KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, August 30, 2011

ALGERIA KUTUA DAR USIKU


ALGERIA KUTUA DAR USIKU

Timu ya Taifa ya Algeria (Desert Warriors) itawasili Septemba Mosi mwaka huu saa 2.50 usiku kwa ndege maalum. Algeria itacheza mechi ya mchujo kuwania tiketi ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitakazofanyika mwakani nchini Equatorial Guinea na Gabon. Mechi hiyo itachezwa Septemba 3 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni. Viingilio kwa mechi hiyo ni viti vya kijani ni sh. 3,000, viti vya bluu sh. 5,000, viti vya rangi ya chungwa sh. 7,000, VIP C sh.10,000, VIP B sh. 20,000 na VIP A sh. 30,000. Tiketi zitaanza kuuzwa Septemba Mosi mwaka huu. Vituo vya kuuza tiketi ni Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Kituo cha Mafuta cha Big Bon (Kariakoo), Mgahawa wa Steers ulioko Mtaa wa Samora na Ohio, Uwanja wa Uhuru na Kituo cha Mafuta cha OilCom Ubungo. Mchezaji Idrisa Rajab anayechezea Sofapaka ya Kenya amewasili jana usiku na tayari ameripoti kwenye kambi ya Taifa Stars. Stars inaendelea na mazoezi Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume jijini Dar es Salaam.

MASHITAKA DHIDI YA RAGE, SENDEU

Kamati ya Nidhamu na Usuluhishi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) chini ya Mwenyekiti wake Alfred Tibaigana iliyokuwa ikutane jana kusikiliza malalamiko dhidi ya Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage na Ofisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu imeahirisha kikao chake. Kwa mujibu wa Tibaigana, kikao kimeahirishwa kutokana na Kamati kutotimiza akidi (column) kwa wajumbe wake. Walalamikiwa wataarifiwa siku ambayo kikao kitapangwa tena. IVAN KNEZEVIC AOMBEWA ITCAliyekuwa kipa wa Yanga, Ivan Knezevic ameombewa Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) na Chama cha Mpira wa Miguu cha Serbia (FAS) ili kujiunga na klabu yake mpya nchini humo. Knezevic ameombewa ITC kama mchezaji wa ridhaa katika klabu ya FK Borac ya nchini humo. TFF itampatia hati hiyo kwa vile mkataba wake katika klabu ya Yanga ulikuwa umemalizika.

11 WATEULIWA KUTATHMINI WAAMUZI

Kamati ya Waamuzi ya TFF imeteua watathmini 11 wa waamuzi (referees assessors) kwa ajili ya mechi za Ligi Kuu ya Vodacom. Watathmini hao watasimamia baadhi ya mechi za ligi hiyo. Walioteuliwa ni Alfred Lwiza (Mwanza), Soud Abdi (Arusha), Charles Mchau (Kilimanjaro), Manyama Bwire (Dar es Salaam), Joseph Mapunda (Ruvuma), Isabela Kapela (Dar es Salaam), Paschal Chiganga (Mara), Emmanuel Chaula (Rukwa), Mchungaji Army Sentimea (Dar es Salaam), David Nyandwi (Rukwa) na Leslie Liunda (Dar es Salaam).
Boniface Wambura.
Ofisa HabariShirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Saturday, August 27, 2011

SAMAHANI NILIKUWA MJENGONI

Mmiliki wa blogu hii, wa pili kulia akituma habari za mwisho mwisho za Bunge mara baada ya kuahirishwa jana mjini Dodoma.


Kwa sababu ambazo zilikuwa nje ya uwezo wangu, sikuweza kupost chochote kwenye blogu yangu katika kipindi cha wiki mbili zilizopita kwa sababu nilikuwa mjengoni Dodoma kuripoti habari za Bunge kwa ajili ya gazeti ninalolifanyiakazi. Nimerejea leo na mambo sasa yatakuwa mswano na kama kazi. Niwieni radhi, hasa wasomaji wangu mliopo majuu.

Friday, August 12, 2011

MECHI YA SIMBA NA YANGA

Mechi ya Ngao ya Jamii (Community Shield) kufungua msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom kati ya mabingwa watetezi Yanga na Makamu Bingwa Simba itachezwa usiku (Agosti 17 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Uamuzi wa mechi hiyo kuchezwa kuanzia saa 2.00 usiku umetokana na sababu kadhaa, kubwa zikiwa mbili; Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan na pia Agosti 17 mwaka huu kuwa ni siku ya kazi.

Pambano hilo litatanguliwa na mechi ya vikosi vya pili (U20) vya timu hizo ambayo yenyewe itaanza saa 10.30 jioni. Mechi ya Ngao ya Jamii baada ya dakika 90 kama mshindi hatapatikana, zitaongezwa dakika 30. Katika muda huo nao kama mshindi atakuwa bado hajapatikana, itatumika mikwaju ya penalti.

Mechi hiyo imepata mwekezaji (Bigbon) na hivi sasa wadau wake wakuu- Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na klabu husika ziko katika mazungumzo ya mwisho mwekezaji huyo.

Kwa redio ambazo zinataka kutangaza mechi hiyo moja kwa moja zinatakiwa kuwasiliana na Idara ya Habari na Mawasiliano ya TFF ili kupewa masharti ya kufanya hivyo.

Pia unafanyika utaratibu wa kuuzwa futari uwanjani mara baada ya mechi ya vikosi vya pili ili kuwawezesha washabiki waliofunga kutohangaika kutafuta sehemu ya kufuturu.

Thursday, August 11, 2011

SUNZU, KAGO, OKWI NI MOTO

EMMANUEL Okwi

VICTOR Costa


HARUNA Moshi


Boban, Costa wana soka la Ulaya

KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Victors ya Uganda, Joseph Mutiaba amekichambua kikosi cha Simba kwa kusema, baadhi ya wachezaji wake ni tishio na wengine wanahitaji kunolewa zaidi.
Mutiaba alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita mjini hapa mara baada ya Simba kupambana na Victors na kuchapwa bao 1-0.
Pambano hilo lilikuwa sehemu ya tamasha la ‘Simba Day’, lililofanyika kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini hapa na kuhudhuriwa na mashabiki lukuki.
Kocha huyo alisema katika pambano hilo, Simba ilionyesha kiwango kizuri, lakini baadhi ya wachezaji wake walionekana kuwa na mapungufu kadhaa.
Mutiaba alisema mshambuliaji Emmanuel Okwi ni winga machachari, ana kasi na mwepesi wa kupiga chenga, lakini anahitajika kufanya mazoezi zaidi ili kujiweka fiti.
Alisema kisoka, Okwi ni mchezaji mzuri, lakini anahitaji muda zaidi wa kuelewana na washambuliaji wenzake ili waweze kupanga mashambulizi ya uhakika na kufunga mabao kirahisi.
Kocha huyo alisema, katika pambano hilo, Okwi alitoa pasi nyingi, lakini zilishindwa kufanyiwa kazi na wachezaji wenzake kutokana na kuzidiwa kasi na mipira.
Kwa upande wa Gervas Kago, kocha huyo alisema ni mchezaji mwenye nguvu na stamina na uwezo wa kumiliki mpira, lakini anahitaji msaada wa karibu kutoka kwa mawinga wenzake.
Mutiaba alisema, mchezaji huyo kutoka Jamhuri ya Afrika ya Kati alikuwa akishindwa kufanya maamuzi sahihi na ya haraka kutokana na kukosa msaada kutoka kwa wenzake na hivyo kupiga mipira mbele bila malengo.
Alimwelezea mshambuliaji Felix Sunzu kutoka Zambia kuwa, ni mchezaji mzuri, lakini mashabiki wa Simba wamekosa uvumilivu na kumpa muda wa kutosha kuisoma soka ya Tanzania.
Alisema Sunzu hana tofauti na mshambuliaji Fernando Torres, aliyesajiliwa kwa dau kubwa la pesa na Chelsea, akitokea Liverpool, lakini ameshindwa kuonyesha cheche zake kutokana na mashabiki kutompa muda wa kuzoea mchezo wa timu yake mpya.
“Kilichojidhihirisha kwa Torres ni kupatwa na kiwewe kila anapokuwa uwanjani kutokana na hofu ya jinsi ya kuwakonga nyoyo mashabiki wa Chelsea, hali ambayo pia imejitokeza kwa Sunzu,”alisema.
Mutiaba amewataka mashabiki wa Simba kumpa muda Sunzu wa kuizoea soka ya Tanzania na pia wasimruhusu kujawa na hofu moyoni kila anapokuwa uwanjani kwani wakifanya hivyo, watamfanya ashindwe kabisa kucheza soka.
Alimwelezea kiungo mpya Patrick Mafisango kutoka Rwanda kuwa, ana kazi nzito ya kumudu soka ya Tanzania kwa vile ni mchezaji pekee mpya aliyesajiliwa na Simba katika safu hiyo na hivyo kukosa ushirikiano wa kutosha.
Hata hivyo, Mutiaba alisema Mafisango ni mchezaji mwenye mipango na uwezo binafsi hivyo iwapo atapewa muda wa kutosha, anaweza kutoa msaada mkubwa kwa Simba.
“Kama mlivyoona, katika mchezo huu, amekuwa akizunguuka huku na kule akitafuta nani wa kupokezana naye mipira na kutoa pasi fupi fupi, lakini nadhani wenzake hawajauzoea mchezo huo,”alisema.
Akiwazungumzia beki Victor Costa na mshambuliaji Haruna Moshi ‘Boban’, kocha huyo alisema, wana uwezo wa juu kisoka, lakini wanapaswa kucheza kwa ushirikiano zaidi na wenzao wageni.
Mbali na kuwasifu wachezaji hao kimchezo, kocha huyo alisema, kutokana na soka waliyoionyesha, wanapaswa kucheza soka ya kulipwa barani Ulaya.

Timbe kuifumua Yanga


KOCHA Mkuu wa Yanga, Sam Timbe amesema atakifumua na kukisuka upya kikosi chake kabla ya pambano lao la kuwania Ngao ya Hisani dhidi ya Simba litakalochezwa Agosti 17 mwaka huu.
Timbe alisema hayo jana muda mfupi mara baada ya timu hiyo kuwasili kwenye uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere mjini Dar es Salaam ikitokea Sudan.
Kocha huyo kutoka Uganda alisema, amefikia uamuzi huo baada ya kubaini kasoro kadhaa za kiufundi kwa baadhi ya wachezaji wake, baada ya kucheza mechi mbili za kirafiki dhidi ya El-Merreikh ya Sudan.
Katika mechi hizo zilizochezwa juzi na Jumapili iliyopita, Yanga ilichapwa mabao 3-1 kila mechi na El-Merreikh.
Timbe alisema ataanza kukifumua kikosi hicho katika mazoezi yatakayofanyika leo kwenye uwanja wa Kaunda uliopo Jangwani mjini Dar es Salaam.
Akizungumzia vipigo hivyo, Timbe alisema vilitokana na kiwango cha juu kilichoonyeshwa na wapinzani wao, ambao aliwaelezea kuwa wapo juu kisoka ikilinganishwa na Yanga.
“Hatukucheza vizuri mechi ya kwanza kwa sababu tulishindwa kufanya mazoezi na kuzoea hali ya hewa ya huko. Tulicheza mechi siku moja baada ya kuwasili Sudan, hali hiyo ilituathiri,”alisema.
“Lakini kikubwa ni kwamba, wachezaji wangu hawakuwa vizuri kisaikolojia kutokana na matatizo mbalimbali yaliyojitokeza kwa timu yetu, lakini tutayarekebisha matatizo hayo,”aliongeza bila kubainisha matatizo hayo.
Pamoja na kupata vipigo hivyo, Timbe aliwasifu wachezaji wake kwa kuonyesha kiwango cha juu kisoka na kuongeza kuwa, mapungufu yaliyojitokeza katika mechi hizo, atayafanyiakazi.
Akizungumzia pambano lao dhidi ya Simba, kocha huyo alisema atatumia siku chache zilizosalia kuiandaa vyema timu yake kukabiliana na wapinzani wao hao wa jadi na kusisitiza kuwa, ushindi ni muhimu.
Wakati huo huo, Yanga juzi ilipata kipigo kingine cha mabao 3-1 kutoka kwa El-Merreikh ya Sudan katika mechi ya kirafiki iliyochezwa mjini Khartoum.
Kipigo hicho kilikuwa cha pili kwa Yanga kutoka kwa El-Merreikh katika ziara yake ya mechi za kirafiki nchini Sudan kwa ajili ya maandalizi ya michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara.
Katika mechi ya awali kati ya timu hizo, iliyochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita, Yanga ilipata kichapo cha idadi hiyo ya mabao kutoka kwa El-Merreikh.
Awali, Yanga ilikuwa icheze mechi nyingine ya kirafiki dhidi ya El-Hilal, lakini pambano hilo lilifutwa dakika za mwisho.
Kama ilivyokuwa katika mechi ya kwanza, Yanga ilionyesha uhai katika kipindi cha kwanza, lakini ilionekana kuzidiwa kipindi cha pili, ambapo wenyeji walitawala mchezo.
Yanga ilikuwa ya kwanza kupata bao kipindi cha kwanza, lililofungwa na mshambuliaji wake wa kimataifa kutoka Ghana, Kenneth Asamoah.
Mabingwa hao wa Tanzania Bara walipata pigo kipindi cha pili baada ya kipa wake, Yaw Berko kuumia na kuingia Saidi Mohamed.
Kutoka kwa Berko kulitoa mwanya kwa wenyeji kufunga mabao hayo matatu na hatimaye kutoka uwanjani na ushindi.

Mwajabu awa Vodacom Miss Top Model 2011



MREMBO Mwajabu Juma, ametwaa taji la 'Miss Top Model' katika shindano lililofanyika juzi usiku katika Hoteli ya Giraffe mjini Dar es Salaam.
Katika shindano hilo lililowashirikisha warembo 30 wanaowania taji la Vodacom Miss Tanzania 2011, Mwajabu alipata kura nyingi kutoka kwa majaji.
Majaji hao Asia Idarous, Kisa Zimba na Mariam Hashim walimpa pointi nyingi mshiriki huyo kutokana na kuonekana kuwa na vigezo vyote vinavyostahili kwa mwanamitindo na kuwabwaga wenzake walioingia hatua ya tano bora.
Warembo hao, kanda wanazotoka zikiwa kwenye mabano ni Jenifer Kakolaki (Ilala), Cynthia Kimasha (Temeke), Alexia Williams (Ilala) na Zerulia Manoko (Kanda ya Kati).
Kutokana na matokeo hayo, warembo hao wamekata tiketi ya kuingia moja kwa moja katika hatua ya 15 bora ya shindano hilo.
Akizungumza jana, Mkurugenzi wa Kamati ya Vodacom Miss Tanzania, Hashim Lundenga, alisema mfumo wa kumpata mshindi mwaka huu umebadilika na ni lazima washiriki washinde mataji madogo madogo ili waingine katika fainali.
Lundenga alisema kutokana na mabadiliko hayo, warembo 15 pekee ndio watakaoingia katika hatua ya 15 bora baada ya kupatikana katika mataji mengine. Aliyataja mataji hayo kuwa ni la kipaji, mvuto wa picha, michezo na mwonekano halisi, ambapo kila taji litatoa washindi watano.
Alisema warembo wengine, ambao hawatashinda mataji hayo, hawatapata nafasi ya kuingia katika hatua ya 15 bora, ambayo warembo wake watawania nafasi ya kuingia 10 bora, tano bora na hatimaye kumpata mshindi.
Warembo wanaoshiriki shindano hilo na kanda wanazotoka katika mabano ni Jenifer Kakolaki (Ilala), Leyla Juma (Nyanda za Juu Kusini), Mwajabu Juma (Temeke), Mariaclara Mathayo (Kanda ya Mashariki), Cythia Kimasha (Temeke), Christine William (Nyanda za Juu Kusini), Hamisa Hassan (Kinondoni), Alexia Williams (Ilala), Stacy Alfred (Kanda ya Kaskazini), Asha Salehe (Kanda ya Mashariki), Zubeda Seif na Rose Hubert (Kanda ya Kaskazini), Maua Kimambo (Kanda ya Kati) na Grolr Samuel (Kanda ya Ziwa).
Wengine ni Neema Mtitu (Chuo Kikuu Huria), Atu Daniel (Nyanda za Juu Kusini), Blessing Ngowi (Elimu ya Juu), Weirungu David (Chuo Kikuu Huria), Chiaru Masonobo (Chuo Kikuu DSM), Irene Karugaba (Kanda ya Ziwa), Delilah Gharib (Kanda ya Kati), Tracy Sosppeter (Kanda ya Ziwa), Husna Twalib (Temeke), Loveness Flavian (Kanda ya Mashariki), Christine Mwegoha (Kanda ya Kati), Husna Maulid (Kinondoni), Zerulia Manoko (Kanda ya Kati), Salha Israel (Ilala), Groly Lory (Vyuo Vikuu) na Stella Mbuge (Kinondoni).

Sudan Kusini yaomba kucheza Chalenji


SUDAN Kusini imewasilisha maombi ya kutaka kujiunga na Baraza la Vyama vya Soka vya Afrika Mashariki na Kati (CECAFA).
Katibu Mkuu wa CECAFA, Nicholas Musonye alisema kwa njia ya simu juzi kutoka Nairobi kuwa, Sudan Kusini iliwasilisha maombi hayo mapema mwezi uliopita.
Hata hivyo, Musonye alisema nchini hiyo haiwezi kupata uanachama wa CECAFA hadi itakapopata baraka za Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA) na lile la Afrika (CAF).
Musonye alisema, kabla ya kuwasilisha maombi hayo, Sudan Kusini ilikuwa imeonyesha nia ya kutaka kushiriki kwenye mashindano ya Kombe la Chalenji yanayotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu nchini Tanzania.
“Wanapaswa kusubiri kabla ya kuruhusiwa kushiriki katika michuano inayoandaliwa na CECAFA,”alisema Musonge.
Kwa mujibu wa Musonye, nchi hiyo inapaswa kwanza kupata uanachama wa FIFA na CAF ndipo iruhusiwe kushiriki katika michuano inayoandaliwa na baraza hilo.
“Tunafurahia kuwa na nchi nyingine mpya ndani ya ukanda huu wa Afrika, lakini ushiriki wake kwenye michuano ya Kombe la Chalenji, utategemea baraka za CAF na FIFA,”alisema.
“Tumesaliwa na miezi minne kabla ya michuano hiyo kuanza na sidhani kama kwa wakati huo Sudan Kusini itakuwa tayari imeshapata baraka za vyama hivyo,”alisema.
Kwa kawaida, huchukua muda mrefu kabla ya nchi mpya kukubaliwa kuwa mwanachama wa CAF na FIFA. Zanzibar imekuwa ikiruhusiwa kushiriki michuano ya CECAFA, lakini bado haijaruhusiwa kushiriki kwenye mashindano ya FIFA kama taifa huru.
Kwa sasa, CECAFA inaundwa na nchi wanachama 11. Nchi hizo ni Sudan Kaskazini, Uganda, Kenya, Rwanda, Burundi, Zanzibar, Somalia, Djibouti, Eritrea, Ethiopia na Tanzania Bara.

NCHIMBI: Saidieni michezo mingine


WAZIRI wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Emmanuel Nchimbi ametoa changamoto kwa taasisi, mashirika na watu binasfi kuona umuhimu wa kutoa misaada kwa michezo mingine badala ya soka pekee.
Dk. Nchimbi alitoa changamoto hiyo juzi wakati alipokuwa akikabidhiwa vifaa vya mchezo wa ngumi, vilivyotolewa na Mfuko wa Pensheni ya Watumishi wa Serikali za Mitaa (LAPF) mjini hapa.
LAPF imetoa vifaa hivyo vyenye thamani ya sh. milioni tano kwa Chama cha Ngumi za Ridhaa nchini (BFT) kwa ajili ya timu ya taifa, itakayoshiriki Michezo ya Afrika nchini Msumbiji mwezi ujao.
Waziri Nchimbi alisema vyama vingi vya michezo vinahitaji kupatiwa misaada mbalimbali ili viweze kutekeleza majukumu yake na kuinua viwango vya michezo husika.
“Kwa niaba ya serikali, naishukuru sana LAPF kwa msaada huu wa vifaa vya michezo, ambavyo naamini vitaiwezesha timu yetu ya ngumi kufanya maandalizi mazuri kwa ajili ya michezo ya Afrika,”alisema.
Alitoa mwito kwa mfuko huo, kuandaa bajeti maalumu kuanzia mwakani kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya michezo, kama zinavyofanya kampuni na taasisi mbalimbali.
Akizungumza katika hafla hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa LAPF, Don Kida alisema,licha ya mfuko huo kukusanya michango ya wafanyakazi, pia unawajibika kuisaidia jamii ya watanzania. “Kwa maana hiyo, wanamichezo ni sehemu ya jumuia za vijana wetu, ambao kama taasisi, tuna wajibu wa kusaidia kila inapowezekana ili kurudisha sehemu ya mafanikio yanayotokana na utendaji wa mfuko huu”, alisema.
Kida aliyataka mashirika na taasisi zingine, kuiga mfano wao ili ziweze kuchangia maendeleo ya michezo nchini.
Vifaa vilivyotolewa na mfuko huo kwa timu hiyo ni glovu za mikono, vifaa vya kuhami kichwa, padi za mazoezi, viatu vya mazoezi, traki suti, bukuta, fulana za mashindao na vifaa vya mazoezi ya ‘speed ball’.

Majaliwa aanza kuonyesha cheche Sikinde


MWIMBAJI mpya wa bendi ya muziki wa dansi ya Mlimani Park Orchestra, Shukuru Majaliwa ameibuka na wimbo wake mpya wa kwanza ndani ya bendi hiyo, unaokwenda kwa jina la ‘Fadhila ya punda mateke.’
Majaliwa ametunga wimbo huo, ikiwa ni wiki chache tangu alipojiunga na bendi hiyo, inayotumia miondoko ya Sikinde, akitokea bendi ya Msondo Ngoma.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, mmoja wa viongozi wa bendi hiyo, ambaye hakupenda jina lake litajwe gazetini alisema, tayari wimbo huo umeshaanza kufanyiwa mazoezi.
Kwa mujibu wa mwanamuziki huyo, kibao hicho kitaanza kusikika rasmi wakati wa sikukuu ya Idi.
“Wimbo huu ni miongoni mwa nyimbo mpya, ambazo tumekuwa tukizifanyia mazoezi katika kipindi hiki cha mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani na tutaanza kuzipiga wakati wa sikukuu ya Idi,”alisema.
Majaliwa amejiunda na Sikinde akiwa ‘deiwaka’ kwa vile ni mwajiriwa wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), akiwa anaitumikia bendi ya Mwenge Jazz ‘Paselepa’.
Mwanamuziki huyo alianza kupata umaarufu baada ya kujiunga na Msondo Ngoma, akiwa ‘deiwaka’, ambapo umahiri wake wa kuiga sauti ya marehemu Moshi William ulimfanye atumike kama mwimbaji ‘kiraka’.
Akizungumza wakati wa utambulisho wake ndani ya Sikinde, Majaliwa alisema ameamua kujiunga na bendi hiyo kwa ridhaa yake mwenyewe na bila ya ushawishi wa mtu yeyote.
Aliongeza kuwa, kabla ya kujiunga na Sikinde, aliwaeleza viongozi wa bendi hiyo sababu za kuondoka kwake Msondo na kuongeza kuwa, walimwelewa ndio maana walimkubalia ombi lake.

Kabeya awaponda wanaojiita 'wazee wa masauti'


MWANAMUZIKI mkongwe nchini, Kabeya Badu amewaponda wanamuziki wanaojiita ‘wazee wa masauti’ kwa madai kuwa uwezo wao kimuziki ni mdogo.
Akihojiwa katika kipindi cha Mwanamuziki Wetu cha TBC FM mwishoni mwa wiki iliyopita, Kabeya alisema sifa wanazojipa wanamuziki hao hazilingani na uwezo wao na hawapendi kujifunza.
Kabeya alisema tatizo hilo lipo kwa wanamuziki wengi nchini hivi sasa na linatokana na kutopenda kwao kupata ushauri na maelekezo kutoka kwa wakongwe wa fani hiyo.
Hata hivyo, mwanamuziki huyo kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo alisema, zipo baadhi ya bendi nchini, hasa zile kongwe, ambazo zinapiga muziki wenye mvuto na unaoweza kupendwa kimataifa.
Alisema baadhi ya bendi hizo, kama vile Msondo Ngoma na Mlimani Park Orchestra, zinaweza kupata mashabiki kokote barani Afrika kwa vile zinapiga muziki wa kuvutia.
“Wakati nakuja nchini, nilikuwa nikipenda sana kwenda kwenye maonyesho ya Sikinde na Msondo. Nilikuwa nikivutiwa sana na wimbo wa Kassim uliopigwa na Sikinde na sauti ya Gurumo,”alisema mkongwe huyo, aliyeingia nchini mwaka 1978.
Kabeya alisema muziki wa Tanzania unapendwa sana nchini Congo na kuna wakati alipokwenda huko kwa mapumziko, alilazimika kuacha nyumbani kanda za kaseti za Tuncut, Msondo, Sikinde na Maquiz kutokana na rafiki zake wengi kuzigombea.
Mwanamuziki huyo mkongwe aliletwa nchini na wanamuziki Kikumbi Mwanza Mpango ‘King Kikii’ na Nguza Vicking na kujiunga moja kwa moja na bendi ya Maquiz.
Hata hivyo, alishindwa kudumu kwenye bendi hiyo kutokana na kile alichodai kuwa, kutofautiana na viongozi wake kuhusu maslahi. Alisema hali waliyoikuta Maquiz ilikuwa tofauti na alivyoelezwa.
Baada ya kuondoka Maquiz, alijiunga na Orchestra Safari Sound (OSS) wakati huo ikiwa chini ya Kikii na baadaye Fred Ndala Kasheba. Akiwa OSS, alijipatia umaarufu mkubwa kutokana na kibao chake cha Ziada.
Kabeya alisema aliutunga wimbo huo akiwa ndani ya gari, akielekea mazoezini na kwamba lengo lake lilikuwa ni kuacha kumbukumbu ya kudumu. Kabeya aliimba wimbo huo mwanzo hadi mwisho.
Kwa sasa, Kabeya yupo kwenye bendi ya La Capital ‘Wazee Sugu’, inayoundwa na baadhi ya wanamuziki wakongwe wa hapa nchini na kutoka Congo.

STELLA: Siwanii taji la Miss Tanzania ili nipate gari


MREMBO wa Kinondoni wa mwaka 2011, Stella Mbuge amesema hawanii taji la mrembo wa Tanzania mwaka huu kwa lengo la kunyakua zawadi ya gari.
Stella amesema anashiriki shindano hilo kwa lengo la kujifunza mambo mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kukutana na watu tofauti, kujifunza tabia zao pamoja na mambo yao.
Mwanadada huyo, ambaye pia ni mrembo wa kitongoji cha Tabata, alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha Jambo Tanzania, kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha TBC 1.
Stella ni miongoni mwa warembo 30 walioingia kambini mwanzoni mwa wiki hii kwenye jumba la Vodacom House kwa ajili ya maandalizi ya shindano hilo linalotarajiwa kufanyika Septemba 10 mwaka huu mjini Dar es Salaam.
Mrembo huyo alisema, shindano la Miss Tanzania lina maana kubwa kwa warembo zaidi ya kuwania taji na zawadi zingine zinazotolewa kwa washiriki.
“Mimi sishiriki Miss Tanzania kwa kufuata gari. Ninayo mambo mengi ya kujifunza kutokana na shindano hili,”alisema mwanadada huyu.
Stella amesema amepanga kuyatumia mataji yake ya Miss Tabata na Miss Kinondoni kuwahamasisha wasichana katika maeneo ya vijijini kushiriki katika mashindano hayo.
Alisema wapo wasichana wengi wenye sifa za kushiriki mashindano hayo vijijini, lakini hakuna watu wa kuwafuatilia ili kuibua vipaji vyao na kuwaendeleza.
“Mimi binafsi natoka Morogoro Vijijini, wapo wasichana wengi wazuri na wenye sifa za kushiriki mashindano hayo, lakini hawajulikani,”alisema.
“Hivyo moja ya majukumu yangu yatakuwa ni kuwafuatilia wasichana hawa kwa lengo la kuibua vipaji vyao na kuwaendeleza,”alisema.
Mrembo huyo alisema anaona fahari kubwa kuona kila anapopita mitaani, watu wanamnyooshea kidole na kuelezana habari zake. Alisema kwake, hiyo ni faraja kubwa.
Stella alisema hafurahishwi na dhana iliyojengeka miongoni mwa jamii kwamba, mashindano ya urembo ni uhuni. Alisema dhana hiyo imepitwa na wakati kwa vile fani hiyo imewawezesha washiriki wengi kunufaika kimaisha.

Ndoa ilinishinda-Aunt Ezekiel


MWIGIZAJI nyota wa filamu nchini, Aunt Ezekiel amesema aliwahi kuolewa, lakini ndoa ilimshinda baada ya mume wake kurudi nyumbani akiwa amevaa kondomu.
Akizungumza wiki iliyopita katika kipindi cha luninga ya Clouds, kinachoendeshwa na Zamaradi Mketema, msanii huyo alisema alishituka baada ya kumuona mumewe amevaa mpira huo wa kiume.
Aunt Ezekiel alisema, hakutegemea kama angemkuta mume wake na mpira huo na baada ya hapo, alibeba kilicho chake na kuitema ndoa yake.
"Siku hiyo mume wangu alirudi asubuhi akiwa hajavua kondomu aliyokuwa ametoka kuitumia. Nilishindwa kuvumilia, nikaondoka," alisema Aunt Ezekiel, ambaye aliwahi kuzaa mtoto, akafariki dunia.
Msanii huyo aliyezaliwa mwaka 1986 jijini Dar es Salaam, akiwa ni mtoto wa mwanasoka, aliyewahi kutamba nchini katika miaka ya 1970 hadi 1980, Ezekiel Greyson pia, alikiri kuwa anapenda fedha na si mabwana wenye nazo kama inavyoelezwa.
"Sijui kama kuna mtu hataki pesa, hata wewe (Zamaradi) naona unataka pesa na mimi pia nazitafuta," alisema.
Mcheza filamu huyo mwenye mvuto aliongeza kuwa, hata mabwana wenye fedha, ni wao wanaomfuata, si kwamba yeye anajilengesha kwao kwa ajili ya kutaka pesa.
Katika kipindi hicho, Aunt Ezekiel alizungumzia mengi katika maisha yake ya filamu, ikiwa ni pamoja na kukiri kwamba, aliwahi kumchapa makonde msichana mmoja, aliyetumwa kumvamia kwa madai ya kutembea na bwana wa mtu.
"Yule msichana baada ya kunivamia, sikumlazia damu, nilimchangamkia na baada ya kumfikisha polisi, alisema alitumwa na dada mmoja aje kunivamia kwa madai namchukulia bwana wake," alisema.
Hata hivyo, hakutaja jina la mwanamke aliyepigana naye wala aliyemtuma na kusisitiza kuwa, hatembei na huyo mwanaume kama inavyodaiwa.

K-SHER: Nilijitoa Tip Top kuheshimu ndoa yangu



Asema hawezi kuwatumikia mabwana wawili kwa wakati mmoja

Alitaka kuasili mtoto albino ili kumsaidia, lakini mama yake aligoma


MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Khadija Shaaban ‘K-Sher’ amesema, aliamua kujitoa katika kundi la Tip Top Connection kwa lengo la kuheshimu ndoa yake.
K-Sher amesema, asingeweza kuendelea kuwemo kwenye kundi hilo kwa vile asingeweza kuwatumikia mabwana wawili kwa wakati mmoja.
Msanii huyo mwenye sauti maridhawa, alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita alipokuwa akihojiwa na kituo cha Radio France International.
K-Sher alisema si kweli kwamba aliondoka kwenye kundi hilo baada ya kutimuliwa kama ilivyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari hapa nchini.
“Wakati nilipokuwa Tip Top Connection, nilikuwa peke yangu, sikuwa nimeolewa. Lakini kwa sasa mimi ni mama na mke wa mtu, napaswa kupanga mambo yangu mwenyewe,”alisema msanii huyo, ambaye mwanaye anajulikana kwa jina la Jam K.
“Nisingeweza kumudu kuendelea na muziki nikiwa Top Top Connection na wakati huo huo kuihudumia familia yangu kwa wakati mmoja, ndio sababu nimeamua kupiga muziki kwa kujitegemea ili niweze kupanga mambo yangu mwenyewe,”alisema.
K-Sher alisema madai kwamba aliondoka Tip Top Connection kwa kutimuliwa, hayana ukweli wowote na kusisitiza kuwa, yalitolewa na mmoja wa viongozi wa kundi hilo kwa lengo la kumpaka matope.
Alisema wakati alipoamua kuachana na kundi hilo, alitoa taarifa kwa uongozi, lakini kiongozi mmoja hakuufurahia uamuzi wake huo kwa vile yeye ndiye aliyekuwa chachu.
“Kiongozi huyo hakufurahia kuona nimeondoka Tip Top halafu nimekaa kimya. Alishangaa. Akaanza kunipakazia kwenye vyombo vya habari,”alisema.
“Kinachoshangaza, licha ya kiongozi huyo kunipakazia, akasema wananiruhusu nirudi. Sasa inakuwaje mtu aliyetimuliwa kundini kwa makosa ya utovu wa nidhamu anarejeshwa?” Alihoji.
“Na ni kwa nini nionekane mtovu wa nidhamu kwenye kundi? Mimi naheshimika na watu wote ndio sababu najuana na watu wengi,”alisisitiza msanii huyo, ambaye amewahi kuimba na wasanii mbalimbali nyota wa muziki huo.
Msanii huyo alisema, hafikirii iwapo kuondoka kwake Tip Top Connection kumeacha pengo, kwa vile wapo wasanii wengi wa kike wenye vipaji wanaoweza kuchukua nafasi yake.
K-Sher alikiri kuwa, yeye ni mmoja wa wasanii wachache wa muziki huo, ambao hawajawahi kukumbwa na kashfa ya aina yoyote na hiyo ni kutokana na kujiheshimu kwake mbele ya jamii.
Alisema malezi aliyoyapata kutoka kwa wazazi wake tangu akiwa mdogo yalifuata maadili ya kiislamu na ni watu wanaoheshimika, hivyo anapaswa kulinda heshima yao.
Mwanamama huyo alisema, licha ya kufanyakazi peke yake hivi sasa, ana matumaini makubwa ya kufanya vizuri kwa vile anajuana na watu wengi hivyo anasikiliza na kuheshimu ushauri wao kwake.
Kwa sasa, K-Sher ameingia mkataba wa kufanyakazi katika Programu ya Wanamuziki Hai, ambayo lengo lake ni kutoa elimu kwa jamii inayokabiliwa na matatizo mbalimbali ya maisha. Kwa kuanzia, elimu hiyo imekuwa ikitolewa katika mkoa wa Shinyanga na Mererani mkoani Manyara.
Kwa mujibu wa K-Sher, anaifurahia programu hiyo kwa vile imemwezesha kutembelea katika vijiji mbalimbali, kukutana na watu wengi na kujifunza mazingira tofauti ya maisha ya watu.
“Huko nyuma sikuwa nikifikiria maisha ya watu wengine, lakini sasa nimeweza kujifunza hilo na kubaini kuwa, asilimia kubwa ya watanzania, hasa wanaoishi vijijini, wanaishi maisha ya dhiki sana,”alisema.
Msanii huyo mwenye sauti maridhawa, inayofanana na ile ya ndege mnana wa porini alikiri kuwa, kuna wakati alitaka kuasili mtoto wa kike, ambaye ni albino, lakini mzazi wa mtoto huyo hakuwa tayari kumkubalia.
Alisema uamuzi wake huo, ulilenga kumsaidia mtoto huyo kwa vile alimpenda sana, hakufurahishwa na maisha ya wazazi wake na pia alitaka amwezesha kukabiliana na kadhina wanazopata watu wa jamii ya aina yake.
Alipoulizwa iwapo ni jambo linalowezekana kwa nchi za Afrika kuungana na kuwa kitu kimoja, K-Sher alisema hilo haliwezekani kutokana na tofauti ya maisha na mitazamo.
“Hilo ni jambo gumu hata kwa wasanii kwa sababu kila mtu anatoka katika mazingira tofauti, wapo wasomi na wasiosoma, wapo wanaoelewa na wasioelewa, wapo wanaoweka mbele na wasiopenda pese, hivyo ni vigumu,”alisema.
“Ingekuwa sote tuna mtazamo mmoja, jambo hilo lingewezekana,”alisisitiza.
K-Sher ni msemaji wa Umoja wa Wasanii wa Muziki wa Kizazi kipya nchini, ambao lengo lake ni kuwaunganisha wasanii wa muziki huo katika kushughulikia matatizo yao.
Aliyataja baadhi ya matatizo hayo kuwa ni pamoja na kuhakikisha sheria ya hakimiliki inafuatwa na kuheshimiwa na pia usambazaji wa kazi zao unafanyika kwa njia ya halali.
Aliwataja wanamuziki wa kimataifa wanaomvutia, na ambao angependa siku moja afanye nao kazi kuwa ni P-Square, Fali Ipupa, Kofi Olomide, Salif Keita na Yvonne Chakachaka.

Tuesday, August 9, 2011

SHINDANO LA TOP MODEL LAFANYIKA

Washiriki wa shindano la kumsaka Top Model wakifuatilia kwa makini shindano hilo kwenye hoteli ya Giraffe mjini Dar es Salaam juzi.

Warembo watano kati ya 30 wanaowania taji la Vodacom Miss Tanzania 2011, ambao wamefanikiwa kuingia fainali za kusaka taji la Top Model wakiwa wamejipanga mbele ya majaji baada ya kufanikiwa kuingia katika hatua hiyo usiku wa Agosti 9,2011 katika Hotel ya Giraffe Ocean View jijini Dar es Salaam. Mshindi wa taji la Top Model atajinyakulia tiketi ya moja kwa moja ya kuingia nusu fainali ya Vodacom Miss Tanzania 2011.






Monday, August 8, 2011

Yanga yachapwa 3-1 na El-Hilal



Timu ya Yanga ya Jangwani ambayo iliondoka Jumamosi kuelekea nchini Sudan kwa mwaliko wa michezo ya kirafiki na timu ya Al- Hilal ya huko, jana ilibanjuliwa mabao 3-1.


Aliyepatia Yanga bao la kufutia machozi ni mganda, Hamis Kiiza. Timu hiyo itashuka dimbani tena kesho kumenyana na timu ya El- Mereikh ya huko na baada ya hapo, itarejea nyumbani kwa ajili ya mchezo wao wa kuwania ngao ya Hisani dhidi ya watani wao wa jadi Simba.


El-Mereikh ilishiriki katika Kombe la Kagame Castle mwezi uliopita nchini Tanzania na kushika nafasi ya tatu huku Yanga wakichukua ubingwa huo. Katika mchezo wa makundi wa michuano hiyo, timu hizo zilitoka sare ya mabao 2-2.

WAREMBO WA MISS TANZANIA WAANZA KAMBI

MKURUGENZI wa Kampuni ya Lino Agency, Anko Hashim (nayetabasamu kulia) kama kawaida yake, akizungumza na warembo wa Tanzania mara baada ya kuwasili hotelini leo.

WASHIRIKI wa shindano la Miss Tanzania 2011 wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuwasili hoteli ya Giraffe mjini Dar es Salaam.

MREMBO wa Tanzania wa mwaka 2010, Genevieve Emmanuel akigonganisha glasi na washiriki wa shindano hilo mwaka huu mara baada ya kuwasili kwenye hoteli ya Giraffe mjini Dar es Salaam.


JUMLA ya warembo 30 kutoka kanda tofauti nchini leo (jana) wameanza rasmi kambi ya Vodacom Miss Tanzania 2011 yaliyopangwa kufanyika Septemba 10 kwenye ukumbi wa Mlimani City kwa mfumo tofauti na ule uliozoeleka miaka ya nyuma ambapo warembo walikuwa wakikaa kambini katika Hotel ya Giraffe iliyopo jijini Dar es Salaam.
Vodacom Tanzania ambao ndio wadhamamini wakuu wa shindano la Vodacom Miss Tanzania kwa miaka kadhaa mfululizo safari hii wamebadilisha kabisa muundo wa awali na hivyo walimbwende hao watakaa ndani ya jumba maalum lililopewa jina ‘Vodacom House’.
Mkuu wa Udhamini wa kampuni hiyo George Rwehumbiza amesema jijini Dar es Salaam kuwa lengo la kufikiwa kwa mabadiliko hayo ni kulifanya shindano hilo liwe na muonekano tofauti kama ilivyo kwa Vodacom ambayo imebadili muonekano wake na kasi ya utoaji huduma.
“Safari hii warembo 30 wanaoshiriki shindano hili la Vodacom Miss Tanzania wataishi kwenye jumba maalum ‘Vodacom House’ na humo watafundishwa vitu mbalimbali ikiwemo jinsi ya kukabiliana na vishawishi hususan katika masuala ya kimapenzi,” alisema Rwehumbiza.
Akitaja malengo mengine ya kuwaweka washiriki hao ndani ya jumba hilo Mkuu huyo wa udhamini alisema kampuni yake kwa sasa inatoa huduma kwa teknolojia yenye kasi zaidi hivyo warembo hawana budi kuendana nayo kwa kufundishwa aina ya kula, kuondoa ulimbukeni mara wanapopata umaarufu.
Mabadiliko haya yatalifanya shindano hili kuwa bora na linaloenda na wakati kama zilivyo huduma zetu yaliyotokana na mabadiliko ya nembo yetu. Wakiwa ndani ya jumba warembo watakaa kwa wiki tatu wakijifunza masuala ya kijamii, alisema Rwehumbiza.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Lino Agency waandaaji wa shindano hilo Hashim Lundenga amesema kwa mwaka huu wanataka warembo wenye sifa ikiwemo elimu, muonekano na tabia nzuri ili mshindi atakayepatikana aweze kutuwakilisha vema katika medani za kimataifa.
“Sisi hatuangalii mshiriki ametoka wapi iwe kijijini au mjini, tunachozingatia ni mrembo kukidhi viwango vya shindano ikiwemo sifa tunazozitaka ili mwisho wa siku kila mtu ajivunie mafanikio aliyoyapata akiwa ndani ya jumba la Vodacom House na atumie kigezo hicho kufanikiwa kimaisha,” alisema Lundenga.
Lundenga alisema kuwa mfumo wa mashindano ya mwaka huu, umebadilika ambapo jumla ya warembo 15 wataingia hatua ya nusu fainali baadala ya 10 kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.
Alisema kuwa kati ya warembo hao 10, watano watapatikana katika mashindano maalum wakiwa katika Vodacom House. Kwa mujibu wa Lundenga, kutakuwa na mashindano ya Top Model ambayo yatafanyika leo na baadaye kufuatiwa na mashindano ya Vipaji (Talent), Mrembo bora wa muonekano katika picha (Miss Photogenic), Mrembo bora wa michezo (Top Sports Woman) na mrembo atakayeonyesha ushirikiano mkubwa na uchangamfu katika kambi, Miss Personality.
Ili kuishirikisha jamii, maisha ya washiriki hao wa Vodacom Miss Tanzania 2011 ndani ya Vodacom House yatakuwa yakioneshwa moja kwa moja ‘Live’ na vituo vya Startv pamoja na Clouds TV ili kutoa nafasi kwa watazamaji kumpigia kura mrembo anayefaa kuvikwa taji hilo na kumrithi Genevieve Mpangala mshindi anayemaliza muda wake.

OSCAR JOSHUA ATINGA POLISI

KATIBU Mkuu wa TFF, Angetile Osiah



LYON YAPEWA HADI AGOSTI 17 KULIPA WACHEZAJI

Kamati ya Katiba, Sheria na Hadhi za Wachezaji iliyokutana Agosti 7 mwaka huu kupitia masuala mbalimbali imeiagiza klabu ya African Lyon iwe imewalipa wachezaji wake wawili kufikia Agosti 17 mwaka kwa kuvunja mikataba yao na klabu hiyo.


Wachezaji ambao kila mmoja anadai sh. milioni 4.3 ni Godfrey Komba na Abdul Masenga. Awali kamati hiyo katika kikao chake cha Januari 7 mwaka huu iliagiza klabu hiyo kutosajili mchezaji mpya msimu wa 2011/2012 hadi itakapokuwa imemaliza suala la wachezaji hao. Lyon imeomba kusajili wachezaji wapya wanane kati ya 23 inayotaka kuwatumia kwa msimu mpya.


Kwa kuzuiwa kusajili wachezaji wapya iwapo haitakuwa imemalizana na Komba na Masenga kufikia Agosti 17, Lyon itakuwa imebaki na wachezaji 15 hivyo kikanuni kutokuwa na sifa ya kushiriki Ligi Kuu ya Vodacom. Kanuni inaagiza timu inayoshiriki ligi hiyo kuwa na wachezaji wasiopungua 18 na kuzidi 30.


PINGAMIZI LA YANGA DHIDI YA SIMBA


Kamati haikusikiliza pingamizi la Yanga dhidi ya Simba kuhusu wachezaji iliyotoa kwa mkopo baada ya kubaini kuwa wachezaji ambao Simba imewatoa kwa mkopo ni wane tu; Haruna Shamte (Villa Squad), Aziz Gilla (Coastal Union), Ahmed Shiboli (Kagera Sugar) na Mohamed Kijuso (Villa Squad).


Wachezaji wengine waliotajwa na Simba kupelekwa kwa mkopo katika klabu mbalimbali ilibainika kuwa ni wa kikosi cha pili (U20) ambao hawahusiki na kanuni ya mkopo. Wachezaji wanaoweza kutolewa kwa mkopo ni wa kulipwa tu (wenye mikataba).


Kwa upande wa Athuman Idd na Juma Jabu ambao hawakuonekana kwenye orodha ya usajili ya Simba, kamati imesema ni wachezaji halali wa klabu hiyo kwa vile wana mikataba nayo. Idd ana mkataba wa miaka miwili wakati Jabu mkataba wake umebakiza mwaka mmoja kumalizika. Kamati imesisitiza kuwa kitu kikubwa kinachoangaliwa kwenye usajili wa wachezaji wa Ligi Kuu ni mikataba na si kusaini fomu za usajili.


MCHEZAJI AMANI PETER KYATA


Kyata aliombewa usajili katika klabu mbili za African Lyon na Yanga. Lyon walimuombea kwa timu ya wakubwa, wakati Yanga walimuorodhesha katika timu ya pili (U20).


Kamati ilibaini kuwa mchezaji huyo ni wa kituo cha Tanzania Soccer Academy (TSA) kinachomilikiwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na hakuna mchakato wowote uliofanyika kumsajili, hivyo usajili wake haujakamilika Yanga wala Lyon.


SUALA LA MCHEZAJI OSCAR JOSHUA


Sekretarieti ya TFF imeelekezwa kupeleka suala la mchezaji huyo Polisi kwa ajili ya uchunguzi kwa vile kuna barua mbili zinazopingana kutoka timu yake ya Ruvu Shooting- ya kwanza ikiridhia achezee Yanga na ya pili ikipinga kuwa taratibu hazikufuatwa katika kujiunga na timu yake mpya.


Uamuzi huo wa kamati umelenga kubaini ipi ni barua halali kati ya mbili zilizowasilishwa TFF kuhusu usajili wake Yanga, na zote zikionesha kutoka katika timu yake ya Ruvu Shooting.


Pia kamati imeamua kuwa kwa vile TFF ilifanyia kazi barua ya kwanza ya kumruhusu kwenda Yanga, hivyo kumpatia leseni, mchezaji ataendelea kutumia leseni hiyo hadi taarifa ya uchunguzi wa Polisi kuhusiana na barua hizo mbili itakapotolewa.


HARUNA MOSHI v POULSEN


Kuhusu mchezaji Haruna Moshi ‘Boban’ kutoitikia mwito wa Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Jan Poulsen kucheza mechi kati ya U23 na Shelisheli zilizofanyika Arusha, kamati kwa sasa imeliacha suala hilo kwa kocha huyo kwa vile kuna maagizo ametoa kwa mchezaji huyo.


Poulsen amemtaka Boban binfasi kwenda kumueleza sababu ya kutoitikia mwito wake wa kucheza mechi dhidi ya Shelisheli kabla hajafanya uamuzi mwingine kuhusu mchezaji huyo.

Wednesday, August 3, 2011

MONALISA, ARINZE, OMOTOLA WANENA

OMOTOLA JALADE

SEGUN Arinze

MONALISA Chinda
LAGOS, Nigeria
MWIGIZAJI machachari wa Nigeria, Monalisa Chinda amesema hajutii kuachana na mumewe kwa sababu anayamudu na kuyafurahia maisha anayoishi hivi sasa.
Monalisa alisema mjini hapa wiki hii kuwa, ameshayazoea maisha hayo kwa sababu siku zote amekuwa akijipa moyo kwamba hakuna, ambalo hawezi kulifanya.
“Ni kwa sababu nimeshazoea. Kama utajiambia moyoni kwamba hili ni gumu, siwezi kulifanya, itakuwa hivyo. Kwa sasa mimi ni kama mwanaume, mwanamke na mama. Sina mwanaume wa kunisaidia,”alisema.
“Ni kweli najihisi kukosa kitu fulani, lakini sijali. Ndiye ninayepaswa kuhakikisha nyumba ipo katika hali nzuri, kuwasha jenereta na kupeleka gari kwa fundi. Hizi ni kazi za wanaume, lakini sina wa kuzifanya,”aliongeza.
“Sitaki kumtegemea mtu yeyote kwa sababu nikifanya hivyo, nitaonekana dhaifu. Niliweza kuzifanya kwa kupenda nilipoolewa, hivyo sioni tofauti. Sipendi watu wanifanyie mambo yangu,” alisema mwigizaji huyo.
Monalisa alisema ameamua kuanzisha safu maalumu kwenye gazeti moja la kila wiki la nchi hiyo kwa lengo la kuelezea uzoefu wake katika maisha ya ndoa.
Alisema tangu akiwa mdogo, alipenda kuandika matukio yake ya kila siku kwenye kitabu cha kumbukumbu na alikuwa akifanya hivyo hata baada ya kuolewa.
Mwigizaji huyo alisema, baada ya matatizo kuanza kutokea katika ndoa yake, mtu wa kwanza kumwendea alikuwa mama yake mzazi, ambaye alimuomba ushauri juu ya nini la kufanya.
Kwa mujibu wa Monalisa, mama yake alimshauri kufanya kile, ambacho moyo wake utamwelekeza kukifanya.
Katika hatua nyingine, mmoja wa waigizaji wenye mvuto nchini Nigeria, Segun Arinze amesema, hakujitosa kwenye fani hiyo kwa bahati ama upendeleo, bali alikuwa akiipenda tangu alipokuwa mdogo.
Arinze alisema wiki hii mjini hapa kuwa, baba yake hakuwa akipenda awe mwigizaji kwa vile alipendelea zaidi awe mwanasheria, lakini baadaye alikubaliana na uamuzi wake.
Alisema baba yake alilazimika kuukubali uamuzi wake huo baada ya kufurahishwa na filamu aliyocheza na kuonyeshwa kwenye TV ya nchi hiyo.
“Baba alipoiona, alikuja akaniamsha ili nami niione. Alipokwenda kazini asubuhi, watu wengi walimweleza kwamba waliniona kwenye TV. Lakini bibi yangu hakuvutiwa na kazi hiyo. Alitaka niwe mwanasheria. Alidai kuwa, kazi hiyo hailipi na ya kihuni,”alisema.
Arinze, ambaye alianza uigizaji mwaka 1984 alisema, hali ilikuwa tofauti kwa mama yake mzazi, ambaye siku zote alikuwa akimuunga mkono.
Kwa mujibu wa Arinze, bibi yake alibadili msimamo siku alipomtembelea nyumbani kwake Suleja, ambako umati mkubwa ulikuwa ukimfuata kwa nyuma huku ukipaza mayowe kwa kusema Black Arrow.
“Ninaposema kundi la watu, namaanisha zaidi ya watu alfu nne. Bibi alichanganyikiwa. Hakuyaamini macho yake na aliona fahari juu yangu na kazi niliyoichagua,”alisema.
Mbali na uigizaji, Arinze ambaye ana shahada ya sanaa, pia ni mwanamuziki, mtayarishaji na mwongozaji wa filamu.
Wakati huo huo, nyota wa uigizaji nchini Nigeria, Omotola Jalade amesema kuolewa na mume, ambaye hajihusishi na fani hiyo, kumekuwa na faida kubwa kwake.
Omotola aliueleza mtandao wa GSC wiki hii kuwa, iwapo angeolewa na mwigizaji mwenzake, ama mtu yeyote anayejihusisha na fani hiyo, huenda ndoa yake isingedumu hadi sasa.
“Mume wangu hajihusishi na fani yangu, hivyo simuoni mara kwa mara na pia mimi sihusiani na fani yake, hivyo hanioni mara kwa mara. Kwa jumla, hatuonani mara kwa mara,”alisema.
“Nadhani hiyo inatupa nafasi, kitu ambacho ni muhimu katika ndoa. Anayo nafasi, nami ninayo nafasi. Usisahau kwamba, ndoa ni muungano wa watu wawili tofauti,”aliongeza.
“Nilikuwa na maisha yangu kabla ya kukutana naye, kama ilivyo kwake yeye, hivyo tunahitaji kuelewana, kuheshimu uhuru wa kila mmoja wetu na mambo yetu binafsi,” alisema mwanamama huyo mwenye watoto wanne.
“Nadhani moja ya sababu zinazofanya ndoa nyingi kuwa kwenye matatizo ni wanandoa kutoelewa kwamba wao ni watu tofauti na wapo kwenye muungano wa maisha,”alisema.
“Sababu kubwa ya sisi kuwa pamoja ni kujaribu kuyafanya maisha yetu yawe mepesi siyo magumu. Ninachomaanisha ni kwamba, sipaswi kukufuatilia muda wote nawe hupaswi kufanya hivyo,” aliendelea kulonga mwanamama huyo.

AGBANI DAREGO: Nitafunga ndoa nitakapompata mwanaume anayenifaa




LAGOS, Nigeria
KWA kawaida, Agbani Darego hahitaji utambulisho wa aina yoyote kwani tayari jina lake lipo kwenye kitabu cha kumbukumbu cha Guiness, kufuatia kuwa mwanamke wa kwanza wa kiafrika kushinda taji la mrembo wa dunia.
Agbani (29) alishinda taji hilo miaka kumi iliyopita katika jiji la Sun City, lililopo nchini Afrika Kusini baada ya kuwabwaga washiriki wengine 92 kutoka katika nchi mbalimbali duniani.
Mrembo huyo, ambaye wiki iliyopita aliteuliwa kuwa balozi wa bidhaa za Arik, alisema wiki iliyopita kuwa, hana wazo la kuolewa kwa sasa na kwamba atafanya hivyo pale atakapompata mwanaume atakayemfaa.
“Unauliza lini nitafunga ndoa? (Anafikiri kwa muda). Nadhani ni pale utakapofika wakati mwanaume atakaponiomba nifunge naye ndoa na kuamini kwamba ndiye atakayenifaa,”alisema mrembo huyo.
Hata hivyo, mrembo huyo hakuwa tayari kuweka wazi iwapo anaye rafiki wa kiume kwa madai kuwa, hayo ni mambo yanayohusu maisha yake binafsi.
Alidokeza kuwa, anapenda kuwa na mwanaume mwenye uwezo wa kumfanya awe na furaha, bila kujali iwapo ana mvuto au la. Alisema kwake, mwonekano wa mwanaume haupi uzito.
Agbani alisema hadi sasa bado anaona fahari kubwa kwa kufanikiwa kutwaa taji la mrembo wa dunia akiwa na umri mdogo na siku zote amekuwa akimshukuru Mungu kwa mafanikio hayo.
Kwa mujibu wa mrembo huyo, kwa sasa fani hiyo imekuwa na mabadiliko makubwa kama zilivyo sekta nyingine na kuongeza kuwa, anafurahi kwa vile yeye ni sehemu ya maendeleo hayo.
Mrembo huyo alikataa kuweka wazi kuhusu mkataba kati yake na Arik, lakini alisema anaona fahari kubwa kuwa balozi wa kinywaji hicho.
Alisema jukumu lake la kwanza baada ya kuteuliwa kuwa balozi wa Arik ni kupiga picha za kutangaza bidhaa hizo na kwamba mambo mengine yatafuata baadaye.
Agbani alisema amefanikiwa kuwa mwanamitindo baada ya kushinda taji la dunia na kusisitiza kuwa, anaifuahia kazi hiyo kwa sababu imemwezesha kupata mafanikio makubwa kimaisha.
Licha ya kazi yake hiyo kumfanya awe akisafiri mara kwa mara katika sehemu mbalimbali duniani, Agbani alisema hilo halimzuii kutekeleza majukumu yake mengine.
Agbani alisema anaona fahari kuzaliwa akiwa mwanamke kwa sababu ana uwezo wa kupata chochote anachokitaka, ikiwa ni pamoja na kurudi shule kusoma huku akiendelea kufanyakazi.
Mwanadada huyo wa Kinigeria hakuwa tayari kueleza iwapo kuna siku yoyote aliyowahi kupatwa na jambo lililomkatisha tamaa. Pia hakuwa tayari kueleza ni mambo gani yanayomfanya awe na furaha.
Lakini alidokeza kuwa, anapendelea zaidi kusoma vitabu na magazeti, kusikiliza muziki, hasa nyimbo za Dr. Sid, Tu Face na D’banj. Alisema anafurahia mafanikio ya wanamuziki hao wa Kinigeria.
Agbani alisema kwa sasa, hafikirii kuwa mwigizaji wa filamu kwa vile kazi hiyo inahitaji kuwa na kipaji zaidi. Alisema anafurahia kazi inayofanywa na waigizaji wa nchi hiyo, lakini haelewi iwapo anao uwezo huo.
“Lakini ninachoweza kusema kamwe usiseme hapana, siku moja naweza kujikuta nami nikijitosa kwenye fani hiyo,”alisema.
Agbani alisema ameweza kuufanya mwili wake uendelee kuwa ulivyo kwa kipindi cha zaidi ya miaka 10 kutokana na kula mlo maalumu na pia kufanya mazoezi.
Alisema amekuwa akifanya mazoezi hayo chini ya mkufunzi maalumu nchini Marekani na pia ni mpenzi sana wa kucheza mchezo wa Yoga.
Mrembo huyo alisema kamwe katika maisha yake hatarajii kupiga picha za uchi ili apate pesa na kusisitiza kuwa, mwili wake hauuzwi. Amewataka wanawake wenzake wajiamini na kujaribu kufanya kila kitu bila kukata tamaa.

Warembo Miss Tanzania kambini J'Tatu


WASHIRIKI wa shindano la kumsaka mrembo wa Tanzania, Vodacom Miss Tanzania 2011 wanatarajiwa kuingia kambini Agosti 8 mwaka huu.
Mkurugenzi wa Kampuni ya Lino Agency International, inayoratibu mashindano hayo, Hashim Lundenga, alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, warembo 30 wanatarajiwa kuwania taji hilo.
Lundenga alisema warembo hao walipatikana baada ya kufanya vizuri katika ngazi ya wilaya, mikoa na kanda. Alisema jumla ya kanda kumi na moja zilishirikishwa katika hatua hiyo.
Kwa mujibu wa Lundenga, kambi ya warembo hao itakuwa katika Jiji la Dar es Salaam, lakini hakutaja hoteli watakayoishi. Aliwataka washiriki wote kuripoti kwenye ofisi za Miss Tanzania zilizopo mtaa wa Mkwepu kuanzia saa nne asubuhi.
Lundenga alisema, iwapo itatokea mshiriki kushindwa kufika kwa wakati na tarehe iliyotajwa hapo juu, atakuwa amejiondoa mwenyewe katika mashindano hayo na nafasi yake kupewa mshiriki mwingine. Aliwataja warembo waliopata tiketi ya kushiriki kwenye shindano hilo kuwa ni Chiaru Masonobo (Dares Salaam), Zerulia Manoko, Maua Kimambo, Dalilah Ghalib, Christine Mwenegoha (kanda ya kati), Chritine William, Atu Daniel, Leyla Juma (nyanja za juu kusini), Zubeda Seif, Stacey Alfred, Rose Hubert (kanda ya kaskazini).
Washiriki wengine ni Husna Twalib, Cynthia Kimasha, Mwajab Juma (kanda ya Temeke), Neema Mtitu, Weirungu David (open university), Glory Lory, Blessing Ngowi (higher learning), Loveness Flavian, Asha Salehe, Mariaclara Mathayo, (kanda ya mashariki), Trace Sospeter, Irene Karugaba, Glory Samwel (kanda ya ziwa), Stella Mbuge, Husna Maulid, Hamisa Hussein (kanda ya Kinondoni), Salha Israel, Alexia Willims, Jenifer Kakolaki (Ilala).
Mkuu wa Udhamini wa Vodacom Tanzania, George Rwehumbiza alisema, kampuni yake ipo tayari kuwapokea warembo kwani mwaka huu wamejiandaa vya kutosha na wanatarajia kuyafanya mashindano hayo kuwa ya kimataifa zaidi.
Rwehumbiza alisema kauli mbio ya mashindano ya mwaka huu ni 'Kazi ni kwako'.

SIMBA, YANGA VICHEKO TUPU

MKURUGENZI wa Masoko wa Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), David Minja (wa pili kushoto), akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa klabu za Simba, Yanga na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), mara baada ya utiaji saini wa mikataba mipya kati ya kampuni hiyo na klabu hizo. Kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange 'Kaburu', wa tatu kushoto ni Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah na kulia ni Mwenyekiti wa Yanga, Lloyd Nchunga. (Na mpiga picha wetu).


NEEMA imezishukia klabu za Simba na Yanga baada ya Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), kupitia bia yake ya Kilimanjaro, kuingia mkataba wa udhamini wa miaka minne na klabu hizo.
Katika mkataba huo, uliotiwa saini jana kwenye hoteli ya Double Tree mjini Dar es Salaam, TBL imeongeza fedha za mishahara kwa wachezaji kutoka sh. milioni 16 hadi sh. milioni 25 kila mwezi.
Akizungumza katika hafla ya utiaji saini mikataba hiyo, Mkurugenzi wa Masoko wa TBL, David Minja alisema, kampuni hiyo pia itatoa basi moja kwa kila klabu lenye uwezo wa kubeba abiria 54 na pia kugharamia mikutano ya wanachama ya kila mwaka.
Minja alisema kampuni hiyo pia itatoa sh. milioni 20 kwa kila klabu kwa ajili ya kugharamia matamasha ya ‘Simba Day’ na ‘Yanga Day’ kila mwaka pamoja na kutoa vifaa vya michezo vyenye thamani ya sh. 35 kwa kila msimu wa ligi.
Mkurugenzi huyo alisema, TBL pia imeongeza viwango vya zawadi kwa timu hizo, ambapo ile itakayotwaa ubingwa wa ligi kuu, itazawadiwa sh. milioni 25 na ile itakayotwaa nafasi ya pili itapata sh. milioni 15.
Minja alisema, mkataba huo wenye thamani ya zaidi ya sh. bilioni tano, unatarajiwa umeanza Agosti 8 mwaka huu na unatarajiwa kumalizika Julai 31, 2016.
Katika hafla hiyo, Simba iliwakilishwa na Makamu Mwenyekiti, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ wakati Yanga iliwakilishwa na Mwenyekiti wake, Lloyd Nchunga. Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), liliwakilishwa na Katibu Mkuu wake, Angetile Osiah.
Awali, TBL iliingia mkataba wa udhamini na klabu hizo kwa miaka mitatu kuanzia mwaka 2008.
“Tunazishukuru klabu zote mbili kwa kukubali kushirikiana na Kilimanjaro kwa awamu nyingine tena,”alisema Minja na kuzitaka klabu hizo kuheshimu mikataba hiyo.
Kwa upande wake, Nchunga alisema TBL imekuwa mfano wa kuigwa kwa maendeleo ya soka nchini na kwa vile inatumia fedha nyingi kuzifanya klabu hizo zifanye vizuri katika michuano mbalimbali.
Naye Kaburu aliishukuru kampuni hiyo kwa kuendelea kuidhamini klabu yake na kuongeza kuwa, watautumia udhamini huo kuiletea mafanikio makubwa zaidi Simba.

JACKLINE WOLPER: Sipendi kufuatwafuatwa


TASNIA ya filamu nchini imezidi kushika kasi kiasi cha baadhi ya wasanii kuanza kufaidika kimaisha na kupata umaarufu maradufu.
Miongoni mwa wasanii hao, kuna walioanza mbali na kuteseka kuitangaza sanaa hiyo hadi kuja kupendwa na wengi na sasa imekuwa lulu nchini.
Wasanii kama Steven Kanumba, Vicent Kigosi ‘Ray’, Jacob Steven ‘JB’, Yvonne Charly ‘Monalisa’, Lucy Komba na wengineo wametoka mbali na jahazi la filamu hadi kupanda chati na kuvutia kizazi kipya.
Moja ya wasanii wa kizazi hicho ni Jackline Wolper, ambaye karibu miaka minne, amekuwa mwigizaji nyota wa filamu kutokana na kazi zake kukubalika ipasavyo.
Akizungumza katika mahojiano yaliyofanyika mapema wiki hii kwenye viwanja vya Leaders Club, Kinondoni, Dar es Salaam, mwigizaji huyo ameeleza mambo mbalimbali kuhusu maisha yake ya uchezaji filamu na alivyofika alipo sasa.
Jackline katika moja ya mambo ya msingi, kwanza kabisa anasema licha ya kujikita kwenye uigizaji filamu kwa miaka michache, amekuwa staa anayekabiliwa na migogoro mingi, ambayo anadai haipendi kwa vile si tabia yake.
Amesema anapenda kuelewana, kucheka na kila mtu na hata kubadilishana mawazo, lakini anajuta kwa jinsi umaarufu unavyomuingiza katika bifu na watu mbalimbali.
“Ndiyo inatokea hivyo na wakati mwingine magazeti huwa yanaandika tu, lakini sitaki ugomvi na mtu yeyote napenda kuelewana na wenzangu,” anasema Jackline.
Akielezea tukio la kudaiwa alivamia jukwaa na kumtolea lugha chafu Rais wa Shirikisho la Wasanii Tanzania (TAFF), Simon Mwakifwamba mwezi uliopita, Jackline anasema hakuwa na lengo hilo na kilichoandikwa kimepotoshwa.
“Nilikwenda jukwaani kutaka anipe nafasi nizungumze kutolea ufafanuzi wa kitu alichokuwa anasema na sikutaka kumfanyia vurugu kabisa,” anasema Jackline.
Mkutano huo uliofanyika kwenye viwanja vya Leaders Club mwezi uliopita, uliitishwa na Mwakifwamba kuzungumzia wasanii wa filamu kukosa nidhamu kwa kuvaa nguo zisizofaa kwa maadili na wingi wa kashfa zao za ngono kuchapishwa katika magazeti ya udaku.
Jackline anadaiwa alifura kwa hasira baada ya matamshi ya rais huyo wa TAFF kuonyesha kama yalikuwa yamemlenga yeye na baadhi ya kampani yake.
Akielezea dhana ya kuanzishwa Club ya Bongo Movie, ambayo yeye ni katibu wa umoja huo, anasema imelenga kuwashirikisha wasanii katika kusaidiana kwa hali na mali.
Jackline anakanusha kwamba walianzisha umoja huo kwa ajili ya kutaka kuua shirikisho la filamu nchini.
“Hiyo si maana yake bali tumeanzisha umoja wa kusaidiana kwa shida na raha na kuendeleza sanaa ya filamu nchini,” anafafanua Jackline.
Msanii huyo ametoa changamoto kwa wasanii wenzake wa filamu, wasiendekeze bifu kwa vile hazijengi na badala yake wakaze buti ili kuendeleza sanaa hiyo kwa vile sasa imekuwa na soko kubwa ndani na nje ya nchi.
Amesema kwa sababu hiyo, wawekezaji wazalendo nao wawekeze katika filamu kuliko kuwaachia Watanzania wenye asili ya Kiasia pekee.
Jackline anadai kuwa, kujitokeza kwa Waasia wengi kuwekeza mitaji yao katika filamu, kuna maanisha kuwa ina faida, ambapo amewataka wazawa kuingiza mitaji yao ili kuongeza ushindani wa malipo kwa wasanii na kuondoa unyanyasaji uliokithiri.
“Kampuni zinazojihusisha na masuala ya kutengeneza filamu na kusambaza ni chache na karibu zote zinashikwa na waasia, tunataka na watanzania wengine waweke mitaji yao ili tulipwe vizuri na kutuinua wasanii wa filamu,” anasema.
Jackline amesema kuwa ana furaha baada ya kuingia mkataba wa kufanya kazi za filamu na Kampuni ya Papa-Z Entertainment kwa vile, inamlipa vizuri na ushindani uliopo umesaidia wasanii wengine kupata maslahi bora.
Amesema kuwepo kampuni chache kulisabisha baadhi yao wawe wanyonge kutokana na kunyanyasika katika usambazaji wa kazi, ambapo sasa kila inapoongezeka kampuni nyingine ya usambazaji, inakuwa nafuu kwao.
“Sasa mimi nina jeuri ya kuishi mjini kutokana na kampuni ya Papa-Z ambao wananilipa vizuri na ninashirikiana nao katika kazi nyingi,” anaeleza Jackline, ambaye pia ana kampuni inayoitwa Line Wolper Production, ambayo inasimamia kazi zake.
Akizungumzia manufaa aliyopata katika maisha yake tangu awe msanii wa filamu, anasema ukiacha ustaa, amenufaika kwa vingi ambavyo amedai ni siri yake.
Jackline amesema pamoja na unyonyaji wanaofanyiwa katika filamu, anamshukuru Mungu kwa alichopata maishani mwake, ambapo amekiri wasanii wenye majina makubwa angalau wanaambulia kitu kuliko chipukizi.
“Kwa sisi ambao tayari tuna majina makubwa kidogo alhamdulilah, lakini kwa chipukizi ndiko kuna kilio kikubwa sana kama cha hakimiliki kwani imekuwa vigumu kudhibiti na nadhani hili tatizo halitakwisha vizazi na vizazi,” anasema msanii huyo.
Jackline aliibuka katika filamu mwaka 2007 baada ya kushawishiwa na msanii Lucy Komba ajikite kwenye fani hiyo.
Anasema aliungwa mkono na kuelekezwa vitu vingi na msanii huyo mzoefu na alicheza filamu nyingi za ‘Ama zako ama zangu’, ‘Kipenzi changu’, ‘Red Valentine’ na ‘Family Tears’, ambazo ziliteka soko na kumfanya ajulikane.
Baadaye alitunga filamu zake mbili ya ‘Wekeend’ na ‘My Princess’, ambazo zilifanya vizuri sokoni na akapata moyo wa kuwa mwigizaji rasmi.
Filamu nyingine alizoigiza ni ‘Utumwa wa mapenzi’ na ‘All About Love’ iliyotungwa na Jennifer Kiaka ‘Odama’, ambayo anasema aliipenda kutokana na kuvaa vyema uhusika kwa kuwa aliigiza kama mtoto.
Jackline pia anasema katika filamu iliyomsisimua sana tangu awe msanii ni ‘Last Minutes’ ya Leah Richard a.k.a Lamata, ambayo alicheza na Bajomba.
“Naipenda na huwa nairudia kuitazama kwa sababu inaelimisha, kuna siku wakati natoka super market (dukani) kuna mtu mmoja alilia baada ya kukutana na mimi mlangoni alisema niliigiza maisha yake lakini, bahati nilikuwa pamoja na mtunzi (Lamata) alimuelewesha hakumtungia mtu kisa kile,” anasema msanii huyo.
Jackline amesema kuwa kwanza anajipenda mwenyewe halafu Irene Uwoya kutokana na kufanana naye kiasi cha kudiriki kumuita pacha wake, ambaye anadai vitu anavyofanya katika filamu na maisha yake kwa ujumla anavikubali.
Nje ya nchi anampenda msanii nyota wa filamu wa Marekani, Halle Berry kwa alivyo mtulivu katika uigizaji na msafi.
Msanii huyo amesema mwakani anatarajia kwenda Malyasia kusomea masuala ya biashara na masoko kwa vile matarajio yake ya baadaye kujikita katika fani hiyo.
Jackline Wolper alizaliwa Moshi Mjini mwaka 1988 na alisoma kwenye shule tatu tofauti, lakini aliishia kidato cha tano katika shule ya Masai mwaka 2007 na baada ya hapo hakuendelea na masomo ya sekondari kutokana na sababu ambazo hakutaka kuzitaja.
Baadaye alijiunga na chuo cha USA Contact na kuhitimu stashahada ya masoko na biashara. Wazazi wa msanii huyo wanaishi Kibaha, Pwani na ni wafanyabiashara.

Wasanii wawashukia wasambazaji wa kazi zao


WASANII wa kazi mbalimbali za sanaa nchini wamewatupia lawama wasambazaji wa kazi zao kwa madai kuwa, wamevuruga mfumo wa usambazaji.
Wakizungumza kupitia programu ya kila wiki ya Jukwaa la Sanaa kwenye ofisi za Baraza la Sanaa Tanzania (BASATA) mwanzoni mwa wiki hii, wasanii hao walisema wasambazaji wa zamani wameshindwa kuhimili mfumo wa sasa.
Walizitaja sababu zilizosababisha kuvurugika kwa mfumo huo kuwa ni pamoja na wasambazaji hao kushusha bei za CD/DVD hadi shilingi elfu moja na pia kuwashusha thamani wasanii chipukizi.
Sababu zingine zilizotajwa na wasanii hao ni kuwabana wasanii wenye majina makubwa washirikiane na wale chipukizi na pia ununuaji wa hakimiliki za wasanii kinyume cha sheria.
Kwa mujibu wa wasanii hao, sababu nyingine ni kutokuwepo kwa mfumo mzuri wa kugawa kazi za wasanii kwenye madaraja.
“Leo hii, CD zinauzwa mtaani kwa shilingi elfu moja, hivi kweli kazi za wasanii wa Tanzania zimefikia kiwango cha kuuzwa kwa kiasi hicho cha pesa? Ni msambazaji gani ataweza kuhimili ushindani wakati kuna kampuni imeshusha thamani ya kazi za wasanii kwa kiwango hicho?” Alihoji Michael Sangu, ambaye ni msanii wa filamu.
Akijibu hoja za wasanii hao, Meneja wa Uzalishaji wa Kampuni ya Steps Entertainment, Kambarage Ignatus alisema, kampuni yake inafanya biashara, hivyo inajikita zaidi kutafuta faida.
Ignatus alisema kwa kuzingatia ukweli huo, kampuni yake inatilia mkazo kusambaza kazi zenye ubora na kuuzika.
Alikanusha madai kuwa, kampuni yake imekuwa ikiwabana wasanii maarufu ili wasifanyekazi na wale wanaochipukia na kusisitiza kuwa, kazi yoyote ya msanii ni makubaliano kati yake na kampuni.
“Hatuwezi kusambaza kila kazi ya msanii, wasanii ni wengi sana, isipokuwa tunalenga zile zenye ubora na kuuzika,”alisisitiza.

RATIBA YA LIGI KUU TANZANIA BARA

TAREHE MECHI UWANJA
Agosti 20, 2011 Coastal Union vs Mtibwa Sugar Mkwakwani
Kagera Sugar vs Ruvu Shooting Kaitaba
Toto African vs Villa Squad CCM Kirumba
Polisi Dodoma vs African Lyon Jamhuri
Azam vs Moro United Chamazi
Agosti 21, 2011 JKT Oljoro vs Simba Amri Abeid
Yanga vs JKT Ruvu Taifa
Agosti 23, 2011 Azam vs African Lyon Chamazi
Agosti 24, 2011 Polisi Dodoma vs Ruvu Shooting Jamhuri
JKT Oljoro vs Mtibwa Sugar Amri Abeid
Toto African vs Ruvu Shooting CCM Kirumba
Kagera Sugar vs Villa Squad Kaitaba
Yanga vs Moro United Taifa
Coastal Union vs Simba Mkwakwani
Agosti 27, 2011 African Lyon vs Toto African Chamazi
Agosti 28, 2011 JKT Ruvu vs Kagera Sugar Chamazi
Septemba 7, 2011 Mtibwa Sugar vs Yanga Jamhuri
Polisi Dodoma vs Ruvu Shooting Jamhuri
Simba vs Villa Squad Taifa
JKT Oljoro vs Azam Amri Abeid
Coastal Union vs Moro United Mkwakwani
Agosti 30, 2011 Moro United vs Toto African Chamazi
Agosti 31, 2011 Mtibwa Sugar vs Kagera Sugar Manungu
Villa Squad vs Polisi Dodoma Chamazi
Septemba 1, 2011 African Lyon vs Coastal Union Chamazi
Septemba 2,2011 JKT Ruvu vs JKT Oljoro Chamazi
Septemba 4, 2011 Ruvu Shooting vs JKT Oljoro Mlandizi
Mtibwa Sugar vs Toto African Manungu
Moro United vs Kagera Sugar Chamazi
Septemba 5, 2011 JKT Ruvu vs Coastal Union Chamazi
Septemba 10, 2011 Azam vs Simba Taifa
Septemba 11, 2011 Ruvu Shooting vs Yanga Taifa
Septemba 13,2011 Villa Squad vs Azam Chamazi
Septemba 14, 2011 Simba vs Polisi Dodoma Taifa
Septemba 15, 2011 African Lyon vs Yanga Taifa
Septemba 17, 2011 Toto African vs JKT Ruvu CCM Kirumba
Villa Squad vs Mtibwa Sugar Chamazi
JKT Oljoro vs African Lyon Amri Abeid
Ruvu Shooting vs Coastal Union Mlandizi
Septemba 18, 2011 Azam vs Yanga Taifa
Kagera Sugar vs Simba Kaitaba
Septemba 19, 2011 Moro United vs Polisi Dodoma Chamazi
Septemba 21, 2011 Kagera Sugar vs JKT Oljoro Kaitaba
Toto African vs Simba CCM Kirumba
Yanga vs Villa Squad Taifa
Coastal Union vs Azam Mkwakwani
Ruvu Shooting vs African Lyon Mlandizi
Septemba 22,2011 Polisi Dodoma vs Mtibwa Sugar Jamhuri
JKT Ruvu vs Moro United Chamazi
Septemba 24, 2011 Yanga vs Coastal Union Taifa
Toto African vs JKT Oljoro CCM Kirumba
Septemba 25, 2011 Simba vs Mtibwa Sugar Taifa
Kagera Sugar vs Polisi Dodoma Kaitaba
Septemba 26, 2011 JKT Ruvu vs Villa Squad Chamazi
Ruvu Shooting vs Azam Mlandizi
Septemba 27, 2011 African Lyon vs Moro United Chamazi
Oktoba Mosi, 2011 Polisi Dodoma vs Toto African Jamhuri
JKT Oljoro vs Coastal Union Amri Abeid
Mtibwa Sugar vs Ruvu Shooting Manungu
Villa Squad vs Moro United Chamazi
Oktoba 14, 2011 Yanga vs Kagera Sugar Taifa
Oktoba 15, 2011 JKT Ruvu vs Azam Chamazi
Oktoba 16, 2011 Simba vs African Lyon Taifa
Oktoba 8,2011 Coastal Union vs Villa Squad Mkwakwani
African Lyon vs Kagera Sugar Chamazi
JKT Oljoro vs Moro United Amri Abeid
Oktoba 9, 2011 JKT Ruvu vs Mtibwa Sugar Chamazi
Oktoba 19, 2011 Simba vs Ruvu Shooting Taifa
Oktoba 20,2011 Yanga vs Toto African Taifa
Oktoba 21, 2011 Azam vs Polisi Dodoma Chamazi
Oktoba 22, 2011 Simba vs JKT Ruvu Taifa
Coastal Union vs Polisi Dodoma Mkwakwani
Oktoba 23, 2011 Yanga vs JKT Oljoro Taifa
Oktoba 24, 2011 African Lyon vs Villa Squad Chamazi
Oktoba 25, 2011 Moro United vs Ruvu Shooting Chamazi
Mtibwa Sugar vs Azam Manungu
Oktoba 26,2011 Toto African vs Kagera Sugar CCM Kirumba
Oktoba 28,2011 JKT Ruvu vs African Lyon Chamazi
Oktoba 29, 2011 Yanga vs Simba Taifa
Polisi Dodoma vs JKT Oljoro Jamhuri
Toto African vs Coastal Union CCM Kirumba
Oktoba 30, 2011 Kagera Sugar vs Azam Kaitaba
Villa Squad vs Ruvu Shooting Chamazi
Mtibwa Sugar vs Moro United Manungu
Novemba 5, 2011 JKT Oljoro vs Villa Squad Amri Abeid
Moro United vs Simba Taifa
Polisi Dodoma vs Yanga Jamhuri
Toto African vs Azam CCM Kirumba
Kagera Sugar vs Coastal Union Kaitaba
Mtibwa Sugar vs African Lyon Manungu
Ruvu Shooting vs JKT Ruvu Mlandizi