KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, December 9, 2011

DILUNGA, MAHADHI WALIWEKA HISTORIA TANZANIA



MSHAMBULIAJI Maulid Dilunga wa Yanga na kipa Omar Mahadhi wa Simba ni wachezaji pekee wa Tanzania walioweka historia ya kuteuliwa kuunda kikosi cha Afrika.
Uteuzi huo ulifanywa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF), mara baada ya kumalizika kwa michezo ya All Africa Games, iliyofanyika mwaka 1973 mjini Lagos, Nigeria.
Katika michezo hiyo, Taifa Stars ilifanikiwa kufika hatua ya nusu fainali. Katika mechi za awali, Stars ilitoka suluhu na Nigeria A, ikaichapa Nigeria B mabao 2-1 kabla ya kuzifunga Ghana na Togo bao 1-0 kila moja.
Katika hatua iliyofuata, Stars ilitoka suluhu na Nigeria, ikatoka sare ya bao 1-1 na Misri kabla ya kufungwa mabao 2-1 na Algeria.
Dilunga ndiye aliyeibuka mchezaji nyota wa Taifa Stars katika michezo hiyo baada ya kuifungia mabao yote katika kila mechi.
Licha ya Stars kutolewa hatua ya nusu fainali, Dilunga na Mahadhi hawawezi kuisahau michezo hiyo kutokana na kuteuliwa kwenye kikosi cha kombani ya Afrika.
Mara baada ya uteuzi huo, kikosi hicho kilifanya ziara katika mataifa sita ya Ulaya na Amerika, ambako kilicheza mechi kadhaa za kirafiki.
Baadhi ya mataifa hayo ni Mexico, Guatemala, Uruguay, Peru, Hungary na Bulgaria. Katika ziara hiyo, kikosi hicho cha Afrika kilishinda mechi tatu, kilitoka sare mbili na kufungwa moja.
Uteuzi wa Dilunga kwenye kikosi hicho uliingia utata baada ya kilichokuwa Chama cha Soka nchini (FAT) wakati huo, kudhani mchezaji aliyeteuliwa ni Abdalla Kibadeni.
Katika taarifa yake kwa FAT, CAF ilisema inamhitaji mchezaji aliyekuwa akivaa jezi namba 10. Na katika kikosi cha Stars wakati huo, wachezaji waliokuwa wakivaa jezi hiyo ni Dilunga na Kibadeni.
Ikabidi FAT iombe ufafanuzi kwa CAF na ndipo ilipobainika kwamba, mchezaji aliyekuwa akihitajika ni Dilunga na siyo Kibadeni.
Kilichoivutia CAF kumteua Dilunga kwenye kikosi hicho ni uwezo wake mkubwa wa kufunga mabao, hasa katika mechi yao dhidi ya Nigeria B, ambapo alipachika wavuni mabao mawili.
Dilunga pia aliwahi kupata nafasi ya kwenda kucheza soka ya kulipwa Ulaya mwaka 1970 wakati timu ya daraja la pili ya West Bromwich ya England ilipofanya ziara nchini.
Hata hivyo, kuna madai kuwa, aliyekuwa mwenyekiti wa FAT wakati huo, Saidi Hamad El-Maamry alimzuia kwenda huko ili aweze kuichezea Taifa Stars katika michuano ya kimataifa.
Viongozi wa West Bromwich walikuja nchini wakiwa wageni wa Yanga na baada ya kucheza mechi moja ya kirafiki, walivutiwa na uwezo wa Dilunga.
Mbali na kuzuiwa na El-Maamry kwenda Uingereza, mwamko mdogo kwa wanasoka wa Tanzania kwenda kucheza soka ya kulipwa nje nao ulichangia kumfanya Dilunga apuuze mwito huo.

Taifa Stars, Simba, Yanga hazijawakuna Watanzania

KIKOSI cha Taifa Stars

KIKOSI cha Simba


KIKOSI cha Yanga


TIMU ya soka ya Taifa, Taifa Stars haina rekodi kubwa ya kujivunia katika michuano ya Afrika. Rekodi pekee ilizoweza kufikia ni kufuzu kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 1980 na fainali za Afrika kwa wachezaji wa ndani (CAN) mwaka 2010.
Mshambuliaji Peter Tino ndiye aliyeiwezesha Taifa Stars kufuzu kucheza fainali za Mataifa ya Afrika za mwaka 1980 baada ya kuifungia bao la kusawazisha katika mechi ya marudiano dhidi ya Zambia.
Katika mechi ya awali kati ya timu hizo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam, Taifa Stars iliibuka na ushindi wa bao 1-0 lililofungwa na mshambuliaji Thuweni Ally.
Katika mechi ya marudiano iliyochezwa mjini Ndola, Zambia ilikuwa mbele kwa bao 1-0 hadi Tino alipoifungia Taifa Stars bao la kusawazisha na hivyo kuiwezesha kusonga mbele kwa ushindi wa jumla wa mabao 2-1.
Hata hivyo, Taifa Stars haikuweza kufanya vizuri katika fainali za michuano hiyo zilizochezwa mjini Lagos, Nigeria baada ya kufungwa mechi mbili na kuambulia sare mechi moja.
Katika mechi yake ya kwanza, Taifa Stars ilikubali kipigo cha mabao 3-2 kutoka kwa Nigeria. Mabao ya Nigeria yalifungwa na Lawal, Onyedika na Odegbami wakati bao la kujifariji la Taifa Stars lilifungwa na Thuweni.
Taifa Stars ilikubali tena kipigo katika mechi yake ya pili dhidi ya Misri, ambapo ilichapwa mabao 2-1. Mabao ya Misri yalifungwa na Hassan Shehata na Mosaad Nour wakati bao la Stars lilifungwa na Thuweni.
Katika mechi yake ya mwisho, Taifa Stars iliilazimisha Ivory Coast kutoka nayo sare ya bao 1-1. Bao la Ivory Coast lilifungwa na Kobenan wakati lile la Stars lilifungwa na Thuweni.
Kufuatia matokeo hayo, Taifa Stars ilimaliza mechi za kundi lake ikiwa ya mwisho baada ya kuambilia pointi moja wakati Nigeria ilishika usukani kwa kuwa na pointi tano.
Hatua nyingine ya juu iliyofikiwa na Taifa Stars katika michuano ya kimataifa ni kufuzu kucheza fainali za CAN mwaka 2009 nchini Ivory Coast baada ya kuitoa Sudan.
Katika mechi yake ya kwanza, Taifa Stars ilipigwa mweleka wa bao 1-0 na Senegal kabla ya kuibuka na ushindi wa idadi hiyo ya bao dhidi ya Ivory Coast.
Hata hivyo, matumaini ya Stars kusonga mbele yalizimwa na Zambia baada ya kulazimishwa kutoka sare ya bao 1-1. Zambia ndiyo iliyoongoza kundi hilo na kufuzu kucheza nusu fainali.
Rekodi nyingine ya kujivunia kwa Taifa Stars ni kufuzu kucheza hatua ya nusu fainali katika michezo ya All Africa Games iliyofanyika mwaka 1973 mjini Lagos, Nigeria.
Katika michuano hiyo iliyochezwa kwa mtindo wa ligi, Taifa Stars ilitoka sare mechi mbili dhidi ya Nigeria na Misri na kufungwa mechi ya mwisho mabao 2-1 na Algeria.
Kabla ya hatua hiyo, Taifa Stars ilitoka suluhu na Nigeria A, ikaichapa Nigeria B mabao 2-1 kabla ya kutoa kipigo cha bao 1-0 kwa Ghana na Togo. Mshambuliaji Maulid Dilunga ndiye aliyeibeba Taifa Stars baada ya kuifungia mabao yote kwenye michuano hiyo.
Taifa Stars haijawahi kufika hatua za mbali katika michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia. Mara zote ilizoshiriki, imekuwa ikitolewa aidha raundi ya kwanza ama ya pili.
Katika michuano ya Kombe la Chalenji, Tanzania Bara ililitwaa kombe hilo kwa mara ya kwanza mwaka 1974 kabla ya kusubiri kwa miaka 20 na kulitwaa tena mwaka 1994. Bara ilitwaa kombe hilo kwa mara ya mwisho mwaka 2010 baada ya kuifunga Ivory Coast bao 1-0 kwa njia ya penalti katika mechi ya fainali.
Kwa upande wa timu za taifa za vijana, hatua pekee ya juu ilifikiwa na timu ya vijana wa chini ya miaka 17, Serengeti Boys mwaka 2004, ilipofuzu kucheza fainali za Afrika baada ya kuitoa Zimbabwe.
Hata hivyo, Shirikisho la Soka Afrika (CAF), liliiengua Serengeti Boys kushiriki kwenye fainali hizo zilizofanyika Gambia baada ya kubainika kuwa, ilimchezesha mchezaji Nurdin Bakari, ambaye umri wake ulikuwa zaidi ya miaka 17.
Mbali na Serengeti Boys kuenguliwa kwenye fainali hizo, CAF pia iliifungia Tanzania kushiriki kwenye michuano inayozingatia umri kwa kipindi cha miaka miwili kwa kosa hilo.
Timu ya vijana wa chini ya umri wa miaka 20, Ngorongoro Heroes haijawahi kufika mbali katika michuano yote iliyoshiriki kama ilivyokuwa kwa timu ya vijana wa chini ya miaka 23, Vijana Stars. Timu hizo zimekuwa zikitolewa hatua ya awali kila ziliposhiriki michuano ya Afrika na ile ya Olimpiki.
Timu ya taifa ya wanawake, Twiga Stars iliyoanzishwa mwanzoni mwa miaka ya 2000, imekuwa ikijitutumia katika michuano ya Afrika na kufuzu kucheza fainali mara mbili.
Mara ya kwanza ilikuwa mwaka juzi ilipofuzu kucheza fainali hizo nchini Afrika Kusini kabla ya kufuzu kucheza fainali za All African Games zilizofanyika mwaka huu nchini Msumbiji.
Katika fainali za mwaka juzi, Twiga Stars ilishindwa kufanya vizuri kutokana na wachezaji wake kutokuwa na uzoefu wa kutosha katika michuano ya kimataifa.
Akina dada hao walipoteza mechi zote tatu za hatua ya makundi, ambapo katika mechi ya kwanza, walichapwa mabao 2-1 na wenyeji Afrika Kusini. Katika mechi yake ya pili, Twiga Stars ilichapwa mabao 3-2 na Mali kabla ya kucharazwa mabao 3-0 na Nigeria.
Twiga Stars pia ilichemsha katika fainali za mwaka huu za All Africa Games zilizofanyika mjini Maputo, Msumbiji. Katika mechi yake ya kwanza, ilitoka sare ya mabao 2-2 na Afrika Kusini, ikachapwa mabao 2-1 na Ghana kabla ya kufungwa idadi hiyo ya mabao Zimbabwe.

Simba ndiyo timu pekee iliyoweka rekodi ya juu katika michuano ya kimataifa, ambapo mwaka 1993 ilifuzu kucheza fainali ya Kombe la CAF, lakini ikafungwa na Stella Abidjan ya Ivory Coast.
Katika mechi ya awali ya fainali iliyochezwa mjini Abidjan, timu hizo mbili zilishindwa kutambiana baada ya kutoka suluhu. Simba ilicheza fainali hiyo ikiwa chini ya makocha Abdalla Kibadeni na Eshente kutoka Ethiopia.
Matokeo hayo yaliwapa imani kubwa mashabiki wa soka nchini kwamba, huenda Simba ingeweka rekodi ya kuwa timu ya kwanza ya Tanzania kutwaa taji la Afrika.
Maandalizi kabambe ya kusherehekea ushindi yalifanyika. Kamati maalumu zikaundwa kwa ajili ya kuhakikisha ushindi unapatikana nyumbani na kanga zikachapishwa zikiwa na maandishi ‘Simba Bingwa CAF 1993’.
Hata hivyo, mambo yaligeuka katika mechi ya marudiano iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Katika mechi hiyo, iliyoweka rekodi ya kuhudhuriwa na mashabiki lukuki, Simba ilichezea kichapo cha mabao 2-0.
Kipigo hicho kilizusha huzuni kubwa, si kwa wachezaji tu wa Simba, bali hata kwa viongozi, wanachama na mashabiki wa klabu hiyo, ambao walishuhudia Rais Ali Hassan Mwinyi akikabidhi kombe la ubingwa kwa nahodha wa Stella Abidjan.
Kabla ya kufuzu kucheza fainali hiyo, Simba ilikuwa imeweka rekodi ya kuwa timu ya kwanza ya Tanzania kutinga hatua ya nusu fainali ya michuano ya klabu bingwa Afrika mwaka 1974 huku ikitoa vichapo kwa vigogo kadhaa vya soka. Ilicheza hatua hiyo ikiwa chini ya Kocha Nabi Camara kutoka Guinea.
Katika mechi ya awali ya nusu fainali iliyochezwa mjini Dar es Salaam, Simba iliichapa Mehala El-Kubra ya Misri bao 1-0, lakini ikatolewa kwa njia ya penalti baada ya Wamisri kushinda mechi ya marudiano kwa idadi hiyo ya bao.
Simba pia iliweka rekodi ya kufuzu kucheza ligi ya mabingwa wa Afrika hatua ya makundi mwaka 2003, ikiwa chini ya Kocha James Siang'a kutoka Kenya, baada ya kuwatoa waliokuwa mabingwa watetezi, Zamalek ya Misri kwa njia ya penalti, kufuatia matokeo ya jumla kuwa sare ya bao 1-1.
Katika hatua hiyo ya makundi, Simba ilishinda mechi mbili kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, dhidi ya Enyimba na ASEC, lakini ikakubali vipigo vitatu ugenini. Ilimaliza hatua hiyo ikiwa ya pili kutoka mkiani.
Rekodi zingine za kujivunia kwa Simba ni kuweza kuziadhiri timu vigogo za Misri katika mechi tofauti za michuano ya kimataifa. Mwaka 1974 iliichapa mehara El-Kubra bao 1-0 mjini Dar es Salaam, miaka tisa baadaye iliicharaza Al-Ahly mabao 2-1 mjini Mwanza, mwaka 1995 iliinyuka Arab Contractors mabao 3-1 kabla ya kuilaza Ismailia bao 1-0 mjini Dar es Salaam.
Pengine rekodi pekee ya kujivunia kwa Simba ni kutwaa ubingwa wa michuano ya klabu za Afrika Mashariki na Kati (sasa Kombe la Kagame) miaka ya 1974, 1991, 1992, 1995, 1996 na 2002. Ndio timu pekee iliyotwaa kombe hilo mara nyingi, ikilinganishwa na klabu zingine za ukanda huu.
YANGAYanga ni timu nyingine ya Tanzania iliyoweka rekodi ya kufuzu kucheza robo fainali ya michuano ya klabu bingwa Afrika mara mbili mwaka 1969 na 1970, lakini mara zote ilitolewa na Asante Kotoko ya Ghana.
Katika robo fainali ya mwaka 1969, Yanga ilitolewa na Asante Kotoko kwa njia ya kura ya shilingi baada ya matokeo ya jumla kuwa sare ya bao 1-1.
Katika robo fainali ya pili mwaka 1970, Yanga ilikutana tena na Asante Kotoko, ambapo katika mechi ya awali, zilitoka sare ya bao 1-1 na katika mechi ya marudiano, hazikufungana.
Mshindi wa pambano hilo ilibidi apatikane katika muda wa nyongeza, lakini kutokana na giza kutanda uwanjani, mechi ilivunjika dakika ya 19 na hivyo kuhamishiwa kwenye uwanja huru wa mjini Addis Ababa, Ethiopia.
Katika mechi hiyo ya tatu, Yanga ilikubali kipigo cha mabao 2-0 kutoka kwa Asante Kotoko na kutolewa kwenye hatua hiyo. Kikosi cha Yanga wakati huo kilikuwa chini ya Victor Stanculescu kutoka Romania.
Yanga pia iliweka rekodi ya kuwa timu ya kwanza katika ukanda wa Afrika Mashariki kufuzu kucheza ligi ya mabingwa wa Afrika mwaka 1998, ikiwa chini ya kocha Raoul Shungu kutoka Congo, lakini ilivurunda kwenye hatua ya makundi. Ligi hiyo ilianzishwa rasmi mwaka 1997.
Timu hiyo kongwe nchini ilimaliza mechi za makundi ikiwa mkiani baada ya kupokea kipigo cha mabao 3-0 kutoka kwa ASEC ya Ivory Coast katika mechi yake ya mwisho iliyochezwa mjini Dar es Salaam.
Katika hatua hiyo ya makundi, Yanga pia ilipokea kipigo kizito cha mabao 6-0 kutoka kwa Raja Casablanca ya Morocco na kutoka sare ya bao 1-1 na Manning Rangers ya Afrika Kusini.
Rekodi pekee ya kujivunia kwa Yanga ni ile ya kutwaa ubingwa wa klabu za Afrika Mashariki na Kati mara nne, mwaka 1975, 1993, 1999 na 2010.
Klabu zingine za Tanzania zilizowahi kushiriki michuano ya Afrika ni Cosmopolitan (1967), Mseto (1975), Pan African (1982), Tukuyu Stars (1986), Coastal Union (1988), Mtibwa Sugar (1999 na 2000), lakini zote ziliishia hatua ya awali.

KITWANA MANARA; Tumepiga hatua kimaendeleo, si kimashindano

KITWANA Manara (kushoto) akiwa na mwanasoka mwenzake mkongwe, Peter Tino



KAMA kuna mwanasoka aliyewahi kuweka rekodi ya pekee na ya aina yake hapa nchini, si mwingine zaidi ya mkongwe Kitwana Manara.Ndiye mchezaji pekee aliyeweza kucheza nafasi ya kipa kwenye kikosi cha timu ya taifa, Taifa Stars na nafasi ya mshambuliaji kwenye klabu yake ya Yanga.
Mkongwe huyo pia ndiye mchezaji pekee aliyeweka rekodi ya kucheza soka kwa miaka mingi kuliko mchezaji mwingine yeyote Tanzania. Alianza kucheza soka mwaka 1960 na kutundika daruga zake ukutani mwaka 1980.
Manara alianza kuvaa jezi za Taifa Stars mwaka 1961 akitokea klabu ya Cosmo ya Dar es Salaam. Alistaafu kuichezea timu hiyo mwaka 1975 akiwa klabu ya Yanga.
Alikuwa miongoni mwa wachezaji wa Yanga walioiwezesha timu hiyo kuwa ya kwanza nchini kufuzu kucheza robo fainali ya michuano ya klabu bingwa Afrika mara mbili, 1969 na 1970.
Katika hatua zote hizo mbili, Yanga ilitolewa na Asante Kotoko ya Ghana, ambapo katika robo fainali ya mwaka 1969, iliondoshwa kwa njia ya kura ya shilingi baada ya matokeo ya jumla kuwa sare ya bao 1-1.
Katika robo fainali ya pili mwaka 1970, Yanga ilikutana tena na Asante Kotoko, ambapo katika mechi ya awali, zilitoka sare ya bao 1-1 na katika mechi ya marudiano, hazikufungana.
Mshindi wa pambano hilo ilibidi apatikane katika muda wa nyongeza, lakini kutokana na giza kutanda uwanjani, mechi ilivunjika dakika ya 19 na hivyo kuhamishiwa kwenye uwanja huru wa mjini Addis Ababa, Ethiopia.
Katika mechi hiyo ya tatu, Yanga ilikubali kipigo cha mabao 2-0 kutoka kwa Asante Kotoko na kutolewa kwenye hatua hiyo. Kikosi cha Yanga wakati huo kilikuwa chini ya Victor Stanculescu kutoka Romania.
Manara pia alikuwa miongoni mwa wachezaji walioiwezesha Taifa Stars kufuzu kucheza michezo ya All Africa Games mwaka 1973 na kutinga nusu fainali, ambapo ilitolewa na Algeria baada ya kuchapwa mabao 2-1.
“Kwa kweli kama ni rekodi ya mwanasoka aliyecheza soka kwa miaka mingi hapa nchini na kwa nafasi mbili tofauti, hakuna anayeweza kuifikia rekodi yangu,”alisema. “Mimi nilianza kuichezea timu ya taifa kuanzia kwenye michuano ya Gossage hadi ilipobadilishwa jina na kuitwa Chalenji.”
Akizungumza na Uhuru hivi karibuni kuhusu mafanikio ya soka katika miaka ya 50 ya Uhuru, Manara alisema Tanzania imepiga hatua kubwa na kupata mafanikio ya kuridhisha.
Akitoa mfano, Manara alisema japokuwa kiwango cha uchezaji soka miaka ya nyuma kilikuwa juu ikilinganishwa na hivi sasa, kuwepo kwa vifaa vingi vya michezo na viwanja vya kisasa vya kuchezea mchezo huo ni miongoni mwa mafanikio makubwa yaliyopatikana.
Alisema miaka ya nyuma, vifaa vya michezo vilikuwa vichache na viwanja vilivyotumika kuchezea mchezo huo vilikuwa vya kawaida.
“Hivi sasa, timu yetu ya taifa imepata udhamini mkubwa, wachezaji wanalipwa vizuri, klabu zinamiliki viwanja vyao vya kuchezea soka, haya yote kwangu mimi ni mafanikio makubwa,”alisema.
Manara pia alieleza kufurahishwa kwake kuona Taifa Stars ikipata maandalizi kama ilivyo kwa baadhi ya nchi za mataifa ya Ulaya huku ikipatiwa huduma zote muhimu.
Alisema miaka ya nyuma, ilikuwa vigumu kwa mashabiki kujitokeza kwa wingi kuishangilia timu hiyo kila ilipocheza ama kuhamasika na kuvaa fulana zenye rangi ya bendera ya taifa.
Manara alisema pia kuwa, soka inayochezwa hivi sasa ni ya kasi ikilinganishwa na miaka ya nyuma, lakini baadhi ya vitu vinavyofanywa na wanasoka maarufu duniani kama vile Lionel Messi wa Barcelona ya Hispania si vigeni kwa Tanzania.
Aliwataja baadhi ya wanasoka wa zamani waliokuwa na uwezo wa kucheza na mpira wanavyotaka, kupiga chenga na kupangua idadi kubwa ya mabeki kwa wakati mmoja kuwa ni pamoja na Mbwana Abushiri, Emily Kondo, Arthur Mambeta, Sunday Manara na Abdalla Kibadeni.
Alisema uwezo wa wanasoka hao haukuweza kutambulika kimataifa kutokana na kutokuwepo kwa vyombo vingi vya habari kwa ajili ya kuwatangaza. Alisema vyombo vilivyokuwepo wakati huo kama vile magazeti, vilikuwa vichache na teknolojia ya televisheni haikuwepo.
Manara alisema Tanzania ni nchi pekee kwa nchi za ukanda wa Afrika Mashariki iliyoweza kutoa wanasoka wengi nyota, ikilinganishwa na nchi za Kenya na Uganda.
Akizungumzia uongozi wa soka nchini, Manara alisema viongozi wa zamani wa klabu hawakuwa na elimu kubwa, lakini waliweza kubuni vitu vingi na kuziletea mafanikio makubwa klabu zao.
Akitoa mfano, alisema viongozi wa Yanga waliweza kununua nyumba mtaa wa Mafia kwa sh. milioni 11 kutokana na mapato ya sh. milioni 20 katika mechi kati yao na Abaluya ya Kenya na siku hiyo wachezaji hawakulipwa hata nauli.
“Hivyo utaona kuwa, uongozi wa zamani ulikuwa wa kujitolea zaidi na viongozi walihakikisha kila mchezaji anatafutiwa kazi na walicheza kwa moyo kwa sababu walikuwa wanachama wa klabu wanazochezea hivyo ilikuwa vigumu kuzihujumu,”alisema.
Alisema viongozi wa sasa wa klabu wana elimu kubwa, lakini wanakosa ubunifu na mashabiki wa klabu kongwe za Simba na Yanga wamekosa imani kwa viongozi wao, hasa timu zao zinapofungwa katika mechi muhimu.
Mkongwe huyo alisema ubunifu wa viongozi wa zamani ulianza kutoweka miaka ya 1976, ambapo klabu za Simba na Yanga zilianza kutawaliwa na migogoro mingi, iliyosababisha zigawanyike.
Alisema migogoro hiyo ndiyo iliyosababisha klabu ya Yanga kugawanyika na kuzaliwa Pan African na ile ya Simba nayo kugawanyika na kuzaliwa Nyota Nyekundu.
Manara alisema migogoro ya mara kwa mara ndani ya klabu hizo, ilichangia kwa kiasi kikubwa kudumaza maendeleo ya soka na timu ya taifa kwa vile Simba na Yanga ndizo zinazotoa mchango mkubwa kwenye timu ya taifa.
“Asikudanganye mtu, mafanikio ya Taifa Stars yanapaswa kuanzia klabuni. Kukiwa na migogoro kwenye klabu hizo mbili, timu yetu ya taifa nayo itakuwa mbovu,”alisema.
Manara ameupongeza uongozi wa sasa wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa kuleta mageuzi makubwa katika mchezo huo, ikiwa ni pamoja na kurejesha nidhamu kwa viongozi na kuleta utendaji mzuri.
“Kwa kweli mabadiliko katika uongozi wa chama cha soka yameonekana. Zamani pale uwanja wa Karume kulikuwa na jengo dogo tu kwa ajili ya ofisi za chama, lakini hivi sasa kuna ghorofa na uwanja wa kisasa wa mazoezi. Haya ni mafanikio makubwa,”alisema.
“Serikali nayo imejitahidi sana kutuletea makocha wa kigeni kwa ajili ya timu ya taifa na wachezaji wamekuwa wakihamasika kuichezea. Haya nayo ni mafanikio makubwa,”aliongeza.
Manara alimmwagia sifa kemkem Rais wa TFF, Leodegar Tenga kuwa ni kiongoni pekee aliyeleta mageuzi makubwa katika uongozi wa soka nchini na pia kuleta heshima kwa chama hicho.
Alisema nidhamu ndani ya shirikisho hilo imekuwa kubwa na kamati zimeachwa zifanyekazi zake kwa uhuru mkubwa bila ya kuingiliwa.
“Kwa kweli hajatokea kiongozi aliyeleta amani na utulivu katika chama cha soka kama Tenga. Waswahili wanasema, mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni. Tenga anastahili pongezi,”alisema.
Hata hivyo, Manara alisema wapo viongozi wengine wa chama hicho waliofanya vizuri huko nyuma, lakini hakuna anayeweza kufikia rekodi ya Tenga.
Manara amelitaka shirikisho hilo kufanya jitihada zaidi liwe na uwanja wake wa kuchezea soka kwa ajili ya kuongeza mapato yake, tofauti na ilivyo sasa, ambapo linategemea zaidi mgawo wa mechi za ligi kuu na za kimataifa.
Ameiomba serikali ifikirie kupunguza kodi kwenye vifaa vya michezo ili vijana wengi zaidi waweze kumudu kuvinunua na hivyo kuongeza hamasa kwao ya kushiriki katika mchezo huo.
Manara pia ametoa mwito kwa viongozi wa klabu na vyama vya soka, wawe wabunifu wa vyanzo vya mapato na uendeshaji wa mchezo huo kisasa zaidi badala ya kuweka mbele maslahi yao binafsi.
"Umefika wakati sasa, lazima kuwe na mabadiliko. Kiongozi anapochaguliwa kuongoza klabu, awe mtendaji wa kazi anayeipenda klabu yake. Asiwe mtu wa kuweka mbele mapato,"alisema.
Amewataka wanasoka wa Tanzania waone thamani ya kucheza soka kwa sababu mpira ni ajira na mchezaji anaweza kulipwa mamilioni ya shilingi kwa ajili ya usajili pekee.
“Kama mchezaji anaweza kulipwa milioni 60 kwa msimu, anapaswa kuuheshimu mpira katika maisha yake kwa sababu ndiyo ajira yake,”aliongeza.
Amewataka viongozi wa klabu kuzithamini timu za vijana kwa vile ndizo chimbuko la wanasoka. Alisema timu hizo zinapaswa kupewa huduma zote muhimu kama ilivyo kwa timu za wakubwa ikiwa ni pamoja na kuzipatia usafiri wa uhakika.
Manara alianza kucheza soka katika timu za mitaani za Sambwisi, Young Boys, Cosmo, TPC ya Arusha, Feisal na baadaye Yanga na Pan African. Alistaafu rasmi kucheza soka mwaka 1983 akiwa Yanga, ambayo katika miaka miwili ya mwisho, aliifundisha akiwa kocha mchezaji.

JELLA MTAGWA; Nahodha aliyeiongoza Stars kwa miaka 10

Jella Mtagwa

HII ni stempu ya lililokuwa shirika la posta na simu wakaati huo


HAKUNA kitu kilichowahi kumkera mwanasoka mkongwe nchini, Jella Mtagwa katika maisha yake kisoka, kama picha yake kutumika kwenye stempu ya lililokuwa Shirika la Posta, bila ridhaa yake. Tukio hilo lilitokea mwaka 1982, kipindi ambacho Jella bado alikuwa aking'ara kisoka.
Jella (58) hakuhusishwa kwa lolote kuhusu uamuzi huo na wala hakulipwa hata senti moja. Alishtukia tu picha yake ikiwa imewekwa kwenye moja ya stempu zilizokuwa zikitumiwa na Posta wakati huo.
Alipouliza kwa viongozi wa kilichokuwa Chama cha Soka nchini (FAT) wakati huo, Saidi El Maamry (mwenyekiti) na marehemu Patrick Songora (katibu), jibu alilopewa ni kwamba, Posta waliomba kwa chama hicho kiwapatie jina la mchezaji wanayeona anafaa picha yake kuwekwa kwenye stempu kama kivutio na kuitangaza Tanzania kimataifa.
Viongozi hao wawili walimweleza Jella kwamba, waliamua kumpendekeza yeye kwa vile alitoa mchango mkubwa katika kikosi cha timu ya Taifa, Taifa Stars kilichofuzu kucheza fainali za Afrika mwaka 1980 na pia alikuwa mchezaji bora wa ligi msimu wa 1981/1982.
Kwa sasa, Jella hajihusishi na lolote katika mchezo wa soka kama ilivyo kwa baadhi ya wanasoka wenzake wa zamani, kutokana na kupatwa na maradhi ya kupooza baadhi ya viungo vyake vya mwili. Alipatwa na maradhi hayo miaka takriban mitatu iliyopita.
Hata hivyo, hali ya Jella kwa sasa ina nafuu kwani anaweza kutembea umbali mrefu kwa ajili ya kujipa mazoezi. Ameshauriwa kufanya hivyo na madaktari. Na kutokana na kuwa mdau wa soka, hupenda sana kutembelea jengo la makao makuu ya klabu ya Pan Africa, lililopo mtaa wa Swahili, Dar es Salaam. Akizungumza na Uhuru mjini Dar es Salaam hivi karibuni kuhusu mafanikio ya mchezo wa soka katika miaka 50 ya uhuru, Jella alisema Tanzania imepiga hatua kubwa hasa kutokana na uwazi uliopo katika Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na pia Taifa Stars kufanya vizuri katika michuano ya kimataifa.
Hata hivyo, Jella alisema wachezaji wengi waliopo kwenye kikosi hicho hivi sasa, hawajapitia misingi mizuri ya soka tangu wakiwa wadogo, ndio sababu timu hiyo inashindwa kupata mafanikio makubwa zaidi kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.
Jella ameishauri TFF kuwatumia wanasoka wakongwe, hasa waliocheza fainali za Afrika mwaka 1980 kwa ajili ya kutoa ushauri kwa wachezaji wa Taifa Stars ili waweze kufanya vizuri katika michuano ya kimataifa.
"Nadhani huu unaweza kuwa msaada na mchango wetu mkubwa kwa Taifa Stars kwa sababu baadhi yetu tulicheza soka na kupata mafanikio makubwa. Tunaweza kuwaeleza mengi kuhusu mbinu za soka kuliko watu wengine,"alisema. Mkongwe huyo anayeishi maeneo ya Manzese Friends Corner, Dar es Salaam, amemtaka mshambuliaji nyota wa zamani wa Yanga na Pan African, Sunday Manara kuwa ndiye mchezaji pekee aliyekuwa akimsumbua kila alipokutana naye uwanjani.
Baadaye alikuja kuvutiwa na Zamoyoni Mogella, lakini kwa sasa haoni mchezaji yeyote mwenye mvuto licha ya kuwepo kwa wachezaji kadhaa nyota kwenye ligi kuu walionunuliwa kwa mamilioni ya pesa.
Jella alikuwa miongoni mwa wachezaji walioiwezesha Taifa Stars kucheza fainali za Afrika kwa mara ya kwanza mwaka 1980 mjini Lagos, Nigeria. Ndiye aliyekuwa nahodha wa timu hiyo, iliyokuwa ikiundwa na nyota wengi kama vile Leodegar Tenga, Thuweni Ally, Peter Tino, Hussein Ngulungu, Juma Pondamali na wengineo.
Hata hivyo, Taifa Stars haikuweza kufanya vizuri katika fainali hizo. Katika mechi yake ya kwanza, ilichapwa mabao 3-1 na Nigeria, ilifungwa mabao 2-1 na Misri kabla ya kuilazimisha Ivory Coast kutoka nayo sare ya bao 1-1. Katika mechi zote hizo, mabao ya Taifa Stars yalifungwa na Thuweni.
Jella alianza kucheza soka tangu alipokuwa akisoma katika shule ya msingi ya Mwembesongo ya mkoani Morogoro. Kwake mpira ulikuwa ni kipaji alichojaliwa na Mungu kwani enzi zake, alikuwa beki wa aina yake na asiyetishwa ama kubabaishwa na mshambuliaji yeyote.
Alianza kucheza soka ya ushindani mwaka 1970 katika timu ya Nyota Afrika ya Morogoro. Aliteuliwa kuichezea timu ya mkoa huo katika mashindano ya Kombe la Taifa mwaka 1973, ambapo ilitwaa ubingwa baada ya kuichapa Tanga mabao 2-1 katika mechi ya fainali iliyochezwa uwanja wa Nyamagana, Mwanza.
Mwaka huo huo, akiwa bado anasoma shule ya sekondari ya Morogoro, uongozi wa Yanga uliokuwa chini ya mwenyekiti Tabu Mangara na meneja, Shirazi Sharrifu, ulivutiwa na kipaji chake na kuamua kumsajili. Akawa anaichezea Yanga huku akiendelea na masomo.
Alihamia rasmi katika Jiji la Dar es Salaam mwaka 1975 baada ya kumaliza masomo ya sekondari. Kikosi cha Yanga wakati huo kilikuwa kinaundwa na baadhi ya wachezaji kadhaa nyota kama vile Maulid Dilunga, Elias Michael, Abdalah Juma, Muhidin Fadhili, Athuman Kilambo, Omari Kapera, Leonard Chetete na wengineo.
Jella alikuwa miongoni mwa wachezaji walioiwezesha Yanga kutwaa ubingwa wa klabu za Afrika Mashariki na Kati mwaka 1975 baada ya kuwabwaga watani wao wa jadi Simba mabao 2-0 katika mechi ya fainali iliyopigwa Zanzibar.
Aliitwa kwenye kikosi cha Taifa Stars kwa mara ya kwanza mwaka 1973 na kushiriki kwenye michuano ya Kombe la Chalenji, lakini walitolewa kwenye fainali baada ya kufungwa na Uganda mabao 2-1. Jella hakupewa nafasi ya kucheza kwenye michuano hiyo iliyofanyika mjini Kampala kutokana na umri wake kuwa mdogo.
Jella aliteuliwa kuwa nahodha wa Taifa Stars mwaka 1973 kutoka kwa Omari Zimbwe. Alishika wadhifa huo hadi mwaka 1983, ambapo nafasi hiyo ikaenda kwa kiungo Charles Boniface. Aliichezea Taifa Stars kwa miaka 10.
Mkongwe huyo aliamua kustaafu soka mwaka 1984 akiwa Pan African baada ya kuumia goti. Alilazimika kufanyiwa operesheni na daktari bingwa wa mifupa, Profesa Phillemon Sarungi.
Ameitaja sababu kubwa iliyomfanya aihame Yanga kuwa, ni mgogoro uliotokea mwaka 1976, ambao ndio uliosababisha kugawanyika kwa klabu hiyo na kuundwa kwa Pan Africa. Alikuwa mmoja wa wachezaji waanzilishi wa Pan Africa.

PETER TINO; Mwanasoka aliyeipeleka Stars fainali za Afrika 1980


Peter Tino (kulia) akiwa na mwanasoka mwenzake mkongwe, Kitwana Manara


IKUWA Agosti 26,1979 wakati timu ya soka ya Taifa, Taifa Stars ilipokuwa ikirudiana na timu ya soka ya Taifa ya Zambia katika mechi ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika za mwaka 1980 zilizofanyika nchini Nigeria.Pambano hilo lilichezwa mjini Ndola.
Mechi hiyo ilikuwa na umuhimu mkubwa kwa Taifa Stars kwa vile ilikuwa ikihitaji sare ya aina yeyote ili iweke historia ya kufuzu kucheza fainali hizo kwa mara ya kwanza , tangu ilipoanza kushiriki michuano hiyo mwaka 1968.
Katika mechi ya kwanza iliyochezwa wiki mbili nyuma kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Taifa Stars iliishinda Zambia bao 1-0. Bao hilo lilifungwa na kiungo Mohammed Rishard Adolph.
Ushindi huo ulipatikana kwa mbinde kiasi kwamba mashabiki wengi hawakuwa na imani iwapo Taifa Stars ingeshinda ama kupata sare katika mechi ya marudiano. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa kwani Wazambia walifanikiwa kupata bao la kuongoza dakika za mapema na kudumu nalo kwa takriban dakika 86.
Zikiwa zimesalia dakika tatu pambano hilo kumalizika, mshambuliaji mrefu mwenye kasi na mashuti makali, Peter Tino alibadili sura ya mchezo na kufanya kile kilichokuwa kikisubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa mchezo huo nchini.
Ilipigwa kona kwenye lango la Taifa Stars, kipa Juma Pondamali akaupangua mpira kwa ngumi, ukamkuta kiungo Leodegar Tenga, aliyetoa pasi ndefu kwa kiungo mwenzake, Hussein Ngulungu, ambaye naye alitoa pasi ndefu kwa Tino.
Akiwa amezungukwa na mabeki watatu wa Zambia, Tino alilazimika kupiga hesabu za haraka haraka. Aliwachomoka mbio mabeki nao na kukimbia na mpira kwa kasi. Alipofika nje kidogo ya eneo la hatari la Zambia, alifumua shuti kali la mguu wa kulia, lililompita kipa Shileshi wa Zambia na mpira kutinga wavuni.Bao hilo lilipatikana baada ya pasi tatu.
Katika mechi hiyo, Taifa Stars iliwakilishwa na kipa Juma Pondamali,mabeki ni Leopard Tasso, Mohammed Kajole/ Ahmed Amasha, Salim Amir, Jella Mtagwa, viungo ni Leodegar Tenga, Hussein Ngulungu na washambulaji ni Omari Hussein, Peter Tino, Mohamed Salim na Thuweni Ally.
Kikosi hicho kilichokuwa chini ya Kocha Slowmir Work kutoka Poland, akisaidiwa na Joel Bendera na Ray Gama, ndicho kilichoiwakilisha Tanzania katika fainali za kombe hilo zilizofanyika nchini Nigeria.
Katika fainali hizo, Taifa Stars ilichapwa mabao 3-1 na wenyeji Nigeria katika mechi ya ufunguzi, ilitoka sare ya mabao 2-2 na Ivory Coast kabla ya kuchapwa mabao 2-1 na Misri na kutolewa hatua ya makundi.
Hivi sasa Tino hajihusishi kabisa na masuala ya soka, si kwa kazi ya ukocha wala uongozi. Aliamua kutundika daruga zake ukutani mwishoni mwa miaka ya 1980 akiwa klabu ya Yanga. Alistaafu soka kwa kile alichodai kuwa, mwili wake umechoka na pia alitaka kutoa nafasi kwa wanasoka chipukizi kuonyesha vipaji vyao.
Akizungumzia maendeleo ya soka hivi sasa hapa nchini, Tino alisema ni mazuri hasa ikizingatiwa kuwa, serikali ipo mstari wa mbele kuihudumia timu ya taifa na pia wamejitokeza wafadhili wengi, lakini tatizo lipo kwa wachezaji.
Alisema wanasoka wa Tanzania kwa sasa, kuanzia ngazi ya klabu hadi taifa, hawana upendo miongoni mwao, hawajitunzi, wanabweteka na sifa na wameweka mbele zaidi anasa, tofauti na wachezaji wa zamani.
"Enzi zetu hatukuwa tukibweteka na sifa za wapenzi. Binafsi nimechezea timu ya taifa kwa miaka minane mfululizo kwa sababu nilijitunza na sikuwa nikiendekeza anasa,"alisema.
"Lakini sasa hivi, mchezaji msimu wa kwanza anachezea Yanga, wa pili Simba, mara msimu huu anacheza vizuri, msimu unaofuata anavurunda," aliongeza.
Tino alisema enzi zao, kila walipokuwa wakisifiwa na mashabiki, walijiona kama vile wanadanganywa na bado hawajafika kiwango cha juu, tofauti na hivi sasa, ambapo alidai kuwa, wachezaji huanza kujiona nyota baada ya kucheza soka kwa kipindi kifupi.
Mshambuliaji huyo nyota wa zamani wa klabu za Pan African, African Sports na Yanga alisema, hata mazoezi waliyokuwa wakiyafanya wachezaji wa zamani, ni tofauti na sasa na kwamba, walikuwa na nidhamu ya hali ya juu na waliheshimu makocha na viongozi wao.
"Hivi sasa wapo baadhi ya wachezaji wanawazidi nguvu viongozi na makocha na kuamua wanavyotaka, ndio sababu hata viwango vyao vinashuka haraka. Mchezaji mechi mbili anacheza vizuri, ya tatu kiwango kinashuka," alisema.
Tino alisema maslahi ya wachezaji wa zamani yalikuwa madogo, lakini kwa vile soka ilikuwa kwenye damu yao, walicheza kwa nguvu na kujituma.
Alisema iwapo maslahi wanayopata sasa wachezaji wa Taifa Stars, yangekuwepo enzi zao, Tanzania ingeweza kufuzu kucheza fainali za kombe la Dunia miaka ya 1980.
Akitoa mfano, Tino alisema katika mechi ya mwisho ya michuano ya kucheza fainali za kombe hilo mwaka 1982, Taifa Stars iliilazimisha Nigeria kutoka nayo sare ya bao 1-1 katika mechi ya awali iliyochezwa mjini Lagos. lakini ziliporudiana mjini Dar es Salaam, Taifa Stars ulifungwa mabao 2-0.
"Tulikuwa tukihitaji sare ya bila kufungana ili tufuzu kucheza fainali. Tungekuwa tunapata maslahi mazuri na motisha kama ilivyo sasa, nina hakika tungefuzu kucheza fainali kwani Nigeria wasingetufunga nyumbani,"alisema.
"Hivi sasa Rais Jakaya Kikwete ni mhamasishaji mkuu wa maendeleo ya soka, kampuni nyingi zimejitokeza kuidhamini Taifa Stars na wachezaji wamekuwa wakilipwa mamilioni ya pesa. Enzi zetu ukizungumzia soka, ni wachezaji, chama cha soka na labda waziri mwenye dhamana ya michezo,"aliongeza.
Akizungumzia sababu za kufungwa mara kwa mara kwa Taifa Stars katika mechi za kimataifa zinazochezwa hapa nchini, Tino alisema ni kutokana na matatizo binafsi ya wachezaji.
Tino alisema wanasoka wanaoteuliwa kuichezea Taifa Stars wanashindwa kwenda na kasi ya mchezo, kubadilika kulingana na mchezo unavyoendelea na pia kuondokana na dhana kwamba, kumiliki mpira ndio ushindi.
Mwanasoka huyo mkongwe alisema, kama wachezaji wa Taifa Stars wangekuwa na kawaida ya kuonyesha uwezo wao binafsi, wangeweza kushinda mechi nyingi za kimataifa zinazochezwa hapa nchini.
"Mimi huwa nasikitika sana ninapoona wachezaji wa hapa nchini wanapata huduma nzuri, wanalipwa vizuri, wanaye kocha mzuri, lakini wanakosa juhudi binafsi. Ukibebwa unatakiwa ung'ang'anie," alisisitiza.
Alizitaja kasoro zingine alizozigundua kwa wanasoka wengi wa Tanzania kuwa ni pamoja na kukosa ujanja na mbinu za kimchezo, kutojiamini na kutohamasishana wanapokuwa uwanjani.
Akitoa mfano, Tino alisema mchezaji anaweza kuwa peke yake na mpira, lakini badala ya kuuvuta na kwenda nao mbele, anatoa pasi hovyo kwa kuogopa lawama. Alisema mchezo wa soka ni wa lawama, hivyo wachezaji hawapaswi kuziogopa.
"Ni nadra hivi sasa kuwapata washambuliaji wajanja wajanja kama ilivyokuwa kwa Zamoyoni Mogella, Issa Athumani, Saidi Suedi na wengineo. Vilevile ni nadra kuwakuta wachezaji wakihamasishana uwanjani. Enzi zetu tulikuwa tunaongea kwa kustuana. Hivi sasa, vijana wetu wanacheza kama mabubu," alisema.
Tino alisema kama enzi zao kungekuwepo na televisheni, wachezaji wa sasa wangeweza kujifunza mengi kutoka kwao na kupata akili kuhusu soka.
Mshambuliaji huyo mkongwe pia alieleza kushangazwa kwake na maumbile ya wachezaji wa sasa, ambayo alisema ni tofauti na yale waliyokuwa nayo wachezaji wa zamani. Alisema enzi zao walikuwepo wachezaji wafupi kama vile Omari Hussein na Shaaban Katwila, lakini walikuwa na nguvu na kasi.
Ametoa mwito kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kuteua wasaidizi wa makocha wa kigeni wenye upeo wa mchezo huo. Alisema wasaidizi wanaoteuliwa sasa, wanashindwa kugundua makosa ya wachezaji na kutoa ushauri wa maana kwa makocha wa kigeni.
Tino alizaliwa mwaka 1956 katika hospitali ya Ocean Road mjini Dar es Salaam, akiwa mtoto wa tano katika familia ya watoto tisa wa mzee Peter Agustino. Familia hiyo ilikuwa ikiishi maeneo ya Msimbazi, Dar es Salaam.
Alianza kucheza soka mwaka 1967 katika timu ya mtaani ya Bonde Sports kabla ya kuhamia Young Kinya ya Kariakoo na baadaye Englebeth ya Manzese. Kutokana na kipaji alichokuwa nacho katika soka, aliajiriwa na kiwanda cha nguo cha urafiki na kuichezea kuanzia mwaka 1974 akiwa na marehemu Gibson Sembuli, Adam Juma, Awadh Gesani, Abdulrahman Juma na Wengineo.
Mwaka 1975 alihamia Mwanza na kujiunga na Mwatex, aliyoichezea kwa miezi mitatu. Mwaka huo huo, alikwenda Arusha na kujiunga na klabu ya Kurugenzi kabla ya kuhamia Tanga na kujiunga na African Sports.
Aliichezea African Sports hadi mwaka 1979 akiwa na baadhi ya wachezaji waliong'ara nchini enzi hizo kama vile Abdalla Luo, Kassim Mwabuda, Omar Bawazir, Peter Mhina, Francis Chausa na Mhando Mdeve.
Aliitwa kwenye kikosi cha Taifa Stars kwa mara ya kwanza mwaka 1977 na kuichezea hadi mwaka 1985. Aliichezea timu hiyo kwenye michuano mbalimbali ya awali ya kombe la Chalenji, Kombe la Afrika na Kombe la Dunia.
Mwaka 1980, aliihama African Sports na kujiunga na Pan African ya Dar es Salaam. Aliichezea klabu hiyo kwa miaka minne katika ligi ya Tanzania Bara na michuano ya Kombe la Washindi la Afrika kabla ya kuhamia Yanga hadi alipostaafu soka mwaka 1989.

Tuesday, December 6, 2011

VENGU APATA AHUENI






HALI ya msanii Joseph Shamba 'Vengu' wa kundi la Orijino Komedi inaendelea vizuri na amehamishwa kutoka kwenye chumba cha wagonjwa mahututi (ICU) na kulazwa kwenye wodi ya Mwaisela katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Dar es Salaam.
Vengu, ambaye aliwekwa kwenye chumba hicho kwa zaidi ya miezi miwili kutokana na kusumbuliwa na ugonjwa, ambao bado haujawekwa wazi, alihamishiwa kwenye wodi ya Mwaisela juzi.
Akizungumza baada ya kumtembelea msanii huyo kwenye wodi hiyo juzi ili kujua maendeleo ya afya yake, Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara alisema hali ya Vengu inaendelea vizuri.
Dk. Fenella alikanusha taarifa zilizosambazwa kwenye baadhi ya mitandao ya habari mwishoni mwa wiki iliyopita kwamba Vengu amefariki dunia.
"Binafsi nimemtembelea wodini leo hii (juzi) na kusema kweli hali yake inaendelea vizuri kwa sababu unapotolewa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi na kuhamishiwa wodini, maana yake ni kwamba madaktari wameridhishwa na maendeleo yako,"alisema.
Dk. Fenella alisema kinachofanyika kwa sasa ni msanii huyo kuendelea kutumia dawa alizoandikiwa na madaktari huku akiendelea kufanyiwa uchunguzi zaidi wa afya yake.
Kaka wa msanii huyo,Steven Shamba alisema wanamshukuru Mungu kuona hali ya msanii huyo inaendelea vizuri baada ya kutolewa ICU.
"Tunachoshukuru ni kwamba matibabu yake yanasimamiwa na profesa na kitendo cha kutolewa chumba cha wagonjwa mahututi na kulazwa wodini kinaashiria kwamba maendeleo yake ni mazuri,"alisema.
Kiongozi wa kundi la Orijino Komedi, Sekione David, maarufu kwa jina la Seki alisema, matibabu ya Vengu kwa sasa yanagharamiwa na Rais Jakaya Kikwete hivyo kama kuna umuhimu kwa msanii huyo kupelekwa nje kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi, ndiye pekee mwenye uamuzi huo.
"Watu wengi wamekuwa wakitulalamikia kwamba kwa nini asipelekwe India kupatiwa matibabu. Tunachoweza kusema ni kwamba yanaweza kupatikana hapa hapa, kwa nini apelekwe India? Tunachoshukuru Mungu ni kwamba, matibabu yake yanagharamiwa na Rais Jakaya Kikwete,"alisema.
Seki alieleza kusikitishwa kwake na taarifa potofu zilizosambazwe kwenye mitandao wiki iliyopita, zikidai kwamba msanii huyo amefariki dunia. Alisema taarifa za aina hiyo si nzuri kwa jamii na ni vyema wahusika wapate taarifa sahihi kutoka kwa vyanzo husika vya habari kuliko kukurupuka na kueneza uvumi wa uongo.
Vengu hajaonekana kwenye vipindi vya Orijino Komedi vinavyoonyeshwa na kituo cha televisheni cha TBC 1 kwa takriban miezi miwili sasa kufuatia kulazwa Muhimbili.
Hata hivyo, bado haijawekwa wazi kuhusu ugonjwa unaomsumbua, lakini kuna habari kuwa, anasumbuliwa na maumivu ya kichwa.
Msanii huyo alijipatia umaarufu mkubwa kutokana na kuweza kumwigiza Mwenyekiti wa chama cha TLP, Augustine Mrema kwa mavazi na sauti yake wakati wa maonyesho ya Orijino Komedi.

KOCHA MPYA WA SIMBA ATOA YA MOYONI



Na Ezekiel Kamwaga

KLABU ya soka ya Simba hivi karibuni ilimtangaza Profesa Milovan Cirkovic kuwa kocha wake mkuu akichukua nafasi ya Moses Basena.Cirkovic (inatamkwa Chirkovich) ameingia mkataba wa miezi sita kuifundisha Simba na mkataba huo umeanza rasmi Desemba Mosi mwaka huu.Tovuti ya Simba, www.simba.co.tz ilifanya naye mahojiano hivi karibuni ambapo alieleza kwa kirefu mambo ambayo wapenzi wa Simba na mchezo wa soka nchini kwa ujumla wangependa kuyafahamu.Pata uhondo.

Simba: Karibu tena Simba Sports Club.

Milovan: Ahsante sana. Naipenda Simba. Naipenda Tanzania na kwa kweli nimefurahi kurejea hapa.

Simba: Tanzania na Serbia ni mbali kwelikweli. Kabla hujaja Tanzania kuifundisha Simba kwa mara ya kwanza miaka ya nyuma, je ulikuwa umewahi kusikia chochote kuhusu Simba au Tanzania?

Milovan: Kusema ukweli, sikuwa nimewahi kusikia chochote kuhusu Simba hadi nilipokuja kufundisha. Kila kitu nilikipata hapa kuhusu Simba.Hata hivyo, nilikuwa nafahamu kuhusu nchi ya Tanzania. Nilisoma shuleni na sisi tunafundishwa mengi sana katika jiografia. Na usisahau kuwa mimi nimewahi kuwa mwalimu wa Chuo Kikuu na hivyo kwa wasomi ni rahisi kufahamu mambo ya nchi za mbali.

Simba: Jambo gani ambalo bado unalikumbuka kuhusu Tanzania ulipokuja mara ya kwanza.

Milovan: (Anacheka). Siku moja nilikuwa matembezini na Hagila (Evarist, miongoni mwa waliokuwa viongozi wa Simba wakati Milovan alipokuja mwaka 2007) na ghafla nyani akatokea mbele yetu.Sitaisahau siku hiyo kwa sababu hiyo ndiyo ilikuwa mara ya kwanza kwangu kumwona nyani uso kwa uso. Mara zote nimekuwa nikiwaona kupitia luninga.Hilo nalikumbuka sana.

Simba: Turudi kwenye soka sasa. Hebu kwanza tueleze kwa kifupi historia yako kisoka

Milovan: Ok. Nilizaliwa katika iliyokuwa Yugoslavia ya zamani katika mji wa Cacak (inatamkwa tatak) mwaka 1955.Nilicheza soka hadi kiwango cha daraja la kwanza na niliachana na soka wakati nilipovunjika mguu mpirani wakati nilipokuwa na miaka 31. (Anaonyesha kovu la jeraha lake mguuni).Niliwahi kuchezea klabu maarufu ya Partizan Belgrade na mara baada ya kuumia nikaingia katika masuala ya taaluma kiasi cha kuwa mwalimu katika Chuo Kikuu cha Belgrade.Nina vyeti mbalimbali vya ukocha kuanzia Shahada ya Chuo Kikuu katika Elimu ya Viungo (Physical Education) na nimefundisha pia somo hilo vyuo vikuu na ndiyo maana naitwa Profesa.Nina leseni ya ukocha inayotambuliwa na UEFA, pamoja na vyeti vingine vinavyotambuliwa.

Simba: Kwanini uliamua kuwa kocha wa soka?

Milovan: Mara baada ya kuachana na kucheza soka mapema, niliona njia pekee ya kuendelea kubaki katika mchezo huu ni kuwa kocha.Napenda sana mpira wa miguu na sidhani kama ningeweza kufanya kingine chochote kwenye maisha yangu zaidi ya kucheza au kujihusisha kwa namna yoyote ile na mchezo huu.

Simba: Serbia si miongoni mwa nchi kubwa za Ulaya lakini imekuwa na sifa kubwa ya kutoa makocha wazuri duniani hususani katika nchi za Afrika na Asia. Nini unafikiri ni siri ya mafanikio haya?

Milovan: Kwanza tunapenda sana mpira –sisi raia wa Serbia. Kwa hiyo kuwa kocha au mchezaji mzuri kunakuja tu kwenye damu.Lakini la pili ni kuwa kuna vyuo vingi sana vya ukocha kule kwetu na pia tuna uwezo wa kuishi katika mazingira magumu.Mimi nimekuja Tanzania na sina ndugu, jamaa wala rafiki yeyote. Kila kitu nawaamini ninyi. Inahitaji roho ngumu kidogo kuchukua maamuzi magumu kama haya.Hizo zinaweza kuwa sababu za msingi zaidi.

Simba: Nimesikia kuwa mmoja wa marafiki zako wa karibu zaidi ni Milovan Rajevac, Kocha aliyeipeleka Ghana katika Fainali za Kombe la Dunia mwaka 2010 nchini Afrika. Je taarifa hizi zina ukweli wowote?

Milovan: Milovan ni rafiki yangu. Nilipokuwa kocha wa FC Borak Cacak mwaka 2008, yeye alikuwa msaidizi wangu kwa maana ya kocha msaidizi.Ni rafiki yangu wa karibu sana.

Simba: Nini falsafa yako ya soka? Unataka soka ichezweje na wachezaji wako?

Milovan: Rahisi. Timu zote zinazofundishwa na mimi zinakuwa na sifa ya kucheza soka la pasi nyingi na zinazomiliki mpira.Nataka timu ianze kucheza kuanzia nyuma. Nafahamu kuwa kuna wakati timu inaweza kutengeneza nafasi na kufunga kwa pasi chache lakini si kitu cha kutokea mara kwa mara.Nataka timu icheze kama Barcelona ya Hispania. Mimi nimeanza kuipenda Barcelona zamani kabla hata Josep Guardiola hajawa kocha wa timu hiyo.Siku zote Barcelona imekuwa ikicheza vizuri. Real Madrid inatwaa makombe lakini Barca inacheza soka la kuvutia zaidi. Soka ni burudani na inanoga zaidi kama inaendana na ushindi. Hata Arsenal ya miaka mitano iliyopita ilikuwa inacheza soka ninayoipenda.Ninachokisema ni hivi, Simba si Barcelona. Lakini inaweza kucheza kama Barca kwa kiwango chake. Huo ndiyo mtazamo wangu.

Simba: Kuna wachezaji wowote wa Simba uliowafundisha miaka minne iliyopita na bado unawakumbuka?

Milovan: Namkumbuka Chollo (Nassor Said Masoud), mimi ndiye niliyembadilisha kucheza kutoka kiungo na kuwa mlinzi wa pembeni.Nilimuona tu namna ya uchezaji wake na nikashauriana na wenzangu katika benchi la ufundi kuwa anafaa kuwa mlinzi wa pembeni.Nimefurahi kuwa sasa ni mlinzi wa kulia tegemeo kwa taifa. Namkumbuka pia Juma Nyoso, Victor Costa, ingawa alikuwa anaumwa goti wakati nilipokuja na Emmanuel Gabriel ambaye alikuwa anajua sana kufunga.
Nimeangalia michuano ya Chalenji na tayari nimewaona Jabu, Kapombe, Kaseja, Kazimoto na Okwi. Wote ni wachezaji wazuri na nasubiri kwa hamu kufanya nao kazi.

Simba: Kikosi cha pili cha Simba maarufu kwa jina la U20, hivi karibuni kimetwaa Kombe la Uhai na wengi wanakizatama kama sehemu muhimu ya mafanikio ya Simba katika miaka ijayo. Una mpango gani na kikosi hiki.

Milovan: Kwanza nimefurahi sana kwa Simba kuwa na kikosi hiki cha vijana. Huu ndiyo utaratibu duniani kote, huwezi kuwa na timu nzuri ya wakubwa kama huna timu nzuri ya vijana.Kwa bahati nzuri, mimi nina historia ya kufundisha timu za wakubwa na watoto ndani na nje ya Serbia. Nina uzoefu na najua nini wanahitaji.Sifa yangu moja kubwa ni kuwa, kama kijana akiwa na uwezo, hata kama ni mdogo, mimi ninampa nafasi. Lakini ni lazima nihakikishe yuko tayari kiakili kukabiliana na changamoto alizonazo.Kama mchezaji ni mzuri, atapata nafasi.

Simba: Hebu tueleze kuhusu familia yako kwa ufupi.

Milovan: Nina mke, Dionezia na watoto watatu wa kike – Anna, Sara na Marta.S: Unavuta sigara gani? Ngapi kwa siku.M: Navuta Malboro. Kwa kawaida huwa navuta pakiti moja na nusu kwa siku.

Simba: Una jina lolote la utani?

Milovan: Ukienda Serbia na ukaniulizia kwa jina la Milovan hutonipata. Uliza Profesa Cirko (Profesa Chirco). Kwa hiyo, sina tatizo kama Watanzania watakuwa wakiita kwa ufupi Chirco.

Simba: Miongoni mwa wanasoka maarufu zaidi kutoka Serbia kwa sasa ni Nemanja Vidic. Je, unamfahamu kivipi?

Milovan: Sifahamiani naye kibinafsi. Isipokuwa anatoka katika eneo la Uzice (tamka Ujitse), kijiji kinachofuata kutoka cha kwangu cha Cacak.

Simba: Unawaahidi nini wapenzi na wanachama wa Simba watakaosoma mahojiano haya.

Milovan: Nawaomba waipe timu muda wa kunielewa na mimi kuwaelewa wachezaji wangu. Soka si sawa na spea ya gari ambayo ukiiweka gari inawaka hapohapo.Itachukua muda kidogo kuelewana na hivyo naomba uvumilivu kutoka kwa washabiki. Kwa bahati nzuri washabiki wa Simba ni watu waelewa sana na nadhani watavuta subira kidogo.
Simba: Kila la kheri kocha.

Milovan: Ahsante sana.

BAYI ASHINDA TUZO YA MIAKA 50 YA UHURU

Filbert Bayi alivyo sasa

Filbert Bayi akiwa ameshikilia tuzo aliyoshinda enzi zake



BINGWA wa zamani wa dunia wa mbio za mita 1500, Filbert Bayi ameibuka mshindi wa tuzo ya mwanamichezo bora wa miaka 50 ya Uhuru wa Tanganyika baada ya kuzoa kura 13.
Upigaji kura kwa ajili ya kuwania tuzo hiyo umefanyika kupitia blogu hii ya liwazozito. Kura alizopata Bayi ni sawa na asilimia 72 ya kura zilizopigwa na wasomaji wa blogu hii.
Bayi alikuwa mwanariadha wa kwanza wa Tanzania kushinda medali ya dhahabu baada ya kushinda mbio za mita 1500 katika michezo ya Jumuia ya Madola iliyofanyika mwaka 1974 mjini Christchurch, New Zealand.
Mshindi wa pili wa mbio hizo alikuwa John Walker wa New Zealand wakati nafasi ya tatu ilinyakuliwa na Ben Jipcho wa Kenya.Bayi pia aliweka rekodi ya dunia ya mbio hizo kwa kutumia dakika 3:32:16
Mwaka 1975 Bayi alivunja rekodi ya mbio hizo iliyodumu kwa miaka minane iliyokuwa ikishikiliwa na Ryun baada ya kukimbia kwa dakika 3:51:0 mjini Kingston, Jamaica. Hata hivyo rekodi hiyo ilidumu kwa miezi michache baada ya kuvunjwa na Walker, aliyekimbia kwa dakika 3:49.4.
Bayi pia alishinda medali ya fedha katika mbio za mita 3000 kuruka vikwazo katika michezo ya Olimpiki ya mwaka 1980 iliyofanyika Moscow, Russia. Alishinda mbio hizo kwa kutumia dakika 8:12:5.
Mwanariadha huyo mkongwe pia alishinda mbio za mita 1500 katika michezo ya All Africa-Games iliyofanyika mwaka 1973 mwaka 1978 na kumbwaga Kipchoge Keino, aliyeambulia medali ya fedha.
Bayi won a silver medal in the 3000 m steeplechase at the 1980 Summer Olympics in
Moscow. He ran 8:12.5 behind Bronisław Malinowski.
Kwa sasa, Bayi ni Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) na anamiliki Taasisi ya Bayi, ambayo lengo lake kubwa ni kuibua, kukuza na kuendeleza vipaji vya vijana katika michezo.
Bayi pia anamiliki shule ya awali na msingi za Filbert Bayi zilizopo Kimara pamoja na shule ya sekondari iliyopo Kibaha mkoani Pwani.

Mshindi wa pili wa tuzo hiyo ni bondia Habibu Kinyogoli, ambaye alishinda medali ya fedha katika michezo ya All Africa-Games iliyofanyika mwaka 1978 nchini Nigeria.

Kinyogoli ni mmoja wa mabondia wanaoheshimika nchini kutokana na mchango mkubwa aliotoa katika ndondi za ridhaa na zile za kulipwa. Ni kocha aliyewafundisha mabondia wengi wa ndondi hizo nchini.

Kinyogoli amepata kura nne, ambazo ni sawa na asilimia 22 ya kura zilizopigwa na wasomaji wa blogu hii.

Nafasi ya tatu imechukuliwa na mwanasoka mkongwe Jella Mtagwa, aliyepata kura mbili ambazo ni sawa na asilimia 11 wakati Peter Tino ameshika mkia kwa kutoambulia kura.

Jela ni nahodha aliyeiongoza Taifa Stars kwa miaka 10 na picha yake ilikuwa kutumika katika moja ya stempu zilizotengenezwa na lililokuwa shirika la posta na simu Tanzania miaka ya 1980, lakini hakulipwa chochote. Tino ndiye mchezaji aliyeiwezesha Taifa Stars kufuzu kucheza fainali za Afrika kwa mara ya kwanza mwaka 1980 baada ya kuifungia bao la kusawazisha katika mchezo kati yake na Zambia uliofanyika mjini Ndola mwaka 1979.

Hongera sana Bayi kwa kuibuka mshindi wa tuzo hii. Blogu ya liwazozito inakutakia kila la heri katika maisha yako. Pia tunawapongeza Kinyogoli, Jella na Tino, ambao tuliwashirikisha bila ridhaa yenu, lakini kwa kutambua mchango mkubwa mlioutoa katika maendeleo ya michezo hapa nchini.

Pia tunawashukuru wale wote walioshiriki kuwapikia kura wanamichezo hawa. Mungu awabariki.

Friday, December 2, 2011

HISTORIA FUPI YA MR. EBBO



Jina kamili ni Abel Loshilaa Motika a.k.a Mr Ebbo, azaliwa tarehe 26 may 1974 jijini Arusha. Elimu ya msingi aliianza mwaka 1982 katika shule ya msingi kijenge baadae mwaka 1984 aliamia tanga na kuendelea na masomo katika shule ya msingi nguvumali na kumaliza elimu ya msingi mwaka 1988.

Alijiunga na elimu ya sekondari katika shule iitwayo jumuiya sec school. iliyopo jijini Tanga. Alimaliza elimu ya sekondari mwaka 1992. Na kwa kipindi hicho chote wakati yuko shuleni alikuwa akiimba kwaya kanisani kwenye kanisa la kisosora (lutheran church) ambapo ilimsaidia sana kujifunza muziki.

Alirudi Arusha mwaka 1993 na kubahatika kupata kazi kwenye night club ambapo alitumia mishahara yake kurekodi nyimbo ambazo hazikumpa mafanikio yeyote isipokuwa zilimuweka katika ramani ya muziki.

Baada ya hapo alifanya kazi ya kuandaa matangazo ya biashara na vipindi vya redio kwenye studio iliyojulikana kama Supreme recording studios iliyopo mjini Arusha. kipindi hicho kilijulikana kama “Mambo gani haya”

Alirekodi nyimbo kadhaa ambazo hazikumpa mafanikio yoyote kwa mara nyingine na hali hiyo ikamkatisha tamaa kabisa.

Baadae mwaka 1995 alipata kazi ya kuuza nguo kwenye duka la JJ BLACK lililopo jijini Arusha. Mwaka 1999 aliamua kurudi jijini Tanga na akafanikiwa kufunga ndoa na kubahatika kupata watoto wawili Ashley na baadaye Alicia.

Alianza kazi ya uwakala wa kuuza magazeti mwaka 2000, kazi ambayo pia haikumletea mafanikio yeyote makubwa kama alivyokuwa anatarajia. Baadaye mwaka 2001 akaanzisha biashara ya kuuza mchele kwa jumla ambayo pia haikuwa na mafanikio aliyoyatarajia.

Kipindi hicho chote alipokuwa Tanga, alifahamiana na wasanii wa muziki wa Bongo Fleva,Professor J na Wagosi wa kaya, na wao pia walijua kuwa Mr. Ebbo ni msanii asilia.

Baadae alijiunga na chuo cha kozi za computer jijini tanga.Wagosi waliporekodi wimbo wao wa Tanga kunani ,Mr Ebbo alihamasika kurudi tena kwenye Muziki na ndipo alipoandika wimbo wa kwanza wa "Mimi Mmasai mwaka 2002". Wimbo huo ukatambulisha album yake ya kwanza kisha wimbo wa 'Fahari yako'. Baadaye mwaka 2003 akafungua studio ( MOTIKA RECORDS) ambayo ilifanikiwa kuwatambulisha wasanii kama Danny Msimamo, Dr Leader, Mo-Kweli, na wengineo wengi , wote hawa aliwaproduce yeye mwenyewe kama producer wa MOTIKA RECORDS.

Mwaka 2003 akarekodi Album yake ya pili iliyojulikana kwa jina la Bado Ijasungumiswa. Mwaka 2004 akarekodi Album yake ya tatu iliyoitwa Kazi gani. Mwaka 2005 akarekodi Album ya nne iliyoitwa Alibamu. Mwaka 2006 akarekodi Album ya tano inayoitwa Kamongo.ambayo ndio albamu ya mwisho kwa uhai wake.

Mr. Ebbo kuzikwa J'tatu, sababu za kifo chake zaelezwa


Na Shabani Mdoe, Arusha
MSANII maarufu wa muziki wa kizazi kipya Abel Motika maarufu kama Mr.Ebbo amefariki dunia usiku wa kuamkia leo katika hospitali ya Mission Usa River wilayani Arumeru mkoani Arusha.
Akizungumza na Uhuru kwa nja ya simu, msemaji wa familia hiyo ambae pia ni msanii mwenzake wa muziki huo, Fred Maliki (Mkoloni) alisema, Ebbo alifariki majira ya saa 5 usiku katika hospitali hiyo alikokuwa amelazwa kwa matibabu.
Mkoloni alisema Ebbo alifariki kutokana na ugonjwa uliokua ukimsumbua wa kukaukwa na damu mwilini hali iliyosababisha kupatiwa matibabu pamoja na kuongezewa damu kila mara katika hospitali mbalimbali.
Alisema Ebbo mara ya mwisho alikwenda katika hospitali ya rufaa ya KCMC mjini Moshi,ambapo alifanyiwa uchunguzi mbalimbali pasipo kuonekana sababu ya kukaukwa na damu,hali iliyolazimu kuongezewa damu.
Alisema kutokana na tatizo hilo kuonekana kuwa kubwa na la kila mara, alilazimika kuhamisha makazi yake kwa muda toka mkoani Tanga alikokuwa anafanya kazi yake ya sanaa na kuhamia eneo la Sekei jijini Arusha, ambako ndiko nyumbani kwao kwa ajili ya kupatiwa matibabu katika hospitali hiyo ya Mission.
Aidha alisema katika siku za hivi karibuni, Ebbo alikuwa amepumzika nyumbani akisubiri majibu ya vipimo vyake vilivyofanyika ili kubaini tatizo lililokuwa likisababisha kukaukwa na damu kila mara.
Mkoloni alisema msanii huyo anatarajiwa kuzikwa nyumbani kwao Sekei jijini Arusha siku ya jumatatu na mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hospitali ya mkoa wa Arusha ya Mount Meru ukisubiri taratibu za maziko.
Alisema Ebbo ameacha mke na watoto wawili wote wa kike wenye umri katika ya miaka 5 hadi 9 ambao ni wanafunzi wa shule ya msingi.


Hadi marehemu Ebbo anafariki, alikuwa akiendelea na shughuli zake na muziki katika studio yake iliyoko mkoani Tanga ya Motika Recods na haijafahamika kama ameacha albamu au wimbo wowote mpya aliokuwa ameandaa siku za hivi karibuni.
Mara ya mwisho, msanii huyo alionekana mkoani hapa akitumbuiza katika mikutano ya kampeni za ubunge na urais za mgombea ubunge wa jimbo la Arusha kupitia Chama cha Mapinduzi, Dk.Batilda Buriani.
Akizungumzia kifo hicho, Dk. Batilda alisema kimemsikitisha sana na kwamba yupo bega kwa bega na familia ya msanii huyo na wengine pamoja na watanzania wote katika kipindi hiki kigumu kwa kumuombea dua njema marehemu huyo pamoja na ndugu na watoto ili wapewe wepesi na pepo njema.
Dk.Batilda, ambaye katika baraza lililopita la mawaziri alikuwa waziri wa nchi ofisi ya makamu wa rais mazingira alisema, Mr. Ebbo atakumbukwa kwa mengi ikiwa ni pamoja na kuenzi mila za kabila la kimasai kwa nyimbo alizokuwa akiimba pamoja na kuhamasisha amani ya taifa.

Mr Ebbo afariki dunia


MWIMBAJI nguli Tanzania aliyeibuka na staili ya bongofleva kwa ‘tune’ na staili ya Kimasai, Abel Rusheraa Motika, almaarufu – Mr Ebbo amefariki dunia.
Habari za uhakika zilizoifikia blogu hii leo zinaeleza kwa, Mr. Ebbo alifariki kufuatia kusumbuliwa na ugonjwa wa kichomi kwa muda mrefu.
Amefariki akiwa nyumbani kwa familia yake, maeneo ya Usa River, Arusha.Mwanamuziki huyo alifahamika zaidi kwa nyimbo zake zenye lafudhi ya Kimasai, ikiwamo – Mi Mmasai Bwana, Kamongo na nyingine nyingi zilizoteka uwanja wa muziki.
Pia alikuwa miongoni mwa wanamuziki walioinukia kwa kufanya ‘kolabo’ na wanamuziki wengine, hasa wanaotoka Mkoa wa Tanga wakiwamo; Wagozi wa Kaya.
Mipango ya mazishi inafanywa na familia yake na huenda akapumzishwa katika mashamba ya familia yake yaliyoko Usa River.
Blogu hii inatoa pole kwa mashabiki wa muziki, marafiki, watoto, ndugu jamaa na marafiki wote wa marehemu Mr. Ebbo.

Innalilah Wainailaihi rajiuun
Bwana ametoa, Bwana ametwaa, jina lake litukuzwe.

Wednesday, November 30, 2011

Masikini Mercy Johnson





LAGOS, Nigeria
NI vigumu kuamini, lakini habari za uhakika kutoka vyanzo mbalimbali ndivyo zinavyosema. Kwamba jicho la kulia la mwigizaji nyota wa filamu nchini Nigeria, Mercy Johnson limeharibika.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo vya habari, Mercy aliumia jicho lake hilo hivi karibuni wakati akiwa kwenye eneo la kuchezea filamu huko Asaba katika Jimbo la Delta.
Vyanzo hivyo vimesema mrembo huyo alipatwa na maumivu hayo baada ya kutokea ugomvi kati yake na mwigizaji mwenzake, ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja.
Taarifa zinasema familia ya mcheza filamu huyo, aliyefunga ndoa hivi karibuni, imekuwa ikihaha ili kuhakikisha anafanyiwa operesheni ya kurekebisha jicho lake mjini London, Uingereza.
Kuumia kwa Mercy kumeelezwa kuwa, kumemtia majonzi makubwa kiasi cha kumfanya asiwe na raha huku akiwaza nini la kufanya ili aweze kurejea katika hali ya kawaida.
Gazeti la Sun la Nigeria lilijaribu kuwasiliana na Mercy mara kadhaa ili kupata ukweli wa tukio hilo, lakini simu yake imekuwa ikiita kwa muda mrefu bila kupokelewa.
Filamu aliyokuwa akicheza Mercy imeandaliwa na Kampuni ya Magic Movies, imeandikwa na Micheal Jaja na kuongozwa na Jaja.

Hatimaye Aki afunga ndoa


LAGOS, Nigeria
HATIMAYE msanii nyota wa filamu wa Nigeria, Chinedu Ikedieze amefunga ndoa na mchumba wake wa muda mrefu, Nneoma Hope Nwajah.
Harusi hiyo ya kimila ilifanyika Jumamosi iliyopita kwenye kanisa katoliki la St. Theresa lililopo Obolo, Isiala Mbano, Jimbo la Imo.
Miongoni mwa watu maarufu waliohudhuria harusi hiyo ni pamoja na wacheza filamu nyota nchini humo, Segun Arinze, Uche Jombo, Oby Edozien na Ejike Asiegbu.
Watu wengine maarufu waliohudhuria harusi hiyo ni Gavana wa jimbo la Abia na mkewe pamoja na swahiba mkubwa wa Aki, Osita Iheme ‘Ukwa’.
Katika harusi hiyo, Aki alikuwa kivutio kikubwa kwa wageni waalikwa kutokana na kuvaa kofia na miwani myeusi pamoja na kushika fimbo kubwa ya kutembelea.
Maharusi hao wawili walioanza kuchumbiana miaka mitatu iliyopita, walitunzwa fedha nyingi na wageni waalikwa na muda wote walionekana kujawa na furaha kubwa.
Sherehe nyingine ya harusi hiyo imepangwa kufanyika Desemba 10 mwaka huu mjini Lagos.

Msondo, Sikinde uso kwa uso Krismas


BENDI kongwe za muziki wa dansi nchini, Msondo Ngoma na Mlimani Park Orchestra zimepanga kufanya onyesho la pamoja Desemba 25 mwaka huu kwenye viwanja vya klabu ya Sigara, Chang’ombe, Dar es Salaam.
Wakizungumza na Burudani kwa nyakati tofauti mjini Dar es Salaam juzi, viongozi wa bendi hizo walisema, onyesho hilo litadhaminiwa na Kampuni ya Konyagi.
Meneja wa Msondo Ngoma, Saidi Kibiriti alisema lengo la onyesho hilo ni kuimarisha umoja na ushirikiano kati ya wanamuziki wa bendi hizo kongwe nchini.
Kibiriti alisema bendi zote mbili zimekubaliana kuporomosha nyimbo mchanganyiko, zikiwemo za miaka 50 iliyopita na za sasa kwa lengo la kuwapa mashabiki burudani yenye vionjo na ladha tofauti.
“Hili si pambano la kutafuta nani mkali kati yetu, tunawaomba mashabiki waelewe hivyo, ni onyesho na kujenga na kuimarisha mshikamano kati ya wanamuziki wetu,”alisema.
Kwa upande wake, Katibu wa Mlimani Park, Hamisi Milambo alisema, maandalizi kwa ajili ya onyesho hilo yameshaanza na yanaendelea vizuri.
Milambo alisisitiza kuwa, lengo la bendi hizo si kupambana ili kumtafuta nani mkali kati yao, bali ni kuwapa mashabiki burudani kabambe ya muziki.
Hii itakuwa ni mara ya pili kwa Msondo na Mlimani Park kufanya onyesho la pamoja mwaka huu. Zilikutana kwa mara ya kwanza Juni mwaka huu katika onyesho lililofanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.
Onyesho hilo lilifanyika siku chache baada ya mwimbaji machachari nchini, Shabani Dede kuihama Mlimani Park na kujiunga na Msondo Ngoma.

JB: Tumeweza, tunasonga mbele



MSANII mkongwe wa fani ya filamu nchini, Jacob Steven amesema, maendeleo ya fani hiyo kwa sasa ni makubwa ikilinganishwa na miaka iliyopita.
Akihojiwa na kituo cha redio cha Clouds FM cha mjini Dar es Salaam wiki hii, Jacob alisema wakati fani hiyo ilipoanza, wasanii walikuwa wachache na walishindwa kunufaika nayo.
Msanii huyo, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la JB alisema, kadri miaka inavyosonga mbele, wasanii wamekuwa wakiongezeka na pia yamejitokeza mabadiliko makubwa katika utayarishaji wa filamu.
JB alisema hali hiyo imekuwa ikiwafanya wasanii nao waanze kunufaika na vipaji vyao kutokana na soko la filamu kuwa kubwa.
“Maendeleo wakati ule yalikuwa madogo kwa sababu ilikuwa ndio kwanza tunaanza. Wasanii wengi wa wakati ule hivi sasa hawapo,”alisema.
Aliwataja wasanii waanzilishi wa fani hiyo, iliyoanza kujipatia umaarufu miaka ya 1900 na ambao kwa sasa wamejiweka kando kuwa ni Bishanga, Aisha, Waridi na Mama Bishanga.
“Nina hakika katika miaka michache ijayo, ushindani katika fani ya filamu utakuwa mkubwa zaidi kwa sababu wasanii watazidi kuongezeka,”alisema.
Alisema katika miaka ya hivi karibuni, kumejitokeza wasanii wengi wa mitindo ya mavazi, urembo na wasomi wa kada mbalimbali, ambao wamezidi kuzinadhifisha filamu za kibongo na kuzifanya ziwe na mwonekano wa kimataifa.
“Kwa sasa tunao wasomi kutoka vyuo vikuu mbalimbali pamoja na Taasisi ya sanaa Bagamoyo. Kujitokeza kwao kwa wingi kunadhihirisha wazi kuwa, fani ya filamu hivi sasa inakubalika,”alisema.
Mbali na ongezeko la wasanii, JB alisema teknolojia inayotumika sasa katika kutengeneza filamu nayo ni ya juu zaidi na hivyo kuufanya ushindani uwe mkali.

Twenty Percent, Man Walter sasa ni chui na paka




HUWEZI kuamini. Pia unaweza kuita ni mchezo wa kuigiza ama filamu ya mauzauza. Ni kwa sababu kilichotokea, hakuna aliyekitarajia.
Ni kwamba mshindi wa tuzo tano za muziki za Kilimanjaro mwaka jana, Abbas Kinzasa 'Twenty Percent' na prodyuza wake, John Shariza, maarufu kwa jina la Man Walter hivi sasa hawaelewani. Ni sawa na chui na paka.
Unajua kisa ni nini?
Hakuna kingine zaidi ya mkwanja. Ndivyo inavyokuwa miaka yote utakaposikia msanii na prodyuza wake wamekorofishana. Sababu kubwa huwa ni kudhulumiana malipo.
Hivyo ndivyo ilivyotokea kwa Twenty Percent na Man Walter, ambao hivi karibuni walitoleana lugha kali, kila mmoja akimshutumu mwenzake kwamba ndiye chanzo cha kutokuelewana kwao.
Akihojiwa na kituo cha Radio One Stereo mwishoni mwa wiki iliyopita, Man Walter, ambaye ndiye mmiliki wa studio ya Combination Sound alisema, chanzo cha kutokuelewana huko ni ugomvi uliotokea kati yao kabla ya kuanza kwa onyesho lililofanyika mjini Morogoro.
Prodyuza huyo alisema, aliamua kuandaa onyesho hilo kwa ajili ya kumpongeza Twenty Percent na pia kuwashukuru mashabiki kwa kumpigia kura nyingi.
Alisema kabla ya kuanza kwa onyesho hilo, alifuatwa na Twenty Percent na kumtaka ampe malipo yake mapema. Alisema alipompa kwa mara ya kwanza, msanii huyo alikataa kupokea kiasi cha pesa alicholipwa kwa madai kuwa ni kidogo.
“Akaomba akabidhiwe malipo hayo mbele ya polisi, pia akakataa kupokea. Baadaye nikwamwita Afande Sele na kumkabidhi malipo hayo mbele yake, ndipo akakubali kupokea,”alisema Man Walter bila ya kufafanua kiwango hicho cha pesa.
Kwa mujibu wa Man Walter, licha ya kupokea malipo hayo, msanii huyo alitoa lugha kali kwake, akimshutumu na kumwita tapeli, aliyetumia kipaji chake kujinufaisha kimaisha.
Aliongeza kuwa, msanii huyo pia aliapa mbele za watu kwamba, hatorekodi tena nyimbo zake kwenye studio yake na wala asitarajie kufanyanaye kazi zingine.
“Kwa kweli maneno aliyoyatamka kwangu sikuyatarajia kabisa. Hata mashabiki waliofika ukumbini kushuhudia onyesho hilo walilalamika sana na kutoka nje,”alisema Man Walter.
Prodyuza huyo alisema, kilichomsikitisha zaidi ni kumsikia msanii huyo akiapa kwamba, atamfanyia kitu mbaya. Alisema alichokifanya si haki hata kidogo.
“Mimi ndiye niliyemtoa na kumpatia umaarufu kimuziki. Kutokana na makubaliano tuliyokuwa nayo, hakupaswa kurekodi nyimbo mpya kwa prodyuza mwingine. Alipaswa kunipa angalau nyimbo mbili,”alilalamika.
Kwa upande wake, Twenty Percent alisema si kweli kwamba haelewani na Man Walter, isipokuwa amerekodi nyimbo zake mpya kwenye studio zingine kwa lengo la kuzipa ladha tofauti.
“Sina ugomvi wowote na Man Walter, isipokuwa watu walipotuona tukibadilishana maneno makali, wakachukulia kwamba ugomvi wetu ni mkubwa,”alisema.
Msanii huyo alisema yeye na Man Walter ni marafiki wakubwa, iwe kikazi ama wanapokuwa mtaani wanapoishi na amekuwa akimchukulia kama kaka yake.
Alisema sababu kubwa iliyomfanya aamue kurekodi nyimbo zake mpya kwenye studio zingine ni kutokana na Man Walter kutingwa na kazi nyingi.
“Haya ni mabadiliko ya kawaida kimuziki. Nilichokifanya ni kubadili ladha ya muziki wangu ili nitoke kivingine badala ya vile nilivyozoeleka,”alisema.
“Man Walter ni kama kaka yangu. Tunapokuwa mtaani, yeye ndiye anayenipa mawazo mbalimbali kuhusu maisha, hatuna ugomvi, tupo pamoja,”alisisitiza.

MAVITUZ YA TWANGA PEPETA LONDON





MWIMBAJI wa bendi ya muziki wa dansi ya Twanga Pepeta International, Hamisi Amigolas akicheza huku akiwa amembeba mcheza shoo wa bendi hiyo, Tina Mjapan wakati wa onyesho lililofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita mjini London, Uingereza.Juu ni mcheza shoo huyo akifanya mavituz. (Picha kwa hisani ya blogu ya Freddy Macha)

Chondechonde mwacheni Vengu-Seki


UONGOZI wa kundi la Orijino Komedi umevitaka vyombo vya habari nchini kuacha kumfuatilia msanii wake, Joseph Shamba ‘Vengu’ aliyelazwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Dar es Salaam.
Mbali na kuviasa vyombo vya habari, kundi hilo pia limewaomba mashabiki wake kuacha kumsumbua msanii hiyo kwa kulazimisha kuingia kwenye chumba alimolazwa hospitalini hapo.
Kiongozi wa kundi hilo, Sekione David alisema mjini Dar es Salaam juzi kuwa, madaktari wanaomtibu Vengu wameshauri asibughudhiwe na watu.
“Madaktari na familia yake hawataki jambo hili liwe wazi kwa kila mtu, ugonjwa ni siri ya mgonjwa na madaktari kwa manufaa ya hospitali,”alisema Sekione, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Seki.
Kiongozi huyo wa Orijino Komedi alisema, binafsi haruhusiwi kutoa taarifa zinazomhusu msanii huyo kutokana na kuzuiwa kufanya hivyo na madaktari.
“Hizi ni taratibu walizoweka madaktari na ndugu zake, hatuwezi kwenda kinyume ya hapo,”alisisitiza Seki.
Vengu amelazwa Muhimbili kwa zaidi ya miezi miwili huku ugonjwa wake ukifanywa kuwa siri kubwa. Kuna habari kuwa, msanii huyo anasumbuliwa na kichwa.
Kufuatia kulazwa hospitalini hapo kwa muda mrefu, baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikitoa taarifa tofauti kuhusu ugonjwa unaomsumbua msanii huyo.
Katika kipindi cha Orijino Komedi wiki iliyopita, msanii maarufu kwa jina la Masanja alisikika akisema kwa masikitiko kwamba, hali ya Vengu bado haijatengemaa.
“Jamani jamani, Vengu anaumwa. Masikini jembe langu, linaumwa,”alisema.
Masanja alisema hayo, kufuatia mashabiki wengi wa kipindi hicho kuwapigia simu wakitaka kujua maendeleo ya afya ya msanii huyo.
Kutokana na kuthamini mchango wa msanii mwenzao, Masanja alisema wataendelea kutumia kazi zake zilizopita ili kuwaliwaza mashabiki wao.

Shakur aipiga jeki Uhuru SC



MFANYABIASHARA Shakur Sanya ameipatia klabu ya michezo ya Uhuru vifaa vya michezo kwa ajili ya timu yake ya soka.
Shakur, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Mipango, Uchumi na Fedha ya CCM Kata ya Jangwani, alikabidhi vifaa hivyo juzi kwa Katibu wa klabu ya Uhuru, Rashid Zahor.
Vifaa vilivyotolewa na Shakur kwa klabu ya Uhuru ni seti moja ya jezi na mipira mitatu, vyote vikiwa na thamani ya sh. 500,000.
Hafla ya kukabidhi vifaa hivyo, ambayo ilifanyika kwenye ofisi za Shakur, mtaa wa Mafia, Dar es Salaam, pia ilihudhuriwa na nahodha wa timu ya soka ya Uhuru, Mussa Hassan.
Akizungumza wakati wa kukabidhi vifaa hivyo, Shakur alisema ameamua kutoa msaada huo kwa lengo la kuiimarisha timu ya Uhuru.
“Msaada huu pia ni utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, ambayo inasisitiza umuhimu wa kuibua vipaji vya michezo na kuviendeleza,”alisema.
Shakur alisema msaada huo ni wa mwanzo kwake kwa Uhuru, lakini hautakuwa wa mwisho, hivyo ameahidi kuendelea kuisaidia kila itakapohitaji msaada kutoka kwake.
“Ninayo taarifa kwamba timu yenu imekuwa ikisafiri mara kwa mara mikoani kucheza mechi za kirafiki na hivi karibuni mnatarajia kwenda Arusha, nitajitahidi katika siku zijazo kuendelea kuwasaidia,”alisema.
Kwa upande wake, Zahor alimshukuru Shakur kwa kuwapatia msaada huo wa vifaa vya michezo na kuahidi kuwa, watautumia kwa malengo yaliyokusudiwa.
Alisema msaada huo umekuja wakati mwafaka kwa timu yake kwa vile wamepanga kucheza mechi kadhaa za kirafiki kwa ajili ya kujiandaa na michuano ya Kombe la NSSF.
Uhuru ilitwaa kombe hilo mara mbili mfululizo mwaka 2007 na 2008 na mwaka 2009 ilishika nafasi ya pili wakati mwaka jana ilishika nafasi ya tatu. Timu ya netiboli nayo ilitwaa kombe hilo mwaka 2007.
Klabu ya michezo ya Uhuru pia imewahi kutwaa ubingwa wa jumla wa bonanza la vyombo vya habari mwaka 2010 na 2009.
Klabu ya Uhuru inaundwa na wafanyakazi wa Kampuni ya Uhuru Publications Ltd, wachapishaji wa magazeti ya Uhuru, Mzalendo na Burudani, kituo cha Radio cha Uhuru FM na ofisi ndogo ya CCM.

Friday, November 25, 2011

Asante Kotoko kutua Dar Des 9



TIMU ya soka ya Kumasi Asante kotoko ya Ghana inatarajiwa kuwasili nchini Desemba 9 tayari kucheza mchezo mmoja wa kirafiki dhidi ya kombaini ya timu za Yanga na Simba siku ya Desemba 11 kwenye uwanja wa Taifa. Mchezo huo ni sehemu ya kukamilisha maadhimisho ya sherehe za miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania na maandalizi yake yamekwisha kamilika kwa mujibu wa mwenyekiti mtendaji wa kampuni ya Future Century Limited, Helen Masanja. Masanja alisema kuwa timu hiyo itafikia Zanzibar na baadaye kuja jijini Dar es Salaam kwenye hotel ya Lamada tayari kwa mchezo huo ambao umedhaminiwa na PPF, Kenya Airways, Vanedrick Tanzania Limited, Lamada Hotel na Vanne Fashion Tabata. Alisema kuwa wanatarajia kuwa na burudani ya aina yake kwani tayari kombaini ya timu ya Yanga na Simba itaundwa na wachezaji nyota wanaocheza Ligi Kuu ya Tanzania Bara msimu huu. Aliongeza kuwa makocha wawili, mkongwe, Abdallah “King Mputa” Kibaden na Fred “ Minziro” Felix ndiyo watakuwa wakuu wa benchi la ufundi la timu hiyo ambayo itaundwa na wachezaji 20 watakaotangazwa hapo baadaye. Wengine katika benchi la ufundi na meneja, Boniface Pawasa na daktari wa timu, Juma Sufiani. Alifafanua kuwa uteuzi wa timu hiyo hautajali uraia wa wachezaji hivyo kama wachezaji kutoka nchi za nje ambao wanachezea timu hizo watateuliwa, basi watacheza mchezo huo.Masanja alisema kuwa Yanga na Simba zimekubaliana na kuweka historia kwa mara ya kwanza tangu timu hizo zitengane mwaka 1935. Alisema kuwa historia inaonyesha kuwa timu hizo zilikuwa pamoja kuanzia mwa 1922. Mwenyekiti wa Yanga Lyod Nchunga alisema kuwa mechi hiyo itaondoa tofauti iliyopo baina ya mashabiki wa Simba na wale wa Yanga hasa zinapotokea timu hizo zinacheza mechi za kimataifa ambapo imekuwa ni kawaida mashabiki wa timu hizo kushangilia timu pinzania. Wakati Nchunga akisema hayo, Katibu Mkuu wa Simba, Evodius Mtawala alisema kuwa muungano huo utaleta tija kwa timu hizo ambapo mashabiki wa Simba na Yanga siku hiyo watakuwa kitu kimoja kwa ajili ya kuishangilia timu yao tofauti na ilivyokuwa miaka ya nyuma.Alisema kuwa huu ndiyo mwanzo wa kuanza kushirikiana katika mechi za kimataifa na kuwataka mashabiki kufika kwa wingi na kutoa sapoti kubwa kwao

Tenga awa balozi wa malaria



Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania, Leodegar Tenga ambaye pia ni Rais wa CECAFA, akipokea tuzo baada ya kutangazwa kuwa Balozi wa United Against Malaria Tanzania na mmoja wa viongozi wa taasisi ya Johns Hopkins nchini, Anna McMartney (kushoto) katika hafla ya kuyakaribisha mashindano ya Tusker Challenge Cup yanaliyoanza kutimua vumbi jijini Dar es Salaam jana. Hafla hiyo iliyoandaliwa na United Against Malaria ilifanyika jana jijini humo.

KANIKI, JOHN WILLIAM WAPATA TIMU SWEDEN





Wachezaji wawili wa kitanzania, Joseph Kaniki (Golota) na William John wamefanikiwa kujiunga na timu ya ligi daraja la pili KonyaSpor (KIF) nchini Sweden, baada ya kufanikiwa kupita katika majaribio( Trials). Majaribio hayo yalijumuisha wachezaji zaidi ya thelathini ambapo wachezaji watano walichaguliwa kujiunga na klabu hiyo ya ligi daraja la pili KonyaSpor (KIF)

DIAMOND AIPUA ALBAMU MPYA



Nyimbo yangu mpya inaitwa Mawazo, nimerekodi studio za AM RECORD, producer Maneke, inapatikana katika albam yangu mpya ya inayoitwa LALA SALAMA, album ina nyimbo kumi ambazo ni

1) Moyo Wangu

2) lala salama

3) Chanda chema

4) Nimpende nani

5) najua

6) Mawazo

7) Kwanini

8) Gongolamboto

9) Natamani

10)Kizaizai

FAINALI KOMBE LA UHAI YASOGEZWA



Mechi ya fainali ya michuano ya soka ya vijana wenye umri chini ya miaka 20 ya Kombe la Uhai (Uhai Cup) kwa klabu za Ligi Kuu sasa itachezwa kesho (Novemba 26 mwaka huu) saa 3.00 asubuhi kwenye Uwanja wa Karume.

Awali fainali hiyo kati ya Simba, ambayo iliingia hatua hiyo kwa kuitandika Toto Africans mabao 4-1 na Azam, iliyofuzu kwa kuizamisha Serengeti Boys (timu ya Taifa ya vijana chini ya miaka 17) mabao 3-0, ilikuwa ichezwe leo (Novemba 25 mwaka huu) saa 9.00 kwenye uwanja huo.

Mabadiliko hayo yamefanyika ili kutoa nafasi kwa mashabiki kushuhudia mechi za michuano ya Kombe la Chalenji inayoanza leo (Novemba 25 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa.

Kila siku kwenye michuano ya Chalenji zinachezwa mechi mbili; ya kwanza saa 8.00 mchana na nyingine saa 10.00 jioni.

Michuano ya Kombe la Uhai inadhaminiwa na Kampuni ya S.S. Bakhresa kupitia maji Uhai ambapo bingwa atapata sh. milioni 1.5, mshindi wa pili sh. milioni moja wakati wa tatu atapata sh. 500,000.

Mbali ya fedha hizo, bingwa atapata medali za dhahabu, makamu bingwa medali za fedha na mshindi wa tatu medali za shaba. Mchezaji bora sh. 400,000, mfungaji bora (sh. 300,000), kipa bora (sh. 300,000) na timu yenye nidhamu sh. 300,000.

VIINGILIO MICHUANO YA KOMBE LA CHALENJI

Viingilio kwa mechi za hatua ya makundi kwa michuano ya Kombe la Chalenji inayoanza leo (Novemba 25 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam vitakuwa kama ifuatavyo;

Kwa viti vya rangi ya bluu na kijani ambavyo ni zaidi ya 30,000, kiingilio kitakuwa sh. 1,000 wakati viti vya rangi ya chungwa ambavyo ni zaidi ya 10,000 kiingilio kitakuwa sh. 3,000. VIP C na B ambayo jumla ya viti vyake ni 8,000 kiingilio kitakuwa sh. 5,000 wakati VIP A yenye viti 700 kiingilio ni sh. 10,000.

Tenga achaguliwa tena kuongoza CECAFA



TENGA ACHAGULIWA TENA CECAFA

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga amechaguliwa tena kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA).

Tenga amechaguliwa leo (Novemba 24 mwaka huu) bila kupingwa baada ya mpinzani wake Fadoul Hussein wa Djibouti kutotokea kwenye uchaguzi.

Kutokana na hali hiyo, mjumbe kutoka Uganda alitoa hoja ya Tenga kupitishwa bila kupingwa, hoja ambayo iliungwa mkono na Kenya, Tanzania, Uganda, Sudan, Zanzibar, Ethiopia, Burundi na Eritrea.

Jumla ya nchi wanachama zilizopiga kura katika uchaguzi uliofanyika hoteli ya New Africa ni kumi na moja, na kila moja ilikuwa na kura moja tu.

Kwa upande wa nafasi nne za wajumbe wa Kamati ya Utendaji kulikuwa na wagombea wanane. Waliopita katika raundi ya kwanza na kura zao kwenye mabano ni Abdiqani Saeed Arab wa Somalia (8), Tariq Atta Salih wa Sudan (8) na Raoul Gisanura wa Rwanda (8). Wengine katika raundi ya kwanza na kura walizopata kwenye mabano ni Sahilu Wolde wa Ethiopia (4), Justus Mugisha wa Uganda (4), Tesfaye Gebreyesus wa Eritrea (4), Hafidh Ali Tahir wa Zanzibar (2) naAbubakar Nkejimana wa Burundi (3).

Mjumbe aliyefanikiwa kushinda katika raundi ya pili na kuingia kwenye Kamati ya Utendaji ni Wolde wa Ethiopia aliyepata kura tano dhidi ya nne za Mugisha na mbili za Gebreyesus. Mwenyekiti anakaa madarakani kwa miaka minne wakati wajumbe wa Kamati ya Utendaji wanachaguliwa kila baada ya miaka miwili.

ZIMBABWE YAZIBA NAFASI YA NAMIBI

Timu ya Taifa ya Zimbabwe (Might Warriors) imeteuliwa na CECAFA kushiriki michuano ya Kombe la Chalenji inayoanza Novemba 25 mwaka huu jijini Dar es Salaam kuziba nafasi ya Namibia iliyojitoa. Zimbabwe itawasili Novemba 26 mwaka huu jijini Dar es Salaam na itakuwa kundi A pamoja na timu za Tanzania Bara, Rwanda na Djibouti.

KIKOSI CHA KILIMANJARO STARS

Kocha Mkuu wa timu ya Tanzania Bara (Kilimanjaro Stars), Charles Boniface Mkwasa ametaja kikosi cha mwisho cha wachezaji 20 kwa ajili ya michuano hiyo inayoanza kesho.

Wachezaji waliobaki kati ya 28 waliokuwa wameitwa awali ni Juma Kaseja (Simba), Shabani Kado (Yanga), Shomari Kapombe (Simba), Godfrey Taita (Yanga), Juma Jabu (Simba), Ibrahim Mwaipopo (Azam) ,Juma Nyoso (Simba), Said Murad (Azam), Erasto Nyoni (Azam) na Shabani Nditi (Mtibwa Sugar), Nurdin Bakari (Yanga), Haruna Moshi (Simba) na Mwinyi Kazimoto (Simba).

Wengine ni Said Maulid (Angola), Musa Mgosi (DC Motema Pembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo-DRC), Mrisho Ngassa (Azam), Ramadhan Chombo (Azam), Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC), Mbwana Samata (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC) na Rashid Yusuf (Coastal Union).

Kilimanjaro Stars itacheza mechi yake ya kwanza Novembe 26 mwaka huu dhidi ya Rwanda.

Wednesday, November 23, 2011

GOFU KUSAIDIA WAGONJWA WA MACHO



Benki ya NIC Tanzania kwa kushirikiana na klabu ya Lions ya Dar es Salaam, imejitokeza kudhamini mashindano ya mchezo ya gofu kwa lengo la kusaidia watu wenye matatizo ya macho. Katika mashindano hayo, benki hiyo imetoa jumla ya dola za Kimarekani 2,000 (sawa na sh. milioni 3.5 za Tanzania) kwa lengo la kuinua afya za wananchi, hasa wanaosumbuliwa na matatizo ya macho.Pichani, Mkurugenzi na Mtendaji Mkuu wa NIC Tanzania, James Muchiri (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Meneja Mikopo wa benki hiyo, Regina Mwengi, Prisalla Karobia na David Muthungu kabla ya kuanza kwa michuano hiyo iliyofanyika juzi kwenye viwanja vya Gymkhana, Dar es Salaam.

Ferej alalamikia ukiukwaji wa katiba ZFA


VURUGU zinazotokea mara kwa mara katika Chama cha Soka cha Zanzibar (ZFA) ni matokeo ya kukiukwa kwa katiba na kanuni za kuendesha mchezo huo.
Hayo yamesemwa na Rais wa ZFA, Ali Ferej Tamim wakati wa mkutano mkuu wa dharula wa chama hicho uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita mjini hapa.
Mbali na kujadili masuala mbalimbali, mkutano huo uliitishwa kwa lengo la kufanya marekebisho ya katiba ya chama hicho.
Ferej alitoa kauli hiyo baada ya baadhi ya wajumbe wa kamati ya utendaji ya chama hicho kutoka Pemba, kulalamika kuwa, kimekuwa kikitoa maamuzi mengi bila ya kufuata katiba.
Wajumbe hao walilalamikia uamuzi wa ZFA wa kuirejesha Malindi katika ligi kuu bila kufuata taratibu ama kuishirikisha kamati ya utendaji ya chama hicho katika kutoa maamuzi.
Akijibu malalamiko hayo, Ferej alisema katika soka, hakuna kitu kinachoitwa makubaliano, kinachotakiwa ni kufuatwa kwa katiba na kanuni katika kutoa maamuzi.
Ferej alisema ni kweli kwamba yeye ni mwanachama wa klabu ya Malindi, lakini hawezi kutoa maamuzi kwa lengo la kuibeba.
Rais huyo wa ZFA alisema tatizo kubwa linaloikabili soka ya Zanzibar ni ukiukwaji wa kanuni na kusisitiza kuwa, iwapo halitapatiwa ufumbuzi, litakwamisha maendeleo ya mchezo huo.
Alisema yapo baadhi ya mambo, ambayo klabu zinaweza kukubaliana kama vile mfumo wa mgawo wa mapato, lakini si uendeshaji wa ligi.
“Katika hili, ni kweli kwamba kanuni zimevunjwa na timu zilizoshuka daraja, zimeonewa,”alisema rais huyo wa ZFA, ambaye ameichezea Malindi kwa miaka 11 na pia kuiongoza kwa kipindi kama hicho.

Kambi ya Misri yaipa jeuri Zanzibar Heroes


TIMU ya soka ya Zanzibar, Zanzibar Heroes imerejea nchini juzi kutoka Misri, ilikokwenda kuweka kambi kwa ajili ya kujiandaa na michuano ya Kombe la Chalenji.
Ofisa Habari wa Chama cha Soka cha Zanzibar (ZFA), Munir Zakaria alisema mjini hapa juzi kuwa, timu hiyo iliweka kambi Misri kwa wiki mbili.
Mbali ya kuweka kambi, Munir alisema timu hiyo ilicheza mechi tatu za kirafiki dhidi ya timu za Misri, ambapo ilishinda mechi moja na kufungwa mechi tatu.
Munir alisema timu hiyo ilipata ushindi wake wa pekee dhidi ya timu ya taifa ya vijana wa chini ya miaka 17 ya Misri. Katika mechi hiyo, Zanzibar Heroes ilishinda mabao 3-2.
Zanzibar Heroes ilikwenda Misri ikiwa chini ya Kocha Hemed Morocco, ambaye ndiye atakayeiongoza katika michuano ya Kombe la Chalenji, inayotarajiwa kuanza kesho.
Akizungumzia kambi hiyo, Munir alisema ilikwenda vizuri na kwamba mechi nne za kirafiki walizocheza, zimewaweka wachezaji katika hali nzuri kwa ajili ya Kombe la Chalenji.
Alisema kikosi hicho kwa sasa kipo fiti kwa ajili ya michuano hiyo na kuongeza kuwa, wachezaji wana ari kubwa ya kuibuka na ushindi.
Wakati huo huo, Munir amesema hatma ya Kocha John Stewart kutoka Uingereza kwa sasa ipo mikononi mwa ZFA.
Stewart, ambaye pia ni Kocha Mkuu wa Azam FC, alishindwa kujiunga na Zanzibar Heroes ilipokuwa Misri kwa madai kuwa, hati yake ya kusafiria ilikuwa imejaa.
Hata hivyo, utetezi wake huo umepingwa na baadhi ya viongozi wa chama hicho kwa madai kuwa, alifahamu mapema kuhusu safari hiyo.
Licha ya kuifundisha Azam, inayoshiriki michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara, Stewart pia ana mkataba wa kuifundisha Zanzibar Heroes wakati wa michuano mbalimbali.

SMG afurahia kuitwa Kilimanjaro Stars

MSHAMBULIAJI Saidi Maulid ‘SMG’ anayecheza soka ya kulipwa nchini Angola, amesema amefurahia kuitwa kwenye kikosi cha Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars kitakachoshiriki katika michuano ya mwaka huu ya Kombe la Chalenji.
SMG alisema hayo mjini Dar es Salaam juzi, alipokuwa akizungumzia kuitwa kwake kwenye kikosi hicho baada ya kuachwa kwa zaidi ya miaka mitano.
Alisema kwa mchezaji yeyote wa kulipwa anayecheza nje ya nchi yake, huwa ni fahari kubwa kwake kuitwa kwenye timu ya taifa kwa sababu kunaonyesha anavyothaminiwa.
Mshambuliaji huyo wa zamani wa klabu za Simba na Yanga alisema, amekuwa akiisubiri nafasi hiyo kwa muda mrefu na baada ya kuipata amepania kuonyesha uwezo wake.
Hata hivyo, SMG alisema kufanya vizuri kwa Kilimanjaro Stars katika michuano hiyo kutategemea ushirikiano wa wachezaji uwanjani na kutiwa moyo na mashabiki.
Alisema wao kama wachezaji, watajitahidi kucheza kadri ya uwezo wao, lakini wanahitaji sapoti kubwa kutoka kwa mashabiki.
SMG aliichezea Taifa Stars mwanzoni mwa miaka ya 2000 ilipokuwa chini ya makocha wazalendo na baadaye Marcio Maximo kutoka Brazil, lakini alitemwa baada ya kwenda Angola.
Awali, SMG hakuwemo kwenye kikosi hicho, lakini makocha Charles Boniface Mkwasa na Jamhuri Kihwelu walilazimika kumwita baada ya kuumia kwa John Bocco.
Mkataba wa mshambuliaji huyo kucheza Angola unatarajiwa kumalizika Desemba 2012.

Mwaikimba amwaga wino Azam FC


MSHAMBULIAJI Gaudence Mwaikimba wa Moro United amejiunga rasmi na Azam FC kwa ajili ya mzunguko wa pili wa michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara.
Ofisa Habari wa Azam, Jafari Iddi alisema mjini Dar es Salaam juzi kuwa, tayari mshambuliaji huyo ameshatia saini mkataba wa kuichezea timu hiyo.
Jafari alisema wameamua kumsajili Mwaikimba kwa lengo la kuziba pengo la mshambuliaji wao kutoka Ghana, ambaye ameachwa kutokana na kiwango chake kushuka.
Msemaji huyo wa Azam alisema, Mwaikimba anatarajiwa kuanza mazoezi na timu hiyo mara baada ya kumalizika kwa michuano ya Kombe la Chalenji.
Alisema wanaamini, Mwaikimba atashirikiana vyema na mshambuliaji John Bocco na Mrisho Ngassa kuunda safi kali ya ushambuliaji.
Kwa mujibu wa Jafari, lengo la timu yake ni kuhakikisha kuwa, wanamaliza msimu huu wa ligi wakiwa mabingwa ama kushika nafasi ya pili ili waweze kushiriki michuano ya kimataifa mwakani.
Kwa sasa, Mwaikimba yumo kwenye kikosi cha Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars kitakachoshiriki michuano ya Kombe la Chalenji, inayotarajiwa kuanza kesho mjini Dar es Salaam.
Mwaikimba alianza kujipatia umaarufu alipokuwa akichezea Ashanti kabla ya kuchukuliwa na Yanga na baadaye kuhamia Kagera Sugar ya Bukoba.
Mchezaji huyo alikuwemo kwenye kikosi cha timu ya Taifa, Taifa Stars kilipokuwa chini ya Kocha Marcio Maximo kutoka Brazil kabla ya kutemwa kwa madai ya kiwango chake kushuka.