KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, September 30, 2010

MREMBO WA TANZANIA AKABIDHIWA BENDERA

MREMBO wa Tanzania, Genevieve Emmanuel akiwa ameshika bendera ya taifa aliyokabidhiwa jana, ikiwa ni ishara ya kuliwakilisha taifa katika shindano la dunia linalotarajiwa kufanyika mwezi ujao nchini China.

WAANDISHI WANAPOKETISHWA NYUMA YA UZIO!


BAADHI ya waandishi kutoka vyombo mbalimbali vya habari wakiripoti mechi ya ligi kuu ya soka ya Vodacom kati ya Yanga na Kagera Sugar wakiwa nyuma ya uzio wa uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro baada ya kuzuiwa kuingia ndani ya uwanja huo. Katika mechi hiyo iliyochezwa wiki iliyopita, Yanga ilishinda mabao 2-0.


Tuesday, September 28, 2010

Waliozibeba Simba, Yanga wafungiwa

Rungu la kamati ya mashindano ya shirikisho la soka nchini TFF limewashukia waamuzi wanne wa ligi kuu Tanzania bara baada ya kuwafungia kwa kipindi cha miezi sita kuchezesha michezo ya ligi hiyo baada ya kushindwa kutafsiri sheria 17 za soka katika michezo kazaa iliyopita.

Ofisa habari wa TFF, FOLRIAN KAIJAGE, aliwataja waamuzi walifungiwa ni METHEW AKRAMA na FRANK KOMBA waliochezesha mchezo kati ya mabingwa watetezi Simba dhidi ya AZAM FC mchezo ulichezwa kwenye uwanja wa mkwakwani mkoani Tanga septemba 11 na Simba kuibuka kidedea kwa ushindi wa mabao mawili kwa moja.

KAIJAGE pia akawataja wamuzi wengine waliofungiwa na kamati hiyo kuwa ni RONALD SWAI na Msaidizi wake SAMUEL PENZU waliochezesha mchezo kati ya YANGA na KAGERA SUKARI kwenye uwanja wa JAMHURI MKOANI MOROGORO na wamuzi hao kushindwa kutafrisi kwa usahihi sheria za soka na kusababisha YANGA kufunga bao la kwanza,katika mchezo huo YANGA ilipata ushindi wa mabao MAWILI kwa BILA.

KAIJAGE kayataja maamuzi mengine ambayo yamefikiwa na kamati ya mashindano kuwa ni kuipiga faini klabu ya majimaji ya Songea ya shilingi LAKI TATU kwa kile alichoeleza kuwa majimaji ilichelewa kuingia uwanjani kwa dakika 15 na kusababisha mchezo huo kati yake na AFRICAN LYON kuchelewa kuanza,Majimaji wamedaiwa kuchelewa kuingia uwanjani kutokana na imani za kishirikiana katika mchezo ulipigwa kwenye uwanja wa majimaji SEPTEMBA 28.

KAIJAGE amesema kamisaa wa mchezo kati ya YANGA na KAGERA SUKARI yeye amefungiwa kwa mwaka mmoja kwa kushindwa kuandika taarifa sasahihi za mchezo huo.

Wednesday, September 22, 2010

TENGA: CECAFA imepata mafanikio makubwa


RAIS wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Leodegar Tenga amekiri kuwa, kumekuwepo na maendeleo makubwa ya soka katika nchi za ukanda huu wa Afrika ikilinganishwa na miaka iliyopita. Tenga alisema hayo alipohojiwa na mtandao wa Cafonline hivi karibuni. Makala hii ya Cafonline inafafanua zaidi.

Cafonline: Kipi unachoweza kusema kuhusu maendeleo yaliyoletwa na Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA)?

Tenga: Tumeleta maendeleo makubwa, hasa katika kuwavutia wadhamini zaidi katika michuano yetu na kuleta ushindani zaidi kwa sababu viwango vya zawadi vimeongezeka katika michuano ya Kombe la Chalenji na Kombe la Kagame. Pia kuzialika timu kama Zambia na Malawi katika Kombe la Chalenji kumesaidia kuwapa nafasi ya kujifunza wachezaji wa ukanda wetu.

Cafonline: Kwa nini nchi za ukanda wa CECAFA zimekuwa zikipata tabu kufuzu katika fainali za Kombe la Dunia na Kombe la Mataifa ya Afrika?

Tenga: Kadri tulivyoweza kuleta maendeleo katika ukanda huu, nafikiri hatukuwekeza vya kutosha katika masuala yanayohusu soka ya vijana kama walivyofanya kaka zetu wa Kaskazini, Kusini na Magharibi mwa Afrika wanavyofanya mipango kwa ajili ya Kombe la Dunia na Mataifa ya Afrika. Soka ni biashara kubwa na tunahitaji kuwekeza zaidi katika kuwapa mafunzo makocha na pia masuala ya utawala kama tunataka kufuzu kucheza michuano mikubwa ya Kombe la Dunia na pia siku zote kuwa na timu katika fainali za Mataifa ya Afrika.

Cafonline: CECAFA inadhani kwamba kuzileta timu mwalika katika michuano yake kunaweza kuleta miujiza?

Tenga: Katika njia moja au nyingine, ni kweli tunapata mafanikio kwa kuzialika timu hizi. Siku zote nimekuwa nikimshukuru Rais wa Chama cha Soka cha Zambia, Kalusha bwalya, ambaye siku zote amekuwa akituma timu tunapowaalika. Ndani ya shirikisho letu, pia tunafikiri mambo makubwa zaidi na hii itasaidia kuleta maendeleo ya muda mrefu katika ukanda wetu. Kwa mfano, Uganda inaanzisha ligi ya kulipwa mwaka huu na sisi Tanzania tutafuata nyayo hizo msimu ujao.

Cafoline: Ni vipi CECAFA na mashirikisho yake katika ukanda huu yanavyoweza kumudu kuwa na udhamini katika kipindi hiki kigumu wakati baadhi ya kampuni zimekuwa zikijitoa katika kudhamini soka?

Tenga: Japokuwa serikali katika nchi zinazounda CECAFA zinachukua nafasi kubwa katika kudhamini soka, kampuni binafsi zimekuwa zikijitokeza kuunga mkono mchezo huo. Kwa mfano, nchini Uganda wiki iliyopita, Kampuni ya MTN imetoa dola 700,000 za Marekani kwa ajili ya maendeleo ya timu ya taifa na soka ya vijana. Katika nchi kama Tanzania, Rwanda na Kenya, ligi zinadhaminiwa na kampuni binafsi na haya ni mafanikio makubwa.

Cafonline: Katika michuano ya hivi karibuni ya vijana wa chini ya miaka 20 iliyofanyika Eritrea, kulikuwepo na malalamiko ya kudanganya umri wa wachezaji kwa baadhi ya timu na Zanzibar ilitolewa kwa sababu ya kosa hilo. Unasemaje kuhusu hili?

Tenga: Udanganyifu wa umri ni tatizo kubwa si kwa sababu michezo ni amani na unapaswa kufuata sheria. Lakini tatizo hilo halipo katika nchi za ukanda wetu pekee, lipo zaidi Afrika Magharibi na Asia. Katika CECAFA tumechukua hatua madhubuti kuhakikisha tunakabiliana nalo, japokuwa tunapaswa kuendelea kuwaelimisha watu kuhusu hilo. Tutaendelea kuwa makini na wakali katika jambo hilo na kuchukua hatua kali kwa wahusika.

Cafonline: Unadhani kuwa na wanasoka wengi wa kulipwa ni muhimu kwa timu ya taifa, hasa katika ukanda wenu ili kuzisaidia nchi kufuzu kucheza katika michuano mikubwa?

Tenga: Binafsi, naamini tunapaswa kuwapa nafasi wachezaji wote kwenda kucheza soka ya kulipwa nje bila kuwazuia kwa sababu kutafungua milango zaidi kwa maendeleo ya soka katika siku zijazo. Tazama nchi za Afrika Magharibu kama Nigeria yenye wanasoka wengi wa kulipwa. Kumewasaidia kupata soko la wachezaji wengi zaidi na pia timu yao ya taifa tangu wachezaji hao walipoanza kwenda nje na kufanya kila kitu kitaalamu na pia kuwa na nidhamu. Acha tupeleke wanasoka wengi kadri iwezekanavyo kucheza soka ya kulipwa na matunda yake utayaona.

Cafonline: Una maoni gani kuhusu ushiriki wa timu za CECAFA katika michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Afrika za 2012?

Tenga: Nafikiri karibu timu zote zilizocheza nyumbani, zilishinda mechi zake ukiondoa Ethiopia na huu ni mwanzo mzuri. Kwa timu kufuzu katika michuano hiyo, siku zote ni muhimu kupata pointi zote za nyumbani na pia kupata pointi chache ugenini. Nilipata furaha kubwa niliposikia kwamba nchi yangu Tanzania ilipata pointi moja ugenini dhidi ya Algeria. Lakini timu zote za ukanda wa CECAFA hazipaswi kubweteka, zinapaswa kuendelea kuwa makini katika michezo yote.

Cafnline: Michuano ya vijana wa chini ya miaka 20 iliyofanyika Eritrea ilikuwa na mafanikio gani? Na Tanzania inajiandaaje kuwa mwenyeji wa michuano ya Kombe la Chalenji itakayofanyika Novemba hadi Desemba mwaka huu?

Tenga: Michuano ya Eritrea ilikuwa na ushindani mkubwa na ilitusaidia kuvumbua vipaji vipya vya vijana. Kujumuishwa kwa Yemen kama timu mwalikwa pia kulitusaidia kwa sababu kuliwapa nafasi ya kujifunza wachezaji wetu vijana. Lakini mwisho wa mashindano, timu bora, Eritrea na Uganda zilifuzu kucheza fainali na mabingwa watetezi Uganda walitwaa ubingwa kwa njia ya penalti.

Kama CECAFA, tunafanya kila tunaloweza kuona kwamba tunakuwa na michuano mizuri ya Kombe la Chalenji nchini Tanzania na tayari chama cha soka cha Tanzania kimeanza kutafuta wadhamini kwa lengo la kuifanya iwe na mafanikio makubwa zaidi.

SIKINDE YAMKABIDHI MAUFI GITA LA SOLO

MWANAMUZIKI Kaingilila Maufi (wa tatu kulia) akikabidhiwa gita la solo na kiongozi wa bendi ya Mlimani Park Orchestra, Habibu Abbas ‘Jeff’ (wa tatu kushoto) wakati wa onyesho lililofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye ukumbi wa DDC Kariakoo, Dar es Salaam.


UONGOZI wa bendi ya muziki wa dansi ya Mlimani Park Orchestra umemkabidhi rasmi mwanamuziki Kaingilila Maufi jukumu la kuwa mpiga gita la solo.
Hafla ya kumkabidhi jukumu hilo Maufi, ilifanyika mwishoni mwa wiki iliyopita wakati wa onyesho la bendi hiyo lililofanyika kwenye ukumbi wa DDC Kariakoo, Dar es Salaam.
Maufi alikabidhiwa gita hilo na kiongozi wa bendi hiyo, Habibu Abbas Jeff na kushuhudiwa na wanamuziki wenzake pamoja na baadhi ya wanachama wa Sikinde Family.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, mwanamuziki Hassan Kunyata alisema, Maufi amekabidhiwa gita hilo kutokana na uhodari wake wa kujifunza kupiga ala nyingi za muziki.
Kabla ya kuanza kupiga solo, Maufi alikuwa gita la rythim na ni mmoja kati ya watunzi hodari wa nyimbo.
Onyesho hilo, lililohudhuriwa na mashabiki lukuki, lilikuwa la kwanza kwa Mlimani Park mjini Dar es Salaam baada ya kumalizika kwa mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Bendi hiyo ilialikwa kwenda kufanya maonyesho katika mikoa ya Mwanza, Shinyanga na Kagera wakati wa sikukuu ya Idd El Fitri.
Wakati huo huo, msemaji mkuu wa bendi hiyo, Jimmy Chika alisema Mlimani Park inajiandaa kupakua vibao vipya vitatu vilivyotungwa wakati wa mwezi wa Ramadhani.

KARUME, MAALIM SEIF KUSHUHUDIA MECHI YA SOKA

Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
RAIS wa Zanzibar Dk. Amani Abeid Karume na Katibu Mkuu wa CUF, Seif Sharrif Hamad wanatarajiwa kushuhudia mechi ya soka ya kirafiki kati ya timu za kombaini za Unguja na Pemba .
Mechi hiyo itakayochezwa Oktoba Mosi mwaka huu kwenye Uwanja wa Amaan, imeandaliwa na Chama cha Soka cha Zanzibar (ZFA) kwa lengo la kuunga mkono maridhiano yaliyofikiwa na viongozi hao wawili na kuridhiwa na wananchi wote wa Zanzibar .
Mbali na viongozi hao wawili, ZFA pia imetoa mwaliko kwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano Dk. Ali Mohamed Shein, ambaye pia ni mgombea urais wa Zanzibar kupitia CCM na mgombea mwenza wa urais wa Tanzania , Dk. Mohammed Gharib Bilal.
Katibu Msaidizi wa ZFA, Masoud Attai alisema mjini hapa juzi kuwa, tayari chama chake kimeshatuma mwaliko kwa viongozi hao kwa ajili ya kushuhudia mechi hiyo ya kihistoria.
Attai alisema kutokana na umuhimu wa pambano hilo , wana hakika viongozi hao wataungana na mashabiki wa soka wa Zanzibar kuwashuhudia vijana kutoka visiwa hivyo viwili wakisakata kabumbu.
Aliongeza kuwa, mipango inafanywa ili Naibu Waziri Kiongozi na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Ali Juma Shamuhuna awe mgeni rasmi katika mechi hiyo.
“Tayari vikosi vya timu hizo mbili za Unguja na Pemba vimeshapatikana na vimeshaanza maandalizi kwa ajili ya mechi hiyo, inayolenga kuwaunga mkono viongozi wetu katika kufikia maridhiano kwa ajili ya kuijenga upya Zanzibar ,”alisema.
Kwa mujibu wa Attai. Kocha Mkuu wa Zanzibar , Stewart John Hall atautumia mchezo huo kuteua wachezaji watakaounda kikosi cha timu ya visiwa hivyo, itakayoshiriki katika michuano ya mwaka huu ya Kombe la Chalenji itakayofanyika Novemba mwaka huu mjini Dar es Salaam.
Aliongeza kuwa, fedha zitakazopatikana katika mechi hiyo, zitatumika kuchangia maandalizi ya Zanzibar katika michuano ya Chalenji, itakayozishirikisha timu za mataifa yanayounda ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

GURUMO ANAPOPONGEZWA NA WATOTO


BAADHI ya wanafunzi wa shule za msingi za mkoa wa Dar es Salaam wakigombea kumpa mkono kiongozi wa bendi ya muziki wa dansi ya Msondo Ngoma, Muhidin Gurumo wakati wa onyesho lililofanyika jana kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja, Dar es Salaam kwa ajili ya maadhimisho ya siku ya Amani Afrika.

Wachezaji Twiga Stars wajigamba


WACHEZAJI wa timu ya soka ya taifa ya wanawake, 'Twiga Stars' wametamba kufanya vizuri katika michuano ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika itakayofanyika mwezi ujao nchini Afrika Kusini.
Majigambo ya wachezaji hao yamekuja siku moja baada ya timu hiyo kupangwa kundi A katika michuano hiyo, pamoja na wenyeji Afrika Kusini, mabingwa wa zamani, Nigeria na Mali.
Upangaji wa makundi ya michuano hiyo ulifanyika juzi nchini Afrika Kusini na kundi hilo limebatizwa jina la kifo kutokana na kuundwa na vigogo vya soka ya wanawake barani Afrika.
Akizungumza kwa niaba ya wenzake, nahodha wa Twiga Stars, Sophia Mwasikili alisema, wanatambua vyema kwamba kundi walilopangwa ni gumu, lakini maandalizi waliyoyafanya yanawapa matumaini ya kufanya vizuri.
"Tupo kambini muda mrefu na kila siku tunafanya mazoezi ya nguvu na kujituma kwa pamoja, kitu ambacho kimetujengea hali ya kuelewana vyema uwanjani, hivyo nadhani tutafanya vizuri," alisema
Michuano hiyo, inayotarajiwa kuanza Octoba 29 hadi Novemba 14 mwaka huu, itashirikisha timu nane, ambapo Tanzania inashiriki kwa mara ya kwanza baada ya kuzitoa Ethiopia na Eritrea.
Nchi zingine zitakazoshiriki kwenye fainali hizo, ambazo zimepangwa kundi B ni bingwa mtetezi Equatorial Guinea, Ghana, Cameroon na Algeria.

SIMBA: Tunahujumiwa

Na Peter Katulanda, Mwanza
SIKU chache baada ya kupata kipigo cha bao 1-0 kutoka kwa Polisi ya Dodoma, wachezaji wa timu ya soka ya Simba wamedai kuwa, wamekuwa wakihujiwa na uongozi wa Toto African.
Wakizungumza mjini hapa juzi, baadhi ya wachezaji hao (majina yanahifadhiwa) walidai kuwa, uongozi wa Toto African hauitakii mema timu yao na unafanya juhudi za makusudi za kuihujumu.
“Kinachofanyika ni kwamba Toto African imekuwa ikifanya mikakati ya makusudi ya kuzisaidia timu zingine tunazocheza nazo kwenye Uwanja wa CCM Kirumba ili tufungwe,”alisema mmoja wa wachezaji hao.
Mchezaji huyo alisema, hujuma hizo pia zilifanyika katika mechi kati yao na Ruvu Shooting, iliyochezwa wiki mbili zilizopita kwenye uwanja huo, lakini hazikufanikiwa. Simba iliichapa Ruvu Shooting mabao 2-1.
Mchezaji mwingine aliongeza kuwa, siku zote Toto African haiitakii mema Simba kutokana na kuwafanyia hujuma kila wanapocheza kwenye uwanja huo, lakini sasa wamezibaini na watapigana kufa na kupona kuishinda.
Aliongeza kuwa, kinachofanywa na Toto African ni kuhakikisha Simba inafungwa mechi zake zote za Mwanza ili wahame katika mji huo na kuhamishia kituo chao kwingine.
Simba inatarajiwa kupambana na Toto African keshokutwa katika mechi itakayochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba. Mabingwa hao watetezi wanashika nafasi ya pili katika msimamo wa ligi hiyo, wakiwa na pointi tisa baada ya kucheza mechi nne, nyuma ya wapinzani wao wa jadi Yanga, wanaoongoza kwa kuwa na pointi kumi.
Kwa upande wake, Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Phiri alisema, wamejipanga vyema kuhakikisha kuwa, wanashinda mechi zao zote zilizosalia.
Phiri alisema kuanzia mechi yao ya keshokutwa dhidi ya Toto African, amepanga kuwatumia baadhi ya wachezaji wake waliokuwa majeruhi, akiwemo kipa namba moja Juma Kaseja.
Kaseja hakuweza kuichezea Simba tangu ligi hiyo ilipoanza, kufuatia kuvunjika kidole cha mkono wakati wa mazoezi ya timu ya taifa, Taifa Stars. Tayari kipa huyo ameshaanza mazoezi na wenzake.
Kocha huyo amewatupia lawama wachezaji wake kwa kucheza chini ya kiwango, hasa safu ya ushambuliaji, ambayo alisema imekuwa ikipoteza nafasi nyingi za wazi za kufunga mabao.
Naye Kocha Mkuu wa Toto African, Choki Abeid alisema Simba isitafute mchawi, aliyesabisha wafungwe na Polisi kwa sababu kiwango chao msimu huu kimeshuka.
Alisema kikosi chake kimejiandaa vyema kukabiliana na Simba na kuongeza kuwa, watahakikisha wanatoka uwanjani na pointi zote tatu.

Friday, September 17, 2010

ALI MUSTAFA BARTHEZ


UNAPOWAZUNGUMZIA wachezaji tegemeo kwa sasa ndani ya kikosi cha Simba, ni vigumu kuacha kulitaja jina la kipa Ali Mustapha 'Barthez', aliyeanza kujizolea sifa baada ya kuumia mkono kwa kipa namba moja Juma Kaseja. Kipa huyo amekuwa gumzo siku za hivi karibuni baada ya kuonyesha uwezo mkubwa wa kulinda lango la timu hiyo kwenye michezo aliyopangwa, hususan ya Ligi Kuu ya Vodacom msimu huu. Katika makala hii ya ana kwa ana iliyoandikwa na mwandishi wa blogu hii, kipa huyo anaelezea mafanikio yake kisoka.

SWALI: Kipa Ali Mustapha, unaweza kueleza historia yako kwa ufupi?
JIBU: Nimezaliwa jijini Dar es Salaam mwaka 1984, wazazi wangu wanaishi Ukonga, Majumba Sita. Nilihitimu elimu ya msingi katika shule ya Karakata mwaka 2001 na sikubahatika kuendelea na elimu ya sekondari. Nilianza kucheza soka tangu nilipokuwa nasoma.
SWALI:Ulicheza katika timu zipi kabla ya kusajiliwa na Simba?
JIBU:Nimecheza timu nyingi zikiwemo Mogo FC ya Karakata, Pentagon, Mkunguni, Kumbukumbu, Ashanti United iliyokuwa Ligi Kuu na nyingine nyingi za nje ya mkoa wa Dar es Salaam.
SWALI: Unakumbuka ulisajiliwa Simba mwaka gani?
JIBU:Nilijiunga na kikosi cha Simba mwaka 2005 na kuanzia hapo nilizidi kujifunza mengi kuhusu klabu hiyo na mchezo wa soka kwa ujumla.
SWALI: Nini kilikuvutia hadi kuamua kuchezea Simba badala ya timu nyingine?
JIBU:Mtu aliyenisukuma nitue Simba ni golikipa Mohamed Mwameja, ambaye alikuwa ananivutia sana enzi zake alipokuwa anadakia klabu hiyo. Sio siri huyu jamaa alinivuta sana kuichezea Simba kutokana na uwezo aliokuwa nao na mimi nimeiga baadhi ya mbinu zake.
SWALI:Mambo gani ambayo umejifunza tangu ulipojiunga na kikosi cha Simba?
JIBU:Unajua timu kama Simba ina watu wenye uelewa tofauti; kuna wasomi na wenye elimu ya kawaida ambao kila mmoja ana tabia zake. Kutokana na kuwepo hali hiyo, nimekumbana na wakati mgumu timu inapopata matokeo mabaya, lakini tunapofanikiwa kutwaa kombe lolote, kinakuwa kipindi kizuri kwetu wachezaji na wana Simba wote kwa sababu furaha inatawala kila mahali.
SWALI: Changamoto zipi umekutana nazo Simba?
JIBU:Changamoto ni kubwa kwani bila ya kujituma nisingedumu miaka hiyo na nafikiri ningekuwa nimeshaondoka siku nyingi. Naheshimu kazi inayonipa riziki ya kila siku na familia yangu na nimefika hapa kutokana na maelekezo mazuri ya makocha walionifundisha katika timu zote nilizocheza. Siwataji majina, lakini nawashukuru sana.
SWALI: Umekuwa unapambana na kipa Juma Kaseja kusaka namba katika kikosi cha kwanza cha Simba, unazungumziaje ushindani huo?
JIBU:Mchuano upo kati yetu, lakini sio siri napenda kumpongeza Kaseja, amekuwa ananipa changamoto kubwa ya kuongeza juhudi katika mazoezi na tunashirikiana vizuri.Bado kuna kazi kubwa ya kufikia malengo. La muhimu ni kujituma kwenye mazoezi na kuwa makini kwa mambo mengine ya nje ya uwanja na kuzingatia masharti ya vyakula na afya.
SWALI: Kukosekana Kaseja baada ya kuumia kidole kumekupa mwanya wa kuonyesha uwezo wako, je unajisikiaje?
JIBU:Binafsi nimesikitika Kaseja kuumia, lakini nimepata muda wa kuonyesha uwezo wangu.Nilikuwa najifua kwa nguvu ili niweze kufanya vitu vyangu kwenye michezo hiyo, ukiwemo dhidi ya Yanga wa kuwania Ngao ya Hisani.
Licha ya mchezo huo, ambao tulipoteza kwa bahati mbaya, nimeweza kuonyesha uwezo wangu katika mechi ya kirafiki dhidi ya Gor Mahia ya Kenya na Azam, ambayo ilikuwa ya Ligi Kuu iliyochezwa wiki iliyopita mkoani Tanga.
SWALI: Nini siri ya mafanikio yako katika mechi hizo?
JIBU: Kwanza kabisa siri ya mafanikio yangu ni kufanya mazoezi muda mwingi na kingine ni umoja uliopo ndani ya kikosi cha Simba. Pia najitahidi kusoma mbinu mbalimbali za kuzuia mashuti langoni ili niwe katika kiwango cha juu. Miiko ya soka ni suala ambalo pia nalizingatia ninapokuwa kambini.
SWALI: Je, umeoa na una watoto wangapi?
JIBU:Nimeoa na nimebahatika kupata mtoto mmoja, ambaye anaitwa Mustapha ana umri wa mwaka mmoja na nusu. Kwa kweli nazingatia sana kutunza mwili wangu ili niendelee kudaka miaka mingi.
SWALI:Timu zipi za nje unazopenda kuziona zinapocheza uwanjani?
JIBU:Mimi ni mpenzi mkubwa wa timu ya Manchester United, ambayo kila inapocheza inavuta hisia zangu. Navutiwa na timu hiyo kwa sababu ya kufanya vizuri kwenye mashindano mbalimbali. Napata changamoto ya kujituma ili niwe mchezaji mzuri kila mara kama walivyo wa timu ya Mashetani Wekundu.
SWALI:Kipi unapenda kuwaeleza wapenzi wa soka nchini?
JIBU:Nawaomba viongozi na wapenzi wa soka wajaribu kuwaamini wachezaji wao. Kila mtu anafahamu wazi majukumu yake. Hakuna mchezaji ambaye anaweza kuhujumu timu hata siku moja, kwani tunajua timu inapofanya vizuri tunanufaika. Viongozi watazame upya mbinu za kudhibiti mapato milangoni kwa sababu sisi ndio ajira yetu, hatuna vyanzo vingine vya mapato, wachezaji tunajisikia vibaya tunaposikia watu wamekamatwa na tiketi bandia. Wakati tunavuja jasho uwanjani, kumbe kuna wengine wananufaika kitu ambacho ni kibaya. Udhibiti wa mapato uongezwe.
Mwisho, naiomba serikali ijenge viwanja zaidi vya michezo kwa ajili ya kuongeza hamasa ya mchezo wa soka. Ikifanyika hivyo, vijana wengi wenye vipaji watajitokeza na watalisaidia taifa kupiga hatua mbele zaidi kisoka.

USHINDI MTAMU!

Wachezaji wa Yanga wakishangilia baada ya timu hiyo kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya AFC katika mechi ya ligi kuu ya Vodacom iliyochezwa kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha.

YANGA ARUSHA WAMPA TUZO MBUNA


UONGOZI wa tawi la klabu ya Yanga la mjini Arusha umempa tuzo maalumu mchezaji Fred Mbuna kutokana na kudumu kwenye timu hiyo kwa miaka kumi.
Mbali na tuzo hizo, ambazo ni cheti na ngao, tawi hilo pia limemzawadia mchezaji huyo pesa taslimu sh. 300,000.
Mbuna alikabidhiwa tuzo hizo na Mwenyekiti wa Yanga tawi la Arusha, Haji Haji wakati wa mechi ya ligi kuu ya soka ya Vodacom kati ya timu hiyo na AFC iliyochezwa kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid.
Beki huyo aliyesajiliwa na Yanga mwaka 2000 akitokea Majimaji ya Songea, alikabidhiwa tuzo hizo wakati wa mapumziko, mbele ya Mwenyekiti wa klabu hiyo, Llyord Nchunga na Mkuu wa mkoa wa Arusha, Isidore Shirima.
Katibu Mipango wa tawi hilo, Angelo Mweleka alisema wameamua kumzawadia Mbuna tuzo hizo kutokana na kuthamini mchango wake kwa timu ya Yanga.
“Mbuna ni mchezaji pekee wa Yanga aliyedumu kwenye klabu hiyo kwa miaka kumi bila kutoka na ametoa mchango mkubwa kwa Yanga na ni mfano wa kuigwa kwa wachezaji wengine,”alisema.
Mweleka alisema tawi lao kwa kushirikiana na uongozi wa Yanga, wanafanya mipango ili mchezaji huyo apatiwe nafasi ya kusomea ukocha baada ya kustaafu soka.
Akizungumza baada ya kupokea tuzo hizo, Mbuna aliishukuru uongozi wa Yanga tawi la Arusha na kuzitaka klabu zingine ziige mfano huo.
Mbuna alisema binafsi hakutarajia kupewa tuzo hizo na kuwataka wachezaji wengine wa Tanzania kuiga mfano wake kwa kudumu kwenye klabu zao kwa muda mrefu.

Thursday, September 16, 2010

BASATA: Marufuku wacheza shoo kuvaa nusu uchi

BARAZA la Sanaa la Taifa (BASATA) limewataka viongozi wa bendi za muziki wa dansi nchini, kuacha mara moja tabia ya kuwadhalilisha wacheza shoo (wanenguaji) kwa kuwavalisha mavazi ya kutia aibu na yanayodhalilisha utu wao.
Mbali na kupiga marufuku uvaaji wa mavazi hayo, BASATA imewataka wanenguaji hao, kuthamini utu wao na kufikiria upya dhana kwamba bila kuvaa nusu uchi, sanaa ya muziki wa dansi haiwezi kupata soko na kuvutia watazamaji wakati wa maonyesho.
Akizungumza wakati wa semina ya Jukwaa la Sanaa, inayoandaliwa kwa pamoja na BASATA na Chama cha Waandishi wa Habari za Sanaa na Utamaduni (CAJAtz),Katibu Mtendaji wa baraza hilo, Ghonche Materego alisema, lazima wadau wa muziki wa dansi wafikirie upya na kubadili mara moja tabia ya kuendekeza maonyesho yanayochafua maadili ya mtanzania.
“Wanenguaji lazima wafikie hatua waseme kwamba, udhalilishaji huu wa nusu uchi basi tena.Wavae mavazi yenye heshima kama wanavyovaa wale wa kiume,” alisema.
Aliongeza kuwa, dhana kwamba bila wanenguaji kuvaa nusu uchi maonyesho ya muziki wa dansi hayapati watazamaji na biashara haifanyiki, ni ya uongo na inaonyesha jinsi wasanii wa dansi walivyokosa ubunifu wa kuvutia watu kwenye maonyesho yao, badala yake kubaki wakiendeshwa na hisia zisizo za kisanaa.
“Ushindani wa kibiashara, ambao unaomfanya msanii kuwa dhalili ili kuvuta watu kwenye maonyesho haukubaliki, bali unawafanya wasanii kuwa makapuku na wanaopoteza thamani yao,” aliongeza.
Alisisitiza kwamba, BASATA imekuwa ikikemea na kuchukua hatua za kisheria dhidi ya unenguaji wa nusu uchi, lakini mabadiliko yamekuwa ni ya muda na baadaye kurudi kwenye udhalilishaji uleule.
Aliongeza kuwa kwa sasa, baraza lake linafanya utafiti kwenye sanaa ya unenguaji na mara utakapokamilika, mwongozo kwenye sanaa hii utatolewa na kutakiwa kufuatwa na wadau wote.
Kwa upande wake, mwasilishaji wa mada ya unenguaji wa nusu uchi,Nsao Shalua, ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Sanaa ya BASATA alisema, mavazi katika kazi ya sanaa yapo kwa ajili ya kuwakilisha tamaduni za jamii husika, hivyo vichupi vinavyoonekana kwenye majukwaa havina utambulisho wala maana yoyote.
“Maleba (mapambo/mavazi) katika sanaa yoyote yanakuwa na utambulisho wa jamii na kazi husika, hivyo vivazi vya nusu uchi vinavyovaliwa havina nafasi,” alisema.
Katika Jukwaa hilo la sanaa, lililopambwa na maonyesho ya wanenguaji kutoka bendi mbalimbali nchini, waliokuwa katika mavazi tofauti, wadau wengi walilamika juu ya mavazi ya kutia aibu wanayovaa wanenguaji na kutoa mwito kukomeshwa mara moja.

KOPA: Mtasema sana, sijafulia, nazidi kupeta


BAADA ya ukimya wa muda mrefu, mwimbaji machachari wa muziki wa taarab nchini, Khadija Omar Kopa ameibuka na kusema kuwa hajafilisika kiusanii.
Badala yake, Khadija amesema bado anaendelea kuteza katika muziki huo na kwamba ataendelea hivyo kwa kipindi kirefu kijacho.
Khadija amesema kauli zinazotolewa na baadhi ya wadau wa muziki huo kwamba ukimya wake unaonyesha amefilisika, hazina ukweli wowote.
“Mimi sijafulia, wanaosema hivyo watasema sana, bado nipo juu na ninazidi kupeta, wanaofikiria nimefulia, wanajidanganya nafsi zao,”alisema.
Khadija alisema hayo wiki iliyopita wakati wa mkutano wa kampeni wa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Jakaya Kikwete uliofanyika katika mji wa Kilosa.
Katika mkutano huo uliohudhuriwa na watu lukuki, Khadija alitoa burudani kali alipoimba kibao chake kipya, kinachokwenda kwa jina la Wanaume magumegume.
Khadija alijigamba kuwa, yeye bado ni malkia wa muziki wa mipasho nchini na kwamba hana mpinzani. Aliisifu CCM kwa namba inavyotekeleza ilani yake ya uchaguzi.
Khadija alianza kupata umaarufu alipokuwa katika kikundi cha taarab cha Culture cha Zanzibar, ambako alitamba kwa vibao vyake vya Daktari, Kadandie na Wahoi.
Baadaye aliibukia kwenye kundi la Tanzania One Theatre (TOT-Plus) kabla ya kuhamia kundi la Muungano na kisha East African Melody.

SIMBA YAPETA, YANGA YABANWA



MABINGWA watetezi wa ligi kuu ya soka ya Vodacom, Simba jana waliendelea kuvuna pointi tatu baada ya kuichapa Ruvu Shooting mabao 2-1 katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini hapa.
Mshambuliaji Mussa Hassan ‘Mgosi’ ndiye aliyeibeba Simba baada ya kuifungia mabao yote mawili, dakika ya tano na 20 wakati bao la kujifariji la Ruvu Shooting lilifungwa na Mashaka Maliwa dakika ya 16.
Kwa matokeo hayo, Simba bado inaendelea kuongoza ligi hiyo kwa kuwa na pointi tisa baada ya kucheza mechi tatu na kushinda zote wakati Ruvu Shooting haina pointi hadi sasa.
Wakati huo huo, timu kongwe ya Yanga jana ilibanwa mbavu baada ya kulazimishwa kutoka sare ya bao 1-1 na Mtibwa Sugar katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.
Sare hiyo iliifanya Yanga iendelee kushika nafasi ya pili katika msimamo wa ligi hiyo, ikiwa na pointi saba baada ya kucheza mechi tatu wakati Mtibwa ni ya tano kwa kuwa na pointi tano baada ya kucheza idadi hiyo ya mechi.
Pambano hilo lilianza kwa kasi huku kila timu ikipania kuwa ya kwanza kupata bao. Yanga nusura ipate bao dakika ya sita wakati Jerry Tegete alipopewa pasi akiwa nje kidogo ya mita 18, lakini shuti lake lilitoka nje.
Mtibwa ilifanya shambulizi kali kwenye lango la Yanga dakika ya 23 wakati Yona Ndabila alipoingia na mpira ndani ya eneo la hatari, lakini shuti lake liliokolewa na kipa Yaw Berko.
Dakika mbili baadae, kibao kiliigeukia Mtibwa baada ya Nsa Job kupewa pasi safi akiwa ndani ya eneo la hatari, lakini shuti lake liliokolewa na kipa Shabani Kado.
Mtibwa ilihesabu bao lake dakika ya 33 kupitia kwa Obadia Mungusa, aliyeunganisha wavuni kwa kichwa mpira wa kona uliopigwa na Yusuf Ndula.
Yanga ilisawazisha dakika ya 73 kwa bao lililofungwa na Abdi Kassim kwa shuti la umbali wa mita 30 lililotinga moja kwa moja wavuni.

YANGA: Yaw Berko, Shadrack Nsajigwa, Stephano Mwasika, Isaack Boakye, Nadir Haroub ‘Canavaro’, Ernest Boakye, Athumani Iddi ‘Chuji’, Abdi Kassim/Nurdin Bakari, Jerry Tegete/Yahya Tumbo, Nsa Job na Geofrey Bonny.
MTIBWA:Shabani Kado, Juma Abdul, Yusuf Nguya, Obadia Mungusa, Salvatory Ntebe, Shaaban Nditi, Zuberi Katwila, Masoud Chile/Ally Mohamed, Thomas Maurice/Saidi Rashid, Yona Ndabila, Salum Machaku.

Sunday, September 12, 2010

GENEVIEVE EMMANUEL NDIYE MISS TANZANIA 2010

MREMBO wa Tanzania, Genevieve Emmanuel akipongezwa na mama yake mara baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa taji hilo mwishoni mwa wiki iliyopita.
MREMBO wa Tanzania, Genevieve Emmanuel akiwa ndani ya gari aina ya Hyundai alilozawadiwa baada ya kushinda taji hilo.

MRWMBO wa Tanzania wa mwaka 2010, akiwa na mshindi wa pili na wa tatu mara baada ya kuvikwa taji katika shindano lililofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam.


KIEMBA: Simba, Yanga timu ngumu kuzichezea


SWALI: Wewe ni miongoni mwa wachezaji wachache, ambao wamewahi kuzichezea timu za Simba na Yanga kwa nyakati tofauti. Hebu tueleze, umejifunza nini kutokana na kuzichezea timu hizo kongwe nchini?
JIBU: Ukweli ni kwamba klabu hizi mbili hazina tofauti kubwa kiuendeshaji. Pia tabia za wanachama na viongozi wake na mambo mengine ya kiutendaji yanafanana. Lakini nisingependa kuzungumza kiundani sana kuhusu mambo hayo.
Lakini kilicho wazi ni kwamba, mashabiki wengi wa soka nchini wanazipenda klabu hizi na kila mchezaji anakuwa kwenye wakati mgumu anapoichezea moja kati ya timu hizi mbili kwa sababu ushindani wa namba unakuwa mkubwa na unapofanya kosa katika mechi kati ya timu hizi mbili, lawama zake huwa ni kubwa na nzito.
SWALI: Una maoni gani kuhusu kikosi cha Simba msimu huu na nafasi yako kwenye kikosi cha kwanza?
JIBU: Uongozi wa Simba umefanya usajili mzuri msimu huu na kwa malengo mazuri. Nadhani benchi la ufundi liliangalia zaidi kila idara kuhakikisha tatizo lililokuwepo msimu uliopita, linatafutiwa ufumbuzi.
Mbali na hilo, bado kuna vita kali hivi sasa ya kila mchezaji kutaka namba kwenye kikosi cha kwanza. Kila mchezaji amekuwa akijifua kwa nguvu zake zote ili kuhakikisha anakuwa fiti muda wote na pia hakosi nafasi ya kucheza.
Kila mchezaji amekuwa akifanya jitihada kubwa ya kumshawishi Kocha Patrick Phiri ampe namba kwenye kikosi cha kwanza. Changamoto hiyo ndiyo iliyonifanya niongeze muda mwingi wa kufanya mazoezi kwa siku ili niweze kufikia kiwango kitakachokubalika kwa kocha wangu.
Ukichezea Simba au Yanga, mchezaji unapaswa kuwa makini sana na kuonyesha uwezo wako wote uwanjani. Vinginevyo, ukizubaa tu, unapoteza namba na kuishia kwenye benchi.
SWALI: Una maoni gani kuhusu kikosi cha sasa cha Taifa Stars? Wewe binafsi una malengo yoyote ya kutaka kuitwa kwenye timu hiyo siku zijazo?
JIBU: Kikosi cha Taifa Stars kwa sasa ni kizuri na nina hakika kama wataendelea kupewa ushirikiano mkubwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na wadau wengine wa soka, kinaweza kufuzu kucheza fainali za kombe la Mataifa ya Afrika.
Lakini jambo la msingi ni kwa Kocha Jan Poulsen na benchi zima la ufundi la timu hiyo, kupewa nafasi ili waweze kutimiza majukumu yao.
Kwa upande wangu, niliwahi kuitwa kwenye kikosi hicho na kocha wa zamani, Mshindo Msolwa mwaka 2006 na kwenda kushiriki michuano ya Kombe la Chalenji iliyofanyika nchini Rwanda.
Mawazo ya kutaka kurejea tena ndani ya kikosi hicho bado yapo kichwani mwangu kwani enzi hizo wachezaji walikuwa wakiitwa kwenye timu, wanatafuta sababu ili wasijiunge nayo, lakini kwa sasa kila mchezaji anapenda kuichezea Taifa Stars baada ya kujitokeza kwa wafadhili wengi.
SWALI: Kwa nini unasema hivyo?
JIBU: Zamani tulipokuwa tukiitwa kwenye kambi ya Taifa Stars, kila mchezaji alilazimika kwenda na vifaa vyake vya michezo. Kuna wakati hata chakula kwa wachezaji kilikuwa cha tabu, tofauti na sasa, ambapo wachezaji wanapata huduma zote muhimu na za ziada na kuwekwa kwenye hoteli zenye hadhi.
SWALI: Unayaonaje maendeleo ya soka hapa nchini hivi sasa ikilinganishwa na miaka ya nyuma?
JIBU: Maendeleo yanaridhisha kwa sababu ushindani katika michuano ya ligi kuu umeongezeka na karibu kila timu ya ligi kuu, inayo timu ya vijana wa chini ya miaka 20 na kumeanzishwa michuano mbalimbali ya vijana.
Ushauri wangu kwa TFF ni kutafuta wadhamini wengine zaidi kwa ajili ya michuano ya vijana kwa lengo la kuongeza ushindani zaidi. Nasema hivyo kwa sababu ushindani kwa michuano ya vijana hivi sasa umekuwa mkubwa na vijana wengi wanajitokeza kwa lengo la kuonyesha vipaji vyao.
Jambo lingine la muhimu ni kwamba naiomba TFF itafute wadhamini kwa ajili ya kuendesha mafunzo kwa makocha kwa sababu wengi waliopo sasa, walisoma miaka mingi iliyopita hivyo wanashindwa kwenda na wakati. Naamini wakiwa wanapata mafunzo ya mara kwa mara, kiwango kitazidi kuongezeka.
SWALI: Ni jambo gani, ambalo limekuwa likikukera katika uendeshaji wa soka hapa nchini?
JIBU: Binafsi nachukizwa sana na baadhi ya waamuzi wa soka nchini, ambao hushindwa kutimiza majukumu yao uwanjani kwa kuweka pembeni sheria 17 za soka na kuchezesha kwa upendeleo. Pia huwa nakerwa sana na tabia za baadhi ya mashabiki wa soka nchini, kupenda kuwashutumu wachezaji kwamba wamehujumu timu zao bila ya kuwa na ushahidi.
Hili la pili ndilo baya zaidi. Mimi ni muislamu safi, siwezi kuwa tayari kukiuka maagizo ya Mungu kwa kufanya mambo kinyume na dini. Ninachowaomba mashabiki wa soka nchini ni kuwaamini wachezaji wao na kama kuna jambo wanalitilia wasiwasi, ni vyema wafanye kwanza uchunguzi badala ya kutoa tuhuma nzito kwa wachezaji kwa sababu kufanya hivyo ni kuwavunja moyo.
SWALI: Elezea historia ya maisha yako na jinsi ulivyojitosa katika soka badala ya michezo mingine.
JIBU:Mimi ni mtoto wa pili wa mzee Ramadhan Kiemba, kati ya watoto watano, ambao mzee alijaliwa kuzaa. Nimesoma shule ya msingi mkoani Arusha na sekondari katika shule ya Jitegemee ya mjini Dar es Salaam.
Nilianza kucheza soka tangu nikiwa mdogo. Nilichezea timu nyingi, lakini ya kwanza kubwa ni Kagera Sugra ya Bukoba. Nilivutiwa sana na Kagera Sugar kwa sababu kulikuwepo utaratibu mzuri wa kutoa maslahi kwa wachezaji ili waweze kujituma uwanjani. Pia nimechezea timu za Yanga, Miembeni, Moro United na sasa nipo Simba.
SWALI: Unaweze kueleza ni kwa nini umekuwa ukihama kutoka timu moja hadi nyingine?
JIBU: Hakuna kingine zaidi ya kutafuta maslahi mazuri zaidi. Sina hakika na maendeleo ya Kagera Sugar yalivyo hivi sasa, lakini kama bado wanaendelea na mfumo uliokuwepo zamani, nina hakika ni timu inayopaswa kuwa mfano wa kuigwa.

CHEGGE: Wasanii wa kweli wameanza kuonekana, wazushi wametoweka


MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Saidi Juma Hassan ‘Chegge Chigunda’ ametamba kuwa, hakuna wimbo uliowahi kuvuma kwa kipindi kirefu kama ‘Mkono mmoja’, aliourekodi kwa kushirikiana na Mheshimiwa Temba na Wahu kutoka Kenya.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Chegge alisema wimbo huo umekaa kwenye chati za nyimbo bora kwa zaidi ya miezi mitatu nab ado unazidi kukubalika kwa mashabiki wengi.
Chegge, ambaye ni mmoja wa wasanii wanaounda kundi la TMK Wanaume Family alisema, ujumbe uliomo kwenye wimbo huo ni mwepesi na hauchoshi kuusikiliza kutokana na mpangilio wake kuwa mzuri.
“Kwa kweni ni wimbo uliotuweka kwenye chati ya juu na naweza kusema kila mahali unakubalika,”alisema Chegge, ambaye mara nyingi hupenda kurekodi nyimbo zake kwa kushirikiana na Temba.
Msanii huyo aliyesokota nywele zake kwa mtindo wa rasta alisema, kumekuwepo na mabadiliko makubwa katika muziki wa kizazi kipya hivi sasa na kwamba wasanii wa kweli wameanza kuonekana na wazushi wameanza kupotea.
"Ukiangalia muziki umekuwa mgumu sana. Hivi sasa kila kukicha kunakuwepo na mabadiliko ya kila aina, huyu yupo yule hayupo, ndio mambo yanavyokuwa, watu wameelewa nani mkweli na nani anafoji,” alitamba msanii huyo mwenye makeke anapokuwa stejini.
"Wasanii wameanza kujichuja wenyewe, msanii wa ukweli anabaki kuwa wa ukweli, ambaye hajui anachokifanya anapotea,” aliongeza.
"Ndio maana utaona wale wanaoweza muziki ndio wamebaki kuwa juu siku zote na ambao hawawezi, wanaonekana hawawezi. Inaonekana wameshindwa ingawa siwezi kujua sababu nyingine zinazowakwamisha,” alisema Chegge.
"Lakini kwa wenye akili, wakiangalia wanaona ni wazi wanaojua wanachokifanya ndio wanapeta, wengine wamechemsha. Huwezi kufoji kipaji, kama huna, huna tu, na kama hujui, hujui tu,"aliongeza msanii huyo.
Chegge alisema kufuatia mafanikio makubwa aliyoyapata katika kibao hicho, ameamua kuandaa wimbo mwingine mpya utakaojulikana kwa jina la ‘Fungeni milango’. Alisema atarekodi wimbo huo kwa kushirikiana tena na Temba. "Tuna utaratibu wetu wa kazi tuliojiwekea, kwamba sasa kwenye kundi ni zamu ya watu fulani kufanyakazi na muda fulani ni zamu ya watu fulani,” alisema.
"Sasa ni zamu yangu na Temba, ndio maana unaona kazi zetu ndiyo nyingi zimepewa nafasi, baada ya muda utasikia wengine na kundi hali kadhalika," aliongeza.
"Mfumo huo ndio tumekuwa tukitumia tangu awali na napenda kusisitiza kuwa, kundi letu bado lipo imara kama kawaida na tutazidi kufanya vizuri kwa vile tuna ushirikiano wa dhati na kila mmoja ana uwezo na kile anachokifanya," alisisitiza.
Chegge, ambaye anaishi maeneo ya Sinza, Dar es Salaam, alisema katika maisha yake, anachukia watu wanaopenda kukwamisha maendeleo yake pamoja na wezi wa kazi za wasanii.
Akizungumzia mipango yake ya baadaye, alisema kuwa ni pamoja na kujenga nyumba ya kuishi na kuoa mke mwenye heshima na adabu wakati wote na asiye na ubaguzi wa aina yoyote.
Kuhusu ratiba yake, Chegge alisema kwa kawaida huwa anapenda kuamka saa nne asubuhi na kwenda kwenye mazoezi ya muziki na kundi lake la TMK na anaporejea nyumbani, hutumia muda mwingi kupumzika na kuandika mashairi ya nyimbo zake.
Mbali na kutamba na kibao cha ‘Mkono mmoja’, Chegge pia amewahi kutamba kwa vibao vyake kama vile ‘Karibu kiumeni’ na ‘Mambo bado’ alichomshirikisha Judith Wambura ‘Lady JayDee’.

Thursday, September 2, 2010

KOCHA MPYA WA NETIBOLI ATUA NCHINI


KOCHA wa timu ya taifa ya netiboli, Queen Stars,Simone Macknis (wapili kushoto), akiwa na Mwenyekiti wa Chama Cha Netiboli nchini(CHANETA), Anna Bayi,kocha huyo alipowasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam,jana.Kushoto ni Nahodha wa timu hiyo, Jacqueline Sikozi.

USAJILI WA WACHEZAJI ENGLAND

ARSENAL
WAPYA: Sebastien Squillaci (Sevilla, pauni mil 6.5), Laurent Koscielny (Lorient, pauni mil 10), Marouane Chamakh (Bordeaux, huru), Kyle Ebecilio (Feyenoord, huru), Phillip Roberts (Norwich, huru)
WALIOUZWA: Philippe Senderos (Fulham, huru), Fran Merida (Atletico Madrid, huru), Mikael Silvestre (Werder Bremen, huru), Sol Campbell (ameruhusiwa), William Gallas (Tottenham, huru), Francis Coquelin (Lorient, mkopo), Eduardo (Shakhtar Donetsk, pauni mil sita), Sol Campbell (Newcastle, huru), Sanchez Watt (Leeds, mkopo), Jay Simpson (Hull, ada haikutajwa), Armand Traore (Juventus, mkopo)

ASTON VILLA
WAPYA: Stephen Ireland (Manchester City, mabadilishano)
WALIOUZWA: James Milner (Manchester City, pauni mil 26), Andy Marshall (ameruhusiwa), Wilfred Bouma (PSV Eindhoven, huru), Marlon Harewood (Blackpool, huru), Nicky Shorey (West Bromwich, ada haikutajwa)

BIRMINGHAM
WAPYA: Enric Valles (NAC Breda, huru), Ben Foster (Manchester United, pauni mil sita), Nikola Zigic (Valencia, pauni mil sita), Matt Derbyshire (Olympiakos, mkopo), Alexander Hleb (Barcelona, mkopo), Martin Jiranek (Spartak Moscow, ada haikutajwa), Jean Beausejour (Club America, pauni mil nne)
WALIOUZWA: Gary McSheffrey (Coventry, huru), Gregory Vignal (ameruhusiwa), Jared Wilson (ameruhusiwa), Lee Carsley (Coventry, huru), Artur Krysiak (Exeter, huru), Frank Queudrue (ameruhusiwa), Christian Benitez (Santos Laguna, huru), Marcus Bent (Wolves, mkopo)

BLACKBURN
WAPYA: Hugo Fernandez (Union Deportiva Cornella, ada haikutajwa), Mame Biram Diouf (Blackburn, mkopo), Benjani (Manchester City, huru)
WALIOUZWA: Steven Reid (West Brom, huru), Yildiray Basturk (ameruhusiwa), Zurab Khizanishvili (Reading,mkopo)

BLACKPOOL
WAPYA: Luke Varney (Derby, mkopo), Dekel Keinan (Maccabi Haifa, huru), Craig Cathcart (Manchester United, ada haikutajwa), Marlon Harewood (Aston Villa, huru), Elliot Grandin (CSKA Sofia, ada haikutajwa), Ludovic Sylvestre (Mlada Boleslav, ada haikutajwa), Malaury Martin (Monaco, ada haikutajwa), Matt Phillips (Wycombe, huru), DJ Campbell (Leicester, ada haikutajwa), David Carney (FC Twente, mkopo)
WALIOUZWA: Daniel Nardiello (ameruhusiwa), Hameur Bouazza (ameruhusiwa), Al Bangura (ameruhusiwa), Danny Mitchley (ameruhusiwa), Joe Martin (ameruhusiwa), Stephen McPhee (ameruhusiwa), Ben Burgess (Notts County, huru)

BOLTON
WAPYA: Martin Petrov (Manchester City, huru), Robbie Blake (Burnley, huru), Marco Alonso (Real Madrid, pauni mil 1.6), Tom Eaves (Oldham, ada haikutajwa), Rodrigo Moreno (Benfica, mkopo)
WALIOUZWA: Ricardo Vaz Te (Panionios, huru), Ali Al Habsi (Wigan, mkopo), Nicky Hunt (Bristol City, huru).

CHELSEA
WAPYA: Yossi Benayoun (Liverpool, pauni mil sita), Matej Delac (Inter Zapresic, pauni mil 2.7), Tomas Kalas (Sigma Olomouc, pauni mil 5.2), Ramires (Benfica, pauni mil 18)
WALIOUZWA: Michael Mancienne (Wolves, mkopo), Joe Cole (Liverpool, huru), Michael Ballack (Bayer Leverkusen, huru), Juliano Belletti (Fluminese, huru), Miroslav Stoch (Fenerbahce, pauni mil 2.5), Tomas Kalas (Sigma Olomouc, mkopo), Ryan Bertrand (Nottingham Forest, mkopo), Scott Sinclair (Swansea, pauni mil moja), Jack Cork (Burnley, mkopo), Nemanja Matic (Vitesse Arnhem, mkopo), Slobodan Rajkovic (Vitesse Arnhem, mkopo), Franco di Santo (Wigan, ada haikutajwa)

EVERTON
WAPYA: Joao Silva (Desportivo Das Aves, pauni 500,000), Jan Mucha (Legia Warsaw, huru), Jermaine Beckford (Leeds, huru), Magaye Gueye (Strasbourg, ada haikutajwa).
WALIOUZWA: John Ruddy (Norwich City, huru), Dan Gosling (Newcastle, huru), Carlo Nash (Stoke City,huru), Joseph Yobo (Fenerbahce, mkopo).

FULHAM
WAPYA: Rafik Halliche (Benfica, pauni mil 1.3), Moussa Dembele (AZ Alkmaar, pauni mil tano), Philippe Senderos (Arsenal, huru), Jonathan Greening (West Bromwich, ada haikutajwa), Carlos Salcido (PSV Eindhoven, ada haikutajwa), Lauri Dalla Valle (Liverpool, ada haikutajwa) Alex Kacaniklic (Liverpool, ada haikutajwa).
WALIOUZWA: Chris Smalling (Manchester United, pauni mil 10), Erik Nevland (Viking, huru), Elliot Omozusi (Leyton Orient, huru), Christopher Buchtmann (Cologne, ada haikutajwa), Wayne Brown (Bristol Rovers, huru), Toni Kallio (ameruhusiwa), Paul Konchesky (Liverpool, ada haikutajwa).

LIVERPOOL
WAPYA: Joe Cole (Chelsea, huru), Jonjo Shelvey (Charlton, pauni mil 1.7), Milan Jovanovic (Standard Liege, huru), Danny Wilson (Rangers, pauni mil tano), Christian Poulsen (Juventus, pauni mil 4.5), Brad Jones (Middlesbrough, pauni mil 2.3), Raul Meireles (Porto, pauni mil11.5), Paul Konchesky (Fulham, ada haikutajwa), Emiliano Insua (Galatasaray, mkopo)
WALIOUZWA: Alberto Aquilani (Juventus, mkopo), David Martin (MK Dons, huru), Mikel San Jose (Atletico Bilbao, ada haikutajwa), Robbie Threlfall (Bradford, huru), Yossi Benayoun (Chelsea, pauni mil sita), Albert Riera (Olympiakos, ada haikutajwa), Krisztian Nemeth (Olympiakos, ada haikutajwa), Diego Cavalieri (Cesena, ada haikutajwa)

MANCHESTER CITY
WAPYA: James Milner (Aston Villa, pauni mil 26), Yaya Toure (Barcelona, pauni mil 28), Jerome Boateng (Hamburg, pauni mil 10), David Silva (Valencia, pauni mil 24), Aleksandar Kolarov (Lazio, pauni mil 17), Alex Henshall (Swindon Town, huru), Albert Rusnak (MFK Kosice, ada haikutajwa), Mario Balotelli (Inter Milan, pauni mil 23)
WALIOUZWA: Stephen Ireland (Aston Villa, sehemu ya mabadilishano), Craig Bellamy (Cardiff, mkopo), Valeri Bojinov (Parma, pauni mil 4.5), Martin Petrov (Bolton, huru), Benjani (Manchester City, huru), Sylvinho (ameruhusiwa), Robert Mak (Nuremberg, pauni 500,000), Gunnar Nielsen (Tranmere, mkopo), Javier Garrido (Lazio, pauni mil 2.5), Vladimir Weiss (Rangers, mkopo), Robinho (AC Milan, ada haikutajwa), Adam Clayton (Leeds, ada haikutajwa).

MANCHESTER UNITED
WAPYA: Chris Smalling (Fulham, pauni mil 10), Javier Hernandez (Guadalajara, pauni mil 10), Marnick Vermijl (Standard Liege, ada haikutajwa), Bebe (Vitoria Guimaraes, pauni mil 7.4).
WALIOUZWA: Ben Foster (Birmingham, pauni mil sita), Zoran Tosic (CSKA Moscow, pauni mil nane), Tom Heaton (Cardiff, huru), Danny Drinkwater (Cardiff, mkopo), Danny Welbeck (Sunderland, mkopo), Craig Cathcart (Blackpool, ada haikutajwa), Mame Biram Diouf (Blackburn, mkopo), Rodrigo Possebon (Sao Paulo, ada haikutajwa), Tom Cleverley (Wigan, mkopo).

NEWCASTLE
WAPYA: Cheik Tiote (Twente, ada haikutajwa), Dan Gosling (Newcastle, huru), James Perch (Nottingham Forest, ada haikutajwa), Sol Campbell (Arsenal, huru), Hatem Ben Arfa (Marseille, mkopo).
WALIOUZWA: Nicky Butt (ameruhusiwa), Fabrice Pancrate (ameruhusiwa), Fraser Forster (Celtic, mkopo)

STOKE
WAPYA: Jon Walters (Ipswich, pauni mil 2.75), Carlo Nash (Everton, huru), Florent Cuvelier (Portsmouth, huru), Kenwyne Jones (Sunderland, pauni mil nane), Eidur Gudjohnsen (Monaco, mkopo), Jermaine Pennant (Real Zaragoza, mkopo), Marc Wilson (Portsmouth, ada haikutajwa).
WALIOUZWA: Andy Griffin (Reading, pauni 250), Steve Simonsen (Sheffield United,huru), Amdy Faye (ameruhusiwa), Diego Arismendi (Barnsley, mkopo), Ibrahima Sonko (Portsmouth, mkopo), Nathaniel Wedderburn (Northampton, huru), James Beattie (Rangers, pauni mil 1.5), Carl Dickinson (Portsmouth, mkopo), Dave Kitson (Portsmouth, mkopo), Liam Lawrence (Portsmouth, mkopo).

SUNDERLAND
WAPYA: Titus Bramble (Wigan, pauni mil moja), Cristian Riveros (Cruz Azul, huru), Simon Mignolet (Sint Truidense, pauni mil mbili) , Ahmed Al-Muhammadi (ENPPI, mkopo), Marcos Angeleri (Estudiantes, pauni mil mbili), Danny Welbeck (Manchester United, mkopo), John Mensah (Lyon, mkopo), Asamoah Gyan (Rennes pauni mil 13).
WALIOUZWA: Daryl Murphy (Celtic, pauni mil 1.5), Jamie Chandler (Darlington, huru) Roy O'Donovan (Coventry, ada haikutajwa), Lorik Cana (Galatasaray, pauni mil tano), Nyron Nosworthy (Sheffield United, mkopo), Kenwyne Jones (Stoke, pauni mil nane), Marton Fulop (Ipswich, ada haikutajwa), Matthew Kilgallon (Middlesbrough, mkopo), Martyn Waghorn (Leicester, pauni mil tatu).

TOTTENHAM
WAPYA: William Gallas (Arsenal, huru), Sandro (Internacional, pauni mil sita), Stipe Pletikosa (Spartak Moscow, mkopo).
WALIOUZWA: Jimmy Walker (ameruhusiwa), David Button (Plymouth, mkopo), Adel Taarabt (QPR, pauni mil moja), John Bostock (Hull, mkopo).

WEST BROMWICH
WAPYA: Pablo Ibanez (Atletico Madrid, huru), Gabriel Tamas (Auxerre, pauni 800), Steven Reid (Blackburn, huru), Boaz Myhill (Hull, pauni mil 1.5), Nicky Shorey (Aston Villa, ada haikutajwa), Peter Odemwingie (Locomotiv Moscow, pauni mil 2.5), Somen Tchoyi (Red Bull Salzburg, ada haikutajwa), Marc Antoine Fortune (Celtic, ada haikutajwa), Paul Scharner (Wigan, huru), Craig Dawson (Rochdale, ada haikutajwa)
WALIOUZWA: Andwele Slory (ameruhusiwa), Robert Koren (Hull, huru), Filipe Teixeira (ameruhusiwa), Jonathan Greening (Fulham, huru), Borja Valero (Villareal, mkopo).

WEST HAM
WAPYA: Thomas Hitzlsperger (Lazio, huru), Pablo Barrera (Pumas, pauni mil nne), Frederic Piquionne (Lyon, pauni mil moja), Tal Ben Haim (Portsmouth, mkopo), Winston Reid (Midtjylland. pauni mil nn), Victor Obinna (Inter Milan, mkopo)
WALIOUZWA: Alessandro Diamanti (Brescia, pauni mil 1.8), Guillermo Franco (ameruhusiwa), Ilan (ameruhusiwa), Josh Payne (ameruhusiwa), Fabio Daprela (Brescia, ada haikutajwa)

WIGAN
WAPYA: James McArthur (Hamilton, pauni mil moja), Mauro Boselli (Estudiantes, pauni mil sita), Ali Al Habsi (Bolton, mkopo), Antolin Alcaraz (Club Brugge, huru), Ronnie Stam (Twente, pauni mil tatu), Steven Caldwell (Burnley, hurue), Tom Cleverley (Manchester United, mkopo), Franco di Santo (Chelsea, ada haikutajwa)
WALIOUZWA: Titus Bramble (Sunderland, pauni mil moja), Tomasz Cywka (Derby, huru), Mario Melchiot (Umm Salal, huru), Paul Scharner (ameruhusiwa), Jason Koumas (Cardiff, mkopo), Jason Scotland (Swansea, pauni 750,000)

WOLVES
WAPYA: Michael Mancienne (Chelsea, mkopo), Jelle Van Damme (Anderlecht, pauni mil 2.5), Steven Fletcher (Burnley pauni mil 6.5), Stephen Mouyokolo (Hull, pauni mil 2.5), Stephen Hunt (Hull, pauni mil tatu), Adlene Guedioura (Charleroi, pauni mil mbili), Geoffrey Mujangi Bia (Charleroi, mkopo), Marcus Bent (Birmingham, mkopo).
WAPYA: Jason Shackell (Barnsley, ada haikutajwa), Mark Little (ameruhusiwa), Daniel Jones (ameruhusiwa), George Friend (ameruhusiwa), Chris Iwelumo (Burnley, ada haikutajwa), Alan Irvine (Sheffield Wednesday, huru), Andrew Surman (Norwich, pauni 500), Sam Vokes (Bristol City, mkopo), Carl Ikeme (Leicester, mkopo), Matt Murray (amestaafu)
000000

MR. NICE: Maadui zangu ndio walionifikisha nilipo


Akanusha madai kuwa amefilisika na kufulia
Albamu yake mpya ya ‘Wakinuna’ ipo sokoni

MSANII machachari wa muziki wa kizazi kipya nchini, Lucas Nkenda, maarufu kwa jina la Mr. Nice amesema maadui zake ndio waliofikisha alipo sasa kimuziki.
Akihojiwa katika kipindi cha Mamboyoyo kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha ITV mwishoni mwa wiki iliyopita, Mr. Nice alisema amefanikiwa kupanda tena chati kimuziki kutokana na kuwa maadui wengi.
Mr. Nice alisema bila kuwa na maadui, si rahisi kwa msanii ama mtu mwingine yeyote kupata mafanikio katika maisha yake kwa sababu ni wao ndio wanaompa nguvu ya kufanya ayafanyayo.
“Kuna rafiki yangu mmoja wa karibu sana aliwahi kuniambia, ‘siku zote anayefanya mazuri huandamwa na mambo mengi katika maisha yake’. Nami sasa nimeamini, usipokuwa na maadui wengi huwezi kufanikiwa. Maadui zangu ndio walionifikisha hapa nilipo,”alisema msanii huyo.
Msanii huyo, ambaye amekumbwa na misukosuko mingi kimaisha, alisema ameifanyia mambo mengi makubwa Tanzania, ikiwa ni pamoja na kuitangaza kimataifa.
Alisema katika maisha yake kimuziki, ameshafanya maonyesho zaidi ya 28 katika sehemu mbalimbali duniani, ikiwa ni pamoja na kubuni aina yake ya muziki, ambayo imeigwa na wanamuziki wengi, ndani na nje ya Tanzania.
Mr. Nice alisema japokuwa kwa sasa amesahaulika kimuziki huku baadhi ya watu wakidai kuwa, amefilisika kimuziki, ipo siku ukweli utabainika na itajulikana umuhimu wake kimuziki.
Katika kudhihirisha hilo, Mr. Nice alisema kwa sasa anajiandaa kupakua albamu yake mpya, itakayojulikana kwa jina la ‘Wakinuna’. Alisema albamu hiyo itakuwa na vibao vinane alivyovipiga katika miondoko tofauti.
“Albamu yangu mpya itakuja na vitu tofauti, itadhihirisha kwamba ukimya wangu haukuwa wa bure,” alisema msanii huyo.
Mr Nice alisema amerekodi nyimbo zilizomo kwenye albamu hiyo kupitia kampuni yake binafsi, inayojulikana kwa jina la Bushclick na pia kufanyakazi ya kuisambaza yeye mwenyewe ili kupambana na tatizo la wizi wa kazi za wasanii.
“Nimeamua kuyafanya yote hayo ili hata kama itakuwa haina ubora, lawama zote zije kwangu,”alisema.
Msanii huyo mwenye makeke awapo stejini alisema vibao vyake vingi vilivyomo kwenye albamu yake mpya, vinaweza kuonekana kama vile vinazungumzia masuala ya mapenzi, lakini ndani yake kuna ujumbe mzito.
“Kuna vijembe vya hatari, kuna mambo ya mapenzi, siasa, chuki na bila kuwasahau watoto wadogo, ambao ndio kanisa langu na mhimili wangu mkubwa,”alisema.
Msanii huyo aliyejizolea umaarufu mkubwa katika nchi za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati alisema anawashukuru watu mbalimbali waliompa moyo baada ya kuonekana amefilisika kimuziki.Alisema watu hao ndio waliomwezesha kujipanga upya ili aweze kutoka kivingine.
Amekanusha katakata madai kuwa amefilisika kimuziki na kuongeza kuwa, ukimya wake ni ishara kwamba alikuwa akijipanga upya ili kutoka na staili nyingine tofauti.
“Huwezi kusema kuwa nimefulia kimuziki ama kifedha wakati aina ya muziki wangu hakuna mtu anayeweza kuiga wala kuifanya. Bado niko mwenyewe na matoleo niliyoyatoa bado yanafanya vizuri sokoni,”alisema.
“Kama kukaa kimya bila kutoa albamu mpya au kupanda jukwaani ama kutoonyesha uwezo wako kifedha ndiyo maana ya kufulia, basi mimi sijafulia tena niko juu zaidi,” aliongeza.
“Kuna watu waliofulia tunawafahamu na hatuwezi kuwasema. Walianza muziki kwa mbwembwe na baadaye wakakwama ghafla na hii ilitokana na kubebwabebwa tu na baadhi ya watu kwa sababu ya faida za wachache, lakini sio kweli kwamba wana uwezo mkubwa kisanaa.
“Baada ya kutoa singo zao ama albamu zao za kuungaunga, wakajiona masikio yanazidi kichwa na walipoachwa ili waonyeshe uwezo wao wenyewe, wakashindwa. Hao ndiyo waliofulia, sio mimi bwana mi niko juu sana,”alisema msanii huyo.
“Mimi muziki kwangu ni kazi na ndiyo ajira yangu hivyo ni lazima niwe na malengo makubwa ili ninufaike katika maisha yangu yote kwa sababu nimebaini kuwa ni kazi pekee inayonifaa na kunipa mafanikio makubwa ndani na nje ya nchi,” aliongeza.
Mr. Nice alijizolea umaarufu mkubwa alipoibuka na vibao vyake vilivyotamba kama vile ‘Kidali po’, ‘Kila mtu na demu wake’, ‘Kikulacho’, ‘Fagilia’, ‘Mbona umeniacha’, ‘Rafiki’ na ‘First Lady’.

K-Sher apigwa stop Tip Top Connection


MSANII pekee wa kike katika kundi la muziki wa kizazi kipya la Tip Top Connection, Khadija Shaaban amesimamishwa kufanya maonyesho ndani ya kundi hilo kwa muda usiojulikana.
Khadija, maarufu kwa jina la K-Sher, amesimamishwa ndani ya kundi hilo kwa tuhuma za makosa ya utovu wa nidhamu.
Meneja wa kundi hilo lenye maskani yake Manzese, Dar es Salaam, Khamis Tale alithibitisha wiki hii kuhusu kusimamishwa kwa msanii huyo.
Tale alisema wamefikia uamuzi huo baada ya msanii huyo kuonyesha vitendo vya utovu wa nidhamu kwa muda mrefu na kukataa kubadilika kila alipoonywa na viongozi.
“Mara nyingi K-Sher amekuwa akifanya vitu, ambavyo vinaleta usumbufu kwa wenzake,”alisema Tale.
“Kwa mfano, hivi karibuni tulikuwa na onyesho Mwanza, lakini yeye alishindwa kufika kwa sababu tulishindwa kupata tiketi ya ndege ya kumsafirisha kwa muda huo, wenzake walikuja kwa basi na kufanya onyesho kisha wakarudi Dar,”aliongeza.
“Tulipofika Dar, akawa anadai alipwe pesa za onyesho hilo huku akitishia kujitoa kundini iwapo hatalipwa. Yapo mambo mengine mengi, ambayo msanii huyo amekuwa akiyafanya na kusababisha usumbufu kwa wenzake, kitu ambacho kimetusukuma sisi viongozi kuchukua uamuzi wa kumsimamisha mpaka hapo baadaye,” alisema Tale.

NSAJIGWA: Tutawafunga Waalgeria kwao


SWALI: Ukiwa nahodha wa Taifa Stars, mnakwenda kucheza na Algeria, ukiwa ni mchezo wa kwanza wa michuano hiyo chini ya kocha mpya, Jan Poulsen. Nini matarajio yenu katika mechi hiyo?
JIBU: Ni kweli kuna mabadiliko kidogo katika timu yetu, lakini makocha wote wawili ni wazuri, wamekuwa wakitufundisha mbinu za hali ya juu na kila mchezaji ana hamu kubwa ya kutaka kuifunga Algeria kwao ili tujiweke kwenye nafasi nzuri ya kusonga mbele.
Kocha Poulsen ameonyesha uwezo mkubwa wa kufundisha soka kama ilivyokuwa kwa Marcio Maximo, ambaye kwa kweli tunamshukuru kwa kazi kubwa aliyofanya, licha ya kuwepo kwa kasoro ndogo, ambazo ni za kawaida kwa binadamu yoyote.Kwa kifupi ni kwamba kikosi chetu kimejiandaa vyema kwa pambano hilo.
SWALI: Tumeona mara baada ya Poulsen kuanza kuifundisha Taifa Stars, aliwaita wachezaji, Athumani Iddi na Juma Kaseja, ambao Maximo aliwatema kwenye kikosi chake. Una maoni gani kuhusu kitendo hicho cha Poulsen?
JIBU: Kwa kawaida, kila kocha ana mawazo na mtazamo wake. Ninachoweza kusema ni kwamba huo ni uamuzi wake, ambao amejipangia kwa lengo la kutimiza majukumu yake. Isipokuwa napenda kusema kuwa hayo ni mambo mazuri, ambayo yamelenga kuiletea mafanikio mazuri timu yetu.
SWALI: Hivi ni kweli mmejidhatiti vyema kuishinda Algeria kwao ama ni maneno ya kujipa moyo tu? Mliwaona walivyocheza kwenye fainali za Kombe la Dunia zilizofanyika mwaka huu Afrika Kusini?
JIBU:Tumeona na kujifunza mengi kuhusu Algeria. Ni timu nzuri na ngumu, lakini na sisi tumejipanga vizuri kukabiliana nao nyumbani kwao. Tumefanya mazoezi ya nguvu kuhakikisha kwamba tunakwenda kushinda.
Pia tumejifunza mbinu zao zote za kimchezo, ndani na nje ya uwanja. Tumeshaujua mfumo wanaoutumia wanapocheza nyumbani kwao na hata ugenini. Hatuoni sababu, ambazo zitatufanya tufungwe katika mchezo huo kama tutayafuata vyema maelekezo ya kocha wetu. Hata hivyo, tutalazimika kucheza kwa tahadhari kubwa.
SWALI: Kipi hasa kinachowapa moyo na nguvu ya kujigamba kwamba mnao uwezo wa kuifunga Algeria nyumbani kwao?
JIBU: Siku zote mchezo wa mpira wa miguu ni maandalizi. Tunazo sababu tatu za msingi za kuishinda Algeria kwao. Ya kwanza tunakwenda kushindana baada ya kufanya maandalizi ya kutosha, pili kikosi chetu kimekamilika katika kila idara na ya tatu wachezaji wote tumekuwa tukipatiwa huduma zote muhimu, kwa maana hiyo hatuna kisingizio tukifungwa.
SWALI: Una maoni gani kuhusu wadhamini wa Taifa Stars, ambao wamekuwa wakijitolea kuisaidia timu yenu kwa kuipeleka nje ya nchi kufanya mazoezi kabla ya kushiriki michuano mikubwa?
JIBU: Hilo ni jambo muhimu katika soka. Kwa upande wetu sisi wachezaji, hatuna cha kusema zaidi ya kucheza soka ya ushindani ili kuwaongezea nguvu ya kutudhamini zaidi. Lakini ukweli ni kwamba, mnapokwenda kufanya mazoezi nje ya nchi, mnajenga uwezo wa kujiamini zaidi na pia kuwa tayari kukabiliana na lolote.
Tunawashukuru sana wadhamini wetu, Kampuni ya Bia ya Serengeti na Benki ya NMB na wadhamini wengine, ambao wamekuwa wakijitolea kutusaidia kwa hali na mali. Pia hatutakuwa na shukurani iwapo hatutamtaja Rais Jakaya Kikwete, ambaye kwa kiasi kikubwa ameleta changamoto ya aina yake katika mchezo wa soka.
Vilevile kwa niaba ya wachezaji wenzangu, tunapenda sana kumshukuru Rais mstaafu Benjamin Mkapa kwa kufanikisha ujenzi wa uwanja mpya wa soka, ambao umeiwezesha Taifa Stars kupata nafasi ya kucheza na timu kubwa duniani kama vile Brazil, Cameroon, Ivory Coast na zinginezo na kukutana na baadhi ya wachezaji nyota duniani, ambao hatukuwa na mawazo iwapo siku moja tutacheza nao ana kwa ana.
SWALI: Ndani ya kikosi chenu kuna baadhi ya wachezaji, ambao wanacheza nje ya nchi na wengine wanacheza hapa nyumbani. Kuna tofauti yoyote kati yenu, ambayo umeshaiona hadi sasa?
JIBU: Tofauti ipo, tena kubwa tu, lakini bado kuna wachezaji wengi wazuri hapa nyumbani, lakini hawajapata bahati ya kupata timu nje. Kinachotakiwa kufanyika ni wachezaji hawa kuongeza bidii katika mazoezi ili uwezo wao uweze kuongezeka.
Yapo mafanikio mengi kisoka na kimaisha yaliyopatikana kwa wanasoka wa Tanzania waliopo nje ya nchi. Na hii ni changamoto kubwa kwetu sisi tuliopo hapa nyumbani kuongeza juhudi ili tuweze kupata nafasi hiyo.
SWALI: Tumeona kuna matatizo kwa baadhi ya wachezaji, ambao wanakwenda kufanya majaribio ya kucheza mpira wa kulipwa nje ya nchi, ambapo huwalalamikia mawakala kwa kutokuwa wakweli. Una maoni gani kuhusu jambo hilo?
JIBU: Sina hakika sana kuhusu malalamiko, ambayo yamekuwa yakitolewa na wachezaji kwa mawakala hao. Lakini kama kuna mawakala au viongozi wanaotaka kufanya ujanja wa kuwanyima haki wanazostahili wachezaji, hili jambo si sahihi na linapaswa kupigwa vita kwa sababu kila mtu anafanyakazi ili apate kula.
SWALI: Una maoni gani kuhusu utaratibu mzuri wa kuwapata wachezaji wa Taifa Stars, ili timu hiyo iweze kutisha zaidi katika mashindano ya kimataifa?
JIBU: Mimi binafsi nafikiri kuna umuhimu zaidi wa kumpa nafasi Kocha Paoulsen aweze kupanga mikakati yake ya kutafuta wachezaji ili aweze kuwa na kikosi imara na kitakacholeta heshima kwa nchi kimataifa.
SWALI: Una ushauri gani kwa viongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuhusu kuziimarisha timu za Taifa Stars, Ngorongoro Heroes, Serengeti Boys na Twiga Stars?
JIBU: Wanapaswa kuzitafutia wadhamini timu zote nne, yaani kila moja iwe na mdhamini wake. Hii itasaidia kuongeza hamasa zaidi kwa wachezaji, kuliko ilivyo hivi sasa, ambapo udhamini mkubwa upo kwa Taifa Stars na kuziacha timu zingine zikisuasua katika ufadhili.
Hali hii imesababisha TFF iwe na wakati mgumu katika kuziandaa timu zingine tatu zinaposhiriki michuano ya kimataifa. Nawaomba wafanyabiashara na kampuni mbalimbali zijitokeze kuzidhamini timu hizo tatu ili nazo ziweze kufika mbali na kupata mafanikio makubwa zaidi kisoka.

Manchester Band yatimua wanne, yaajiri wapya watano

BENDI ya muziki wa dansi ya Manchester imewatimua wanamuziki wake wanne wa zamani na kuajiri wengine wapya wanne kutoka bendi mbalimbali.
Mkurugenzi wa bendi hiyo, Jerome Mponda alisema mjini Dar es Salaam juzi kuwa, wameamua kuajiri wanamuziki wapya kwa lengo la kujiimarisha zaidi.
Aliwataja wanamuziki waliotimuliwa kuwa ni pamoja na mwimbaji, Amina Renny, wapiga magita Peter Kanuti na Juma Yegela na mpiga drums, Riziki Salehe ‘Chocholi’.
Jerome alisema wamefikia uamuzi wa kuwatimua wanamuziki hao wanne kwa makosa mbalimbali ya utovu wa nidhamu, ikiwa ni pamoja na ulevi wa kupindukia na kuchelewa mazoezini.
Kwa mujibu wa Jerome, wanamuziki wapya walioajiriwa na bendi hiyo hivi karibuni ni wacheza shoo Mariam Hussein kutoka Akudo, Monalisa Saidi, Judith Dalu na Merisa Joseph kutoka kundi la Nyamwela.
Katika orodha hiyo, pia yumo mwimbaji Hija Kimodo, ambaye amerejea tena kwenye bendi hiyo baada ya kurejea kutoka kwao Songea, alikokwenda kushughulikia matatizo ya familia yake.
Jerome alisema wameamua kuajiri wacheza shoo wengi ili kuipa bendi hiyo mvuto zaidi kwa mashabiki na pia kuifanya iende na wakati.
“Kwa kawaida wacheza shoo wana mvuto wa aina yake bendi inapokuwa jukwaani ikitumbuiza, hivyo tumewaajiri hawa wanne kwa lengo la kuongeza mvuto stejini,”alisema.
Mkurugenzi huyo alisema kwa sasa bendi yake ipo kwenye mapumziko ya mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani na inatarajia kuanza maonyesho siku ya Idd el Fitr.
Alisema watalitumia onyesho la sikukuu ya Idi Mosi kutambulisha albamu yao mpya inayojulikana kwa jina la ‘Kijuba wa mtaa’, yenye nyimbo sita.

Sikinde kula Idd el Fitri mikoani

BAADA ya mapumziko ya mwezi mtukufu wa Ramadhani, bendi ya muziki wa dansi ya Mlimani Park Orchestra ‘Sikinde’ imepanga kula sikukuu ya Idd el Fitr katika mikoa ya Mara, Geita na Kagera.
Msemaji wa bendi hiyo, Emmanuel Ndege alisema mjini Dar es Salaam juzi kuwa, wamealikwa kufanya maonyesho katika miji hiyo na Kampuni ya JOFAT Entertainment ya Mara.
Ndege alisema bendi hiyo itafanya onyesho lake la kwanza siku ya Idd Mosi kwenye ukumbi wa Bwalo la Magereza mjini Musoma na kufanya onyesho la pili siku ya Idd Pili kwenye ukumbi wa Ambassador Pub wa mjini Geita.
Alisema onyesho la tatu litafanyika Idd Tatu kwenye ukumbi wa New Kahama uliopo mjini Kahama kabla ya kuhamishia mashambulizi yao mjini Biharamulo Septemba 16 mwaka huu.
Ndege alisema maonyesho mengine yatafanyika Septemba 17 mwaka huu kwenye ukumbi wa California mjini Muleba kabla ya kuhitimisha ziara yao Septemba 18 kwa kufanya onyesho kwenye ukumbi wa Lines mjini Bukoba.
Msemaji huyo amewashukuru Mkurugenzi wa JOFAT, Fatuma Mavazi na meneja wake, Joseph Mbwiliza kwa kufanikisha ziara hiyo, ambayo alisema wanatarajia itakuwa ya aina yake.
Alisema wamepanga kuitumia ziara hiyo kuwaonyesha mashabiki wa miji hiyo makali ya bendi yao kimuziki na pia kutambulisha nyimbo zao kadhaa mpya.
Amewataka mashabiki wa miji hiyo kukaa mkao wa kula kwa vile watapata burudani safi na murua, ambayo huenda hawajaipata katika kipindi kirefu cha maisha yao.
Amewaomba radhi mashabiki wao wa mjini Dar es Salaam kwa kutokuwa nao wakati wa sikukuu hiyo na kuwataka wajiandae kupata burudani kabambe baada ya bendi hiyo kurejea maskani yake DDC Kariakoo.
WAREMBO watakaoshiriki katika shindano la Vodacom Miss Tanzania 2010,wakipata maelezo ya namna ya utengenezaji wa bia zinazozalishwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kutoka kwaofisa wa kampuni hiyo upande wa upishi,Tumaini Moses walipotembelea makao makuu ya kampuni hiyo jana mjini Dar es Salaam.


Wednesday, September 1, 2010

Robinho atua AC Milan, Asamoah atinga Sunderland


LONDON, England
KLABU kadhaa za ligi kuu za Ulaya juzi zilikamilisha usajili wa wachezaji wake wapya kwa ajili ya msimu wa ligi wa 2010-2011.
Katika usajili huo, klabu ya AC Milan ya Italia ilifanikiwa kumnyakua mshambuliaji wa kimataifa wa Brazil, Robinho de Souza kutoka klabu ya Manchester City ya England.
Kabla ya kusajiliwa na AC Milan, Robinho aliichezea kwa mkopo klabu yake ya zamani ya Santos ya Brazil.
Wachezaji kadhaa nyota waliong’ara katika fainali za mwaka huu za Kombe la Dunia zilizofanyika nchini Afrika Kusini nao walitumia nafasi hiyo kujiunga na klabu zingine, akiwemo mshambuliaji wa kimataifa wa Ghana, Asamoah Gyan aliyejiunga na Sunderland ya England akitokea Rennes ya Ufaransa.
Katika usajili huo, kiungo wa kimataifa wa Uholanzi, Rafael van der Vaart amejiunga na klabu ya Tottenham ya England akitokea Real Madrid ya Hispania wakati Klaas-Jan Huntelaar, Jose Manuel Jurado na beki Nicolas Plestan wamejiunga na Schalke ya Ujerumani.
Klabu za Barcelona, Real Madrid, Inter Milan, Manchester United na Chelsea hazikufanya usajili wowote wa kutisha katika dakika za mwisho baada ya kukamilisha usajili wa awali wiki kadhaa zilizopita.
Usajili wa wachezaji wa ligi kuu ya England msimu huu haukuwa mkubwa ikilinganishwa na msimu wa 2009. Pauni milioni 100 za Uingereza zinakadiriwa kutumika katika usajili wa msimu huu.
Klabu pekee iliyoripotiwa kutumia fedha nyingi kusajili wachezaji wapya msimu huu ni Manchester City. Klabu hiyo inayomilikiwa na mfanyabiashara Sheikh Mansour kutoka Arabuni, inakadiriwa kutumia zaidi ya pauni milioni 300 za Uingereza.
Miaka miwili iliyopita, Manchester City iliishtua dunia baada ya kumsajili dakika za mwisho mshambuliaji Robinho akitokea Real Madrid. Usajili wa mshambuliaji huyo uliigharimu Manchester City pauni milioni 32. ikiwa ni rekodi kwa klabu za England.
Hata hivyo, Robinho alishindwa kuonyesha cheche zake katika ligi hiyo, hatua iliyosababisha Manchester City imuuze kwa mkopo kwa klabu yake ya zamani ya Santos.
AC Milan imeripotiwa kutumia pauni milioni 15 kumsajili Robinho kwa mkataba wa miaka minne. Mbrazil huyo atalazimika kupigania namba kwenye kikosi cha kwanza cha timu hiyo chenye wachezaji wengine nyota kama vile Zlatan Ibrahimovic, Ronaldinho Gaucho na Alexander Pato.
Lengo la AC Milan kufanya usajili kabambe msimu huu ni kumaliza ukame wa miaka mitano wa kushindwa kushinda taji la ligi ya Serie A ya Italia. Taji hilo limekuwa likinyakuliwa mara kwa mara na mahasimu wao Inter Milan.
Kuwasili kwa Robinho kwenye klabu hiyo kulitoa nafasi kwa mshambuliaji, Huntelaar kuhamia Schalke ya Ujerumani kwa mkataba wa miaka mitatu.
“Lengo letu linapaswa kuwa ni kushinda kila taji,” alisema Robinho baada ya kumwaga wino AC Milan. “Wabrazil wote kwenye timu watanipa sapoti kwenye kikosi. Natarajia kuweka historia kwa klabu.”
Kocha Mkuu wa Schalke, Felix Magath, ambaye amewatema wachezaji kadhaa wakongwe, amemuongeza kwenye kikosi chake Plestan kutoka Lille ya Ufaransa kwa mkataba wa miaka mitatu na kiungo Jurado kutoka Atletico Madrid kwa mkataba wa miaka minne.
Birmingham ya England nayo ilifanya usajili wa wachezaji watatu kwa mipigo dakika za mwisho, akiwemo kiungo Alexander Hleb kutoka Barcelona, kiungo Jean Beausejour kutoka Club America ya Mexico na beki Martin Jiranek kutoka Spartak Moscow ya Russia.
Sunderland iliweka rekodi mpya ya usajili baada ya kumnyakua mshambuliaji Fraizer Campbell. Kabla ya usajili huyo Campbell alikuwa majeruhi kwa miezi sita.
Kadhalika, mmiliki wa klabu hiyo Ellis Short amelipa zaidi ya pauni milioni 13 kwa ajili ya kumsajili mshambuliaji Gyan, ambaye mabao yake yaliisaidia Ghana kutinga robo fainali kwa mara ya kwanza katika michuano ya Kombe la Dunia mwaka huu.
Mshambuliaji Eidur Gudjohnsen wa Monaco amerejea tena katika ligi kuu ya England, lakini safari hii amejiunga na klabu ya Stoke City kwa mkopo wa muda mrefu. Klabu hiyo pia imemsajili Jermaine Pennant kwa mkataba wa miezi sita akitokea Real Zaragoza ya Hispania.
Liverpool ndiyo klabu pekee kongwe ya England iliyofanya usajili dakika za mwisho baada ya kumnasa beki Paul Konchesky kutoka Fulham. Beki huyo ametia saini mkataba wa miaka minne.
Konchesky amesajiliwa ili kuziba pengo la beki chipukizi wa Argentina, Emiliano Insua, aliyeihama Liverpool na kujiunga na klabu ya Galatasaray ya Uturuki.
Joseph Yobo wa Everton ameihama klabu hiyo na kujiunga na Fenerbahce ya Uturuki wakati Armand Traore wa Arsenal ametua rasmi Juventus ya Italia.
Usajili uliosisimua katika ligi kuu ya Hispania ni wa mchezaji David Trezeguet, aliyejiunga na klabu mpya katika ligi hiyo, Hercules kwa mkataba wa miaka miwili. Trezeguet aliichezea Juventus ya Italia kwa misimu 10.
Nayo Valencia imefanikiwa kumsajili kwa mkopo mshambuliaji Marius Stankevicius kutoka Sampdoria ya Italia ilu kuziba pengo la mabeki Carlos Marchena na Alexis Ruano, waliouzwa kwa Sevilla wiki iliyopita.
Klabu ya Bordeaux ya Ufaransa nayo imemsajili kiungo Abdou Traore kutoka Nice, akiwa ni mchezaji wa pili baada ya kusajiliwa kwa mshambuliaji wa kimataifa wa Serbia, Danijel Ljuboja kutoka Grenoble.

POULSEN: Kuzifunga Algeria na Morocco ni kazi ngumu

Asema anahitaji muda zaidi kujua uwezo wa wachezaji wake

KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya Taifa, Taifa Stars, Jan Pulsen amesema itakuwa vigumu kwa timu yake kufuzu kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika za mwaka 2012.
Akizungumza na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) wiki hii, Poulsen (64) alisema hafikirii iwapo timu yake itakuwa na uwezo wa kuzishinda Algeria na Morocco katika michuano hiyo.
Kocha huyo kutoka Denmark alikuwa akizungumzia maandalizi yake katika michuano hiyo, inayotarajiwa kutimua vumbi kwenye viwanja mbalimbali vya Afrika mwishoni mwa wiki hii.
Taifa Stars inatarajiwa kutupa karata yake ya kwanza kesho kwa kumenyana na Algeria mjini Algiers. Timu zingine zilizopangwa kundi moja na Taifa Stars ni Morocco na Jamhuri ya Afrika ya Kati.
“Soka si kama kiwanda, ambako utakwenda na kuwasha mashine kisha unaanza kazi,”alisema kocha huyo, ambaye chini yake, Taifa Stars imecheza mechi moja na kulazimishwa kutoka sare ya bao 1-1 na Kenya.
“Unafanyakazi na watu na inachukua muda, inachukua miezi, inawezekana hata mwaka mmoja na nusu,”aliongeza.
Poulsen alisema anaamini itakuwa vigumu kwa Taifa Stars kufuzu kucheza fainali hizo, zitakazoandaliwa kwa pamoja na Gabon na Equatorial Guinea mwaka huo.
“Unadhani tunaweza kuzifunga timu kama Morocco? Unaelewa wazi kwamba hiyo itakuwa kazi ngumu na unaelewa kabla hujauliza swali,”alisema kocha huyo.
Kwa mara ya mwisho, Taifa Stars ilifuzu kucheza fainali hizo mwaka 1980 zilipofanyika nchini Nigeria. Tangu wakati huo, timu hiyo imekuwa ikishiriki katika michuano hiyo na kutolewa hatua za awali.
Poulsen aliteuliwa kuwa kocha mpya wa Taifa Stars mapema mwaka huu, akichukua nafasi ya kocha wa zamani, Marcio Maximo.
Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), lilikataa kumuongezea mkataba Maximo baada ya kushindwa kuiwezesha timu hiyo kufuzu kucheza fainali za mwaka 2008 na 2010.
Hata hivyo, Poulsen alisisitiza kuwa, bado anahitaji muda zaidi kuwaelewa vyema wachezaji wake.
Alisema timu aliyonayo sasa, ameiteua kwa msaada mkubwa wa makocha wazalendo, hivyo anahitaji muda zaidi kutambua uwezo wao.