KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, September 29, 2017

UONGOZI MPYA TFF WATEMBELEWA NA SERENGETI BREWERIES


Uongozi mpya wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ukiongozwa na Rais wake, Wallace Karia, umetembelea Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) ambayo ni wadhamini wakuu wa timu ya Taifa, Taifa Stars.

Ziara hii imefanywa na uongozi mpya wa TFF ikiwa ni wiki moja kabla ya mechi ya kirafiki ya kimataifa itakayozikutanisha Taifa Stars na Malawi, mchezo utakaofanyika  kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

Tangu imepata udhamini wa SBL mwezi Mei mwaka huu, Taifa Stars imecheza mechi nane kati ya 12 ikiwa ni mechi za kimataifa na kufanikiwa kuweka rekodi nzuri kwenye mechi zote ilizocheza.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Rais wa mpya wa TFF aliishukuru SBL kwa udhamini wake kwa timu ya taifa na aliihakikishia SBL kuwa uongozi wake umeunda  menejimenti ya Taifa Stars ili kuhakikisha kuwa timu ya taifa inapata ushindi kwenye kila mechi.

“Tunaishukuru SBL kwa kutoa msaada uliokuwa unahitajika sana na ambao umeiwezesha timu yetu ya taifa kujiandaa vyema na mechi na kufanya vizuri kwa ngazi ya kitaifa na kimataifa,” alisema Karia

Karia alisisitiza kuwa fedha zilizotolewa kwa ajili ya udhamini wa timu ya taifa, zitatumika vizuri na kuongeza kuwa uongozi wa TFF unalenga kuongeza imani kwa wadhamini wa Taifa Stars na wadau wa soka kwa ujumla wake.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa SBL Helene Weesie alimpongeza Rais mpya wa TFF pamoja na timu yake kwa kuchaguliwa na kueleza kuwa SBL itaendelea kutoa misaada inayolenga kuendeleza michezo hapa nchini.

“SBL inatambua mchango muhimu ambao michezo inatoa kwenye maendeleo ya kiuchumi na kijamii na ndiyo maana tunaamini kuwa tunapoidhamini Taifa Stars, tunachangia katika kuwaburudisha na kuwaunganisha Watanzania wakiwa na bia yao bora ya Serengeti ikwa na ujumbe wake wa sifa yetu, bia yetu, nchi yetu,” alisema

Mwezi Mei mwaka huu, TFF iliingia mkataba wa ufadhili kwa Taifa Stars utakaodumu kwa kipindi cha miaka 3 utagharimu shilingi blioni 2.1na kuifanya SBL kuwa mdhamini mkuu wa timu ya taifa.

Ikizalishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1996, bia ya Serengeti imetengenezwa na kimea kwa asilimia 100 huku ikiweza kushinda tuzo zaidi ya 10 kwa ngazi ya kitaifa na kimataifa kutokana na ubora wake wa kimataifa.

KOCHA PLUIJM WA SINGIDA UNITED APEWA KIBANO


Kamati ya Bodi ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi, iliyoketi hivi karibuni imepitia taarifa mbalimbali ya michezo iliyofanyika ya Ligi Kuu ya Vodacom na Ligi Daraja la Kwanza na kufikia uamuzi ufuatao.

Kamati hiyo maarufu kwa jina la Kamati ya Saa 72, imepitia mchezo namba 18 (Majimaji v Yanga).

Katika mchezo huo Mwamuzi Msaidizi Namba Moja, Bw. Hassan Uhako kutoka Arusha hakuwa makini, hivyo kutomuona mchezaji wa Majimaji, Juma Salamba jezi namba 12 aliyempiga kiwiko mchezaji Emmanuel Martin wa Yanga na kumsababishia maumivu hadi kupoteza fahamu.

Kutokana na kitendo hicho Kamati imeelekeza Mwamuzi Msaidizi huyo ameandikiwa barua ya Onyo Kali kwa kukosa umakini. Adhabu hiyo dhidi ya Mwamuzi huyo ni kwa mujibu wa Kanuni ya 38(5) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti wa Waamuzi.

Pia mchezaji Salamba wa Majimaji kutokana na kumpiga mwenzake kiwiko amesimamishwa na suala lake linapelekwa Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kwa ajili ya kuchukuliwa hatua za kinidhamu. Uamuzi wa kumsimamisha umezingatia Kanuni ya 9(5) ya Ligi Kuu.

Mechi namba 22 (Stand United v Singida United).

Kocha wa timu ya Singida United, Hans van der Pluijm amepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kuingia katika vyumba vya wachezaji na kutoa maelekezo wakati akiwa anatumikia adhabu ya kukosa mechi tatu aliyopata msimu uliopita akiwa na timu ya Yanga.

Adhabu dhidi ya Kocha Pluijm imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 40(13) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti wa Makocha.

Mmiliki wa Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga ameandikiwa barua kwa uwanja huo kukosa maji ya bomba na badala yake kutumia maji ya kwenye ndoo au madumu hali hiyo ambayo inahatarisha afya za wachezaji.

LIGI DARAJA LA KWANZA

Mechi namba 2 Kundi A (Mvuvumwa v African Lyon). Timu ya Mvuvumwa FC imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kuchelewa kwenye kikao cha maandalizi ya mechi na kuhudhuria wakiwa pungufu. Pia timu hiyo ilichelewa kufika uwanjani ambapo ilifika saa 9.20 mchana badala ya saa 9.00 mchana.

Adhabu dhidi ya Mvuvumwa FC imetolewa kwa mujibu wa Kanuni ya 14(49) ya Ligi Daraja la Kwanza. Kwa kuchelewa kwenye kikao cha maandalizi ya mechi, uwanjani na kuhudhuria kikao wakiwa pungufu ni ukiukaji wa Kanuni za 14(2a) na 14(9) za Ligi Daraja la Kwanza.

Mechi namba 1 Kundi B (Mlale JKT v Polisi Tanzania).

Timu JKT Mlale imepigwa faini ya sh. 200,000 (laki mbili) kwa kosa la kuchelewa kufika uwanjani. Iliingia saa 9:20 mchana badala ya saa 9:00 mchana. Kitendo hicho ni uvunjifu wa Kanuni ya 14(9) ya Ligi Daraja la Kwanza, na adhabu dhidi yao ni kwa mujibu wa Kanuni ya 14(49).

Mechi namba 2 Kundi C (Rhino Rangers v Alliance).

Timu ya Alliance imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kutoingia vyumbani wakati wa ukaguzi na wakati wa mapumziko, kitendo ambacho ni kinyume na Kanuni ya 14(13) ya Ligi Daraja la Kwanza, na adhabu imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 14(49) ya Ligi Daraja la Kwanza.

Pia viongozi wa benchi la ufundi la Alliance, Kocha Msaidizi Kessy Mziray, Kocha wa makipa Tade Hussein, Mtunza vifaa Josephat Munge na Meneja wa timu James Bwire wamepigwa faini ya sh. 200,000 (laki mbili) kila mmoja kwa kosa la kumbughudhi mwamuzi wakimtaka kumaliza mpira kabla ya muda wakidai muda umekwisha wakati kazi ya kutunza muda si yao. Adhabu hiyo ni kwa mujibu wa Kanuni ya 41(2) ya Ligi Daraja la Kwanza.

Rhino Rangers imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) na barua ya Onyo kutokana na mashabiki wa timu hiyo kufanya fujo baada ya mechi kumalizika. Adhabu hiyo ni kwa mujibu wa Kanuni ya 42(1) ya Ligi Daraja la Kwanza.

Mechi namba 3 Kundi C (Biashara Utd Mara v Toto Africans). Msimamizi wa Kituo ameandikiwa barua kuelezwa juu ya upotevu wa muda unaofanywa na waokota mipira (ball boyz).

Ball Boyz hao wamelalamikiwa katika mechi hiyo iliyochezwa Septemba 17, 2017 kwenye uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma, hivyo ni vizuri wakafahamishwa kuwa kuokota mipira kwa haraka ndiyo wajibu wao unaowafanya wawepo uwanjani.

Mechi namba 4 Kundi C (Dodoma FC v Pamba). Meneja wa timu ya Pamba FC, Salmin Kamau amepigwa faini ya sh. 200,000 na kufungiwa mwezi mmoja kwa kosa la kutoa lugha chafu kwa mwamuzi. Adhabu dhidi yake imezingatia Kanuni ya 41(2) ya Ligi Daraja la Kwanza kuhusu Udhibiti wa Viongozi.

AJENDA 13/MSC/2017- MALALAMIKO YA RUVU SHOOTING

Kamati imetupa malalamiko ya klabu ya Ruvu Shooting dhidi ya Adeyum S. Ahmed kupinga mchezaji huyo kuichezea Kagera Sugar bila kuwa na barua ya kumruhusu (release letter) kutoka klabu ya Stand United.

Malalamiko hayo yametupwa baada ya Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya TFF kueleza kuwa Adeyum ni mchezaji halali wa Kagera Sugar, kwani wakati anasajiliwa na timu hiyo alikuwa mchezaji huru kwa vile mkataba wake na Stand United ulishavunjika, hivyo kutohitaji release letter wakati anajiunga na Kagera Sugar.

KUZIONA TANZANITES, FALCONETS MIA TANO


Timu ya Taifa ya Mpira wa Miguu – wasichana wenye umri wa chini ya miaka 20 ya Nigeria ‘Falconets’ inatarajiwa kutua nchini usiku wa kumkia Ijumaa Septemba 29, mwaka huu.

Wakitokea Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Nnamdi Azikiwe, ulioko Abuja nchini Nigeria, Falconets watatumia ndege ya Shirika la Ndege la Ethiopia ikiwa ni kikosi cha watu 31 miongoni mwake wako maofisa 13 kuja Dar es Salaam, Tanzania.

Timu hiyo ya wasichana yenye wachezaji 18, watatua Dar es Salaam saa 9.40 (03h40) usiku na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania, limewapangia kuishi katika Hoteli ya Urban Rose iliyoko katikati ya jiji la Dar es Salaam katika kipindi cha siku tatu watakazokuwa hapa jijini.

Wanakuja kucheza na timu ya Taifa ya wasichana wenye umri wa chini ya miaka 20 ya Tanzania ‘Tanzanite’ kwenye mchezo wa marudiano kuwania kucheza fainali za Kombe la Dunia. Fainali za Kombe la Dunia zitafanyika Ufaransa hapo mwakani.

Mchezo huo wa marudiano utafanyika Jumapili Oktoba mosi, mwaka huu kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es Salaam kuanzia saa 10.00 jioni.

Tanzania ina matumaini ya kufanya vema kwenye mchezo huo wa marudio licha ya kupoteza kwa mabao 3-0 katika mchezo wa kwanza uliofanyika Uwanja wa Samwel Oigemudia ulioko Jimbo la Benin, Nigeria.

TASWA YALAANI TUKIO LA CHIRWA KUMPIGA MWANDISHI WA HABARI



CHAMA Cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) na wahariri wa habari za michezo nchini, tumepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kushambuliwa kwa mwanahabari John Dande, zinazodaiwa kufanywa na straika wa Yanga, Obrey Chirwa, juzi Jumanne Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

TASWA na wahariri wa habari za michezo, tunaalani tukio hilo la kushambuliwa kwa Dande ambaye ni mpigapicha wa Kampuni ya New Habari 2006 Limited, kwani kitendo hicho si cha kiungwana bali ni udhalilishaji wa taaluma ya habari na hujuma kwa tasnia na mambo kama haya  yanadhoofisha nguzo muhimu ya kujenga jamii yenye uelewa wa mambo yanayoendelea nchini na kudhoofisha mfumo wa kidemokrasia, ambao tunajitahidi kuuimarisha nchini.

Kukaa kimya, hata tukiliwazwa na kuombwa samahani kwa jambo hili, hakutatoa tafsiri nyingine kwa wana taaluma ya habari na jamii kwa ujumla isipokuwa kuliona jambo hili kama ni la kawaida.

Kama tukio hilo lingefanyika eneo la starehe au mitaani na mwandishi hakuwa kazini, tungelichukulia suala hilo kama faragha inayowahusu watu wawili, aliyepiga na aliyepigwa, lakini kutokana na kumtokea mwandishi akiwa kazini tena uwanjani, ndio tumelazimika kutekeleza wajibu wetu wa kuitetea taaluma na haki ya mwandishi wa habari kufanya kazi bila kusumbuliwa au vitisho.

Kifungu cha 7 cha sheria za huduma za habari Na 12 ya mwaka 2016 kinaaainisha uhuru wa habari katika kukusanya habari kwa muktadha wa kuwepo maeneo ya matukio kama hakuna sababu nyingine za kuzuiwa. Hivyo ni vyema wadau wetu wakatambua kuwa uandishi wa habari ni taaluma adhimu na nadhifu inayopaswa kuheshimiwa, kuenziwa, kulindwa na kutoingizwa katika migogoro.

Tunatoa tamko hili la kulaani kitendo hicho kwa sababu sio cha kawaida hapa nchini kama ilivyo baadhi ya nchi nyingine ambazo waandishi wanapigwa na hata kuuliwa. Lakini tunachelea kulifumbia macho tukio hili kwa sababu kufanya hivyo ni kusema tunaridhika kupigwa na wachezaji na baadaye viongozi na hata mashabiki.

TASWA na wahariri wa habari za michezo na waandishi wa habari kwa ujumla hawana na hawatakuwa na muhali na mchezaji, kiongozi au shabiki yeyote wa michezo anayefanya kitendo kama hiki, kwani huo ni uhuni na sio mwanzo mzuri na tunataka mwendo kama huu ukome mara moja na yeyote mwenye malalamiko kwa mwandishi wa habari binafsi, au chombo chake afuate taratibu za kistaarabu zilizopo.

Hata hivyo kwa kuwa mhusika ameripoti tukio hilo kwenye vyombo vya usalama, tunawaomba waandishi wa habari wawe watulivu na waziachie mamlaka husika zitekeleze majukumu yake kwa mujibu wa sheria za nchi.

Tunaomba ushirikiano mzuri kati ya waandishi, wachezaji na viongozi wa michezo ili tucheze na tufurahie michezo kwa amani na kila mmoja aheshimu kazi ya mwenzake. Michezo iwe furaha kwa wote. Tucheze bila kupigana.

                UANACHAMA AIPS

Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Duniani (AIPS), chenye makao yake makuu Lausanne, Uswisi,  kimeanza kupokea maombi ya kadi kwa wanachama mwaka 2018/2019 kwa waandishi wa habari za michezo kutoka nchi mbalimbali duniani.

Maombi hayo yanafanyika kwa njia ya mtandao kwa wanachama wapya na wale wa zamani kupitia mtandao wao wa www.aipsmedia.com, ambapo ukiingia katika hiyo tovuti, utakuta maelekezo ya namna ya kupata kadi mpya, haichukui dakika tano kujaza na ukishaituma itakupa maelekezo zaidi ya hatua ya kufuata.
Tunawahimiza wanachama wetu kuchukua pia uanachama wa AIPS, kwani una faida nyingi, ikiwa ni pamoja na kupata kadi ya uanachama ambayo inatoa fursa mbalimbali ikiwemo mafunzo ya muda mrefu na semina za michezo mbalimbali.

               UCHAGUZI MKUU

Mapema mwezi huu tulitoa tamko la kuwepo Uchaguzi Mkuu wa chama chetu na kuwataka wanachama ambao wapo kwenye leja kuanzia Julai mwaka 2007 hadi Julai mwaka huu walipie ada zao za mwaka mmoja, ili kuhuisha uanachama wao na mwisho wa kufanya hivyo ni Septemba 30.

Lakini kutokana na muitikio mdogo sana katika ulipaji wa ada, Kamati ya Utendaji ya TASWA imeongeza muda hadi Oktoba 10 mwaka huu wanachama wote wahakikishe wanalipia ada hizo ili wahesabike wapo hai.

Monday, September 25, 2017

TFF YAINGIA MKATABA NA KCB



Shirikisho la soka nchini TFF, leo Septemba 25 limesaini mkataba na benki ya KCB wenye thamani ya shilingi 325,000,000.

Akizungumza wakati wa kusaini mkataba huo Rais wa TFF Wallace Karia amesema huo ni ushahidi kuwa shirikisho lina ushirikiano na wadau mbalimbali wa mpira nchini.

Aidha Karia amesema fedha hizo zitaelekezwa kwenye kukuza vipaji vya soka pamoja na maendeleo ya soka nchini kwa ujumla.

Huu ni mkataba mkubwa wa kwanza kusainiwa na shirikisho hilo tangu uongozi mpya chini ya Rais Wallace Karia ulioingia madarakani August 12 mwaka huu.

Sunday, September 24, 2017

MAYANGA AWAREJESHA NYOTA WAWILI KIKOSI CHA TAIFA STARS


KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Salum Shabani Mayanga amewarejesha kwenye kikosi cha timu hiyo, kipa Peter Manyika wa Singida United na mshambuliaji Ibrahim Hajib wa Yanga.
Mayanga leo ametaja kikosi kitakachocheza na Malawi ‘The Flame’ katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa chini ya utaratibu wa kalenda ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).
Wiki ya FIFA kwa mechi za kimataifa inatarajiwa kuanza Jumatatu Oktoba 2 hadi Jumatano ya Oktoba 11, mwaka huu ambako Tanzania imekubaliana kucheza Malawi kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam Jumamosi ya Oktoba 7, 2017 katika mchezo utakaoanza saa 10.00 jioni.
Katika kikosi hicho cha wachezaji 22, Kocha Mayanga ambaye aliteuliwa Januari 4, mwaka huu ameita nyota watano wanacheza soka nje ya mipaka ya Tanzania akiwamo nahodha wa kikosi hicho, Mbwana Ally Samatta.
Kikosi hicho kinachotarajiwa kuingia kambini Ijumaa Oktoba 1, mwaka huu kwenye Hoteli ya Sea Scape iliyoko Kunduchi, Dar es Salaam kina makipa Aishi Manula (Simba SC), Ramadhani Kabwili (Yanga) na Peter Manyika (Singida United).
Mabekii ni Gardiel Michael (Yanga), Boniphace Maganga (Mbao FC), Abdi Banda (Baroka FC/Afrika Kusini), Kelvin Yondani (Yanga), Salim Mbonde (Simba SC), Erasto Nyoni (Simba SC) na Adeyum Ahmed (Kagera Sugar).
Viungo ni Himid Mao ambaye pia ni Nahodha Msaidizi (Azam FC), Hamisi Abdallah (Sony Sugar/Kenya), Muzamil Yassin (Simba SC), Raphael Daud (Yanga), Simon Msuva (Difaa El Jadidah/Morocco), Shiza Kichuya (Simba SC), Abdul Hilal (Tusker/Kenya) na Morel Orgenes (FC Famalicao/Ureno).
Washambuliaji ni Mbwana Samatta (KRC Genk/Ubelgiji), Ibrahim Hajib (Yanga) na Mbaraka Yussuph (Azam FC).
Benchi la Ufundi la Mayanga linaundwa na yeye mwenyewe ambaye ni Kocha Mkuu, Fulgence Novatus (Kocha Msaidizi), Ame Ninje (Kocha Msaidizi), Patrick Mwangata (Kocha wa Makipa), Danny Msangi (Meneja), Dkt. Richard Yomba (Daktari wa timu), Dkt. Gilbert Kigadye (Daktari wa Viungo) na Ally Ruvu (Mtunza Vifaa).

YANGA YAIPIGA NDANDA BAO 1-0, AZAM YAZIDI KUNG'ARA


YANGA SC imepata ushindi mwembamba wa 1-0 dhidi ya Ndanda FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, uliochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam.
Shukrani kwake, mfungaji wa bao hilo pekee, mshambuliaji mpya kutoka kwa mahasimu, Simba SC, Ibrahim Hajib Migomba aliyefunga dakika ya 34 baada ya kazi nzuri ya beki wa kati, Kevin Patrick Yondan.
Beki wa kulia, Juma Abdul Mnyamani alimuanzishia kona fupi Yondan, ambaye alijitengeneza na kutia krosi maridadi iliyounganishwa nyavuni na Hajib kwa staili ya kujipinda maarufu kama baiskeli.

Lakini Yanga itamkosa kiungo wake mpya, Mkongo Papy Kabamba Tshishimbi katika mchezo wake ujao na Mtibwa Sugar Septemba 30, baada ya kuonyeshwa kadi ya njano na refa Jeonisya Rukyaa wa Kagera leo, ambayo inakuwa kadi yake ya tatu mfululizo.
Wakati huo huo, timu ya Azam FC, imeendelea kufanya kweli kwenye Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, baada ya kuichapa Lipuli bao 1-0, mchezo uliofanyika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam usiku wa Jumapili.
Kwa ushindi huo Azam FC imefanikiwa kuikamata Mtibwa Sugar baada ya kufikisha jumla ya pointi 10 zikiwa zinalingana kileleni huku ikiwa timu pekee ambayo haijaruhusu bao lolote tokea ligi hiyo ilipoanza Agosti 26, mwaka huu.
Bao pekee la Azam FC limefungwa na Mbaraka Yussuf dakika ya 11 akipokea pasi safi ya Nahodha Himid Mao ‘Ninja’, likiwa ni bao lake la pili kwenye mechi ya pili mfululizo, lingine akiitungua timu yake ya zamani Kagera Sugar katika ushindi wa 1-0.
Nayo Mtibwa Sugar imepunguzwa kasi katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya kulazimishwa sare ya 1-1 na Ruvu Shooting Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.

Friday, September 22, 2017

SIMBA YAVUTWA MKIA NA MBAO FC


TIMU kongwe ya soka ya Simba jana ilishindwa kuendeleza ubabe baada ya kulazimishwa kutoka sare ya mabao 2-2 na Mbao FC katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara iliyochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Simba itabidi ijilaumu kwa kushindwa kutoka uwanjani na ushindi, kwani iliweza kuwa mbele ya Mbao mara mbili, lakini wapinzani wao hao waliweza kusawazisha.

Wakongwe hao wa soka nchini waliuanza mchezo huo kwa kasi na kufanikiwa kupata bao la kwanza dakika ya 16 kupitia kwa Shiza Kichuya, aliyeunganisha wavuni kwa kichwa krosi kutoka kwa beki Erasto Nyoni. Bao hilo lilidumu hadi mapumziko.

Mbao ilipata bao la kusawazisha dakika ya 46 kupitia kwa Habibu Kondo kwa shuti kali la mbali lililompita kipa Aishi Manula na mpira kujaa wavuni.

Dakika tatu baadaye, Simba iliongeza bao la pili lililofungwa na James Kotei, aliyeunganisha wavuni mpira wa adhabu uliopigwa na Nyoni baada ya Haruna Niyonzima kuchezewa rafu.

Zikiwa zimesalia dakika tisa pambano hilo kumalizika, Mbao ilisawazisha kwa bao lililofungwa na Boniface Maganga, akiwa nje kidogo ya eneo la hatari.

Tuesday, September 19, 2017

NAIBU WAZIRI WA MICHEZO AIPONGEZA TFF



Na Benedict Liwenga-WHUSM.

Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Anastazia Wambura amelipongeza Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kwa ufanisi wao wa kazi huku akiwataka kufanya kazi kwa ukaribu na Serikali ya Awamu ya Tano ili kuleta maendeleo katika soka.
 

Wambura ameyasema hayo leo Jijini Dar es Salaam wakati alipotembelea ofisi za Shirikisho hilo ili kujua namna wanavyotekeleza majukumu yao ikiwemo changamoto za shirikisho pamoja na maendeleo ya soka nchini.

Akiongea na Viongozi mbalimbali na wadau wa soka katika ziara yake hiyo, amesema kwamba anaridhishwa na kazi wanazofanya TFF na amewapongeza kwa kupata uongozi mpya wa Shirikiho hilo na kuwasisitizia kujenga mahusiano ya karibu na wadau wa soka ikiwemo kuwajengea uwezo vijana ili kukuza vipaji vyao na hatimaye kuleta heshima kwa Taifa.

“TFF hongereni kwa kazi kubwa na nzuri mnayoifanya, hakika mnajitahidi sana lakini niwaombeni muzidi kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha kwamba tunapata maendeleo mazuri katika soka, hivyo ni vema mkawa mnajenga mawasiliano na Viongozi wa Serikali mara kwa mara ili na sisi tupate kujua mambo yanayofanyika”, alisema Mhe. Wambura.

Sambamba na hilo, Naibu Waziri Wambura amesisitiza juu ya suala la ugawaji wa vifaa vya michezo ikiwemo mipira ya kuchezea katika maeneo mbalimbali nchini huku akisema kuwa, ugawaji huo uwe wa uwiano sawa ili pasitokee eneo moja likawa linakosa vifaa hivyo kwakuwa vijana wote ni Watanzania na wana haki sawa ya kushiriki katika michezo.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Shirikisho hilo, Bw. Kidao Wilfred amesema kwamba, TFF imejitahidi kuwasaida vijana mbalimbali wakiwemo Serengeti Boys kwa kuwapatia vitendea kazi na amepokea ushauri wa Naibu Waziri wa kuendelea kujenga uhusiano wa karibu na Serikali ili kukuza soka nchini.

“TFF tumekuwa tukiwaandaa vijana mbalimbali ili kuweza kuwapata wenye vipaji vizuri na tumepanga kuwa vijana hawa waweze kupatiwa shule ambapo watakuwa wanajifunza masuala mazima ya soka na nikieleze tu Mheshimiwakwamba ushauri wako wa kujenga ushirikiano na Serikali tumeupokea na tunaufanyia kazi”, alisema Wilfred.

Monday, September 18, 2017

SIMBA YAIBAMIZA MWADUI MABAO 3-0



Mshambuliaji wa kimataifa kutoka Uganda Emmanuel Okwi ameendelea kuweka rekodi yake baada ya kufunga magoli mawili wakati Simba ikiilaza Mwadui FC jumla ya magoli 3-0 Mchezo uliochezwa kwenye uwanja wa Uhuru maarufu kama Shamba la bibi jijini Dar es salaam.

Okwi amecheza mechi mbili akiwa na Simba na tayari amefikisha jumla ya magoli 6 baada ya ufunguzi kufunga magoli 4 wakati Simba ilipoidungua Ruvu Shooting jumla ya magoli 7-0 yaani wiki.
 

Okwi alianza kuwanyanyua mashabiki wa Simba dakika ya saba baada ya kupokea pokwiasi toka kwa winga Shiza Kichuya na kupiga shuti la mita 20 na kumuacha hoi Golikipa wa Mwadui,Arnold Massawe ambaye alionekana kutokuwa makini mara nyingi alikuwa anatoka toka golini.
 

Mwadui pamoja na kumiliki vizuri mpira walipopata nafasi, lakini hawakuwa na mipango kabisa ya kuipenya ngome imara ya Simba chini ya mabeki wa timu za taifa za Uganda na Tanzania, Juuko Murshid na Salim Mbonde hadi mapumziko Simba walikuwa mbele kwa goli 1-0.
 

Kipindi cha pili nyota ya Simba iliendelea kung’ara na dakika ya 67, Okwi tena akawainua vitini mashabiki wa Wekundu wa Msimbazi kwa kufunga la pili kwa shuti la umbali wa mita zisizopungua 20 baada ya pasi ya beki Mohammed Hussein ‘Tshabalala’.
 

Mashabiki wa Simba walizomea mabadiliko yaliyofanywa na kocha Mcamroon, Joseph Marius Omog mara mbili kwanza akimtoa Mghana Nicholaus Gyan na kumuingiza Mwinyi Kazimoto dakika ya 61 na baadaye akimtoa Kichuya na kumuingiza Mrundi, Laudit Mavugo dakika ya 65 wakionekana kabisa kutaka mshambuliaji John Bocco ndiye atolewe.
 

Bocco akawaonyesha mashabiki wa Simba kwamba Omog alikuwa sahihi katika mabadiliko yake kwa kufunga bao la tatu dakika ya 72 kwa shuti la umbali wa mita 20 na zaidi pia.
 

Baada ya kucheza mechi tatu wakiwa jijini Dar es salaam wekundu wa Msimbazi Simba  watasafri kwenda kanda ya Ziwa ambapo watacheza mechi mbili ya kwanza watacheza kwenye uwanja wa CCM Kirumba na wenyeji timu ya Mbao FC na baadaye wakwenda mkoani Shinyanga kucheza na Stand United.

YANGA YABANWA MBAVU NA MAJIMAJI


Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania timu ya Yanga wameshindwa kutamba kwenye uwanja wa Maji Maji Mjini Songea baada ya kulazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na wenyeji wana rizombe MajiMaji.

Mpira ulianza kwa kasi huku Yanga wakionekana kulishambulia lango la MajiMaji kama washambuliaji akina Ngoma,Ajib pamoja na Chirwa wangekuwa makini wangetoka kipindi cha pili na bao hadi mapumziko timu zote zilikwenda sare ya bila kufungana.

Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote kufanya mabadiliko na MajiMaji waliongeza umakini na kulishambulia lango la Yanga kama Nyuki na kunako dakika ya 54 Mshambuliaji wa zamani wa Mbeya City Peter Mapunda aliwanyanyua mashabiki wa Maji Maji baada ya kufunga goli safi kwa kumzidi maaarifa beki kisiki wa Yanga Kelvin Yondani.

Kuingia kwa bao hili liliwachanga Mabingwa hao watetezi na kuanza kuliandama lango la Maji Maji dakika ya 81 Mshambuliaji wa Kimataifa Donald Dombo Ngoma aliisawazishia bao Yanga kwa kichwa akipokea krosi ya Obrey Chirwa na kumuacha Mlinda Mlango wa Zamani wa Simba,Andrew Ntalla akiruka bila majibu.

Dakika ya 84 Yanga walipata pigo baada ya winga wao hatari , Emmanuel Martin aliumia na kukimbizwa hospitali  baada ya kugongana na mchezaji wa Maji Maji, Marcel Kaheza.

Hadi Mwamuzi anamaliza Mpira timu zote zimeweza kugawana pointi moja moja na kwa matokeo hayo Yanga wamefikisha alama tano wakiwa wamecheza mechi tatu na wanatarajia kurudi jijini Dar es salaam baada ya kucheza mechi mbili ugenini na watakuja kuvaana na timu ya Mtibwa Sugar ya Morogoro kwenye uwanja wa Uhuru.

Monday, September 11, 2017

YANGA YAZINDUKIA NJOMBE




Mabingwa Watetezi Wa Ligi Kuu Vodacom Tanzania bara baada ya kuibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya wenyeji Njombe Mji ,Mchezo uliopigwa katika uwanja wa Saba Saba uliopo Mjini Njombe.

Mshambuliaji hatari wa Zamani wa Simba,Ibrahim Ajibu Migomba aliwanyanyua mashabiki wa Yanga baada ya kufunga goli maridadi kunako dakika ya 16 kwa shuti la Faulo ambalo sawa na umbali wa mita 30 lililoenda moja kwa moja na kumuacha Mlinda Mlango wa Njombe Mji hana la kufanya.

Huu ni ushindi wa kwanza kwa George Lwandamina msimu mpya wa Ligi baada ya mchezo wa kwanza kulazimishwa sare ya kufungana goli 1-1 dhidi ya Lipuli Fc mchezo ambao ulipigwa uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam.

Yanga waliongeza kasi ya mashambulizi baada ya bao hilo, lakini hawakuwa na bahati ya kufunga zaidi kutokana na kushindwa kutumia vizuri nafasi walizotengeneza.
 
Yanga  walitawala vizuri mchezo kipindi chote cha kwanza na wangeweza kuvuna mabao zaidi kama wangekuwa makini katika utumiaji wa nafasi ambazo walizipata
 
Kipindi cha pili kilibadilika kidogo na vijana wa Hassan Banyai wakaanza kuwavimbia mabingwa watetezi wa Ligi Kuu walio chini ya kocha Mzambia, George Lwandamina.
 
Sifa zimuendee kipa Mcameroon wa Yanga, Youthe Rostand aliyeokoa michomo mingi ya hatari kipindi hicho cha pili na kuinusuru timu yake kufungwa.
 
Katika kipindi hicho, beki wa Njombe Mji, Remmy Mbuligwe alikimbizwa hospitali baada ya kuumia kufuatia kugongana na beki wa Yanga Juma Abdul.

Awali ya hapo, Yanga nayo ilipata pigo baada ya kiungo wake Mzimbabwe, Thabani Kamusoko kuumia na kushindwa kuendelea na mchezo, nafasi yake ikichukuliwa na Raphael Daudi dakika ya 49.   
 
Katika mechi nyingine za leo; Lipuli FC imeilaza 1- 0 Stand United, Mbeya City imefungwa nyumbani 1-0 na Ndanda FC, Singida United imeifunga 2-1 Mbao FC, Kagera Sugar imelazimishwa sare ya 1-1 Ruvu Shooting, Mtibwa Sugar imeshinda 1-0 dhidi ya FC Mwadui.

Kikosi cha Njombe Mji kilikuwa; David Kisu, Agaton Mapunda, Remmy Mbuligwe, Laban Kamboole, Peter Mwangosi, Joshua John, Awadh Salum, Hassan Kapalata/Behewa Sembwana dk80, Notikeli Masasi, Ditrim Nchimbi na David Nakpa/Raphael Siame dk47.

Yanga SC; Youthe Rostand, Juma Abdul, Gardiel Michael, Andrew Vincent, Kevin Yondan, Papy Kabamba Tshishimbi, Juma Mahadhi, Thabani Kamusoko/Raphael Daudi dk49, Donald Ngoma/Obrey Chirwa dk56, Ibrahim Hajib na Emmanuel Martin/Yussuf Mhilu dk70.

SIMBA, AZAM HAKUNA MBABE


KLABU Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, imetoka sare ya bila kufungana dhidi ya Simba katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) uliofanyika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Huo ni mchezo wa kwanza wa kihistoria kwa timu hiyo kuweza kucheza katika uwanja wake wa nyumbani dhidi ya Simba, ambao ulitawaliwa kwa ubabe kwa pande zote mbili huku Refari akionesha kadi za njano kama jungu.

Ulikuwa ni mchezo wa kugawana vipindi, ambapo Azam FC ilionekana kutawala kipindi cha pili huku wapinzani wao wakitawala kipindi cha kwanza na pande zote zikikosa mabao.

Winga wa Azam FC, Enock Atta, alipiga shuti la umbali dakika ya 18 lilidakwa na kipa wa timu hiyo, Aishi Manula, ambaye alikuwa akirejea kwa mara ya kwanza Azam Complex tokea asajiliwe na Simba msimu huu akitokea kwa mabongwa hao,

Wachezaji wengine waliokuwa wakirejea ndani ya viunga hivyo, ni gwiji wa Azam FC John Bocco ‘Adebayor’ na Erasto Nyoni, waliosajiliwa pia wakitokea kwa mabingwa hao wa Afrika Mashariki na Kati.

Dakika ya 33 Atta alimsetia pasi nzuri Yahaya Mohammed, alliyeingia na mpira huo ndani ya eneo la 18 lakini shuti alilopiga lilitoka sentimita chache ya lango na kuufanya mchezo huo kumaliza kipindi cha kwanza kwa suluhu hiyo.

Mabadiliko yaliyofanywa na benchi la ufundi la Azam FC ya kumuingiza kiungo Frank Domayo na kupumzishwa Atta yaliiongezea ubora timu hiyo kwenye eneo la kiungo hali iliyowafanya kutawala mchezo huo.

Dakika ya 63 Azam FC ilipata pigo baada ya beki wake wa kulia, Daniel Amoah, kuumia na nafasi yake kuchukuliwa na Ramadhan Singano ‘Messi’, mabadiliko hayo yalimlazimu nahodha Himid Mao, kuhamia beki wa kulia  na eneo la kiungo kubakia Stephan Kingue, Domayo na Salum Abubakar ‘Sure Boy’.

Dakika 10 za mwisho za mchezo huo, Yahaya Mohammed na Sure Boy, almanusura waipatie mabao Azam FC, lakini shuti alilopiga kiungo huyo lilitoka sm chache ya lango na kichwa alichopiga Yahaya kiliweza kudakwa na kipa.

Sare hiyo inaifanya Azam FC kupata pointi moja na kufikisha jumla ya pointi nne ikisogea hadi nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi hiyo sawa na Tanzania Prisons na Simba zilizokuwa juu yake kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa.

Mara baada ya mchezo huo, kikosi cha Azam FC kitapumzika kesho Jumapili kabla ya kurejea mazoezini Jumatatu jioni tayari kabisa kujiandaa na mtanange ujao dhidi ya Kagera Sugar, utakaofanyika Uwanja wa Azam Complex Septemba 15 saa 1.00 usiku.

JEFF AKABIDHIWA UKURUGENZI SIKINDE



UONGOZI wa bendi ya muziki wa dansi ya Mlimani Park Orchestra (Sikinde), umemteua mwanamuziki mkongwe na mpiga drums nguli nchini, Habibu Abbas 'Jeff' kuwa mkurugenzi wa bendi.

Uteuzi huo umelenga kuuimarisha uongozi wa bendi, hasa katika masuala ya udhibiti wa mapato na matumizi ya fedha na nidhamu kwa wanamuziki.

Mmoja wa viongozi waandamizi wa bendi hiyo, Hassan Bitchuka, alisema jana kuwa, uteuzi huo ulifanywa wakati bendi hiyo ilipokuwa ziarani nchini Kenya, mwezi uliopita.

"Katika bendi yetu kumekuwa na matatizo makubwa ya utovu wa nidhamu kwa wanamuziki, hivyo tumemteua Jeff kuwa mkurugenzi kwa lengo la kudhibiti vitendo hivyo," alisema mwanamuziki huyo mkongwe.

"Baadhi yetu sisi ni wapole na huwa tuna huruma sana linapokuja suala la kumchukulia hatua mwanamuziki anayeonyesha vitendo vya utovu wa nidhamu mara kwa mara. Lakini sasa tunaamini Jeff ataimudu kazi hiyo kwa sababu hana woga,"aliongeza.

Kwa mujibu wa Bitchuka, hiyo ndio itakayokuwa kazi na majukumu ya Jeff na kwamba shughuli za viongozi wengine zitaendelea kama kawaida.

Mbali na Jeff, viongozi wengine wa Mlimani Park kwa sasa ni Abdalla Hemba, ambaye ni kiongozi mkuu na Mjusi Shemboza, ambaye ni katibu wa bendi. Bitchuka ni kiongozi mwandamizi.

Akizungumzia uteuzi huo, Jeff alisema ameupokea kwa mikono miwili na atashirikiana na viongozi wenzake kuhakikisha kuwa, bendi hiyo inapata mafanikio makubwa zaidi.

"Ni kweli nimeteuliwa kuwa mkurugenzi wa bendi, nitakayeshughulikia nidhamu na kusimamia mapato na matumizi na mikataba yote itakayoingiwa na bendi,"alisema Jeff.

Hii ni mara ya pili kwa Jeff kuteuliwa kwenye uongozi wa bendi hiyo. Katika uongozi uliopita, Jeff alikuwa kiongozi mkuu huku Hamisi Milambo akiwa katibu wa bendi na Ramadhani Mapesa akiwa mtunza hazina.

WITNESS: NAJIVUNIA NA KUUTHAMINI UTANZANIA WANGU






MSHINDI wa taji la Miss Garden Route 2017/2018, lililoshindaniwa nchini Afrika Kusini, Witness Kavumo, amesema anaona fahari na kujivunia kuwa Mtanzania na pia kuonyesha uzalendo kwa nchi yake.

Amesema licha ya kukabiliwa na changamoto nyingi kwa muda wote aliokuwa akisoma Afrika Kusini, ikiwemo ubaguzi wa rangi, amekuwa akikabiliana nazo kwa kujivunia rangi yake na utaifa wake.

Witness (21), amesema katika shindano hilo lililoandaliwa na Kampuni ya The Role Models Foundation, ikishirikiana na Gemini Modelling Agency', alikuwa mshiriki pekee mweusi. Shindano hilo liliwashirikisha mabinti 600 katika hatua za awali.

Amesema baada ya mchujo wa awali, alikuwa miongoni mwa warembo 12, waliotinga fainali na hatimaye kuibuka mshindi, ambapo alizawadiwa Randi 4,000 za Afrika Kusini, sawa na sh. 640,000.

Shindano hilo, ambalo washiriki wengi walikuwa wazungu, lilifanyika Mei 6, mwaka huu, katika mji wa George, Afrika Kusini.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma, hivi karibuni, Witness alisema alikwenda Afrika Kusini kwa ajili ya masomo, lakini alipenda kutumia muda wake wa ziada kujihusisha na masuala ya urembo.

Binti huyo mzaliwa wa mkoa wa Arusha, amesema washindani katika hatua ya mwisho waliwapa wakati mgumu majaji kutokana na kuwa na mvuto na uchangamfu, lakini hatimaye aliibuka mshindi.

Licha ya kuwa ugenini, Witness anasema alishiriki katika shindano hilo akijitambulisha kuwa ni Mtanzania na baada ya kushinda, ameamua kuja kujitambulisha katika Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo ili serikali imtambue.

"Nilikutana na vikwazo vingi, ikiwemo ubaguzi wa rangi na kukosa ushirikiano hata kwa Watanzania wenzangu, lakini nilikabiliana navyo na hatimaye nikaibuka mshindi," amesema binti huyo anayezungumza kwa kujiamini.

Amewataka wanawake wenzake kusimama imara, kujiamini na kukabiliana na vikwazo vyote wanavyokumbana navyo katika maisha, bila kujali wapo nyumbani au ugenini kwa sababu hakuna linaloshindikana.

"Nauthamini na kujivunia utanzania wangu ndio sababu nilifanikiwa kushinda," amesema binti huyo.

Witness amesema anawashukuru wazazi wake kwa kumuunga mkono na kumpa moyo wa kushiriki kwenye mashindano mbalimbali ya urembo, yakiwemo ya vyuo vikuu mkoani Arusha, ambapo aliibuka mshindi akiwa na umri wa miaka 18.

Kutokana na kuibuka mshindi wa shindano la Miss Garden Route, Witness amepata mkataba wa kufanyakazi za urembo chini ya udhamini wa kampuni za The Role Models Foundation na Gemini Modelling Agency.

Witness anasema japokuwa zawadi aliyopata kwa kushinda shindano hilo ni ndogo, lakini anajisikia faraja kupata mkataba wa udhamini wa kufanyakazi ya urembo na kampuni hizo mbili za Afrika Kusini.

Akizungumzia ushindi wa binti huyo, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Anastazia Wambura, amewataka vijana nchini kutumia muda vizuri na mazingira yanayowazunguka ili kufikia azma ya malengo waliyojiwekea katika kujiletea maendeleo yao na taifa kwa ujumla.

Naibu Waziri Anastazia alitoa kauli hiyo alipokuwa akimpongeza Witness, ambaye pia alitambulishwa kwa wabunge, katika moja ya vikao vya bunge vinavyoendelea mjini Dodoma.

“Ni dhahiri umetumia ujuzi, ubunifu, sanaa, imani, bidii, desturi, maadili na sheria, ambavyo umevipata  kutoka kwa familia, jamii ya Kitanzania na pia kwa jamii ya watu wa  Afrika Kusini,” amesema Anastazia.

“Vijana wa Kitanzania, Witness  amewaonesha njia, mjenge utamaduni wa kupambana na mazingira ili kufikia azma mnazojiwekea,” amesisitiza Naibu Waziri.

Aidha, amesema mrembo huyo ameonyesha uzalendo kwa nchi yake, kwa kuamua kwenda Dodoma na kutoa taarifa ya mafanikio yake kama Mtanzania, kutokana na ushindi alioupata katika mashindano hayo ya ubunifu.

Amesema hatua hiyo inaonyesha kuwa Witness ameumeuthamini Utanzania wake na kuonyesha kujali kutumia muda wa ziada katika masuala ya fani ya urembo licha ya kwamba, jukumu lake la msingi nchini humo ni masomo.

Naibu Waziri amesema fani ya ubunifu na mitindo inatambulisha utamaduni, kuongeza kipato, kuinua uchumi na kukuza utalii kwa kuongeza juhudi, maarifa na kufanyakazi kwa bidii, hatua ambayo inaleta matokeo mazuri yenye tija.

Amemshauri Witness, kutumia bidhaa zenye asili ya Tanzania katika fani yake ili kuzitangaza katika soko la ndani na la nje, kuvutia utalii, kuingiza kipato na  kukuza uchumi katika ngazi zote za mnyororo wa thamani katika sekta ya ubunifu wa mavazi na mitindo, kwake yeye binafsi na kwa Taifa.

Friday, September 8, 2017

TFF YATANGAZA KAMATI YA TUZO



Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia ameunda Kamati ya Tuzo za Ligi Kuu ya Vodacom  Tanzania Bara msimu wa 2017/18.

Kamati hiyo itaongozwa na Mwenyekiti Ahmed Mgoyi wakati Makamu Mwenyekiti ni Almas Kasongo ilihali  Amiri Mhando ameteuliwa kuwa Katibu wa kamati hiyo ya tuzo.

Mhando ni Mhariri wa Gazeti la Spotileo linalotolewa na Kampuni ya Magazeti ya Serikali - Tanzania Standard Newspaper (TSN).

Wajumbe ambao wameteuliwa ni Ibrahim Kaude; Mkuu wa Kitengo cha Michezo katika Kampuni ya Azam Media, Patrick Kahemele na Kocha mkongwe wa soka, Kenny ‘Mzazi’ Mwaisabula.

Kadhaika Mhariri Mtendaji wa Kampuni ya Uchapishaji ya Global (Global Publisher inayochapisha magazeti kadhaa likiwamo Championi), Saleh Ally; Mtangazaji mahiri wa michezo kutoka Kituo cha Redio cha EFM, Ibrahim Masoud na Mtangazaji wa Vipindi katika Kituo cha Radio ya Watu, Fatma Likwata.

Pia wamo Mwandishi Mwandamizi wa Michezo wa Gazeti la Mwanaspoti linalochapishwa na Kampuni ya Mwananchi Communication (MCL), Gift Macha; Katibu Mkuu wa Chama cha Wachezaji wa Mpira wa Miguu, Said George na Mhariri wa Michezo wa Gazeti la HabariLeo linalotolewa na TSN, Zena Chande.

TAARIFA KUHUSU WA WAAMUZI TANZANIA


Kamati ya Utendaji ya Chama cha Waamuzi wa Mpira wa Miguu Tanzania (FRAT) ilikuwa na kikao chake cha kwanza kilichofanyika Julai 6, 2017 hapa jijini Dar es Salaam.
 
Mambo muhimu yafuatayo yalitolewa uamuzi.


1. Kumpongeza Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania, Bw. Wallace Karia na Makamu wa Rais, Bw. Michael Wambura pamoja na Wajumbe wote wa Kamati ya Utendaji ya TFF kwa kuchaguliwa kwao.


2. Tumesimamisha kozi zote kwa waamuzi wapya kuanzia Septemba 7, mwaka huu. Mitihani iliyokwishafanywa kabla ya Septemba 7, mwaka huu ni halali na itumwe kwa Katibu Mkuu wa FRAT - Taifa mara moja ikiambatanishwa na ada zake.


3. Makatibu wote wa FRAT - Mkoa kwa mikoa yote ya Tanzania Bara wakumbushwe majukumu yao kwani inaonekana ni kama wamepitiwa ikiwa ni pamoja na kutuma kwa Katibu Mkuu FRAT - Taifa orodha ya waamuzi wote wa madaraja yote walio hai kwa kuchezesha na walio hai kiuanachama.


4. Tumekumbusha waamuzi kuwa na darasa la mara moja kwa wiki lijulikanalo kama ‘Sunday Class’ madarasa hayo yawe kila Makao Makuu ya Mkoa na Makao Makuu ya Wilaya.


5. Tumekubaliana uchaguzi mdogo ufanyike wakati wa mapumziko ya ligi ya wiki mbili za mwezi Januari. Tayari tumewasiliana na na Kamati ya Uchaguzi.


6. Kuwaleta pamoja waamuzi (wanachama) wote nchini bila kujali umri.


7. Kuendelea kuzalisha waamuzi wapya toka kwenye shule za sekondari, vyuo na nje ya shule za sekondari na vyuo kwa wenye sifa.


8. Kuboresha mafunzo na upandaji wa madaraja kwa waamuzi wenye madaraja.


9. Kukemea na Kupambana na rushwa kwa waamuzi hadharani kwa kushirikiana na TFF na Takukuru.


10. Kutetea kwa nguvu zote haki za waamuzi.


11. Kuboresha mawasiliano kwa ngazi zote na kwa mwanachama ye yote.


12. FRAT kiwe chama cha mfano kwa wanachama wake kwa kuwa na maadili mema, yanayompendeza Mungu.


13. Misingi kumi ya “FIFA FAIR PLAY” ni msingi wa maendeleo ya mwamuzi.


14. Wote kwa pamoja tukatae rushwa na tuiangamize rushwa kwa maendeleo ya mpira wetu.

SIMBA, AZAM KUONYESHANA UBABE LEO, PAMBANO KUANZA SAA 10 JIONI


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), limefanya mabadiliko kidogo ya muda wa kuanza mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, kati ya Azam FC na Simba SC.
 
Mchezo huo utafanyika kesho Jumamosi Septemba 9, 2017 kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, nje kidogo ya jiji la Dar es Salam kama ulivyopangwa awali.


Kuhusu muda, mchezo huo ulipangwa ufanyike kuanzia saa 1.00 usiku, lakini sasa utaanza saa 10.00 jioni - uamuzi uliofanyika baada ya kupokea ushauri kutoka Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Dar es Salaam, chini ya Mwenyekiti wake, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Paul Makonda.


Mbali ya mchezo huo, mechi nyingine ya kesho Jumamosi Septemba 9, mwaka huu  itakuwa ni kati ya Tanzania Prisons na Majimaji ya Songea uliopangwa kufanyika Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.


Mechi nyingine za Ligi Kuu ya Vodacom, zitakuwa Jumapili Septemba 10, mwaka huu ambako Njombe Mji FC na Young Africans SC zitacheza Uwanja wa Sabasaba mjini Makambako wakati Mtibwa Sugar FC na Mwadui FC ya Shinyanga kwenye Uwanja wa Manungu mkoani Morogoro.


Kadhalika Lipuli FC itacheza na Stand United FC Uwanja wa Samora mjini Iringa wakati Singida United itacheza na Mbao kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.


Pia Kagera Sugar itacheza na Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba huku Mbaya City ikiwa wenyeji wa Ndanda ya Mtwara kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania linapenda kuwatangazia wananchi kuwa viingilio katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kati ya Azam na Simba.

Viingilio vitakuwa shilingi elfu kumi (Sh 10,000) kwa Jukwaa Kuu ambalo lina uwezo wa kubeba mashabiki 1,000 tu walioketi, wakati mzunguko (popular) kiingilio kitakuwa ni shilingi elfu saba tu (Sh 7,000).

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania linapenda kuwatangazia wanafamilia ya mpira wa miguu kukata tiketi kuanzia leo Jumatano Septemba 6, mwaka huu ili kujiepusha na usumbufu wa aina yoyote.

Kadhalika tunapenda kuwatangazia wananchi kwamba kwa ye yote ambaye hana tiketi ni vema wasiende uwanjani kwani ujio wake hautakuwa na tafasiri nyingine zaidi ya kuonekana kuwa ni mleta fujo.

Vyombo vya usalama vitakuwa makini kudhibniti kila aina ya vurugu uwanjani hapo hasa ikizingatiwa kuwa mchezo huo utafanyika wakati jua limezama.

WALIOPITISHWA KUWANIA UONGOZI BODI YA LIGI WATAJWA


Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), imepitisha majina ya wagombea wafuatao kuwania uongozi katika  nafasi mbalimbali katika uchaguzi wa Kamati ya Uongozi wa Bodi ya Ligi Kuu.

Majina hayo yamepitishwa mara baada ya kuwafanyia usaili uliofanyika Jumapili Septemba 3, mwaka huu kwenye Ukumbi wa TFF, Dar es Salaam. Uchaguzi Mkuu wa Kamati ya Uongozi wa Bodi ya Ligi utafanyika Oktoba 15, mwaka huu.

Kwa mujibu wa ratiba ya uchaguzi inayotokana na kanuni za uchaguzi za TFF, majina hayo yanapaswa kutangazwa sasa.

Waliopita na majina yao kutangazwa ni Clement Sanga na Hamad Yahya wanaowania uenyekiti wakati Shani Christoms amepitishwa kuwania nafasi ya Makamu Mwenyekiti.

Wanaowania nafasi ya ujumbe wako Hamisi Madaki na Ramadhani Mahano. Hawa wamepitishwa kuwania nafasi hizo kutoka Klabu za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.

Pia wamo Almasi Kasongo ambaye anawania nafasi hiyo  kupitia Klabu za Ligi Daraja la Kwanza wakati Edgar Chibura anawania nafasi ya ujumbe kupitia Klabu za Ligi Daraja la Pili. James Bwire yeye hakupitishwa kwa sababu hakufika kwenye usaili.

LIGI NDOGO YA WANAWAKE KUANZA KARIBUNI


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), limeagiza Makatibu wa Vyama vya Mikoa kutuma haraka majina ya timu mabingwa wa mikoa wa soka la wanawake wa msimu wa 2016/17.

Viongozi wa mikoa wamekumbushwa kutuma timu ili kufanya maandilizi ya haraka ya Ligi Ndogo itakayofanyika Septemba 22 hadi 29, mwaka huu.

Ligi Hiyo ndogo inachezwa kutafuta timu mbili zitakazopanda daraja kucheza Ligi Kuu soka ya wanawake msimu wa 2017/2018.

Huu ni msimu wa pili wa ligi ya wanawake kwani msimu uliopita, timu shiriki zilikuwa 12 na Mlandizi Queens ya Pwani iliibuka bingwa wa kwanza katika historia ya soka hapa nchini.

Mara baada ya kumalizika kwa Ligi Ndogo, TFF itaanza taratibu za kupanga kuanza kwa Ligi Kuu kwani wakati huo tayari tutafahamu timu ambazo zimepanda. Ligi Ndogo haitahusisha timu ambazo zimecheza Ligi Kuu msimu wa 2016/17.

Monday, September 4, 2017

TAIFA STARS YAICHAPA BOTSWANA MABAO 2-0, MSUVA APIGA ZOTE MBILI



MABAO mawili ya winga mpya wa klabu ya Difaa Hassan El- Jadida yameipa Tanzania ushindi wa 2-0 dhidi ya Botswana katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa jioni ya leo Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Msuva aliyejiunga na timu ya Ligi Kuu ya Morocco mwezi uliopita leo alikuwa mwiba kwa safu ya ulinzi ya The Zebras na amefunga bao moja kila kipindi mbele ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe.
Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Elly Sasii aliyesaidiwa na Soud Lila na Frank wote wa Tanzania, hadi mapumziko Taifa Stars walikuwa mbele kwa bao 1-0.
Simon Msuva alipokea pasi ndefu ya kiungo Hamisi Abdallah wa Sony Sugar ya Kenya, akaikontroo vizuri  na kumpasia kiungo wa Simba, Muzamil Yassin kabla ya kuiombea mbele na kuingia nayo kwenye boksi kwa kasi na kufumua shuti kali lililompita kama upepo kipa wa The Zebras, Mwambule Masule dakika ya sita.
Katika kipindi hicho, ilishuhudiwa Taifa Stars wakicheza vizuri zaidi na kutengeneza nafasi chache za kufunga, ambazo hata hivyo walimudu kuitumia vizuri moja tu kupata bao.
Mashambulizi ya Taifa Stars leo ambayo katika benchi la Ufundi imeongezewa nguvu na mchezaji wa zamani, Amy Ninje aliyecheza hadi Uingereza Ligi za Madaraja ya chini na kocha wa zamani wa Azam, Dennis Kitambi ambaye kwa sasa anafundisha AFC Leopards ya Kenya.
The Zebras nao hawakuwa wanyonge kabisa uwanjani, kwani walipeleka mashambulizi langoni mwa Taifa Stars na kukaribia kufunga mara mbili kama su uhodari wa kipa wa Simba, Aishi Salum Manula.
Kipindi cha pili, Zebras walirudi kwa nguvu na kuanza kusukuma mashambulizi mfululizo langoni mwa Taifa Stars, lakini safu ya ulinzi ikiongozwa na mkongwe Kevin Yondan ilikuwa imara kudhibiti hatari zote.
Hatimaye Msuva akawainua tena vitini mashabiki wa nyumbani kwa kufunga bao la pili dakika ya 63 baada ya kugongeana vizuri na winga wa Simba SC, Shiza Ramadhani Kichuya.
Nahodha, Mbwana Samatta anayechezea KRC Genk ya Ubelgiji alicheza vizuri pamoja na kudhibitiwa vikali na akakaribia kufunga mara mbili – unaweza kusema bahati haikuwa ya kwake leo.
Kiungo wa Tenerife ya Hispania, Farid Mussa na mshambuliaji wa Dhofar ya Oman wote waliingia kipindi cha pili na wakacheza vizuri sawa na chipukizi, Emmanuel Martin wa Yanga aliyempokea Msuva.
Kikosi cha Tanzania kilikuwa; Aishi Manula, Erasto Nyoni, Gardiel Michael, Abdi Banda, Kevin Yondan, Himid Mao, Simon Msuva/Emmanuel Martin dk82, Hamisi Abdallah/Said Ndemla dk80, Muzamil Yassin/Raphael Daudi dk57, Mbwana Samatta/Elias Maguri dk82 na Shiza Kichuya/Farid Mussa dk66.
Botswana; Mwambule Masule, Mosha Gaolaolwe/Jackson Lesole dk74, Edwin Olerile/Tmisang Orebonye7 dk4, Simisami Mathumo, Lopang Mogise, Alphonce Modisaotsile, Maano Ditshupo/Katlego Masole dk70, Gift Moyo, Segolame Boy, Kabelo Seakanyeng na Ontireste Ramatlhakwana.
IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA BIN ZUBEIRY

BODI YA WADHAMINI TFF YAKUTANA NA UONGOZI MPYA



Bodi ya Wadhamini wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania, imekutana na viongozi wakuu wa Shirikisho katika Ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Sea Scape, Kunduchi, Dar es Salaam.

Bodi hiyo imekutana na uongozi wakuu wa TFF jana Septemba 2, mwaka huu kwa mara ya kwanza tangu ithibitishwe na Mkutano Mkuu wa TFF.

Madhumuni ya Bodi hiyo kukutana na viongozi wa TFF  - Rais Wallace Karia; Makamu wa Rais, Michael Wambura na Kaimu Katibu Mkuu, Kidao Wilfred ni kufahamiana.

Kwa upande wa Bodi walikuwa Mhe. Mohammed Abdulaziz, Mhe. Balozi Dk. Ramadhani Dau, Mhe. Abdallah Bulembo na Mhe. Stephen Mashishanga. Mjumbe Dk. Joel Bendera hakuhudhuria kwa udhuru.

Kadhalika Bodi hiyo kwa mujibu wa katiba ya TFF, walipata nafasi ya kuchagua Mwenyekiti wa Bodi ambako Mhe. Mohammed Abdulaziz alichaguliwa kushika wadhifa huo. Mhe. Abdulaziz alikuwa Mlezi wa timu ya Daraja la Kwanza ya Kariakoo ya Lindi

Kwa niaba ya Wajumbe wa Bodi, Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Mhe. Mohammed Abdulaziz ambaye ni Mbunge wa zamani wa Jimbo la Lindi Mjini, aliupongeza uongozi mpya wa TFF ulioingia madarakani Agosti 12, mwaka huu akisema: “Mmeanza vizuri.”

Kadhalika Mwenyekiti ambaye alipata kuwa Mkuu wa Mikoa ya Tabora, Tanga na Iringa kwa nyakati tofauti , aliahidi ushirikiano kwa uongozi wa TFF ambako kwa upande wa TFF, Rais Karia alipokea pongezi hizo na baraka tele za kuanza vema na ushirikiano.

Mhe. Balozi Dk. Dau - alikuwa Mkurugenzi wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), ni mwanafamilia ya mpira wa miguu aliyejitolea hata kwa nguvu zake binafsi kusaka vipaji vya mpira wa miguu kwa vijana.

Mhe. Joel Bendera ni Mkuu wa Mkoa wa Manyara. Ni Kocha wa zamani wa timu ya Tanzania ‘Taifa Stars’ aliyekuwa na mchango mkubwa kuifikisha kucheza fainali za Kombe la Mataifa Huru ya Afrika (CAN 1980) sasa michuano hiyo inafamika kwa jina la AFCON. Fainali za mwaka 1980 zilifanyika Lagos, Nigeria.

Mhe. Stephen Mashishanga ni Mkuu wa zamani wa Morogoro mwenye historia nzuri ya unafamilia wa mpira wa miguu akitoa mchango mkubwa katika maendeleo tangu alipokuwa kiongozi hadi sasa. Pia alipata kuwa Mlezi wa timu ya Milambo ya Tabora iliyoshiriki Ligi Kuu Bara.

Mhe. Abdallah Bulembo ni Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Tanzania ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), aliyepata kuwa Makamu Mwenyekiti wa kilichokuwa Chama cha Mpira wa Miguu Tanzania (FAT).