KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, December 8, 2013

TFF YATANGAZA NAFASI ZA KAYUNI NA KAWEMBA, IDARA ZAFANYIWA MAREKEBISHO


SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limetangaza nafasi saba za kazi, ikiwemo ya katibu mkuu na mkurugenzi wa ufundi.
Nafasi zingine zilizotangazwa na TFF ni ya mkurugenzi wa fedha na utawala, mkurugenzi wa sheria na uanachama, mkurugenzi wa mashindano, meneja wa biashara na ofisa habari na mawasiliano.
TFF imetangaza nafasi hizo za kazi, kupitia kwenye vyombo mbalimbali vya habari na kuwataka watu wenye sifa zinazotakiwa, kuwasilisha maombi yao kabla ya Desemba 15 mwaka huu.
Uamuzi wa TFF kutangaza nafasi hizo, umekuja siku chache baada ya shirikisho hilo kupata uongozi mpya, katika uchaguzi uliofanyika Novemba mwaka huu.
Katika uchaguzi huo, Jamal Malinzi alichaguliwa kuwa rais na Wallace Karia alichaguliwa kuwa makamu mwenyekiti.
Siku chache baada ya uchaguzi huo, kamati ya utendaji ya TFF iliamua kumpa likizo yenye malipo, aliyekuwa katibu mkuu wa shirikisho hilo, Angetile Osiah. Mkataba wa Angetile ilikuwa umalizike mwishoni mwa mwezi huu.
Kwa sasa, nafasi ya katibu mkuu inashikiliwa kwa muda na Ofisa Habari wa shirikisho hilo, Boniface Wambura.
Habari kutoka ndani ya TFF zimeeleza kuwa, uongozi mpya umeamua kuzifanyia marekebisho baadhi ya idara kwa lengo la kuongeza ufanisi, ambapo idara ya fedha imeunganishwa na utawala wakati idara ya utawala imeunganishwa na sheria.
Awali, idara ya fedha ilikuwa chini ya Yonaza Seleki na idara ya utawala ilikuwa chini ya Mtemi Ramadhani.
Kwa mujibu wa habari hizo, TFF pia imeamua kuunda idara mpya ya biashara, ambayo zamani ilikuwa ikijulikana kama idara ya masoko.
Nafasi ya mkurugenzi wa ufundi kwa sasa inashikiliwa na Sunday Kayuni wakati  mkurugenzi wa mashindano ni Saad Kawemba.

No comments:

Post a Comment