KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, January 29, 2012

Twiga Stars yaichezesha kwata Namibia







TIMU ya soka ya taifa ya wanawake, Twiga Stars jana ilifuzu kucheza raundi ya pili ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Afrika baada ya kuicharaza Namibia mabao 5-2 katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Matokeo hayo yaliiwezesha Twiga Stars kusonga mbele kwa ushindi wa jumla wa mabao 7-2, kufuatia kuichapa Namibia mabao 2-0 katika mechi ya awali iliyochezwa mjini Whindhoek.

Mshambuliaji Mwanahamisi Omary ndiye aliyeibuka shujaa wa Twiga Stars baada ya kuifungia mabao matatu kati ya matano. Mwanahamisi alizawadiwa pesa nyingi na mashabiki.

Twiga Stars sasa itakutana na mshindi kati ya Misri na Ethiopia, ambazo zilitarajiwa kurudiana jana mjini Addis, Ababa. Katika mechi ya awali, Misri ilishinda mabao 4-2.

Saturday, January 28, 2012

Twiga Stars watishia kugomea mechi yao na Namibia kesho


SIKU moja kabla ya timu ya soka ya taifa ya wanawake, Twiga Stars kushuka dimbani kumenyana na Namibia katika mchezo wa marudiano wa raundi ya kwanza wa kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, wachezaji wa timu hiyo wametishia kugoma.
Wakizungumza mjini Dar es Salaam jana kwa masharti ya kutotajwa majina yao, wachezaji hao walisema, wamefikia uamuzi huo kutokana na kulipwa pesa kidogo za posho kutoka katika sh. milioni saba walizopewa na wabunge.
Wachezaji hao walisema, mara baada ya wabunge kuwakabidhi fedha hizo juzi jioni, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) jana asubuhi liliwagawia sh. 100,000 kila mchezaji na kufanya jumla ya malipo kwa wachezaji wote waliopo kambini kuwa sh. milioni tano.
Kwa mujibu wa wachezaji hao, kiasi cha pesa kilichotolewa kwa kila mchezaji, hakiendani na hesabu ya sh. milioni saba zilizotolewa na wabunge. Walisema wanashangaa kuona kuwa, TFF imepiga panga sh. milioni mbili bila kuwapa maelezo yoyote.
"Tulipokabidhiwa zile fedha juzi, wabunge walisema shilingi milioni saba ni kwa ajili ya posho za wachezaji na sh. milioni tatu zitakwenda TFF, sasa TFF wamechukua fedha zao na pia wametukata shilingi milioni mbili zetu, jambo hili limetuuma sana," alisema mmoja wa wachezaji hao.
Wachezaji hao walisema kukatwa kwa pesa hizo kumepunguza morali waliyokuwa nayo kwa ajili ya mechi yao na Namibia na kuongeza kuwa, wamekuwa wakicheza kwa kujituma na kutumia nguvu zaolakini wanaishia kukatishwa tamaa.
Kwa mujibu wa hesabu za wachezaji hao, kikosi chao kina wachezaji 20 hivyo kutokana na sh. milioni saba walizopewa na wabunge, kila mmoja alistahili kupata zaidi ya sh. 100,000 walizopewa na TFF.
Wakati akikabidhi pesa hizo kwa wachezaji, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Ummy Mwalimu aliwaasa viongozi wa TFF wasichakachue fedha hizo kwa vile zimetolewa kwa ajili ya wachezaji tu.
Twiga Stars inatarajiwa kurudiana na Namibia kesho katika mechi itakayopigwa kuanzia saa 10 jioni kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Katika mechi ya awali, iliyochezwa wiki mbili zilizopita mjini Whindhoek, Twiga Stars ilishinda mabao 2-0. Ili isonge mbele, inahitaji sare ya aina yoyote.
Akizungumzia malalamiko hayo ya wachezaji wa Twiga Stars, Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura, alisema yamewasikitisha kwa vile wameshindwa kuelewa mchanganuo wa fedha hizo, ambazo walizipokea wenyewe.
Wambura alisema fedha hizo zilipokelewa na nahodha wa timu hiyo, Sophia Mwasikili, ambaye alizikabidhi kwa Meneja wa timu, Furaha Francis, ambaye naye aliziwasilisha kwa Mkurugenzi wa Fedha wa TFF, Ahmed Naheka.
Alisema fedha hizo ziliwasilishwa kwa Naheka ili ziingizwe katika hesabu za TFF na pia zionekane zimetoka kwa ajili gani ili wakaguzi wajue mapato na matumizi ya fedha za shirikisho hilo.
Wambura alisema TFF iliamua kuwapa wachezaji sh. milioni tano kati ya sh. milioni saba, zikiwa ni posho zao kwa siku saba na sh. milioni mbili zilikatwa kwa lengo la kufidia posho zao za siku tano, ambazo tayari shirikisho hilo lilikuwa limeshawalipa.
Ofisa huyo alisema hakuna kilichoharibika kwa wachezaji kulipwa fedha hizo kwa sababu zile zilizotolewa na wabunge zilikuwa za siku 13 na kwamba TFF imekuwa ikigharamiachakula na mahitaji mengine ya timu hiyo, ambayo imekuwa ikikaa bure katika kambi ya Jeshi.
"TFF inatoa fedha kwa ajili ya chakula wanachokula, tumenunua mashuka na vyandarua, hivyo si kwamba wanakaa bure katika kambi hiyo, fedha zinazopatikana pia zinahudumia maeneo mengine," alisema Wambura.
Wakati huo huo, Bodi ya Dawa nchini imetoa sh. milioni 10 kwa ajili ya timu hiyo ukiwa mwendelezo wa kuisaidia wakati Chama cha Mapinduzi wilaya ya Ilala kimetoa katoni 10 za maji zenye thamani ya sh. 26,000.

Friday, January 27, 2012

MWASIKILI, NGELEJA NA MDEE BWANA!

NAHODHA wa timu ya soka ya taifa ya wanawake, Twiga Stars, Sophia Mwasikili akionyesha kitita cha sh. milioni saba, ambazo timu hiyo ilizawadiwa na wabunge kwa ajili ya malipo yao ya posho katika hafla iliyofanyika juzi kwenye uwanja wa Karume, Dar es Salaam.

WAZIRI wa Nishati na Madini, William Ngeleja (kushoto) akiteta jambo la Mbunge wa Kawe (CHADEMA), Halima Mdee kabla ya kuanza kwa mechi ya kirafiki kati ya timu ya wabunge na timu ya taifa ya wanawake, Twiga Stars, iliyochezwa juzi kwenye uwanja wa Karume, Ilala, Dar es Salaam. Twiga Stars ilishinda mabao 2-1.



Angola, Sudan zashindwa kutambiana



MSHAMBULIAJI Didier Drogba (kushoto) wa Ivory Coast akianguka baada ya kuliwa kwanja na beki Charles Kabore wa Burkina Faso timu hizo zilipomenyana juzi katika mechi ya michuano ya fainali za Kombe la Afrika.


MALABO, Equatorial Guinea
SUDAN na Angola juzi zilishindwa kutambiana baada ya kutoka sare ya mabao 2-2 katika mechi ya kundi B ya michuano ya soka ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika iliyochezwa mjini hapa.
Mshambuliaji Ahmed Bashir aliibuka shujaa wa Sudan baada ya kuifungia mabao yote mawili, yakiwa ni mabao ya kwanza kwa nchi hiyo katika fainali hizo kwa miaka 36 iliyopita.
Angola ndiyo iliyotangulia kufunga bao kupitia kwa mshambuliaji wake nyota, Manucho dakika ya tano baada ya kumpokonya mpira beki Nagmaldien Abdullah wa Sudan.
Bashir aliisawazishia Sudan dakika ya 30 baada ya kuwatoka mabeki wawili wa Angola na kufumua shuti lililotinga moja kwa moja wavuni. Timu hizo zilikwenda mapumziko zikiwa sare ya bao 1-1.
Manucho aliiongezea Angola bao la pili kwa njia ya penalti muda mfupi baada ya kuanza kwa kipindi cha pili baada ya Mateus kuangushwa ndani ya eneo la hatari.
Akitumia udhaifu wa mabeki wa Angola, Bashir aliisawazishia Sudan dakika ya 73 kwa shuti kali akiwa ndani ya eneo la hatari la timu pinzani.
Pambano hilo lilihudhuriwa na watazamaji wachache, tofauti na ilivyokuwa katika pambano kati ya Ivory Coast na Burkina Faso, ambapo mashabiki wengi walikuwa na kiu ya kuwaona wachezaji wanaocheza soka ya kulipwa nchini Uingereza.
Sudan, mabingwa wa michuano hiyo mwaka 1979, walifunga bao kwa mara ya mwisho katika fainali za mwaka 1976 zilizofanyika Zaire.
Tangu wakati huo, Sudan imefuzu kucheza fainali hizo mara moja mwaka 2008, ambapo ilifungwa katika mechi zote tatu kwa kipigo cha mabao 3-0 katika kila mechi.
Wachezaji wote 23 waliomo kwenye kikosi cha Sudan, wanacheza soka katika ligi ya nchi hiyo, wakiwemo wachezaji saba wanaochezea klabu ya Al Hilal.

Kocha wa Senegal hatarini kutimuliwa


MALABA, Equatorial Guinea
SHIRIKISHO la Soka la Senegal (SFF) limesema, hatma ya Kocha Amara Traore itajulikana baada ya kumalizika kwa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika.
Senegal ni miongoni mwa nchi zilizokuwa zikipewa nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa, lakini imekuwa ya kwanza kufungasha virago mapema baada ya kupoteza mechi zote mbili za mwanzo.
Katika mechi yake ya kwanza, Senegal ilichapwa mabao 2-1 na wenyeji Equatorial Guinea kabla ya kufungwa idadi hiyo ya mabao na Zambia.
Rais wa SFF, Augustin Senghor alisema juzi kuwa, ni mapema kujadili hatma ya kocha huyo kwa sasa.
“Anapaswa kupewa muda kumaliza michuano. Bado ana mkataba hivyo si jambo zuri kwa sasa kujadili iwapo ataendelea na kibarua chake ama atimuliwe,”alisema.
“Yeye ni kocha katika fainali hizi za Mataifa ya Afrika na baada ya michuano kumalizika, bado mkataba wake utakuwa unaendelea, ambao bado unamweka kwenye kibarua chake. Kila kitu kitaamuliwa baada ya kufanyika tathmini,”aliongeza.
Senghor alisema Traore alipewa malengo kwa ajili ya michuano hiyo, lakini huu si wakati mwafaka kutoa maelezo ya kumkandamiza.
Alisema kocha huyo atalazimika kuwasilisha ripoti yake baada ya michuano hiyo, ambayo itajadiliwa na kamati ya utendaji ya shirikisho hilo na ndiyo itakayoamua hatma yake.
Traore alitia saini mkataba wa kuifundisha Senegal kwa miaka mitatu mwezi uliopita baada ya kufanya mazungumzo na SFF.
Kocha huyo alisema angependa kuendelea na kibarua chake baada ya michuano hiyo, lakini uamuzi wa mwisho upo mikononi mwa shirikisho hilo.
“Hiki ni kikosi cha vijana nab ado kinajengwa na kinahitaji muda zaidi kuimarika,”alisema.
“Sina sababu za kuwalaumu wachezaji wangu, ambao walicheza vizuri na kutengeneza nafasi nyingi za kufunga mabao,”aliongeza.

Ivory Coast yatinga robo fainali

KIUNGO Yaya Toure (kushoto) wa Ivort Coast akidhibitiwa na beki Mahamadou Kere wa Burkina Faso, timu hizo zilipomenyana juzi katika mechi ya kundi B ya michuano ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika iliyochezwa mjini Malabo. Ivory Coast ilishinda mabao 2-0.



MALABO, Equatorial Guinea
IVORY Coast juzi ilifuzu kucheza robo fainali ya michuano ya soka ya Kombe la Mataifa ya Afrika baada ya kuichapa Burkina Faso mabao 2-0 katika mechi ya kundi B iliyochezwa mjini hapa.
Matokeo hayo yaliiwezesha Ivory Coast kuongoza kundi hilo ikiwa na pointi sita baada ya kucheza mechi mbili, ikifuatiwa na Angola yenye pointi nne na Sudan yenye pointi moja. Burkina Faso bado haijaambulia pointi na imeshatolewa hatua za awali.
Angola na Sudan sasa zinagombea nafasi moja iliyosalia ya kufuzu kucheza robo fainali kutoka kundi hilo, ambapo kila moja italazimika kushinda mechi za mwisho.
Katika mechi hizo zitakazochezwa Jumatatu ijayo, Sudan itamenyana na Burkina Faso mjini Bata wakati Angola itavaana na Ivory Coast mjini Malabo.
Mshambuliaji Salomon Kalou aliifungia Ivory Coast bao la kuongoza dakika ya 16 baada ya kupokea krosi kutoka kwa Yaya Toure na kufumua shuti lililompita kipa Daouda Diakite.
Bao la pili la Ivory Coast lilitokana na uzembe wa beki Bakary Kone wa Burkina Faso kujifunga dakika ya 82 wakati akiwa kwenye harakati za kuokoa hatari iliyoelekezwa kwenye lango la timu yake.
Katika mechi hiyo, Ivory Coast ilimchezesha kwa mara ya kwanza mshambuliaji wake, Didier Zokora baada ya kukosa mechi ya awali dhidi ya Sudan kutokana na kutumikia adhabu ya kufungiwa. Zokora alichukua nafasi ya Igor Lolo.
Licha ya safu ya ushambuliaji ya Ivory Coast kuundwa na washambuliaji wake nyota kama vile, Didier Drogba, Kalou na Gervinho, ilipata wakati mgumu wa kuipita ngome ya Burkina Faso na hivyo kumpa kazi kubwa kiungo wake Yaya Toure kuhaha huku na huko.
Akizungumza baada ya mechi hiyo, Kocha Mkuu wa Burkina Faso, Paulo Duarte alieleza kusikitishwa kwake kutokana na kupoteza mechi hiyo.
Hata hivyo, Duarte alikataa kuzungumzia hatma yake kwa madai kuwa, walifungwa kwa bahati mbaya na si kwa kuzidiwa kimchezo.
Kocha Mkuu wa Ivory Coast, Francois Zahoui alisema ameridhishwa na ari waliyonayo vijana wake, lakini alikiri kuwa, bado wanahitajika kuwa makini zaidi katika mechi zijazo.

BASATA, Jeshi la Polisi waandaa programu ya sanaa




Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi Tanzania limeandaa programu maalumu ya Polisi Jamii na Sanaa Shirikishi itakayofanyika Jumatatu ya Tarehe 30/01/2012 kwa lengo la kuwaelimisha wasanii, wadau wa sanaa na jamii kwa ujumla kuhusu dhana ya ulinzi shirikishi kupitia sanaa.

Programu hiyo inatarajiwa kufanyika makao makuu ya BASATA yaliyoko Ilala Sharif Shamba jijini Dar es Salaam ambapo lengo kuu ni kutoa fursa kwa wasaniii, wadau wa sanaa na wananchi kwa ujumla kujifunza na kuona umuhimu wa matumizi ya sanaa shirikishi katika kujenga dhana ya ulinzi shirikishi inayoratibiwa na kusimamiwa na Jeshi la Polisi Tanzania.

Aidha, programu hii, inalenga kutoa elimu kwa wasanii na wadau wa sanaa juu ya mbinu mbalimbali za kutumia sanaa katika kupambana na vitendo vya kihalifu ili kujenga jamii yenye amani na utulivu.

Ikumbukwe kuwa, BASATA kila Jumatatu limekuwa likiendesha Programu ya Jukwaa la Sanaa ambayo imekuwa ikitumika kama chanzo mahsusi cha habari na elimu kwa wasanii na wadau wa sanaa.
Programu hii ya Polisi Jamii na Sanaa Shirikishi itatumia jukwaa hili katika kuifikia jamii.Katika programu hii, vitengo mbalimbali vya Jeshi la Polisi kama uhamiaji, zima moto, usalama
barabarani, udhibiti madawa ya kulevya nk. vinatarajia kushiriki ambapo mbali ya kupambwa na burudani kutoka jeshi hilo, itakuwa na kipindi cha maswali na majibu ambapo changamoto na kero mbalimbali kuhusu usalama wa raia zitatolewa ufafanuzi.

Ili kuonesha jinsi sanaa shirikishi ilivyoweza kuleta mabadiliko kwenye dhana ya polisi jamii nchini, kundi la sanaa la Lumumba Theatre la jijini Dar es Salaam nalo linatarajia kutoa burudani kemkem ambazo zitabeba elimu juu ya Sanaa Shirikishi na Polisi Jamii.
Baraza linatoa wito kwa Wasanii na wadau wote wa Sanaa kujitokeza kwa wingi kwenye programu hiyo ili kujifunza mbinu mbalimbali za kufikisha ujumbe kupitia sanaa na hata kuitumia sanaa katika kujenga jamii yenye utulivu.
Sanaa ni Kazi, kwa pamoja Tuikuze na Kuithamini


Godfrey Lebejo - KATIBU MTENDAJI (K)

Waethiopia kuzichezesha Yanga na Zamalek



Waamuzi kutoka Ethiopia ndiyo watakaochezesha mechi namba 7 ya Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Yanga na Zamalek ya Misri itakayochezwa Februari 18 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limemteua Bamlack Tessema kuwa mwamuzi wa kati kwenye mechi hiyo wakati waamuzi wasaidizi ni Yilma Knife na Mussie Kindie. Mwamuzi wa akiba (fourth official) atakuwa Waziri Sheha wa Tanzania na Kamishna wa mchezo huo ni Charles Kafatia wa Malawi.

KOZI YA UKOCHA NGAZI PEVU FEB 12

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeandaa kozi ya ukocha ngazi pevu (advanced level) itakayofanyika Dar es Salaam kuanzia Februari 12-25 mwaka huu.

Wakufunzi watakuwa Kocha wa Taifa Stars, Jan Poulsen ambaye pia ni mkufunzi wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), Mkurugenzi wa Ufundi wa TFF, Sunday Kayuni ambaye pia ni mkufunzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) na Kocha wa timu za Taifa za vijana Kim Poulsen ambaye pia ni mkufunzi wa Chama cha Mpira wa Miguu cha Denmark (DBU).

Mwisho wa kupokea maombi kwa makocha wanaotaka kushiriki kozi hiyo ambayo ada yake ni sh. 60,000 itakuwa Februari 5 mwaka huu. Sifa kwa waombaji ni kuwa elimu ya kuanzia kidato cha nne, wawe wanafanya kazi hiyo ya ukocha na wamefaulu vizuri mafunzo ya ukocha ngazi ya kati (intermediate level).

Pia wawe wamefundisha angalau kwa miaka miwili baada ya kupata cheti cha intermediate level.Pia wanatakiwa maombi yao yawe yameidhinishwa na ama vyama vya makocha wa mpira wa miguu vya mikoa, vyama vya mpira wa miguu vya wilaya au vyama vya mpira wa miguu vya mikoa.

Kwa makocha watakaofaulu kozi hiyo watakuwa wamepata sifa ya kuhudhuria kocha ya ukocha yaLeseni C ya CAF.

Thursday, January 26, 2012

SAUTI ZA BUSARA; Ni siku nne za shangwe za muziki wa Kiafrika



Baada ya kupokea maombi zaidi ya 560 kutoka vikundi mbalimbali ambavyo vinataka kufanya maonyesho yao katika tamasha la tisa la Sauti za Busara, hatimaye vikundi 31 vimechaguliwa kufanya maonyesho katika tamasha la tisa la sauti za busara ambalo limepangwa kufanyika kuanzia tarehe 8 mpaka 12 Februari katika ukumbi wa kihistoria wa Ngome Kongwe, Zanzibar.
Orodha ya wasanii imejumuisha wasanii mashuhuri kutoka Afrika Mashariki, Nigeria, Sudan,Cape Verde, Afrika Kusini, Kongo Brazaville,Comoro, Madagaska na kutoka Visiwa vya ushelisheli. Wasanii watakaopanda jukwaani ni Nneka (Nigeria),Tumi&The Volume (South Africa), Fredy Massamba(Congo), FM Academia (Tanzania) na Super Mazembe (Kenya).
Matukio mbalimbali ya ziada ya busara yataanza jumatano ya tarehe 8, milango itafunguliwa kwa matukio mbalimbali. Mji mkongwe utakuwa na maonyesho ya vikundi mbalimbali kama Nadi Ikhwan Safaa (aka Malindi Taarab), Maulidi ya Homu ya Mtendeni,Black Roots, Culture Musical Club na wengineo wengi.
Tamasha litafunguliwa na maandamano ya aina yake siku ya Alhamisi tarehe 9 Februari 2012 ambayo yataanzia katika viwanja vya Kisonge (Michenzani). Vikundi vitakavyoshiriki ikiwemo Kozman Ti Dalon,beni brass, kikundi cha wanawake cha mwanandege,wacheza kapoera na sarakasi, maandamano yatazunguka katika baadhi ya mitaa na kumalizikia Mji Mkongwe katika ukumbi wa Ngome Kongwe kwa ufunguzi rasmi wa tamasha la tisa.
Siku ya kwanza ya ufunguzi itapambwa na burudani kutoka kwa vikundi vifuatavyo Swahili Vibes, Shirikisho Sanaa,Tandaa Traditional group, Wanafunzi wa SOS (vyote kutoka Zanzibar), Mkota Ngoma kutoka Pemba na Ary Morais kutoka Cape Verde.
Siku ya pili tarehe 10 ijumaa, itapambwa na mkongwe wa taarab mwenye historia Afrika mashariki Bi Kidude kutoka Zanzibar na Ogoya Nengo kutoka Kenya. Wasanii wengine ambao watafanya onyesho siku hiyo ni Hanitra (Madagascar), Camirata Group (Sudan), Tausi Women’s Taarab na Utamaduni JKU (Zanzibar), Kozman Ti Dalon (Reunion), Fredy Massamba (Congo) na Super Mazembe (Kenya).
Jumamosi kutakuwa na mpambano wa vikundi vya mchiriku kutoka katika mitaa ya Dar es Salaam,Tanzania,Seven survivor na Jagwa Music, vikitanguliwa na Tunaweza Band (Tanzania), Ndere Troupe (Uganda), Jembe Culture Group (Tanzania), Camirata Group (Sudan) pamoja na Nneka,mwanadada kutoka Nigeria na mshindi wa tuzo ya MOBO ya mwaka 2009 ya mwanamuziki bora wa Afrika.
Jumapili tarehe 12 tutatumbuizwa na Qwela (Uganda), Leo Mkanyia (Tanzania), Lumumba Theatre Group (Tanzania), Chebli Msaidie (Comoros), Kidumbaki JKU (Zanzibar), Tumi & The Volume (South Africa) na FM Academia (Tanzania).
Siku ya jumapili ya tarehe 12, siku ya mwisho ya tamasha, tamasha litafungwa Qwela (Uganda), Leo Mkanyia (Tanzania), Lumumba Theatre Group (Tanzania), Chebli Msaidie (Comoros), Kidumbaki JKU (Zanzibar), Tumi & The Volume (South Africa) na FM Academia (Tanzania).
Kutakuwa na maonyesho ya filamu za muziki wa taarab, hiphop, kuduro na bongo flava,ambazo zitaonyeshwa kila siku kuanzia saa moja mpaka saa sita usiku, filamu zitakwenda sambamba na maonyesho ya muziki, upande wa pili wa ukumbi wa Ngome Kongwe.
Pati ya mwisho ya tamasha itafanyika siku ya wapendanao (Valentine Day) katika hotel ya Kendwa Rocks, kaskazini mwa zanzibar, kwa ajili ya wafanyakazi, waandishi wa habari na marafiki wa Busara.
Kuhusu Sauti za Busara Sauti za Busara inawapa fursa wanamuziki wa ndani kujifunza muziki kutoka sehemu mbalimbali za Afrika na wakati huo huo kuutambulisha muziki wa Afrika mashariki kwa wageni. Katika jamii yoyote fursa kama hii ni chache mno. Sauti za Busara inaandaa tamasha la mfano wa kuigwa kwa wenyeji na wageni, thamani ya kipekee na utajiri wa muziki kutoka Afrika. Inaonyesha uzuri wa utamaduni wetu katika ajira na kuongeza kipato.
Sanaa, warsha za ufundi na semina ni sehemu ya shughuli muhimu za Busara, lengo kuu ni kwa wanamuziki,wataalamu wa vyombo vya habari, mameneja wa sanaa na wafanyakazi wa sanaa. Warsha hizi zinasaidia kuongeza ujuzi na maarifa wa muda mrefu kwa watu wa Afrika mashariki.
Wadhamini wa Tamasha Sauti za busaraa 2012 linawezeshwa na: The Norwegian Embassy, HIVOS, Mimeta, Roskilde Festival Charity Society, Goethe Institut, The Embassy of France, Grand Malt, Toyota,Commercial Bank of Africa,African Leisure Centre, fly540, Memories, Zanzibar Grand Palace Hotel, Maru Maru Hotel, SMOLE II, Zanlink, Azam Marine, ZanAir, fRoots, Times FM,WOMEX, Multi-Color Printers, Ultimate Security, Southern Sun Dar es Salaam,Tabasam Tours, Emerson Spice, Monsoon Restaurant, Mercury's Restaurant,Archipelago Restaurant, Stone Town Café, http://www.zanzibar.net/.

WARUNDI KUCHEZESHA MECHI YA SIMBA NA KIYOVU



Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeteua waamuzi kutoka Burundi kuchezesha mechi ya Kombe la Shirikisho kati ya Simba ya Tanzania na Kiyovu Sport ya Rwanda itakayochezwa jijini Kigali.
Waamuzi hao ni Thierry Nkurinziza atakayekuwa katikati wakati wasaidizi wake ni Jean-Claude Birumushahu na Jean-Marie Hakizimana. Mwamuzi wa akiba atakuwa Hudu Munyemana kutoka Rwanda. Kamishna wa mechi hiyo ni Abbas Sendyowa kutoka Uganda.
Mechi hiyo namba 13 itachezwa Februari 18 mwaka huu kwenye Uwanja wa Amahoro jijini Kigali, na itaanza saa 9.30 kwa saa za Rwanda. Mechi ya marudiano itachezwa Machi 4 mwaka huu, Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
CAF YAMTEUA LIUNDA KUSIMAMIA MECHI

Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limemteua Leslie Liunda wa Tanzania kuwa Kamishna wa mechi namba 3 ya Ligi ya Mabingwa kati ya AS Vita Club ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) na Atletico Olympique ya Burundi itakayochezwa kati ya Februari 17, 18 na 19 mwaka huu jijini Kinshasa.
Waamuzi wa mechi hiyo ambao wanatoka Gabon watakuwa Mbourou Roponat, Wilfred Nziengu na David Obamba. Mwamuzi wa akiba kutoka DRC ni Mupemba Nkongolo.
Mechi ya marudiano kwa timu hizo itachezwa kati ya Machi 2, 3 na 4 jijini Bujumbura ambapo Kamishna atakuwa Eugene Katamban kutoka Uganda.
TAMASHA LA KUVUMBUA VIPAJI (GRASSROOT) DAR

Tamasha la mafunzo ya kuhamasisha watoto kucheza mpira wa miguu na kuvumbua vipaji (Grassroot) kwa shule maalum zilizochaguliwa katika Mkoa wa Dar es Salaam linaendelea Februari 3 mwaka huu.Siku hiyo tamasha hilo litafanyika katika Shule ya Msingi Mtoni Kijichi wilayani Temeke kuanzia saa 3 asubuhi hadi saa 6 mchana. Februari 10 mwaka huu tamasha lingine litafanyika katika Shule ya Msingi Kinyerezi wilayani Ilala.
Watoto (wa kike na kiume) wanaotakiwa kushiriki katika matamasha hayo ambayo yataendelea kila wiki katika shule mbalimbali za Dar es Salaam hadi Agosti 24 mwaka huu ni wa kuanzia umri wa miaka 6 hadi 12.
Matamasha hayo ni mwendelezo wa uzinduzi wa Grassroot katika tamasha (festival) kubwa lililofanyika Desemba 17 mwaka jana Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kuhudhuriwa na watoto 1,200 baada ya semina iliyoendeshwa na Mkufunzi kutoka Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).

Nando sasa ruksa kuichezea Angola


MALABO, Equatorial Guinea
MSHAMBULIAJI Nando Rafael wa Angola ameruhusiwa kuichezea timu hiyo katika michuano ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika.
Shirikisho la Soka Afrika (CAF) limethibitisha kuwa, Nando aliyeichezea timu ya taifa ya vijana wa chini ya miaka 21 ya Ujerumani, anaruhusiwa kisheria kuichezea Angola.
Nando hakuichezea Angola katika mechi yake ya ufunguzi dhidi ya Burkina Faso, iliyochezwa Jumatatu iliyopita, ambapo timu hiyo ilishinda bao 1-0.
Shirikisho la Soka la Angola (FAF), lilianza kufuatilia taratibu za kumuombea ruhusa hiyo Nando wiki iliyopita.
Kwa uamuzi huo wa FIFA, Nando alitarajiwa kushuka dimbani jana katika mechi ya kundi B dhidi ya Sudan.
“Ninayo furaha kubwa kuwepo hapa na nipo tayari wakati kocha atakaponihitaji, nadhani nitakuwa na msaada mkubwa kwa timu,” alisema Nando juzi alipohojiwa na BBC.
“Jambo la muhimu ni kwamba nipo fiti na nimekuwa nikifanya mazoezi na wenzangu na nimejifunza mambo mengi kwa sababu kila kitu ni kipya kwangu,”aliongeza.
Nando (28) hajawahi kuichezea Angola katika michuano mikubwa, lakini amesisitiza kuwa, siku zote alikuwa na uhakika wa kupata nafasi hiyo.
Kamati ya Haki za Wachezaji ya FIFA ilikutana Jumanne iliyopita mjini Zurich, Uswisi kujadili maombi hayo ya Angola na kuamua kuwa, kwa sasa Nando anaruhusiwa kisheria kuichezea timu hiyo.
Kocha Mkuu wa Angola, Lito Vidigal alisema maandalizi ya timu yake katika mechi ijayo hayatabadili, kufuatia uamuzi wa kumruhusu Nando kuichezea timu hiyo.
“Rafael ni mmoja wa wachezaji 23 kwenye kikosi changu na kama wachezaji wengine, kama anayo nafasi ya kucheza, atacheza,”alisema.

GYAN: Tulikuwa na bahati kuifunga Botswana


LIBREVILLE, Gabon
MSHAMBULIAJI nyota wa timu ya taifa ya Ghana, Asamoah Gyan amekiri kuwa, ushindi walioupata dhidi ya Botswana ulitokana na bahati.
Ghana iliishinda Botswana idadi hiyo ya bao Jumanne iliyopita katika mechi ya kundi D ya michuano ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika iliyochezwa mjini hapa.
Asamoah alikiri kuwa, yeye na wachezaji wenzake hawakufurahishwa na ushindi huo.
Katika mechi hiyo, Ghana ilikuwa na wakati mgumu kufuatia kupata upinzani mkali kutoka kwa Botswana, ambayo inashika nafasi za chini kwa ubora wa viwango vya soka duniani.
Hata hivyo, Gyan alisema Ghana itaendelea kuimarika kadri michuano hiyo itakavyokuwa ikisonga mbele.
“Tulikuwa na bahati kubwa kushinda, lakini hii inaonyesha hali halisi ya vijana,”alisema.
“Siku zote kila mechi ya kwanza huwa ni ngumu, lakini cha muhimu ni pointi tatu,”aliongeza.
“Nilieleza kabla ya kuanza kwa michuano hii kwamba, tutarajie maajabu mengi kwa sababu timu yoyote inaweza kushinda wakati wowote,”alisema Gyan.
Mchezaji huyo, anayechezea klabu ya Al Ain ya Abu Dhabi, ameahidi kuwa, kikosi chake kitakuwa imara na chenye makali zaidi katika mechi yao ijayo dhidi ya Mali. Mechi hiyo itapigwa kesho.
Mabingwa hao wa zamani mara nne wa Afrika wamepania kufuta ukame wa kushindwa kutwaa kombe hilo katika kipindi cha miaka 30 iliyopita. Kwa mara ya mwisho, walitwaa kombe hilo mwaka 1982.
Gyan alisema ana hakika Mali watacheza mchezo tofauti na wa Botswana, ambayo iliwapa wakati mgumu wa kuipenya ngome yake.
“Kikosi chetu kina uzoefu mkubwa na tunaelewa tunahitaji nini, tumedhamiria kuwapa furaha mashabiki wetu,”alisema.
Katika mechi yao ijayo, Ghana itacheza bila ya beki wake, John Mensah, ambaye anatumikia adhabu ya kukosa mechi moja baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu.

Mtoto wa rais Eq Guinea awamwagia mapesa wachezaji



BATA, Equatorial Guinea
MTOTO wa Rais wa Equatorial Guinea, Teodoro Nguema Obiang Mangue ametimiza ahadi aliyotoa kwa wachezaji wa timu ya taifa ya nchi hiyo baada ya kuwakabidhi zawadi ya dola milioni moja za Marekani (sh. bilioni 150).
Teodoro alitoa ahadi hiyo kabla ya kuanza kwa michuano ya fainali za Kombe la Afrika, ambapo aliahidi kuizawadia timu hiyo kiasi hicho cha fedha wakishinda mechi yao ya ufunguzi dhidi ya Libya.
Mbali na ahadi hiyo, Teodoro pia aliahidi kuizawadia timu hiyo dola 20,000 za Marekani (sh. milioni 30) kwa kila bao watakalofunga.
Katika mechi ya ufunguzi iliyochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita, Equatorial Guinea iliichapa Libya bao 1-0 na juzi iliifunga Senegal mabao 2-1.
Mtoto huyo wa rais aliwakabidhi wachezaji wa Equatorial Guinea kitita hicho katika hafla iliyofanyika Jumanne iliyopita. Teodoro alikabidhi hundi ya kiasi hicho cha pesa kwa nahodha wa timu hiyo, Juvenal Edjogo.
Mshambuliaji Javier Balboa, aliyeifungia timu hiyo bao pekee na la ushindi katika mechi dhidi ya Libya, naye alikabidhiwa dola 20,000.
Mwingine aliyezawadiwa dola 20,000 ni Ivan Bolado, ambaye alifunga bao kipindi cha kwanza katika mechi dhidi ya Libya, lakini likakatiwa na mwamuzi kwa vile alikuwa ameotea.
Mtoto huyo wa rais ameahidi kuwazawadia pesa nyingine wachezaji wa timu hiyo iwapo watashinda mechi zijazo za kundi A.
Hii inamaanisha kwamba, wachezaji wa Equatorial Guinea watazawadiwa dola zingine milioni moja kwa kuishinda Senegal na dola 40,000 kwa mabao yaliyopatikana katika mechi hiyo.
Zawadi aliyotoa mtoto huyo wa rais kwa kikosi cha Equatorial Guinea, imezua utata kwa baadhi ya wanaharakati, ambao wameupongeza uamuzi wake huo, lakini wanahoji amepata wapi pesa hizo.
Mwaka jana, serikali ya Marekani ilianzisha uchunguzi dhidi Teodoro kuhusu mali zake zinazokadiriwa kuwa na thamani ya zaidi ya dola milioni 70 huku akituhumiwa kutumia vibaya madaraka yake ya uwaziri katika serikali ya nchi hiyo.
Imeelezwa kuwa, wananchi wengi wa Guinea wanaishi maisha ya dhiki licha ya nchi hiyo kupata pesa nyingi kutokana na kuuza mafuta. Rais wan chi hiyo amedumu madarakani kwa zaidi ya miongo mitatu.

Equatorial Guinea yatinga robo fainali, Senegal nje

ABUBAKAR Suiuenei Obaidy (kushoto) wa Libya akigombea mpira na Rainford Kalaba wa Zambia timu hizo zilipomenyana juzi katika mechi ya kundi A ya michuano ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, iliyochezwa mjini Bata. Timu hizo zilitoka sare ya mabao 2-2.


BATA, Equatorial Guinea
WENYEJI Equatorial Guinea juzi walionyesha maajabu katika fainali za michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika baada ya kuichapa Senegal mabao 2-1 katika mechi ya kundi A iliyochezwa mjini hapa.
Kipigo hicho kimeifanya Senegal, iliyokuwa ikipewa nafasi kubwa ya kufanya vizuri kwenye fainali za mwaka huu, ifungashe virago mapema.
Ushindi huo uliiwezesha Equatorial Guinea kuwa timu ya kwanza kufuzu kucheza robo fainali ya michuano hiyo wakati timu nyingine ya kundi hilo itajulikana baada ya mechi za mwisho.
Mshambuliaji Kily ndiye aliyewapa furaha mashabiki wa Equatorial Guinea waliokuwa wamefurika uwanjani baada ya kuifungia bao la pili na la ushindi dakika za majeruhi.
Equatorial Guinea ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 62 lililofungwa na Randy, kufuatia kazi nzuri iliyofanywa na Kily.
Senegal ilisawazisha bao hilo dakika moja kabla ya mchezo kumalizika kupitia kwa Moussa Sow. Alifunga bao hilo kufuatia mpira wa adhabu uliopigwa na Niang.
Kutokana na matokeo hayo, ili ifuzu kusonga mbele, Senegal sasa italazimika kuishinda Libya katika mechi yake ya mwisho keshokutwa huku ikiomba dua Zambia ifungwe na Equatorial Guinea.
Senegal ndiyo timu pekee iliyokuwa ikiundwa na safi kali ya washambuliaji katika fainali hizo, lakini wameshindwa kuonyesha makali yao.
Ushindi wa Equatorial Guinea ulipokelewa kwa furaha kubwa na Kocha Mkuu wa timu hiyo, Gilson Paulo, ambaye alikabidhiwa jukumu la kuinoa wiki tatu kabla ya kuanza kwa fainali hizo.
Katika mechi nyingine ya kundi hilo iliyochezwa juzi, Libya ilitoshana nguvu na Zambia baada ya kutoka sare ya mabao 2-2.
Pambano hilo halikuwa na mvuto kutokana na hali ya uwanja kutokuwa nzuri, kufuatia kujaa madimbwi ya maji baada ya mvua kunyesha kutwa nzima katika mji wa Bata.
Mechi hiyo ilichelewa kuanza kwa saa moja na Libya ilikuwa ya kwanza kuuzoea uwanja na kupata bao kupitia kwa mshambuliaji wake Ahmed Saad Osman.
Mchezaji huyo pia ndiye aliyeifungia Libya bao la pili kabla ya Ummanuel Mayuka kufufua uhai kwa Wazambia baada ya kufunga la kwanza na Christopher Katongo kusawazisha.
Kocha Mkuu wa Zambia, Herve Renard aliwashutumu maofisa wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kwa kuruhusu mechi hiyo ichezwe huku uwanja ukiwa umejaa maji.
“Nimesikitishwa sana kuona mwamuzi akiruhusu mchezo kuanza kwa sababu ilikuwa vigumu kucheza kwenye uwanja ukiwa katika hali hii,”alisema.
Renard alisema timu zote zilishindwa kuonyesha uwezo wake, badala yake mchezo ulikuwa wa kubutua na kukimbia badala ya kucheza soka.
Msimamo wa kundi A baada ya mechi za juzi ni kama ifuatavyo:
P W D L GF GA Pts

Eq. Guinea 2 2 0 0 3 1 6

Zambia 2 1 1 0 4 3 4

Libya 2 0 1 1 2 3 1

Senegal 2 0 0 2 2 4 0

HAWA NDIO MATAJIRI WA KIKE NOLLYWOOD

Ini Edo

Uche Jombo

Rita Dominick

Genevieve Nnaji

Monalisa Chinda

Funke Akindele

Kate Henshaw

Omotola Jalade

Stephanie Okereke

Mercy Johnson


LAGOS, Nigeria
WAKATI fani ya uigizaji filamu ilipoanza kubisha hodi nchini Nigeria, watu wengi hawakuipa uzito. Ilionekana kama vile ni kazi ya kujifurahisha na isiyo na kipato chochote cha maana.
Lakini miaka michache baadaye, fani hiyo iliyoonekana kuwa ni kichekesho, sasa imeweza kubadili maisha ya watu wengi nchini Nigeria na kuifanya nchi hiyo iwe maarufu barani Afrika na duniani.
Fani hiyo, ambayo ni maarufu zaidi kwa jina la Nollywood, imezifanya filamu za Kinigeria ziwe gumzo duniani kutokana na kubeba uhalisia na upekee wa aina yake. Imetoa ajira kwa raia na wasio raia katika nchi hiyo na kuwafanya baadhi yao wawe matajiri wa kutupwa.
Nollywood imedhihirisha kuwa, Nigeria na bara zima la Afrika hazipaswi kuwekwa pembeni katika masuala ya filamu. Ni fani iliyotoa utambulisho kwa taifa la Nigeria.
Kutokana na umaarufu wa filamu za Kinigeria, baadhi ya waigizaji wake, hasa wa kike, wameweza kujipatia sifa na umaarufu mkubwa, ikiwa ni pamoja na kupewa nafasi ya kucheza filamu za Hollywood.
Lakini kikubwa zaidi ni kwamba, baadhi ya waigizaji hao wa kike hivi sasa ni matajiri na wana mvuto na ushawishi mkubwa kwa jamii. Maisha yao ni ya kifahari, wanamiliki majumba makubwa na kuendesha magari ya starehe.
Ifuatayo ni orodha ya wanawake 18 wa Nollywood, ambao ni matajiri kutokana na kulipwa fedha nyingi kwa kucheza filamu kwa sasa. Lakini utajiri wake hauwezi kuwafikia wacheza filamu wa Hollywood ama Bollywood.
1-INI OBONG EDO- Naira milioni 130
Ini Edo ndiye anayeongoza kwa utajiri miongoni mwa waigizaji nyota nchini Nigeria. Licha ya kukumbwa na vikwazo vingi, mafanikio aliyoyapata hadi sasa ni makubwa, ikiwa ni pamoja na kutayarisha filamu zake mwenyewe. Ni mwigizaji pekee wa kike anayecheza filamu nyingi zaidi kwa mwaka. Kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita, picha zake zimekuwa zikitumika kwenye matangazo ya Globacom, Noble Hair na kumwingizia Naira milioni 90. Anamiliki vitega uchumi vingi pamoja na maduka ya nguo na mitindo.
2- UCHE JOMBO- Naira milioni 127
Ni mwigizaji mwenye vituko vingi. Mbali ya uigizaji, pia ni mtayarishaji wa filamu na mfanyabiashara. Rafiki zake wakubwa ni Desmond Elliot, Ini Edo, Monalisa Chinda na Emen Isong. Kwa mwaka 2010, Uche alitengeneza Naira zipatazo milioni 50 kutokana na mikataba mbalimbali na pia kucheza filamu nyingine. Vitega uchumi vyake vingine ni kampuni ya kutengeneza filamu, kampuni ya kuuza na kuagiza bidhaa nje. Ni mwigizaji wa kwanza wa kike kutengeneza filamu yake, ambayo ilimpatia malipo makubwa na kuwafanya wenzake wafuate nyayo zake.
3- RITA DOMINIQUE- Naira milioni 100
Ni mwigizaji wa kike mwenye mvuto zaidi Nollywood, ambaye amekuwa akiingia mikataba ya matangazo na kampuni mbalimbali kama vile Nokia, Globacom na Arik Air.Kwa sasa, anaandaa filamu yake, ambayo inatarajiwa kuanza kuonyeshwa hivi karibuni nchini Nigeria.

4- GENEVIEVE NNAJI- Naira milioni 96
Katika muongo mmoja uliopita, Genevieve ndiye aliyekuwa akiongoza kwa utajiri miongoni mwa waigizaji nyota wa kike nchini Nigeria. Ni mwigizaji mwenye mvuto na anayeheshimika miongoni mwa Wanigeria. Anamiliki kampuni ya mitindo ya mavazi. Na hivi karibuni, Genevieve alikuwa miongoni mwa wacheza filamu waliopewa tuzo ya heshima na Rais Goodluck Jonathan wa Nigeria. Ndiye msanii anayelipwa fedha nyingi kuliko wote kwa kucheza filamu moja.
5- MONALISA CHINDA- Naira milioni 92
Ni mwigizaji anayetumika kutangaza bidhaa nyingi. Alianza kuitangaza Globacom, ikaja Carnirive na sasa Vita500, kinywaji kinachotengenezwa Korea Kusini.Kama ilivyo kwa Genevieve na Rita, umaarufu wa Monalisa umekuwa ukiongezeka kadri miaka inavyosonga mbele. Na hivi sasa anatengeneza filamu yake, inayojulikana kwa jina la ‘Kiss and Tell’.

6- FUNKE AKINDELE- Naira milioni 90
Inawezekana kwa sasa Funke yupo kwenye kiwango cha juu zaidi. Mwigizaji huyo mwenye kipaji amepata mafanikio kutokana na filamu nyingi alizocheza kuwa na mvuto kwa watazamaji. Alianzia filamu za Yoruba na sasa za Kiingereza. Funke pia ni mfanyabiashara. Filamu yake inayotamba hivi sasa ni The Return of Jenifa, ambayo inatarajiwa kuingiza Naira milioni 40 mwaka huu.
7- KATE HENSHAW – Naira milioni 80
Kuachika kwake kwa mumewe hakujamfanya achuje katika fani ya uigizaji wa filamu. Mwaka 2008, Kate alikuwa mmoja wa wacheza filamu walioshika nafasi za juu kwa utajiri nchini Nigeria na ameendelea kuwa hivyo hadi sasa, japokuwa amezidiwa kete na wengine. Mbali na uigizaji, anamiliki vitega uchumi vya aina mbalimbali.
8- OMOTOLA JALADE EKEINDE – Naira milioni 75
Mwanadada huyu mwenye sura na umbo lenye mvuto, aliyeolewa na rubani wa ndege na kuzaa naye watoto wanne, amecheza filamu nyingi. Mbali na kucheza filamu, Omotola pia ni mwanamuziki na amesharekodi albamu zaidi ya mbili. Mapato yake pia yanatokana na picha za matangazo.
9- STEPHENY OKEREKE- Naira milioni 72
Baada ya kupata mafunzo ya uigizaji katika shule moja ya filamu nchini Marekani, Stepheny amedhihirisha kuwa, chochote kile kinachofanywa na wanaume, wanawake nao wanakiweza. Filamu yake ya kwanza aliyoitengeneza, inayokwenda kwa jina la ‘Through The Glass’ imedhihirisha ukweli huo na kumwezesha kupata tuzo kadhaa za kimataifa. Stepheny pia ni mwanamitindo na muongozaji filamu. Pia ni balozi wa kampuni ya Kenekelon Hair ya Japan.
10- MERCY JOHNSON – Naira milioni 70
Ni mwanadada aliyevamia soko la filamu kwa kasi kubwa. Ni mwigizaji wa pili wa kike kwa umaarufu katika Nollywood baada ya Genevieve. Kuvunjika kwa ndoa yake nusura kummalize, lakini aliweza kusimama imara na kupambana na masaibu yote yaliyomkumba. Kwa kipindi cha mwaka 2007-2010, aliweza kutengeneza zaidi ya Naira milioni 40. Anamiliki vitega uchumi vingi katika mji wa Lagos.

11- CHIOMA CHUKWUKA AKPOTHA – Naira milioni 70
Ni mwigizaji pekee, ambaye hajawahi kukumbwa na skendo ya aina yoyote nchini Nigeria na kamwe huwa hakubali kurudi nyuma. Hivi karibuni, Chioma naye aliamua kujitosa katika kundi la watayarishaji wa filamu wa kike na kucheza katika baadhi ya filamu alizoziandaa. Kwa sasa, anamiliki kampuni yake binafsi ya filamu.
12. OBI EDOZIE – Naira milioni 60
Filamu yake ya ’Save Our Soul’ ilimwezesha kutengeneza zaidi ya Naira milioni 35. Kwa sasa, yupo kwenye hatua za mwisho za kutengeneza filamu ya ’Mr and Mr’. Anachukuliwa kama mfanyabiashara mzuri zaidi kuliko mwigizaji filamu.
13- OMONI ONOBOLI – Naira milioni 54
Ameendelea kupanda kwenye chati za juu katika fani ya uigizaji filamu nchini Nigeria na anatarajiwa kufanya mambo makubwa zaidi katika miaka michache ijayo. Mbali na uigizaji, Omoni pia ni mtayarishaji wa filamu na mwandishi mahiri wa muswada wa filamu. Hivi karibuni, Omoni aliteuliwa kuwa balozi wa detol.
14- OGE OKOYE – Naira milioni 45
Licha ya kutoonekana kwa muda mrefu, Oge ameweza kupata mafanikio makubwa katika uigizaji kutokana na umahiri na umakini wake katika kazi hiyo. Kwa sasa, Oge analipwa pesa nyingi kutokana na uigizaji kuliko ilivyokuwa miaka ya nyuma na amepania kurejea kwenye chati za juu.
15- TONTO DIKE- Naira milioni 27
Umchukie ama umpende, ukweli ni kwamba Tonto ni mmoja wa waigizaji maarufu na wenye mvuto katika Nollywood kwa sasa kama ilivyo kwa Mercy. Skendo zilizowahi kumkumba kimaisha ndizo zilizozidi kumuongezea umaarufu. Mbali ya uigizaji, Tonto anafanya biashara mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuagiza magari nje ya nchi.
16- EMPRESS NJAMAH – Naira milioni 20
Mapato ya Empress hayatokani na uigizaji wa filamu pekee, bali pia kutokana na uanamitindo wa mavazi, upambaji wa maharusi, uagizaji wa bidhaa kutoka nje na umiliki wa ardhi.

17- CHIKA IKE – Naira milioni 15
Anaweza kuonekana si maarufu, lakini amekuwa mmoja wa wachezaji filamu wenye mafanikio makubwa kwa sasa katika Nollywood. Pia anamiliki duka kubwa la mavazi katika mji wa Abuja, linalokadiriwa kuwa na thamani ya Naira milioni saba.

18- HALIMA ABUBAKAR – Naira milioni 10
Ni mwigizaji mwenye sura na umbo lenye mvuto, akiwa anafanya vizuri kwenye fani. Anamiliki nyumba kadhaa za kifahari. Kwa sasa anajiandaa kutengeneza filamu yake mwenyewe, inayotarajiwa kuanza kuonyeshwa hivi karibuni.

Wabunge kuwamwagia mapesa Twiga Stars leo

BAADHI ya wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wamejitokeza kuendesha harambee kwa ajili ya kuichangia timu ya soka ya taifa ya wanawake, Twiga Stars ili iweze kufanya vizuri katika mechi yake ya marudiano ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Afrika dhidi ya Namibia, itakayochezwa Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Wabunge hao walisema hayo jana walipokuwa wakihojiwa katika kipindi cha Leo Tena cha kituo cha Clouds FM. Pichani, kutoka kulia ni mbunge wa viti maalum (CCM), ambaye pia ni Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia na Watoto, Ummy Ally Mwalimu, wa tatu kulia ni mbunge wa viti maalum CCM, Vicky Kamata, mbunge viti maalum, Zainab Kawawa, mbunge wa viti maalumu CHADEMA, Grace Kihwelu na mbunge wa viti maalumu CCM, Zainabu Vulu. Wa pili kulia ni mtangazaji wa kipindi cha Leo Tena, Dina Marios. (Picha kwa hisani ya blogu ya Michuzi).

WABUNGE wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, leo wanatarajiwa kuipatia misaada mbalimbali timu ya soka ya taifa ya wanawake, Twiga Stars.
Michango hiyo ya wabunge itatolewa mara baada ya kumalizika kwa mechi ya kirafiki kati ya Twiga Stars na wabunge, itakayochezwa kwenye uwanja wa Karume, Dar es Salaam.
Twiga Stars inajiandaa kwa mechi yake ya marudiano ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Afrika dhidi ya Namibia. Mechi hiyo inatarajiwa kupigwa Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Katika mechi ya awali iliyochezwa wiki iliyopita mjini Whindoek, Twiga Stars iliichapa Namibia mabao 2-0. Ili isonge mbele, inahitaji sare ya aina yoyote katika mechi ya Jumapili.
Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura alisema jana kuwa, msaada utakaotolewa na wabunge kwa timu hiyo bado haujajulikana.
Alisema Twiga Stars inatarajiwa kurudi Dar es Salaam leo mchana, ikitokea Mlandizi mkoani Pwani, ambako ilikwenda kuweka kambi kwa ajili ya mechi hiyo.
“Mechi ya Twiga Stars na wabunge ni ya kujifurahisha na itachezwa kwa muda mfupi,”alisema Wambura.
Wachezaji waliomo kwenye kikosi cha Twiga Stars ni Sophia Mwasikili , Fatuma Bushiri Fatuma Omari, Mwajuma Abdallah , Asha Rashid, Mwanahamisi Omari, Ettoe Mlenzi, Zena Khamis, Fatuma Khatib, Maimuna Said na Fadhila Hamad.
Wengine ni Fatuma Mustapha, Rukia Hamisi, Mwapewa Mtumwa, Judith Hassan, Aziza Mwadini, Sabai Yusuf, Semeni Abeid, Pulkaria Charaji, Mwanaidi Hamisi, Hanifa Idd na Fatuma Gotagota.

Wednesday, January 25, 2012

Simba raha tupu


VINARA wa ligi kuu ya soka ya Tanzania Bara, Simba jana waliendelea kujikita kileleni baada ya kuichapa Coastal Union mabao 2-0 katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Ushindi huo uliiwezesha Simba kuendelea kuongoza ligi hiyo kwa kuwa na pointi 31 baada ya kucheza mechi 14 na kuiacha nyuma Yanga kwa tofauti ya pointi tatu. Yanga inazo pointi 28.
Mabao yaliyoiwezesha Simba kutoka uwanjani na pointi zote yalifungwa na Haruna Moshi na Gervas Kago, moja katika kila kipindi. Coastal ilijipatia bao lake kwa njia ya penalti kupitia kwa Hamisi Shengo.
Simba ilikuwa ya kwanza kulikaribia lango la Coastal Union dakika ya 24 wakati Haruna alipopiga mpira wa adhabu karibu na lango, lakini shuti lake lilitoka nje.
Dakika nane baadaye, Kago aliikosesha bao Simba baada ya kumegewa pasi safi na Juma Jabu, lakini shuti lake lilidakwa na kipa Godson Mmasa wa Coastal Union.
Coastal Union ilijibu mapigo dakika ya 34 wakati Mohamed Ibrahim alipogongeana vizuri na Daniel Lianga, lakini beki Kevin Yondani wa Simba alitokea na kuokoa hatari hiyo.
Simba ilipoteza nafasi nzuri ya kufunga bao dakika ya 36 wakati Haruna alipomtengenezea krosi maridhawa Kago, ambaye alikuwa amebaki ana kwa ana na goli baada ya kipa Mmasa wa Coastal Union kutoka langoni, lakini kichwa chake hakikuweza kulenga lango.
Bao la kwanza la Simba lilifungwa na Haruna dakika tano kabla ya mapumziko kwa shufi hafifu, kufuatia kazi nzuri iliyofanywa na Kapombe.
Ikiwa imesalia dakika moja kabla ya mapumziko, Simba ilipata nafasi nyingine nzuri ya kufunga bao wakati Mafisango alipopewa pasi akiwa ndani ya 18 huku kipa Mmasa akiwa ameanguka chini, lakini shuti lake lilitoka pembeni ya lango. Timu hizo zilikwenda mapumziko Simba ikiwa mbele kwa bao 1-0.
Uzembe wa beki Nassoro Chollo wa Simba nusura uiwezeshe Coastal kupata bao dakika ya 54 baada ya kupangua mpira vibaya, ukamkuta Ibrahim, aliyepiga shuti kali lililopaa juu ya lango.
Lango la Simba lilikuwa hatarini tena dakika ya 68 wakati Benard Mwalala alipojitwisha kwa kichwa mpira wa krosi, lakini ulipanguliwa na kipa Juma Kaseja.
Bao la pili la Simba lilifungwa na Kago dakika ya 77 kwa shuti kali baada ya kazi nzuri iliyofanywa na Haruna.
Coastal Union ilipata bao dakika ya 80 lililofungwa kwa njia ya penalti na Shengo baada ya beki Juma Nyoso kumchezea rafu mbaya Samwel Tennysona katika eneo la hatari.
Wakati huo huo, mashabiki wa Simba jana walikuwa wakigombea kununua jezi za timu ya Zamalek ya Misri, zilizokuwa zikiuzwa uwanjani na baadhi ya wafanyabiashara.
Zamalek inatarajiwa kumenyana na Yanga katika mechi ya raundi ya kwanza ya michuano ya klabu bingwa Afrika, inayotarajiwa kupigwa Februari 19 mwaka huu mjini Dar es Salaam.
Simba: Juma Kaseja, Nassoro Chollo, Juma Jabu, Juma Nyoso, Kevin Yondani, Shomari Kapombe, Mwinyi Kazimoto/ Ramadhani Singano, Jonas Gerrard, Patrick Mafisango, Haruna Moshi, Gervas Kago/ Edward Christopher.
Coastal Union: Godson Mmasa, Mbwana Hamisi, Ramadhani Wasso, Jamal Machelenga, Felix Stanley, Hamisi Shengo, Daniel Lianga/ Lameck Dayton, Mohamed Ibrahim, Benard Mwalala, Samwel Tennysona/ Rashid Mandawa, Salum Gila.

PAPIC MAJI SHINGONI, ALIA ATAKUFA NA MTU



KOCHA Mkuu wa Yanga, Kostadin Papic amewekwa kiti moto na uongozi wa klabu hiyo, kufuatia kuwepo na madai ya kuwabagua baadhi ya wachezaji.
Papic aliwekwa kiti moto jana kwenye hoteli ya Serena mjini Dar es Salaam, katika kikao kilichoongozwa na Mwenyekiti wa klabu hiyo, Lloyd Nchunga, ambapo alitakiwa aeleze iwapo ni kweli anabagua wachezaji.
Mbali na kudaiwa kubagua wachezaji, Papic pia alitakiwa aeleze sababu za Yanga kuvurunda katika mechi yake ya ligi kuu dhidi ya Moro United mwishoni mwa wiki iliyopita.
Katika mechi hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Yanga na Moro United zilishindwa kutambiana baada ya kutoka sare ya mabao 2-2.
“Ni kweli tumepanga kumuhoji Papic kuhusu mambo mbalimbali, lakini kubwa tunataka atueleze kwa nini hataki kuwatumia baadhi ya wachezaji,” alisema jana mmoja wa viongozi wa Yanga, alipozungumza na Burudani.
Kiongozi huyo alisema wachezaji, ambao inadaiwa kuwa Papic hataki kuwachezesha ni wale waliosajiliwa na kocha wa zamani wa timu hiyo, Sam Timbe kutoka Uganda.
Kocha huyo mwishoni mwa wiki iliyopita alinsurika kupigwa na baadhi ya mashabiki wa klabu hiyo, waliokuwa wamelizunguka basi dogo la Yanga lenye namba za usajili T 838 AZM.
Mashabiki hao waliamua kulizunguka basi hiyo baada ya kukerwa na matokeo ya mechi kati ya Yanga na Moro United, ambapo timu hiyo kongwe ilicheza chini ya kiwango.
Baadhi ya mashabiki hao walisikika wakimshutumu kocha huyo kwa kushindwa kupanga timu nzuri na kutowatumia baadhi ya wachezaji, ambao uwezo wao upo juu.
Tayari kocha huyo ameshapewa mechi tatu za kupima uwezo wake na iwapo Yanga itavurunda, huenda akatimuliwa na nafasi yake kuchukuliwa na kocha mwingine.
Uchunguzi zaidi uliofanywa na Burudani umebaini kuwa, wachezaji wa Yanga kwa sasa wamegawanyika katika makundi mawili na hivyo kusababisha hali ya kutokuelewana.
Wakati huo huo, Papic amesema hatamvumilia mchezaji yeyote, ambaye atashindwa kuwajibika ipasavyo na kumsababishia matatizo katika kibarua chake.
Papic alisema hayo jana mara baada ya kumalizika kwa mazoezi ya timu yake yaliyofanyika katika uwanja wa shule ya sekondari ya Loyola iliyopo Mabibo, Dar es Salaam.
Akionekana kutokuwa na masihara, kocha huyo kutoka Serbia alisema, atahakikisha kila mchezaji anawajibika na iwapo atashindwa kufanya hivyo, atafute timu nyingine ya kuchezea.
Papic alisema amekuwa akipokea lawama nyingi kutokana na uzembe wa wachezaji wachache na hivyo kupata matatizo makubwa kwa uongozi, wanachama na mashabiki.
Alisema kuanzia sasa, atahakikisha kila mchezaji anakuwa na nidhamu ya hali ya juu na kutimiza wajibu wake ipasavyo.
"Tumevumiliana vya kutosha, hakuna sababu ya kuendelea kumvumilia mtu ambaye hatimizi wajibu wake ipasavyo, badala yake anakalia maneno tu," alisema Papic.

RASHID CHAMA: Simba, Yanga zibadilike


SWALI: Timu yako imeanza vizuri mechi za mzunguko wa pili wa ligi kuu kwa kuifunga JKT Ruvu. Nini siri ya mafanikio hayo?
JIBU: Ninachoweza kusema ni kwamba, siri ya mafanikio haya ni kuwepo kwa umoja kati ya viongozi, wapenzi na wachezaji kwa jumla, ambapo kila moja anatimiza majukumu yake.
Lakini jambo la msingi ni kwamba, Polisi Dodoma imebadilika na kila mchezaji ana hamu kubwa ya kutaka kuona timu yake inashika mojawapo ya nafasi za juu katika ligi kuu msimu huu.
Kwa upande mwingine, naweza pia kusema kuwa mafanikio haya yametokana na wachezaji wote kuwa fiti, hakuna wachezaji majeruhi hadi sasa, kitu ambacho kwa kweli kinanipa faraja sana.
SWALI: Unadhani ni kwa nini timu yako haikufanya vizuri katika mechi za mzunguko wa kwanza?
JIBU: Kulikuwepo na matatizo madogo ya kiufundi, ambayo tayari viongozi wa jeshi la polisi mkoa wa Dodoma wameshayafanyiakazi.
Unajua miongoni mwa sera za jeshi hilo ni kuhakikisha polisi wanashiriki kikamilifu katika michezo na hii imesaidia sana kuifanya timu yetu na zinginezo za jeshi hili kuwa na mafanikio makubwa katika ngazi zilizopo.
SWALI: Nini matarajio yako katika mechi zijazo baada ya kuibuka na ushindi dhidi ya JKT Ruvu? Unapenda kuwaahidi nini mashabiki wenu?
JIBU: Lengo letu ni kushinda mechi zetu zote za mzunguko wa pili wa ligi. Tumejipanga kuendeleza wimbi la ushindi katika mechi yetu ijayo dhidi ya African Lyon na zile zitakazofuata. Lengo ni kuhakikisha tunachukua tena pointi tatu.
Sina hofu na mchezo huo na mingineyo kwa sababu bado naendelea na kazi ya kuisuka timu yangu ili kuhakikisha tunafanya vizuri kwenye michezo yote ya ligi kuu mzunguko wa pili.
SWALI: Timu yako imekuwa ikipata ushirikiano wowote kutoka kwa viongozi wa soka mkoani Dodoma na polisi makao makuu?
JIBU: Tangu nimejiunga na Polisi, nimegundua kwamba baadhi ya wadau wa soka mkoani Dodoma wanatoa ushirikiano wa hali ya juu kwa timu yetu.
Lakini kupitia gazeti lako, nawaomba wakazi wa mkoa huu kujitokeza kwa wingi kutusaidia vitu mbalimbali na pia kuishangilia kila inapocheza kwa sababu hii ni timu ya mkoa wao, ikishuka daraja, hawatapata nafasi ya kushuhudia mechi za ligi.
Ningependa kuwaona wadau wa soka katika mkoa wa Dodoma wakiipa sapoti timu yao, hata pale itakapokuwa ikicheza na timu kubwa za Simba na Yanga, waishangilie kwa hamasa zote ili kuwaongezea ari wachezaji.
SWALI: Katika miaka ya nyuma uliwahi kuichezea timu ya Yanga, ambayo mwaka huu inashiriki katika michuano ya klabu bingwa Afrika wakati wapinzani wao wa jadi, Simba watashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho. Una maoni gani kuhusu ushiriki wa timu hizo kongwe katika michuano hiyo?
JIBU: Napenda kuwashauri viongozi wa klabu hizo wawe makini katika maandalizi ya timu zao ili ziweze kufanya vizuri na kupeperusha vyema bendera ya taifa.
Viongozi wa klabu hizo wanapaswa kusikiliza na kupokea ushauri wa kitaalam kutoka kwa makocha wao kwa sababu wanakuwa wameshaandaa programu zao, ambazo zinapaswa kutekelezwa.
Ukweli ni kwamba, iwapo viongozi wa Simba na Yanga watashindwa kutekeleza programu za makocha wao, haitakuwa rahisi kwa timu hizo kupata mafanikio.
Timu zinapaswa kukaa kambini mapema na kwa muda mrefu ili kuwafanya wachezaji waweze kucheza kwa uelewano na kushika mafunzo ya makocha wao.
Pia ni muhimu kwa viongozi kuhakikisha kuwa, wachezaji wanalipwa haki zao zote na kwa wakati ili kuepuka kuwepo na malalamiko ama manung’uniko. Hii itasaidia kuzifanya akili za wachezaji ziwe kwenye mchezo muda wote badala ya kufikiria vitu vingine.
SWALI: Yanga wanacheza mechi yao ya kwanza dhidi ya Zamalek ya Misri. Unauzungumziaje mchezo huu? Unadhani Yanga wana uwezo wa kuitoa Zamalek?
JIBU: Hakuna kisichowezekana katika soka. Jambo la msingi ni kwa kila mmoja kutimiza wajibu wake. Ushauri wangu kwa Kocha Kostadin Papic ni kuimarisha zaidi safu zake za ulinzi na ushambuliaji. Nilivyoiona Yanga hadi sasa, tatizo lake kubwa lipo kwenye safu ya ulinzi. Haichezi kwa uelewano mkubwa.
Kasoro nyingine ipo kwenye ufungaji wa mabao. Tatizo hili linapaswa kufanyiwa kazi mapema ili washambuliaji wa timu hiyo wawe na uwezo wa kufunga mabao mengi katika mechi moja.
Ni kweli kwamba Zamalek ni moja ya timu ngumu na tishio nchini Misri na barani Afrika, lakini iwapo viongozi, makocha na wachezaji wa Yanga watajipanga vizuri, wanaweza kuitoa kwenye mashindano.
Moja ya mbinu zinazotumiwa sana na timu za Misri ni kutafuta ushindi mkubwa nyumbani na kulazimisha sare ugenini, hasa inapokutana na timu ngumu. Hivyo Yanga nayo inapaswa kuhakikisha wanashinda mechi ya nyumbani.
Kwa upande wa Simba, naona kidogo wao wapo makini kutokana na kuiweka timu kambini mapema, ingawa nimesikia kocha wao, Milovan Cirkovic ameamua kuifumua timu hiyo.
Uzuri wa Simba ni kwamba walianza kambi kabla ya kwenda Zanzibar kushiriki mashindano ya Kombe la Mapinduzi, waliporejea wakaendelea na kambi na kucheza mechi ya kirafiki dhidi ya Tusker ya Kenya.
Jambo la msingi kwa benchi la ufundi la Simba ni kurekebisha dosari zote zilizojitokeza kwa timu hiyo katika mechi zake za hivi karibuni. Naamini kocha wao ameziona na ndio sababu ameamua kuisuka upya timu yake.
SWALI: Unauonaje mwenendo wa michuano ya ligi kuu hadi sasa? Unadhani ligi inaendeshwa kwa kufuata kanuni na kwa mfumo mzuri?
JIBU: Kwa maoni yangu, nadhani kuna umuhimu wa kufanya mabadiliko kidogo katika uendeshaji wa ligi kuu ili iweze kuwa na ushindani mkali zaidi.
Ilivyo sasa, baadhi ya timu, hasa zile kubwa na zenye uwezo kipesa, zimekuwa zikishinda mechi zake kimizengwe. Baadhi ya timu zimekuwa zikishinda kwa kutumia mbinu chafu za nje ya uwanja. Nina hakika kuwa, bingwa wa ligi hiyo msimu huu atapatikana kwa kazi ngumu.
Kasoro nyingine niliyoiona kwenye ligi ni uchache wa timu. Haipendezi kuona bingwa wa ligi kuu anapatikana baada ya kucheza mechi 26. Anapaswa kucheza mechi nyingi zaidi. Hivyo ligi yetu inapaswa kuwa na timu nyingi zaidi ili iwe ndefu na bingwa apatikane baada ya kucheza mechi nyingi.
Vilevile ningependa kulishauri Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) liboreshe zaidi mkataba wake na wadhamini, Kampuni ya Simu za Mkononi ya Vodacom, ili timu ziweze kupata maslahi bora zaidi.
Kama itawezekana, nadhani ni vyema TFF itafute wadhamini wengine zaidi kwa ajili ya kudhamini ligi hiyo ili maslahi kwa timu na wachezaji yawe bora. Tuachane na ukiritimba wa sasa wa ligi kudhaminiwa na kampuni moja pekee.
Ilivyo sasa, timu zinazonufaika zaidi kutokana na udhamini ni Simba na Yanga kwa sababu mbali ya kupata udhamini wa Vodacom, pia zinadhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL).
SWALI: Unapenda kutoa mwito gani kwa serikali kuhusu michezo?
JIBU: Naishauri serikali iendelee kuhimiza michezo yote ichezwe kuanzia katika shule za msingi, sekondari, vyuo na taasisi mbalimbali kwa sababu huko ndiko wanakoweza kupatikana wanamichezo wengi zaidi.
Vilevile naishauri serikali iendelee kuwachukulia hatua kali viongozi wa manispaa, ambao watabainika kuuza viwanja vya michezo. Tatizo hili limekuwa sugu na kusababisha watoto wengi wakose mahali pa kuchezea na hivyo kushindwa kuonyesha vipaji vyao.

TBL, SBL ruksa kudhamini michezo Z'bar kwa vinywaji visivyo na kilevi



Na Aboud Mahmoud, Zanzibar
SERIKALI ya Zanzibar imesema kampuni zinazotengeneza pombe nchini zinaruhusiwa kudhamini michezo visiwani humu lakini kwa kutumia vinywaji visivyo na kilevi.
Hayo yalisemwa kwenye kikao cha Baraza la Wawakilishi jana na Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Abdilahi Jihad Hassan alipokuwa akijibu swali la mwakilishi wa Rahaleo, Nassoro Salum Aljazira.
Waziri Jihad alisema serikali haina pingamizi kwa kampuni za bia kudhamini michezo, lakini zinapaswa kufuata taratibu, ikiwa ni pamoja na udhamini wake kuhusisha vinywaji visivyo na kilevi.
Katika swali lake, Aljazira alitaka kujua iwapo serikali ya Zanzibar inaruhusu udhamini wa kampuni za bia katika michezo kwa kutumia vinywaji visivyo na kilevu kama vile Malta Guiness.
Kampuni maarufu kwa kutengeneza pombe nchini ni Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) na Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL).
"Hatuna mashaka kwa michezo kudhaminiwa na vinywaji baridi, lakini kampuni hizo lazima zitimize masharti ya msingi tutakayokubaliana," alisema waziri huyo
Aliongeza kuwa, kwa sasa serikali hairuhusu udhamini wa pombe katika michezo visiwani Zanzibar na kwamba serikali itaendelea kusimamia sera hiyo kwa lengo la kulinda maadili ya Wazanzibar.
Hata hivyo, Jihad alisema kama itatokea kwa timu za Zanzibar kupata udhamini huo, zinaruhusiwa kuutumia kwa michezo itakayofanyika nje ya visiwa hivyo.
Akitoa mfano, alisema hivi karibuni timu ya soka ya Baraza la Wawakilishi iliruhusiwa kutumia jezi zenye nembo ya moja ya kampuni hizo, lakini michezo iliyoshiriki haikufanyika Zanzibar.
Waziri Jihad alisema kila nchi inapaswa kufuata utamaduni wake na kwa Wazanzibar, utamaduni wao hauruhusu unywaji wa pombe hadharani.
Akijibu swali la msingi la Muyuni Jaku Hashim, Naibu Waziri wa wizara hiyo, Bihindi Hamad Khamis alisema kwa mujibu wa sera ya michezo ya mwaka 2007 kifungu cha 2.10.1, ufadhili wa michezo kupitia kampuni za bia haukubaliki katika visiwa vya Zanzibar.
Bihindi alisema agizo hilo linalindwa ndani ya mipaka ya Zanzibar, lakini timu yoyote inaruhusiwa kufanya hivyo nje ya visiwa hivyo.
Katika swali lake, Muyuni alitaka kujua kwa nini timu ya Baraza la Wawakilishi iliruhusiwa kuvaa jezi zenye nembo ya bia wakati ilipocheza na timu ya bunge la Jamhuri ya Muungano.

Thabiti Abdul azua kasheshe Mashauzi Classic

Thabiti Abdul

Isha Mashauzi

Baadhi ya waimbaji wa Mashauzi Classic


KIKUNDI cha taarab cha Mashauzi Classic kimeanza kumong’onyoka baada ya waimbaji wake watatu wa kike kuamua kujivua gamba.
Waimbaji hao, ambao ni ndugu wa familia moja, walitangaza kujiondoa Mashauzi Classic mwishoni mwa wiki iliyopita kwa madai ya kuchoshwa na kero za bosi wao, Isha Ramadhani ‘Mashauzi’.
Mmoja wa waimbaji hao, Rahma Machupa alikieleza kituo cha redio cha Clouds wiki hii kuwa, binafsi amefikia uamuzi huo kutokana na Isha kumtuhumu kwamba ana uhusiano wa kimapenzi na mpiga kinanda Thabiti Abdul.
Rahma na waimbaji wenzake hao wawili, ndio walioshiriki kuimba nyimbo zilizomo kwenye albamu binafsi ya Isha inayojulikana kwa jina la Mama nipe radhi na baadaye kushiriki katika kuanzisha kundi hilo.
Mwanadada huyo alisema, awali Isha alikuwa na tabia ya kumsema kimafumbo kila walipokuwa wakifanya maonyesho katika kumbi mbalimbali za Dar es Salaam kabla ya kumshushia tuhuma hizo ‘laivu’.
Alisema baadaye, Isha aliamua kumsimamisha kazi kwa mwezi mmoja kwa tuhuma za utovu wa nidhamu, lakini alibadili uamuzi huo na kumrejesha kundini.
“Kuna siku alikuja nyumbani, akazungumza na mama yangu na kuniomba nirudi, nikakubali, lakini matatizo hayakumalizika,”alisema mwimbaji huyo mwenye umbo lenye mvuto.
Rahma alisema kilichomsikitisha zaidi ni kuona kuwa, aliyekuwa akitoa tuhuma hizo nzito kwake ni kiongozi wa kikundi, hivyo alishindwa kuvumilia na kuamua kujiengua.
“Afadhali ugomvi huo ungekuwa kati yetu sisi wasanii, hapo mtu unaweza kuelewa, lakini unamuhusisha kiongozi wa kikundi? Halafu anakutolea mafumbo stejini? Nimeshindwa kuelewa,”alisema Rahma.
Hata hivyo, Rahma alikanusha madai hayo ya Isha na kusema kuwa, anamuheshimu Thabiti kama kiongozi wake ndani ya kikundi hicho.
Kwa sasa, Rahma ameamua kujiunga na kikundi cha Jahazi Modern Taarab na amekuwa akiimba baadhi ya nyimbo za msanii nyota wa kundi hilo, Khadija Yusuph.
Kwa upande wake, Thabiti alithibitisha kuondoka kwa Rahma, lakini alikanusha madai kuwa alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwimbaji huyo.
“Ni kweli alinipigia simu na kunieleza kwamba yeye na ndugu zake wameamua kujitoa kwenye kundi letu na sisi hatuna kinyongo,”alisema Thabiti.
“Nilichomweleza ni kumtakia kila la heri huko aendako kwa sababu cha msingi ni kufanya kazi, mafanikio yanapatikana kwa kufanya kazi,”aliongeza.
Thabiti alimtetea Isha kwa madai kuwa, ana uwezo wa kumchukulia hatua msanii yeyote kwa sababu ndiye kiongozi mkuu wa kikundi.
“Sidhani kama Isha alifanya makosa kumsimamisha Rahma kwa sababu anayo mamlaka hayo anapoona msanii anakwenda kinyume na kikundi,” alisisitiza.
Alipoulizwa iwapo ana uhusiano wa kimapenzi na Isha na ndio sababu iliyomfanya kiongozi huyo wa Mashauzi Classic awe mkali kwa Rahma, mpapasa kinanda huyo alikanusha katakata.
“Mimi sina uhusiano wowote wa kimapenzi na Isha na wala sikuwa na uhusiano wowote na Rahma, hizo taarifa sio za kweli hata kidogo,”alisema.
Rahma alianza kupata umaarufu kwenye kundi la Mashauzi Classic kutokana na uimbaji wake kufanana na ule wa Isha.
Hata hivyo, baadhi ya wadau wa taarab hawakuwa wakivutiwa na uimbaji huo na kumshauri awe na uimbaji wa peke yake kwa lengo la kuwapa mashabiki ladha tofauti.
Juhudi za kumtafuta Isha ili azungumzie suala hilo hazikuweza kufanikiwa kwa vile simu yake ya mkononi ilikuwa haipatikani.

Tuesday, January 24, 2012

Ni Simba na Coastal kesho Dar, viingilio vyatajwa



Mzunguko wa 14 wa Ligi Kuu ya Vodacom unamalizika kesho (Januari 25 mwaka huu) kwa mechi mbili zitakazochezwa kwenye viwanja tofauti jijini Dar es Salaam.
Simba itakuwa mwenyeji wa Coastal Union kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Viingilio vitakuwa sh. 3,000 kwa viti vya bluu na kijani, sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, sh. 10,000 kwa VIP B na C, sh. 15,000 kwa VIP A.

Nayo Azam itakuwa mgeni wa African Lyon katika mechi namba 97 itakayochezwa Uwanja wa Chamazi. Viingilio katika mechi hiyo ni sh. 10,000 kwa Jukwaa Kuu na sh. 3,000 mzunguko.
Wakati huo huo, kamati ya Ligi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imefanya marekebisho madogo kwenye ratiba ya Ligi Kuu ya Vodacom kutokana na Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza kutumika kwa sherehe za kitaifa za kuzaliwa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Mechi namba 111 kati ya Toto Africans na African Lyon ambayo kwa mujibu wa ratiba ilikuwa ichezwe Februari 5 mwaka huu Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza sasa itachezwa Aprili 18 mwaka huu.
Mabadiliko hayo yamefanyika baada ya wamiliki wa Uwanja wa CCM Kirumba, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kueleza kuwa watautumia kwa sherehe za kuzaliwa chama chao, hivyo hautakuwa na nafasi kwa Februari 4, 5 na 6 mwaka huu.
Uamuzi huo umesababisha pia mabadiliko kwa mechi nyingine mbili. Mechi namba 168 kati ya Villa Squad na African Lyon iliyokuwa ichezwe Aprili 18 mwaka huu Uwanja wa Chamazi jijini Dar es Salaam, sasa itachezwa Aprili 22 mwaka huu.
Pia mechi namba 170 kati ya Azam na Toto Africans iliyokuwa ichezwe Aprili 29 mwaka huu jijini Dar es Salaam sasa imerudishwa nyuma hadi Aprili 26 mwaka huu ambayo ni Sikukuu ya Muungano.

FIFA yaiamuru Yanga imlipe Njoroge mil. 17/-



Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kupitia kitengo chake cha utatuzi wa migogoro (Dispute Resolution Chamber- DRC) limeagiza klabu ya Yanga kumlipa mchezaji John Njoroge sh. 17,159,800 ikiwa ni fidia kwa kuvunja mkataba wake kinyume cha taratibu.
Uamuzi huo wa DRC chini ya Jaji Theo van Seggelen ambaye ni raia wa Uholanzi ulifanywa Desemba 7 mwaka jana jijini Zurich, Uswisi na kutumwa TFF kwa njia ya DHL, Januari 17 mwaka huu.
Njoroge ambaye ni raia wa Kenya aliwasilisha kesi yake FIFA kupinga Yanga kuvunja mkataba alioingia wa kuichezea timu yao kinyume na makubaliano. Mchezaji huyo hivi sasa anachezea timu ya Tusker ambayo ni mabingwa wa Kenya.
Yanga ina siku nne za kukata rufani kupinga uamuzi huo kuanzia tarehe iliyoupokea kama inataka kufanya hivyo. Klabu hiyo inatakiwa iwe imeshamlipa Njoroge ndani ya siku 30 tangu ilipopokea uamuzi huo. Ikishindwa kulipa ndani ya muda huo, itatozwa riba ya asilimia 5 kwa mwaka ya fedha hizo.
Ikiwa Yanga itashindwa kulipa ndani ya muda huo vilevile suala hilo litafikishwa mbele ya Kamati ya Nidhamu ya FIFA kwa hatua zaidi.

Viingilio mechi ya Twiga Stars, Namibia vyatajwa



Kiingilio cha chini kwa mechi ya kufuzu kwa fainali za Afrika kwa Wanawake (AWC) kati ya Twiga Stars na Namibia itakayochezwa Jumapili (Januari 29 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kitakuwa sh. 2,000.
Kiwango hicho ni kwa washabiki kwa viti vya bluu na kijani. Viti hivyo kwa pamoja vinachukua jumla ya watazamaji 36,693 kwenye uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua washabiki 60,000.
Pia kutakuwa na kiingilio cha watoto wenye umri wa chini ya miaka 10 ambacho ni sh. 1,000. Watoto watakaotumia tiketi hizo wanatakiwa kuingia uwanjani wakiwa na wazazi au walezi wao.
Viingilio vingine kwa mechi hiyo ni sh. 3,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, sh. 5,000 kwa VIP B na C n ash. 10,000 kwa VIP A.
Namibia inatarajia kuwasili nchini Ijumaa (Januari 27 mwaka huu) saa 12.45 jioni kwa ndege ya South Africa Airways.

Monday, January 23, 2012

Kwa kweli Rihana ni moto si mchezo!














Waswahili wanasema, mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni. Kusema ule ukweli, mwanamuziki Rihana wa Marekani ameumbwa na kuumbika, ametonwa na kutoneka, amenakshiwa na kunakshika si mchezo. Sura nzuri, umbo zuri kiasi kwamba nakosa maneno mengine mazuri zaidi ya kumwelezea nikaeleweka vyema. Ee Mwenyezi Mungu endelea kuumba viumbe wa aina hii ili waje waipambe dunia yako hii yenye wingi wa adha na madhila na starehe zilizovuka mpaka na kuwafanya baadhi yetu uliowajalia utajiri na maisha mazuri, wasahau kwamba kuna kitu kinaitwa kifo.

Saturday, January 21, 2012

Equatorial Guinea, Libya kazi ipo leo

JUVENAL Owono

SAMIR Aboud- Misri


BATA, Equatorial Guinea
HAYAWI hayawi, hatimaye yamekuwa. Michuano ya soka ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika inaanza kutimua vumbi leo kwa mechi mbili za ufunguzi za kundi A zitakazochezwa mjini hapa.
Katika mechi ya kwanza, wenyeji Equatorial Guinea watafungua dimba kwa kumenyana na Libya kabla ya vigogo vya soka barani Afrika, Senegal kuchuana na Zambia.
Mechi zote mbili zinatarajiwa kuwa na ushindani mkali kutokana na maandalizi yaliyofanywa na kila timu, huku zingine zikiwa zimeahidiwa mamilioni ya pesa iwapo zitashinda.
Serikali ya Equatorial Guinea juzi iliahidi kuwazawadia wachezaji wa timu hiyo bonasi ya dola milioni moja za Marekani iwapo wataishinda Libya.
Ahadi hiyo ya pesa imetolewa na mtoto wa rais wa nchi hiyo, Teodoro Obiang Nguema kupitia kwa msemaji wa shirikisho la soka la nchi hiyo.
Msemaji huyo, David Monsuy alisema juzi kuwa, ahadi hiyo imeongeza ari kubwa kwa wachezaji wa timu hiyo kufanya vizuri katika patashika hiyo.
Mbali na kiasi hicho cha fedha, timu hiyo pia imeahidiwa kupewa dola 20,000 za Marekani kwa kila bao itakalofunga katika michuano hiyo.
Equatorial Guinea, maarufu kwa jina la Nzalang Nacional, inanolewa na Kocha Paulo Gilson kutoka Brazil, aliyekabidhiwa kibarua hicho mwanzoni mwa mwezi huu baada ya kutimuliwa kwa kocha wa zamani, Henri Michel.
Mbrazil huyo ameteua wachezaji wengi zaidi wazalendo kwenye kikosi chake huku akiongeza nyota watano wanaocheza nje ya nchi hiyo. Nyota hao ni pamoja na kiungo Juvenal Edjogo-Owono anayecheza soka nchini Hispania.
Kikosi cha Libya, kitashuka dimbani kikiwa chini ya Kocha Marcos Paqueta na nahodha Samir Aboud. Hii ni mara ya tatu kwa Libya kushiriki kwenye fainali hizo na kiliwahi kushika nafasi ya pili katika fainali za mwaka 1982.
Pambano kati ya Zambia na Senegal ndilo linalovuta hisia za mashabiki wengi wa soka barani Afrika, kufuatia historia ya nchi hizo na ushiriki wake wa mara kwa mara kwenye fainali hizo.
Senegal, ambayo ni maarufu zaidi kwa jina la Simba wa Teranga, inashika nafasi ya 44 katika takwimu za ubora duniani na inafundishwa na Kocha Amara Traore. Nahodha wa timu hiyo ni Mamadou Niang.
Tegemeo kubwa la Traore katika kikosi chake litakuwa kwa washambuliaji wake, Mamadou, Demba Ba, Papiss Demba Cisse na Moussa Sow. Senegal inatumia mfumo wa 4-3-3.
Kwa upande wa Zambia, inashika nafasi ya 79 kwa ubora wa soka duniani, ikiwa inafundishwa na Kocha Herve Renard. Nchi hiyo imefuzu kucheza fainali za Afrika mara 15 na imewahi kushika nafasi ya pili katika fainali za 1974 na 1994.
Zambia, ambayo ni maarufu zaidi kwa jina la Chipolopolo, imepania kutwaa kombe hilo mwaka huu kwa lengo la kuwaenzi wachezaji wake waliokufa katika ajali ya ndege iliyotokea mwaka 1993 nchini Gabon.
Kocha huyo kutoka Ufaransa atawategemea zaidi nahodha wake, Chris Katongo na mdogo wake, Felix pamoja na Joseph Musonda, kipa Kennedy Mweene na kiungo Isaac Chansa.

MZEE YUSUPH ATINGA MAREKANI



MWIMBAJI Mzee Yusuph wa kundi la muziki wa taarab la Jahazi, akiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi wawili wa ofisi ya ubalozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani alipotembelea ofisini hapo juzi. Mzee yupo nchini Marekani kwa ziara ya maonyesho kadhaa ya taarab na onyesho lake la kwanza litafanyika leo.