KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, January 9, 2012

BAUSSI: Tulishinikizwa kuibeba Simba

NA ABOUD MAHMOUD,ZANZIBAR
KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Miembeni United, Salum Baussi Nassor amefichua siri kuwa, walilazimishwa waibebe Simba katika michuano ya Kombe la Mapinduzi.
Baussi alifichua siri hiyo juzi mara baada ya timu yake kuchapwa mabao 4-3 na Simba katika mechi ya michuano hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Amaan mjini hapa.
Mbali na kufichua siri hiyo, Baussi ametangaza kujiuzulu kuifundisha timu hiyo kwa madai kuwa, shinikizo alilopewa la kuibeba Simba limeshusha hadhi yake.
“Kusema kweli kitendo kilichofanywa na uongozi wa Miembeni kulilazimisha benchi la ufundi kuibeba Simba katika mechi hiyo kimeonyesha dharau kubwa kwetu na kunishushia hadhi mimi binafsi,”alisema kocha huyo huku akionyesha sura ya masikitiko. Baussi alisema tangu alipoanza kufundisha soka visiwani Zanzibar, hajawahi kukutana na tukio la aina hiyo na kuongeza kuwa, huko ni kudumaza maendeleo ya mchezo huo.
Kocha huyo alisema timu yoyote inapaswa kushinda mechi kutokana na uwezo wake na si kubebwa na timu pinzani na kwamba mashabiki wamekoseshwa burudani waliyoitarajia.
“Viongozi walishinikiza tuiachie Simba ishinde ili yapatikane mapato mengi katika mechi ya fainali. Kitendo hiki kimeniumiza sana na kwa kweli kimenishushia hadhi yangu,”alisisitiza mchezaji huyo wa zamani wa Zanzibar.
Alisema katika mechi hiyo, wachezaji wake walionyesha uwezo wa juu wa kucheza soka ikilinganishwa na wapinzani wao, lakini wamevunjwa moyo kutokana na shinikizo lililotolewa na uongozi.
Hata hivyo, Baussi hakuwa tayari kutaja majina ya viongozi wa Miembeni waliotoa shinikizo hilo, lakini baadhi ya vyombo vya habari jana vilimtaja mmiliki mkuu wa timu hiyo, Ahmed Makungu.
Baussi alisema wakati sasa umefika kwa watanzania kuacha kuzipa kipaumbele Simba na Yanga katika soka kwa vile kufanya hivyo kunadumaza vipaji vya wanasoka chipukizi.
Katika mechi hiyo, Simba ilijipatia mabao yake kupitia kwa Felix Sunzu, aliyefunga mawili, Patrick Mafisango na Haruna Moshi. Mabao ya Miembeni yalifungwa na Peter Elanda, Issa Othman na Ibrahim Khamis.

No comments:

Post a Comment