nilienda kituo cha Manchester United, Sunderland, Real Madrid kwa hapa Afrika nilikwenda Asec Mimosas (Ivory Coast) na TP Mazembe (Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC) kuona wanafanyaje, ziara ikazaa matunda kwani tulikubaliana na Madrid na ndio wamekuja kusaini mkataba leo (jana),” alifafanua Dk Dau.

Naye Mkuu wa Vituo vya Michezo wa Real Madrid, Rayco Garcia aliishukuru NSSF wa kuwa na mpango huo na kuahidi kufanya kazi ili kuipatia Tanzania mafanikio.

“Tukifanikiwa kuwatoa vijana hao, Tanzania itaweza kushiriki kwenye michuano mikubwa kama alivyosema Dk Dau, inabidi tufanye kazi ili vijana wafanikiwe, wafike mbali,” alisema Garcia.

Mbali na Garcia ambaye pia ni kocha wa timu ya vijana chini ya umri wa miaka 18 ya Madrid, wengine walioambatana kwenye msafara huo ni Mkurugenzi wa Ufundi wa Klabu hiyo, Ruben de la Red, Kocha Mkuu wa timu za vijana, Francisco Martin Ramos na Juan Jose San Roman Milla. Mwaka jana, wachezaji wa zamani wa Real Madrid walifanya ziara nchini

Monday, January 26, 2015

SIMBA, AZAM HAKUNA MBABE, OKWI APOTEZA FAHAMU UWANJANI


TIMU za soka za Simba na Azam jana zilishindwa kutambiana baada ya kutoka sare ya bao 1-1 katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Simba ilikuwa ya kwanza kupata bao kipindi cha kwanza kupitia kwa Emmanuel Okwi kabla ya Azam kusawazisha kipindi cha pili kupitia kwa Kipre Tchetche.

Katika mechi hiyo, timu zote mbili zilicheza kwa kasi huku kila moja ikipania kutoka uwanjani na ushindi.

Wakati huo huo, mshambuliaji Emmanuel Okwi wa Simba jana alipoteza fahamu uwanjani baadaya kupigwa kiwiko na mchezaji mmoja wa Azam.

Kutokana na tukio hilo, Okwi alilazimika kukimbizwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, ambako alilazwa na kuruhusiwa baada ya saa kadhaa.

Akizungumzia tukio hilo, daktari wa Simba, Salim Gembe, alisema mshambuliaji huyo amenusurika kufa.

"Okwi aligongwa kiwiko nyuma ya kichwa kwenye mishipa ya fahamu, kwa hiyo akapoteza
fahamu uwanjani. Ilikuwa mbaya sana, angeweza kupoteza maisha, lakini hali ile tuliidhibiti
wakati tunampa huduma ya kwanza uwanjani,”alisema.

“Baada ya hapo, tukaingia naye ndani kwenye zahanati ndogo ya uwanja, kuendelea kumpa tiba
hadi fahamu zikamrejea, lakini hali yake haikuwa nzuri sana, ikabidi tumkimbize Muhimbili,
ambako baada ya tiba ya takriban saa mbili, sasa yuko vizuri,”amesema Gembe.

Sunday, January 25, 2015

MRWANDA AIBEBA YANGA, YAICHAPA POLISI MORO BAO 1-0

Na Mwandishi Wetu, Morogoro

YANGA jana ilirejesha imani kwa mashabiki wake baada ya kuichapa Polisi Moro bao 1-0 katika mechi ya ligi kuu ya soka ya Tanzania Bara, iliyochezwa kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.

Mshambuliaji Danny Mrwanda ndiye aliyeifungia Yanga bao hilo la pekee dakika ya 42, akimalizia mpira uliopanguliwa na kipa Tony Kavishe, kufuatia shuti la Simon Msuva.

Kutokana na ushindi huo, Yanga sasa imechupa nafasi ya pili katika msimamo wa ligi hioyo, ikiwa na pointi 18 baada ya kucheza mechi 10. Azam inaendelea kuongoza ikiwa na pointi 20.

Katika mechi hiyo, Yanga ilicheza vizuri kipindi cha kwanza, lakini tatizo kubwa lilikuwa umaliziaji mbovu wa washambuliaji wake.

Yanga SC ilicheza vizuri kipindi cha kwanza, lakini ugonjwa wa kukosa mabao ya wazi ulijirudia kabla ya Mrwanda kuupatia tiba mwishoni mwa kipindi hicho.

Polisi ilizinduka katika kipindi cha pili na kufanya mashambulizi kadhaa kwenye lango la Yanga, ikiongozwa na Saidi Bahanuzi, lakini haikuwa na bahati ya kupata bao.

Saturday, January 24, 2015

6 ZAFUZU KUCHEZA ROBO FAINALI KOMBE LA TAIFA WANAWAKE


Timu za mikoa sita tayari imepata tiketi za kucheza robo fainali ya michuano ya Kombe la Taifa la Wanawake itakayoanza Januari 26 mwaka huu jijini Dar es Salaam wakati nyingine mbili zinajulikana leo (Januari 23 mwaka huu).

Mikoa ambayo timu zake tayari zina tiketi za robo fainali ya michuano hiyo inayodhaminiwa na kampuni ya Proin ni Ilala, Kigoma, Mwanza, Pwani, Tanga na Temeke.

Matokeo ya mechi za leo kati ya Iringa na Ruvuma, na ile kati ya Mbeya na Katavi ndiyo yatakayoamua ni timu zipi mbili kati ya hizo zinakwenda Dar es Salaam kucheza robo fainali.

Timu zote zilizofuzu hatua ya robo fainali zinatakiwa kuripoti Dar es Salaam keshokutwa (Januari 25 mwaka huu). Fainali ya michuano hiyo itachezwa Februari Mosi mwaka huu.

Wednesday, January 21, 2015

KLABU KUJIGHARAMIA HOTELI MICHUANO YA CAF

Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limefanyia marekebisho kanuni zake za michuano ya ngazi ya klabu kwa upande wa malazi ambapo sasa timu zitachagua na kujilipia zenyewe hoteli zinapokuwa kwenye mechi za ugenini.

Kabla ya marekebisho ya kanuni hiyo, timu ngeni ilikuwa ikilipiwa hoteli na timu mwenyeji kwa msafara usiozidi watu 25. CAF ilikuwa imepitisha hoteli maalumu katika kila nchi ambapo mwenyeji alitakiwa kuziweka timu ngeni.

Kwa marekebisho hayo, Chama cha Mpira wa Miguu cha nchi mwenyeji kitakuwa na wajibu wa kuitafutia hoteli timu ngeni iwapo tu kitaombwa kufanya hivyo, lakini jukumu la kulipia malazi litakuwa la timu yenyewe.

Mwaka huu Tanzania inawakilishwa na timu mbili za Azam na Yanga katika michuano ya CAF. Azam inacheza Ligi ya Mabingwa (CL) ambapo itaanzia nyumbani Februari 15 mwaka huu kwa kuikaribisha El Merreikh ya Sudan kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam.

Nayo Yanga itacheza michuano ya Kombe la Shirikisho (CC), na imepangiwa kucheza mechi ya kwanza nyumbani dhidi ya BDF IX ya Botswana. Mechi hiyo itafanyika Februari 14 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Tuesday, January 20, 2015

WACHEZAJI, VIONGOZI 12 KUHUKUMIWA NA KAMATI YA NIDHAMU YA TFF


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limewapeleka wanamichezo 12 wakiwemo viongozi, makocha na wachezaji kwenye Kamati ya Nidhamu kwa ajili ya kuchukuliwa hatua za kinidhamu kutokana na matukio mbalimbali kwenye Ligi Daraja la Kwanza (FDL) na michuano ya Kombe la Taifa la Wanawake.

Wachezaji Dihe Makonga, Swalehe Idd Hussein, Ramadhan Mwinyimbegu na Shaibu Nayopa wa Oljoro JKT, na Nassib Lugusha wa Polisi Dodoma wanalalmikiwa katika Kamati ya Nidhamu kwa kushambulia waamuzi na kufanya vurugu kwenye benchi la timu pinzani katika mechi zao za FDL.

Mtunza Vifaa (Kit Manager) wa Polisi Mara, Clement Kajeri analalamikiwa kwa kuongoza mashambulizi dhidi ya waamuzi kwenye mechi kati ya timu yake na Mwadui iliyochezwa Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma.

Naye Mtunza Vifaa (Kit Manager) wa Rhino Rangers, Albert Mbunji anapelekwa katika Kamati hiyo kwa kupinga maamuzi na kuwatukana waamuzi kwenye mechi dhidi ya Polisi Dodoma iliyochezwa Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.

Pia Mtunza Vifaa (Kit Manager) wa Oljoro JKT, Eliud Justine Mjarifu analalamikiwa kwa matukio mawili; alimpiga Kocha wa Burkina Faso, CR Mwakambaya kwenye mechi ya FDL iliyochezwa Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro. Pia alimtukana mwamuzi akiba (fouth official) Mussa Magogo kwenye mechi dhidi ya Toto Africans iliyochezwa Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Kocha wa Polisi Tabora, Kim Christopher analalamikiwa kwa kumtolea mlugha chafu mwamuzi wa mechi kati ya timu yake na Panone FC iliyochezwa Uwanja wa Ushirika mjini Moshi.

Msimamizi wa Kituo cha Musoma, Katibu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Mara (FAM), Mugisha Galibona naye anapelekwa katika Kamati ya Nidhamu kwa tuhuma za kutotoa ushirikiano kwa maofisa wa mechi na kuchochea maofisa hao (waamuzi) kupigwa.

Kwa upande wake, Kamati ya Mpira wa Miguu wa Wanawake ya TFF imependekeza Katibu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Simiyu, Emmanuel Sologo, na Kaimu Katibu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Singida (SIREFA), Gabriel Gunda kupelekwa kwenye kamati ya Nidhamu kwa matukio mbalimbali yaliyojitokeza kwenye mechi za Kombe la Taifa la Wanawake.

Sologo anatuhumiwa kumpiga kibao mwamuzi wa mechi ya marudiano kati ya timu yake ya Simiyu na Shinyanga iliyochezwa mjini Shinyanga, tukio ambalo lilimfanya mwamuzi huyo avunje mchezo.

Naye Gunda analalamikiwa kwa kushindwa kuhakikisha timu yake ya Singida inaingia uwanjani kwenye mechi ya marudiano dhidi ya Dodoma iliyokuwa ifanyike kwenye Uwanja wa Namfua mjini Singida.

SDL KUANZA MZUNGUKO WA PILI JANUARI 31
Mzunguko wa pili wa Ligi Daraja la Pili (SDL) sasa utaanza Januari 31 mwaka huu, badala ya Januari 24 mwaka huu kama ilivyopangwa awali ili kutoa fursa kwa Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kupitia usajili wa dirisha dogo.

Timu zinazocheza ligi hiyo katika makundi manne tofauti ni; Milambo FC, Mji Mkuu FC (CDA), Mvuvumwa FC, Singida United, na Ujenzi Rukwa (Kundi A), Arusha FC, Bulyanhulu FC, JKT Rwamkoma FC, Mbao FC, na Pamba SC (Kundi B).

Nyingine ni Abajalo FC, Cosmopolitan, Kariakoo Lindi, Kiluvya United, Mshikamano FC, na Transit Camp (Kundi C), wakati Kundi D ni Magereza Iringa, Mji Njombe, Mkamba Rangers, Town Small Boys, Volcano FC, na Wenda FC.

WACHEZAJI WAWILI WA LIGI KUU NA FDL WATOZWA FAINI


Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imewapiga faini na kuwafungia mechi wachezaji wawili wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) na Ligi Daraja la Kwanza (FDL) kwa kufanya vitendo kinyume na kanuni zinazotawala ligi hizo.

Mshambuliaji Haruna Chanongo wa Stand United amefungiwa mechi tatu na kupigwa faini ya sh. 500,000 kwa kumpiga teke mwamuzi wa mechi dhidi ya Polisi Morogoro iliyochezwa Januari 3 mwaka huu Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro. Adhabu hiyo imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 37(3) ya Ligi Kuu.

Kipa Amani Simba wa Oljoro JKT amepigwa faini ya sh. 300,000 kwa kukataa kupeana mkono na viongozi wakati wa kusalimia kabla ya kuanza mechi kati ya timu yake na Toto Africans iliyofanyika jijini Mwanza. Adhabu hiyo imetolewa kwa mujibu wa kanuni ya 14 ya FDL.

Timu ya Polisi Mara imepigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na vurugu za washabiki wake wakati wa mechi ya FDL dhidi ya Mwadui ya Shinyanga iliyochezwa Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma. Pia Polisi Tabora imepigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na vurugu za washabiki wake kwenye mechi namba 40 dhidi ya Geita Gold, adhabu ambazo zimetolewa kwa mujibu wa kanuni ya 41.

Sunday, January 18, 2015

MTIBWA SUGAR YAPUNGUZWA KASI NA JKT RUVU



MTIBWA Sugar imepunguzwa kasi baada ya kulazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na JKT
Ruvu katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Azam Complex,
Chamazi, Dar es Salaam jana.

Matokeo hayo yanairejesha Mtibwa kileleni baada ya kufikisha pointi 17, baada ya mechi tisa,
sawa na mabingwa watetezi, Azam FC, lakini timu ya Manungu inapandishwa kwa wastani wa
mabao.

JKT Ruvu imefikisha pointi 17 pia baada ya mechi 11, lakini inabaki nafasi ya tatu mbele ya vigogo
Yanga pointi 15 na Simba 12.

JKT ndiyo waliokuwa wa kwanza kupata bao dakika ya saba, mfungaji Samuel Kamuntu ambaye
aliuwahi mpira uliotemwa na kipa Said Mohammed Kasarama.

Mtibwa walifanikiwa kusawazisha bao hilo dakika ya 36, mfungaji Ame Ally aliyemalizia kwa
kichwa kona iliyochongwa na Shijja Kichuya.

Katika mchezo mwingine wa ligi hiyo jana, Coastal Union imelazimishwa sare ya bila kufungana
na Polisi Moro Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

SIMBA, AZAM ZASHINDA LIGI KUU, YANGA YABANWA

SIMBA jana ilizoa pointi zote tatu kutoka kwa Ndanda FC baada ya kuichapa mabao 2-0 katika mechi ya ligi kuu ya soka ya Tanzania Bara iliyochezwa kwenye Uwanja wa Nangwande Sijaona mjini Mtwara.

Ushindi huo ni wa pili kwa Simba tangu ligi hiyo ilipoanza na umepokelewa kwa faraja kubwa na mashabiki wa timu hiyo baada ya kuishuhudia timu yao ikipata sare saba mfululizo na kupoteza mechi moja.

Mabao ya Simba yalifungwa na Dan Ssenkuruma dakika ya 26 aliyemalizia kwa shuti la mguu wa kushoto krosi kutoka kwa Ramadhani Singano 'Messi'.

Bao la pili lilifungwa na Elias Maguri dakika ya 68 baada ya kumalizia pasi kutoka kwa Ssenkuruma.

Mabingwa watetezi wa ligi hiyo,Azam walijikita kileleni mwa ligi hiyo baada ya kuichapa Stand United bao 1-0 mjini Shinyanga.

Bao pekee na la ushindi la Azam lilifungwa na kiungo Frank Dumayo, ambaye ilikuwa mechi yake ya kwanza ya ligi kwa timu hiyo baada ya kuwa majeruhi kwa muda mrefu.

Nayo timu kongwe ya Yanga ilishindwa kutamba mbele ya Ruvu Shooting baada ya kulazimishwa kutoka suluhu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

SIMBA, YANGA KURUDIANA MACHI 8


Ratiba ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) imeingizwa mechi za viporo zilizotokana na timu za Azam,

Mtibwa Sugar na Simba kucheza michuano ya Kombe la Mapinduzi 2015 iliyomalizika wiki hii
kisiwani Zanzibar.

Vilevile mechi za viporo zimeingizwa kwa kuzingatia ushiriki wa timu za Azam kwenye Ligi ya
Mabingwa Afrika (CL) na Yanga kwenye Kombe la Shirikisho (CC) pamoja na mechi za kirafiki za
Taifa Stars.

Yanga itacheza na BDF ya Botswana kwenye mchezo utakaofanyika Februari 14 mwaka huu
Uwanja wa Taifa wakati Azam itaikabili El Merreikh ya Sudan kwenye Uwanja wa Azam Complex,
Februari 15 mwaka huu.

Mechi za viporo itakuwa kama ifuatavyo; Januari 20- Kagera Sugar na Azam (Mwanza),
Januari 28- Simba na Mbeya City (Dar es Salaam), Februari 4- Coastal Union na Yanga
(Tanga), Februari 11- Azam na Mtibwa Sugar (Dar es Salaam) na Februari 11- Mgambo Shooting
na Simba (Tanga).

Februari 11- Yanga na Ndanda (Dar es Salaam), Februari 21- Mbeya City na Yanga (Mbeya),
Februari 25- Mtibwa Sugar na Tanzania Prisons (Morogoro), Februari 28- Simba na Mtibwa
Sugar (Dar es Salaam), Machi 4- Ruvu Shooting na Azam (Pwani), na Machi 4- JKT Ruvu na
Yanga (Dar es Salaam).

Machi 4- Mtibwa Sugar na Polisi Morogoro (Morogoro), Machi 8- Simba na Yanga (Dar es
Salaam), Machi 11 Azam na Mbeya City (Dar es Salaam), Machi 11- Yanga na Kagera Sugar (Dar
es Salaam), Machi 18- Azam na Ndanda (Dar es Salaam), Machi 18- Yanga na Stand United (Dar
es Salaam), Aprili 8- Simba na Tanzania Prisons (Dar es Salaam).

AMAVUBI KUTUA MWANZA JAN 21


Timu ya Taifa ya Rwanda (Amavubi) inawasili Mwanza, Januari 21 mwaka huu kwa ajili ya mechi
ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya Taifa Stars Maboresho itakayochezwa kwenye Uwanja wa CCM
Kirumba jijini humo.

Amavubi yenye msafara wa watu 26, wakiwemo wachezaji, benchi la ufundi na viongozi
itawasili kwa ndege ya RwandAir na siku hiyo hiyo jioni itafanya mazoezi kwenye Uwanja wa CCM
Kirumba. Timu hiyo itafikia kwenye hoteli ya JB Belmont.

Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager inaingia kambini keshokutwa (Januari 18
mwaka huu), na siku inayofuata itakwenda Mwanza tayari kwa ajili ya mechi hiyo itakayofanyika
Januari 22 mwaka huu.

Kikosi hicho cha Kocha Mart Nooij ambacho ni sehemu ya maandalizi ya mechi za mchujo za
michuano ya Afrika kwa Wachezaji wanaocheza Ligi za Ndani (CHAN) kinaundwa na wachezaji
26.

MICHUANO YA KOMBE LA TAIFA WANAWAKE YAINGIA RAUNDI YA PILI




Michuano ya Kombe la Taifa kwa Wanawake inaingia raundi ya pili kesho (Januari 17 mwaka
huu) kwa mechi za kwanza za raundi hiyo zitakazochezwa katika miji ya Bukoba, Arusha,
Mlandizi, Dar es Salaam na Katavi.

Jijini Dar es Salaam kutakuwa na mechi mbili ambapo mkoa wa kisoka wa Ilala utacheza na
Mtwara kwenye Uwanja wa Karume, wakati Uwanja wa Chuo cha Bandari uliopo Tandika
utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Temeke na Dodoma.

Mechi nyingine za michuano hiyo inayodhaminiwa na kampuni ya Proin zitakuwa kati ya Kagera
na Mwanza itakayochezwa mjini Bukoba, Arusha na Tanga (Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri
Abeid), Pwani na Kinondoni (Uwanja Mabatini, Mlandizi), na Katavi na Mbeya zitakazoonesha kazi
kwenye Uwanja wa Azimio.

Nazo Ruvuma na Iringa zitacheza Januari 19 mwaka huu kwenye Uwanja wa Majimaji. Mechi
hiyo itachezwa tarehe hiyo ili kusubiri matokeo ya mechi ya marudiano kati ya Shinyanga na
Simiyu.

Kamati ya Mpira wa Miguu wa Wanawake ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
ilikutana jana (Januari 15 mwaka huu) kupitia ripoti ya mechi ya marudiano ya raundi ya kwanza
kati ya Shinyanga na Simiyu ambayo ilivunjwa na mwamuzi katika daika ya 70.

Baada ya kupitia ripoti, Kamati imebaini kuwa licha ya vurugu alizofanyiwa mwamuzi, bado
mechi hiyo ingeweza kuendelea kwa kuchezeshwa na mwamuzi wa akiba kwa vile usalama
ulikuwepo baada ya yeye kupigwa.

Pia Kamati imeagiza Katiba wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Simiyu, Emmanuel Sologo
aliyeripotiwa kumpiga mwamuzi suala lake lipelekwe kwenye Kamati ya Nidhamu ya TFF kwa
hatua zaidi, wakati Kocha wa Simiyu, Emmanuel Babu ambaye naye alishiriki kumpiga mwamuzi
amesimamishwa wakati akisubiri kuchukua hatua zaidi.

Kamishna wa mechi hiyo Idd Mbwana, na mwamuzi Joseph Pombe wamefungiwa kwa miaka
miwili.

Mechi kati ya Shinyanga na Simiyu itamaliziwa dakika kumi zilizobaki kesho (Januari 17 mwaka
huu) mjini Shinyanga. Kila chama cha mkoa kitabeba gharama zake katika uendeshaji wa mechi
hiyo ambayo mwenyeji ni Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Shinyanga (SHIREFA).

Timu itakayosonga mbele baada ya mechi hiyo itacheza mechi ya kwanza ya raundi ya pili
ugenini Januari 19 mwaka huu dhidi ya Kigoma. Mechi za marudiano za raundi ya pili
zitachezwa kati ya Januari 21 na 22 mwaka huu.

Hatua ya robo fainali hadi fainali ambayo mechi zake zitachezewa jijini Dar es Salaam itaanza
Januari 26 mwaka huu. Fainali itachezwa Februari Mosi mwaka huu.

Vilevile Kamati ya Mpira wa Miguu wa Wanawake ya TFF imemfungia kwa miaka miwili Kaimu
Katibu Mkuu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Singida (SIREFA), Gabriel Gunda kwa
kushindwa kuingiza timu yake uwanjani kwenye mechi ya marudiano ya raundi ya kwanza dhidi
ya Dodoma iliyokuwa ichezwe kwenye Uwanja wa Namfua mjini Singida.

Thursday, January 15, 2015

NOOIJ KUTAJA KIKOSI CHA TAIFA STARS MABORESHO



Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Mart Nooij anatarajia kutaja kikosi cha Maboresho kitakachoingia kambini Januari 18 mwaka huu kujiandaa kwa mechi ya kirafiki dhidi ya Rwanda itakayofanyika Januari 22 mwaka huu jijini Mwanza.

Nooij atataja kikosi hicho kwenye mkutano na waandishi wa habari utakaofanyika kesho (Januari 15 mwaka huu) saa 5 asubuhi kwenye ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Uwanja wa Karume.


RAUNDI YA PILI TAIFA CUP WANAWAKE JUMAMOSI
Mechi za kwanza za raundi ya pili ya mashindano ya Taifa ya mpira wa miguu kwa wanawake (Taifa Cup Wanawake) zinachezwa wikiendi hii (Januari 17 mwaka huu) kwenye miji minane tofauti nchini.

Timu tisa zilizofuzu kutoka raundi ya kwanza baada ya mechi za nyumbani na ugenini akiwemo mshindwa bora (best loser) zitaungana na Ilala, Kinondoni na Temeke kucheza raundi ya pili. Mechi za marudiano za raundi hiyo zitachezwa Januari 21 mwaka huu.

Hatua ya robo fainali itakayochezwa Januari 26 na 27 mwaka huu pamoja na nusu fainali na fainali ya michuano hiyo inayodhaminiwa na Proin Promotions itafanyikia jijini Dar es Salaam.

RAMBIRAMBI MSIBA WA STEPHEN NSOLO

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko taarifa ya msiba wa Katibu Mkuu wa zamani wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Shinyanga (SHIREFA) uliotokea jana (Januari 13 mwaka huu) jijini Mwanza.

Msiba huo ni pigo kwa wadau wa mpira wa mpira wa miguu kwani wakati wa uhai wake, Nsolo alitoa mchango mkubwa akiwa kiongozi. Aliongoza SHIREFA akiwa Katibu kuanzia mwaka 1975 hadi 1994.

Kabla ya hapo alikuwa Katibu wa Chama cha Mpira wa Miguu Wilaya ya Shinyanga kwa kipindi cha miaka kumi. Pia aliwahi kuwa mwamuzi wa daraja la kwanza na kamishna wa mpira wa miguu kwa muda mrefu.

TFF inatoa salamu za rambirambi kwa familia ya marehemu, SHIREFA na Chama cha Waamuzi wa Mpira wa Miguu Tanzania (FRAT) na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu kwa msiba huo.

Marehemu anatarajiwa kuzikwa leo (Januari 14 mwaka huu) katika makaburi ya Shinyanga Mjini. Bwana alitoa, Bwana ametwaa. Jina lake lihimidiwe.

POLISI MARA YAZUIWA KUCHEZA UWANJA WA KARUME


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeizuia timu ya Polisi Mara kutumia Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma kwa mechi zake za Ligi Daraja la Kwanza (FDL) kuanzia leo mpaka hapo itakapotangazwa vinginevyo.

Uamuzi huo umechukuliwa kutokana na matukio ya vurugu na uvunjifu wa amani ambayo yamekuwa yakitokea kwenye mechi za FDL zinazochezwa kwenye uwanja huo, ikiwemo ile ya Jumamosi iliyopita dhidi ya Mwadui ya Shinyanga ambapo waamuzi walipigwa.

Kamati zinazohusika zitakutakana hivi karibuni kupitia matukio yote ya utovu wa nidhamu kwenye FDL, na hatua kali zitachukuliwa kwa wahusika ikiwemo na viwanja ambavyo vimekuwa na sifa ya vurugu.

Vyama vya mpira wa miguu vya mikoa vina wajibu wa kutoa ulinzi wa kutosha viwanjani wakati wa mechi.

TANZANIA KUIKABILI KENYA BEACH SOCCER AFRICA



Timu ya Taifa ya Tanzania ya mpira wa ufukweni (beach soccer) imepangiwa kucheza na Kenya katika raundi ya kwanza ya michuano ya Afrika kwa ajili ya fainali za Afrika za michuano hiyo zitakazofanyika Aprili mwaka huu nchini Shelisheli.

Mwenyekiti wa Kamati ya Beach Soccer, Ahmed Idd Mgoyi amesema jijini Dar es Salaam, leo kuwa Tanzania itaanzia ugenini ambapo mechi ya kwanza itachezwa kati ya Februari 13 na 15 mwaka huu nchini Kenya.

Mechi ya marudiano itafanyikaa nchini kati ya Februari 20 na 22 mwaka huu. Iwapo timu ya Tanzania itasonga mbele, katika raundi ya pili itacheza na Misri ikianzia nyumbani kati ya Machi 13 na 15 mwaka huu.

Mgoyi alisema maandalizi ya Tanzania kushiriki kwenye mashindano hayo yameanza ambapo timu ya Tanzania Bara itacheza na Zanzibar ikiwa ni sehemu ya mchakato wa kupata kikosi kimoja kitakachoingia kwenye michuano hiyo ya Afrika.

Alisema benchi za ufundi la timu ya Tanzania litaongozwa na John Mwansasu wakati Msaidizi wake ni Ali Shariff 'Adolf' kutoka Zanzibar, na Meneja wa timu hiyo ni George Lucas. Wote hao walishiriki kwenye kozi ya ukocha wa beach soccer iliyoendeshwa mwaka jana nchini na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).

Kocha Mwansasu atatangaza timu ya Tanzania Bara, Januari 19 mwaka huu, na mazoezi ya pamoja na timu ya Zanzibar yatafanyika Januari 24 na 25 mwaka huu.

Wachezaji wa timu ya Tanzania Bara watatokana na michuano ya beach soccer iliyofanyika mwaka jana ikishirikisha timu za vyuo vya elimu ya juu vya Mkoa wa Dar es Salaam.

SIMBA BINGWA KOMBE LA MAPINDUZI


TIMU kongwe ya soka ya Simba jana ilitwaa ubingwa wa michuano ya Kombe la Mapinduzi baada ya kuichapa Mtibwa Sugar kwa penalti 5-4 katika mechi ya fainali iliyopigwa kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
Mshindi wa pambano hilo ilibidi apatikane kwa njia ya penalti tano tano baada ya timu hizo kumaliza dakika 90 zikiwa suluhu.
Kipa Ivo Mapunda, aliyeingia dakika za mwisho ndiye aliyeibuka shujaa wa Simba baada ya kupangua penalti ya mwisho ya Mtibwa iliyopigwa na Vicent Barnabas.
Pambano hilo lilikuwa kali na gumu kutokana na kila timu kupania kushinda ili kuibuka na ubingwa.
Katika michuano hiyo, mshambuliaji Simon Msuva aliibuka kuwa mfungaji bora baada ya kupachika wavuni mabao manne na kumpiku mshambuliaji chipukizi wa Simba, Ibrahim Hijabu, aliyefunga mabao matatu.
Kipa Saidi Mohamed wa Mtibwa Sugar aliibuka kuwa kipa bora wa michuano hiyo wakati beki Salim Mbonde wa Mtibwa Sugar aliibuka kuwa mwanasoka bora.

Tuesday, January 13, 2015

RONALDO ASHINDA TENA TUZO YA MWANASOKA BORA WA DUNIA 2014



 
 
 
 
MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Ureno na klabu ya Real Madrid ya Hispania, Cristiano Ronaldo,

amechaguliwa kuwa mwanasoka bora wa dunia kwa mwaka 2014.

Hii ni mara ya tatu kwa mshambuliaji huyo wa zamani wa klabu ya Manchester United ya
England kushinda tuzo hiyo.

Mara baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa tuzo hiyo, Ronaldo alishangilia kwa staili ya aina
yake kabla ya kwenda kwenye kipaza sauti na kutoa hotuba ya shukurani.

" Naweza kumuona mama yangu, familia yangu. Napenda kuwashukuru wote walionipigia kura, kocha wangu, wachezaji wenzangu na rais wa klabu yangu,"alisema.

Ronaldo alishinda tuzo hiyo baada ya kupata asilimia 37.66 ya kura zilizopigwa na kumbwaga
Lionel Messi, aliyepata asilimia 15.76 na Manuel Neuer aliyepata asilimia 15.72.

Mshambuliaji huyo alikabidhiwa tuzo yake na mwanasoka nyota wa zamani wa Arsenal na
Ufaransa, Thierry Henry.

MTEMVU AIAHIDI VYOMBO VIPYA VYA MUZIKI SIKINDE


MBUNGE wa Jimbo la Temeke (CCM), Abbas Mtemvu (kushoto), akizungumza na wanamuziki wa bendi ya Mlimani Park Orchestra 'Sikinde' wakati wa hafla ya kuwapongeza wenyeviti wapya wa serikali za mitaa, iliyofanyika juzi kwenye ukumbi wa Kata ya 15, Temeke, Dar es Salaam. Wengine pichani ni  wanamuziki wa bendi hiyo, Hassan Bitchuka, Mbaraka Othman na Ramadhani Mapesa. (Picha na Emmanuel Ndege).

Na Emmanuel Ndege

MBUNGE wa Jimbo la Temeke (CCM), Abbas Mtemvu, ameahidi kuinunulia vyombo vipya vya muziki bendi ya muziki wa dansi ya Mlimani Park Orchestra 'Sikinde'.

Mtemvu alitoa ahadi hiyo juzi wakati wa sherehe za kuwapongeza wenyeviti wapya wa serikali za mitaa kutoka CCM waliochaguliwa katika uchaguzi uliofanyika Desemba 14, mwaka huu.

Katika sherehe hizo zilizofanyika kwenye ukumbi wa Kata ya 15, Temeke, Dar es Salaam, bendi za Sikinde, Msondo Ngoma na kikundi cha taarab cha Mashauzi Classic vilitoa burudani.

Mtemvu alisema ameamua kuinunulia vyombo vipya bendi hiyo, kutokana na maombi aliyoyapata kutoka kwa wanamuziki wake.

Mbunge huyo aliwahi kuwa mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi ya Shirika la Uchumi na Maendeleo la mkoa wa Dar es Salaam (DDC), lililokuwa likiimiliki bendi hiyo, ambapo pia aliwahi kuinunulia vyombo vya muziki.

"Viongozi wa Sikinde waliwahi kuniomba niwanunulie vyombo vipya na nilikuwa tayari kufanya hivyo, lakini ufuatiliaji wao haukuwa mzuri. Kwa vile mmewasilisha tena ombi hilo leo (juzi), naahidi kufanya hivyo hivi karibuni,"alisema Mtemvu huku akishangiliwa na wanamuziki wa bendi hiyo.

Kwa mujibu wa Mtemvu, atatekeleza ahadi hiyo wiki ijayo na aliwataka wanamuziki wa bendi hiyo kujituma zaidi ili waweze kupata mafanikio makubwa zaidi.

Kiongozi wa bendi hiyo, Abdalla Hemba, alimshukuru Mtemvu kwa kulikubali ombi lao na kuahidi kuvitumia vyombo hivyo kuongeza ufanisi zaidi ili waweze kufika matawi ya juu zaidi.

Wakati huo huo, bendi ya Mlimani Park, imeamua kuwarejesha kundini wanamuziki wake wa zamani, mpiga solo Gasper Kanuti na mwimbaji Eddo Sanga.

Hemba alisema juzi kuwa, Kanuti alitambulishwa rasmi mwishoni mwa wiki iliyopita wakati Eddo atatambulishwa Jumapili ijayo.

Monday, January 12, 2015

SIMBA, MTIBWA SUGAR KUWANIA KOMBE LA MAPINDUZI KESHO



TIMU za soka za Simba na Mtibwa Sugar, zinatarajiwa kushuka dimbani kesho kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar, kumenyana katika mechi ya fainali ya michuano ya Kombe la Mapinduzi.

Pambano hilo linalosubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa soka nchini, linatarajiwa kuwa na ushindani mkali kwa vile kila timu itapania kushinda ili kuibuka na ubingwa.

Simba ilifuzu kucheza fainali baada ya kuichapa Polisi Zanzibar bao 1-0 wakati Mtibwa Sugar iliitoa JKU kwa njia ya penalti tano tano baada ya kumaliza dakika 90 zikiwa sare.

Akizungumzia pambano hilo, Kocha Mkuu wa Simba, Goran Kopunovic, alisema hana wasiwasi wa timu yake kutwaa ubingwa.

Kocha huyo kutoka Serbia alisema, timu yake ipo imara na hawana hofu na wapinzani wao kwa vile wana uhakika mkubwa wa kutwaa ubingwa.

Goran alisema vijana wake wote wapo katika hali nzuri na wana ari kubwa ya kuweka rekodi ya kutwaa ubingwa wa michuano hiyo ya kihistoria.

Kwa upande wake, Kocha Mkuu wa Mtibwa Sugar, Mecky Maxime,alisema dakika 90 za mchezo ndizo zitakazoamua bingwa wa michuano hiyo.

Mecky alisema kikosi chake kipo mara na kinatambua nini la kufanya katika mechi hiyo na kusisitiza kuwa, hana hofu na wapinzani wao.

Sunday, January 11, 2015

STARS MABORESHO KUKIPIGA NA RWANDA JAN 22 MWANZA


Kikosi cha Taifa Stars Maboresho kitacheza mechi ya kirafiki na timu ya Taifa ya Rwanda itakayofanyika Januari 22 mwaka huu kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Mechi hiyo ni sehemu ya programu ya Kocha Mart Nooij kuiandaa timu hiyo kwa ajili ya mechi za mchujo michuano ya Afrika kwa Wachezaji wanaocheza Ligi za Ndani (CHAN). Mechi za mchujo za michuano hiyo ambayo fainali zake zitafanyika mwakani nchini Rwanda zinaanza Mei mwaka huu.

Kocha Nooij anatarajia wakati wowote kutangaza kikosi cha timu hiyo inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager ambacho kitakusanyika Januari 18 mwaka huu jijini Dar es Salaam, na siku moja baadaye kwenda jijini Mwanza.

TAIFA CUP WANAWAKE KUPIGWA JUMAMOSI
Mechi za kwanza za raundi ya kwanza za mashindano ya Taifa ya mpira wa miguu kwa wanawake (Taifa Cup Wanawake) zinachezwa kesho (Januari 10 mwaka huu) kwenye miji 11 tofauti nchini.

Katika mashindano hayo yanayodhaminiwa na kampuni ya Proin, Geita itakuwa mwenyeji wa Kagera (Uwanja wa Geita), Tabora itacheza na Kigoma kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora, Simiyu na Shinyanga (Uwanja wa Simiyu), Arusha na Manyara (Sheikh Kaluta Amri Abeid), na Kilimanjaro na Tanga (Uwanja wa Ushirika).

Mechi nyingine ni Lindi itaikaribisha Mtwara kwenye Uwanja wa Ilulu, Ruvuma na Njombe (Uwanja wa Majimaji), Mbeya na Iringa (Uwanja wa Sokoine), Katavi na Rukwa (Uwanja wa Katavi), Dodoma na Singida (Uwanja wa Jamhuri) na Pwani itakuwa mwenyeji wa Morogoro katika Uwanja wa Mabatini.

Timu hizo zitarudiana Januari 13 mwaka huu, ambapo baada ya matokeo ya nyumbani na ugenini timu iliyoshinda ndiyo itakayoingia hatua inayofuata ambayo pia itashirikisha mikoa ya kisoka ya Ilala, Kinondoni na Temeke.

Hatua hiyo, mechi zake za kwanza zitachezwa Januari 17 mwaka huu wakati zile za marudiano zitafanyika Januari 21 mwaka huu.

Baada ya hapo, hatua itakayofuata ni robo fainali, nusu fainali na fainali ambayo ndiyo itakayotoa bingwa wa michuano hiyo inayofanyika kwa mara ya kwanza nchini.

KILUVYA UTD, NJOMBE ZAKIMBIZA LIGI YA SDL




Kiluvya United ya Pwani na Njombe Mji ya mkoani Njombe ndizo timu pekee zilizomaliza mzunguko wa kwanza wa Ligi Daraja la Pili (SDL) kwa kushinda mechi zote katika makundi yao, hivyo kujipatia pointi 15 kila moja.

Njombe Mji imeongoza kundi D lenye timu za Mkamba Rangers ya Morogoro iliyofikisha pointi nane, Wenda ya Mbeya pointi sita, Volcano FC ya Morogoro pointi sita, Town Small Boys ya Ruvuma pointi tano na Magereza ya Iringa yenye pointi moja.

Katika kundi C, Kiluvya United inafuatiwa na Mshikamano ya Dar es Salaam yenye pointi kumi, Abajalo pia ya Dar es Salaam pointi saba, Cosmopolitan na Transit Camp za Dar es Salaam ambazo kila moja imemaliza mzunguko huo ikiwa na pointi tano. Kariakoo ya Lindi haina pointi.

Mji Mkuu (CDA) ya Dodoma na Singida United ya Singida ndizo zinazochuana katika kundi A kila moja ikiwa na pointi nane. Mvuvuma FC ya Kigoma yenye pointi tano ndiyo inayofuatia, wakati Milambo ya Tabora ina pointi nne huku Ujenzi Rukwa ikikamata mkia kwa pointi moja.

Pia mchuano mkali uko katika kundi B ambapo JKT Rwamkoma ya Mara na Mbao FC ya Mwanza ziko kileleni kila moja ikiwa na pointi tisa. AFC ya Arusha inafuatia kwa pointi sita, Bulyanhulu FC ya Shinyanga ina pointi nne wakati Pamba FC ya Mwanza iko mkiani kwa pointi moja.

Mzunguko wa pili wa ligi hiyo itakayotoa timu nne zitakazopanda daraja kucheza Ligi Daraja la Kwanza msimu ujao (2015/2016) utaanza kutimua vumbi Januari 24 mwaka huu.

Tuesday, January 6, 2015

TFF YAWAKABIDHI BEJI ZA FIFA WAAMUZI 18 WA TANZANIA

 RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza kwenye sherehe za kuwatunuku beji za FIFA waamuzi 18 wa Tanzania.
 Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF),Jamal Malinzi akimkabidhi Beji ya FIFA,Mwamuzi Msaidizi, Sudi Hilla katika hafla iliyofanyika leo kwenye Viwanja vya Karume Mchikichini,Jijini Dar es salaam.Kushoto ni Mwenyekiti wa Kamati ya Wamuzi Tanzania,Salim Chama.
 Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF),Jamal Malinzi akimkabidhi Beji ya FIFA,Mwamuzi Kiongozi Mujuni Mkongo katika hafla iliyofanyika leo kwenye Viwanja vya Karume Mchikichini,Jijini Dar es salaam.Kushoto ni Mwenyekiti wa Kamati ya Wamuzi Tanzania,Salim Chama.

 Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF),Jamal Malinzi akimkabidhi Beji ya FIFA,Mwamuzi Msaidizi Grace Muhindi katika hafla iliyofanyika leo kwenye Viwanja vya Karume Mchikichini,Jijini Dar es salaam.
 Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF),Jamal Malinzi akimkabidhi Beji ya FIFA,Mwamuzi Florentina Zabron katika hafla iliyofanyika leo kwenye Viwanja vya Karume Mchikichini,Jijini Dar es salaam.
Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF),Jamal Malinzi akimkabidhi Beji ya FIFA,Mwamuzi Sophia Mtongori katika hafla iliyofanyika jana kwenye Uwanja vya Karume Mchikichini,Jijini Dar es salaam.


Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF),Jamal Malinzi akimkabidhi Beji ya FIFA,Mwamuzi Jonesia Rukyaa katika hafla iliyofanyika jana kwenye Uwanja vya Karume Mchikichini,Jijini Dar es salaam.

Monday, January 5, 2015

FLOYD MAYWEATHER AFANYA KUFURU, AONYESHA MALI ZAKE, IKIWEMO NDEGE BINAFSI NA MAGARI LUKUKI


BONDIA Floyd Mayweather wa Marekani amefanya kufuru baada ya kupiga picha akiwa mbele ya ndege yake  binafsi na magari manane ya thamani kubwa anayoyamiliki.

Mayweather, anayetajwa kumiliki utajiri wenye thamani ya pauni milioni 66.1, imeelezwa kuwa thamani ya magari yote manane anayoyamiliki ni pauni milioni tanio.

Mbabe huyo wa masumbwi huenda akaingiza mamilioni ya fedha iwapo atakubali kupambana na Manny Pacquiao.






MESSI AIPELEKA SIMBA ROBO FAINALI KOMBE LA MAPINDUZI




TIMU ya soka ya Simba jana ilifuzu kucheza robo fainali ya michuano ya Kombe la Mapinduzi baada ya kuichapaJKU bao 1-0 katika mchezo wa kundi C uliochezwa kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar.

Bao pekee na la ushindi la Simba lilipachikwa wavuni na mshambuliaji machachari, Ramadhani Singano 'Messi' dakika ya 12.

Messi alifunga bao hilo kwa shuti kali la mguu wa kushoto baada ya kupokea pasi maridhawa kutoka kwa Saidi Ndemla.

Kwa matokeo hayo, Simba imetwaa uongozi wa kundi hilo ikiwa na pointi sita, ikifuatiwa na Mtibwa Sugar yenye pointi tano.

Pambano hilo lilikuwa na ushindani mkali kutokana na timu zote mbili kuonyesha soka ya kiwango cha juu, hasa katika kipindi cha pili.

Katika mechi nyingine ya kundi hilo iliyochezwa jana, Mtibwa na Mafunzo ziligawana pointi moja moja baada ya kutoka suluhu.

Michuano hiyo inatarajiwa kuendelea leo wakati KCCA ya Uganda itakapomenyana na KMKM, Azam na Mtende wakati Yanga itavaana na Shaba. Mechi hizo zitaanza kuchezwa saa tisa alasiri.

AZAM YAICHAPA KMKM 1-0


Mabingwa wa Tanzania Bara, Azam FC wamepata ushindi wa kwanza katika Kombe la Mapinduzi, baada ya kuwalaza mabingwa wa Ligi Kuu visiwani hapa, KMKM 1-0 Uwanja wa Amaan, Zanzibar usiku huu.


Sifa zimuendee beki Shomary Kapombe aliyesababisha bao hilo pekee dakika ya 18, na kuifanya Azam FC sasa ifikishe pointi nne baada ya awali kutoa sare ya 2-2 na mabingwa watetezi, KCCA ya Uganda.

Bao hilo lililfungwa na Khamis Ali ‘Chichi’, Nahodha wa KMKM aliyejifunga kwa kichwa akijaribu kuokoa shuti la Shomary Kapombe alilopiga kutoka umbali wa mita 25.

Mchezo ulikuwa mkali na timu hizo zilishambuliana kwa zamu muda wote, huku KMKM wakipoteza nafasi nyingi za kufunga kipindi cha pili.

KCCA sasa inaongoza Kundi B kwa pointi zake nne, sawa na Azam FC, lakini yenyewe ina wastani mzuri wa mabao baada ya jioni ya leo kuifunga Mtende mabao 3-0.

Mechi nyingine zilizochezwa leo, Taifa ya Jang’ombe imeilaza 1-0 Shaba Uwanja wa Mao dze Tung, wakati Yanga SC imeifunga Polisi mabao 4-0, mechi zote za Kundi A.

Michuano hiyo, itaendelea kesho kwa mechi za mwisho za Kundi C, Mtibwa Sugar wakimenyana na Mafunzo Saa 10:00 jioni na baadaye Simba SC na JKU Saa 2:15 usiku Uwanja wa Amaan, Zanzibar.

Azam FC; Mwadini Ali, Shomary Kapombe, Gardiel Michael, David Mwantika, Aggrey Morris, Mudathir Yahya, Erasto Nyoni, Salum Abubakar, John Bocco, Amri Kiemba na Brian Majwega.

KMKM; Mudathir Khamis, Abdulkadir Nemihi, Mwinyi Hajji Mngwali, Ibrahim Khamis Khatib, Khamis Ali Khamis, Iddi Mbegu Mrisho, Nassor Ali Omar, Tizo Chombo, Fakhi Mwalimu, Halid Hebi na Maulid Ibrahim Kapenta.

Thursday, January 1, 2015

KOCHA MPYA SIMBA ATUA DAR, WACHEZAJI WANANE WAGOMA KWENDA ZANZIBAR



KOCHA Mkuu mpya wa timu ya soka ya Simba, Goran Kopinovic, ametia saini mkataba wa kuinoa Simba kwa miaka miwili.


Goran, raia wa Serbia, alimwaga wino jana baada ya kufanya mazungumzo marefu na viongozi wa Simba.

Kocha huyo aliwasili nchini jana asubuhi na kufikia kwenye hoteli ya Double Tree iliyoko Masaki mjini Dar es Salaam.

Habari kutoka ndani ya Simba zimeeleza kuwa, kocha huyo anatarajiwa kwenda Zanzibar leo kujiunga na timu hiyo, inayoshiriki kwenye michuano ya Kombe la Mapinduzi.

Simba imepangwa kufungua dimba la michuano hiyo leo usiku kwa kumenyana na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kuwasili nchini jana, Goran alisema amekuja nchini kufanyakazi na anaamini atapata ushirikiano mzuri kutoka kwa viongozi wa klabu hiyo.

Goran anachukua nafasi ya kocha wa zamani wa Simba, Patrick Phiri, ambaye alitupiwa virago mwanzoni mwa wiki hii kutokana na mwenendo mbovu wa timu hiyo katika michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara.

Wakati huo huo, kikosi cha Simba kimeondoka mjini Dar es Salaam leo kwenda Zanzibar bila ya wachezaji wake wanane nyota.

Wachezaji hao, wakiwemo Waganda watano, wamegoma kujiunga na timu hiyo kutokana na kutolipwa fedha zao za usajili.

Wachezaji wa Uganda waliomo kwenye mgomo huo ni Emmanuel Okwi, Joseph Owino, Dan Ssenkuruma, Simon Ssenkuruma na Juuko Murshid.

Kwa upande wa wachezaji wazalendo, ni kipa Ivo Mapunda, aliyekwenda Mbeya kwenye msiba wa mama yake, Shabani Kisiga na Jonas Mkude.

Kocha msaidizi wa timu hiyo, Selemani Matola, amesema hana taarifa za kutoweka kwa wachezaji hao. Amesema mchezaji pekee, aliyepata taarifa zake ni Mapunda.

Matola amekiri kuwa, anakwenda Zanzibar akiwa na wachezaji wachache, lakini aliahidi kuiongoza vyema timu hiyo kufanya vizuri katika michuano hiyo.