KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, May 30, 2017

TAIFA STARS KUWEKA KAMBI MISRI, MKUDE ABAKI


Kikosi cha wachezaji 20 wa timu ya mpira wa miguu ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kinachodhaminiwa na Kampuni ya Bia ya Serengeti, kinatarajiwa kuondoka kesho Jumanne saa 10.45 jioni kwenda Misri.
 

Taifa Stars ambayo itakuwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa kesho saa 7. 45 mchana inakwenda Misri kufanya kambi ya siku nane kujindaa na mchezo dhidi ya Lesotho utakaofanyika Juni 10, 2017 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
 

Wachezaji hao 20 kutoka hapa Tanzania wataungana na na wengine watatu, Nahodha Mbwana Samatta, Thomas Ulimwengu na Faridi Mussa wanaocheza ughaibuni katika kikosi hicho na kufanya jumla ya wachezaji kuwa 23 nchini Misri.
 

Nahodha Msaidizi, Jonas Mkude hatakuwako kwenye msafara huo kutokana na ushauri wa madaktari walioelekeza kwamba nyota huyo wa Simba apate mapumziko ya angalau siku nne.
 

Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Salum Mayanga ameridhia na kusema kuwa Mkude ataungana na wenzake Juni 8, mwaka huu timu itakaporejea kutoka Misri. Mayanga hajajaza nafasi ya Mkude.
 

Mchezo dhidi ya Lesotho ni muhimu kwa Tanzania ikiwa ni mechi ya kwanza kwa Taifa Stars katika Kundi ‘L’ kuwania nafasi muhimu ya kucheza fainali za Kombe la Mataiafa ya Afrika (AFCON) za mwaka 2019 zitakazofanyika NCHINI Cameroon.
 

Mbali ya Lesotho na Tanzania, mataifa mengine katika Kundi ‘L’ ni Uganda na Cape Verde ambao pia wikiendi ya Juni 9, 10 na 11, mwaka huu watakuwa katika mchezo wa kwanza pia kuwania nafasi hiyo.
 

Kikosi cha Taifa Stars kinachofundishwa na Kocha Salum Mayanga kinaundwa na makipa Aishi Manula  (Azam FC), Benno Kakolanya  (Yanga SC) na Said Mohammed (Mtibwa Sugar).

Walinzi wa pembeni upande wa kulia ni Shomari Kapombe    (Azam FC) na Hassan Kessy (Yanga SC) wakati upande wa kushoto wapo Mohammed Hussein (Simba) na Haji Mwinyi  (Yanga SC).

Walinzi wa kati Erasto Nyoni  (Azam FC), Salim Mbonde (Mtibwa Sugar), Abdi Banda (Simba SC) na Agrey Morris  (Azam FC) ilihali viungo wa kuzuia ni Himid Mao (Azam FC) na Jonas Mkude kutoka Simba SC ambaye hatasafiri na timu kwa sasa.

Viungo wa kushambulia Salum Abubakar (Azam FC), Said Ndemla  (Simba SC) na Mzamiru Yassin (Simba) wakati viungo wa pembeni ni Simon Msuva (Yanga SC), Shizza Kichuya (Simba SC) na Farid Mussa (Teneriffe, Hispania).
 

Washambuliaji wapo Mbwana Samatta (KRC Genk- Ubelgiji), Thomas Ulimwengu (AFC Eskilstuna – Sweden), Ibrahim Ajib (Simba SC), Mbaraka Yusufu (Kagera Sugar) na Abdurahman Mussa (Ruvu Shooting).
 

Wasaidizi wa Mayanga katika benchi la ufundi ni Novatus Fulgence ambaye ni kocha msaidizi Patrick Mwangata - kocha wa makipa pia yumo Meneja wa timu, Danny Msangi; Mtunza Vifaa, Ally Ruvu, Daktari wa timu ni Richard Yomba na Daktari wa viungo ni Gilbert Kigadya.

Timu hiyo iliingia kambini Machi 23, 2017 kwenye Hoteli ya Urban Rose, Dar es Salaam kabla ya kesho kwenda Misri na baadaye itarejea Tanzania kucheza na Lesotho, Juni 10, mwaka.

MAREKEBISHO YA KANUNI ZA LIGI KUU YA VODACOM NA LIGI DARAJA LA KWANZA



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), linatangazia klabu zote zinazoshiriki Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu wa 2017/18 na zile za Ligi Daraja la Kwanza (FDL) msimu wa 2017/18 kwamba kipindi hiki ni cha kuwasilisha maoni na mapendekezo mbalimbali kuhusu marekebisho ya kanuni za ligi husika.

TFF inaagiza klabu zote - kwa nafasi walizonazo kama wanafamilia ya mpira wa miguu, kuwasilisha mapendekezo na maoni kuhusu marekebisho ya katiba kwa njia ya kuyatuma kupitia anwani za sanduku la Barua 1574, Dar es Salaam au barua pepe tplb.tplb@yahoo.com au yaletwe moja kwa moja ofisi za Bodi ya Ligi au TFF.

Maoni hayo tayafanyiwa kazi na Bodi ya Ligi kabla ya kupelekwa kwenye kikao cha Kamati ya Utendaji kabla ya kuanza msimu husika wa mashindano baada ya kupita msimu uliopita.

SIMBA YATWAA KOMBE LA FA


SIMBA imefanikiwa kutwaa Kombe la Shirikisho la Azam baada ya kuibwaga Mbao FC mabao 2-1 katika mechi ya fainali iliyochezwa kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.

Mshindi wa pambano hilo ilibidi apatikane katika muda wa nyongeza wa dakika 30, baada ya timu hizo kumaliza dakika 90 zikiwa suluhu.

Simba ilikuwa ya kwanza kupata bao katika muda huo wa nyongeza lililofungwa na Frederick Blagnon kabla ya Mbao FC kusawazisha kupitia kwa Robert Ndaki.

Zikiwa zimesalia dakika chache za muda wa nyongeza kumalizika, Simba ilipata bao la pili lililofungwa kwa njia ya penalti na Shiza Kichuya baada ya beki mmoja wa Mbao kuunawa mpira ndani ya eneo la hatari.

Thursday, May 25, 2017

MANULA,TSHABALALA,NIYONZIMA WACHEZAJI BORA LIGI KUU,MECKY MEXIME AMBWAGA OMOG TUZO YA KOCHA BORA


Mchezaji wa  Simba SC, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ amefanikiwa kushinda tuzo ya Mchezaji Bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara katika sherehe zilizofanyika usiku wa Jumatano ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam.
Tshabalala anayecheza upande wa kushoto, baada ya msimu mzuri akiiwezesha Simba kumaliza nafasi ya pili kwenye Ligi Kuu nyuma ya mahasimu, Yanga walioibuka mabingwa, amewabwaga
Aishi Manula wa Azam, Simon Msuva wa Yanga, Shiza Kichuya wa Simba na Haruna Niyonzima wa Yanga.
Lakini kiungo wa Rwanda, Niyonzima ‘akainua kwapa’ kwa kunyanyua tuzo ya Mchezaji Bora wa Kigeni, akiwashinda beki Mzimbabwe wa Simba, Method Mwanjali na beki Mrundi wa Mbao FC, Yusuph Ndikumana.
Manula naye akainua tuzo ya Kipa Bora akiwashinda Owen Chaina wa Mbeya City na Juma Kaseja wa Kagera Sugar, wakati Msuva amebeba tuzo ya Mfungaji Bora kwa pamoja na Abdulrahman Mussa wa Ruvu Shooting baada ya wote kufungana kwa mabao 14 kila mmoja.
 Mecky Mexime amewashinda makocha wa kigeni, Mcameroon wa Simba, Joseph Omog na Ettiene Ndayiragije wa Mbao FC.
Mshambuliaji chipukizi wa Kagera Sugar, Mbaraka Yussuf Abeid ameshinda tuzo ya Mchezaji Bora Chipukizi wa Ligi Kuu akiwaangusha Shaaban Iddi wa Azam FC na Mohammed Issa ‘Banka’ wa Mtibwa Sugar.
Shaaban Iddi naye akawaangusha mchezaji mwenzake wa Azam, Abdallah Masoud ‘Cabaye’ na
Mosses Kitambi wa Simba katika tuzo ya Mchezaji Bora wa U-20, inayojulikana kama tuzo ya Ismail Khalfan wakati Shiza Kichuya akashinda tuzo ya Bao Bora la Msimu alilofunga kwenye mechi dhidi ya Yanga katika ushindi wa 2-1 akiyazidi mabao ya Peter Mwalyanzi wa African Lyon na Zahoro Pazi wa Mbeya.
Refa Bora ni Elly Sasii wa Dar es Salaam aliyewashinda Shomari Lawi wa Kigoma na Hance Mabena wa Tanga, wakati Tuzo ya Heshima imekwenda kwa gwiji Kitwana Manara aliyeanza kucheza kama kipa na baadaye mshambuliaji kwa mafanikio makubwa timu ya taifa na klabu ya Yanga na Mwadui FC imeshinda tuzo ya timu yenye Nidhamu.

BOCCO AMWAGA WINO SIMBA MIAKA MIWILI



Mshambuliaji wa timu ya Azam FC ,John Bocco ni mali ya Simba.

Taarifa zinaeleza amesaini miaka miwili katika kikosi cha Simba.

Taarifa zinaeleza mkataba huo ni wa awali na inaonekana Bocco ameamua kutua Simba baada ya makubaliano yake na Azam baada ya mkataba wake kwisha, kuonekana unakwenda kombo.

Hata hivyo, Bocco amekuwa hapokei simu ili kulithibitisha hilo suala ingawa hivi karibuni alikanusha kila kilichoandikwa kwenye akaunti yake ya Instagram kuhusiana na kwamba ana mpango wa kuondoka Azam.

Alidai akaunti yake ilikuwa imetekwa lakini hali halisi ilionyesha kwamba hakuwa amezungumza lolote.

Afisa Habari wa Azam FC, Jaffar Iddi yeye alisema walikuwa katika mazungumzo na Bocco baada ya mkataba wake kufikia tamati.

SINGIDA UNITED YAMNASA KENNY ALLY WA MBEYA CITY



Matajiri wa Mkoa wa Singida ambao wamepanda Ligi Kuu Msimu huu wameanza kujiweka fiti katika usajili wa wachezaji wa ndani na mchezaji wa kwanza kusaini ni Kiungo Mkabaji wa Mbeya City, Kenny Ally MWambungu sasa ni mali ya Singida United.
Huu ni usajiri wa sita baada ya kuwasajili wachezaji watano wa kigeni na kwa mujibu wa katibu Mkuu wa klabu hiyo inataka kusajili jumla ya wachezaji 14.
Kenny Ally alikuwa kwenye vichwa vya habari katika timu kubwa zilizokuwa zinawaania saini ya mchezaji huyu wakiwemo wakongwe Simba na Yanga na nyingine kama vile Azam FC,Mwadui Fc.
Singida United ambayo ipo chini ya Kocha mwenye mafanikio Tanzania hata bara la Afrika na mwenye uzoefu wa Ligi Hans Van Der Pluijm ambaye alikuwa kocha wa Zamani wa Mabingwa wa Kihistoria Yanga ambapo aliwapa mataji mawili mfululizo hata huu ubingwa wa tatu unachangizwa na Juhudi zake kwani aliiongoza Msimu wa kwanza na msimu wa pili alimuachia George Lwandamina.

SIMBA NA YANGA KUWANIA MILIONI 60 ZA SPORTPESA SUPER CUP,VIGOGO WA KENYA NDANI


Kampuni ya SportPesa imeandaa mashindano maalum ya soka yatakayojulikana kama SportPesa Super Cup yatakayoshirikisha timu za Tanzania, Zanzibar na Kenya.
Mkurugenzi wa Utawala na Utekelezaji wa Kampuni ya SportPesa Tanzania, Tarimba Abbas amesema leo katika mkutano na Waandishi wa Habari kwamba, bingwa wa michuano hiyo atapata dola za Kimarekani 30,000 na nafasi ya kucheza dhidi ya timu ya England.
Amezitaja timu hizo kuwa Simba SC, Yanga SC na Singida United kwa Tanzania Bara, Jang’ombe Boys ya Zanzibar, Gor Mahia, AFC Leopards, Nakuru All Stars na Tusker FC za Kenya.
Tarimba amesema kwamba michuano hiyo itaanza Juni 5, mwaka huu hadi Juni 11 na itafanyika Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam.
“Tunatarajia mashindano haya yatakuwa changamoto nzuri kwa timu zote zitakazoshiriki na pia burudani nzuri kwa wapenzi wa mpira wa miguu nchini, hususan mashabiki wa timu zenyewe,”amesema Tarimba. 

RATIBA YA SPORTPESA SUPER CUP
Juni 5, 2017
Singida United Vs FC Leopard
Yanga SC Vs Tusker FC
Juni 6, 2017
Jang`ombe Boys vs Gor Mahia
Simba Vs Nakuru All Star
NUSU FAINALI
Juni 8, 2017
Group A:Singida United/AFC Leopards Vs Yanga SC/Tusker FC
Group B:Simba SC/Nakuru All Star Vs Jangombe Boys/Gor Mahia
FAINALI

MSUVA, MUSSA WAGAWANA KIATU CHA DHAHABU


Washambuliaji Abdulrahman Mussa wa Ruvu Shooting na Simon Msuva wa Yanga wameibuka wafungaji bora kwenye Ligi Kuu ya Vodacom msimu wa 2016/2017 iliyomalizika Mei 20 mwaka huu.


Kutokana na wachezaji hao kuibuka vinara kwa ufungaji ambapo kila mmoja amefunga mabao 14, watapata zawadi ya mfungaji bora ambayo ni sh. 5,800,000 kwa kila mmoja.
 

Yanga imemaliza Ligi hiyo ikiwa bingwa kwa ponti 68 na kufunga jumla ya mabao 57, wakati Ruvu Shooting iliyomaliza katika nafasi ya saba kwa ponti 36 imepachika jumla ya mabao 28.
 

Watakabidhiwa zawadi hiyo katika hafla ya tuzo za Mchezaji Bora wa Ligi Kuu ya Vodacom msimu wa 2016/2017 itakayofanyika keshokutwa (Mei 24 mwaka huu) kwenye ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.

MCHEZAJI BORA WA MWEZI MEI VPL NI MOHAMMED HUSSEIN


Mchezaji wa timu ya Simba SC, Mohamed Hussein amechaguliwa kuwa mchezaji bora wa Ligi Kuu ya Vodacom wa mwezi Mei kwa msimu wa 2016/2017.

Hussein aliwashinda wachezaji Haruna Niyonzima wa Yanga na Shabani Idd wa Azam FC.

Katika mwezi Mei kulikuwa na raundi tatu ambazo Hussein alicheza kwa dakika zote 270 na kutoa mchango mkubwa katika kuisadia timu yake kubaki katika nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom.

Pia alionesha nidhamu ya hali ya juu, hivyo kutopewa onyo la aina yoyote.

Kwa kushinda tuzo hiyo, Kaseja atazawadiwa kitita cha sh. 1,000,000 (milioni moja) kutoka kwa wadhamini wa Ligi hiyo, kampuni ya Vodacom Tanzania.

Wachezaji wengine walioshinda tuzo za mwezi za Ligi Kuu ya Vodacom msimu wa 2016/2017 ni John Bocco wa Azam (Agosti), Shiza Kichuya wa Simba (Septemba), Simon Msuva wa Yanga (Oktoba) na Riphat Said wa Ndanda (Novemba).

Wengine ni Method Mwanjali wa Simba (Desemba), Juma Kaseja wa Kagera Sugar (Januari), Hassan Kabunda wa Mwadui (Februari), Mbaraka Yusuf wa Kagera Sugar (Machi) na Abdulrahman Musa wa Ruvu Shooting (Aprili).

WACHEZAJI SERENGETI BOYS SASA WAHAMISHIWA KIKOSI CHA NGORONGORO HEROES




Rais wa TFF, Jamal Malinzi amesema kikosi cha timu ya taifa ya vijana wa chini ya umri wa miaka 17, Serengeto Biys, sasa watnaunda kikosi kipya cha taifa cha vijana wenye umri wa chini ya miaka 20, Ngorongoro Heroes.

Amesema kauli mbiu ya Ngorongoro Heroes, ni kanyaga twende mpaka kufuzu fainali za AFCON u 20 mwaka 2019, ambapo michezo ya kufuzu kwa hatua hiyo ya fainali za U-20 zitaanza Aprili, mwakani.

Alisema vijana hao wataingia kambini  Oktoba, mwaka huu na watacheza mechi ya kimataifa ya kujipima nguvu.

“Mpira huwa haulali, unachezwa saa 24 katika wiki duniani ambako huanzia Januari hadi Desemba, likimalizika shindano hili linakuja jingine. Maumivu ya kufungwa huwa ni mafupi, mashabiki siku zote huwa wanafkiria mechi ijayo. Tujiandae na Qulifiers za 2019 AFCON u-20, haziko mbali,” amesema.

Timu hiyo ya vijana ilikuwa jijini Libreville nchini Gabon kushiriki fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika ya vijana iliyofanyika katika miji miwili ya Libreville na Port Gentil ambako iliondolewa kwenye hatua ya makundi na Niger.

Serengeti Boys ilifungwa bao 1-0 na Niger katika mchezo uliofanyika Port Gentil, hivyo kufanya matokeo ya timu zote mbili yaani Niger na Tanzania kufanana kwa pointi, idadi ya mabao ya kufunga na kufungwa tangu kuanza kwa fainali hizi za AFCON, Mei 15, mwaka huu.

Serengeti Boys iliyokuwa Kundi B iliondolewa Kundi B iliondolewa na Niger iliyopenya kwenda hatua ya Nusu Fainali kwa faida ya kupata ushindi katika mchezo ambao umekutanisha timu hizo kwani Tanzania ilifungwa 1-0 katika mchezo wa mwisho hatua ya makundi. 

Kanuni hiyo ya mashindano ya CAF inajieleza kuwa matokeo ya ‘head to head’ kwa maana zinapokutana timu mbili zenye uwiano wa pointi na magoli matokeo huamualiwa kwa mshindi kupewa nafsi katika mchezo uliokutanisha timu hizo mbili.

Tuesday, May 23, 2017

SPORTPESA YAMWAGA MAMILIONI SINGIDA UNITED




Kampuni ya michezo ya kubashiri ya SportPesa imeendelea kuonesha dhamira yake katika kuhakikisha Ligi Kuu soka Tanzania bara msimu ujao 2017/2018 kunakuwa na ushindani wa kweli kutoka katika timu mbalimbli kutokana na jitihada zake za kudhamini vilabu kadhaa.

Baada ya kuingia mkataba wa udhamini na Simba na Yanga katika kipindi cha miaka mitano wenye thamani ya zaidi ya Tsh Bilioni 4, leo May 23 wametangaza kuingia mkataba wa mwaka mmoja wa udhamini na club ya Singida United ya Singida wenye thamani ya Tsh milioni 250.

SportPesa kuonesha kuwa wanajali kuinua vipaji na kulenga kuinua soka la Bongo wameidhamini Singida United licha ya kuwa ndio imepanda Ligi Kuu Tanzania bara msimu huu na itashiriki Ligi Kuu msimu ujao wa 2017/2018.

MANJI ABWAGA MANYANGA YANGA




Monday, May 22, 2017

SERENGETI BOYS YAFUNGASHA VIRAGO MICHUANO YA AFCON, YACHAPWA BAO 1-0 NA NIGER


TANZANIA imetolewa katika michuano ya vijana chini ya umri wa miaka 17, baada ya kufungwa 1-0 na Niger katika mchezo wa mwisho wa Kundi B usiku huu Uwanja wa Port Gentil mjini Gentil, Gabon.

Matokeo hayo yanazifanya Niger na Tanzania zifungane pointi na wastani wa mabao ya kufunga na kufungwa, hivyo mshindi katika mechi baina yao anafuzu Kombe la Dunia Oktoba mwaka huu India na pia kwenda Nusu Fainali ya michuano hiyo.

Niger anaungana na Mali iliyoongoza kundi kwa pointi zake saba, baada ya ushindi wa mechi mbili na sare moja, wakati Tanzania na Angola zote zinatolewa.

Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Daniel Laryea wa Ghana, aliyesaidiwa na Seydou Tiama wa Burkina Faso na Attia Amsaad wa Libya, Niger walipata bao lao kipindi cha kwanza, mfungaji Ibrahim Boubacar Marou dakika ya 41 baada ya shambulizi zuri lililowachanganya walinzi wa Serengeti Boys.

Lakini Niger wangetoka uwanjani wanaongoza kwa mabao zaidi baada ya dakika 45 kama za kipindi cha kwanza kama si umahiri wa kiopa Ramadhan Awam Kabwili kuokoa michomo zaidi ya mitatu ya wazi.

Kwa ujumla, Serengeti Boys ilizidiwa mchezo kipindi cha kwanza na kipindi cha pili hali iliendelea kuwa hivyo na hatimaye Niger wakaitoa Tanzania. Wachezaji wa Tanzania walikuwa wenye huzuni baada ya mchezo huku wakilia.

Mbali na Mali na Niger, timu nyingine zilizofuzu Nusu Fainali ni Ghana na Guinea kutoka Kundi A.

Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Daniel Laryea wa Ghana, aliyesaidiwa na Seydou Tiama wa Burkina Faso na Attia Amsaad wa Libya, Niger walipata bao lao kipindi cha kwanza, mfungaji Ibrahim Boubacar Marou dakika ya 41 baada ya shambulizi zuri lililowachanganya walinzi wa Serengeti Boys.

Lakini Niger wangetoka uwanjani wanaongoza kwa mabao zaidi baada ya dakika 45 kama za kipindi cha kwanza kama si umahiri wa kiopa Ramadhan Awam Kabwili kuokoa michomo zaidi ya mitatu ya wazi.

Kwa ujumla, Serengeti Boys ilizidiwa mchezo kipindi cha kwanza na kipindi cha pili hali iliendelea kuwa hivyo na hatimaye Niger wakaitoa Tanzania. Wachezaji wa Tanzania walikuwa wenye huzuni baada ya mchezo huku wakilia.

Mbali na Mali na Niger, timu nyingine zilizofuzu Nusu Fainali ni Ghana na Guinea kutoka Kundi A.

IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA BIN ZUBEIRY

SHEREHE ZA TUZO ZA LIGI KUU 2016/17 ZIMEWADIA


SHEREHE za Tuzo ya Mchezaji Bora wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inatarajiwa kufanyika Mei 24 mwaka huu ukumbi wa Mlimani City Dar es Salaam.

Kamati Maalum iliyoundwa kusimamia tuzo hiyo imefanya mabadiliko kiasi kwa kuongeza baadhi ya tuzo ambazo hazikuwepo msimu uliopita lengo ikiwa ni kuboresha tuzo.

Tuzo zilizoongezwa ni: Tuzo ya Heshima (ambayo itatolewa kwa mwanasoka nguli wa zamani mwenye historia nzuri kwa soka la Tanzania).

Nyingine  ni: Tuzo ya Kikosi Bora cha Msimu (Itatolewa kwa wachezaji Bora 11 wa Ligi Kuu (VPL XI 2016/2017) walioteuliwa kutokana na ufanisi wao katika ligi hiyo msimu huu.

Pia imeongezwa Tuzo ya Mchezaji Bora mwenye chini ya umri wa miaka 20 (Hii itatolewa kwa wachezaji waliofanya vizuri katika ligi ya vijana ya timu za Ligi Kuu ya Vodacom.

Tuzo hiyo ya Mchezaji Bora wa Ligi ya Vijana itajulikana kama Tuzo ya Ismail Khalfan ikiwa ni heshima ya kumbukumbu ya mchezaji Ismail Khalfan wa Mbao FC aliyefia uwanjani katika mashindano hayo yaliyofanyika mkoani Kagera.

Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limefikiria kutoa tuzo hiyo kama njia mojawapo ya kuonesha kuthamini kipaji cha mchezaji huyi wakati wa uhai wake.

Kutokana na mabadiliko hayo tuzo zitakazotolewa katika sherehe hizo pamoja na Tuzo ya Mchezaji Bora wa Ligi Kuu ya VPL ambayo ndiyo tuzo kuu, pia ni Bingwa wa Ligi Kuu, Mshindi wa Pili, Mshindi wa Tatu, Mshindi wa Nne na  Mfungaji Bora.

Nyingine ni Mchezaji Bora wa Ligi Kuu, Golikipa Bora, Kocha Bora, Mwamuzi Bora, Mchezaji Bora wa Heshima, Mchezaji Bia anayechipukia, Goli Bora la Msimu, Mchezaji Bora wa Kigeni, Mchezaji Bora wa Chini ya Umri wa Miaka 20 na Timu Yenye Nidhamu.

Tuzo za Bingwa, mshindi wa pili, wa tatu na wa nne na Mfungaji Bora hizi zipo kulingana na msimamo wa ligi ulivyo.

Hata hivyo Mfungaji Bora safari hii kuna wachezaji wawili wamefungana, hivyo kamati itapitia vigezo vilivyopo katika Kanuni za kumpata Mfungaji Bora w Ligi Kuu Tanzania Bara ili kupata mshindi ambaye atatangazwa siku hiyo ukumbini.

Wafuatao wameteuliwa kuwania tuzo hizo kutokana na vigezo mbalimbali:

Mchezaji Bora wa Ligi Kuu

Aishi MANULA – Azam

Simon MSUVA – Yanga

Shiza KICHUYA – Simba

Haruna NIYONZIMA – Yanga

Mohammed HUSSEIN – Simba

(Majina ya wanaowania tuzo hiyo yalitolewa Jumatano iliyopita na upigaji kura unaendelea ukiwahusisha Makocha wa timu za Ligi Kuu na Makocha Wasaidizi,Wahariri wa habari za michezo na Manahodha wa timu za Ligi Kuu, ambapo mwisho wa kufanya hivyo ni Jumanne Mei 23 mwaka huu).

KIPA BORA

Aishi MANULA – Azam

Owen CHAIMA – Mbeya City

Juma KASEJA – Kagera Sugar

KOCHA BORA

Joseph OMOG – Simba

Mecky MEXIME – Kagera Sugar

Ettiene NDAYIRAGIJE – Mbao

MWAMUZI BORA

Shomari LAWI – Kigoma

Elly SASII – Dar es Salaam

Hance MABENA – Tanga

MCHEZAJI BORA WA KIGENI

Haruna NIYONZIMA – Yanga

Method MWANJALE – Simba

Yusuph NDIKUMANA – Mbao

MCHEZAJI BORA ANAYECHIPUKIA

Mbaraka ABEID – Kagera Sugar

Shaaban IDD – Azam

Mohammed ISSA – Mtibwa

TUZO YA ISMAIL KHALFAN – (U-20)

Shaaban IDD – Azam

Abdalah MASOUD – Azam

Mosses KITAMBI – Simba

TUZO YA HESHIMA

(Atatangazwa aliyeteuliwa siku hiyohiyo ya sherehe za tuzo).

GOLI BORA LA MSIMU

(Tayari yamepatikana mabao bora 10 ambayo yataoneshwa siku hiyo ukumbini ikiwemo lile bora la msimu mzima).

TIMU YENYE NIDHAMU

(Mshindi atatangazwa ukumbini siku hiyo kulingana na vigezo vilivyopo).

WACHEZAJI 11 BORA WA MSIMU – VPL XI 2016/17

(Watatangazwa ukumbini siku hiyo ya sherehe).

Kamati inayohusika na usimamizi wa tuzo inawaomba wadau wote ambao wameombwa kupiga kura katika Tuzo ya Mchezaji Bora wafanye hivyo kulingana na fomu walizotumiwa na mchango wao una thamani kubwa.

Sunday, May 21, 2017

NI KARATA MUHIMU KWA SERENGETI BOYS LEO

 
Serengeti Boys - Timu ya Taifa ya vijana wa Tanzania wenye umri wa chini ya miaka 17, kesho Jumapili Mei 21, mwaka 2017 inarusha karata muhimu katika mchezo hitajika dhidi ya Niger kuwania nafasi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika - AFCON u-17.
 

Serengeti Boys itaingia Uwanja wa Port Gentil hapa mjini Port Gentil huku mkononi ikiwa na pointi 4 ilizovuna katika michezo yake miwili ya awali kwani ilianza kupata sare tasa dhidi ya Mali Mei 15, mwaka huu kabla ya kuifunga Angola Mabao 2-1 katika mechi zilizofanyika Uwanja wa l’Amitee jijini Libreville.
 

Vijana wa Serengeti Boys ambao wamefikia Hoteli ya Strange Complex, wana ari ya ushindi dhidi ya vijana wenzao wa Niger ambao wana alama moja waliyoipata kwenye sare ya mabao 2-2 dhidi ya Angola walipocheza mwanzoni mwa wiki hii. Niger walipoteza mchezo wa pili dhidi ya Mali. Walifungwa mabao 2-1.
 

Kocha Mkuu wa Serengeti Boys, Bakari Nyundo Shime amesema: “Huu ni mchezo muhimu wa kupata matokeo muhimu kwa vijana wetu. Tumejiandaa vema kuwania nafasi ya angalau kuingia nusu fainali.”
 

Shime ambaye wakati wote amekuwa akishukuru uongozi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), kwa namna unavyojitoa kuiandaa timu hiyo kwa kuipa kambi tulivu nchi mbalimbali, amesema: “Hili ni deni.”
 

Akifafanua zaidi, Shime ambaye anafahamika zaidi kwa jina la Mchawi Mweusi, anasema: “…Nina deni. Nadaiwa na uongozi wa TFF chini ya Jemedari Jamal Malinzi, pia nina deni kwa Watanzania ambao wamekuwa wakihaha kutuombea dua na kuichangia timu hii.
 

“Nawashukuru sana kwa namna wanavyojitolea kwetu, na ndio maana nasema hili ni deni na niwaahidi tu kwamba nitaendelea kulilipa kesho kwa matokeo mzuri. Katika kila mchezo huwa na mipango yangu na mpango wa kesho ni ushindi tu. Tutacheza soka la kushambulia.”
 

Shime ambaye alisema kwamba ataingia kwa mfumo mwingine kesho, hatarajii kikosi chake kikawa na mabadiliko makubwa labda mpaka atakapoangalia mazoezi yatakayofanyika jioni ya leo kwenye Uwanja Sogara.
 

Nahodha wa timu hiyo, Dickson Job aliwatoa shaka Watanzania akisema vijana wote wako vema kwa ajili ya mchezo huo kwani mpira wa miguu kwao ni ajira kwa manufaa ya yao binafsi, familia kadhalika taifa ambalo limewatua Gabon kutafuta Kombe la Mataifa ya Afrika.
 

“Kuna watu wanadhani tunapochukuliwa na watu wa doping ni kama tunatumia dawa, hapana. ni utaratibu wa mechi za kimataifa kwamba mara baada ya mchezo wowote wa kimataifa, kanuni zinaruhusu madaktari kuchukua wachezaji kadhaa na kuwapima ili kuandika ripoti ya kila mchezo.
 

“Mchezo wa kwanza dhidi ya Mali nilichukuliwa mimi na Israel Patrick Mwenda na wachezaji wa Mali wawili. Mchezo wa pili alichukuliwa Abdul Suleiman na Kelvin Naftal na wenzetu wa Angola wawili. Ni jambo la kawaida ni ni utaratibu kwa kitengo cha Doping,” alifafanua Job.
 

Serengeti Boys inahitaji sare ya aina yoyote ili iwezi kuvuka ilihali Niger ambayo ina alama moja na ikishika mkini, imejiwekea matumaini ya kusonga mbele ikitamba kwmaba itafunga Tanzania.
 

Hakuna shaka kuwa dua za Watanzania zitakuwa pamoja na timu nzima ya Serengeti Boys ambayo kwa sasa imekuwa ikichungwa na timu pinzani katika kuwania nafasi hii muhimu ya ujio mpya wa mpira wa miguu wa Tanzania.

KOCHA MAYANGA ATANGAZA KIKOSI CHA TAIFA STARS


Kocha Mkuu wa timu ya Tanzania, Salum Mayanga leo Ijumaa  Machi 19, 2017 ametangaza majina ya wachezaji 24 watakaounda kikosi hicho cha Timu ya Taifa Stars ambacho sasa kinachodhaminiwa na Kampuni ya Bia ya Serengeti.

Katika mkutano na wanahabari uliofanyika Makao Makuu ya TFF, yaliyoko Uwanja wa Karume, Ilala jijini Dar es Salaam, Mayanga alisema kikosi hicho kinaundwa na makipa Aishi Manula  (Azam FC), Benno Kakolanya  (Yanga SC) na Said Mohammed (Mtibwa Sugar).

Walinzi wa pembeni upande wa kulia aliwataja Shomari Kapombe    (Azam FC) na Hassan Kessy (Yanga SC) wakati upande wa kushoto wapo Mohammed Hussein (Simba) na Haji Mwinyi  (Yanga SC).

Mayanga aliwataja walinzi wa kati Erasto Nyoni  (Azam FC), Salim Mbonde (Mtibwa Sugar), Abdi Banda (Simba SC) na Aggrey Morris  (Azam FC) ilihali aliwataja viungo wa kuzuia kuwa ni Himid Mao (Azam FC) na Jonas Mkude (Simba SC).

Kadhalika wako viungo wa kushambulia Salum Abubakar (Azam FC), Said Ndemla  (Simba SC) na Muzamiru Yassin (Simba) wakati viungo wa kulia waliotajwa ni Simon Msuva (Yanga SC) na Shizza Kichuya (Simba SC).

Viungo wa kushoto ni Farid Mussa (Teneriffe, Hispania)  wakati washambuliaji ni Mbwana Samatta (KRC Genk- Ubelgiji), Thomas Ulimwengu (AFC Eskilstuna – Sweden), Ibrahim Ajib (Simba SC), Mbaraka Yusufu (Kagera Sugar) na Abdurahman Mussa (Ruvu Shooting).

Pia Mayanga aliwataja wasaidizi wake kuwa ni Kocha Msaidizi kuwa ni Novatus Fulgence  wakati Kocha wa Makipa, Patrick Mwangata wakati Meneja wa atakuwa Danny Msangi; Mtunza Vifaa, Ally Ruvu wakati Daktari wa timu atakuwa Richard Yomba huku Daktari wa viungo   akiwa ni Gilbert Kigadya.

Timu hiyo itaingia kambini Machi 23, 2017 kwenye Hoteli ya Urban Rose, Dar es Salaam mpaka tarehe 29 baada ya hapo itasafiri kwenda Misri kwa kambi ya wiki moja kabla ya kurejea kuja kucheza mchezo wa kufuzu Mataifa huru ya Afrika mchezo  na Lesotho, mchezo utachezwa Tarehe 10  mwezi wa 6 mwaka huu jijini Dar es Salaam.

Wednesday, May 17, 2017

SPORTPESA WAINGIA MKATABA MNONO NA KLABU YA YANGA


Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara timu ya Yanga  Leo wameingia mkataba na Kampuni ya Michezo ya Kubashiri ya SportPesa  na kuwa klabu ya pili kudhaminiwa baada ya watani zao Simba kuwa wa kwanza kuingia kwenye udhamini huo.
Mkataba huo utakuwa ni wa miaka mitano na utagharimu kitita cha Sh bilioni 5.173 huku mwaka wa kwanza Yanga ikiingiza Sh milioni 950.
Mkataba huo umesainiwa  katika makao makuu ya klabu ya Yanga mbele ya waandishi wa habari ambapo SportPesa wakiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa SportPesa,Pavel Slavkov pamoja na Mkurugenzi wa Utawala na Utekelezaji wa SportPesa,Abbas Tarimba huku Yanga waliongozwa na Makamu mwenyekiti Clement Sanga na Katibu Mkuu Bonifance Charles Mkwasa.
Makubaliano hayo yatahusisha kuwepo kwa nembo ya SportPesa kwenye jezi za klabu kuanzia msimu ujao wa Ligi yaani 2017-18 hadi 2021-22.
Mmoja wa Wakurugenzi wa Yanga, Abbas Tarimba amesema leo kuwa mkataba wa Yanga na ule wa Simba haina tofauti na bingwa msimu ujao atalipwa Sh milioni 100 kutoka SportPesa.
“Kwa yule atakayefanikiwa kuchukua ubingwa wa Afrika, yeye tutatoa Sh milioni 250, hii ni sehemu ya bonus kwenye mkataba,” alisema.
Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Clement Sanga aliwashukuru SportPesa kuungana nao.
“Tunaamini ni sehemu ya kuleta mabadiliko, wamekuja kuunga nasi, tumewapokea na tunawaahidi ushirikiano. Hii ni kati ya kampuni nimeona kwa mara ya kwanza tumejadili mambo mengi. Mengine yatatokea huko mbele lakini ni mambo ya maendeleo,” alisema.
SportPesa ilianzishwa mwaka 2014 nchini Kenya na kuanzishwa kwake imefanikiwa kukua kimataifa kwa kushirikiana na timu kubwa za England ambapo wana mikataba na Hull City,Everton,Arsenal na Southampton pamoja na Ligi Kuu ya Hispania.

MALINZI ATOA SIRI SARE SERENGETI BOYS KUIGOMEA MALI


Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Emil Malinzi ametoa siri ya uimara wa timu ya Tanzania ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 17 akisema: “Haya yote kayafanya Dk. Harrison Mwakyembe.”

Akizungumza mjini Libreville, Malinzi amesema: “Ujumbe wa kuitakia kheri Serengeti Boys ulitolewa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo umeisukuma timu hiyo kufanya vema.

“…Ndiyo, timu imekuwa ikijindaa physical, lakini kupata neno la mzazi kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mheshimiwa Dk. John Magufuli kupitia Waziri wa Michezo, Mheshimiwa Mwekyembe liliwatia nguvu vijana kufanya vema na kuzuia Mali kuIshinda Serengeti.”

Vyombo vya habari vya hapa Libreville, vimesema Serengeti Boys ni timu ya kuchungwa mara baada ya matokeo ya jana dhidi ya Mabingwa watetezi – Mali ambayo pia ni makamu bingwa katika Kombe la Dunia la FIFA kwa vijana chini ya miaka 17.

Vyombo vya habari vya hapa vimesema ni matokeo mazuri na hata ya kushangaza kwani Mali ni timu ambayo hakuna timu inapenda kukutana nayo.

“La kushangaza kwa timu ya Tanzania ambayo pamoja na Angola zina vijana wanaoonekana kuwa na umri mdogo kulinganisha na timu za Afrika Magharibi, ni uwezo wao wa kubaki kwenye mpango wa mchezo hata walipokumbana na mawimbi makali,” limesema gazeti la Le Moniour.

Serengeti Boys imeanza kufuatiliwa na kuangalia matokeo yake ya mechi za nyuma na kuonekana imepoteza mechi chache za kimataifa na kuzifunga timu kama za Afrika Kusini, kutoka sare na Korea Kusini na Marekani katika michuano mbalimbali .

WATANZANIA KUSIMAMIA GHANA, GABON KESHO

Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), limewateua Watanzania watatu kuwa maofisa waandamizi wa kusimamia mchezo wa kundi A kati ya  Ghana na Gabon wa michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa vijana wenye umri wa chini ya miaka 17 utakaofanyika Uwanja wa Port Gentil utakaofanyika kesho Mei 17, 2017.

Watanzania hao ni Mwesigwa Joas Selestine atakayekuwa Kamisha wa mchezo huo wakati Frank John Komba atakuwa mwamuzi msaidizi na katika kitengo cha kitaalamu cha uchunguzi kwa wachezaji wanaotumia dawa za kusisimua misuli atakuwa Dk. Paul Gasper Marealle.

Hii ni fahari kwa nchi yetu Tanzania kwa viongozi wake kuthaminiwa na kuaminika katika nyanja za kimataifa.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linawapongeza viongozi hao na inawatakia kila la kheri katika kutimiza majukumu waliyopangiwa kesho na baadaye hasa ikizingatiwa kuwa fainali zijazo za vijana kama hizi, zitafanyika Tanzania mwaka 2019.

YALIYOJIRI KAMATI YA SAA 72 HAYA HAPA, MWAMUZI NGOLE MWANGOLE AONDOLEWA KUCHEZESHA LIGI KUU YA VODACOM


Kamati ya Bodi ya Uendeshaji na Kusimamia Ligi (Kamati ya Saa 72), iliketi mwishoni mwa wiki iliyopita na kupitia mchezo mmoja baada ya mwingine na kuibuka na uamuzi ufuatao.

Mechi namba 212 (Yanga 2 Vs Kagera Sugar 1). Kamati imefuta kadi nyekundu ya moja kwa moja aliyopewa mchezaji Mbaraka Yusuf wa Kagera Sugar baada ya kubaini hakutenda kosa lililosababisha mwamuzi ampe adhabu hiyo. Uamuzi huo umefanywa kwa mujibu wa Kanuni ya 9(8) ya Ligi Kuu.

Pia Mwamuzi wa mechi hiyo, Ngole Mwangole ameondolewa kuchezesha Ligi Kuu ya Vodacom kwa vile uamuzi aliofanya haukuwa sahihi. Hatua dhidi ya Mwamuzi Mwangole imechukuliwa kwa kuzingatia Kanuni ya 38(1a) ya Ligi Kuu.

Hii ni mara ya pili kwa Ngole kushindwa kutafsiri sheria uwanjani kwani katika duru la kwanza alionywa baada ya kukataa bao JKT Ruvu ilipocheza na Mtibwa Sugar katika Ligi Kuu ya ismu huu wa 2016/17.

Mechi namba 214 (JKT Ruvu 2 Vs Azam 2). Klabu ya Azam FC imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kutoingia vyumbani, na badala yake kukaa nje. Kitendo hicho ni kwenda kinyume na Kanuni ya 14(13) ya Ligi Kuu, na adhabu imetolewa kwa mujibu wa Kanuni ya 14(48) ya Ligi Kuu.

Mechi namba 215 (Mbao FC 1 Vs Tanzania Prisons 0). Mchezaji Jeremiah Juma wa Tanzania Prisons amefungiwa mechi tatu na kupigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na kuonyeshwa kadi nyekundu baada ya kumpiga ngumi mpinzani wake. Adhabu hiyo imetolewa kwa mujibu wa Kanuni ya 37(3) ya Ligi Kuu.

Pia timu ya Tanzania Prisons imeagizwa kurudisha mpira uliochukuliwa na mshabiki wake baada ya kumalizika mechi hiyo iliyofanyika Aprili 16, 2017 kwenye Uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza.

Msimamizi Msaidizi wa Kituo cha Mwanza aliripoti kwa Meneja wa Prisons, Bw. Enock Mwanguku tukio la shabiki huyo aliyechukua mpira huo na kuingia kwenye gari la timu hiyo. Meneja huyo aliahidi kufuatilia, lakini hadi timu yake inaondoka uwanjani hakutoa mrejesho wowote.

Mechi namba 220 (Majimaji 3 Vs Mwadui 0). Klabu ya Majimaji imepigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na timu yake kuingia uwanjani kwa kutumia mlango usio rasmi. Adhabu hiyo ni kwa mujibu wa Kanuni ya 14(48) ya Ligi Kuu.

Mechi namba 224 (Yanga 2 Vs Tanzania Prisons 0). Klabu zote zimepigwa faini ya sh. 500,000 kila moja kwa timu zao kutoingia vyumbani na kusababisha wachezaji wakaguliwe wakiwa nje ya vyumba. Adhabu hiyo ni uzingativu wa Kanuni ya 14(48) ya Ligi Kuu.

YANGA BINGWA


BAO lililofungwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Burundi, Amis Tambwe, jana liliiwezesha Yanga kuichapa Toto African bao 1-0 na kutwaa tena taji la ligi kuu ya soka ya Tanzania Bara.

Katika mechi hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, huku ikiwa na ushindani mkali, Yanga ilipata bao hilo la pekee dakika ya 72 baada ya Tambwe kujitwisha kwa kichwa krosi kutoka kwa beki Juma Abdul.

Hii ni mara ya tatu mfululizo kwa Yanga kutwaa taji hilo, safari hii ikiwa chini ya Kocha George Lwandamina kutoka Zambia. Awali, Yanga ilitwaa taji hilo mara mbili ikiwa chini ya Hans Van Der Puijm.

Kipigo hicho kimeiweka Toto African kwenye hatari ya kushuka daraja msimu ujao huku ikiwa imesaliwa na mechi moja dhidi ya Mtibwa Sugar, itakayochezwa kwenye uwanja wa Manungu, ulioko Turiani, Morogoro.

Kwa upande wa Yanga, ushindi huo umeiwezesha kuwa na pointi 68, ikifuatiwa na Simba yenye pointi 65 huku kila timu ikiwa imesaliwa na mechi moja kumaliza ligi.

Simba itamaliza ligi kwa kuvaana na Mwadui kwenye Uwanja wa Taifa wakati Yanga itavaana na Mbao FC kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Simba itaweza kutwaa ubingwa iwapo itaifunga Mwadui mabao 10-0 na wakati huo huo Yanga kufungwa na Mbao.

Tuesday, May 16, 2017

SERENGETI BOYS YAWATOA NISHAI MABINGWA WATETEZI MALI


LIBREVILLE, Gabon

TIMU ya soka ya Taifa ya Vijana wa chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys, jana walianza vyema michuano ya fainali za kuwania ubingwa wa Afrika baada ya kuwalazimisha kutoka suluhu mabingwa watetezi Mali.

Katika mechi hiyo ya kundi B iliyochezwa mjini hapa, Mali ilicheza vizuri kipindi cha kwanza na kulitia msukosuko mara kwa mara lango la Serengeti Boys, lakini haikuwa na bahati ya kupata bao.

Katika kipindi hicho, Serengeti Boys ilipwaya kutokana na safu yake ya kiungo kuzidiwa na wapinzani wao. Hadi kilipomalizika, hakuna timu iliyoweza kupata bao.

Kocha Bakari Shime alifanya mabadiliko mawili ya wachezaji kipindi cha pili, ambayo yaliongeza uhai kwa Serengeti Boys, iliyowapa kazi ya ziada mabeki wa Mali kuokoa mipira ya hatari na kupunguza nguvu yao ya kushambulia.

Katika kipindi hicho, Serengeti Boys ilifika kwenye lango la Mali zaidi ya mara tatu, lakini mashuti ya washambuliaji wake Nashon, Yohanna Mkomola na Nickson Kibambage yalishindwa kulenga lango.

Kipa Ramadhani Kambwili aliiokoa Serengeti Boys iisifungwe dakika ya 77 baada ya kuzuia kwa mguu shuti la Lassan Traole, lililokuwa likielekea wavuni na mpira kuwa kona.

Serengeti Boys imesaliwa na mechi mbili dhidi ya Niger na Angola na iwapo itashinda zote, itafuzu kucheza nusu fainali na kupata tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika nchini India.

Monday, May 15, 2017

MO DEWJI NA HANS POPPE WAJIWEKA PEMBENI SIMBA



Mwanachama na kijana tajiri barani Afrika kwa sasa, Mohammed Dewji, anayetaka kununua hisa Simba, amesikitishwa na uongozi wa klabu hiyo kwa kuingia mkataba wa udhamini na kampuni ya SportPesa bila kumshirikisha.

Habari ambazo hazijathibitishwa na upande wowote, zinasema Mo Dewji, Mbunge wa zamani wa Singida Mjini, ameuandikia barua uongozi wa klabu hiyo chini ya Rais wake, Evans Aveva, kutaka alipwe fedha zake, sh bilioni 1.4, alizokuwa anaikopesha Simba kwa kulipa mishahara ya wachezaji na benchi la ufundi, sh milioni 80 kila mwezi.
Imedaiwa Mo Dewji alikuwa anatoa fedha hizo kwa makubaliano zitalipwa wakati mpango wake wa kununua hisa za klabu utakapokamilika. Mo alikubaliana na uongozi wa Simba kununua asilimia 51 ya hisa kwa Sh. Bilioni 20 mara baada ya mchakato wa mabadiliko ya Katiba utakapokamilika.
Lakini zoezi hilo linaelekea kuingia doa baada ya Mo Dewji kuandika katika ukurasa wake wa Twitter akilalamikia uongozi wa klabu kuingia mkataba na SportPesa bila kumshirikisha. 

Mwenyekiti wa kamati ya Usajili Zacharia Hans Poppe, mmoja wa wanachama na viongozi maarufu wa Klabu ya Simba, ameamua kuachia ngazi kwenye kamati ya utendaji.
Uamuzi wake wa kuondoka kamati ya utendaji, moja kwa moja unamuondoa kwenye nafasi ya mwenyekiti wa kamati ya usajili.
Hans Poppe amesema kuwa, ameondoka baada ya jopo lililoongozwa na Rais wa Simba, Evans Aveva kuingia mkataba na Kampuni ya Michezo ya Kubashiri ya SportsPesa ambao wamesaini mkataba wa Sh bilioni 4.9 kwa miaka mitano.
Akizungumza katika mahojiano maalum , Hans Poppe amesisitiza, ameamua kukaa pembeni na huyu ndiye amekuwa injini ya usajili katika kikosi cha Simba akipambana na mahasimu wao wakubwa nchini Yanga
“Nitabaki kama mwanachama wa kawaida wa Simba. Nitaendelea na shughuli zangu nyingine,” alisema na alipoulizwa sababu za kujiuzulu alisema:

 “Mambo yamekwenda kwa uficho, mkataba umekuwa ukifichwa. Kamati ya utendaji imetaarifiwa siku moja kabla ya kusainiwa. Ilikuwa Alhamisi, Ijumaa wamesaini, nini kinafichwa.
“Mimi nakaa pembeni, nimeshaandika na barua. Sitaki kuwa sehemu ya watu wasio waungwana. Angalia hata Mo Dewji hakuwa akijua, lakini huyu mtu mwaka mzima ndiye katukopesha mishahara.
“Dewji alisema, mkitaka kusaini mkataba kama mmepata mdhamini mniambie. Maana na yeye tulimpa jukumu la kutafuta mdhamini, hata mimi nilipewa jukumu hilo, lakini leo unasikia wenzako wameingia mkataba na mdhamini mpya.
“Kabla tumekuwa tukishirikiana kwa kila jambo, kwenye shida na raha. Vipi leo, nini kimefanya tusiwe pamoja?
“Kawaida walitakiwa waje na mkataba, tuujadili na kuangalia vipengele. Kama kuna sehemu zikarekebishwe au kuongezwa vifanyiwe kazi, mwisho wakija tuseme hapa sawa, basi usainiwe. Nani atakataa mdhamini kama unaona ana faida na klabu?” alihoji Hans Poppe.
Ijumaa SportPesa Tanzania ilitangza rasmi udhamini wake wa miaka mitano kwa klabu ya Simba ya Dar es Salaam, wenye thamani ya Sh. Bilioni 4.96.
Mkurugezi wa Utawala wa SportPesa, Tarimba Abbas alisema kwamba wameingia mkataba huko kwa dhumuni la kuendeleza soka nchini na kuisaidia klabu ya Simba kufikia malengo yake.
Akifafanua, Tarimba ambaye ni Mwenyekiti wa zamani wa mahasimu wa Simba, Yanga alisema kwamba, katika mkataba wao kwa mwaka wa kwanza wadhamini hao watatoa Sh. Milioni 888 na miaka itakayofuata wataongeza asilimia 5 na miaka miwili ya mwisho watatoa Sh. Bilioni 1 na kwamba fedha hizo zitatolewa kwa awamu nne kwa mwaka.
Tarimba alisema kwamba Simba watapaswa kuyathibitisha matumizi ya fedha hizo kwamba yalifanyika kwa maendeleo ya soka.
Alisema licha ya mkataba huo, pia kutakuwa na motisha klabu hiyo ikishinda mataji, mfano kwa ubingwa wa Ligi Kuu watapewa zawadi ya Sh. Milioni 100.
“Pia ikishinda michuano kama (Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati) Kombe la Kagame pia watapewa zawadi na wakifanya vizuri katika Ligi ya Mabingwa Afrika watapata zawadi ya Milioni. 250,”alisema Tarimba.

MSHAMBULIAJI WA MAMELOD SUNDOWNS ATUA SINGIDA UNITED


Singida United imedhamiria kuleta mapinduzi ya soka hapa nchini baada ya klabu hiyo kuendelea kujiimarisha zaidi kwenye usajili wa wachezaji.

Baada ya kufanikiwa kusajili wachezaji wanne wa kigeni leo hii uongozi wa klabu hiyo umekamilisha usajili wa mshambuliaji aliyewai kuitumikia ya Mamelod Sondowns na Super Sport za nchini Afrika ya Kusini.

Mshambuliaji huyo anaetambulika kwa jina la Nhivi Simbarashe anakuwa mchezaji wa tano kusajili ndani ya klabu hiyo itakayoongozwa na kocha mahili Hans van Der Pluijm na msaidizi wake Fredrick Minziro.

Simbarashe pia ni mshambuliaji wa timu ya Taifa ya Zimbabwe amekuwa na mafanikio makubwa kwenye timu alizochezea ikiwemo kufunga goli pekee ambalo liliwaondosha TP Mazembe katika ushiriki wa michuano ya kombe la klabu bingwa barani Afrika wakati akiitumikia timu ya Mamelod Sondowns.

Uongozi wa Singida United umethibitisha kumpa kandarasi ya miaka miwili mchezaji huyo akitokea klabu ya Caps United ya nchini Zimbabwe ambapo baada ya kutokea Afrika Kusini alijiunga na timu hiyo ya nchini kwake.

SERENGETI BOYS KUIVAA MALI LEO AFCON U-17 GABON


Timu ya Taifa ya vijana chini ya umri wa Miaka 17, Serengeti Boys, leo Jumatatu  inafungua pazia lake katika mashindano ya Kombe la Afrika kwa Vijana, kwa kumenyana na Mali katika michuano hiyo inayofanyika nchini Gabon.
Serengeti Boys ipo Kundi B, pamoja na timu nyingine za Angola na Niger ambazo nazo zitakuwa kibaruani leo.
Akizungumza  kwa njia ya simu jana, kocha mkuu wa kikosi hicho, Bakari Shime, alisema kuwa kikosi chake kipo vizuri na kimejiandaa vya kutosha kuwakabili vijana wa Mali kwenye mchezo huo wa kwanza.
 “Kikosi kipo vizuri na tumejipanga kuikabili vilivyo timu ya Mali kwani tunataka kuwafurahisha Watanzania kwa kutowaangusha na naomba wazidi kutuombea,” alisema Bakari Shime.

timu hiyo imepata pigo baada ya Nahodha Abas Makamba, kuvunjika mguu kwa hiyo hataweza kucheza michuano yote.

YANGA INAHITAJI ALAMA 3 KUTANGAZA UBINGWA KWA MARA YA TATU MFULULIZO


Mabingwa watetezi  Yanga  wamerudi kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kutokana na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mbeya City ya Mbeya jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Ushindi huo unawafanya mabingwa hao watetezi watimize pointi 65 baada ya kucheza mechi 28 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu. Simba inaangukia nafasi ya pili kwa pointi zake 65 za mechi 29, ikizidiwa wastani wa mabao. 
Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Andrew Shamba wa Pwani, aliyesaidiwa na Joseph Pombe wa Shinyanga na Haji Mwalukuta wa Tanga, dakika 45 za kipindi cha kwanza zilimalizika Yanga ikiwa inaongoza 1-0.

Bao hilo lilifungwa na winga Simon Happygod Msuva kwa kichwa dakika ya saba tu akimalizia krosi ya Hassan Kessy.
Hata hivyo, Msuva hakuweza kushangilia bao hilo, kwani wakati anaenda hewani kuunganisha krosi ya Niyonzima aligongana na beki wa Mbeya City, Tumba Lui na kuchanika juu ya jicho la kulia.
Msuva hakuweza kuendelea na mchezo na kupelekwa kwenye zahanati ndogo ya Uwanja wa Taifa kwa matibabu zaidi nafasi yake ikichukuliwa na beki Juma Abdul.
Kwa mabadiliko hayo, Kessy alikwenda kucheza kama winga wa kulia na Abdul akacheza beki ya kulia, ingawa walikuwa wakipokezana kuzuia na kushambulia.
Kipindi cha pili Mbeya City walikianza vizuri na kufanikiwa kupata bao la kusawazisha lililofungwa na beki wake wa kulia, Haruna Shamte dakika ya 57 akitumia mwanya wa mabeki wa Yanga kupoteana.
Hata hivyo, Yanga wakafanikiwa kupata bao la pili lililofungwa na mshambuliaji Mzambia, Obrey Chirwa dakika ya 64 akimalizia mpira wa adhabu wa Juma Abdul.
Mbeya City ilijitahidi kujaribu kusawazisha bao hilo, lakini tayari wapinzani wao, Yanga walikuwa wamekwishaanza kucheza kwa kujihami zaidi na kushambulia kwa kushitukiza.
Mrisho Ngassa aliingia kipindi cha pili upande wa Mbeya City, lakini hakuwa na madhara kwa timu ya timu yake ya zamani zaidi tu ya kusisimua mashabiki kwa uchezaji wake mzuri.

Matokeo mengine ya mechi zilizochezwa leo

Kagera Sugar 2-1 Mbao FC
JKT Ruvu 0-1 Majimaji
Tanzania Prisons 2-1 Ndanda FC
Mtibwa Sugar 4 -2 Mwadui FC
KWA HISANI YA FULLSHANGWEBLOG

Friday, May 12, 2017

MAN UNITED, AJAX SASA KUVAANA FAINALI YA KOMBE LA UROPA



Manchester United wameshashinda kombe la Champions League, klabu bingwa dunia, FA na makombe mengine lakini hawajawahi kishinda kombe la Europa.

United wamepata nafasi kujaribu kushinda kombe hilo kwa mara ya kwanza baada ya hapo jana kutoka suluhu ya bao moja kwa moja dhidi ya Celta Vigo ya nchini Hispania.

Katika mchezo huo timu zote zilimaliza pungufu uwanjani baada ya Eric Bailly kwa upande wa United na Rocanglia wa Celta Vigo kuoneshwa kadi nyekundu ikiwa imebaki dakika moja kwa mchezo kumalizika.

United walianza kupata bao dakika ya 17 baada ya Fellaini kuunganisha kwa kichwa mpira wa Marcus Rashford na bao hilo kuifanya United kwa mara ya kwanza kufunga mabao 100 katika msimu mmoja tangu mwaka 2012/2013.

Dakika zikiwa ximebaki 5 kufikia dakika ya 90 Celta Vigo walisawazisha bao hilo kupitia kwa Sebastian Rocanglia ambaye dakika 4 baadae alipewa kadi nyekundu.suluhu imewafanya United kufudhu kucheza fainali kwa jumla ya mabao 2 kwa 1 kutokana na ushindi wao wa kwanza walioupata ugenini wiki iliyopita.

Fainali hii ni ya 14 kwa kocha wa United Jose katika mashindano yote toka aanze ukocha lakini rekodi yake ikiwa nzuri kwani katika fainali 13 alizowahi kufika, ameshindwa fainali 2 tu kubeba ubingwa.

Huko Ufaransa almanusra Olympique Lyon wabadili matokeo ya mwanzo ambapo walifungwa bao 4 kwa 1 na Ajax mjini Amsterdam na hapo jana wakiwa nyumbani walibakiza bao 1 tu kuweka mambo sawa.

Ushindi wao wa bao 3 kwa 1 haukutosha kuwasogeza katika fainali lakini shukrani kwa Alexandre Lacazatte ambaye alifunga mara mbili kwa Lyon na lile la tatu likifungwa na Rachid Ghezzal huku la Ajax likifungwa na Kasper Dolberg.

Tarehe 24 mwezi huu ndio ambapo bingwa wa Europa atafahamika ambapo United na Ajax watakutana katika dimba la Friends Arena lililoko Stochklom nchini Sweden.

AFRIKA SASA KUWAKILISHWA NA TIMU TISA KOMBE LA DUNIA



Shirikisho la soka duniani FIFA chini ya raisi wake mpya Gianni Infantino linaonekana kujaribu kuinua sana soka katika ukanda wa Afrika, ambako kuna wafuasi wengi wa Infantino.

Shirikisho hilo la soka sasa limeamua kuipa Africa nafasi ya upendeleo kwa kuiongezea nafasi 5 zaidi za ushiriki katika fainali za kombe la dunia la mwaka 2026.Katika fainali hizo timu zitaongezeka kutoka 36 hadi 48 na Afrika itawakilishwa na timu 9 ambapo nyingine ya 10 itapambana katika hatua ya mtoano.

Shirikisho hilo pia limeongeza idadi ya timu kutoka katika bara la Ulaya ambapo mwanzoni zilikuwa ni timu 13 na sasa zitakuwa 16, huku Marekani Kaskazini na kusini zikiwa timu 6 badala ya 3.

Oceania nao wamepewa nafasi moja ya uwakilishi wa moja kwa moja ambapo hapo mwanzo iliwapasa wacheze mchezo wa mtoano na timu za Amerika Kusini ili kufuzu.

Hii itawafanya New Zealand kuwa na nafasi kubwa ya kushiriki kombe la dunia kila mara kutoka na kutokuwa na upinzani mkubwa haswa baada ya Australia kuanza kushiriki michuano ya bara la Asia.

Thursday, May 11, 2017

BLOGU YA LIWAZOZITO YATIMIZA MIAKA SABA, YAFIKISHA WASOMAJI ZAIDI YA MILIONI MOJA


Kwa heshima na taadhima napenda kuwajulisha wasomaji wangu wa blogu ya liwazozito kwamba, blogu yenu pendwa, ambayo ni mahsusi kwa ajili ya habari za michezo na burudani, kesho inatimiza miaka saba tangu ilipoanzishwa mwaka 2010.

Blogu hii ilianza kwa mwendo wa kusuasua kutokana na ugeni wa teknolojia ya mitandao ya kijamii, lakini hatimaye ikaanza kukaza mwendo na sasa inakwenda kwa spidi kali, huku ikiendelea kuwapa habari motomoto zinazohusu michezo na burudani za aina mbalimbali.

Hadi sasa blogu hii imeshafikisha wasomaji 1,003,410 (takwimu za leo-Mei 11,2017), huku ikisomwa na watu wa mataifa mbalimbali barani Afrika, Ulaya, Arabuni na Marekani.

Nawashukuru sana wasomaji wangu wa hapa nchini, ambao wamekuwa wakinipa maoni na mawazo mbalimbali ya jinsi ya kuiboresha.

Wakati mwingine nilijikuta nikipigiwa simu usiku wa manane au alfajiri. Nikipokea, nakutana na maswali ya wasomaji wangu wanaotaka kujulishwa kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu ligi kuu ya Tanzania Bara, Ligi Kuu ya England, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na klabu za Simba na Yanga.

Mwanzoni nilikuwa naona kero, lakini baada ya muda si mrefu nikaanza kuzoea hali hiyo na kuwapa majibu kadri nilivyoweza. Ilikuwa changamoto nzuri, lakini iliweza kunijulisha ni kwa kiasi gani blogu hii inasomwa na watu wengi, hasa ikizingatiwa kuwa wapigaji walikuwa wanatoka katika mikoa karibu yote nchini.

Mafanikio ya blogu hii kihabari (sio matangazo), ndio yaliyoniwezesha kuanzisha blogu nyingine maalumu ya muziki wa taarab, maarufu kwa jina la ramozaone.blogspot.com (rusharoho) na nyingine kuhusu habari za kisiasa, biashara, uchumi na kijamii, inayoitwa tanzaniakwanzadaima.blogspot.com.

Asanteni sana wasomaji wangu kwa kuniunga mkono. Nawapenda sana.

Wednesday, May 10, 2017

TFF YAVITAKA VYOMBO VYA HABARI KUACHA KAMPENI CHAFU


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limevitaka baadhi ya vyombo vya habari nchini kuacha mara moja kampeni za upotoshaji zenye lengo la kuwachafua viongozi wa juu wa shirikisho hilo.

TFF imeshtushwa na taarifa inayoendelea kutolewa kwenye gazeti moja la kila siku ikidai kuwa kuna ufisadi ndani ya shirikisho wakati madai hayo ni ya uongo na yenye lengo la kujenga mtazamo hasi dhidi ya shirikisho na viongozi wake.

Gazeti hilo la kila siku limetumia taarifa ya ukaguzi wa fedha iliyofanywa na wakaguzi kutoka TAC kujenga picha kuwa ni ushahidi tosha wa kuwepo kwa ufisadi ndani ya shirikisho.

Taarifa ya ukaguzi wa fedha ya TAC haikuwahi kuituhumu TFF kwa ufisadi. Taarifa ilibaini maeneo ya kiuhasibu ambayo yalihitaji maelezo ya ziada ya namna baadhi ya malipo yalivyofanyika (audit queries), na ufafanuzi ulitolewa kwa ufasaha na watendaji wa shirikisho na kupelekwa mbele ya Mkutano Mkuu wa Shirikisho.
 
Hata hivyo gazeti hilo ambalo limeonekana kuweka kando kabisa misingi ya uandishi wa habari, limechapisha taarifa bila hata kutoa nafasi kwa wanaotuhumiwa kujibu na kutoa ufafanuzi stahiki.
 
Rais na katibu mkuu wa shirikisho wanahudhuria mikutano ya CAF nje ya nchi wakati gazeti hilo likiendelea kuporomosha mlolongo wa tuhuma bila kutoa haki ya kusikilizwa kwa wanaoandikwa vibaya.
 
TFF inaliangalia suala hili kama kampeini chafu inayofanywa ili kushawishi matokeo ya uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwezi Agosti mwaka huu.
 
Pia taarifa hii potofu inalenga kulihamisha taifa kutoka kwenye masuala ya msingi kama kuiunga mkono Serengeti Boys kwenye mashindano ya Afrika na kuanza kujadili masuala yanayohusiana na siasa za uchaguzi wa TFF.
 
TFF kwa sasa inatafakari hatua za kisheria za kuchukua dhidi ya vyombo vya habari husika na inachukua nafasi hii kuvisihi vyombo vya habari kuacha mara moja kujihusisha na kampeni ya kuchafuana ambayo ni kinyume na misingi ya maadili ya uandishi wa habari.

CAF YAMPA ULAJI TENGA



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linachukua nafasi ya kipekee kabisa kumpongeza Rais wa Heshima wa shirikisho, Leodegar Chilla Tenga kwa kuteuliwa kuwa Rais wa Kamati ya Usimamizi wa Leseni za Klabu katika Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF).

Kwa mujibu wa taarifa ya CAF, Tenga atasaidiwa Dany Jordaan wa Afrika Kusini katika kusimamia mpango huo muhimu kwa maendeleo ya mpira wa miguu barani Afrika.

Uteuzi wake ulitangazwa na Rais wa CAF, Ahmad Ahmad Jumatatu Mei 8, 2017 mara baada ya Kikao cha Kamati ya Utendaji CAF, chini uongozi mpya kilichofanyika katika Hoteli ya Sheraton, Manama, Bahrain.

Kwa niaba ya Kamati ya Utendaji, Rais wa TFF Jamal Malinzi alimpongeza Tenga akisema: “Hii ni fursa nzuri inayojenga taswira ya thamani na uwezo viongozi wetu wa mpira wa miguu nchini na kutambulika nje ya nchi katika taasisi za kimataifa kama CAF.

“Kwa niaba ya Kamati ya Wanafamilia wote wa mpira wa miguu, Wajumbe wa Kamati Utendaji, nachukua nafasi hii kumpongeza sana sana Rais wa Heshima wa TFF, Mzee wetu, Ndugu Leodegar Tenga kwa nafasi nyeti ya kusimamia Kamati ya Leseni za Klabu. Tunamtakia kila la kheri tukiamini nafasi hiyo ana uwezo nayo na bila shaka Mwenyezi Mungu, atakuwa pamoja na Tenga,” amesema Tenga.

Katika katika mkutano wa Bahrain, Rais wa CAF alipendekeza majina ya viongozi wawili kuwa Makamu wa rais, wa kwanza ni Kwesi Nyantakyi kutoka Ghana na wa pili ni Omari Selemani kutoka DR Congo na pendekezo hili lilipitishwa na kamati.

Uteuzi wa wajumbe wawili wa ushirikiano wa Kamati ya Utendaji. Kwa mujibu wa masharti ya sheria, Rais wa CAF alifanya mapendekezo ya wanachama mawili wa ushirikiano kwenye kamati ya utendaji ya CAF ambako wanachama waliopitishwa ni Moses Magogo (Rais wa shirikisho la mpira wa miguu Uganda na Ahmed Yahya – Rais wa Shirikisho la Mpira wa Maurtania.

Muundo wa Kamati ya dharura, Mwenyekiti ni Rais wa CAF, Ahmad Ahmad na wajumbe wake ni Kwesi Nyantakyi (Ghana), Omari Seleman (DR Congo), Fouzi Lekjaa (Morocco), Souleiman Waberi (Djibouti) na Musa Bility (Liberia).

Awali, Rais wa CAF alitoa mapendekezo ya uanzishwaji wa kamati mbili za dharula, kamati hizi zitajumuisha hasa marais wa mashirika wanachama. Moja itakuwa katika malipo ya marekebisho ya katiba na nyingine katika malipo ya fidia, semina zitaandaliwa kwa marais wa mashirika wanachama ili kuwasilisha kazi ya kamati ya marekebisho ya katiba na mchango wao kabla ya kukamilisha rasimu ya kuwasilishwa kwa Kamati ya utendaji na baraza kuu, muundo wa kamati ya dharura ni kama ifuatavyo.

Kamati ya Marekebisho ya Katiba Rais wake ni Kwesi Nyantakyi (Ghana) huku wanachama ni Lamine Kaba Badjo (Gambia), Sita Sangare (Burkina Faso), Moses Magogo (Uganda), Mclean Letshwiti (Botswana), Edouard Ngaissona (Jamhuri ya Afrika ya Kati), Elvis Chetty (Shelisheli) na Ahmed (Misri)

Rasilimali Watu: Ludovic Lomotsy (Mshauri wa Rais CAF).

Kamati ya fidia, Rais ni Fouzi Lekjaa (Morocco) huku wanachama wake ni Monteiro Domingos Fernandes (Sao Tome), Ahmed Yahya (Mauritania), Hani Abo Rida (Misri)

Rasilimali Watu: Essam Ahmed (CAF Kaimu Katibu Mkuu), Mohamed El Sherei (CAF Mkurugenzi Fedha)

Kongamano la mashindano ya CAF. Kamati hii inatarajiwa kupangwa nchini Morocco Julai 15-16, 2017. Shirikisho la soka nchini humo lina mpango wa kubeba gharama kuhusiana na kongamano hili, ambapo litaleta wadau pamoja mbalimbali ya mpira wa miguu Afrika (Wachezaji, Waamuzi, makocha, vyombo vya habari.

Kongamano hilo litajadili masuala yote kuhusiana na mashindano ya CAF ikiwa ni pamoja na shirika, muundo na ratiba na kufuatiwa na mkutano wa Kamati ya Utendaji ya CAF wa Julai 17, 2017 ambako utajadili pamoja na mambo mengine, utekelezaji wa maazimio makuu ya kongamano.

Uteuzi ya marais na makamu wa rais wa Kamati za Kudumu. Kamati ya Fedha, Rais ni Fouzi Lekjaa (Morocco) huku Makamu wa Rais ni Monteiro Domingos Fernandes (Sao Tome). Kamati nyingine ni ya maandalizi kwa ajili ya Kombe la Mataifa ya Afrika ambapo Rais ni Amaju Pinnick (Nigeria) na Makamu wa Rais ni Philip Chiyangwa (Zimbabwe)

Kamati ya maandalizi kwa ajili ya michuano ya Mataifa ya Afrika Rais ni Musa Bility (Liberia) huku makamu akiwa ni Wadie Jari (Tunisia). Kamati ya maandalizi kwa ajili ya Interclub Mashindano Rais ni Fouzi Lekjaa (Morocco) na Makamu ni Mutassim Jaafar (Sudan).

Kamati ya maandalizi kwa ajili ya U-20 Kombe la Mataifa Rais ni Tarek Bouchamaoui (Tunisia) na makamu ni Rui Da Costa (Angola). Kamati ya maandalizi kwa ajili ya mpira wa miguu wanawake Rais ni Isha Johansen (Sierra Leone) na makamu ni Moses Magogo (Uganda).

Kamati ya Maandalizi kwa ajili ya Mpira wa Ufukweni Rais ni Moses Magogo (Uganda) na Makamu Rais ni Kalusha Bwalya. Kamati ya waamuzi Rais ni Soleimani Waberi (Djibouti) na Makamu Rais ni Lim Kee Chong (Mauritius).

Kamati ya ufundi na maendeleo ya mpira wa miguu Rais ni Kalusha Bwalya (Zambia), makamu ni Souleiman Waberi (Djibouti) wakati Kamati ya Mambo ya Sheria, Rais ni Ahmed Yahya (Mauritania) na Makamu Rais ni Augustin Senghor (Senegal). Kamati ya mchezo wa uungwana (fair play), Rais ni Almamy Kabele Camara (Guinea) na Makamu Raisi ni Isha Johansen (Sierra Leone)

Kamati ya Habari Rais ni Amaju Pinnick (Nigeria) na Makamu Rais ni Hedi Hamel (Algeria). Kamati ya matibabu, Rais ni Adoum Djibrine (Chad) na Makamu Rais ni Yacine Zerguini (Algeria) na Kamati ya Masoko na TV Rais ni Danny Jordaan (Afrika Kusini) huku Makamu Rais ni Rui Da Costa (Angola).

LIGI KUU YA VODACOM BARA KUENDELEA KESHO, SIMBA KUVAANA NA STAND UNITED


Mara baada ya michezo ya mwishoni mwa juma lililopita, Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara 2016/2017, inatarajiwa kuendelea Ijumaa Mei 12, 2017 ambako Simba SC itaialika Stand United FC ya Shinyanga kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati Azam FC siku hiyo hiyo ya Mei 12, mwaka huu itakuwa mwenyeji wa Toto Africans ya Mwanza kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es Salaam.

Jumamosi Mei 13, mwaka huu JKT Ruvu itakuwa nyumbani Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga kucheza na Majimaji ya Songea wakati Tanzania Prisons itaikaribisha Ndanda ya Mtwara kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya ilihali Mwadui ya Shinyanga itakuwa mgeni wa Mtibwa Sugar Uwanja wa Manungu ulioko Mvomero, Morogoro huku Mbeya City ikisafiri hadi Dar es Salaam kucheza na Young Africans kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Siku ya Jumapili Mei 14, mwaka huu African Lyon ya Dar es Salaam itacheza na Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam ilihali siku inayofuata, Jumanne Mei 16, mwaka huu Young Africans tena itakuwa mwenyeji wa Toto Africans kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Funga dimba la Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara itakuwa Mei 20, mwaka huu kwa timu zote kucheza ambako Azam FC itakuwa mwenyeji wa Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam wakati Majimaji itamaliza na Mbeya City kwenye Uwanja wa Majimaji mjini Songea wakati Simba na Mwadui zitacheza Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Siku hiyo Mbao FC itaialika Young Africans ya Dar es Salaam kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza wakati Stand United itamaliza na Ruvu Shooting ya Pwani kwenye Uwanja Kambarage mjini Shinyanga ilihali Mtibwa Sugar itakuwa mwenyeji wa Toto Africans ya Mwanza kwenye Uwanja wa Manungu, Morogoro wakati Africans Lyon ikiwa mgeni wa Tanzania Prisons kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya na Ndanda itamaliza na JKT Ruvu mjini Mtwara kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona.

MALINZI AOMBOLEZA WANAFUNZI, WALIMU ARUSHA

          
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), limetoa rambirambi ya Sh 500,000 kwa walengwa walipoteza watoto katika ajali ya gari iliyoua zaidi ya watu 36, wakiwamo wanafunzi 33.


Wanafunzi hao 33 wa darasa la saba, walimu wawili na pamoja na dereva wa gari la shule ya msingi iitwayo Lucky Vicent ya Arusha, walifariki dunia jana Mei 6, mwaka huu.
          
Kwa mujibu wa taarifa za kipolisi, vifo hivyo vilivyotokea saa 3 asubuhi baada ya gari walilokuwa wakisafiria kupata ajali katika eneo Rhotia Marera, Wilaya ya Karatu mkoani Arusha.
 

Wanafunzi na walimu hao walikuwa wakitoka shuleni kwao kwenda shule ya Tumaini kwa ajili ya kufanya mtihani wa ujirani mwema ambako kabla ya kufika basi walilopanda liliacha njia na kisha kutumbukia korongoni ambako limesababisha vifo hivyo na majeruhi watatu.
 

Rambirambi hiyo ya TFF inakwenda sambamba na salamu za rambirambi zilizotolewa na Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi aliyeungana na viongozi mbalimbali akiwamo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli katika kuomboleza msiba huo.
 

Katika salamu zake za rambirambi, Rais Malinzi amesema amepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa taarifa ya vifo hivyo kwani imezima ndoto za watoto waliokuwa wakijiandaa kulitumikia taifa katika tasnia mbalimbali ikiwa ni pamoja na mpira wa miguu kama wachezaji, makocha, viongozi hapo baadaye.

“Mtazamo wetu kwa sasa ni kuendeleza soka la vijana, tena hasa wale walioko mashuleni, hivyo vijana wale ni sehemu ya kutimiza ndoto za TFF katika mpira wa miguu hapo baadaye, tunakubali haya yote kwa kuwa ni ya Mwenyezi Mungu ndiye anayejua siri,” amesema Rais Malinzi.


Salamu za Rais Malinzi zimekwenda kwa wazazi, ndugu, jamaa na marafiki wote wa wanafunzi, walimu na dereva waliopoteza maisha, akisema: “Huu ni wakati mgumu kwa Wana – Arusha, wazazi na walezi hawana budi kuwa na subira kwa sasa.”


Amesema kwamba kwa wanafamilia wote wa mpira wa miguu, “Tuwaombee marehemu wote wapumzishwe mahali pema. Pia wale waliopata majeruhi tunaomba wapone haraka katika ajali hiyo mbaya.


Ee Mwenyezi Mungu zipumzishe Roho za Marehemu hao, Mahala pema peponi.

ABDULRAHMAN MUSSA MCHEZAJI BORA WA VPL MWEZI APRILI, 2017


Mchezaji wa timu ya Ruvu Shooting FC, Abdulrahman Mussa amechaguliwa kuwa mchezaji bora wa Ligi Kuu ya Vodacom kwa mwezi Aprili kwa msimu wa 2016/2017.
    
Abdulrahman  aliwashinda wachezaji Jafar Salum wa Mtibwa Sugar  FC na Zahoro Pazi wa Mbeya City.

Katika mwezi wa Aprili kulikuwa na raundi tatu na timu ya Ruvu Shooting ilicheza michezo miwili ambayo Abdulrahman alicheza dakika zote 180 na kufunga magoli manne(4) kati ya matano yaliyofungwa na timu yake na hivyo kuifanya timu yake kufikia nafasi ya tisa(9) kutoka nafasi ya kumi(10) katika msimamo wa Ligi ya Vodacom.

Abdulrahman alifunga Hat Trick (magoli matatu) katika mchezo wa Ruvu Shooting dhidi ya Majimaji uliofanyika katika uwanja wa mabatini Mlandizi.
    
Kwa kushinda tuzo hiyo, Abdulrahman Mussa  atazawadiwa  kitita cha sh. milioni moja (1,000,000/) kutoka kwa wadhamini wa Ligi hiyo, kampuni ya Vodacom Tanzania.

TFF, WILDAID WASAINI MAKUBALIANO KUPIGA VITA UJANGILI



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Taasisi ya kupigania uhai wa maisha ya wanyama wa mbugani ya Wildaid Alhamisi Mei 4, mwaka huu kwa pamoja wamesaini makubaliano ya vita dhidi ya ujangili.

Makubaliano hayo yalisainiwa jijini Dar es Salaam kati ya Rais wa TFF, Jamal Malinzi na Mwakilishi wa taasisi hiyo, Lily Massa.

Akizungumza kabla ya kusaini makubaliano hayo, Rais wa TFF Jamal Malinzi alisema kwamba, “Hii ni sehemu nyingine ya TFF kujihusisha na shughuli za kijamii licha ya kuwa na majukumu ya kusimamia maendeleo ya mpira wa miguu katika kukuza na kuendesha mashindano.”

Malinzi amesema TFF inaendeleza utamaduni wa shughuli mbalimbali za jamii kwani hata kwa Rais wa Heshima wa TFF, Leodegar Tenga enzi za utawala wake akiwa kiongozi mkuu wa mpira wa miguu, alifanya hivyo katika kampeni za kupinga maambukizi mapya ya UKIMWI.

“Wengi mtakumbuka kuwa kulikuwa pia na vita vya kupigania afya za watoto na kupigania uhai wao pia kampeni za amani ambazo mpira wa miguu umetumika kuelimisha,” amesema.

Kwa hatua hii ya sasa, Rais Malinzi amesema kwamba TFF, inaingia makubaliano hayo na kuiteua timu ya taifa ya vijana Tanzania maarufu kama Serengeti Boys kusimama kidete kupinga uwindaji haramu wa wanyama mbugani kwa kuwa ni hazina kubwa kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Kwa upande wa Mwakilishi wa WildAid, Lily Massa, alishukuru kuingia kwa makubalino hayo akisema kwamba ndoto zao za kupiga vita uwindaji haramu na ujangili, itafanikiwa.

“Tunashukuru kuingia programu hii na ninaamini Mungu atatusaidia,” amesema Massa ambaye taasisi yake iko karibu kila nchi yenye wanyama wa mbugani.

Katika hatua nyingine, Rais Malinzi aliitakia kila la kheri Serengeti Boys ambayo kwa sasa inajiandaa kuingia Gabon kwa ajili ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika. Michuano hiyo inatarajiwa kuanza Mei 14, mwaka huu ambako Serengeti Boys ambayo iko Kundi B itakuwa Libreville - Mji Mkuu wa Gabon. Timu nyingine za Kundi B ni Mali, Niger na Angola.

WANAMUZIKI MSONDO NGOMA WARIDHIA BENDI KUREJESHWA TUCTA


WANAMUZIKI wa bendi ya muziki wa dansi ya Msondo Ngoma wamesema wameridhia bendi yao kurejeshwa kwa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini (TUCTA).

Wamesema uamuzi huo wa TUCTA umeleta ahueni kubwa kwao kwa sababu kwa sasa watakuwa na uhakika wa kupata mishahara kila mwezi, tofauti na sasa, ambapo malipo yao hutegemea viingilio vya mashabiki ukumbini.

Kauli ya wanamuziki hao imekuja siku chache baada ya shirikisho hilo kutangaza rasmi kuirejesha bendi hiyo chini yake kama ilivyokuwa enzi za NUTA, JUWATA na OTTU.

Katibu Mkuu wa TUCTA, Dk. yahaya Msigwa, alitangaza uamuzi huo wakati wa sherehe za maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani, yaliyofanyika kitaifa mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro.

Kutokana na uamuzi huo, wanamuziki wa bendi hiyo ambayo kwa sasa inajulikana kwa jina la TUCTA Jazz Band, watakuwa wakilipwa mishahara kila mwezi, posho mbalimbali, bima ya afya na kulipiwa michango ya kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii.

Meneja wa Msondo Ngoma, Saidi Kibiriti alisema mjini Moshi hivi karibuni kuwa, wameufurahia uamuzi huo kwa sababu umewaondoa katika maisha ya kubahatisha na ya kutegemea viingilio vya mashabiki kujiendesha.

Alisema tayari walishafanya mazungumzo ya awali na uongozi wa TUCTA na kukubaliana mambo kadhaa na kwamba, wanachokikubali kwa sasa ni kutia saini makubaliano hayo.

Kibiriti alisema wanachotaka kuona ni wanamuziki wote wanafaidika kutokana na uamuzi huo, ikiwemo kulipwa mishahara kila mwezi na kuhakikisha kuwa, wanafanyakazi kwa bidii na nidhamu wakiwa chini ya uongozi mpya.

Alisema walicho na uhakika nacho kwa sasa ni kwamba, kila mwanamuziki atakuwa na uhakika wa mshahara, iwe wamefanyakazi au hawajafanya, tofauti na ilivyo sasa, ambapo wamekuwa wakitegemea zaidi kulipana posho kila baada ya onyesho.

"Tumepitia kipindi kigumu sana kwa sababu muziki wa dansi kwa sasa hauna soko kama ilivyokuwa huko nyuma, tumekuwa tukilipana posho kila baada ya maonyesho na wakati mwingine fedha tunazopata ni kidogo.

"Lakini kwa sasa chini ya TUCTA, tuna uhakika wa mishahara kila mwezi. Cha msingi ni kufanyakazi tutakazopangiwa kwa bidii na nidhamu ya hali ya juu ili kuwaridhisha waajiri wetu,"alisema Kibiriti.

Alipoulizwa iwapo wataongeza wanamuziki wapya kwa lengo la kuiimarisha bendi hiyo, meneja huyo alisema hilo litategemea makubaliano ya mwisho watakayofikia na uongozi wa TUCTA.

Alisema kwa hatua waliyofikia, wanapaswa kuiimarisha zaidi bendi hiyo ili iwe bora na imara zaidi na pia kuongeza mvuto kwa mashabiki.

Thursday, May 4, 2017

FAINALI YA KOMBE LA FA KATI YA SIMBA NA MBAO FC SASA KUPIGWA MEI 28, DODOMA



Hatimaye fainali ya Kombe la Shirikisho kati ya Mbao FC dhidi ya Simba itafanyika Mei 28 kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.

Msemaji wa TFF, Alfred Lucas amethibitisha kwamba uwanja utakuwa ni Jamhuri.

“Kweli ni Jamhuri, awali ilikuwa ni droo lakini sasa moja kwa moja tumetangaza Jamhuri,” alisema leo.

Awali, kupitia mitandao ya kijamii, Rais wa TFF, Jamal Malinzi alitangaza uwanja utakaochezewa mechi utapatikana kupitia droo.

Malinzi alisema droo itafanyika ndani ya siku chache zijazo jambo ambalo lilizua mjadala mkubwa kati yake na mashabiki ambao walioenkana kumshangaza.

UPELELEZI KESI YA WEMA WAKAMILIKA



Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeelezwa kuwa kesi ya kukutwa na bhangi inayomkabili Msanii maarufu nchini wa filamu, Wema Isaack Sepetu (28) na wenzake wawili umekamilika.

Wakili wa Serikali, Onolina Moshi aliyaeleza hayo leo  mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kutajwa.

Mheshimiwa, kesi hii leo imekuja kwa ajili ya kutajwa lakini upelelezi umekamilika naomba ahirisho kwa ajili ya kuwasomea washtakiwa maelezo ya awali (PH). Amesema Moshi.Hakimu Simba ameahirisha kesi hiyo   hadi Juni Mosi,2017 kwa PH.

Wema amewakilishwa mahakamani hapo na Wakili Tundu Lissu.

Mbali na Wema washtakiwa  wengine ni mfanyakazi wake wa ndani, Angelina Msigwa (21) na Matrida Seleman Abbas (16) aliyetambuliwa kuwa ni mkulima.Watuhumiwa hao wawili wanatetewa na wakili Peter Kibatala na Hekima Mwesigwa.

Wema ambaye ni mshindi wa taji ya Urembo wa Tanzania (Miss Tanzania) mwaka 2006 alifikishwa mahakamani hapo na kupandishwa kizimbani baada ya kusota mahabusu katika kituo kikuu cha Polisi (Police Central ) Dar es Salaam kwa muda wa siku Sita.

Awali ilidaiwa kuwa, Februari 4 mwaka huu, huko Kunduchi Ununio, wilaya ya Kinondoni, washtakiwa hao walikutwa na msokoto mmoja wa bangi na vipande viwili.

Hata hivyo washtakiwa hao wote walikana mashtaka hayo na wapo nje kwa dhamana.

NI YANGA NA PRISONS J'MOSI; SIMBA NA AFRICAN LYON J'PILI




Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, inatarajiwa kuendelea Jumamosi Mei 6 na Jumapili Mei 7, mwaka huu  kwa jumla ya michezo sita.

Kwa mujjibu wa ratiba, michezo ya Jumamosi kutakuwa na michezo mitano ilihali Jumapili kutakuwa na mechi moja.

Michezo ya Jumamosi itakuwa ni kati ya Toto African na JKT Ruvu Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza wakati Majimaji ya Songea itakuwa mwenyeji wa Mwadui kwenye Uwanja wa Majimaji mjini Songea mkoani Ruvuma.

Kagera Sugar itaalikwa na Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Mabatini ulioko Mlandizi mkoani Pwani wakati Young Africans ya Dar es Salaam itaialika Tanzania Prisons kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Siku hiyo ya Jumamosi Mei 6, mwaka huu Azam FC itaialika Mbao FC ya Mwanza kwenye Uwanja wa Azam Complex ulioko Mbagala, Dar es Salaam ilihali Jumapili kutakuwa na mchezo kati ya Simba SC na African Lyon kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Wakati mechi zote zitaanza saa 10.00 jioni, mchezo kati ya Azam na Mbao utaanza saa 1.00 usiku.