KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Saturday, April 28, 2012

Niyonzima aiweka Yanga njia panda


MJUMBE wa kamati ya utendaji ya klabu ya Yanga, aliyetangaza kujiuzulu, Abdallah Bin Kleb ametoboa siri kuwa, klabu hiyo inakabiliwa na hali mbaya kifedha.
Wakati Bin Kleb akidai klabu hiyo ina hali mbaya kipesa, kiungo Haruna Niyonzima ameiweka njia panda baada ya kukerwa na uamuzi wa uongozi kumkata pesa zake zote za mshahara.
Bin Kleb amesema hali mbaya ya kifedha inayoikabili Yanga ni sawa na kusema kwamba, imefilisika.
Tajiri huyo aliyemsajili kiungo wa kimataifa wa Rwanda, Haruna Niyonzima alisema hayo mjini Dar es Salaam juzi alipotakiwa kufafanua kuhusu sababu za uamuzi wake wa kujiuzulu.
Bin Kleb alisema Yanga imefilisika kutokana na kuwepo kwa usiri mkubwa kuhusu taarifa za mapato na matumizi ya klabu hiyo.
Alisema wafadhili wengi wamekuwa wakitoa pesa zao mifukoni kwa ajili ya kuisaidia Yanga, lakini hawapewi taarifa kuhusu matumizi yake kutoka kwa uongozi.
Bin Kleb amekuwa mjumbe wa tatu wa kamati ya utendaji ya Yanga kutangaza kujiuzulu. Wengine ni Sara Ramadhani na Seif Ahmed, maarufu kwa jina la Magari.
Kuna habari kuwa, wajumbe wengine wawili wa kamati hiyo huenda wakatangaza kujiuzulu leo. Wajumbe hao ni Ally Mayay na Mzee Yusuph.
Wajumbe wengine wanaounda kamati ya utendaji ya Yanga ni Tito Osoro, Mohamed Bhinda, Charles Mngodo, Salum Rupia na marehemu Theonest Rutashoborwa.
Kwa mujibu wa katiba ya Yanga, iwapo wajumbe watano wa kamati ya utendaji watajiuzulu, itabidi uitishwe mkutano mkuu wa dharula kwa ajili ya kujadili hali hiyo na kuchukua hatua.
Makamu Mwenyekiti wa Yanga, David Mosha alishatangaza kujiuzulu wadhifa huo tangu mwaka jana baada ya kutofautiana na mwenyekiti wake, Lloyd Nchunga.
Nchunga amekuwa akikabiliwa na shinikizo kubwa la kumtaka ajiuzulu, kufuatia mwenendo usioridhisha wa Yanga katika michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara, inayotarajiwa kufikia tamati Mei 5 mwaka huu.
Wakati huo huo, kiungo Haruna Niyonzima wa Yanga huenda akafungasha virago wowote, kufuatia uongozi wa klabu hiyo kumkata mshahara wake.
Habari kutoka ndani ya Yanga zimeeleza kuwa, kitendo hicho kilimfanya Niyonzima agome kusafiri na timu hiyo kwenda Arusha kwa ajili ya pambano la ligi dhidi ya JKT Oljoro kabla ya kubadili msimamo wake.
Kwa mujibu wa habari hizo, kiongozi mmoja wa juu wa Yanga aliagiza Niyonzima akatwe sehemu ya pesa za mshahara wake kwa ajili ya kufidia pesa alizokopa alipokwenda Rwanda kuichezea timu ya taifa ya nchi hiyo hivi karibuni.
Imedaiwa kuwa, Niyonzima alikopa pesa hizo kwa uongozi kwa ajili ya kuwapelekea wazazi wake.
Akizungumza na Burudani mjini Dar es Salaam juzi, Niyonzima alisema amekerwa na kitendo cha uongozi kuamua kumkata pesa zake zote za mshahara kwa wakati mmoja ajili ya kufidia deni hilo.
Alisema uongozi ulipaswa kutumia busara kwa kumkata pesa hizo kidogo kidogo hadi deni hilo litakapomalizika.
‘Mimi nina familia, ambayo inanitegemea. Uongozi ulipaswa kunichukulia mimi kuwa ni binadamu mwenye familia, siwezi kusafiri nikaiacha familia yangu bila chakula,”alisema.
Niyonzima alisema pia kuwa, upo uwezekano mkubwa wa kugoma kuingia kambini kwa ajili ya kujiandaa kwa pambano lao la mwisho la ligi dhidi ya Simba kutokana na kukerwa na uamuzi huo wa uongozi.
"Hiki ni kitendo cha uonevu. Siwezi kusafiri na kuwaacha mke wangu na watoto wakilala na njaa. Nilimweleza katibu (Selestine Mwesigwa)
lakini alikaidi kufahamu tatizo langu na amesisitiza kwamba ataendelea kukata deni langu,"alisema mchezaji huyo.
Pamoja na kuiwekea ngumu Yanga, Niyonzima amesema hana mpango wowote wa kutaka kujiunga na klabu ya Azam baada ya mkataba wake na Yanga kumalizika. 
Alikiri kuwa, mkataba wake na Yanga unatarajiwa kumalizika mwaka 2013 na iwapo kuna timu inamuhitaji, inapaswa kuzungumza na viongozi wa klabu yake.

Simba yapania kuwaangamiza Wasudan J'pili


UONGOZI wa klabu ya Simba umejigamba kuwa, umejiandaa vyema kuhakikisha wanashinda pambano lao la awali la raundi ya tatu ya michuano ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Al-Ahly Shandy ya Sudan.
Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, wanatarajia kukutana leo kupanga mbinu za mwisho kwa ajili ya kuiangamiza Shandy.
Rage alisema kikao hicho pia kitapanga zawadi watakazowapatia wachezaji iwapo wataishinda Shandy na kuitoa katika mashindano hayo.
Simba na Shandy zinatarajiwa kumenyana Jumapili katika mechi itakayopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kurudiana wiki mbili zijazo mjini Khartoum.
Rage alisema kikao cha leo kitahudhuriwa na vigogo na wafadhili mbalimbali wa klabu hiyo na kitafanyika kwenye hoteli ya Sapphire Court iliyopo Gerezani, Dar es Salaam.
Mwenyekiti huyo wa Simba alisema, pambano lao la Shandy limepangwa kuanza saa 10 jioni na tiketi zitaanza kuuzwa kesho kwenye vituo mbalimbali vya mjini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Rage, kikosi cha Shandy kikiwa na msafara wa watu 30, kinatarajiwa kutoa nchini leo kwa ajili ya pambano hilo na kimepangiwa kukaa kwenye hoteli ya Durban iliyopo Mnazi Mmoja, Dar es Salaam.
Katika hatua nyingine, uongozi wa Simba umekiri kuwepo nchini kwa mashushushu wa timu ya Al-Ahly Shandy kwa ajili ya kuipeleleza.
Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema jana kuwa, mashushushu hao waliingia nchini siku tano zilizopita ikiwa ni pamoja na kukagua hoteli ya Durban, ambayo timu hiyo itafikia.
Upo pia uwezekano kwa mashushushu hao kuhudhuria mechi ilizocheza Simba hivi karibuni katika ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya JKT Ruvu na Moro United.
Pamoja na kutuma mashushushu wao, Kamwaga alisisitiza kuwa, lazima timu hiyo ipate kipigo katika mechi yao ya Jumapili.

DIAMOND: KUREKODI ALBAMU SASA BASI


MSHINDI wa tuzo tatu za muziki za Kilimanjaro, Naseeb Abdul ‘Diamond’ amesema kuanzia sasa, hatakuwa akirekodi albamu ya nyimbo zake mpya.
Badala yake, Diamond amesema atakuwa akirekodi wimbo mmoja mmoja hadi soko la muziki wa kizazi kipya litakapobadilika nchini.
Diamond alisema hayo mjini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita, alipokuwa akilalamikia nyimbo zake kuvuja mara kwa mara kabla ya uzinduzi wa albamu yake.
Msanii huyo mwenye mvuto alisema, amekuwa akikabiliwa na tatizo hilo tangu alipojitosa kwenye muziki huo na ameona njia pekee ya kukabiliana nalo ni kuacha kutoa albamu,
“Kwa sasa hata ukitoa albamu huwezi kuuza kwa sababu nyimbo zote zinakuwa tayari zipo mitaani na kila mtu anakuwa nazo nyumbani kwake,”alisema.
Diamond alisema anashangaa kuona wimbo wake mpya wa Lala salama umeshatapataa kwenye vituo mbalimbali vya redio wakati hajaanza kuusambaza.
Alisema kuvuja kwa wimbo wa msanii na kuanza kupigwa mara kwa mara kwenye vituo vya radio ni tatizo, hasa kibiashara, lakini inakuwa vigumu kuzuia usipigwe na si rahisi kufanya hivyo.
“Nipo nyumbani, nasikia kwenye redio mashabiki wanaomba wimbo wangu mpya na unasikia unapigwa. Natamani kuzuia isipigwe, lakini nashindwa kwa sababu nikifanya hivyo, nitawakorofisha mashabiki wangu,”alisema.
“Kwa upande mwingine, inaonyesha ni jinsi gani nyimbo zako zinavyopendwa na unavyoheshimika kwa sababu sijawaomba wafanye hivyo ama kuwalipa chochote, hii maana yake wanaheshimu na kuthamini kazi yangu, lakini kibiashara inatuweka kwenye wakati mgumu sana,”aliongeza.
Alisema tatizo hilo lilianza kujitokeza tangu aliporekodi wimbo wake wa kwanza wa Nenda kamwambie na kufuatiwa na wimbo wa Mbagala, ambao alisema uliongoza kwa kuvuja mapema kabla hajaanza kuusambaza.
Msanii huyo alisema wimbo wake mwingine wa Moyo wangu haukuvuja kwa sababu watu wenye tabia ya kuzisambaza nyimbo zake bila ridhaa yake hawakufanikiwa kuupata.
Diamond alisema wimbo wa Mawazo nao ulivuja mapema kwa mashabiki, lakini anashukuru kwamba, baada ya kurekodi video yake, ulionekana mpya zaidi.
“Kusema ule ukweli, vitendo hivi vimekuwa vikinikera sana na kuanzia sasa, kurekodi albamu sasa basi,”alisema Diamond.
“Nitakuwa nikitoa nyimbo baada ya nyimbo hadi soko la muziki wetu litakapobadilika. Hii itanisaidia nyimbo zangu zisizagae hovyo mitaani,”aliongeza.
Diamond ameelezea msimamo wake huo siku chache baada ya kushinda tuzo tatu za muziki za Kilimanjaro, ikiwemo tuzo ya video bora ya mwaka kupitia wimbo wake wa Moyo wangu.
Alitwaa tuzo hiyo baada ya kuzibwaga video za Hakunaga ya Suma Lee, Wangu ya Lady JayDee, Ndoa ndoana ya Casim na Bongo Fleva ya Dully Sykes.
Tuzo nyingine alizoshinda Diamond ni ya mtunzi bora wa mwaka, ambapo aliwabwaga Ally Kiba, Mzee Yussuph, Barnaba na Belle 9 pamoja na tuzo ya mtumbuizaji bora wa kiume, baada ya kuwabwaga Ally Kiba, Dully Sykes, Bob Junior na Mzee Yusuph.
"Namshukuru Mungu, wakati mwingine uvumilivu na subira ni mzuri. Mwaka jana sikupata tuzo, nikamshukuru Mungu, nikaongeza bidii, nikafanya kazi nzuri, leo ninachukua tuzo ya tatu sasa hivi," alisema Diamond baada ya kukabidhiwa tuzo ya tatu.

TOTO: Tutaipa ubingwa Simba



KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Toto African ya Mwanza, Athumani Bilal ametamba kuwa, kikosi chake kitaisambaratisha Azam katika mechi yao ya ligi kuu ya Tanzania Bara itakayochezwa Jumatatu ijayo.
Bilali alisema kwa njia ya simu juzi kutoka Mwanza kuwa, wanakuja Dar es Salaam kwa lengo la kuzoa pointi zote tatu kutoka kwa Azam ili wajinusuru katika janja la kushuka daraja.
Kocha huyo alisema hadi sasa hawajawa na uhakika wa kubaki katika ligi kuu, hasa iwapo watapoteza mechi hiyo dhidi ya Azam na ile ya mwisho dhidi ya Coastal Union itakayochezwa mjini Tanga.
Pambano kati ya Toto African na Azam linasubiriwa kwa hamu kubwa kwa vile ndilo litakaloamua iwapo Simba inaweza kutangaza ubingwa mapema au la.
Simba ilikuwa itangaze ubingwa Jumatatu iliyopita iwapo pambano kati ya Azam na Mtibwa Sugar lingemalizika kwa sare, lakini lilivunjika dakika ya 88 baada ya Mtibwa kugomea penalti. Hadi pambano hilo lilipomalizika, timu hizo zilikuwa sare ya bao 1-1.
Kwa mujibu wa kanuni, hatma ya pambano linalovunjika itasubiri ripoti ya mwamuzi na kamishna, itakayowasilishwa kwa kamati ya ligi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Simba hadi sasa inazo pointi 59 na iwapo itashinda mechi yake ya mwisho dhidi ya Yanga, itakuwa na pointi 62, ambazo haziwezi kufikiwa na timu zingine.
Lakini iwapo Simba itafungwa na Yanga, itabaki na pointi 59, ambazo zinaweza kufikiwa na Azam kama itapewa ushindi katika mechi yake dhidi ya Mtibwa na kushinda mechi zake mbili zilizosalia dhidi ya Toto na Kagera Sugar.
“Matumaini yetu ya kufanya vizuri dhidi ya Azam ni makubwa. Kama tuliweza kuibana Simba na kutoka nayo sare kabla ya kuifunga Yanga, hatuoni kwa nini tushindwe kufanya hivyo kwa Azam,”alisema.
Bilali alisema hawataki kufanya makosa yaliyoifanya timu hiyo ichapwe bao 1-0 na Kagera Sugar mwishoni mwa wiki iliyopita na kuongeza kuwa, wameweza kurekebisha dosari zilizojitokeza katika mechi hiyo.
Iwapo Toto itaifunga Azam ama kutoka nayo sare, itakuwa imeipa ubingwa Simba kwa vile wapinzani wao hata kama watapewa ushindi dhidi ya Mtibwa na kuifunga Kagera, hawataweza kufikisha pointi 59.
"Pambano hili kwetu ni sawa na vita ya kuhakikisha tunabakia kwenye ligi kuu msimu ujao, lakini jambo la msingi kwa vijana wangu ni kucheza soka ya kiwango cha juu na waamuzi kuzingatia sheria 17 za soka,”alisisitiza.

JAMAL BAYSER: Ipo siku mechi za ligi kuu zataleta maafa


WAKATI michuano ya soka ya ligi kuu ya Tanzania Bara msimu huu ikiwa inaelekea ukingoni, mratibu wa timu ya Mtibwa Sugar ya Morogoro, Jamal Bayser ameonya kuwa, iwapo Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) haitakuwa makini, ipo siku mechi za ligi hiyo zitasababisha maafa. Katika makala hii ya ana kwa ana iliyoandikwa na Mwandishi Wetu, ATHANAS KAZIGE, kiongozi huyo wa Mtibwa Sugar anafafanua kuhusu tahadhari yake hiyo.

SWALI: Michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara msimu huu inaelekea ukingoni. Una jambo gani ambalo ungependa kulizungumza kuhusu ligi hiyo?
JIBU: Katika msimu huu wa ligi nimeweza kujionea mambo mengi ya ajabu, ambayo kama hatua za haraka hazitachukuliwa, ipo siku huenda tukapata hasara kubwa.
Nasema hivyo kutokana na kuwepo kwa mambo ya kusikitisha, ikiwa ni pamoja na baadhi ya timu kubwa kubebwa na waamuzi na kusababisha hali ya utulivu katika mchezo wa soka kutoweka.
Nina hakika iwapo hatua hizo zitachelewa kuchukuliwa, ipo siku tutashuhudia waamuzi wetu wakisababisha umwagikaji wa damu katika viwanja vya soka na hivyo kulitia doa jina la Tanzania katika ramani ya soka ulimwenguni.
SWALI: Kwanini unasema hivyo?
JIBU: Unajua hakuna kitu kibaya kama ushabiki ndani ya soka. Kila timu inaingia gharama kubwa kusajili wachezaji, kulipa mishahara,
kuwalipia matibabu wachezaji na mambo mengine mengi, ambayo huchangia kuzifanya timu zetu ziendelee kuwepo. Lakini unapofika uwanjani, unakutana na madudu ya ajabu. Inauma sana.
Unavyoiona timu kama Mtibwa Sugar, unajua inatumia pesa nyingi, lakini inapata mapato kidogo kutokana na mechi za ligi na za wadhamini, lakini lengo kubwa tunataka tufanye vizuri kwa kupata ushindi.
Sasa unapofika uwanjani na kuona timu yako inaonewa na ile isiyokuwa na uwezo inashinda, kwa kweli inauma sana. Fikiria ungekuwa ni wewe ungejisikiaje? Mnatumia pesa nyingi kuihudumia timu, halafu mnafungwa kwa sababu ya hila za wapinzani wenu.
Ndio sababu nimesema kuwa, inabidi TFF wafanye maamuzi magumu kuhusu waamuzi na timu ambazo zimekuwa zikibebwa kutokana na kutumia mbinu chafu kwa sababu mtindo huu umekuwa ukizidi kuota mizizi na hakuna hatua zozote zinazochukuliwa kwa wahusika.
Timu kama Azam imekuwa ikilalamikiwa na timu nyingi. Tayari
Yanga,Villa Squad, Polisi Dodoma zimeshatoa malalamiko kuhusu Azam na sasa sisi Mtibwa Sugar kutokana na mechi zao kutawaliwa na mbinu chafu na kujitokeza kwa vitendo vya vurugu.
Kwa kweli mashabiki wa timu nyingi za ligi kuu wamekuwa wavumilivu, lakini ipo siku uvumilivu wao unaweza kufikia kikomo na kuamua kuingia uwanjani kufanya vurugu na hatimaye damu kumwagika. Lazima TFF ichukue tahadhari mapema.
SWALI: Unadhani nini kifanyike ili kuondoa tatizo hilo, ambalo umelielezea kuwa kwa sasa limekuwa sugu?
JIBU: Mimi binafsi nafikiri kwamba umefika wakati kwa TFF kuhakikisha kila mchezo unarekodiwa ili matukio yote ya uwanjani yaweze kuonekana na kama kuna pingamizi lolote haki iweze kutendeka.
Nasema hivyo kwa sababu hali imekuwa mbaya sana. Kila kukicha watu au viongozi wa baadhi ya timu wamekuwa wakiwalalamikia waamuzi wetu kwa kushindwa kuzitumia vyema sheria 17 za soka.
Pia napenda zitungwe sheria kali kwa yoyote, ambaye atashindwa au kuthibitika amepewa rushwa na timu au kiongozi ili liweze kuwa fundisho kwa watu wengine wenye tabia hiyo.
Nina hakika iwapo itatokea mwamuzi mwingine anafungiwa maisha au kupigwa faini au kufungwa jela kutokana na kupokea rushwa,
litakuwa funzo kubwa kwa wengine na hata kupunguza vitendo hivyo katika soka.
SWALI: Una maoni gani kuhusu utendaji wa TFF? Au tuseme kuna kasoro nyingine yoyote uliyoibaini zaidi ya waamuzi?
JIBU: Mimi naona zipo changamoto chache ndani ya TFF. Miongoni mwa changamoto hizo ni kuwepo kwa mikakati ya kusaka wadhamini zaidi kwenye ligi hiyo na ile ya taifa.
Sio siri, unajua hali ya kifedha ni ngumu kwa baadhi ya timu. Klabu nyingi zina hali mbaya na hata pesa za mdhamini wa ligi hiyo, Vodacom hazitoshi. Inabidi TFF ifanye kazi ya kusaka wadhamini wengine.
Sambamba na jambo hilo, napenda TFF wawekeze nguvu zaidi katika timu za vijana na ikiwezekana waanzishe ligi yao na kuwatafutia wadhamini ili kuongeza ushindani na hapo watakuwa wanakuza mchezo huo.
SWALI: Kikosi cha Mtibwa Sugar msimu huu kimekuwa hakifanyi vizuri katika michezo mbalimbali. Unaweza kueleza tatizo hasa ni nini?
JIBU: Sio kweli kwamba kikosi chetu hakifanyi vizuri. Tumekuwa tukifanya vizuri katika mechi nyingi, isipokuwa yapo baadhi ya matatizo kama vile baadhi ya wachezaji kuwa majeruhi kwa kipindi kirefu na wengine viwango vyao kushuka. Lakini sababu kubwa ni waamuzi kutotutendea haki katika mechi zetu.
Nasema hivyo kwa sababu msimu huu umetawaliwa na mambo mengi ya ajabu. Kila kukicha, timu nyingi zinasaka pointi tatu kwa hila mbalimbali na gharama kubwa. Kwetu sisi hilo jambo halipo kabisa.
Lakini bado tunayo nafasi ya kufanya mabadiliko kwenye kikosi chetu na kitaweza kufanya vizuri msimu ujao, ingawa najua wazi kwamba kazi hiyo itakuwa ngumu.
Benchi letu la ufundi linafanya kazi yake vizuri kuhusu suala hilo kwa kipindi hiki kwa kuangalia mchango wa kila mchezaji na litaleta kwetu
mapendekezo yake ili tuweze kuyafanyia kazi na kujenga kikosi imara na cha ushindi msimu ujao.
SWALI: Katika miaka ya nyuma ulikuwa mmoja wa viongozi wa juu wa TFF. Je, una mpango wowote wa kugombea uongozi katika uchaguzi ujao wa shirikisho hilo unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwaka huu?
JIBU: Swali lako ni sana. Ukweli ni kwamba kwa sasa nina kazi nyingi sana, lakini pia ni mapema mno kuzungumzia jambo hilo, ingawa sina mawazo ya kufanya hivyo.

RAY: Acheni kunifuatafuata


MSANII gwiji wa tasnia ya filamu nchini, Vicent Kigosi ‘Ray’ amevitaka vyombo vya habari pamoja na mitandao kuacha mara moja kumuhusisha na kifo cha msanii mwingine nyota wa fani hiyo, Steven Kanumba.
Ray amesema amepanga kuvichukulia hatua za kisheria vyombo hivyo kwa sababu vinahatarisha usalama wa maisha yake pamoja na kumuweka kwenye wakati mgumu.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Ray alisema ameshangazwa na mtandao mmoja unaojulikana kwa jina la U Turn kwa kumzushia kwamba anahusika na kifo cha Kanumba.
Kanumba alifariki dunia Aprili 7 mwaka huu baada ya kutokea mzozo kati yake na msanii Elizabeth Michael ‘Lulu’, ambaye inadaiwa walikuwa na uhusiano wa kimapenzi. Mazishi ya Kanumba yalifanyika Aprili 10 mwaka huu Kinondoni, Dar es Salaam.
Ray alisema yeye na Kanumba walikuwa wakiishi kama ndugu na familia zao zilikuwa karibu kutokana na urafiki wa muda mrefu waliokuwa nao.
“Tuliishi kama mtu na mdogo wake. Hatukuwa marafiki tena bali ni ndugu wa karibu na tulikuwa tukipambana katika kujiongezea vipato kutokana na utendaji wa shughuli zetu kwa pamoja,”alisema Ray.
Ray alisema amepatwa na hofu zaidi kutokana na wachangiaji wa habari iliyoripotiwa na mtandao huo kuonyesha kutokuwa na imani naye na hivyo kuyaweka maisha yake hatarini.
Alisema tayari amesharipoti polisi kuhusu taarifa zilizoripotiwa na mtandao huo na kuongeza kuwa, mmiliki wake ameshahojiwa.
Alisema kitendo cha mmiliki wa mtandao huo kumuhusisha na kifo cha Kanumba pia kimemvunjia heshima mbele ya jamii kwa vile naye amekuwa akijihusisha na fani ya filamu kwa miaka mingi.
“Mimi nafanya kazi ya kuigiza, ndio maisha yangu, sasa unapoandika kitu kama hicho kwenye mtandao, habari hiyo inafika sehemu kubwa duniani,”alisema.
“Sasa unategemea watu watanichukuliaje kama sio kunivunjia heshima na kunipotezea mashabiki wangu? Nasema hili sitoweza kuliacha, nitalifanyia kazi na nitalifikisha mahakamani ili iwe fundisho kwa watu wengine, sitolichekea hili,”alisema Ray kwa uchungu.
Wasiwasi mwingine ulioonyeshwa na Ray ni kwamba, msanii anapohusishwa na kifo cha msanii mwenzake, hupotea kabisa katika sanaa.
Taarifa kamili iliyowekwa na Ray kupitia kwenye blogu yake ya raythegreatest ni kama ifuatavyo:
Yapata wiki tatu sasa tangu msanii mwenzangu Steven Kanumba aage dunia, na kama ilivyo kwa kila kifo kinapotokea, huandamana na kila aina ya maneno na hisia mbali mbali kutokana na mitazamo ya watu kupishana kuhusiana na jambo husika.
Kulingana na muktadha huo, msiba wa Steven Kanumba umekumbwa na maneno na hisia kama hizo, hususan mazingira ya kifo chake.
Kinachosikitisha zaidi watu wengi (ambao wanajitambulisha kama wapenzi wa Kanumba), na baadhi ya vyombo binafsi vya habari, vimekuwa vikinihusisha na kifo hicho, kwa kusema kwamba kwa njia moja au nyingine ninahusika na mauaji ya Steven Kanumba.
Kwa muda wote huo tangu msiba ulipotokea mpaka leo hii nashika kalamu kujaribu kuyaweka sawa na kuondosha hisia chafu katika fikra za watu, nimekuwa nikipitia katika wakati mgumu sana kwa jinsi, ambavyo nimekuwa nikinyooshewa vidole kila upande nikihusishwa na kifo hicho.
Kiujumla nimezingatia maoni ya wapenzi na mashabiki wangu wakinitaka kuwa na subira,  ila kuna ukweli usemao kwamba, uongo ukirudiwa sana, jamii huusadiki na kuuona ukweli. Nimeona nisikae kimya ila niweke sawa hili kwamba sihusiki na kifo cha Steven Kanumba.
Nasema wazi kwamba sihusiki kabisa na kifo cha Kanumba, kwanza kwa kuzingatia mazingira yenyewe ya kifo kilivyotokea. Wakati kifo hicho kinatokea, nilikuwa sehemu nyingine kabisa na mimi nilikuwa mtu wa tatu kutaarifiwa kwamba Kanumba amepatwa na mkasa ambao baadae ulisababisha kifo chake.
Na na hata nilipofika katika hospitali ya Muhimbili (tofauti na watu wanavyodhani kuwa nilifika nyumbani kwake; ukweli mimi nilimkuta tayari amepelekwa Muhimbili), nilikuta tayari alikuwa ameshafariki ndio maana hata Polisi wanaohusika na usalama wa raia, si tu kwamba hawakuniweka chini ya ulinzi, sikuitwa hata kuhojiwa kwa sababu hakuna mazingira yoyote yanayonihusisha mimi na kifo hicho.
Pili, watu wanahusisha tofauti za kibinadamu zilizokuwepo baina yetu na kifo hicho, nasema hii sio sahihi kwa sababu kwanza ni kawaida kwa binadamu kutofautiana, isipokuwa kwetu sisi baadhi ya vyombo vya habari vilikuwa vinakuza kwa sababu nisizozijua, hivyo jamii ikachukulia kuwa tofauti zile ni uadui kitu, ambacho sio sahihi, kwani sisi hatukuwa watu pekee tunaotofautiana kwani huu ni mwenendo wa kawaida wa dunia.
Hivi karibuni  tumeshuhudia waziri mmoja akieleza bayana katika mkutano na waandishi wa habari kuwa na tofauti na naibu wake, lakini hatujasikia ikiandikwa wana ‘bifu’,  bali imetafutwa lugha nzuri ya kupamba tofauti hizo, kwa kuwa waliohusika ni waheshimiwa, ila kwa wengine kutokana na sababu tusizozijua, inaonekana kama ni haki yetu kuandikwa vibaya.
Kinachosikitisha, kwa nini jambo hili linachukuliwa kwa mkazo mkubwa sana? Kwani hatujawahi kusikia watu wakiwa wanatofautiana na ndugu, jamaa, hata na marafiki zao na inaonekana kawaida tu? Kwani vyombo vya habari havikuwahi kuandika kuwa marehemu Steven Kanumba alikuwa na tofauti na baba yake na yeye mwenyewe alitamka hivyo katika vyombo vya habari? Mbona wameliongea bila kuongeza chumvi na jamii inaona kuwa ni jambo la kawaida la kibinadamu?
Pengine watu wanaojaribu kuongea hayo, hawajui mimi na Steven Kanumba tumetoka wapi? Sisi si watu tuliokutana barabarani, tuna historia katika kazi yetu ya sanaa na pia katika maisha yetu. Mwanzoni kabisa, mimi ndiye niliyempokea Kanumba pale Kaole na ndiye niliyemfundisha sanaa pale (nadhani watu wanakumbuka tamthilia za wakati huo ITV) na baada ya hapo tulienda pamoja katika kampuni ya Game 1st Quality na tukafanya filamu kama Johari, Sikitiko Langu, Dangerous Disire na nyinginezo, na tuliendelea kuwa pamoja katika kampuni hiyo mpaka tulipofanya filamu ya Oprah mwaka 2008, ambapo niliingia rasmi kufanya kazi za kampuni yangu, lakini tuliendelea kuwa pamoja hata wakati nikiendelea na kazi za kampuni yangu.
Pia mimi nilikuwa wa kwanza kuanza kufanya kazi na Steps na baadae Kanumba alipoanza kufanya kazi zake mwenyewe na kunikuta huko, tuliendelea kuwa pamoja kama siku zote.
Kitu kikubwa kilichokuwa kinaendelea baina yetu, ni kwamba tulijenga ushindani wa kuendeleza kazi mbele kwa kila mmoja akitoa kazi, mwingine anamjibu.  Isitoshe hata vitu vyetu binafsi utaona kama kuna kufanana. Kuna wakati Kanumba alinunua Toyota Rav 4 nyeusi, mimi nikanunua ya kijani. Aliponunua Harrier na mimi nikanunua pia, na hata gari za hivi karibuni, ukitazama utaona kuwa zinafana kwa karibu; hii ilikuwa ni kama maisha yetu, hatukuwa na uadui, ilikuwa tunapeana changamoto za maendeleo.
Watu wanaojaribu kuonyesha kuwa tofauti zetu ilikuwa ni uadui, huwa hawajui wapi tulikotoka ndio maana wanasema wasemavyo na katika kuthibitisha kuwa tofauti hizo hazikufikia katika uadui, kuna watu ambao wanafanya kazi nami katika kampuni yangu ya RJ ndio hao hao Kanumba alikuwa anawatumia siku zote katika kazi zake, hata baada ya tofauti hizo hakuna aliyekoma kufanya kazi na yeyote kati yetu.
Hii inathibitisha kuwa tofauti ilikuwa kati yetu kama binadamu, sio chuki za kimafanikio, ingekuwa hivyo watu kama Junior Syaary, ambaye mara nyingi hufanya uhariri wa mwisho katika RJ ndiye huyo huyo alikuwa akifanya na Kanumba.
Ally Yakuti, ambaye anaandika script za RJ, ndiye huyo huyo aliyekuwa anaandika kwa Kanumba, Steven Shoo ambaye ni mtaalamu wangu wa light, ndiye huyo huyo anayetumiwa na Kanumba na wengine wengi kama Juma Chikoka aliyecheza kikamilifu katika filamu ya kijiji cha Tambua Haki, ambaye pia anashiriki filamu nyingi za RJ, na wote hao, hawakuanzia kwa Kanumba, wote wameanza kwangu mimi ndio niliompatia na hata baada ya hayo yanayosemwa kuwa ni uadui, sikuwahi kuwakataza kufanya kazi na Kanumba.
Tatu, kumtuhumu mtu kwa namna yoyote ile bila ya uthibitisho wa tuhuma hizo, ni kosa kwa sheria za nchi na pia kama ni mfuasi wa dini yoyote ni dhambi, kwani wakati ukisema hayo huku, hujui uhalisia bali unasukumwa na nguvu za hisia tu ni sawa na kumchafua mtu huyo katika jamii bila ya kujua jamii inamchukuliaje.
Napenda kusema wazi wazi kuwa, kwa kila anayetekwa na wimbi hili, ajaribu kufikiria leo ipo kwangu mimi, kesho inaweza kuhamia kwako, kwani mimi sio wa kwanza kufikwa na haya, inaweza kukukuta hata wewe au ndugu yako, utajisikiaje.
Na kama kweli mimi nimehusika na kifo cha Kanumba kwa namna yoyote ile, basi Mungu atanihukumu na kila aliye hai atashuhudia, ila kama sijahusika kwa lolote, Mungu hatonihukumu na badala yake ataniinua, kwa kuwa ninapita katika kipindi kigumu mno sasa hivi kwa madhila haya.
Mwisho kabisa napenda kumaliza kwa msemo usemao, ajidhaniaye amesimama, aangalie asianguke, kwani kadri mambo haya yanavyoendelea, usidhani yataishia kwangu, kwani mkono wa dhuluma haushii karibu, ukisikia jirani anapiga kelele za mwizi, usilale kamsaidie, usiseme kuwa hatuhusiki kwani hayupo kwetu, kesho utafikwa na wewe utakosa wa kukusaidia.
Cha msingi kama tunampenda sana ndugu yetu ni kumuombea kwa Mungu, kwani hatujui makao yake huko aliko, na sio kuunda vitu ambavyo kamwe hata yeye angekuwa hai asingeviafiki.

Thursday, April 26, 2012

SIKU LULU ALIPOTINGA KIZIMBANI KWA MARA YA PILI

Ndolanga, El-Maamry watunukiwa urais wa heshima TFF


SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limewatunikia urais wa heshima wenyeviti wa zamani wa kilichokuwa Chama cha Soka Tanzania (FAT), Alhaji Muhidin Ndolanga na Said Hamad El-Maamry.
Uamuzi wa TFF kuwapa heshima hiyo Ndolanga na El-Maamry ulifikiwa wakati wa ufunguzi wa mkutano mkuu wa shirikisho hilo uliofanyika jana kwenye ukumbi wa Water Front mjini Dar es Salaam.
Akifungua mkutano huo, Rais wa TFF, Leodegar Tenga alisema wamefikia uamuzi huo kutokana kuheshimu kazi nzuri iliyofanywa na viongozi hao walipokuwa wakiiongoza FAT.
"Tulishazungumza siku za nyuma kwenye mkutano kama huu kwamba tutakuwa tunatoa nyadhifa za heshima kwa watu, ambao mchango wao unaonekana na unathaminiwa kwenye tasnia ya soka. Hivyo kwa kuanzia, tunawapa Ndolanga na El Maamry urais wa heshima wa TFF," alisema.
Tenga alisema wakati wakiwa viongozi wa FAT, Ndolanga na El Maamry walifanya kazi kwa ari na kujituma na hatimaye kuiletea Tanzania mafanikio makubwa kisoka.
Rais huyo wa TFF alisema anaamini, heshima hiyo itawafanya Ndolanga na El-Maamry waongeze moyo wa kujituma na kusaidia kukuza soka ya Tanzania kila watakapohitajika kufanya hivyo.
Tenga alisema kwa sasa Ndolanga ni mjumbe wa heshima katika Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki (CECAFA) wakati El-Maamry ni mjumbe wa heshima wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF).
Akizungumza baada ya kutunukiwa heshima hiyo, El Maamry aliishukuu TFF kwa kutambua na kuthamini kazi alizofanya wakati wa uongozi wake.
"Leo nimefarijika na nina furaha kubwa kwani hata nyumbani sasa wamekubali na wamethamini mchango wangu kwenye soka ya Tanzania. Kuna msemo unaosema 'Nabii havumi kwao,' lakini sasa umekuwa tofauti, ndiyo maana nimepewa urais wa heshima wa TFF," alisema.
  Kwa upande wake, Ndolanga alisema amefurahishwa na heshima aliyopewa na kuwataka viongozi wa vyama vya mikoa, klabu na TFF kuendelea kumtumia Tenga katika kuboresha soka ya Tanzania kwa sababu bado anahitajika kwa kiasi kikubwa.
"Mara nyingi tumezoea kuwatunuku tuzo za heshima kama hizi watu waliokufa, lakini naishukuru sana TFF kwa kuamua kunipa heshima hii wakati nikiwa hai kwani binafsi imenifurahisha kwa vile inaonyesha ni jinsi gani nilivyochangia kuinua soka yetu," alisema.
Ndolanga pia aliwataka viongozi wa vyama vya soka vya mikoa kuhakikisha kuwa, soka inachezwa katika mikoa yote nchini badala ya kuuacha mkoa wa Dar es Salaam pekee ukitamba katika mchezo huo.
Katika hatua nyingine, TFF imesema fedha ilizoahidi kuvipatia vyama vya soka vya mikoa na vyama shirikishi vya shirikisho hilo, zitaanza kutolewa kesho.
Tenga alisema jana kuwa, fedha hizo zitatolewa kwa njia ya hundi na lazima zitiwe saini na mwenyekiti pamoja na katibu wa chama husika. Alisema kila chama cha soka cha mkoa kitapatiwa sh. milioni mbili wakati vyama shiriki vitapatiwa sh. milioni moja.
Rais huyo wa TFF alisema fedha hizo zinapaswa kutumika kuandaa semina, kozi, kununulia samani za ofisi na kuendesha michuano ya vijana kwa lengo la kuinua viwango vya soka mikoani.

Wednesday, April 18, 2012

BANZA: Sina mkataba na Extra Bongo

MTUNZI na mwimbaji mahiri wa nyimbo za muziki wa dansi nchini, Ramadhani Masanja ‘Banza Stone’ amefichua kuwa, hana mkataba na bendi ya Extra Bongo.
Banza amesema amekuwa akifanyakazi katika bendi hiyo kiurafiki, kutokana na makubaliano waliyofikia kati yake na kiongozi wa Extra Bongo, Ally Choki.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Banza alisema aliamua kujiunga na Extra Bongo kwa vile hakuwa na bendi ya kudumu.
“Choki alinifuata, akaniambia ‘Banza kwa sasa huna mahali, ambako watu wakikutafuta, watakupata. Njoo ujiunge nami Extra Bongo’ nami nikaona ni kweli, nikakubali,”alisema.
“Nilikuwa sina mahali pa kudumu, nilikuwa nahangaika, nikaamua nifanyekazi na Choki na nipo Extra Bongo hadi sasa,”aliongeza mwanamuziki huyo wa zamani wa Twanga Pepeta International.
Banza aliutetea uamuzi wake huo kwamba hauna tatizo kwa vile yeye na Choki ni marafiki na kwamba hata katika maslahi yake, hawezi kumdhulumu.
Mtunzi na mwimbaji huyo mwenye kipaji aliwahi kutamba katika bendi mbalimbali nchini, zikiwemo TOT Plus, Bambino Sound na Rufita.
Mbali na kuimba nyimbo za muziki wa dansi, Banza pia anao uwezo wa kuimba nyimbo za taarab. Kibao chake cha kwanza cha muziki huo kinajulikana kwa jina la ‘Wamezoea kusema’.
Kwa sasa, Banza anajiandaa kurekodi kibao kingine cha muziki huo, akisaidiwa na kiongozi msaidizi wa Mashauzi Classic, Thabiti Abdul.

AT awashukuru mashabiki wake

SIKU chache baada ya wimbo wake wa ‘Kifuku mtu’ kushinda tuzo za muziki za Kilimanjaro, msanii AT amesema alistahili kupata tuzo hiyo kutokana na wimbo wake kukubalika kwa mashabiki.
AT alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, wimbo wake huo umekuwa ukipigwa mara kwa mara na vituo vya redio na televisheni nchini kutokana na mvuto wake.
Kibao hicho cha AT, kilichopigwa katika miondoko ya mduara, kimeshinda tuzo ya wimbo bora wenye vionjo vya kiasili.
“Namshukuru sana Mungu kwa kuniwezesha kushinda tuzo hii na hii ni kutokana na wimbo wangu kukubalika na mashabiki,”alisema.
AT alisema msanii anapotaka kukubalika kwa mashabiki, anapaswa kuwa karibu nao badala ya kujitenga na kuwa mbali mbali nao.
Msanii huyo pia alitoa mwito kwa wasanii kutunga nyimbo zenye mvuto na zinazogusa jamii badala ya kutunga zaidi nyimbo za mapenzi.
“Nawashukuru mashabiki wote walionipigia kura na pia vituo vya redio na televisheni kwa kupiga nyimbo zangu mara kwa mara,”alisema.
Hii ni mara ya tatu kwa AT kushiriki kwenye tuzo hizo. Alishiriki kwa mara ya kwanza mwaka juzi kupitia kibao chake cha Nipigie alichomshirikisha Stara Thomas na mwaka jana kupitia kibao cha Mama ntilie, alichomshirikisha Ray C.

Mashauzi awapa tano waandaaji tuzo za Kili

MWIMBAJI nguli wa muziki wa taarab nchini, Isha Ramadhani ‘Mashauzi’ amewapongeza waandaaji wa tuzo za muziki za Kilimanjaro kwa kufanya mabadiliko makubwa katika utoaji wa tuzo.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Isha alisema wasanii waliopata tuzo mwishoni mwa wiki iliyopita walistahili kutokana na maudhui ya nyimbo zao na pia kukubalika na mashabiki.
Isha, ambaye ameshinda tuzo ya wimbo bora wa taarab wa mwaka kupitia kibao chake cha ‘Nani kama mama’ alisema, ni vyema mwanamuziki apate tuzo kutokana na muziki wake kufanya vizuri na pia kukubalika kwake na mashabiki badala ya kubebwa.
“Kusema kweli, safari hii yapo mabadiliko makubwa na waandaaji wamejitahidi sana kurekebisha dosari zilizokuwa zikijitokeza miaka iliyopita,”alisema.
Mwanamama huyo anayemiliki kundi la taarab la Mashauzi Classic alisema, anaamini kilichomwezesha kushinda tuzo za mwaka jana ni kukubalika kwake na mashabiki wa muziki huo.
“Mwaka jana nilikerwa sana na utoaji wa tuzo hizo kwa sababu wimbo wangu wa ‘Mama nipe radhi’ ulikuwa na maudhui mazuri kuliko nyimbo zingine zilizoshindanishwa na ulipendwa sana na mashabiki.
“Siku zote wimbo mzuri hauchoshi kuusikiliza na wala hauchujiki kwa miaka elfu. Nyimbo za mapenzi zinachosha. Kama ni mapenzi yalianza tangu enzi za Adamu na Hawa na hadi leo watu wanazungumzia mapenzi. Lakini kuna vitu hata vikikaa miaka hamsini, ujumbe wake haufi,”alisema mwanamama huyo mwenye mwili tipwatipwa.
Isha alisema amepata faraja kubwa kuwa miongoni mwa washindi wa tuzo hizo na kuongeza kuwa, lengo lake ni kutunga nyimbo zenye mwelekeo tofauti na masuala ya mapenzi.
Alimshukuru mama yake mzazi, Rukia Juma na kiongozi msaidizi wa Mashauzi Classic, Thabiti Abdul, ambao amewauelezea kuwa wamekuwa msaada mkubwa kwake kimuziki.
Vilevile amewapongeza mashabiki wa muziki huo kwa kumpigia kura nyingi na kusema kuwa, bila wao asingeweza kupata mafanikio aliyonayo sasa.
Hii ni mara ya tatu kwa Isha kushiriki kwenye tuzo hizo. Mwaka juzi alishindanishwa kupitia kibao cha Ya wenzenu midomo juu alichokiimba na kundi la Jahazi na mwaka jana alishiriki kupitia kibao cha Mama nipe radhi.

JUA CALI: Muziki umeniwezesha kumiliki studio



MSANII nyota wa muziki kutoka Kenya, Jua Cali amesema fani hiyo imemwezesha kupata manufaa mengi kimaisha, ikiwa ni pamoja na kumiliki studio yake mwenyewe.
Mbali na kujenga studio, Jua Cali amesema muziki umemwezesha kupata pesa nyingi na kuwasaidia watu kadhaa wenye matatizo.
Jua Cali alisema hayo hivi karibuni alipokuja kufanya onyesho la pamoja na msanii Juma Kassim ‘Nature’ lililofanyika kwenye ukumbi wa Dar Live mjini Dar es Salaam.
“Ukiuheshimu muziki na kufanyakazi kwa kujituma, utaweza kupata mafanikio makubwa kimaisha,”alisema msanii huyo, ambaye ni kipenzi cha walala hoi nchini Kenya.
Jua Cali alisema kwa sasa anakaribia kukamilisha ujenzi wa nyumba yake na hayo yote yametokana na kazi ya muziki.
Kwa sasa, Jua Cali anatamba kwa kibao chake kipya kinachojulikana kwa jina la Genge, ambacho kimekuwa kikishika chati za juu kwenye vituo mbalimbali vya redio na televisheni nchini Kenya.
Akizungumzia muziki wa bongo fleva, Jua Cali alisema anavutiwa na msanii Nature kutokana na nyimbo zake kuwa na mvuto na pia kukubalika na mashabiki wa hali ya chini.
“Nampenda sana Juma Nature kwa sababu nyimbo zake zinawagusa sana watu wa maisha ya chini na anakubalika sana Bongo. Na mimi nakubalika sana Kenya kwa sababu hiyo hiyo,”alisema.
Alipoulizwa kuhusu madhumuni ya onyesho lake na Nature, alisema halikuwa na lengo la kutafuta pesa zaidi ya kuwapa burudani mashabiki.
Jua Cali alisema bado hajafunga ndoa na wala hana mtoto. Alisema anaye mchumba na wanatarajia kufunga ndoa hivi karibuni.

MAFISANGO: NITAENDELEA KUCHEKA NA NYAVU

KIUNGO mahiri wa klabu ya Simba, Patrick Mafisango amesema ataendelea kufunga mabao mengi zaidi katika mechi zao zilizosalia za michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Mafisango alisema yeye na wachezaji wenzake wanafurahia mbinu mpya za soka wanazofundishwa na Kocha Milovan Cirkovic.
Mafisango, ambaye ni raia wa Rwanda alisema, ushirikiano uliopo kati ya viongozi na wachezaji wa Simba ni miongoni mwa mambo yaliyochangia timu hiyo kupata mafanikio.
Kiungo huyo ndiye aliyeifungia Simba bao pekee na la ushindi katika mechi yake ya ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Ruvu Shooting iliyochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
"Lengo letu ni kutwaa ubingwa wa ligi kuu msimu huu na hilo litawezekana kama tutashinda mechi zetu zote zilizosalia na dhamira yangu ni kuendelea kufunga mabao,"alisema.
Mafisango alisema uamuzi wake wa kuja kucheza soka ya kulipwa nchini, umelenga kukuza kipaji chake na pia kuongeza kipato, hivyo hawezi kufanya mzaha katika soka.
Amewashukuru wachezaji wenzake kwa kumpa ushirikiano mkubwa ndani na nje ya uwanja na kuongeza kuwa, mafanikio ya Simba kwa kiasi kikubwa yanachangiwa na mshikamano uliopo miongoni mwao.
Mafisango alisema ana imani Kocha Milovan ataendelea kumwamini na kumpa namba kwenye kikosi chake ili aweze kudhihirisha uwezo wake.

RAGE: Tunawaandalia zawadi nono nyota wetu

MWENYEKITI wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage amejigamba kuwa, wamewaandalia zawadi nzuri wachezaji wao iwapo timu hiyo itatwaa ubingwa wa ligi kuu ya Tanzania Bara msimu huu.
Rage alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, wamefikia uamuzi huo baada ya kukutana na wachezaji wao mwishoni mwa wiki iliyopita.
Mwenyekiti huyo wa Simba alisema wameamua kuwaandalia zawadi wachezaji wao ili kuwaongezea ari katika mechi za mwisho za ligi kuu.
"Tulizungumza na wachezaji mambo mengi ya msingi na kuna mambo mazito tuliyowaandalia kwa sababu wamekuwa wakitupa raha sana. Isingekuwa jitihada zao, hali ingekuwa mbaya sana,"alisema.
Simba inaongoza ligi kuu ya Tanzania Bara kwa kuwa na pointi 53 na jana ilitarajiwa kucheza mechi nyingine dhidi ya JKT Ruvu.
Akizungumzia maandalizi ya mechi yao ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Al Ahly Shandy ya Sudan, Rage alisema wameshaanza kujipanga ili kuhakikisha wanashinda pambano hilo.
Pambano kati ya Simba na Shandy limepangwa kuchezwa Aprili 29 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kabla ya timu hizo kurudiana wiki mbili baadaye nchini Sudan.
"Siwezi kusema tumepanga kufanya nini katika mechi hiyo, lakini uongozi pamoja na benchi la ufundi tumeshafanya kikao cha kujadili mechi hiyo na pia kupeana majukumu ya kufanya,"alisema.

Sistaafu ndondi hadi nipigwe nyakanyaka-Matumla

BONDIA mkongwe wa ngumi za kulipwa nchini, Rashid Matumla 'Snake Boy' amesema hatarajii kustaafu mchezo huo hivi karibuni.
Akihojiwa katika kipindi cha Jambo kilichorushwa hewani na TBC 1 hivi karibuni, Matumla alisema bado hajaona sababu za kumfanya astaafu ndondi hizo.
"Siwezi kustaafu kwa sasa kwa sababu sijaona bondia wa kunisambaratisha,"alisema.
Bondia huyo aliyeweka rekodi ya kutwaa mkanda wa mabara na ubingwa wa dunia wa uzani wa middle alisema, hajawahi kupata kipigo kizito kinachoweza kumfanya aseme sasa basi.
"Sijawahi kupigwa hadi nikachakazwa. Angewahi kutokea bondia wa aina hiyo, ningeshastaafu ngumi miaka mingi iliyopita,"alisema.
Hivi karibuni, Matumla alidundwa kwa pointi na Maneno Osward katika pambano lisilo la ubingwa lililofanyika kwenye ukumbi wa Dar Live, Mbagala, Dar es Salaam.
"Katika ngumi, upo muda wa kustaafu, ukifika nami nitafanya hivyo,"alisisitiza.
Matumla alisema ameshapigana na Maneno mara nyingi na kuongeza kuwa, haoni iwapo ana upinzani mkubwa sana kwake.
Pambano kati ya Matumla na Maneno lilikuwa la tano kuwakutanisha mabondia hao. Matumla ameshinda mapambano matatu wakati Maneno ameshinda mawili.
Kwa mujibu wa Matumla, anatarajia kuzipiga tena na Maneno hivi karibuni mkoani Kilimanjaro.
Alisema ameamua kuzipiga tena na Maneno kwa sababu sheria za ndondi zinaruhusu mabondia kupigana mara zozote na pia iwapo mapromota wataona pambano hilo lina maslahi kwao.
Matumla alisema hahofii sura yake kubadilika kwa sababu ya kukumbwa na ngumi nzito kutoka kwa wapinzani wake kwa sababu hivyo ndivyo mchezo huo ulivyo.
"Katika ndondi, unakwepa na kupiga, mambo ya sura kuharibika ni matokeo,"alisema.
Pamoja na kucheza ngumi kwa miaka mingi, Matumla alisema mchezo huo hauna maslahi makubwa kwa mabondia wa Tanzania na kwamba wanapigana kwa sababu ya kutafuta pesa za kuendesha maisha yao.
Alisema moja ya mikakati yake katika siku zijazo ni kuanzisha shule yake ya ndondi. Alisema anatarajia kuanzisha shule hiyo mkoani Kilimanjaro.
Alimtaja bondia wa ngumi za kulipwa anayemvutia kuwa niFrancis Miyeyusho, ambaye amewahi kupigana mara kadhaa na ndugu yake,Mbwana Matumla.
Matumla, ambaye pia ni mmoja wa viongozi wa kamisheni ya ngumi za kulipwa nchini (TPBC), anaye mtoto wa kiume, ambaye ndiye aliyerithi kipaji chake.

MSONDO KAZINI

KIONGOZI wa bendi ya muziki wa dansi ya Msondo Ngoma, Muhidin Gurumo (katikati) akiimba na waimbaji wengine wa bendi hiyo, Hassan Moshi (kushoto) na Juma Katundu wakati wa onyesho lililofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye viwanja vya klabu ya Sigara, Chang'ombe, Dar es Salaam. (Picha na Emmanuel Ndege).

ALLY CHOKI: Situmii uchawi kuvuta mashabiki



Akiri kutokuwa na uhusiano mzuri na Asha Baraka
Asema hanywi pombe wala kutumia dawa za kulevya

Aziponda tuzo za Kili
KIONGOZI wa bendi ya muziki wa dansi ya Extra Bongo, Ally Choki amekiri kuwa, baadhi ya bendi zimekuwa zikitumia uchawi ili kuvuta mashabiki
Choki amekiri pia kuwa, ugonjwa wa ukimwi umesambaratisha maisha ya wanamuziki wengi kutokana na kuendekeza starehe na kutochukua tahadhari.
Mwanamuziki huyo wa zamani wa bendi za Twanga Pepeta, Achigo, Bantu Group, TOT Plus na Mchinga Sound, alisema hayo mwanzoni mwa wiki hii alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha Mkasi kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha East Africa.
Choki alisema zipo baadhi ya bendi, ambazo hazipigi kwenye kumbi fulani kutokana na kuwepo kwa imani za ushirikiana na hata wanamuziki wake hawasaidiani kwa sababu ya imani hizo.
“Mimi situmii mambo ya uchawi, lakini upo na baadhi ya bendi zinafanya hivyo ili kuvutia mashabiki,”alisema.
Alikuwa akijibu swali aliloulizwa na mtangazaji wa kipindi hicho, Salama Jabir aliyetaka kujua iwapo ni kweli baada ya maonyesho viongozi wa bendi hukusanya vitu fulani ukumbini kwa lengo la kuvifanyia ushirikina.
Choki alisema binafsi hana tatizo na viongozi wa baadhi ya bendi alizowahi kupigia, lakini alikiri kuwa kwa sasa hana maelewano mazuri na mmiliki wa bendi ya Twanga Pepeta, Asha Baraka.
“Tatizo la mama yetu Asha hajui kwamba kila mwanamuziki anahitaji kuwa na maisha mazuri hivyo kuhama kutoka bendi moja kwenda nyingine ni sehemu ya maisha,”alisema.
Mwimbaji huyo mwenye kipaji na mvuto alikiri pia kuwa, utumiaji wa dawa za kulevya umekuwa ukiwaathiri wanamuziki wengi nchini japokuwa wengi wanaofanya hivyo ni kwa sababu yah obi.
Alisema binafsi hajawahi kutumia dawa hizo, lakini aliwahi kunywa pombe miaka kadhaa iliyopita kabla ya kuamua kuacha baada ya kuona haina faida kwake.
“Kama ni kuvuta unga, ningeuvuta nilipokuwa naishi Kinondoni kwa sababu nilikuwa naishi karibu na nyumba ya wavuta unga, lakini sikuthubutu kufanya hivyo kutokana na kutambua athari zake,”alisema.
Alipoulizwa kuhusu athari ya ukimwi kwa wanamuziki, Choki alikiri kuwa, ugonjwa huo umepoteza maisha ya wanamuziki wengi kutokana na ugonjwa huo kwa sababu ya kuendekeza starehe.
Choki alisema pia kuwa, baadhi ya wanamuziki walishindwa kujipanga vyema kwa ajili ya maisha yao ya baadaye na pale waliposhtuka, walijikuta wakiwa na familia kubwa na hivyo kushindwa kuzihudumia inavyotakiwa.
Kiongozi huyo wa Extra Bongo alisema hakuna tukio lililowahi kumshtua na kumuhuzinisha katika maisha yake kama vifo vya wasanii 13 wa kundi la taarabu la Five Stars vilivyotokana na ajali ya gari iliyotokea mwaka jana mkoani Morogoro.
Alisema kabla ya ajali hiyo, alikuwa na mpango wa kurekodi wimbo na mwimbaji Zena Hamisi wa kundi hilo na alizungumza naye kwa simu siku moja kabla ya ajali hiyo akimkumbusha kuhusu azma yake hiyo.
“Nikaja kushtuka kesho yake baada ya kupigiwa simu na kuelezwa kuwa, wanamuziki wote wa Five Stars wamekufa katika ajali ya gari. Muda huo huo nikampigia simu Zena kwa bahati nzuri akapokea, lakini alikuwa akilia kwa sababu walikuwa bado wapo eneo la ajali,”alisema.
Mwanamuziki huyo alisema maisha ya wanamuziki siku zote yapo hatarini kutokana na kusafiri mara kwa mara mikoani na kuongeza kuwa, hata bendi yake iliwahi kunusurika katika ajali ya gari iliyotokea mapema mwaka huu mkoani Iringa.
Choki alisema hapendezwi na tabia ya baadhi ya mapedeshee kupenda kuwatongoza wanawake wanaocheza shoo katika bendi mbalimbali za muziki nchini.
Alisema hawezi kuruhusu tabia hiyo katika bendi yake na aliwaita mapedeshee hao kuwa ni watu wasiojiamini.
Mwimbaji huyo nguli alisema kamwe hawezi kuyasahau matukio matatu makubwa yaliyomtokea alipokuwa katika bendi ya Twanga Pepeta. Aliyataja matukio hayo kuwa ni yale ya kuingia kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee kwa kutumia farasi, ngamia na kijiko.
Alisema tukio la kuingia ukumbini kwa farasa lilikuwa na mvuto zaidi kwa sababu mnyama huyo alimwangusha sakafuni baada ya shabiki mmoja kujaribu kupita katikati ya miguu yake.
Choki alisema pia kuwa, tukio la kuingia ukumbini na ngamia nalo lilikuwa na vioja kwake kwa sababu mnyama huyo aligoma kuendelea na safari baada ya kusikia kelele za mashabiki ukumbini.
Mwanamuziki huyo alisema katika maisha yake, anachukizwa na maneno ya uongo kwa sababu yanaweza kumweka mtu kwenye wakati mgumu kimaisha na hata kupoteza maisha yake kwa kihoro.
Akizungumzia tuzo za muziki za Kilimanjaro, Choki alisema aliamua kujitoa kuanzia mwaka jana baada ya kubaini kuwepo kwa mapungufu kadhaa na pia kutokuwa na mwelekeo mzuri.
Akifafanua, alisema upangaji wa tuzo hizo ni mbovu kutokana na waandaaji kuwashindanisha wasanii wanaopiga aina tofauti ya muziki.
“Huwezi kumshindanisha Khadija Kopa na Shaa au Mzee Yusuph na Diamond kwa sababu muziki wanaopiga ni tofauti na wao wenyewe ni vizazi tofauti.
“Pia huwezi kunishindanisha mimi na Mzee Gurumo kwa sababu ni vizazi tofauti. Kila aina ya muziki inapaswa kuwa na tuzo zake,”alisisitiza.

SIMBA BINGWA 90%, YANGA YATEMA TAJI

SIMBA jana ilizidi kujisafishia njia ya kutwaa ubingwa wa ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kuichapa JKT Ruvu mabao 3-0 katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Wakati Simba ikiibuka na ushindi huo mnono, watani wao wa jadi Yanga jana walichapwa bao 1-0 na Kagera Sugar katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.
Kwa matokeo hayo, Simba inaongoza ligi hiyo kwa kuwa na pointi 56 baada ya kucheza mechi 24, ikifuatiwa na Azam yenye pointi 50. Yanga ni ya tatu ikiwa na pointi 43.
Simba sasa inahitaji kuishinda Moro United zitakapomenyana Aprili 25 mwaka huu ili ijihakikishie kutwaa taji hilo, lakini itategemea zaidi matokeo kati ya Azam na Mtibwa zitakazomenyana Jumamosi.
Iliwachukua Simba dakika moja kuhesabu bao la kwanza lililofungwa na Uhuru Selemani baada ya kupokea pasi maridhawa kutoka kwa Emmanuel Okwi.
Haruna Moshi ‘Boban’ aliifungia Simba bao la pili dakika ya 17 baada ya kuwapiga chenga viungo na mabeki wa JKT Ruvu kabla ya kufumua shuti kali lililopita kushoto kwa kipa Amani Simba.
Simba ilipata nafasi zingine nzuri za kufunga mabao dakika ya 35 na 41 baada ya Uhuru na Kago kupewa pasi wakiwa ndani ya eneo la hatari, lakini mipira waliyopiga ilitoka nje ya lango la JKT.
JKT Ruvu ilipata nafasi pekee nzuri ya kufunga bao dakika ya 44 wakati Hussein Bunu alipopewa pasi murua na Mohamed Banka huku kipa Juma Kaseja wa Simba na mabeki wake wakiwa wamepoteana, lakini shuti lake lilitoka nje.
Bao la tatu la Simba lilifungwa na Mwinyi Kazimoto dakika ya 64 baada ya kuunganisha wavuni kwa shuti kali la mbali mpira wa adhabu ndogo.
Habari kutoka Bukoba zimeeleza kuwa, bao pekee na la ushindi la Kagera Sugar lilifungwa na Shija Mkina katika kipindi cha pili.
Kipigo hicho kilikuwa cha pili kwa Yanga katika muda wa siku nne baada ya mwishoni mwa wiki iliyopita kupigwa mweleka wa mabao 3-2 na Toto African mjini Mwanza.
SIMBA: Juma Kaseja, Shomari Kapombe, Amir Maftah, Juma Nyoso, Kevin Yondan, Patrick Mafisango, Uhuru Selemani, Mwinyi Kazimoto, Gervas Kago, Haruna Moshi ‘Boban’ na Emmanuel Okwi.
JKT Ruvu: Amani Simba, Kessy Mapande, John Mhidze, Hassan Kikutwa, George Minja, Jimmy Shoti, Haruna John, Nashon Matari, Hussein Bunu, Mohamed Banka/George Mketo na Emmanuel Pius.

Sunzo out Simba, Okwi chini ya ulinzi

Felix Sunzu

Emmanuel Okwi


UONGOZI wa klabu ya Simba umesema mshambuliaji Felix Sunzu ni mgonjwa na hataweza kucheza mechi zilizosalia za michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara.
Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, Sunzu anasumbuliwa na maumivu ya tumbo na hali yake si nzuri.
Kamwaga alisema kutokana na kusumbuliwa na ugonjwa huo, Sunzu hakuweza kucheza mechi ya ligi dhidi ya Ruvu Shooting mwishoni mwa wiki iliyopita na alitarajiwa kukosa mechi nyingine dhidi ya JKT Ruvu jana.
Hata hivyo, Kamwaga alisema tayari mshambuliaji huyo kutoka Zambia ameshaanza kupatiwa matibabu na iwapo atapata nafuu haraka, anaweza kucheza mechi hizo.
Baada ya kucheza na JKT Ruvu jana, Simba inakabiliwa na mechi zingine mbili kabla ya kuhitimisha ligi hiyo kwa kupambana na Moro United na Yanga.
Mbali na mechi hizo za ligi, Simba pia inakabiliwa na mechi mbili za raundi ya tatu ya michuano ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Al-Ahly Shandy ya Sudan. Mechi ya awali itachezwa Aprili 29 mjini Dar es Salaam na ya marudiano wiki mbili baadaye nchini Sudan. Katika hatua nyingine, Kamwaga amewataka waamuzi wa ligi kuu kumlinda mshambuliaji Emmanuel Okwi wa Simba kutokana na kukamiwa na timu pinzani.
Kamwaga alisema Okwi amekuwa akichezewa vibaya katika kila mechi kutokana na kiwango chake kuwa juu na kusababisha aumie mara kwa mara.
Akitoa mfano, alisema katika mechi kati ya Simba na Ruvu Shooting, mchezaji huyo alichezewa rafu mara 17, lakini mwamuzi alitoa kadi moja ya njano.
"Kwa kweli Okwi yupo kwenye wakati mgumu kwa sababu wakati mwingine inaonekana wazi kuwa, wachezaji wa timu pinzani wanataka kumvunja, hivyo amekuwa akicheza kwa woga na tahadhari kubwa,”alisema.

BHINDA, MWESIGWA KUTIMULIWA YANGA?

HALI imeanza kuwa si shwari ndani ya klabu ya Yanga baada ya baadhi ya wanachama na wazee wa klabu hiyo kushinikiza Katibu Mkuu, Selestine Mwesigwa na Mkurugenzi wa Ufundi, Mohamed Bhinda wajiuzulu.
Wakizungumza makao makuu ya klabu hiyo mitaa ya Twiga na Jangwani mjini Dar es Salaam jana, wanachama na wazee hao walidai kuwa, viongozi hao wawili wa Yanga wanapaswa kuwajibika.
Shinikizo la wazee na wanachama hao limekuja siku moja baada ya Kamati ya Nidhamu na Usuluhishi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kubariki Yanga kupokwa pointi tatu na Kamati ya Ligi.
Kamati ya Ligi ilifikia uamuzi huo baada ya Yanga kumchezesha beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’ katika mechi yao ya ligi kuu dhidi ya Coastal Union iliyochezwa Machi 31 mwaka huu mjini Tanga wakati alikuwa na kadi nyekundu na alipaswa kukosa mechi tatu.
Wanachama hao, ambao hawakutaka majina yao yatajwe gazetini walidai kuwa, uamuzi wa kamati ya nidhamu na usuluhishikuipoka Yanga pointi tatu ni uthibitisho wa wazi wa viongozi hao kushindwa kutekeleza vyema majukumu yao.
Walisema akiwa mkurugenzi wa ufundi, Bhinda hakupaswa kumruhusu beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’ acheze mechi hiyo kutokana na kuwa na kadi hiyo nyekundu wakati yeye ndiye anayetunza rekodi zote za wachezaji.
“Huu ni uzembe wa hali ya juu na hatuwezi kuuvumilia, hivyo ni vyema Bhinda awajibike mara moja badala ya kusubiri kutimuliwa,”alisema.
Mmoja wa wanachama hao alisema, Mwesigwa naye anapaswa kuondoka madarakani kwa madai kuwa, amekaimu nafasi hiyo kwa miezi sita bila kuthibitishwa na wanachama na hivyo kukiuka katiba ya klabu hiyo.
Wanachama hao pia walihoji uamuzi wa Bhinda kukodi basi kwa ajili ya kuisafirisha timu kwenda Mwanza wakati wangeweza kutumia basi la klabu hiyo lililotolewa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL).
Wamemtaka Mwenyekiti wa klabu hiyo, Lloyd Nchunga kuitisha haraka mkutano wa wanachama ili waweze kujadili masuala mbalimbali, ikiwemo kupokwa pointi kwa timu hiyo katika mechi yake dhidi ya Coastal Union.
Nchunga hakuweza kupatikana jana kuzungumzia madai hayo ya wanachama kutokana na simu yake kutopokelewa wakati simu ya Mwesigwa ilikuwa haipatikani.

MBUNGE AMUUMBUA WAZIRI BUNGENI

MBUNGE wa Kinondoni, Iddi Azzan amemuumbua Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukandala kwa kutoa taarifa potofu.
Azzan amesema pia kuwa, amesikitishwa na majibu yaliyotolewa na serikali, ambayo hayakuwa sahihi na kuongeza kuwa, huenda haikufanya utafiti kutokana na kile ilichoulizwa.
Mbunge huyo alitoa malalamiko hayo bungeni jana baada ya majibu ya Dk. Fennela kwa Ahmed Juma Ngwali (Ziwani), aliyetaka kufahamu mafanikio ya msingi liliyopata Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) tangu lilipojiunga na Shirikisho la Soka Dunia (FIFA) mwaka 1964.
Akijibu swali hilo, Dk. Fenella alisema TFF imepata mafanikio mengi ya msingi, ikiwemo kukuza na kuendeleza mpira wa miguu nchini pamoja na kuweka muundo wa utawala katika ngazi zote ambao unatekelezeka.
Naibu waziri alisema pia kuwa, TFF imeandaa na kuendesha programu mbalimbali ikiwa ni pamoja na mashindano ya timu za vijana, wanawake na watoto kama sehemu ya kuweka misingi bora ya maendeleo ya soka.
Alisema katika kipindi hicho, timu ya taifa iliweza kutwaa kombe la Chalenji mara tano huku klabu za Simba na Yanga zikinyakua Kombe la klabu bingwa Afrika Mashariki mara moja kila mmoja.
Mara baada ya majibu hayo, Azzan alisimama na kuomba kutoa taarifa, ambapo Naibu Spika wa Bunge alimtaka kuvuta subira kwanza.
Alipopewa nafasi hiyo, Azzan alisema majibu yaliyotolewa na serikali kupitia Dk. Fennela si sahihi kwa vile si kweli kwamba Simba na Yanga zimenyakua ubingwa wa Afrika Mashariki mara moja kila moja.
Alisema Simba imenyakua ubingwa huo mara sita, Yanga mara tano na timu ya Taifa imebeba Kombe la Chalenji mara tatu.
“Majibu ya serikali yanasikitisha mno na nadhani hayajafanyiwa utafiti,” alisema mbunge huyo na kuufanya ukumbi kuwa kimya.

MARUFUKU KUMTEMBELEA LULU MAHABUSU

JESHI la Magereza nchini limepiga marufuku watu wasiokuwa na uhusiano na msanii chipukizi wa filamu nchini, Elizabeth Michael ‘Lulu’ kumtembelea katika mahabusu ya Segerea.
Lulu anashikiliwa katika gereza hilo kwa tuhuma za mauaji ya msanii nyota wa filamu nchini, Steven Kanumba baada ya kufikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza wiki iliyopita.
Habari zilizotangazwa na kituo cha Radio One jana zilieleza kuwa, kwenye ubao wa matangazo ndani ya gereza hilo, kumeandikwa barua inayotoa maelekezo kuhusu watu wanaopaswa kumuona Lulu.
Kwa mujibu wa barua hiyo, watu wanaopaswa kumtembelea Lulu kwenye mahabusu hiyo ni mama yake mzazi, dada yake na mjomba wake, ambao picha zao zimebandikwa kwenye ubao huo wa matangazo.
“Watu wamezusha sana maneno kuwa, askari wamepiga marufuku hakuna mtu yeyote kumtembelea Lulu, ni uzushi tu,” alisema mmoja wa watangazaji wa kipindi hicho aliyetembelea kwenye mahabusu hiyo juzi.
Lulu anatuhumiwa kuhusika na kifo cha Kanumba, aliyefariki usiku wa kuamkia Aprili 7 na mazishi yake kufanyika Aprili 10 mwaka huu. Alifikishwa kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Kisutu kwa mara ya kwanza wiki iliyopita na kesi yake itatajwa tena Aprili 23 mwaka huu.
Wakati huo huo, upande wa mashitaka katika kesi ya kutakatisha fedha haramu inayomkabili msanii maarufu wa filamu nchini, Kajala Masanja na mumewe Faraji Chambo inatarajiwa kuwa na mashahidi 13 na vielelezo tisa.
Kajala na Chambo walipandishwa kizimbani jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam mbele ya Hakimu Mkazi, Sundi Fimbo.
Wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCB), Leonard Swai alidai kesi hiyo ilifikishwa mahakamani hapo kwa ajili ya kuwasomea maelezo ya awali washitakiwa hao.
Katika maelezo hayo, washitakiwa walikubali baadhi ya mambo kuwa ni mume na mke, waliuza nyumba kwa Emiliana Regarulila na Chambo alikubali alikuwa ni mtumishi wa benki ya NBC mwaka 2008.
Washitakiwa walikataa kupewa notisi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali wasiuze nyumba hiyo kwa sababu ilikuwa kwenye uchunguzi, hawakwenda kinyume na notisi hiyo na kumuuzia nyumba Emiliana.
Mambo mengine waliyokataa ni kwamba hawakuhamisha nyumba hiyo kwa Emiliana kwa kutumia fedha za rushwa.
Swai alidai wanatarajia kuwa na mashahidi hao na vielelezo hivyo na Hakimu Mkazi Sundi alisema kesi hiyo itaanza kusikilizwa Aprili 30, mwaka huu.

Saturday, April 14, 2012

BONGO MOVIE KUICHANGIA TWIGA STARS

Timu ya Taifa ya mpira wa miguu kwa wanawake (Twiga Stars) itacheza mechi ya kirafiki na timu ya wasanii wa filamu ya Bongo Movie itakayofanyika Jumamosi (Aprili 14 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Lengo la mechi hiyo ya maonesho (exhibition) ni kuichangia Twiga Stars ambayo hivi sasa iko kwenye mashindano ya mchujo ya Kombe la Afrika kwa Wanawake (AWC) ambayo fainali zake zitafanyika Novemba mwaka huu nchini Equatorial Guinea.

Pia asilimia mbili ya mapato yatakayopatikana kwenye mechi ya Twiga Stars na Bongo Movie yatakwenda kwenye familia ya mwigizaji nguli wa filamu Tanzania, Stephen Kanumba aliyefariki dunia Aprili 7 mwaka huu.

Kiingilio katika mechi hiyo kitakuwa sh. 10,000 kwa VIP A, sh. 5,000 kwa VIP C na B na sh. 2,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, kijani na bluu. Mechi itaanza saa 10 kamili jioni.

Machi 10 mwaka huu, Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara alizindua akaunti ya Twiga Stars kupitia Tigo Pesa kuichangia timu hiyo ambayo inashiriki michuano ya AWC. Wachangiaji wanatakiwa kutuma mchango wao kwenda namba 13389.
RUFANI YA YANGA KWA TIBAIGANA

Kikao cha Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kilichokuwa kifanyike kesho (Aprili 14 mwaka huu) kujadili rufani ya Yanga kupinga kunyang’anywa pointi tatu kwa kumchezesha Nadir Haroub katika mechi dhidi ya Coastal Union kimeahirishwa.

Kamati hiyo chini ya uenyekiti wa Kamishna mstaafu wa Polisi, Alfred Tibaigana sasa kitafanyika Jumanne (Aprili 17 mwaka huu) saa 9 alasiri kwenye ofisi za TFF.

MIKOA 13 YAWASILISHA MABINGWA WAKE

Vyama vya mpira wa miguu vya mikoa 17 ya Tanzania Bara vimewasilisha majina ya mabingwa wake kwa ajili ya Ligi ya Taifa iliyopangwa kuanza Aprili 22 mwaka huu katika vituo vitatu.

Mikoa hiyo na mabingwa wake katika mabano ni Kigoma (Kanembwa FC ya Kibondo), Kilimanjaro (Forest FC ya Siha), Ruvuma (Mighty Elephant ya Songea), Dodoma (CDA), Rukwa, (Mpanda Star ya Mpanda), Iringa (Kurugenzi FC ya Mufindi) na Lindi (Lindi SC).

Mingine ni Mtwara (Ndanda FC), Shinyanga (Mwadui FC), Mara (Polisi Mara), Singida (Aston Villa), Arusha (Flamingo SC) na Tabora (Majimaji FC).

Mikoa ambayo haijawasilisha mabingwa wake ni Manyara, Dar es Salaam, Mwanza, Tanga, Morogoro, Pwani na Kagera.

Thursday, April 12, 2012

REST IN PEACE KANUMBA



JK NI MTETEZI MKUBWA WA HAKI ZA WASANII:JB

MSANII nyota wa filamu nchini, Jacob Steven, maarufu kwa jina la JB, amesema hatatokea kiongozi wa nchi mwenye mapenzi na wasanii kama ilivyo kwa Rais Jakaya Kikwete.
JB amesema mbali ya kuwapenda wasanii wa fani zote, Rais Kikwete amekuwa mstari wa mbele kupenda kazi zao na kutaka wanufaike na vipaji vyao.
Msanii huyo alisema hayo siku moja kabla ya mazishi ya nguli wa fani ya filamu nchini, marehemu Steven Kanumba yaliyofanyika juzi kwenye makaburi ya Kinondoni, Dar es Salaam.
“Natamani Rais Kikwete angekuwa kiongozi wa milele wa Tanzania! Jamani, sijawahi kuona kiongozi anayewajali wasanii kama Kikwete,”alisema.
JB alimwelezea Rais Kikwete kuwa ni mtu anayependa kufuatilia kazi za wasanii wa nchi yake na katika kudhihirisha mapenzi yake kwao, amekuwa akiwaalika mara kwa mara Ikulu na kula nao chakula.
“Unaweza kupenda kuangalia kazi za wasanii, lakini usiwajali, lakini kwa Rais Kikwete, anapenda vyote, hatuna budi kumshukuru na kuongeza bidii katika kazi zetu,”alisema.
Msanii huyo pia alielezea kuguswa na uamuzi wa Rais Kikwete kushirikiana bega kwa bega na familia ya marehemu Kanumba pamoja na wasanii wa filamu wakati wote wa msiba wa mwigizaji huyo.
Alisema akiwa kiongozi mkuu wa nchi, Rais Kikwete aliacha shughuli zake zote na kwenda nyumbani kwa marehemu Kanumba kuwapa pole wafiwa na pia kuzungumza machache na wasanii.
“Ni viongozi wachache wenye moyo na sifa za aina hiyo. Tunapaswa kumshukuru na kumpongeza rais wetu kwa ukaribu aliouonyesha kwetu wasanii,”alisema.
Kanumba alifariki dunia Aprili 6 mwaka huu nyumbani kwake Sinza, Dar es Salaam baada ya kutokea ugomvi kati yake na msanii mwenzake wa filamu, Elizabeth Michael ‘Lulu’.
Mazishi ya Kanumba, ambayo yameelezewa kuwa ni ya kihistoria yalifanyika juzi kwenye makaburi ya Kinondoni na kuhudhuriwa na maelfu ya watu, wakiongozwa na Makamu wa Rais Dk. Mohammed Gharib Bilal.
Akiwa nyumbani kwa marehemu Kanumba alikokwenda kuwapa pole wafiwa, Rais Kikwete aliahidi kuwa, ataendelea kuwa bega kwa bega na wasanii ili kuhakikisha wanafaidi matunda ya jasho lao.
Rais Kikwete alisema ametoa maelekezo kwa JB na baadhi ya wasanii wenzake alipowaita Ikulu mjini Dar es Salaam hivi karibuni na kwamba anasubiri mrejesho kutoka kwao ili akamilishe azma yake ya kuwasaidia kimaendeleo.
Katika kikao chake na wasanii hao, Rais Kikwete aliwataka waeleze changamoto mbalimbali zinazowakabili ili aweze kuwasaidia na kutatua matatizo yao.
JB alisema kauli hiyo ya Rais Kikwete inaonyesha dhahiri kwamba, amepania kwa dhati kutatua matatizo mbalimbali yanayowakabili wasanii wa fani hiyo, ikiwa ni pamoja na kuibiwa kazi zao na wafanyabiashara.
Hata hivyo, JB alisema mazungumzo hayo yaliyodumu kwa saa tatu yatazaa matunda iwapo tu yeye na wasanii wenzake watakuwa kitu kimoja na kuondoa tofauti zilizopo kati yao.
Kauli hiyo ya JB imekuja siku chache baada ya msanii mwingine wa fani hiyo, hasa vichekesho, Steve Mengere ‘Nyerere’ kutamka kuwa, wasanii watamkumbuka Rais Kikwete baada ya kuondoka madarakani.
Msanii huyo mahiri kwa kuigiza sauti ya Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Nyerere alisema, binafsi amepata mafanikio makubwa kiusanii baada ya kuingia madarakani Rais Kikwete.
“Mimi nasema Rais Kikwete akiondoka madarakani, wasanii watamkumbuka sana kwa sababu haijawahi kutokea na haitatokea kiongozi wa nchi anayependa sanaa kama JK,”alisema.
Aliitaja faida nyingine aliyoipata kiusanii tangu JK alipoingia madarakani kuwa ni kupata nafasi ya kukaa naye karibu na pia kula naye chakula.
“Lakini kikubwa zaidi ni Rais Kikwete kujua kwamba kuna mtu anaitwa Steve Nyerere,”alisema msanii huyo mwenye vituko na makeke.
Hata hivyo, Steve alikiri kuwa ni vigumu kwa wasanii nchini kupata mafanikio makubwa kiusanii kutokana na kutokuwa na umoja. Alisema sababu kubwa inayowafanya wasanii wasiwe na msimamo ni njaa.
“Wasanii hatuna viwango maalumu vya malipo kwa kazi tunazozifanya. Wewe ukikataa malipo ya shilingi 500,000 kwa kuona ni kiwango kidogo, mwenzako atapokea. Na ukitaka ulipwe shilingi milioni moja, utakufa na njaa,”alisema.

SIMBA, YANGA DIMBANI J'PILI

VIGOGO vya soka nchini, Simba na Yanga vinatarajiwa kushuka tena dimbani wikiendi hii kumenyana na timu za Toto African na Ruvu Shooting katika mechi za ligi kuu ya Tanzania Bara. Wakati Yanga itamenyana na Toto African kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza, Simba itavaana na Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mechi hizo mbili zinatarajiwa kuwa na ushindani mkali kwa vile Simba na Yanga kila moja itapania kushinda ili kujiweka kwenye nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa.
Ligi hiyo ilisimama kwa muda kutokana na Simba kushiriki katika michuano ya kimataifa.
Simba inaongoza ligi iyo kwa kuwa na pointi 50 baada ya kucheza mechi 22, ikifuatiwa na Azam yenye pointi 47 kutokana na idadi hiyo ya michezo. Yanga ni ya tatu kwa kuwa na pointi 43 baada ya kucheza mechi 21.
Kamati ya Ligi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) iliipoka Yanga pointi tatu na mabao matatu ilizopata kwa kuishinda Coastal Union bao 1-0 baada ya kupatikana na hatia ya kumchezesha beki Nadir Haroub anayedaiwa alikuwa na kadi nyekundu kwa kosa la kupigana.
Hata hivyo, Yanga imekata rufani kwa kamati ya nidhamu na usuluhishi ya TFF, ikipinga uamuzi huo wa kamati ya ligi.
Kwa mujibu wa ratiba, ligi hiyo inatarajiwa kuendelea tena Jumamosi wakati Polisi itakapoikaribisha Azam mjini Dodoma, JKT Ruvu watakuwa wageni wa Mtibwa mjini Morogoro, Kagera Sugar itaikaribisha African Lyon mjini Bukoba wakati Moro United itacheza na JKT Oljoro.
Mechi nyingine kati ya Villa Squad na Coastal Union itachezwa Jumapili kwenye uwanja wa Chamazi mjini Dar es Salaam.

Wema alazwa Mwananyamala kwa saa mbili

MREMBO wa zamani wa Tanzania, Wema Sepetu juzi alilazwa kwa saa mbili kwenye Hospitali ya Rufani ya mkoa wa Mwananyamala kutokana na kuishiwa nguvu.
Wema alipelekwa kwenye hospitali hiyo baada ya kuanguka wakati wa mazishi ya msanii nyota wa filamu nchini, Steven Kanumba yaliyofanyika juzi.
Mbali na Wema, wanawake wengine 11 walifikishwa kwenye hospitali hiyo juzi kutokana na kuishiwa nguvu na kujeruhiwa wakati wa mazishi hayo.
Katibu wa Afya wa Hospitali ya Rufani ya Mwananyamala, Edwin Bisakala alisema jana kuwa, wagonjwa wawili walihamishiwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu zaidi.
Bisakala alisema wema alilazwa kwenye hospitali hiyo kwa saa mbili na baada ya kupatiwa matibabu, aliruhusiwa kurejea nyumbani.
“Tatizo la Wema lilikuwa kuishiwa nguvu kama ilivyokuwa kwa wenzake wengine, lakini pia walikuwepo waliojeruhiwa,”alisema.
Mamia ya watu juzi walipoteza fahamu baada ya kushuhudia jeneza la Kanumba lilipofikishwa kwenye viwanja vya Leaders vilivyopo Kinondoni, Dar es Salaam kwa ajili ya kuagwa.
Mwili wa mcheza filamu huyo ulizikwa juzi mchana kwenye makaburi ya Kinondoni, Dar es Salaam, ambapo maelfu ya watu walijitokeza kumsindikiza katika safari yake ya mwisho.
Kanumba alifariki dunia Jumamosi iliyopita baada ya kutokea ugomvi kati yake na rafiki yake wa kike, Elizabeth Michael ‘Lulu’, nyumbani kwake, Sinza Vatican mjini Dar es Salaam.

SYKES: Ni vigumu kuziba pengo la Kanumba

MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Dully Sykes amesema itachukua muda mrefu Tanzania kumpata mcheza filamu atakayeweza kuziba pengo la marehemu Steven Kanumba.
Akizungumza kwa njia ya simu mjini Dar es Salaam jana, Sykes alisema Kanumba alikuwa msanii mwenye kipaji cha aina yake ndio sababu alikuwa kipenzi cha watanzania wengi.
Sykes alisema katika kipindi chote cha uhai wake, Kanumba alikuwa na ushirikiano mkubwa na wasanii wenzake na pia alipenda kuwasaidia.
“Kusema ule ukweli, kifo chake ni pigo kubwa na ni pengo, ambalo sidhani kama linaweza kuzibika ama itachukua muda mrefu kuliziba,”alisema.
Aliongeza kuwa, kutokana na umahiri wake katika utengenezaji wa filamu, marehemu Kanumba aliweza kulitangaza vyema jina la Tanzania kimataifa kupitia fani ya filamu.
Sykes alisema kujitokeza kwa maelfu ya watu wakati wa mazishi yake ni uthibitisho wa wazi kwamba, msanii huyo alikuwa mtu wa watu na kipendi cha watanzania.
“Sijawahi kumsikia mtu akimzungumza Kanumba kwa mabaya, na kama ilitokea hivyo, basi ni watu wachache. Alipendwa na kila mtu,”alisisitiza.
Sykes aliwataka wasanii wa fani mbalimbali nchini kumuenzi Kanumba kwa kuonyesha upendo miongoni mwao na kusaidiana kwa hali na mali wakati wote wa maisha yao.
Alisema iwapo wasanii watajiheshimu na kuwaheshimu wenzao, itakuwa ni rahisi kwa mashabiki nao kuwafurahia na kuwaenzi kwa kujitokeza kwa wingi kuwazika kama ilivyotokea kwa Kanumba.

KANUMBA NDIYE ALIYEFUFUA EXTRA BONGO-CHOKI

MKURUGENZI na mwimbaji wa bendi ya muziki wa dansi ya Extra Bongo, Ally Choki amesema, daima atamkumbuka mwigizaji filamu nyota nchini, Steven Kanumba aliyezikwa juzi, kwa sababu ndiye aliyemshauri kuifufua bendi ya Extra Bongo.
Akizungumza kwa masikitiko makubwa jana kufuatia kifo cha msanii huyo kilichotokea Ijumaa iliyopita nyumbani kwake Sinza Vatican, Dar es Salaam, Choki alisema msiba huo umempa simanzi kubwa na siku alipopata habari hiyo hakuamini.
“Nilipoambiwa Kanumba kafariki, sikuamini na usiku ule ule nilikwenda Muhimbili kujionea mwenyewe. Nimeumia sana, Kanumba alikuwa rafiki yangu na kuna wimbo tuliwahi kuimba pamoja katika mtindo wa zing zong,” alisema Choki.
Alisema anamkumbuka zaidi msanii huyo wa filamu aliyetamba ndani na nje ya nchi kwani, ndiye alimshauri kuifufua bendi ya Extra Bongo baada ya kusambaratika miaka kadhaa iliyopita.
Choki alisema Kanumba aliwakutanisha na mfanyabiashara Chief Kiumbe katika hoteli ya Lamada na kuzungumza kwa kina juu ya umuhimu wa kuirudisha Extra Bongo na mazungumzo hayo yalizaa matunda.
“Kwa hiyo unampotaja Kanumba, naona mtu muhimu kwangu. Alinishauri nianze kujitegemea badala ya kuajiriwa na wazo hilo liliniingia, nikairudisha bendi yangu,” anasema Choki aliyewahi kuimba katika bendi ya African Stars ‘Twanga Pepeta’, Mchinga Generation ‘Timbatimba’ na TOT Plus. Nyota huyo wa muziki wa dansi alisema, kitu kingine kinachomsikitisha baada ya kifo cha Kanumba ni kutomuona tena msanii huyo kama ilivyokuwa zamani, ambapo walikuwa wanabadilishana mawazo na kula pamoja mchana kwa sababu ya ukaribu wa ofisi zao zilizopo Sinza, Dar es Salaam.
Choki ameishauri serikali kuwa na utaratibu maalumu wa kuchukua majukumu ya misiba ya watu mashuhuri kama Kanumba kwa sababu kutasaidia wasanii kupewa heshima.
“Serikali ifanye hivi kwa wanamuziki, waigizaji filamu na watu wa sanaa nyingine. Itazame umashuhuri wao na kubeba jukumu la msiba ili kuwapa heshima wasanii,” alisema Choki.
Akitolea mfano, alisema kamati ya maandalizi ya mazishi, ambayo Choki alikuwa mjumbe, ilijitahidi kuratibu shughuli za msiba wa msanii huyo, lakini imeacha manung’uniko kwa Watanzania wengi waliopenda kushiriki katika maziko.
Alisema watu wengi walipenda kuaga mwili wa Kanumba na ilishindakana kutokana na umati uliojitokeza kwenye viwanja vya Leaders Club kuwa mkubwa kuliko ilivyotarajiwa na kamati.
“Umati ule umenishangaza sana na umeonyesha jinsi gani Kanumba alivyokuwa anapendwa. Na hapa ndipo unapokuja umuhimu wa serikali kujitwisha jukumu kwa kuwa watu wanasema mwili ungeagwa siku mbili katika Uwanja wa Taifa,” aliongeza Choki.

LULU ABURUZWA KORTINI

MSANII wa filamu nchini, Elizabeth Michael, maarufu kwa jina la Lulu, amepandishwa kizimbani kujibu shitaka la mauaji ya msanii mwenzake, Steven Kanumba.
Lulu (18) alipandishwa kizimbani jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Kisutu, Dar es Salaam, mbele ya Hakimu Mkazi Agustina Mbando na kusomewa shitaka linalomkabili.
Wakili wa Serikali Mwandamizi, Elizabeth Kaganda akisoma hati ya mashitaka, alimtaja Lulu kuwa ana miaka 18, lakini alikana na kudai umri wake ni miaka 17.
Elizabeth alidai, Aprili 7 mwaka huu, eneo la Sinza Vatican, Dar es Salaam, mshitakiwa alimuua Kanumba.
Mshitakiwa huyo hakutakiwa kujibu chochote kutokana na mahakama hiyo kutokuwa na uwezo wa kusikiliza shitaka hilo.
Elizabeth alidai upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na aliomba tarehe nyingine ya kutajwa. Hakimu alisema kesi hiyo itatajwa Aprili 23 mwaka huu.
Wakati msanii huyo akifikishwa mahakamani hapo, alikuwa amepakiwa kwenye gari lenye namba T 848 BNV aina ya Suzuki na kwenye vioo vyake lilikuwa na namba PT 2565 huku likisindikizwa na gari la polisi.
Kulikuwepo na usiri mkubwa baina ya watu waliomfikisha mahakamani msanii huyo, ambao walionekana kutotaka watu wengine, hasa waandishi wa habari wafahamu juu ya suala hilo.
Hali hiyo ilisababisha askari hao kufika mahakamani hapo wakiwa katika magari mawili tofauti huku moja, lililombemba likiwa mbele aina ya Toyota Rav 4 lenye namba za usajili T 848 BNV huku likiwa na rangi nyeupe na vioo vyake vikiwa na rangi nyeusi.
Gari hilo liliwasili mahakamani hapo saa tatu asubuhi kwa nyuma likisindikizwa na Defender lenye namba PT 1848 lililokuwa na askari wanne waliobeba silaha.
Licha ya kuwasili kwa magari hayo, hakuna mwandishi au makarani wa mahakama hiyo,walioweza kufahamu iwapo alikuwemo kwenye msafara huo.
Hilo lilitokana na staili iliyotumiwa na askari hao kwa kuwaacha mbali kabisa askari wa ulinzi waliokuwa wanaongozana na gari lililombeba, ambalo lilizunguka nyuma ya mahakama hiyo kwenda kumshusha na kumuingiza kwenye chumba cha mahakama.
Lulu alikuwa ameambatana na askari kanzu wa kike wawili waliomuweka katikati huku wakionekana kama watu wanaozungumza jambo fulani, ambalo kwa mtu wa kawaida asingeweza kutambua kilichokuwa kikiendelea kati yao.
Askari hao waliingia naye hadi chumba cha mahakama na kumuacha kwenda kukaa katika benchi lililokuwepo katika chumba hicho.
Wakati Lulu anakwenda kukaa kwenye benchi, alionekana kutokuwa na wasiwasi wowote kwani alikuwa akitembea kwa madaha huku akiwa amevaa mavazi nadhifu. Alivaa dira jeupe na kiremba cha rangi ya pinki.
Kupandishwa kizimbani kwa msanii huyo, kumeanzisha safari mpya ya maisha ya msanii huyo, aliyejizolea sifa nyingi kutokana na kuigiza filamu mbalimbali zilizompatia sifa kemkem.
Marehemu Kanumba alizikwa juzi kwenye makaburi ya Kinondoni, Dar es Salaam baada ya maiti yake kuagwa na viongozi mbalimbali wa serikali, ndugu na marafiki kwenye viwanja vya Leaders.
Wakati huo huo, Kamanda wa Polisi mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela amesema hawajui kwa nini Lulu ameamua kudanganya umri wake kwani katika maelezo yake aliyoandika polisi, alidai ana umri wa miaka 18.
Kamanda huyo alisema walifanikiwa kupata cheti chake cha kuzaliwa, ambacho kinaonyesha kuwa, atafikisha umri huo mwakani. Kwa sasa, umri wa Lulu ni miaka 17.
“Tunafahamu kwamba kwa kupitia maelezo yake aliyoandika polisi, amedai ana umri wa miaka 18, lakini hatufahamu kwa nini amedanganya kwani ni tofauti na cheti chake cha kuzaliwa, ambacho kinaonyesha ana miaka 17,” alisema Kenyela.
Akizungumzia kuhusu Lulu kupelekwa hospitali ya Mwananyamala, Kamanda Kenyela alisema ni haki ya kila mtuhumiwa, hasa wanaotuhumiwa kwa makosa makubwa kama ya mauaji kupimwa afya zao.
Alisema walimpeleka Lulu hospitali kwa ajili ya kupimwa afya yake kama nzuri na kwa kuzingatia kulikuwa na ugomvi. Pia alisema katika uchunguzi huo, lazima apimwe akili yake na afya yake.
Lulu alifikishwa kwenye hospitali hiyo kwa mara ya kwanza kwanza Jumapili iliyopita saa 11.00 jioni akiwa chini ya ulinzi wa askari zaidi ya watano.
Polisi waliamua kumfikisha Lulu hospitali baada ya kulalamika kuwa anaumwa na kujisikia vibaya. Alifikishwa tena kwenye hospitali hiyo kwa mara ya pili juzi.
Habari kutoka kwa baadhi ya madaktari waliompokea zimeeleza kuwa, msichana huyo hakuonyesha kuwa na wasiwasi wowote na alipoulizwa sababu ya kujisikia vibaya, alidai ni kutokana na kugombana na mpenzi wake.
Kwa mujibu wa habari hizo, baada ya madaktari kumdadisi zaidi, Lulu alimtaja mpenzi wake huyo kuwa ni marehemu Kanumba, ambaye alifariki dunia Jumamosi iliyopita.
Chanzo cha habari kimeeleza kuwa, baada ya Lulu kuona madaktari wakimshangaa kutokana na kutoonyesha wasiwasi wowote, aliwajibu kwamba tayari limeshatokea.

MAMA LULU: Acheni kumuhukumu mwanangu

Mama mzazi wa msanii Elizabeth Michael 'Lulu', anayedaiwa
kusababisha kifo cha msanii Steven Kanumba, Lucresia Kalugila
amewaomba wanaharakati wamsaidie binti yake ili haki itendeke.
Mama huyo alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza katika
kipindi cha Wanawake Live kilichorushwa hewani na kituo cha
televisheni cha East Africa.
Ameitaka jamii iache kumtupia lawama Lulu kutokana na kifo hicho
cha Kanumba, badala yake wasubiri vyombo vya dola vifanye kazi
yake.
"Kutokana na uzito wa tukio hili, nawaomba wanaharakati
wanawake waniunge mkono ili wanisaidie katika suala hili kwa
kuhakikisha haki inatendeka kwa mtoto wangu,"alisema.
Lucresia alisema binafsi amesikitishwa na kifo cha Kanumba kwa
vile hakutegemea iwapo alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na
binti yake. Alisema wote wawili alikuwa akiwaona kama watoto
wake wa kuwazaa.
"Siku zote Kanumba alikuwa akiniita mama, sikuwa na imani
kwamba angeweza kuwa na uhusiano na Lulu, lakini kwa vile
limeshatokea, tuache sheria ichukue mkondo wake,"alisema.
Aliongeza kuwa, si busara kwa baadhi ya watu kwenda kwa mama
mzazi wa marehemu Kanumba kuzungumza maneno ya uongo
dhidi ya binti yake bila kuwa na uhakika wa kile anachokisema.
"Siku ya tukio walikuwepo Kanumba na Lulu, iweje watu wengine
waanze kuzusha maneno wasiyokuwa na uhakika nayo. Tuache
vyombo vya dola vifanyekazi na kutupa majibu,"alisema.
Mama huyo pia alivitaka vyombo vya habari kuripoti habari za
uhakika kwani si kweli kwamba mtoto wake alitaka kwenda
makaburini kwa ajili ya kuuaga mwili wa Kanumba.
"Lulu yupo kituoni chini ya ulinzi wa polisi, iweje leo atake kwenda
msibani kumuaga Kanumba?" Alihoji mama huyo.
Lucresia alisema yupo pamoja na Mama Kanumba kwa vile msiba
huo ni wa wote hivyo amemtaka awe na moyo wa subira na
ustahamilivu kwa vile ukweli utajulikana.
"Mzazi mwenzangu kuwa na subira, tupo pamoja, Kanumba ni
mtoto wetu sote na mimi nina machungu na kifo chake,"alisema.

MAMA KANUMBA: Nipo tayari kumsamehe Lulu

Mama mzazi wa msanii Steven Kanumba, Flora Mutegoa amesema
yupo tayari kumsamehe msanii Elizabeth Michael 'Lulu',
anayetuhumiwa kumuua Kanumba iwapo vyombo vya sheria
vitamuona hana hatia hiyo.
Flora pia alikanusha madai kuwa, marehemu Kanumba
alikorofishana na baba yake ndiyo sababu hakuweza kushiriki
katika mazishi ya mtoto wake.
Akizungumza na waandishi wa habari nyumbani kwa marehemu
Kanumba, Sinza mjini Dar es Salaam, Flora alisema taarifa hizo
hazina ukweli wowote.
"Marehemu Kanumba na baba yake walikuwa na uhusiano mzuri
isipokuwa watu waliipokea tofauti filamu aliyoitoa, ambayo ilikuwa
ikielezea maisha yake. Hata mimi sijui baba yake aliipokea
vipi,"alisema.
Bi Flora aliishukuru serikali na wananchi waliojitokeza katika
mazishi ya mwanaye na kuongeza kuwa, hakutarajia iwapo
angezikwa na watu wengi kiasi kile.
Aliongeza kuwa, Kanumba na baba yake hawakutofautiana kama
inavyodaiwa na baadhi ya watu, isipokuwa anachojua ni kwamba
mtoto wake aliamua kuwa mbali na mzee ili kujitafutia maisha
yake.
Alisema Mzee Charles Kanumba alishindwa kuhudhuria mazishi ya
mwanaye kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya miguu,
ambayo yamempata uzeeni.
"Kwa kweli sina cha kusema zaidi ya kutoa shukurani zangu za
dhati kwa serikali na watu wote wakiwemo wasanii wenzake, hivi
sasa tunaendelea na mambo ya kifamilia,"alisema.
Alipoulizwa ameupokeaje msiba wa mtoto wake, Bi Flora alisema
kifo chake hakina tofauti na vifo vingine na kusisitiza kuwa, kila
binadamu lazima afe.
"Kama familia, tupo tayari kupokea taarifa zozote, ambazo
tutapewa na vyombo husika, daktari aliyeuchunguza mwili wake
pamoja na polisi, ambao bado wanaendelea na uchunguzi. Kwa
sasa siwezi kusema mengi, naiachia serikali ifanyekazi
yake,"alisema.
Mama Kanumba pia alikanusha madai kuwa, kijana wake ameacha
mtoto. Alisema anachofahamu ni kwamba, mwanaye alikutwa na
mauti akiwa hajaoa na wala hakuwahi kupata mtoto.
Alisema marehemu Kanumba ni mtoto pekee aliyezaa na baba
yake, lakini anao watoto wengine wawili aliozaa na mwanaume
mwingine.

PAPIC ASUSA KWENDA MWANZA

KOCHA Mkuu wa Yanga, Kostadin Papic amegoma kusafiri na timu hiyo kwenda Mwanza baada ya kuweka mgomo bardi, kufuatia viongozi wa timu hiyo kukwepa kukutana naye.
Habari zilizopatikana jana kutoka ndani ya Yanga zimeeleza kuwa, kocha huyo amechukizwa na hatua ya viongoziwa klabu yake kugoma kukutana naye ili kuzungumzia hatma yake.
Yanga iliondoka mjini Dar es Salaam jana kwenda Mwanza, ambako Jumapili ijayo itacheza na Toto African katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara, itakayopigwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba.
Kocha huyo kutoka Serbia anatarajiwa kumaliza mkataba wake Aprili 23 mwaka huu na taarifa zisizo rasmi zimeeleza kuwa, tayari uongozi wa Yanga umeshaanza kusaka kocha mwingine.
Hata hivyo, akizungumzia suala la kocha huyo, Ofisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, Papic hakwenda Mwanza kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya tumbo, homa na mapafu.
Sendeu alisema Papic alianza kuugua siku tatu zilizopita na madaktari wamemshauri asisafiri safari ya masafa marefu kwa vile bado hajapona sawasawa.
Kwa mujibu wa Sendeu, kikosi cha Yanga kimekwenda huko kikiwa chini ya Kocha Msaidizi wa timu hiyo, Fred Felix Minziro.
Sendeu alisema Yanga inatarajiwa kucheza mechi moja ya kirafiki itakayochezwa Kahama mkoani Shinyanga dhidi ya timu ya Ambassador kabla ya kuondoka kesho kwenda Mwanza. Katika msafara huo, mshambuliaji Hamizi Kiiza aliachwa kutokana na kuchelewa kuungana na wenzake, lakini anatarajiwa kuondoka leo na kwenda moja kwa moja Mwanza.

Monday, April 9, 2012

MUHIMBILI YATOA RIPOTI KIFO CHA KANUMBA

Madaktari wa Hospitali ya Taifa Muhimbili wamethibitisha kuwa, msanii nyota wa filamu
nchini, Steven Kanumba, amefariki kwa tatizo la mtikisiko wa ubongo unaojulikana
kitaalamu kama 'brain concussion'.'

Brain concussion' ni hali ya ubongo kushindwa kufanyakazi kwa muda kutokana na
mtu kuumizwa kichwa au kushikwa na kiwewe kikali.

Kwa mujibu wa magazeti ya Mwananchi na Mwanaspoti toleo la leo, taarifa za ndani zilizopatikana juzi kutoka kwa jopo la madaktari bingwa watano walioufanyia uchunguzi mwili wa Kanumba,zinaeleza kuwa tatizo hilo linaweza kumfanya mtu apoteze maisha mara moja au baada ya siku kadhaa.

Mmoja wa madaktari hao wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, ambaye hakutaka kutajwa
gazetini kwa kuwa si msemaji, alisema waligundua tatizo hilo baada ya kumfanyia
uchunguzi huo kwa zaidi ya saa mbili.

"Tulianza kuufanyia uchunguzi mwili wa marehemu kuanzia muda wa saa nne asubuhi
hadi saa saba kasoro za mchana na tukagundua kuwa, marehemu alifariki kutokana
na mtikisiko wa ubongo, kwa kitaalamu brain concussion,"alisema.

Daktari mwingine aliyeshiriki katika uchunguzi huo alizungumza kwa ufupi kuwa,
waligundua kwamba ubongo ulikuwa umevimba na kushuka mpaka karibu na uti wa
mgongo na hivyo kuathiri mfumo wa upumuaji na ndiyo maana msanii huyo alikufa
pale pale.

Daktari wa awali alisema Kanumba alipata mtikisiko wa ubongo, ambao husababisha
kufeli kwa mfumo wa upumuaji (cardio-respiratory failure).

"Kilichomuua hasa ni mtikisiko wa ubongo, ambao endapo unatokea katika sehemu ya
nyuma ya ubongo (cerebrum), huua kwa haraka,"alisema daktari huyo.

Aliongeza kuwa, mtikisiko wa ubongo wa nyuma, husababisha matatizo ya mfumo wa upumuaji na hilo limeonekana katika mwili wa Kanumba.

Alisema:" Baada ya ubongo wake kutikiswa kwa nguvu, mfumo wa upumuaji ulifeli na ndio maana tumekuta kucha za Kanumba zikiwa na rangi ya bluu, huku mapafu yake yakiwa yamevilia damu na kubadilika kuwa kama maini, hizo ndizo dalili za kufeli kwa mfumo wa upumuaji."

Aliongeza:" Mtu aliyepata mtikisiko wa ubongo huwezo kutokwa na mapovu mdomoni na hukoropma kabla ya kukata roho na ndivyo ilivyokuwa kwa Kanumba kabla hajafariki."

Daktari huyo alisema, sehemu ya maono na majimaji ya machoni ya marehemu, vimepelekwa kwa mkemia mkuu ili kubaini endapo kuna sumu au kitu kingine katika mwili huo.