KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, December 8, 2013

SIMBA NIPENI HAKI YANGU-KIBADENI


KOCHA Mkuu wa zamani wa Simba, Abdalla Kibadeni ameutaka uongozi wa klabu hiyo kumlipa fedha anazodai mara moja.
Kibadeni amesema, anaukubali uamuzi wa kamati ya utendaji ya Simba, kumsimamisha kazi yeye na msaidizi wake, Jamhuri Kihwelo 'Julio', lakini anaomba alipwe pesa zake.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Kibadeni alisema amepokea barua kutoka uongozi wa Simba kuhusu kusimamishwa kwake kwa madai kwamba, mwenendo wa timu katika mzunguko wa kwanza wa ligi kuu haukuwa mzuri.
"Wanasema uwezo wangu wa kufundisha ni mdogo. Mi sitaki kubishana nao kwenye hilo, isipokuwa watu wenye kujua ndio wanaweza kusema kama hilo ni tatizo.
Narudia kusema, nakubali kuachia ngazi ila nitashukuru wakinipatia haki yangu, ambayo nastahili kupata," alisema kocha huyo, ambaye ameingia mkataba wa kuifundisha Ashanti.
Kibadeni aliamua kuweka mambo hadharani kwa kusema, amekumbana na matatizo mengi wakati akiifundisha Simba, ikiwa ni pamoja na baadhi ya watu walioko nje ya uongozi, kutaka nafasi ya kuingia ndani ya timu.
"Kuna migogoro sana, hata mimi nimechoka hii kazi. Kubwa ilikuwa tuhakikishe kwamba timu inafanya vizuri ili badaye tuje kutafuta ubingwa. Nilikuwa na imani kwamba hata mwaka huu tungeweza kupata ubingwa kwa jinsi timu ilivyokua inakwenda," alisema Kibadeni.
"Tumecheza michezo 13 ya mzunguko wa kwanza, tumeshinda sita, tumetoka sare sita na kupoteza mchezo mmoja. Nafasi tuliyoipata ni ya nne katika michezo 13.
Katika hizo mechi 13, mimi nasema nafasi ya nne sio mahali pabaya kwa sababu timu ilicheza mechi 26 za ligi mwaka jana, ikamaliza nafasi ya nne," aliongeza kocha huyo.
Kamati ya Utendaji ya Simba, iliamua kuwasimamisha kazi Kibadeni na Julio mwishoni mwa mwezi uliopita kwa madai ya kutoridhishwa na ufundishaji wao.
Mbali na makocha hao, kamati hiyo pia ilitangaza kumsimamisha Mwenyekiti, Ismail Aden Rage kwa madai ya kutokuwa na imani na uongozi wake.
Hata hivyo, Rage alipinga uamuzi huo na kudai kuwa, kikao kilichopitisha uamuzi huo, kilikuwa batili kwa vile kikatiba, mwenyekiti ndiye mwenye mamlaka ya kukiitisha. Aliitaja sababu nyingine kuwa ni kamati hiyo kushindwa kumpa nafasi ya kujieleza kuhusu tuhuma dhidi yake.
Kufuatia kuzuka kwa mgogoro huo, kamati ya utendaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), ilimtaka Rage aitishe mkutano mkuu wa dharula wa wanachama ili kujadili suala hilo na kulipatia ufumbuzi. Rage amegoma kuitisha mkutano huo na kwa sasa yuko nje ya nchi.

No comments:

Post a Comment