KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, January 18, 2012

Mzee Yusuph atangaza bingo ya milioni moja


KIONGOZI wa kikundi cha muziki wa taarab cha Jahazi, Mzee Yusuph ameahidi kutoa bingo ya sh. milioni moja kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa ya kuuzwa kwa CD feki za albamu yao mpya.
Akizungumza mjini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita, Mzee alisema ameamua kutoa zawadi hiyo kwa lengo la kupambana na tatizo lililokithiri la wizi wa kazi za sanaa nchini.
Mzee alisema kwa sasa, albamu yao mpya ya Mpenzi Chokolate inapatikana kwenye CD za kusikiliza na kwamba albamu ya video itafuata hivi karibuni.
Alisema albamu hiyo inauzwa na kusambazwa na kampuni yake binafsi ya Mzee Classic na kwamba hawajatoa tenda hiyo kwa kampuni nyingine.
Kiongozi huyo alisema kwa yeyote anayetaka kuuza albamu hiyo kwa jumla ama reja reja, afike ofisini kwake Magomeni Mapipa, Dar es Salaam jirani na hoteli ya Butiama.
“Natangaza zawadi ya shilingi milioni moja kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa kuhusu mahali zinapouzwa ama zinakotengenezwa CD feki,”alisema.
Mzee pia amewataka mashabiki wa taarab waepuke kununua CD feki kwa vile kufanya hivyo ni kuwatajirisha wezi wa kazi za sanaa na kuwaacha wasanii wakiendelea kuwa hohehahe.
“Ni kweli COSOTA (Chama cha Hatimiliki Tanzania) inajitahidi kupambana na tatizo hili, lakini haiwezi kufanyakazi hiyo peke yake,”alisema Mzee.
“Hawa watu ni wezi, si kwa kazi za Jahazi tu, bali bendi zote za muziki wa dansi na za wacheza filamu. Polisi wamekubali kushirikiana nasi, hivyo lazima tupambane nao,”aliongeza.
Mzee alisema baada ya kuwapata wezi hao, watakachokifanya kwanza ni kuwaelimisha ili waache kuuza CD feki, badala yake wauze CD orijino na kwamba wapo tayari kuingia nao makubaliano maalumu.
Kiongozi huyo wa Jahazi alisema wamejipanga vyema kuhakikisha kwamba, wanauanza mwaka 2012 kwa kuendelea kuwa nambari moja katika muziki wa taarab nchini.
Alisema watafanya hivyo kwa kuendelea kutoa kazi nzuri na zenye viwango na kuwaridhisha mashabiki ili nao watambue kwamba, wanaujua vyema muziki huo na wanafanya vizuri.
Alipoulizwa ni kwa nini ameacha kupiga kinanda hivi sasa katika nyimbo za kundi hilo, Mzee alisema taarifa hizo si za kweli kwa vile bado anaendelea kuutumia ujuzi wake huo.
Alisema katika nyimbo tano zilizomo kwenye albamu yao mpya ya Mpenzi Chokolate, amepiga kinanda kwenye nyimbo tatu.
“Hawa wasanii wanaotajwa kwamba wapo juu yangu katika kupiga kinanda hawana lolote. Mimi ndiye mwalimu wa Thabiti Abdul na Ally J katika kupiga kinanda,”alisema.
Kwa mujibu wa Mzee, alianza kupiga kinanda tangu akiwa kikundi cha East African Melody miaka ya mwanzoni mwa 1990 na kujigamba kuwa, yeye ndiye mwasisi wa taarab ya kisasa.
“Mimi ndiye niliyemwingiza Thabiti kwenye taarab, nilianza kumfundisha tangu nikiwa Melody na ndiye niliyempeleka TOT. Alikuja kwangu kuiba ujuzi.
“Na wakati naanza kupiga kinanda, Ally J alikuwa bado mdogo, na ndiye niliyekuwa nikimpa ujiko wakati alipokuwa Jahazi. Sasa kama wao wanajiona wapo juu zaidi, sawa, lakini nasema hawaniwezi,”alisisitiza.
Mzee alisema yupo tayari kupambana na Thabiti na Ally J kwa lengo la kutafuta nani mkali kati yao, lakini hahitaji kuwepo kwa mwandaaji wa pambano hilo kwa vile lengo si kufanya biashara.
“Nitaondoka kwenda Marekani hivi karibuni (Januari 17), nitakaporudi, nitakuwa tayari kukutanishwa na vijana hawa ili tuonyeshane nani mkali,”alisema.

No comments:

Post a Comment