KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, August 30, 2016

TANZANIA BARA YAPANGWA KUNDI MOJA NA ETHIOPIA, RWANDA CHALENJI YA WANAWAKE


TANZANIA imepangwa kundi B pamoja na Ethiopia, Tanzania na Rwanda katika michuano ya ubingwa wa wanawake kwa mataifa ya Afrika Mashariki na Kati.


Katibu wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Nicholas Musonye amewaambia Waandishi wa Habari katika mkutano wa utambulisho wa Challenge hiyo ya wanawake mjini kampala, Jumatatu kwamba, Uganda watakuwa wenyeji wa michuano hiyo.


Katika sherehe za utambulisho wa michuano hiyo iliyofanyika makao makuu ya Shirikisho la Soka Uganda (FUFA), Musonye alisema nchi saba zimethibitisha kushiriki Challenge hiyo ya kwanza ya wanawake, itakayofanyika Jinja.


Mbali za Tanzania, Ethiopia na Rwanda Kundi A linaundwa na timu za Uganda, Kenya, Burundi, na Zanzibar na michuano itaanza Septemba 11 hadi 20, 2016.



PAMBANO LA YANGA, JKT RUVU LASOGEZWA MBELE



Bodi ya Ligi Kuu (TPLB) ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), imethibitisha kuwa mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Young Africans ya Dar es Salaam na JKT Ruvu ya Pwani, ulipangwa kufanyika Jumatano Agosti 31, 2016 kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam imeahirishwa mpaka itakapopangiwa tarehe nyingine.

Mechi hiyo imeondolewa kutokana na timu ya Young Africans kuwa na wachezaji wengi kwenye kikosi cha timu ya Taifa (Taifa Stars) kinachosafiri Agosti 31, 2016 asubuhi kwenda Lagos, Nigeria kwa ajili ya mechi ya mchujo ya michuano ya Kombe la Afrika (AFCON Qualifiers) itakayochezwa Septemba 3, 2016.

Mabadiliko hayo hayatavuruga ratiba ya mechi zinazofuata za Ligi Kuu ya Vodacom kwa timu husika.

Tayari wahusika wakiwamo Young Africans na JKT Ruvu SC, wamejulishwa.

KIPAO ACHUKUA NAFASI YA DIDA KIKOSI CHA STARS



Kocha Mkuu wa timu ya Mpira wa Miguu Tanzania ‘Taifa Stars’, Charles Boniface Mkwasa, amefanya mabadiliko kwenye kikosi kinachotarajiwa kusafiri Jumatano Agosti 31, 2016 kwenda Nigeria kwa ajili ya mchezo wa mwisho wa kuwania kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2017) dhidi ya timu ya taifa ya nchi hiyo, Super Eagles.

Mabadiliko yaliyofanyika ni kwa kumchukua Kipa kinda wa JKT Ruvu, Said Kipao kuchukua nafasi ya Deogratius Munishi ambaye amefiwa na baba yake mzazi katika kifo kilichotokea jijini Dar es Salaam jana Agosti 28, 2016.

Licha ya mchezo huo wa Septemba 3, 2016 kuwa sehemu ya mchuano wa kuwania nafasi ya kucheza fainali hizo za AFCON 2017 huko Gabon, lakini utakuwa ni wa kukamilisha ratiba baada ya Misri kufuzu kutoka kundi G ambalo mbali ya Nigeria na Tanzania, pia ilikuwako Chad ambayo iliyojitoa katikati ya mashindano.

Wachezaji wanaounda kikosi hicho kwa sasa na kuanza kuingia kambini Hoteli ya Urban Rose jijini Dar es Salaam ni:

Makipa-
Said Kipao – JKT Ruvu
Aishi Manula – Azam FC

Mabeki
Kelvin Yondani - Young Africans
Vicent Andrew - Young Africans
Mwinyi Haji - Young Africans
Mohamed Hussein – Simba SC
Shomari Kapombe - Azam FC
David Mwantika - Azam FC

Viungo
Himid Mao - Azam FC
Shiza Kichuya – Simba SC
Ibrahim Jeba – Mtibwa Sugar
Jonas Mkude – Simba SC
Muzamiru Yassin – Simba SC
Juma Mahadhi - Young Africans
Farid Mussa Tenerif ya Hispania

Washambuliaji
Simon Msuva - Young Africans
Jamal Mnyate – Simba SC
Ibrahim Ajib – Simba SC
John Bocco - Azam FC
Mbwana Samatta - CK Genk ya Ubelgiji

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amemtumia salamu za rambirambi Kipa wa Young Africans na timu ya Tanzania ‘Taifa Stars’, Deogratius Munishi kutokana na kifo cha Baba yake mzazi, Mzee Boniventur Munishi kilichotokea jana Agosti 28, 2016.

Rais Malinzi amepokea taarifa za kifo cha Mzee Boniventur Munishi mara baada ya mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) Young Africans na African Lyon uliofanyika jana Agosti 28, 2016 ambako Deogratius aliongoza timu yake Young Africans kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 bila kufahamu kuwa amepoteza baba.

“Ni ujasiri wa aina yake aliokuwa nao Kipa Munishi kwenye mchezo wa Ligi Kuu bila kuonyesha tofauti,” amesema Malinzi ambaye katika zake za rambirambi kwenda kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa na marafiki amewataka kuwa na moyo wa subira wakati huu mgumu wa msiba wa mpendwa wao.

Mwenyezi Mungu aipumzishe roho ya marehemu Mzee Boniventur Munishi mahala pema peponi.

Bwana alitoa, Bwana ametwaa, jina la Bwana lihimidiwe.

Monday, August 29, 2016

YANGA YAISHINDILIA AFRICAN LYON 3-0 LIGI KUU BARA



Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Bara, Yanga SC jana walianza vizuri ligi hiyo baada ya kuishushia kichapo cha mabao 3-0 timu ya African Lyon katika mechi iliyopigwa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Alikuwa Deus Kaseke aliyeanza kuipatia Yanga bao la kwanza baada ya mabeki wa Lyon kujua ameotea katika dakika ya 18 ya mchezo huku Simon Msuva akifunga bao la pili dakika ya 60 akipokea pasi ndefu kutoka kwa Thaban Kamausoko.

Juma Mahadhi alipigilia msumari wa mwisho kwa African Lyon baada ya kuipatia Yanga bao la tatu akipokea pasi safi kutoka kwa Yusuph Mhilu katika dakika ya 90.

Hadi mwisho wa mchezo, Yanga 3, African Lyon 0

Sunday, August 28, 2016

JKT RUVU YAIHENYESHA SIMBA, ZATOKA SULUHU


SIMBA ya jijini Dar es Salaam, jana
ilipunguzwa kasi na maafande wa
JKT Ruvu baada ya kutoka sare
tasa katika mchezo wa Ligi Kuu
Tanzania bara, uliochezwa uwanja wa
Uhuru jijini Dar es Salaam.
Timu zote zilianza pambano kwa
kasi huku washambuliaji wa kila upande
wakifanya juhudi za kutikisa nyavu
dakika za mapema.
Katika dakika ya 10, mshambuliaji
wa Simba Laudit Mavugo, aliikosesha
bao timu yake baada ya mkwaju aliopiga,
kudakwa kiufundi na kipa wa JKT Ruvu.
Nayo JKT Ruvu, ilijibu mapigo dakika
sita baadae, ambapo Said Kipanga alipiga
shuti ambalo halikulenga lango.
Pamoja na kipa wa Simba Agban
Vicent kutoka golini, Kipanga alishindwa
kukwamisha mpira kimiani, lakini beki
wa Simba, Novarty Lufunga alisaidia
kuokoa.
Kasi ya kushambuliana kwa zamu
ilizidi. Dakika ya 23, Shiza Kichuya nae
alikosa bao na mpira kuwababatiza
walinzi wa JKT Ruvu kabla ya kumfi kia
Mavugo ambaye awali, alipasiwa na
Mohammed Hussein.
Katika kuonyesha shughuli ni
pevu tangu dakika za awali, JKT Ruvu
walimpumzisha Michael Aidani na nafasi
yake kuchukuliwa na James Msuya.
Kipindi cha pili kilianza kwa maafande
wa JKT Ruvu kumtoa Msuya na badala
yake, akaingizwa Naftari Nashon. Simba
nao walimtoa Jamal Mnyate na Mwinyi
Kazimoto akaziba pengo hilo.
Jonas Mkude, katika dakika ya 55,
alijaribu bahati yake kwa kuachia shuti,
lakini liliishia mikononi mwa mlinda
mlango wa JKT Ruvu.
Dakika mbili baadae, maafande hao
kupitia kwa Hassan Matalema, alimjaribu
Agban, kipa huyo akadaka.
Katika kuimarisha safu ya
ushambuliaji, Simba ilimuingiza Ibrahim
Ajib, akapumzishwa Fredrick Blagnon.
Baada ya kuingia, Ajib aliongeza
chachu ya mashambulizi langoni mwa JKT
Ruvu. Katika dakika ya 70, mshambuliaji
huyo alipiga shuti fyongo.
Juuko Murshid naye aliingizwa
kuiongezea nguvu Simba dakika ya 74,
akichukua nafasi ya Lufunga.
Dakika zaidi ya 16 ambazo zilisalia
kabla ya mpira kumalizika, ilikuwa ni
kushambuliana kwa zamu na mashuti
yasiyolenga.
Mpaka dakika 90 zinamalizika,
milango ilibaki kuwa migumu. Kwa
matokeo hayo, Simba imefi kisha pointi
nne, kufuatia ushindi wake katika mchezo
wa kwanza dhidi ya Ndanda FC.
JKT Ruvu: Said Kipao, Michael Aidan,
Salum Gila, Nurdin Mohammed, Rahim
Juma, Ismail Amour, Hassan Matalema,
Hassan Dilunga, Atupele Green, Saad
Kipanga na Pera Mavuo.
Simba: Vicent Agban, Malika Ndeule,
Mohammed Hussein, Novat Lufunga,
Jonas Mkude, Method Mwanjali, Shiza
Kichuya, Mzamiru Yassin, Laudit Mavugo,
Fredrick Blagnon na Jamal Mnyate

Wednesday, August 24, 2016

MKWASA ATANGAZA KIKOSI CHA TAIFA STARS KITAKACHOVAANA NA NIGERIA



Kocha Mkuu wa timu ya Mpira wa Miguu Tanzania ‘Taifa Stars’, Charles Boniface Mkwasa, ametangaza wachezaji 20 watakaounda kikosi kitakachosafiri mwishoni mwa mwezi huu kwenda Nigeria kwa ajili ya mchezo wa mwisho wa kuwania kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2017) dhidi ya timu ya taifa ya nchi hiyo, Super Eagles.

Licha ya mchezo huo wa Septemba 3, 2016 kuwa sehemu ya mchuano wa kuwania nafasi ya kucheza fainali hizo za AFCON 2017 huko Gabon, lakini utakuwa ni wa kukamilisha ratiba baada ya Misri kufuzu kutoka kundi G ambalo mbali ya Nigeria na Tanzania, pia ilikuwako Chad ambayo iliyojitoa katikati ya mashindano.

“Tanzania hatuwezi kupuumza mchezo huu, tumeuchukulia serious (kwa umakini) kabisa kwa sababu tunacheza ugenini ambako matokeo mazuri yanaweza kutusongesha mbele na kuingia ndani ya timu 99 bora katika viwango vya FIFA,” amesema Mkwasa.

Katika kikosi chake, Mkwasa ametangaza kutomjumuisha Mshambuliaji wa Kimataifa, Thomas Ulimwengu anayecheza klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) kutokana na majeruhi ya paja kama ilivyo kwa Juma Abdul wa Young Africans ambaye aliumia katika mchezo wa kuwania Kombe la Shirikisho dhidi ya Mo Bejaia ya Algeria.

“Timu itaingia kambini Agosti 28, itakaa kambini kwa siku tano kabla ya kusafiri kucheza mchezo huo wa kukamilisha ratiba ambao Misri tayari wameshafuzu fainali za Afrika,” amesema Mkwasa na kuongeza kuwa kuna mchezaji wa Tanzania, Said Carte Mhando anamfuatilia ili ikiwezekana baadaye amwite kuchezea timu ya taifa. Anakipiga Klabu ya Brencia Calcio ya Italia.

Wachezaji walioitwa:
Makipa-
Deogratius Munishi – Young Africans
Aishi Manula – Azam FC

Mabeki
Kelvin Yondani - Young Africans
Vicent Andrew - Young Africans
Mwinyi Haji - Young Africans
Mohamed Hussein – Simba SC
Shomari Kapombe - Azam FC
David Mwantika - Azam FC

Viungo
Himid Mao - Azam FC
Shiza Kichuya – Simba SC
Ibrahim Jeba – Mtibwa Sugar
Jonas Mkude – Simba SC
Muzamiru Yassin – Simba SC
Juma Mahadhi - Young Africans
Farid Mussa Tenerif ya Hispania

Washambuliaji
Simon Msuva - Young Africans
Jamal Mnyate – Simba SC
Ibrahim Ajib – Simba SC
John Bocco - Azam FC
Mbwana Samatta - CK Genk ya Ubelgiji

YANGA YAPIGWA 3-1 NA TP MAZEMBE DRC

HATIMAYE wawakilishi wa Tanzania katika michuano ya soka ya Kombe la Shirikisho, Yanga wamemaliza hatua ya makundi kwa kupokea kichapo cha mabao 3-1 kutoka kwa TP Mazembe ya DRC.

Mechi hiyo ya mwisho ya kundi A, ambayo ilikuwa ya kukamilisha ratiba kwa Yanga, ilichezwa jana kwenye Uwanja wa Mazembe ulioko katika mji wa Lubumbashi.

Kutokana na matokeo hayo, TP Mazembe imemaliza mechi za kundi hilo ikiwa ya kwanza, kwa kuwa na pointi 13 baada ya kucheza mechi sita, wakati Yanga imeshika mkia kwa kuambulia pointi nne.

Yanga ililazimika kumaliza mchezo huo ikiwa na wachezaji 10 baada ya beki wake, Andrew Vincent Chikupe, kutolewa nje kwa kadi nyekundu dakika ya 30.

Mazembe ilihesabu bao lake la kwanza dakika ya 28 kupitia kwa Jonathan Bolingi baada ya kupokea pasi maridhawa kutoka kwa Deo Kanda.Bao hilo lilidumu hadi mapumziko.

Ranford Kalaba aliiongezea Yanga bao la pili dakika ya 55 kabla ya Bolingi kuongeza la tatu dakika ya 64.

Bao la kujifariji la Yanga lilifungwa na Amissi Tambwe dakika ya 75.


Tuesday, August 23, 2016

SERENGETI BOYS KUTAFUTIWA KAMBI TULIVU



Baada ya kutekeleza ahadi ya mwanzo ya kuipeleka Madagascar kwa ajili ya kambi ya kuivaa Afrika Kusini ‘Amajimbos’, Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amepanga kutekeleza ahadi yake nyingine kwa kuipeleka timu ya taifa ya Tanzania ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 17 ‘Serengeti Boys’ kwenye kambi tulivu, ikiwezekana nje ya nchi.

Rais Malinzi aliahidi na kutekeleza ahadi yake kuipeleka Madagascar, Serengeti Boys baada ya kuitoa Shelisheli katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika, zitakazofanyika Madagascar, mwakani. 


Kadhalika aliahidi kuipeleka timu hiyo nje ya nchi ambayo hata hivyo haijateuliwa baada ya kuindoa Afrika Kusini. Ameahidi kambi hiyo itaanza Septemba mosi, mwaka huuu.

Serengeti Boys ilipiga kambi Hosteli za TFF, zilizo Karume kwa wiki moja kabla ya kuhamia Hoteli ya Urban Rose, katikati ya jiji la Dar es Salaam ambako ilivunjwa kwa muda jana, Agosti 22, 2016 ambako vijana wamekwenda makwao kusalimia ndugu zao na itaitwa mwishoni mwa mwezi huu kwa ajili ya maandalizi ya kambi ya nje ya nchi.

Serengeti Boys imebakiwa na mtihani mmoja kufuzu kucheza fainali hizo kwa kucheza na Congo – Brazaville na mchezo wa kwanza utafanyika Dar es Salaam, Septemba 18, 2016 kabla ya kurudiana Septemba 30, 2016, Oktoba 1 au Oktoba 2, 2016.

TFF imejipanga kwa ajili ya kambi hiyo, na kinachosubiriwa kwa sasa ni mapendekezo ya makocha ili shirikisho itekeleze hatua hiyo ya kambi ya utulivu.

Kocha Mkuu wa Serengeti Boys, Bakari Shime maarufu kama Mchawi Mweusi, amesema kwamba anaamini kuwa mchezo ujao utakuwa mgumu kwa kuwa kila timu nitajipanga kuvuka ili kucheza fainali hizo.

TIMU YA SOKA YA UFUKWENI YA IVORY COAST YATUA NCHINI



Timu ya Taifa ya Mpira wa Miguu Ufukweni ya Ivory Coast, imeingia Dar es Salaam, Tanzania leo saa 8.00 usiku kwa ndege ya Shirika la Ndege la Ethiopia ikitokea jijini Abidjan.

Timu hiyo imekuja Dar es Salaam kwa ajili ya mchezo wa kwanza wa kuwania nafasi ya kucheza Kombe la Mataifa ya Afrika kwa mpira wa miguu wa ufukweni ambako itacheza na wenyeji Tanzania Ijumaa wiki hii kwenye uwanja maalumu ulioandaliwa kwa ajili ya mchezo huo.

Mchezo huo utachezeshwa na waamuzi kutoka Uganda ambao ni Shafic Mugerwa atakayepuliza kipyenga na wasaidizi wake ni Ivan Bayige Kintu na Muhammad Ssenteza.

Mtunza muda katika mchezo huo atakuwa Adil Ouchker wa Morocco huku Kamishna akiwa ni Reverien Ndikuriyo wa Burundi. Timu hizo zinatarajiwa kucheza mechi mbili za kuwania kufuzu kwani mara baada ya mchezo wa Dar es Salaam, zitarudiana tena Ivory Coast na mshindi wa jumla atakuwa amefanikiwa kufuzu kwa fainali.

Kwa upande wa Tanzania, Kocha Mkuu wa timu hiyo, John Mwansasu, anaendelea na mazoezi na wachezaji wake 16 aliowatangaza wiki iliyopita. Kikosi hicho kinaundwa na wachezaji sita kutoka Zanzibar na 10 Tanzania Bara.

Wanaounda kikosi hicho ni Talib Ame, Ahamada Ahmad, Mohammed Makame, Ahamed Rajab (golikipa) Khamis Said na Yacob Mohamed wote kutoka Zanzibar.

Wengine ni Ally Raby, Mwalimu Akida, Khalifa Mgaya, Rolland Revocatus, Juma Sultan, Rajab Ghana, Samwel Salonge, Kashiru Salum, Juma Juma na Kevin Baraka.

PAMBANO LA STARS, NIGERIA SASA KUCHEZWA SEPT 3



Shirikisho la Mpira wa Miguu Nigeria (NFA), limesogeza mbele kwa siku moja mchezo kati ya timu ya taifa ya Nigeria ‘The Super Eagles’ na Tanzania ‘Taifa Stars’ ambako sasa utafanyika Septemba 3, 2016 badala ya Septemba 2, 2016 iliyotangazwa awali.

Na Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Charles Boniface Mkwasa kesho anatarajiwa kutangaza kikosi ambacho atakiandaa maalumu kwa mchezo huo. Mkwasa amesema kwamba anatarajia kuita wachezaji 20 ambao atasafiri nao kwenda Nigeria kwa ajili ya mchezo huo.

“Kutakuwa na mabadiliko kidogo katika kikosi nitakachotangaza. Kwanza watakuwa wachezaji 20 badala ya 24, pili wachezaji ambao nitawachukua ni tofauti tofauti maana wengine kwa sasa ni majeruhi,” amesema Mkwasa.

Mchezo huo ni wa kukamilisha ratiba katika kundi G baada ya Misri kukata tiketi ya kucheza Kombe la Mataifa ya Afrika, fainali zitakazofanyika Gabon, mwakani. Katika kundi hilo, Chad ilijitoa hivyo kuathiri mbio za ushindani wa nafasi hiyo kwa timu za Tanzania na Nigeria.

WACHEZAJI WATANO WAPIGWA STOP KUCHEZA LIGI KUU BARA



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), linapenda kutoa tahadhali kwa timu tano za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) juu ya kuwatumia wachezaji ambao imewasajili, lakini imebainika mbele ya Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji kwamba wanamatatizo kwenye usajili wao.

Majimaji ya Songea

Mchezaji anayefahamika kwa majina ya George Mpole ambaye pia amebainika kuwa ndiye Gerald Mpole wa Majimaji ya Songea amefungiwa kucheza soka kwa mwaka kwa kosa la kubadili jina akiwa na lengo la kufanya udanganyifu kwenye usajili. Majimaji imeagizwa kutomtumia mchezaji huyo kutoka Kimondo FC.

Mwadui FC ya Shinyanga

Mchezaji William Lucian aliyesajiliwa na Mwadui ya Shinyanga kutoka Ndanda ya Mtwara, naye amefungiwa mwaka mmoja kwa kosa la kusajili Mwadui FC ilihali akiwa hajamaliza mkataba na Ndanda. Mwadui isimtumie mchezaji huyo.

Mbeya City ya Mbeya

Mchezaji Saidi Mkopi, pia amefungiwa mwaka mmoja kwa kosa la kujisali timu mbili. Imebainika kuwa akiwa bado na mkataba na Tanzania Prisons ya Mbeya hivyo Mbeya City isi1mtumie mchezaji huyo.

African Lyon ya Dar es Salaam

Mchezaji Rehani Kibingu aliyesajiliwa na African Lyon ya Dar es Salaam, amesimamishwa kuchezea timu hiyo mpaka uongozi wa African Lyon kumalizana na Ashanti United ya Dar es Salaam kabla ya Agosti 27, 2016. African Lyon isimtumie mchezaji huyo kwa sasa.

Mbao FC ya Mwanza

Mchezaji Emmanuel Kichiba aliyesajiliwa Mbao FC, naye amesimamishwa mpaka Mbao watakapomalizana na Ashanti United ya Dar es Salaam, kabla ya Agosti 27, 2016. Mbao FC isimtumie mchezaji huyo kwa sasa.

FIFA YAENDESHA KOZI MAALUMU YA STAMINA


Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), kwa mara nyingine limeipa nafasi Tanzania kwa kutoa kozi maalumu ya stamina (Physical fitness) kwa makocha wa Tanzania wenye leseni kiwango B inayoanza leo Agosti 22, 2016. Kozi hiyo inayoendeshwa na mkufunzi kutoka FIFA, Dk. Praddit Dutta, raia wa India itafikia ukomo Ijumaa wiki hii.

Akifungua kozi hiyo, Katibu Mkuu wa TFF, Mwesigwa Selestine aliishukuru FIFA kwa namna inavyoipa nafasi Tanzania katika kozi mbalimbali hususani za ukocha na uamuzi.

“Si kila nchi inapata privilege (fursa) kama hii. Bila shaka FIFA inatambua uwezo wa makocha wa Tanzania kwa sasa. Mjue kuwa FIFA ina watu wa kuwapa taarifa kila kona. Kama mngekuwa mnafanya vibaya, FIFA wangesema Tanzania bado, kwa hiyo kozi zisipelekwe… lakini inaonekana mnafanya vema, mngefanya vibaya msingefikiriwa,” alisema Mwesigwa aliyekuwa mgeni rasmi katika ufunguzi huo.

Mwesigwa amesema kwa kuwa FIFA ina malengo chanya na Tanzania kwa kutoa kozi mbalimbali ikiwamo hiyo ya physical fitness inayolenga kuwapa ujuzi makocha hao kuwajengea uwezo wachezaji kuwa na stamina.

Hivyo akawataka makocha wanaohudhuria kozi hiyo kutumia fursa hiyo ya mafunzo si kwa ajili yao peke yao bali kuendeleza ujuzi huo kwa wengine ambao hawakubahatika kuwa sehemu ya wateule wa FIFA.

Naye, Mkufunzi wa kozi hiyo, Dk. Dutta alisema: “Bila shaka Tanzania inakwenda kufungua ukurasa mwingine wa soka la weledi kwa kuwa na wataalamu mbalimbali katika ukocha na uamuzi. Mnachotakiwa ni kujitahidi kufanya vema na kozi nyingine nyingi zinakuja.”

FIFA kwa kushirikiana na Idara ya Ufundi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), chini ya Mkurugenzi Salum Madadi, imepitisha majina ya makocha 27 kuhudhuria kozi hiyo inayofanyika katika Hosteli ya TFF iliyoko kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Ilala jijini Dar es Salaam.

Makocha wanashiriki kozi hiyo ni Mohammed Muza, Samwel Moja, Nassa Mohammed, Jemedari Said, Oscar Mirambo, Wane Mkisi, Cletus Mutauyawa, Shaweji Nawanda, Kizito Mbano, Dennis Kitambi, Sebastian Nkoma, Fikiri Mahiza, Nyamtimba Muga, Nassor Mwinchui, Alfred Itaeli, Henry Ngondo, John Tamba, Kidao Wilfred, Luhaga Makunja, Mohammed Tajdin, Mohammed Silima, Salum Ali Haji, James Joseph, Kessy Mziray, Daudi Sichinga, Bakari Shime na Salum Mayanga.

Monday, August 22, 2016

SAMATTA AENDELEA KUNG'ARA UBELGIJI



MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta  amefunga mabao mawili timu yake, KRC Genk ya Ubelgiji ikishinda 3-0 dhidi ya wenyeji, Lokeren Uwanja wa Daknamstadion mjini Lokeren
katika mchezo wa Ligi Daraja la Kwanza A Ubelgiji.


Samatta alifunga mabao yote mawili ya mwanzo, la kwanza dakika ya 34 na la pili dakika ya 38, yote akisetiwa na kiungo kutoka Hispania, Alejandro Pozuelo Melero aliyemsetia pia Mjamaica Leon Bailey
kufunga la tatu dakika ya 48.

SERENGETI BOYS YANUSA FAINALI ZA AFRIKA ZA UNDER 17


TIMU ya vijana wenye umri chini ya miaka 17 Serengeti Boys, imefanikiwa kupenya hatua ya mwisho ya mtoano kucheza fainali za kombe la mataifa ya Afrika baada ya kuichapa Amajimbos ya Afrika Kusini mabao 2-0.
 

Fainali za mataifa ya Afrika kwa vijana, zimepangwa kufanyika mwakani Madagascar, Mchezo huo ulipigwa jana katika uwanja wa Azam Complex Chamazi, Dar es Salaam.
 

Bao la kwanza la Serengeti Boys katika mchezo huo, lilifungwa na Mohamed Abdalah dakika ya 34 akiunganisha krosi iliyochongwa na Hassan Juma huku bao la pili likiwekwa kimiani dakika ya 84 na Husein Makame.
 

Katika mchezo wa awali uliochezwa Afrika Kusini, kwenye Uwanja wa Dobsonville ulioko Soweto, timu hizo zilitoka sare ya bao 1-1.

Mabao yote katika mchezo wa awali, yalipatikana kipindi cha pili kwa mikwaju ya penati kwa kila upande. 


Afrika Kusini ndio walioanza kupata penati dakika 65 iliyofungwa na Luke Gareth kabla ya Ally Msengi kuisawazishia Serengeti Boys katika dakika ya 70.
 

Katika mchezo wa jana, Serengeti Boys ilionekana kuwa na kiu ya kupata ushindi wa mapema baada ya kulisakama lango la Amajimbos mara kwa mara.
 

Kikosi cha Serengeti Boys, kilipata pigo dakika ya 45 baada mwamuzi, Noiret Jim Bacari wa Comoro kumtoa kwa kadi nyekundu mchezaji Ali Hamis baada ya kumfanyia madhambi mchezaji wa Afrika Kusini.
 

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku Serengeti Boys wakiwa pungufu, walijipanga zaidi kuzuia mashambulizi ya wapinzani wao.
 

Timu hizo ziliendelea kushambuiliana kwa zamu huku Amajimboz wakifika langoni mwa Serengeti kwa kushtukiza, lakini mpaka dakika ya mwisho, vijana wa Tanzania waliibuka washindi katika mchezo huo.

Sunday, August 21, 2016

SIMBA YAANZA LIGI KUU KWA KISHINDO, YAINYUKA NDANDA FC MABAO 3-1, AZAM YAAMBULIA SULUHU KWA AFRICAN LYON

SIMBA jana ilianza vyema michuano ya soka ya ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kuichapa Ndanda FC ya Mtwara mabao 3-1, katika mechi ya ufunguzi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mshambuliaji Laudit Mavugo kutoka Burundi alidhihirisha kuwa thamani yake ni dhahabu baada ya kuifungia Simba bao la kuongoza dakika ya 20, akimalizia pasi maridhawa kutoka kwa beki Mohamed Hussein 'Tshabalala.'

Ndanda FC ilifanikiwa kupata bao la kusawazisha dakika ya 37 kupitia kwa mshambuliaji wake machachari, Omary Mponda, baada ya kupokea krosi kutoka kwa nahodha wake, Kiggi Makassy. Mabao hayo yalidumu hadi mapumziko.

Simba ilikianza kipindi cha pili kwa kufanya mabadiliko kadhaa ya wachezaji, ambapo Kocha Joseph Omog aliwapumzisha Jamal Mnyate na Ibrahim Hajib, ambao nafasi zao zilichukuliwa na Mwinyi Kazimoto n Frederick Blagnon.

Mabadiliko hayo yaliongeza uhai kwa Simba, ambayo ilifanikiwa kuongeza mabao mengine mawili kupitia kwa Blagnon na Shiza Kichuya.

Katika mechi nyingine ya ligi hiyo iliyochezwa jana, Azam ilishindwa kuutumia vyema uwanja wake wa nyumbani baada ya kulazimishwa kutoka sare ya bao 1-1 na African Lyon.

Lyon ilikuwa ya kwanza kufunga bao dakika ya 46 kupitia kwa Hood Mayanja kabla ya John Bocco kuisawazishia Azam dakika za majeruhi.

Saturday, August 20, 2016

KUZIONA SERENGETI BOYS, AFRIKA KUSINI BUKU MBILI




Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limetangaza kiingilio cha Sh 2,000 kwa mzunguko na Sh 5,000 kwa jukwaa kuu wakati timu ya taifa ya Tanzania ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 17 itakapocheza na Amajimbos ya Afrika Kusini kwenye mchezo wa kuwania nafasi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika  zitakazofanyika Madagascar, mwakani.

Mchezo huo utaoanza saa 9.00 alasiri Jumapili Agosti 21, 2016 kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi – Mbagala, nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam utachezeshwa na Mwamuzi Noiret Jim Bacari wa Comoro akisaidiwa na Mmadi Faissoil na Said Omar Chebli wakati mezani atakuwa Ali Mohamed Adelaid huku Kamishna wa mchezo huo atatoka Somalia ambaye anaitwa Amir Abdi Hassan.

Jumamosi Agosti 6, 2016, Serengeti ilitoka sare ya 1-1 na Afrika Kusini katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Dobsonville ulioko Soweto, Mji ulioko Kusini – Magharibi mwa jiji la Johannesburg, mabao yote yalipatikana kipindi cha pili yakiwa ni ya penalti kwa kila upande. 

Afrika Kusini ndio walioanza kupata penalti katika dakika 65 iliyofungwa na Luke Gareth kabla ya Ally Msengi kuisawazishia Serengeti Boys katika dakika ya 70.

Penalti ya Afrika Kusini ilitokana na mmoja wa mabeki wa Serengeti Boys kumfanyia madhambi Linamandla Mchilizeli wa Amajimbos ndani ya eneo la hatari wakati ile ya Serengeti Boys ilitoakana na beki Luke Donn wa Amajimbos kunawa mpira eneo la hatari. Mwamuzi wa mchezo huo alikuwa, William Koto kutoka Lesotho.

Kocha Mkuu wa Serengeti Boys, Bakari Shime maarufu kama Mchawi Mweusi amesema: “Watanzania wakaribie Chamazi, waje kutushangilia ili tushangilie ushindi kwa pamoja kikosi change kiko vema na ninamshukuru Mungu kwa hilo, akili yangu na akili za wachezaji wangu ni kumuondoa Msauzi (Afrika Kusini).

MALINZI AMLILIA KELVIN HAULE

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amemtumia salamu za rambirambi Mwenyekiti wa Klabu ya Majimaji ya Songea, mkoani Ruvuma, Humphrey Millanzi kutokana na kifo cha mchezaji wa zamani wa timu hiyo, Kelvin Haule kilichotokea jana Agosti 18, 2016 kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Ruvuma.

Rais Malinzi amesema, amepokea taarifa za kifo cha Haule kwa masikitiko makubwa.

Rais Malinzi amemuelezea Haule kuwa alikuwa na mchango mkubwa katika mafanikio ya timku ya Majimaji ya Songea na Lipuli ya Iringa hivyo ameacha alama ya ucheshi, kujituma na uwajibikaji katika kufanikisha kazi zake katika timu ambazo alichezea.

Salamu za rambirambi za Rais wa TFF Malinzi pia zimekwenda kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa na marafiki na kuwataka kuwa na moyo wa subira wakati huu mgumu wa msiba wa Kelvin Haule.

Mwenyezi Mungu aipumzishe roho ya marehemu Kelvin Haule mahala pema peponi.

Bwana alitoa, Bwana alitoa, jina la Bwana lihimidiwe.

LIGI KUU YA TANZANIA BARA KUANZA KUTIMUA VUMBI LEO



Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu wa 2016/17 inatarajiwa kuanza leo Jumamosi Agosti 20, 2016 kwa michezo mitano huku Bingwa Mtetezi wa Kombe hilo 2015/16, Young Africans ya Dar es Salaam ikisubiri hadi Agosti 31, 2016 kuanza kutetea taji lake.

Young Africans inatarajiwa kusafiri kwenda Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), kucheza na TP Mazembe kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho unaotarajiwa kufanyika Agosti 23, mwaka huu.

Michezo itakayochezwa kesho ni pamoja na Simba SC itakayoikaribisha Ndanda FC ya Mtwara kwenye Uwanja wa Taifa, ulioko Chang’ombe Dar es Salaam, katika mchezo utakaoanza saa 10.00 jioni wakati Azam itakuwa mwenyeji wa African Lyon kwenye Uwanja wa Azam FC ulioko Chamazi-Mbagala, nje kidogo ya jiji.

Kadhalika Stand United ya Shinyanga itakuwa mwenyeji wa Mbao FC ya Mwanza kwenye Uwanja wa CCM Kambarage mkoani Shinyanga sawa na Mtibwa Sugar itakayoikaribisha Ruvu Shooting ya Pwani kwenye Uwanja wa Manungu uliuoko Turiani, Mvomero mkoani Morogoro wakati Prisons ya Mbeya itasafiri hadi Uwanja wa Majimaji ya Songea kucheza na Majimaji FC ya huko.

Wakati ligi ikianza, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linaonya timu kuchezesha wachezaji wa kigeni kama hawana vibali vya kuishi, kufanya kazi na leseni inayomruhusu kucheza ligi husika kwa mujibu wa sheria za nchi na kanuni za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.

Vibali vya kuishi na kufanya kazi vinatolewa na Idara ya Uhamiaji Tanzania (Uhamiaji) wakati leseni ya kucheza inatolewa na TFF. Vilevile tumeziagiza klabu kulipia ada za ushiriki kwa kila timu; leseni za wachezaji, ada za wachezaji na ada za mikataba. Mchezaji hatapewa leseni ya kucheza kama uongozi wa timu hautakamilisha taratibu za malipo.

TFF linapenda kuzikumbusha timu zinazoshiriki Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kwamba hatutatoa leseni ya mchezaji yeyote ambaye timu haikuleta mkataba wakati wa maombi ya usajili, hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 68 vipengele vya 1, 2, 3 na 8 ya Ligi Kuu ya Tanzania toleo la 2016/2017.

Kila timu inatakiwa kuleta nakala tatu za mkataba wa mchezaji, ili kamati ya katiba, sheria na hadhi za wachezaji iweze kupitia na TFF iweze kuidhinisha mikataba hiyo. Baada ya hapo timu na mchezaji, watakuja kuchukulia mikataba hiyo hapa TFF. Ni matarajio yetu kuwa kila klabu itatimiza wajibu wake ili kuondoa migogoro kati ya timu na mchezaji na mchezaji na timu. Tunategemea kupata ushirikiano.

TFF YAMUIDHINISHA KESSY KUICHEZEA YANGA



Kamati ya Sheria na Haki za wachezaji imepisha usajili wa wachezaji wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara huku ikiwa imepitisha jina la Hassan Ramadhani ‘Kesi’ kuitumikia Young Africans kuanzia msimu huu 2016/17 baada ya kuona kuwa hana tatizo katika usajili badala yake madai ambayo pande husika zinaweza kudaiana wakati mchezaji anaendeleza kipaji chake.

Kamati hiyo chini ya Mwenyekiti wake, Richard Sinamtwa imepitia usajili wa timu zote na kujiridhisha kwamba suala la mchezaji Hassan Kessy limeegemea kwenye madai na si usajili ambako Simba ndiye mdai kwa kumtuhumu mchezaji huyo kuwa alianza kuitumikia Young Africans kabla ya kumaliza mkataba wake Simba SC. Mkataba wake ulifika mwisho, Juni 15, 2016.

 Kama ni madai Simba inaweza kuendelea kumdai Kessy au Young Africans wakati mchezaji huyo anatumika uwanjani kwa mwajiri mpya. 

TFF inafuatilia na kuangalia haki ya Simba namna ya kupata haki yake baada ya kuwasilisha madai kuhusu kuvunja mkataba na mwajiri wake wa zamani.

Kanuni hazimzuii mchezaji kuendelea kucheza kwa hoja ya madai badala yake suala hilo linaweza kumalizwa wakati mashindano yanaendelea. 

Kamati inaendelea kupitia malalamiko na pingamizi za wachezaji wengine na inatarajiwa kutoa taarifa rasmi kuhusu wachezaji wote wakati wowote kuanzia sasa.

KAMATI YA RUFANI TFF YAISHUSHIA ZIGO DRFA




Uamuzi wa Kamati ya Rufani za Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), imeona haiwezi kuhalalisha uchaguzi ambao tayari ulikuwa umepingwa na mmoja wa wagombea.

“Kuamua hivyo kutazidi kutazidi kulichimbua shimo soka letu,” amesema Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Wakili Julius Lugaziya.

Badala yake Kamati ya Rufani ya Uchaguzi, imeagiza kuwa Rufaa ambayo Bwana Tom Mazanda, aliiwasilisha kwenye Kamati ya Uchaguzi ya Chama cha Soka Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) isikilizwe kwa mujibu wa Katiba na kanuni zake za Chama cha Mpira wa Miguu Kinondoni (KIFA) zinazohusu masuala ya uchaguzi kwa wiki mbili yaani siku 14 kuanzia Agosti 16, 2016 endapo Mrufani bado atataka kuendelea na rufaa hiyo.

Kwa kipindi cha hapa katikati yaani mpito viongozi waliochaguliwa wataingia ofisini na kuendelea na majukumu yao ya kiungozi ikiwamo kusimamia masuala yote ya KIFA mpaka hapo itakapoamualiwa vinginevyo na matokeo ya rufaa iliyoko DRFA.

Uamuzi huo wa Kamati ya Rufaa ya TFF unatokana rufaa iliyowasilishwa kwenye ofisi za TFF na muomba rufani ambaye Juni 12, 2016 alichaguliwa kuendelea kuwa Mwenyekiti wa KIFA, lakini uchaguzi wake huo na wenzake walioshinda ukatenguliwa na Kamati ya Uchaguzi ya TFF mnamo Juni 18, 2016.

Pamoja na kutengua matokeo hayo, kamati iliagiza uchaguzi urudiwe na kuelekeza kuwa hatua mbalimbali za kimaadili zichukuliwe dhidi ya watu walioona waliosababisha sintofahamu katika zoezi la uchaguzi huo

Friday, August 19, 2016

MALINZI AMPONGEZA RAIS MPYA WA SOKA BOTSWANA, AOMBOLEZA KIFO CHA HAVELANGE



Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amemtumia salamu za pongezi Rais mpya wa Shirikisho la Mpira wa Miguu la Botswana Maclean Letshwiti aliyechaguliwa kushika wadhifa huo katika uchaguzi uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita.

Maclean Letshwiti ambaye ni nguli katika masuala ya biashara, alimshinda Tebogo Sebego kwa kura 32 kwa 28.

Katika barua yake ya pongezi kwenda kwa Letshwiti, Rais Malinzi amemtakia kila la kheri Rais huyo mpya wa BFA aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Klabu ya Mochudi Centre Chiefs maarufu kwa jina la Magosi.

Katika barua hiyo, Malinzi amesema: “Nakuandikia barua hii kwa niaba ya Kamati ya Utendaji ya TFF na kwa niaba yangu mwenyewe, kukupongeza wewe baada ya kushinda nafasi ya urais katika uchaguzi wa Chama cha Mpira wa Miguu Bostwana.”

“Mheshimiwa Rais, uchaguzi wenu ni ushahidi tosha wa kazi nzuri iliyowapa imani katika klabu uliyoiongoza na shirikisho la mpira wa miguu hapo Bostwana.,” amesema Malinzi katika taarifa yake na kuahidi ushirikiano wa kutosha kwa Rais Letshwiti.

Kadhalika, Rais Malinzi aliwapongeza Segolame Ramotlhwa na Marslow Motlogelwa waliochaguliwa kuwa Makamu Rais wa Kwanza na Makamu Rais wa Pili kwa kufuatana.

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amemtumia salamu za rambirambi Rais wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), kutokana na kifo cha Rais wa zamani wa FIFA, Joao Havelange aliyefariki dunia akiwa na umri wa miaka 100.

Katika salamu hizo, Rais Malinzi amesema amepokea taarifa za kifo cha Joao Havelange kwa masikitiko makubwa akimkumbuka zaidi pale aliongeza washiriki wa kombe la dunia kutoka timu 16 hadi 32, ambapo mashindano 6 yalifanyika chini ya utawala wake.

Joao Havelange, raia wa Brazil alikuwa mtangulizi wa Sepp Blatter katika shirikisho la mpira wa miguu duniani kuanzia mwaka 1974 hadi 1998. Blatter alijiuzulu nafasi ya Urais wa FIFA Aprili, 2013 kutokana na ripoti ya uchunguzi wa madai ya kupokea rushwa.

Joao Havelange aligua kwa muda mrefu na kulazwa hospitali tangu mwaka 1999 alipokumbwa na ugonjwa wa mapafu.

Alikuwa mmoja wa wanakamati wa Olimpiki (IOC), kuanzia mwaka 1963 hadi 2011 alipojiuzulu kwa sababu ya kudhoofu kwa afya yake. Havelange aliiwakilisha Brazil katika mashindano ya Olympic ya Kuogelea mwaka 1936, mwaka ambao aliidhinishwa kuwa mwanasheria kabla ya kuchaguliwa na IOC.

Mwenyezi Mungu aipumzishe roho ya marehemu Joao  Havelange mahala pema peponi. Bwana alitoa, Bwana alitoa, jina la Bwana lihimidiwe.

Wednesday, August 17, 2016

TIMU YA NETIBOLI YA JWTZ YATWAA UBINGWA WA AFRIKA MASHARIKI




Na Selemani Semunyu JWTZ
Wachezaji wa Timu ya Mpira wa Pete ya JWTZ wamekabidhiwa Medali za Dhahabu ikiwa ni sehemu ya kunyakua ubingwa wa Mchezo huo katika mashindano ya majeshi kwa nchi za Afrika mashariki yaliyofanyika Kigali nchini Rwanda.
Mbali na zawadi hiyo Mchezaji Nasra Suleiman wa Timu hiyo ya JWTZ ameshinda tuzo ya Most  Valuable Player (MVP) na hivyo kuongeza shangwe kwa T  imu ya Tanzania.
Akitoa tuzo hizo ni Mkuu wa Jeshi la Anga la Rwanda Brigedia Generali  Charles Karamba alisema katika mashindano haya ambayo ushiriki ndio jambo muhimu kwani sote ni washindi lakini wapo waliofanya vizuri wanaopaswa kupongezwa.
Alisema Katika Netball Tanzania imefanya Vizuri ikifuatiwa na Uganda kisha Kenya hivyo ni nafasi nzuri kuwapongeza waliofanya vizuri zaidi na pia waliofanya vibaya ili kujipanga upya katika mashindano yajayo.
Akizungumza na Waadishi wa habari mkuu wa Msafara wa Timu za Tanzania na Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya Timu za Tanzania Brigedia  Jairos Mwaseba aliipongeza Timu hiyo na kuda ushindi huo waliutarajia kutokana na maandalizi yaliyofanyika.
Kwa upande Mlinzi wa Timu hiyo Joyce Kaira na Mshambuliaji Mwanaidi Hasan  walisema wamefurahi kwani waliupoteza ubingwa huo mwaka jana.
Naye Nahodha wa Timu hiyo Dorita Mbunda alisema maandalizi mazuri yaliyofanywa na Jeshi ndio siri ya ushindi huo sambamba na Nidhamu na kujituma.
Timu hiyo inatarajiwa kukabidhiwa kombe katika sherehe za ufungaji wa mashindano hayo katika uwanja wa amahoro ambapo mchezo wa mwisho wa Soka kati ya Rwanda na Tanzania utachezwa na kuamua mshindi wa mchezo huo.

UONGOZI SIMBA WARIDHIA KUMKABIDHI TIMU MO DEWJI


Tuesday, August 16, 2016

MALINZI AUKWAA TENA UENYEKITI WA SOKA KAGERA


Na Mwandishi Wetu, Bukoba

RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi, juzi, alichaguliwa tena kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Soka Kagera (KRFA), baada ya kupata kura 21 kati ya 22.

Katika uchaguzi huo uliofanyika ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Optima, Bananzi, wilayani Misenyi, Salum Chama alitetea nafasi yake ya Katibu Mkuu KRFA kwa kupata kura zote 22.

Naye Pelegrinius Rutahyugwa alitetea nafasi yake ya ujumbe Mkutano Mkuu waTFF kwa kupata kura zote 22

Didas Zimbihile alitetea nafasi ya ujumbe wa mkutano mkuu klabu wa TFF kwa kukusanya kura zote 22.

Malinzi amekuwa Mwenyekiti wa KRFA tangu Machi 17, mwaka 2012 na katika kipindi chake cha kuwa madarakani, amesaidia kwa kiasi kikubwa kurejesha hamasa ya soka kimkoa.

Aidha, Malinzi amesaidia ukarabati wa Uwanja wa Kaitaba, ambao sasa una mwonekano mzuri, ukiwa unapambwa na nyasi bandia.

AKILIMALI AMUOMBA RADHI MANJI NA WANA-YANGA





HATIMAYE mwanachama mkongwe wa klabu ya Yanga na Katibu wa Baraza la Wazee la klabu hiyo, Ibrahim Akilimali, amemuomba radhi mwenyekiti wake, Yussuf Manji.

Akilimali alifikia uamuzi huo leo asubuhi baada ya wanachama wengi wa Yanga kujitokeza hadharani kushutumu kitendo chake cha kupinga Manji kuikodisha timu kwa miaka 10.

Akihojiwa na kituo cha redio cha EFM leo asubuhi, Akilimali alisema amempigia simu Manji kumuomba radhi kuhusu kauli hiyo na kwamba kwa sasa wapo kitu kimoja.

Akilimali alisema kama kuna watu wanaompenda Manji katika Yanga, basi yeye ni namba moja na kusisitiza kuwa hana tatizo naye.

Hivi karibuni, Akilimali alikaririwa na kituo kimoja cha redio akipinga kitendo cha Manji kuomba akodishwe kuisimamia Yanga kwa miaka 10, huku akitaka apewe umiliki wa logo ya klabu hiyo.

Aidha, Akilimali aliuponda mkutano mkuu wa dharula wa Yanga ulioitishwa na Manji kwa madai kuwa, wanachama walikurupuka kupitisha uamuzi huo.

"Nimempigia simu Manji na kumuomba radhi na narudia tena kumuomba radhi hapa ili Watanzania wote wanisikie,"alisema.

Vyombo vingi vya habari nchini leo viliripoti habari ya kujiuzulu kwa Manji, kufuatia shutuma zilizotolewa na Akilimali dhidi yake.

“Hatuna tatizo na Manji, tunampenda na ataendelea kuwa mwenyekiti hadi atakapotaka kuacha mwenyewe. Yanga ni moja, hatutaki tena kurejea kwenye mitafaruku ya kuanza kuitwa Yanga raizoni na Yanga kandambili,” alisema Akilimali.

Kwa mujibu wa mzee huyo, alichokosea Manji ni kutowaita wajumbe wa Baraza la Wazee wa Yanga ili kuzungumzia suala hilo kwanza kabla ya kulifikisha mbele ya wanachama.

Hata hivyo, alikiri kuwa Baraza la Wadhamini ndilo lenye nguvu kikatiba kuhusu masuala ya Yanga na sio Baraza la Wazee, ambalo halimo kwenye katiba.

Wakati huo huo, kikao cha matawi ya klabu ya Yanga yaliyoko mkoani Dar es Salaam, kimetoa pendekezo la kutaka Mzee Akilimali avuliwe uanachama kutokana na kauli zake zinazohatarisha umoja na mshikamano klabuni.

Monday, August 15, 2016

MANJI ASEMA BASI, IMETOSHA



Baada ya taarifa kwamba Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji amejiuzulu uenyekiti kuzagaa, SALEHJEMBE ilifanya kila juhudi kumpata na mwenye akazungumza kwa ufupi.

Alipoulizwa kuhusiana na suala la kujiuzulu na pia kusitiza uamuzi wake wa kutaka kuwekeza au kuikodisha Yanga kwa miaka kumi, alisema basi imetosha.

“Kwa kweli imetosha, imetosha sasa,” alisema.

Alipoulizwa afafanue kuhusiana na kauli hiyo, Manji aliongeza.
 

“Nimesema hivi, imetosha. Naomba uniache, nisingependa kujibu lolote kwa sasa, niache tafadhari."

Kumekuwa na taarifa kwamba Manji ameamua kuachana na wazo lake la kuwekeza Yanga kwa miaka 10 baada ya kuona hata baadhi ya viongozi wa serikali wakimuandama kwa madai wanatumiwa na baadhi ya mamilionea.

Taarifa nyingine zimeelezwa kwamba, wako wanachama wa Yanga ambao wanaona hawatafaidika na maslahi yao binafsi kama Manji atawekeza, hivyo wamekuwa wakipambana kuhakikisha haingii mkataba na kupewa nafasi hiyo kwa kuwa inaweza kuwavuruga.

Awali, kumekuwa na taarifa Manji ameamua kujitoa kwa kuwa kuna juhudi za chini pia zinazohusisha hadi watu wengine wenye mamlaka katika soka ambao wana hofu na uwekezaji wake.


CHANZO CHA HABARI: SALEH JEMBE

SIMBA YATOLEWA JASHO LA URA YA UGANDA


Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
SIMBA SC imebanwa na URA ya Uganda baada ya kulazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 katika mchezo wa kirafiki Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam jioni ya leo.
Mabao yote yalipatikana kipindi cha kwanza katika mchezo huo wa mwisho wa kujipima nguvu kwa timu ya kocha Mcameroon, Joseph Marius Omog kabla ya kuanza kwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara wiki ijayo.
Aliyekuwa nahodha wa Simba SC, Mussa Hassan Mgosi alicheza kwa dakika tatu kabla ya kukamata mpira na kuubusu kisha kuwapungia mkono mashabiki kuwaaga akiashiria kustaafu rasmi soka kwa ujumla.
Nafasi ya Mgosi aliyekwenda kuzunguka pembeni za mwa jukwaa na mtoto wake mdogo kuaga, ilichukuliwa na kiungo mpya, Jamal Mnyate aliyesajiliwa kutoka Mwadui FC ya Shinyanga.
Mgosi aliyepokewa na familia yake, ikiongoawa na mkewe Jasmine baada ya kutoka uwanjani – sasa anakuwa Meneja wa Simba SC.
URA walitangulia kwa bao Shafiq Kagimu aliyefumua shuti dakika ya 19 baada ya kupokea krosi ya Labama Bokota.
Simba ilikuja juu mara baada ya bao hilo na dakika ya 26 Mrundi Laudit Mavugo na Mnyate walishindwa kuunganisha krosi nzuri ya beki wa kushoto Hamad Juma mpira ukaokolewa na mabeki.
Simba ikafanikiwa kusawazisha bao hilo dakika ya 32 kupitia kwa Nahodha mpya, Jonad Gerald Mkude aliyeunganisha kwa kichwa mpira wa adhabu uliopigwa na beki wa kushoto, Mohemed Hussein ‘Tshabalala’ kufuatia Hamad Juma kuchezewa rafu.
Baada ya bao hilo timu hizo ziliendelea kushambuliana kwa zamu na kosa kosa za mabao zikawa za pande zote hadi mwisho wa mchezo.
Mchezaji ghali zaidi kwenye kikosi cha sasa cha Simba, mshambuliaji Muivory Coast, Frederick Blagnon aliingia kumpokea Ibrahim Hajib kipindi cha pili, lakini kwa mara ya pili akashindwa kuwafurahisha mashabiki Uwanja wa Taifa.
Mchezaji huyo aliyesajiliwa kwa dau la zaidi ya Sh. Milioni 100, alipiga shuti moja tu dhaifu kwenye lango la URA baada ya kuingia dakika ya 79. 
Safu ya kiungo ya Simba SC leo haikucheza vizuri kama ilivyokuwa katika mchezo uliopita wakishinda 4-0 dhidi ya AFC Leopard ya Kenya na haikuwa ajabu leo Hajib hakufunga, kwa sababu muda mwingi alilazimika kutafuta mpira kuliko nafasi za kufunga.
Kikosi cha Simba SC leo kilikuwa; Vincent Angban, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Hamad Juma, Novaty Lufunga, Method Mwanjali, Jonas Mkude, Shizza Kichuya/Hajji Ugando dk74, Muzamil Yassin, Laudit Mavugo, Ibrahim Hajib/Frederick Blagnon dk79 na Mussa Mgosi/Jamal Mnyate dk3/Mussa Ndusha dk62.
URA FC; Oscar Agaba, Mathias Muwanga, Sam Sekito, Fahad Kawoya, Shafiq Kagimu, Jimmy Lule, Feni Ali, Labama Bokota, Julius Ntambi na Elkanah Nkugwa.
BIN ZUBEIRY SPORTS ONLINE

YANGA YAFUFUA MATUMAINI KWA KUICHAPA MO BEJAIA 1-0


Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
YANGA SC imefufua matumaini ya kwenda Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika, kufuatia ushindi wa 1-0 jioni ya leo dhidi ya Mouloudia Olympique Bejaia ya Algeria katika mchezo wa marudiano Kundi A Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Shukrani kwake, mshambuliaji wa kimataifa wa Burundi, Amissi Josleyn Tambwe aliyefunga bao hilo pekee mapema tu kipindi cha kwanza.
Ushindi huo wa kwanza baada ya mechi tano, unaifanya Yanga ifikishe pointi nne baada ya awali kufungwa mechi tatu na kutoa sare moja ingawa inaendelea kushika mkia katika Kundi A.
Mazembe inaongoza Kundi A kwa pointi zake 10 baada ya mechi nne, ikishinda tatu na kutoa sare moja, ikifuatiwa na Bejaia na Medeama, ambazo kila moja ina pointi tano za sare tatu na ushindi mmoja.
Tambwe alifunga bao hilo dakika ya pili tu ya mchezo, akimalizia mpira uliookolewa kufuatia Simon Msuva kuunganisha kwa kichwa krosi ya Juma Abdul kutoka upande wa kulia.
Yanga sasa inaomba Medeama ya Ghana ifungwe na TP Mazembe kesho na baadaye ikatoea sare na MO Bejaia ili kwenda Nusu Fainali.
Yanga ingeweza kuondoka na ushindi mnono leo, kama mshambuliaji wake, Obrey Chirwa angekuwa makini na kutumia vizuri nafasi zaidi ya nne za wazi alizotengenezewa.
Nafasi iliyowasikitisha zaidi mashabiki wa Yanga ni ya kipindi cha pili, Chirwa aliporuka kichwa cha mkizi baada ya krosi ya Simon Msuva kutoka kushoto, lakini akapiga hewa akiwa amebaki na kipa, huku mpira ukienda nje.
Kocha Mholanzi, Hans van der Pluijm alilazimika kufanya mabadiliko ndani ya robo ya kwanza ya mchezo, baada ya beki wake, Andrew Vincent ‘Dante’ kuumia na kumuingiza mkongwe, Kevin Yondan aliyemalizia vizuri mchezo.
Na akalazimika pia kumpumzisha beki wake wa kulia, Juma Abdul baada ya kipindi cha kwanza kufuatia kuumia nyama na kumuingiza kiungo Said Juma ‘Makapu’ aliyekwenda kucheza kama kiungo ea ulinzi, huku Mbuyu Twite akihamia beki ya kulia. 
Yanga itahitimisha mechi zake za Kundi A Kombe la Shirikisho kwa kumenyana na wenyeji TP Mazembe ya DRC mjini Lubumbashi Agosti 23, mwaka huu.
Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Deo Munishi ‘Dida’, Juma Abdul/Said Juma ‘Makapu’ dk46, Mwinyi Mngwali, Andrew Vincent ‘Dante’/Kevin Yondan dk17, Vincent Bossou, Mbuyu Twite, Simon Msuva, Thabani Kamusoko, Amissi Tambwe, Obrey Chirwa na Deus Kaseke/Juma Mahadhi.
MO Bejaia; Chamseddine Rahmani, Ismail Benettayeb, Faouzi Rahal, Sofiane Khadir, Soumaila Sidibe, Zakaria Bencherifa, Mohamed Yacine Athmani, Morgan Betorangal, Sofiane Baouali, Amar Benmelouka na Kamel Yesli. 

BINZUBEIRY SPORTS ONLINE

WACOMORO KUZICHEZESHA SERENGETI BOYS NA AFRIKA KUSINI



Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), limemteua Noiret Jim Bacari wa Comoro kuwa mwamuzi wa kati katika mchezo wa marudiano utakaozikutanisha timu za taifa za vijana za Serengeti Boys ya Tanzania na Amajimbos ya Afrika Kusini, utakaofanyika Agosti 21, 2016 Kwenye Uwanja wa Chamazi ulioko Mbagala - nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa taarifa ya CAF iliyofika Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) mapema wiki hii, waamuzi wasaidizi pia wanatoka Comoro. Waamuzi hao ambao ni washika vibendera ni Mmadi Faissoil na Said Omar Chebli wakati mezani atakuwa Ali Mohamed Adelaid huku Kamishna wa mchezo huo atatoka Somalia ambaye anaitwa Amir Abdi Hassan.

Jumamosi iliyopita, ikicheza mbele ya Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi kadhalika Naibu Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, Rosemary Chambe Jairo, timu ya soka ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 17 maarufu kama Serengeti Boys ilitoka sare ya 1-1 na Afrika Kusini.

Katika mchezo huo uliofanyika Uwanja wa Dobsonville ulioko Soweto, Mji ulioko Kusini – Magharibi mwa jiji la Johannesburg, mabao yote yalipatikana kipindi cha pili yakiwa ni ya penalti kwa kila upande. Afrika Kusini ndio walioanza kupata penalti katika dakika 65 iliyofungwa na Luke Gareth kabla ya Ally Msengi kuisawazishia Serengeti Boys katika dakika ya 70.

Penalti ya Afrika Kusini ilitokana na mmoja wa mabeki wa Serengeti Boys kumfanyia madhambi Linamandla Mchilizeli wa Amajimbos ndani ya eneo la hatari wakati ile ya Serengeti Boys ilitoakana na beki Luke Donn wa Amajimbos kunawa mpira eneo la hatari. Mwamuzi wa mchezo huo alikuwa, William Koto kutoka Lesotho.

Itakumbukwa kwamba Afrika Kusini ilianza kwa kasi dakika 10 za mwanzo wa mchezo huo, ilipotea dakika zote 30 za kipindi cha kwanza ambao kukosa bahati na umakini kidogo tu kwa nyota wa Serengeti Boys kulisababisha kukosa mabao matano yakiwamo mawili yaliyogonga mwamba hivyo kuwatia hasira Serengeti Boys ambao walionyesha kuwa na njaa ya mabao.

Kubanwa katika kipindi cha kwanza, kulisababisha Kocha Mkuu wa Amajimbos kufanya mabadiliko ya wachezaji wote watatu kipindi cha pili, wakati Bakari Shime kwa upande wake alimpumzisha Ibrahim na nafasi yake kuchukuliwa na Muhsin ambaye alisaidia kuendedlea kuwabana Afrika Kusini waliokjuwa wanawategemea nyota kama na Mswati Mavuso na Lethabo Mazibuko.

Shukrani za pekee zinaweza kwenda kwa Kipa Ramadhani Kabwili aliyeokoa hatari nyingi ikiwamo mpira uliokuwa unakwenda golini uliotokana na adhabu ndogo. Kadhalika Msengi aliyekuwa nyota wa mchezo huo akimiliki vema idarta ya ulinzi akishirikiaana nDickson Job.

Shime maarufu kama Mchawi Mweusi alisema: “Nashukuru kwa matokeo . Si mabaya kwangu. Tunarudi nyumbani kujipanga. Afrika Kusini ilikuwa inanitia hofu ndio maana nilisema mechi itakuwa ngumu.”

Kwa upande wake, Naibu Balozi Rosemary alisema: “Ahsanteni vijana (Serengeti Boys) kwa kulinda heshima yangu,” wakati Malinzi alisema: “Sina mengi. Mkiwafunga Afrika Kusini Agosti 21, 2016 kambi inapigwa tena nje ya nchi. Sijui ni nchi gani, lakini mtakwenda kujiandaa nje ya nchi.”

WAGANDA KUCHEZESHA SOKA YA UFUKWENI KATI YA TANZANIA NA IVORY COAST



Mchezo Mpira wa Miguu wa Ufukweni kati ya Tanzania na Ivory Coast kuwania nafasi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa utachezeshwa na waamuzi kutoka Uganda ambao ni Shafic Mugerwa katikati na wasaidizi wake ni Ivan Bayige Kintu na Muhammad Ssenteza.

Mtunza muda katika mchezo huo atakuwa Adil Ouchker wa Morocco huku Kamishna akiwa ni Reverien Ndikuriyo wa Burundi. Timu hizo zinatarajiwa kucheza mechi mbili ambako mara baada ya mchezo wa Dar es Salaam, utarudiwa mwingine huko Ivory Coast na mshindi wa jumla atakuwa amefanikiwa kufuzu kwa fainali.

Kocha wa timu hiyo, John Mwansasu, leo Agosti 12, 2016 ametangaza kikosi cha wachezaji 16 watakaoingia kambini kwa ajili ya kujiandaa na mchezo huo utakaofanyika Agosti 26, mwaka huu.

Akizungumza na wandishi wa habari Mwansasu amesema kikosi hicho kinaundwa na wachezaji sita kutoka Zanzibar na 10 Tanzania Bara.

Pia Mwansasu amesema wanatarajiwa kucheza mechi mbili ambako mara baada ya mchezo wa Dar es Salaam, watarudiana huko Ivory Coast na mshindi wa jumla atakuwa amefanikiwa kufuzu kwa fainali.

Kikosi hicho kinaunda  na wachezaji Talib Ame, Ahamada,  Mohammed Makame, Ahamed Rajab (golikipa) Khamis Said na Yacob Mohamed wote kutoka Zanzibar.

Wengine ni Ally Raby, Mwalimu Akida, Khalifa Mgaya, Rolland Revocatus, Juma Sultan, Rajab Ghana, Samwel Salonge, Kashiru Salum, Juma Juma na Kevin Baraka.

FIFA YAFUNGA DIRISHA LA USAJILI, TIMU ZATOZWA FAINI


Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), leo saa 6:00 usiku litafunga tena dirisha la usajili baada ya kulifungua jana kwa saa 48 na imebainika kuwa timu tatu zaidi zilikuwa na dosari katika usajili hivyo kufanya ongezeko la kutoka timu nane zilionekana kwa haraka mapema wiki hii mara baada ya dirisha kufungwa Agosti 6, 2016.

Timu hizo kwa ujumla zilikuwa na dosari ya ama kutokusajili kabisa au kutokamilisha usajili wa ushiriki wa ndani kwa msimu wa 2016/2-17. Timu tatu nyingine zilizobainika leo Agosti 14, 2016 katika mtandao ni pamoja na Toto African ya Mwanza na Stand United ya Ligi Kuu Tanzania Bara kadhalika Arusha FC ya Arusha ambayo msimu huu itashiriki Ligi Daraja la Pili (SDL).

Hadi tunatuma taarifa hii usajili ulikuwa ukiendelea kwa mfumo wa mtandao (TMS) ikiwa na maana ya Transfer Matching System, lakini Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), limerejea kanuni za usajili hivyo kuzitoza faini timu zilizokuwa na dosari. Faini imetozwa kwa viwango tofauti kulingana na mashindano.

Timu zinazohusika na usajili wa mtandao ni zile zinazoshiriki Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL), Ligi Daraja la Kwanza la StarTimes (SFDL) na Ligi Daraja la Pili (SDL) na adhabu ya kushuka daraja na kwenda kushiriki Ligi ya Wilaya kisha Ligi ya Mabingwa Mikoa (RCL) ambayo usajili wake ni wa kutumia karatasi.

Timu za Ligi Kuu ambazo zilikatiwa mawasiliano baada ya kushindwa kuwahi tarehe ya mwisho ya usajili ni Young Africans ambayo haikusajili kabisa. Kwa kufanya makosa hayo, kwa mujibu wa kanuni za Ligi Kuu ya Vodacom, Young Africans imeadhibiwa faini ya shilingi milioni tatu (Sh. 3,000,0000). Young Africans imetozwa faini hiyo kwa kutosajili jina hata moja kabla ya Agosti 6, 2016.

Timu nyingine za Ligi Kuu ambazo hazikukamilisha usajili angalau kufikisha wachezaji 18 ni African Lyon ya Dar es Salaam, Stand United ya Shinyanga na Toto African ya Mwanza ambazo kila timu imetozwa faini ya shilingi milioni moja (Sh.1,000,000).

Kwa timu za Daraja la Kwanza la StarTimes (SFDL), Coastal Union ya Tanga pekee imetozwa faini ya shilingi milioni moja (Sh.1,000,000) wakati timu nyingine za daraja hilo, Kiluvya United na Friends Rangers za Dar es Salaam pamoja nna Panone, zimetoswa faini ya shilingi laki tano (Sh. 500,000) kila moja.

Kadhalika kwa timu za Daraja la Pili (SDL), ambazo ni Kitayose ya Kilimanjaro, Mashujaa ya Kigoma na Arusha FC ya Arusha, zimetozwa faini ya shilingi laki tano (Sh. 300,000) kila moja. Faini hiyo ni kwa timu na uongozi husika hauna budi kuilipa mara moja, kwani TFF haitatoa leseni za wachezaji kama timu haijalipwa faini hiyo.

Kanuni zinazozungumzia usajili ni Sura ya 10 inayozungumzia usajili na 11 inayozungumzia Adhabu Zihusuzo Usajili Na Uhamisho kadhalika Uhamisho Nje ya Nchi.

Wednesday, August 10, 2016

NAPE AWAPA DARASA WASAMBAZAJI WA FILAMU



Na Raymond Mushumbusi WHUSM
 

Wasambazaji wa Filamu na Muziki nchini wameashauriwa kuzingatia na kufuata Sheria za nchi katika usambazaji wa kazi hizo.
 

Ushauri huo umetolewa leo Jijini Dar es Salaam na  Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa, na Michezo Mhe. Nape Moses Nnauye alipokutana na Umoja wa Wasambazaji wa Filamu na Muziki kujadili mustakabali wa usambazaji wa kazi za Sanaa nchini.
 

“ Nia yangu  njema sina nia ya kumuumiza mtu nataka sheria na  taratibu zilizopo zifuatwe mnapotekeleza majukumu yenu ya usambazaji wa Filamu na muziki” alisema Mhe. Nape.

Mhe. Nape Moses Nnauye amewahakikishia wasambazaji hao kuwa Serikali ipo pamoja nao na watashirikiana kwa pamoja ili kuweza kutafuta namna bora ya kuboresha usambazaji wa Filamu na Muziki nchini.
 

Mhe. Nape ameongeza kuwa yuko tayari kupokea mawazo na ushauri kutoka kwa Wasambazaji wa Filamu na Muziki nchini katika kupata namna nzuri ya kutatua changamoto zilizopo na kuboresha njia za usambazaji wa kazi za Sanaa.
 

Naye Mwakilishi wa Umoja wa Wasambazaji wa Filamu na Muziki nchini  Bw. Joseph Lyakurwa amempongeza Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Nape Moses Nnauye kwa jitihada za Serikali katika kupambana na wizi wa kazi za Sanaa nchini na kuomba kuendelea na kuwasaka na kuwachukulia hatua wote wanaokiuka Sheria na taratibu katika usambazaji wa kazi za Sanaa.
 

“ Nakuomba Mhe. Waziri tukishalipa kodi zote zinazotakiwa kwa mujibu wa Sheria na taratibu zilizopo baada ya hapo mfanyabiashara atakayekamatwa amekiuka Sheria na taratibu hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi yake”.alisema Bw. Lyakurwa.
 

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu  Bibi. Joyce Fissoo amewashauri Wasambazaji wa Filamu na Muziki kuzingatia ubora wa kazi wanazozisambaza ili kuweza  kushindana  na soko la filamu na muziki wa nje.
 

“ Nawaomba wasambazaji wa Filamu na Muziki muzingatie ubora wa kazi mnazo zisambaza kwani tunashindana na filamu za jje kwahiyo tukizingatia hilo Filamu na Muziki wetu utasonga mbele” Alisema Bibi. Joyce.
 

Baada ya kikao hicho baina ya Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Nape Moses Nnauye na Umoja wa Wasambazaji wa Filamu na Muziki nchini,kamati ya watu saba imeundwa kukaa na kujadiliana na kupata suluhisho la namna bora ya usambazaji wa kazi za Sanaa na kuwasilisha ripoti kwa Mhe. Waziri.

RATIBA YA LIGI KUU YAFANYIWA MAREKEBISHO



Kutokana na sababu mbalimbali, Bodi ya Ligi (TPLB) ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), imelazimika kubadili Ratiba ya Ligi Kuu kwa michezo kadhaa ya mwanzo kama ifuatavyo.

1. Mchezo Na. 2 – Kagera Sugar vs Mbeya City (20.08.2016)

Mchezo huo sasa utachezwa tarehe 21.08.2016 katika Uwanja wa CCM Kambarage Shinyanga. Sababu ni kuwa uwanja wa Kaitaba bado utakuwa kwenye matengenezo.

 2. Mchezo Na.4 – Toto African vs Mwadui FC (20.08.2016)

Mchezo huo sasa utachezwa tarehe 24.08.2016 katika Uwanja wa CCM Kirumba. Sababu za mabadiliko ni kuwa uwanja huo tarehe 20.08.2016 utakuwa na matumizi mengine ya kijamii.

3. Mchezo Na.13 – Kagera Sugar vs Stand United (27.08.2016)

Mchezo huo sasa utachezwa katika Uwanja wa CCM Kambarage. Awali timu mwenyeji wa mchezo huo ilikuwa ni Kagera Sugar, lakini kwa sasa timu mwenyeji atakuwa ni Stand United.

4. Mchezo Na.55 – Toto vs Ndanda (02.10.2016)

Mchezo huo sasa utachezwa tarehe 03.10.2016 badala ya tarehe 02.10.2016

5. Mchezo Na.80 – Mbao FC vs Ndanda fc (16.10.2016)

Mchezo huo umerudishwa nyuma kutoka tarehe 16.10.2016 hadi tarehe 28.09.2016. Sababu ni kuiwezesha timu ya Ndanda kucheza michezo miwili kwa kanda ya ziwa kwa lengo la kupunguza gharama.

6. Mchezo Na.96 – Tanzania Prisons vs Mbao FC (22.10.2016)

WAPINZANI WA YANGA, MO BAJAIA WATUA DAR


Jumla ya kikosi cha watu 35 ambao ni wachezaji na viongozi wa MO Bajaia kutoka Algeria, wametua Dar es Salaam, usiku wa kuamkia jana Agosti 9, 2016 na imefikia Hoteli ya Ledger Plaza, iliyoko Kunduchi Beach nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam.

Timu hiyo imekuja kucheza na Young Africans ya Dar es Salaam, katika mchezo wa nne wa hatua ya Nane Bora kuwania Kombe la Shirikisho Barani Afrika utakaofanyika Jumamosi Agosti 13, 2016 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Licha ya kwamba Young Africans kuwa na pointi moja, bado ina nafasi ya kushika nafasi za juu katika kundi la A ambalo msimamo wake unaongozwa na TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), huku Mo Bajaia ya Algeria na Medeama ya Ghana, zina pointi tano kila moja. Wakati Young Africans wanacheza na Mo Bajaia iliyoshinda mchezo wa kwanza huko Algeria, Medeama itakipiga na TP Mazembe.

Mchezo wa Young Africans dhidi ya Mo Bajaia utachezeshwa na waamuzi kutoka Ethiopia ambako katikati atakuwa Bamlak Tessema Weyesa akisaidiwa na Kindie Mussie mstari upande wa kusini na Temesgin Samuel Atango katika mstari wa Kaskazini upande wa wakati Mwamuzi wa Akiba atakuwa Haileyesus Bezezew Belete.

Kamishna wa mchezo atakuwa Gaspard Kayijuka kutoka Rwanda wakati Desire Gahuka wa Burundi atasimamia ufanisi wa waamuzi wa mchezo na Mratibu Mkuu wa mchezo atakuwa Isam Shaaban kutoka Sudan. Mratibu huyo anatarajiwa kuwasili leo Agosti 10, 2016 wakati waamuzi watatua kesho Agosti 11, 2016 na msimamizi wa waamuzi atatua Ijumaa Agosti 12, 2016.

Kiingilio katika mchezo huo kitakuwa ni Sh 3,000 kwa mzungunguko kwa maana ya viti vya kijani, bluu na chungwa wakati Viti Maalumu vyenye hadhi ya daraja B na C kiingilio kitakuwa Sh 10,000 wakati A kiingilio kitakuwa ni Sh 15,000 kwa mujibu wa Waratibu wa Young Africans.

Tuesday, August 9, 2016

SIMBA YAWAPA RAHA MASHABIKI WAKE



TIMU ya soka ya Simba jana iliwapa raha mashabiki wake baada ya kuichapa AFC Leopards ya Kenya mabao 4-0 katika mechi ya kirafiki ya kimataifa iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mechi hiyo iliyohudhuriwa na mashabiki lukuki, ilikuwa maalumu kwa ajili ya kupamba tamasha la maadhimisho ya miaka 80 ya klabu ya Simba.

Simba pia ilitumia mechi hiyo kuwatambulisha nyota wake kadhaa wapya, waliosajiliwa kwa ajili ya msimu ujao wa ligi, akiwemo Shiza Kichuya, Pauk Kiongera na Laudit Mavugo.

Bao la kwanza la Simba lilifungwa na Ibrahim Ajib dakika ya 38 kwa shuti kali lililomshinda kipa wa AFC Leopards. Bao hilo lilidumu hadi mapumziko.

Dakika 11 baada ya kuanza kwa kipindi cha pili, Ajib aliiongezea Simba bao la pili kutokana na kazi nzuri iliyofanywa na Kichuya.

Bao la tatu lilifungwa na Kichuya dakika ya 66, akiunganisha wavuni pasi kutoka kwa Blagnen kabla ya Mavugo kuongeza la nne dakika ya 81.