KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, February 28, 2014

27 WAREJESHA FOMU ZA UCHAGUZI TASWA


Waombaji 27 kati ya 28 wamerejesha fomu kuomba kuwania nafasi mbalimbali za uongozi kwenye uchaguzi wa Kamati mpya ya Utendaji ya Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) utakaofanyika Machi 2, 2014 jijini Dar es Salaam.

Mwisho wa kuchukua na kurudisha fomu hizo ilikuwa leo Alhamisi (Februari 27 mwaka huu) saa 9 alasiri.

Waliorejesha kwa nafasi ya ujumbe ni Arone Benedict Mpanduka, Elizabeth Rashid Mayemba, Emmanuel Augustino Muga, Hassan Maulid Bumbuli, Ibrahim Mkomwa Bakari, Masau Kuliga Bwire, Mbozi Ernest Katala, Mroki Timothy Mroki, Mussa Juma, Mwani Omary Nyangassa, Rehure Richard Nyaulawa, Salum Amiri Jaba, Tullo Stephen Chambo na Urick Chacha Maginga.

Mhazini Msaidizi ni Elius John Kambili, Zena Suleiman Chande wakati Mhazini Mkuu ni Shija Richard Shija na Mohamed Salim Mkangara.

Katibu Msaidizi ni Alfred Lucas Mapunda, Grace Aloyce Hoka na Ptarick Raymond Nyembera. Katibu Mkuu ni Amir Ally Mhando pekee.

Waombaji nafasi ya Makamu Mwenyekiti ni Egbert Emmanuel Mkoko, Maulid Baraka Kitenge na Mohamed Omary Masenga. Waliojitosa kwenye nafasi ya Mwenyekiti ni George John Ishabairu, Juma Abbas Pinto.

Ni Shaffih Kajuna Dauda pekee ambaye hakurejesha fomu. Dauda alichukua fomu ya kuwania uenyekiti.

TFF, POULSEN WAKUBALIANA KUVUNJA MKATABA



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Kocha wa Taifa Stars, Kim Poulsen wamekubaliana kuvunja mkataba katika makubaliano ambayo ni siri kwa pande zote mbili.

Uamuzi huo umetangazwa leo (Februari 27 mwaka huu) jijini Dar es Salaam kwa pamoja na Rais wa TFF, Jamal Malinzi na Kocha Poulsen mbele ya waandishi wa habari.

Rais Malinzi kwa niaba ya TFF ametoa shukrani za dhati kwa Kocha Poulsen kwa ushirikiano na mchango ambao ameutoa kwa Tanzania kuanzia kwenye mpira wa miguu wa vijana.

Naye Kim amewashukuru Watanzania kwa ushirikiano waliompatia kwa kipindi cha miaka mitatu alichokaa nchini kuanzia Mei 2011 alipoteuliwa kuwa kocha wa timu za Taifa za vijana, na baadaye Taifa Stars.

Akizungumzia benchi jipya la ufundi la Taifa Stars, Rais Malinzi amesema linatarajiwa kutangazwa hivi karibuni likiongozwa na kocha kutoka nje ya Tanzania.

Amesema kwa upande wa mechi dhidi ya Namibia itakayochezwa Machi 5 mwaka huu jijini Windhoek, Stars itaongozwa na Kaimu Mkurugenzi wa Ufundi, Salum Madadi akisaidiwa na kocha Hafidh Badru kutoka Zanzibar.

Katika hatua nyingine, Kocha Madadi amewaondoa wachezaji watano wa Yanga katika kikosi kilichotajwa awali ili wapate fursa ya kuitumikia timu yao kwenye mechi mbili za Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al-Ahly ya Misri.

Wachezaji hao ni Athuman Idd, David Luhende, Deogratius Munishi, Frank Domayo, Kelvin Yondani na Mrisho Ngasa. Pia kipa Ivo Mapunda ameondolewa katika kikosi hicho baada ya kupata msiba.

Nafasi zao zimezibwa na wachezaji Abdi Banda (Coastal Union), Himid Mao (Azam), Juma Luizio (Mtibwa Sugar), Said Moradi (Azam) na Shabani Kado (Coastal Union).

Taifa Stars itaingia kambini keshokutwa (Machi 1 mwaka huu) jioni kwenye hoteli ya Accomondia jijini Dar es Salaam, na itaondoka Machi 3 mwaka huu alfajiri kwa ndege ya South African Airways na kurejea nchini Machi 7 mwaka huu saa 8.15 mchana.

WACHEZAJI YANGA KUZOA MIL 100/-, KILA BAO KUNUNULIWA KWA MILIONI MOJA


WAKATI kikosi cha timu ya soka ya Al Ahly ya Misri kimewasili Dar es Salaam kiunyonge, uongozi wa Yanga umewaahidi wachezaji wake kitita cha sh. milioni 200 iwapo watawafunga wapinzani wao.

Mbali na zawadi hiyo ya jumla kwa timu nzima, uongozi wa Yanga umeahidi kutoa sh. milioni moja kwa kila mchezaji atakayefunga bao katika mechi hiyo.

Yanga inatarajiwa kumenyana na Al Ahly keshokutwa katika mechi ya awali ya raundi ya pili ya michuano ya klabu bingwa Afrika, itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Habari zilizopatikana jana kutoka ndani ya uongozi wa Yanga zimeeleza kuwa, ahadi hiyo ya pesa imelenga kuwaongezea ari wachezaji ya kucheza kwa kujituma na hatimaye kushinda mechi hiyo.

Awali, uongozi wa Yanga ulipanga kuwazawadia wachezaji wa timu hiyo sh. milioni 100 iwapo watashinda mechi hiyo, lakini umeamua kuongeza zawadi kwa lengo la kuwaongezea ari zaidi ya kuonyesha maajabu.

Kikosi cha Yanga chenye wachezaji 25, kikiwa chini ya Kocha Hans Van der Pluijm, kimeweka kambi kwenye hoteli ya Bahari Beach iliyoko nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam kwa ajili ya kujiandaa kwa mechi hiyo.

Yanga ilianza mazoezi juzi jioni kwenye uwanja wa Kaunda yaliko makao makuu ya klabu hiyo na jana asubuhi iliendelea kujifua kwenye uwanja wa Boko Beach.

HANS ATAMBA
Akihojiwa na tovuti ya Yanga jana, Hans alisema anashukuru vijana wake wote wapo katika hali nzuri na kwamba hadi sasa hakuna mchezaji majeruhi.

Hans alisema wanatambua mchezo wao dhidi ya Al Ahly, ambao ni mabingwa watetezi wa michuano hiyo, utakuwa mgumu kwa vile wapinzani wao wana uzoefu mkubwa wa michuano ya kimataifa.

"Hakuna kinachoshindikana katika soka, nimewahi kucheza nao nikiwa Ghana katika timu ya Berekum Chelsea katika hatua ya makundi ya robo fainali, hivyo nawajua vizuri jinsi wanavyocheza na kocha Mkwasa alipata fursa nzuri ya kuwaona wiki iliyopita, hivyo naamini mambo yatakuwa mazuri,"alisema kocha huyo kutoka Uholanzi.

Hans alisema lengo la Yanga ni kuweka historia ya kushinda mchezo wa keshokutwa na wa marudiano na kwamba, kikubwa ni kukiandaa kikosi chake kiakili, morari, umoja na nidhamu ya ndani na nje ya uwanja.

WAARABU KIMYAA
Wakati huo huo, kikosi cha wachezaji 22, maofisa wanane wa benchi la ufundi na viongozi watano wa Al Ahly, kiliwasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere mjini Dar es Salaam jana kwa ajili ya mechi dhidi ya Yanga.

Kikosi hicho kilitua uwanjani hapo alfajiri ya saa 11.45 kwa ndege ya Shirika la Ndege la Misri na kupanda kwenye basi aina ya Yutong lenye namba za usajili T 391 CRT lililokuwa na maandishi ya Kakote Trans na kupelekwa moja kwa moja kwenye hoteli ya Hyatt Kempsinki.

Hakuna kiongozi yeyote wa timu hiyo ya Misri aliyekuwa tayari kuzungumza na waandishi wa habari wachache waliokuwepo uwanjani hapo. Viongozi na wachezaji wa timu hiyo walitoka nje ya uwanja wakiwa kimya.

Al Ahly imepanga kufanya mazoezi yake jana na leo jioni katika uwanja wa IST ulioko Upanga na kesho jioni itafanya mazoezi yake ya mwisho kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika pambano la keshokutwa kati ya Yanga na Al Ahly.

Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Kimataifa ya Yanga, Seif Ahmed 'Magari', alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, Membe anatarajiwa kutua nchini keshokutwa asubuhi kutoka nje ya nchi.

Magari alisema waamuzi wa mchezo huo kutoka Ethiopia walitarajiwa kutua nchini jana usiku kwa ndege ya Shirika la Ndege la Ethiopia.

Aliongeza kuwa, uongozi wa Yanga kwa kushirikiana na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na Jeshi la Polisi mkoa wa Dar es Salaam, wameandaa ulinzi mkali ili kudhibiti vitendo vya vurugu wakati wa mchezo huo.

Magari alisema pia kuwa, kambi ya Yanga iliyoko hoteli ya Bahari Beach, imewekwa chini ya ulinzi mkali ili kuhakikisha wachezaji hawapati bughudha kutoka kwa mashabiki na jamaa zao.

Tiketi za mchezo huo zinatarajiwa kuanza kuuzwa leo Jijini Dar es Salaam katika vituo 10 vilivyotengwa maalumu kwa kazi hiyo.

Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto amesema kiingilio cha juu kwa VIP A kitakuwa sh. 35,000 wakati VIP B na C ni sh. 25,000.

Viti vya rangi ya chungwa ni sh. 13,000 na viti vya bluu na kijani ni sh. 7000. Mashabiki wameombwa kununua tiketi hizo katika sehemu zilizotangazwa.

Vituo vya mauzo ya tiketi hizo ni makao makuu ya klabu hiyo mitaa ya Twiga na Jangwani, Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Kidongo Chekundu, Buguruni, Uwanja wa Taifa, Dar Live, Stears, Ubungo, Kituo cha Mabasi Mbezi Mwisho na Mwenge.

Tiketi hizo zitakuwa na vipande vinne, ambapo kipande kimoja kitabaki kwa muuzaji, cha pili getini, cha tatu upande anaokaa shabiki na cha nne kitabaki kwa shabiki mwenyewe ili kuepuka kuingia watu zaidi ya wawili kwa kutumia tiketi moja.

WAARABU WANAFUNGIKA-MKWASA



KOCHA Msaidizi wa Yanga, Charles Boniface Mkwasa amesema kikosi chao kina kila sababu ya kushinda mchezo wao wa michuano ya klabu bingwa Afrika dhidi ya Al Ahly ya Misri.

Akizungumza na Burudani mjini Dar es Salaam wiki hii, Mkwasa alisema baada ya kuishuhudia Al Ahly ikicheza na Sfaxien ya Tunisia mjini Cairo, ana hakika Yanga itashinda mechi hiyo.

Yanga inatarajiwa kuvaana na Al Ahly keshokutwa katika mechi ya awali ya raundi ya pili itakayopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kabla ya timu hizo kurudiana wiki mbili baadaye mjini Cairo.

Boniface alikwenda Misri wiki iliyopita kwa lengo la kuichunguza Al Ahly inavyocheza mechi za nyumbani, mbinu zake za nje ya uwanja na uwezo wa timu nzima.

Kocha huyo aliishuhudia timu hiyo ikiichapa Sfaxien mabao 3-2 katika mechi ya fainali ya kuwania Kombe la Super, ambayo huzikutanisha bingwa wa ligi ya mabingwa wa Afrika na mshindi wa Kombe la Shirikisho.

"Tuna uwezo mkubwa wa kuifunga Al Ahly kwa sababu kikosi chetu kwa sasa ni kizuri na kinaundwa na wachezaji wengi wenye kiwango cha juu,"alisema.

Alizitaja sababu zingine zitakazoiwezesha Al Ahly kushinda mechi hiyo kuwa ni umoja na mshikamano uliopo miongoni mwa wanachama, mashabiki na viongozi wa Yanga.

Mkwasa alisema kwenda kwake Misri na kuishuhudia Al Ahly ikicheza na Sfaxien, kumemwezesha kubaini kasoro nyingi zilizoko kwenye kikosi hicho cha waarabu na mbinu wanazopaswa kutumia ili kushinda mechi zote mbili.

"Zipo mbinu nyingi tunazoweza kuzitumia kuwashinda, lakini siwezi kuzizungumza, lakini nilichoweza kugundua ni kwamba wanafungika. Tutazitumia kasoro walizonazo kupata ushindi,"alisema.

Mkwasa alisema jambo muhimu kwa wachezaji wa Yanga ni kucheza kwa ari na kujituma na kuondoa hofu inayoweza kujengeka miongoni mwao kutokana na kupambana na mabingwa hao wa Afrika.

SIMBA KUTUMIA MIL 100/- KUJENGA UWANJA BUNJU




NA AMINA ATHUMANI
KLABU ya Simba imetangaza kujenga uwanja wake ndani ya siku 100 na kuanza kuutumia kwa ajili ya mazoezi ya timu hiyo.

Katibu Mkuu wa Simba, Ezekiel Kamwaga, alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, uwanja huo ambao utawekewa nyasi bandia, utaanza kufanyiwa maandalizi ya ujenzi kuanzia mwishoni mwa wiki hii.

Kamwaga alisema katika maandalizi ya ujenzi wa uwanja huo, wanachama wa klabu hiyo wanaombwa kujitokeza kwa wingi Jumamosi kwenda kufanya usafi kwa ajili ya maaandalizi ya ujenzi huo.

"Klabu sasa imeamua kwa nguvu zote kuanza ujenzi wa uwanja wake, na maandalizi kwa ajili ya ujenzi huo yaatanza Jumamosi," alisema Kamwaga.

Katibu huyo alisema maandalizi mengine kwa ajili ya ujenzi huo yanaendelea vizuri ikiwa ni pamoja na kukamilisha taratibu na kampuni itakayosimamia ujenzi huo.

Alisema kwa sasa klabu yake itajenga sehemu ya uwanja wa kuchezea soka kabla ya kujenga sehemu ya pili ya majukwa na kuwekwa maduka na hosteli za wachezaji.

Alisema ni matarajio yake kuwa uwanja huo utakamilika ndani ya siku hizo kama ilivyopangwa na kuanza kutumika mara moja ikiwa ni pamoja na kufanya maandalizi ya msimu ujao wa ligi.

22 WAITWA TAIFA STARS, KIM POULSEN AFUNGASHIWA VIRAGO


NA AMINA ATHUMAN
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limetangaza kikosi chenye wachezaji 22 kitakachoivaa Namibia katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa uliopo kwenye kalenda ya Shirikisho la Kimataifa la Soka (FIFA), bila ya kumshirikisha Kocha Mkuu wa timu hiyo, Kim Poulsen.

Stars na Nambia zitashuka dimbani Machi 5 mwaka huu, katika mchezo utakaofanyika jijini Windhoek, Namibia.

Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura, alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, timu hiyo ilichaguliwa na Kamati ya Utendaji ya TFF iliyokutana hivi karibuni.

Wambura alisema mbali ya kamati hiyo kuteua kikosi hicho, itatangaza ndani ya saa 48 jina la kocha atakayeifundisha timu hiyo kuelekea mchezo huo.

Alisema timu hiyo itaingia kambini keshokutwa kwenye hoteli ya Accommondia na kufanya mazoezi ya siku mbili kabla ya kuondoka nchini Machi 3 mwaka huu kwenda Windhoek.

Aliwataja wachezaji wanaounda timu hiyo kuwa ni makipa Deogratius Munishi (Yanga), Ivo Mapunda (Simba) na Mwadini Ally (Azam). Mabeki wa pembeni ni Edward Charles (JKT Ruvu), Erasto Nyoni (Azam), Hassan Mwasapili (Mbeya City) na Michael Aidan (Ruvu Shooting).

Wengine ni mabeki wa kati, Aggrey Morris (Azam) na Kelvin Yondani (Yanga) wakati viungo ni Amri Kiemba (Simba), Athuman Idd (Yanga), David Luhende (Yanga), Frank Domayo (Yanga), Jonas Mkude (Simba) na Mwinyi Kazimoto (Markhiya Sports Club, Qatar).

Pia wamo washambuliaji Athanas Mdamu (Alliance Mwanza), Haruna Chanongo (Simba), Khamis Mcha (Azam), Mbwana Samata (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC), Mrisho Ngasa (Yanga), Ramadhan Singano (Simba) na Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC).

UKWA ASHEREHEKEA KUTIMIZA MIAKA 34




LAGOS, Nigeria
MMOJA wa wacheza filamu nyota wa Nigeria, Osita Iheme, maarufu zaidi kwa majina ya Pawpaw na Ukwa, mwishoni mwa wiki iliyopita alisherehekea kutimiza umri wa miaka 34.

Ukwa aliandaa sherehe hiyo kiasili, kijijini kwake Obeagu, Mashariki mwa Nkanu katika Jimbo la Nigeria.

Mshindi huyo wa tuzo mbalimbali za filamu nchini Nigeria, alisherehekea siku hiyo akiwa na rafiki zake, wacheza filamu wenzake na mashabiki wake wanaoishi Obeagu.

Kwa sasa, Ukwa yuko katika maandalizi ya kucheza filamu mpya, akiwa na swahiba wake mkubwa, Chinedu Ikedieze, maarufu kwa jina la Aki na waigizaji wengine.

"Naona fahari na heshima kuwa na watu hawa na pia nimeridhishwa na zawadi ndogo nilizopewa na waigizaji wenzangu hapa kwa ajili ya kusherehekea siku hii,"alisema Ukwa wakati wa sherehe hiyo.

"Ninashukuru kwa upendo waliouonyesha kwangu japokuwa hii ni sherehe ndogo kwa ajili ya siku hii maalumu kwangu. Sherehe kubwa zaidi inakuja baada ya hapa," alithibitisha.

Ukwa alizaliwa Agosti 1982 katika kijiji cha Mbaitoli kilichoko Jimbo la Imo na amejipatia sifa na umaarufu kutokana na kucheza filamu nyingi akiwa na Aki.

GENEVIEVE, MIKEL OBI WATANUA 'SAUZI'





LAGOS, Nigeria
MWIGIZAJI nyota na mwenye mvuto nchini Nigeria, Genevieve Nnaji hivi karibuni alionekana nchini Afrika Kusini akivinjari na mwanasoka nyota wa klabu ya Chelsea na timu ya Taifa ya Nigeria, Mikel Obi.

Genevieve na Obi walionekana wakiwa pamoja kwenye uwanja mmoja wa ndege nchini humo kabla ya kukwea pipa dogo la kukodi kwenda kusikojulikana.

Mwanadada huyo mwenye mtoto mmoja, alikuwa wa kwanza kuwasili kwenye uwanja huo kwa gari dogo la kifahari kabla ya Obi naye kuwasili akiwa kwenye gari lingine la kifahari lenye rangi ya kumeremeta.

Haikuweza kufahamika mara moja nyota hao walikwenda Afrika Kusini kufanya nini na iwapo wana uhusiano wa kimapenzi.

Katika hatua nyingine, Genevieve amewataka wanawake duniani kujenga utamaduni wa kulindana kama wanavyofanya kwa mabinti zao.

Genevieve amesema hayo wiki hii kupitia akaunti yake ya twitter, kauli ambayo imedhihirisha kwamba ni mama anayewajali wanawake wenzake.

"Mtoto wa kike ataushika mkono wako kwa muda, lakini ataushika moyo wako milele. Mlinde kila mwanamke kama utakavyomlinda binti yako," ameeleza Genevieve kwenye ujumbe wake huo.

MERCY JOHNSON AONGOZA KWA UTAJIRI NOLLYWOOD





LAGOS, Nigeria
MCHEZA filamu machachari Mercy Johnson wa Nigeria ndiye anayeongoza kwa utajiri kwa sasa miongoni mwa wacheza filamu wa kike nchini humo.

Mercy, mzaliwa wa kitongoji cha Igbira kilichoko katika Jimbo la Kogi, ndiye mwigizaji anayecheza filamu nyingi kuliko wanawake wenzake wa Nollywood.

Uchunguzi uliofanywa na mtandao wa YES International, umebaini kuwa, Mercy amekuwa akilipwa kati ya Naira milioni 1.5 hadi Naira milioni mbili kwa filamu moja.

Kwa mujibu wa mtandao huo, haipiti mwezi bila kumuona Mercy akicheza filamu zisizopungua mbili katika mwezi mmoja na hivyo kuwa mwigizaji aliye bize kuliko wenzake.

Uchunguzi wa mtandao huo pia umebaini kuwa, watayarishaji wa filamu nchini Nigeria wamekuwa wakiandaa filamu zao huku wakipanga jinsi ya kumshirikisha na hivyo kumuongezea sifa, umaarufu na utajiri.

"Hali imekuwa hivyo kwa muda mrefu sasa. Hata alipokuwa na uja uzito, alikuwa akifanyakazi bila kusimama, ikiwa ni pamoja na kwenda kupiga picha za filamu nchini Marekani akiwa na tumbo kubwa," umeripoti mtandao huo.

Baadhi ya filamu za hivi karibuni, ambazo zimemfanya mwanadada huyo mwenye mtoto mmoja awe tajiri na maarufu ni pamoja na Obioma The Slave Girl, Sleeping Walker, Heart of A Twin 1 & 2, Mud of Hardship, Dumebi and Bitterleaf Cyhtia, There are also Daniella, First Experience na Endless Agony.

Zingine ni Immaculate Heart, Painful Soul, Tears of Madness, Weeping Kingdom, Troubled King, Baby Oku in America, Dumebi in School, Somma The Local Champion, Ebute The Only Girl, Leave My Tears 1 & 2, Mary The Hunter, Cry of A Widow na Voice of A Mother.

Kutokana na utajiri alionao sasa, Mercy amewapiku wacheza filamu wengine nyota wa Nigeria kama vile Genevieve Nnaji, Patience Ozokwor 'Mama G', Omotola Jalade na Ini Edo.

Mercy amefunga ndoa na Odianosen Okojie, ambaye wamezaa mtoto mmoja wa kike, anayeitwa
Purity. Mercy ni mtoto wa nne katika familia yenye watoto saba.

Alizaliwa Agosti 28, 1984. Alijitosa kwenye fani ya filamu kutokana na kuvutiwa na Genevieve. Filamu yake ya kwanza ilimwingizia Naira 50,000.

TWIGA STARS KULIPA KISASI KWA WAZAMBIA LEO?



TIMU ya soka ya Taifa ya Wanawake, Twiga Stars inashuka dimbani kesho kumenyana na Zambia katika mechi ya marudiano ya raundi ya kwanza ya michuano ya kuwania ubingwa wa Afrika.

Twiga Stars itashuka dimbani kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam, ikiwa na kumbukumbu ya kuchapwa mabao 2-1 na Zambia katika mechi ya awali iliyochezwa wiki iliyopita mjini Lusaka.

Ili iweze kusonga mbele katika michuano hiyo, Twiga Stars inahitaji ushindi wa aina yoyote, ikiwa ni pamoja na wa bao 1-0, ambao utaiwezesha kutinga raundi ya pili kwa faida ya bao la ugenini.

Iwapo Twiga Stars itafungwa ama kutoka sare ya aina yoyote, itakuwa imeaga michuano hiyo. Twiga Stars imewahi kucheza fainali za michuano hiyo mara mbili na kutolewa hatua ya awali.

Kikosi cha Zambia kikiwa na wachezaji 18 na viongozi saba, kinatarajiwa kuwasili nchini leo mchana kwa ndege ya Shirika la Ndege la Zambia kwa ajili ya mechi hiyo.
Kocha Mkuu wa Twiga Stars, Rogasian Kaijage, alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, kikosi chake kimejiandaa vyema kushinda mechi hiyo kwa lengo la kusonga mbele.
Kaijage alisema hakuna majeruhi kwenye kikosi chake na wachezaji wote wana ari kubwa ya kulipa kisasi cha kufungwa na Zambia ugenini.
Nahodha wa timu hiyo, Fatuma Mwasikili alisema wamejiandaa vyema kushinda mechi hiyo na amewaomba mashabiki kujitokeza kwa wingi kuwashangilia ili kuwaongezea nguvu.
Kwa mujibu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), hakutakuwa na kiingilio katika mechi hiyo, lengo kubwa likiwa kupata mashabiki wengi wa kuishangilia Twiga Stars kwa lengo la kuipa nguvu.
Mechi hiyo itakayoanza saa 10 jioni, itachezeshwa na waamuzi Ines Niyonsaba, Jacqueline Ndimurukundo, Axelle Shikana na Suavis Iratunga kutoka Burundi. Waamuzi hao walitarajiwa kuwasili nchini jana jioni.
Kamishna wa mechi hiyo atakuwa Fran Hilton Smith kutoka Afrika Kusini, ambaye anatarajiwa kutua nchini leo asubuhi kwa ndege ya Shirika la Ndege la Afrika Kusini.

LULU: KANUMBA ALIKUWA MPENZI WANGU



NA FURAHA OMARY

MSANII nyota wa filamu nchini, Elizabeth Michael, maarufu kama Lulu, amekubali mahakamani
kuwa walikuwa na uhusiano wa kimapenzi na aliyekuwa msanii mwenzake, Steven Kanumba (marehemu), na siku ilipotokea kifo cha msanii huyo walikuwa na ugomvi.

Mcheza filamu huyo alisema hayo jana katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, na kuongeza kuwa, siku ya tukio alikwenda nyumbani kwa Kanumba, Sinza Vatican, ambako ulitokea ugomvi wakiwa chumbani kwa marehemu.

Lulu, ambaye anakabiliwa na kesi ya kumuua Kanumba bila kukusudia, alikubali hayo mbele ya Jaji Rose Teemba baada ya Wakili wa Serikali Mwandamizi, Monica Mbogo, kumsomea maelezo ya shitaka hilo la kuua bila kukusudia.

Katika kesi hiyo, Lulu anadaiwa Aprili 7, 2012, eneo la Sinza Vatican, wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, alimuua Kanumba bila kukusudia. Hata hivyo, mshitakiwa huyo alikana shitaka hilo.
"Nakubali kwamba tulikuwa na uhusiano wa kimapenzi na Kanumba na siku ya tukio nilimtembelea nyumbani kwake na kuingia chumbani kwake na kulikuwa na ugomvi baina yetu. Nakubali nilijaribu kutoka nje, lakini Kanumba alinivuta ndani na kufunga mlango," alisema Lulu.

Lulu pia alikubali kuwa alitoka chumbani na kwenda kumfahamisha mdogo wake,Seth Bosco, kwamba kaka yake ameanguka na kweli baada ya tukio alikamatwa maeneo ya Bamaga na kufikishwa mahakamani.

Awali, akisoma maelezo hayo, Monica alidai kuwa, Aprili 7,2012, Kanumba alikuwa nyumbani kwake maeneo ya Sinza Vatican na mdogo wake, Seth na ilipofika saa sita usiku, alimwambia Seth ajitayarishe waende kustarehe na wakati wanajiandaa, alifika Lulu na kuingia chumbani kwa Kanumba moja kwa moja.

Monica alidai baada ya dakika chache kupita, mdogo wa Kanumba, Seth alisikia malumbano ambapo Kanumba alikuwa akimlalamikia Lulu kwa nini anasikiliza simu ya bwana wake mbele yake na wakaanza kugombana na alimsikia Lulu akilia.

Wakili huyo alidai Seth alisogolea mlangoni na kumkuta mshitakiwa akijitahidi kutaka kutoka nje, lakini Kanumba alimvuta na kumuingiza ndani na kufunga mlango na baada ya muda Lulu alitoka na kumfahamisha kwamba Kanumba amedondoka.

Alidai Seth alikwenda na kumkuta Kanumba yuko sakafuni na hajitambui, hivyo aliamua kumpigia simu daktari wake binafsi, Parpas Kageia, ambaye alifika na alipomfanyia uchunguzi, aligundua ameshafariki, lakini hakumwambia mdogo wake. Alidai daktari alimwambia mdogo wake wamchukue na kumpeleka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), ambako waliufanyia mwili uchunguzi na kubaini ameshafariki.

Monica alidai mshitakiwa alikamatwa siku hiyo alfajiri eneo la Bamaga na kwa mujibu wa ripoti ya kitabibu ya daktari, Kanumba alifariki kwa kushindwa kupumua kutokana na msukumo katika ubongo na alikuwa na uvimbe katika ubongo na pia ulipata mtikisiko.

Wakili huyo alidai wakati wa usikilizwaji wa shauri hilo, wataita mashahidi wanne akiwemo mdogo wa Kanumba, Seth na daktari wake binafsi na hawatakuwa na kielelezo.

Kwa upande wa mawakili wa Lulu, Peter Kibatala na Fulgence Massawe, walidai watakuwa na mashahidi watano na vielelezo viwili, ambavyo ni panga na ripoti ya uchunguzi ya daktari aliyofanyiwa Lulu.

Jaji Rose aliahirisha shauri hilo hadi kikao kingine kitakachopangwa na mahakama.

NYOTA WA HOTELI RWANDA AMZIMIA GENEVIEVE NNAJI





LAGOS, Nigeria

HAKEEM Kae-Kazim ni mcheza filamu wa Nigeria mwenye uraia wa Uingereza, ambaye alijipatia sifa na umaarufu mkubwa mwaka 2004 kwa kuigiza kama Georges Rutaganda katika filamu ya Hotel Rwanda, iliyoshinda tuzo lukuki.

Mnigeria huyo, aliyezaliwa Oktoba Mosi, 1962, amecheza filamu nyingi zilizotengenezwa Hollywood, zikiwemo 24, aliyoigiza kama Kanali Ike Dubaku na tamthilia ya Redemption.

Kwa upande wa filamu za Kinigeria, ameshiriki kucheza chache kama vile Last Flight To Abuja na Half Of A Yellow Sun.

Akihojiwa na mtandao wa naijerules wa Nigeria hivi karibuni, Hakeem alielezea mambo mbalimbali kuhusu kazi yake, maisha ya familia na mengineyo. Yafuatayo ni mahojiano hayo ya ana kwa ana.

SWALI: Unajisikiaje kuishi sehemu kubwa ya maisha yako nje ya Nigeria?

JIBU: Ni jambo zuri, lakini kwangu naona la kawaida. Hakuna kitu maalumu hasa, na kama unavyofahamu mimi ni Mnigeria na ninatumia jina la Kinigeria. Lakini sifikirii iwapo nilikosa chochote kwa sababu hadi miaka miwili iliyopita, nimekuwa na kawaida ya kuja kusherehekea sikukuu ya Krismas hapa Nigeria. Napenda vyakula vya asili, napenda mavazi yetu ya asili.

SWALI: Kwa maana hiyo, huwa unakuja kuitazama familia yako wakati wa Krismas?

JIBU: Ndio, huwa nakuja kumtazama mama kwa sababu nilikuwa na umri wa miaka miwili wakati wazazi wangu waliponichukua mimi na kaka yangu mkubwa kwenda Uingereza na tangu wakati huo, tumekuwa tukiishi huko. Lakini kwa sasa baba yangu ni marehemu na mama yangu amekuwa akisafiri mara kwa mara kati ya Nigeria na Uingereza, lakini kaka yangu mkubwa yuko Uingereza pamoja na familia yake. Mimi natoka Abeokuta hivyo huwa natembelea huko mara kwa mara kwenda kumuona mama yangu.

SWALI: Ulianzaje kazi ya uigizaji?

JIBU: Nilianza kwa kujifunza sanaa za maonyesho na baada ya hapo, nikawa nashiriki kufanya maigizo ya kwenye steji Uingereza. Baadaye nilihamia Afrika Kusini na kucheza filamu nyingi pamoja na matangazo ya biashara katika televisheni ya Afrika Kusini. Baada ya kutoka Afrika Kusini, nilihamia Marekani, ambako naishi sasa, nikiwa naendelea kufanya kile ninachokipenda, uigizaji wa filamu.

SWALI: Umeshiriki kucheza filamu nyingi zilizotamba kama vile Hotel Rwanda na 24, ipi iliyokuletea mafanikio makubwa?

JIBU: Kila moja ni nzuri kutokana na utayarishaji wake. 24 ilikuwa filamu bomba na baadaye Hotel Rwanda, ambayo nilifurahia kushiriki kuicheza. Baadaye nilicheza filamu ya X-Men Origins, Wolverine na Pirates of the Caribbean.

SWALI: Nafikiri haikuwa kazi rahisi. Ni changamoto zipi ulizokumbana nazo ukiwa mwafrika uliyejitosa Hollywood?

JIBU: Ni kweli, mwanzoni haikuwa kazi rahisi kwa sababu kuna wakati niliishiwa na kukosa hata pesa ya chakula. Kupata nafasi ya kucheza filamu pia ilikuwa changamoto kwa sababu hapa Nigeria, unakuwa na uhakika wa kupata muswada wa filamu, lakini haiko hivyo katika nchi kama Uingereza. Kama unapata nafasi ya kucheza filamu leo, huwezi kupata nyingine labda hadi baada ya miezi miwili au mitatu. Lakini yote kwa yote, nimepata uzoefu mzuri.

SWALI: Ulikuja Nigeria siku chache zilizopita na tayari umeshiriki kutengeneza tangazo la Etisalat ukiwa na Genevieve Nnaji. Unajisikiaje kupata nafasi ya kushirikiana naye katika kazi hiyo?

JIBU: Kusema kweli, Genevieve ni msichana mrembo na ni mzuri kwa kila anachokifanya. Hivyo nilipata faraja kufanya naye kazi pamoja.

SWALI: Kama ni mzuri kiasi hicho, unafikiri anaweza kupata nafasi ya kuingia Hollywood?

JIBU: Inategemea na nafasi itakayomjia na namna atakavyojiandaa kuipokea. Kama atapata nafasi nzuri na kucheza filamu yenye kiwango cha kimataifa, anaweza kukipata kile anachokitarajia na kutambulika kimataifa.

SWALI: Ni kitu gani kingine kilichokufanya uje Nigeria?

JIBU: Mbali na tangazo la Etisalat, pia nimekuwa nikifanya kazi kwa kushirikiana na baadhi ya waongozaji filamu wa Nigeria kuhusu jinsi ya kukuza kiwango cha filamu za Nollywood ili kilingane na ladha ya kimataifa. Hivyo najiandaa kufungua shule ya kimataifa ya uigizaji filamu, ambayo watu wetu watapata mafunzo.

SWALI: Unayo mipango yoyote ya kucheza filamu ya Kinigeria hivi karibuni?

JIBU: Hapana

SWALI: Kwa nini miswada yetu ya filamu haikuvutii?

JIBU: Nollywood bado inakua na bado haijafikia kiwango cha kimataifa katika masuala ya uongozaji na utayarishaji. Lakini wapo waongozaji wachache wa filamu Nollywood, ambao wana mtazamo sawa na wa kwangu na nimewahi kufanyanao kazi siku za nyuma.

Nimefanya kazi na Tunde Babalola katika filamu ya Last Flight To Abuja, iliyotengenezwa Uingereza. Ni mtu mwenye mtazamo chanya katika masuala ya filamu. Pia nimecheza filamu ya Half Of A Yellow Sun.

Hivyo kama nitapata watu kama yeye na miswada mizuri, kwa nini nisicheze filamu za Kinigeria. Wakati umefika kwetu kuanza kutengeneza filamu zinazoelezea habari zetu na historia yetu. Hatupaswi kusubiri watu wengine watuelezee habari zetu kwa sababu wataeleza visivyo. Tunao watu mashuhuri kama vile Sango, Nnamdi Azikiwe, Awolowo na wengine. Tunahitajika kutengeneza filamu za kihistoria kuhusu wao.

SWALI: Kwa kawaida, wacheza filamu huwa ni watu wa kuhamahama kutoka sehemu moja hadi nyingine. Unawezaje kuwa na muda wa kufurahi na familia yako?

JIBU: Ninaye mke mwelewa pamoja na watoto watatu. Anaelewa aina ya kazi ninayoifanya na kunisaidia katika mambo mengi.

SWALI: Huwa halalamiki?

JIBU: Ni kweli huwa analalamika kwa sababu muda mwingi nakuwa safarini. Anatoka Afrika Kusini na huko ndiko nilikokutana naye. Tulifunga ndoa na nilikwenda naye Uingereza.Jambo la kufurahisha ni kwamba, kwa sasa natengeneza filamu nyingi Afrika Kusini na mtoto wangu wa mwisho bado hajafikisha umri wa miaka miwili. Lakini nimekuwa nikimuona na kuzungumza naye kupitia mtandao wa Skype kila ninapokuwa sipo nyumbani.

SWALI: Nina hakika unao mashabiki wengi wa kike. Unawezaje kushirikiana nao?

JIBU: Ni kweli ninao mashabiki wengi wa kike, lakini kuna muda maalumu kwa kila kitu. Ninao muda wa kukutana na rafiki zangu, familia na mashabiki wangu, hivyo siwezi kuacha muda huo uingiliane na mwingine. Siku zote huwa napenda kuwajulisha mashabiki wangu wa kike kwamba, nimeoa, hivyo siwaruhusu wawe karibu na mimi bila sababu.
SWALI: Umewahi kukumbana na tukio lolote la kufedhehesha kutoka kwa shabiki wa kike?
JIBU: Ndio, kuna mmoja tulikutana nilipopanda treni akaniona. Akaanza kupiga kelele na kulitaja jina langu. Alitaka kumfanya kila mtu afahamu kwamba mimi ndiye Hakeem na nimecheza filamu fulani na fulani. Lilikuwa tukio la kufedhehesha sana.

Sunday, February 16, 2014

TFF YAREJESHA MICHUNO YA KOMBE LA TAIFA




MASHINDANO maalumu ya mikoa ya kuunda kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ yanatarajiwa kuanza kutimua vumbi Februari 22 hadi Machi 5 mwaka huu, huku ikiigharimu Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) takribani Sh. Milioni 360.

Michuano hiyo maalumu itashirikisha mikoa wanachama ya TFF na itakuwa ikichezwa kwa mfumo wa nyumbani na ugenini kwa timu mbili za kanda moja kuchuana na inatarajiwa kutoa wachezaji bora 60 wataoweka kambi ya siku 30 Tukuyu, Rungwe mkoani Mbeya.

Mashindano ya Kombe la Taifa miaka ya nyuma yalikuwa eneo zuri la kuibua vipaji; Pichani ni nyota wa miaka ya 1980, Abubakar Salum 'Sure Boy' akiichezea Yanga, hapa anamtoka beki wa Simba SC Iddi Selemani 'Meya' katika mechi ya watani mwaka 1989.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mjini Dar es Salaam, Rais wa TFF Jamal Malinzi amesema michuano hiyo ni maalumu kwa ajili ya kuuunda upya kikosi bora cha Stars, ili kiweze kufuzu kwa fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) yatakayofanyika mwakani nchini Morocco.

Malinzi alisema jumla ya timu 32 za Tanzania nzima zitashiriki michuano hiyo, kila mechi moja watakuwepo wasaka vipaji watano ‘Scouts’ kwa ajili ya kumulika wachezaji bora, pia mechi zote zitakuwa zikirekodiwa.

Baada ya zoezi la kuibua vipaji kwenye michuano hiyo, wasaka vipaji wote watajifungia (retreat) kwa muda wiki moja mjini Lushoto, Tanga kupitia rekodi zote za mechi na kuchagua wachezaji 60 bora, ambao watapelekwa Tukuyu, Mbeya kwa ajili ya mazoezi makali na wataalamu mbalimbali.

Wachezaji hao 60 watachujwa baada ya mwezi mmoja na kubaki 30, ambao watachanganywa na wachezaji wa sasa wa Taifa Stars na baadaye kupatikana kikosi bora kwa ajili ya mapambano ya kuwania kufuzu kwa AFCON.

Malinzi alisema wachezaji wa sasa wa Stars nao watakwenda kwenye kambi hiyo mkoani Mbeya mara baada ya kumalizika kwa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) mwezi Aprili.

“Tunaamini mfumo huo utasaidia kupata vijana wapya wa kuboresha kikosi cha Stars, hatutachagua majina wala kuangalia umri kwa kuwa hiki ni kipindi cha mpito na ni muda mchache umebakia kuelekea kwenye michuano hiyo,” alisema Malinzi.

Machi 5 mwaka huu Stars itashuka dimbani kuumana na Namibia katika mechi ya kirafiki inayotambuliwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA).

TAIFA STARS KUWEKA KAMBI UHOLANZI





SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limeanza rasmi mikakati ya kuiwezesha timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kufuzu kwa Fainali za mataifa ya Afrika (AFCON) mwakani baada ya kupanga mpango wa timu hiyo kuweka kambi nchini Uholanzi.

Kambi hiyo itakuwa ni maalumu kwa timu hiyo kuweza kujiandaa na hatua ya kufuzu kwa fainali hizo zitakazofanyika mwakani nchini Morocco na kushirikisha jumla ya mataifa 16 yatakayofuzu.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mjini Dar es Salaam, Rais wa TFF, Jamal Malinzi amesema endapo Stars itafanikiwa kupita katika hatua ya awali ya mchujo ikiwa itapangwa kwenye hatua hiyo, wamepanga kuweka kambi nchini Uholanzi ya timu hiyo, ili kujiandaa na hatua ya pili ya makundi.

Malinzi alisema wameamua kufanya hivyo ili kurudia historia ya mwaka 1980 ya Stars kufuzu kwa mara ya mwisho michuano ya AFCON, iliyofanyika nchini Nigeria, ambapo Stars iliweka kambi Uholanzi mwaka 1979 na kufanikiwa kufuzu kwa fainali hizo.

“Tumepokea barua ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF) inayotueleza kuwa mechi zetu za mchujo zitaanza kati ya mwezi Mei hadi Agosti kutokana na kiwango chetu kuwa chini ya nchi 21 bora za bara hili, hivyo muda si mrefu tunafikiria kurekebisha benchi lote la ufundi kwa pamoja na kuanza mikakati ya timu hiyo.

“Huenda timu yetu ikaanzia hatua ya mchujo kama CAF walivyotuandikia, ikifanikiwa kufuzu katika hatua ya makundi ttumepanga kuweka kambi nje ya nchi katika nchi ya Uholanzi, na huko timu itapata mafunzo ya kisasa ili kufanya vizuri kwenye hatua ya makundi,” alisema Malinzi.

Katika hatua nyingine alisema kwa sasa wameshazungumza na Balozi wa Uholanzi hapa nchini kwa ajili ya mipango yao hiyo, pia wamewataarifu wadhamini wakuu wa Stars, Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia kinywaji chao cha Kilimanjaro Premier Lager ili kuandaa bajeti ya ziara hiyo.

MKUTANO MKUU WA KATIBA SIMBA SASA MACHI 16




Mkutano Mkuu wa Marekebisho ya Katiba ya klabu ya Simba umepangwa kufanyika Machi 16 mwaka huu badala ya Machi 23 kama ilivyokuwa imepangwa hapo awali.

Uamuzi wa kurudisha nyuma tarehe ya mkutano huo ulifikiwa jana (Jumatano), katika kikao cha Kamati ya Utendaji ya Klabu kilichokutana usiku Makao Makuu ya Klabu, Mtaa wa Msimbazi, jijini Dar es Salaam.

Kamati ya Utendaji ya Simba imefikia uamuzi huo kufuatia maelekezo kutoka Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), iliyowataka wanachama wake wote mpaka kufikia Machi 20 mwaka huu wawe wameshazifanyia marekebisho katiba zao kwa kuweka kipengele kinachoitambua Kamati za Maadili.

Simba ilipokea barua hiyo na kwa kuzingatia umuhimu huo Uongozi ukaamua kuifanyia kazi kwa kuitisha Mkutano Mkuu ambapo agenda itakuwa ni moja tu nayo ni marekebisho ya katiba.

Mbali na kipengele hicho mkutano huo pia utajadili mapendekezo yote ya marekebisho ya katiba yaliyowasilishwa kwa uongozi ili kujadiliwa na kutolewa maamuzi.

Uongozi wa Simba unawataka wanachama wake kujitokeza kwa wingi siku hiyo kushiriki katika zoezi hilo kwa maslahi ya klabu yao.

Kwa sasa uongozi unafanya mipango ya kutafuta mahali pazuri utakapofanyika mkutano huo na mara baada ya kupatikana basi uongozi utawatangazia wanachama wake.

Asha Muhaji
Ofisa Habari, Simba Sports Club

TWIGA STARS YAPIGWA 2-1 NA ZAMBIA




Twiga Stars imepoteza mechi ya kwanza ya raundi ya kwanza kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa Wanawake (AWC) baada ya leo kufungwa mabao 2-1 na Zambia (Shepolopolo) kwenye Uwanja wa Nkoloma jijini Lusaka.

Hadi dakika 45 za kwanza zinamalizika katika mechi hiyo iliyochezeshwa na mwamuzi Salma Mukansanga timu hizo zilikuwa suluhu.

Wenyeji ndiyo walianza kupata bao lililofungwa na Hellen Mubanga dakika ya 75. Mfungaji huyo aliyeingia kipindi cha pili nchini alimalizia wavuni mpira uliotemwa na kipa Fatuma Omari.

Dakika nne baadaye Zambia ambao walikuwa wakishangiliwa kwa nguvu na washabiki wao baada ya kufunga la kwanza, walipata bao la pili ambalo nahodha wa Twiga Stars, Sophia Mwasikili alijifunga mwenyewe.

Mwasikili alikuwa akijaribu kutoa nje mpira uliopigwa na nahodha wa Shepolopolo, Mupopo Kabange ambapo ulipishana na kipa Fatuma Omari kabla ya kujaa wavuni.

Bao la Twiga Stars lilifungwa na Donisia Daniel dakika ya 90. Beki huyo wa kushoto ambaye pia ni mchezaji wa Tanzanite alipanda mbele kuongeza mashambulizi ambapo akiwa nje ya eneo la hatari alipiga shuti lililomshinda kipa Hazel Nali.

Akizungumza baada ya mechi, Kocha wa Twiga Stars, Rogasian Kaijage alisema amebaini upungufu katika kikosi chake ambao ataufanyia kazi kabla ya mechi ya marudiano ili timu yake iweze kusonga mbele.

“Kwa matokeo haya bado tuna nafasi ya kufanya vizuri kwenye mechi ya marudiano nyumbani na kusonga mbele,” alisema Kaijage.

Twiga Stars iliwakilishwa na Fatuma Omari, Fatuma Bashiru, Donisia Daniel, Fatuma Issa, Evelyn Sekikubo, Sophia Mwasikili, Vumilia Maarifa, Mwapewa Mtumwa/Amina Ali, Asha Rashid, Etoe Mlenzi/Zena Khamis na Shelida Boniface.

Timu hiyo inarejea nyumbani kesho kwa ndege ya Fastjet ambapo itatua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) saa 7 kamili mchana.

Boniface Wambura Mgoyo
Ofisa Habari na Mawasiliano
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
+260 976375482
Lusaka, Zambia

MABINGWA WA AIRTEL RISING STAR WAJAZWA MANOTI



TIMU ya wasichana ya Tanzania imekabidhiwa zawadi ya Sh milioni 16 baada ya kutwaa ubingwa wa michuano ya vijana walio chini ya umri wa miaka 17 ya Kimataifa ya Airtel Rising Stars iliyofanyika Septemba mwaka jana nchini Nigeria.

Timu hiyo ilitwaa taji hilo baada ya kuifunga Kenya bao 1-0 lililofungwa na Donisia Daniel katika fainali hiyo.

Akipokea fedha hizo jana (Februari 10, 2014) Katibu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA), Msanifu Kondo alisema wanaishukuru Kampuni ya Airtel kwa kutimiza ahadi yao ya zawadi ya fedha hizo na tayari wamezikabidhi kwa makocha na wachezaji wa timu hiyo.

Alisema kila mchezaji amepewa Sh 850,000 wakati kocha mkuu wa timu hiyo Rogasian Kaijage amepewa Sh milioni moja na laki mbili na kocha msaidizi amepewa Sh milioni moja.

“Tunawashukuru Airtel kwa kutoa fedha hizo za zawadi kwa timu hii na sisi tumewakabidhi wahusika,” alisema.

Kwa upande wake Afisa Uhusiano wa Airtel Tanzania Jane Matinde alisema wao kama wadhamini wa mashindano hayo wametimiza ahadi yao kwa kukabidhi fedha hizo kwa mabingwa hao.

“Kwa niaba ya Airtel Tanzania tunaipongeza timu ya wasichana ya Tanzania kwa kutwaa ubingwa huo, lakini pia tumetekeleza ahadi yetu ya kukabidhi zawadi, kama mnavyofahamu kampuni yetu imekuwa mstari wa mbele katika kusaidia mambo ya kijamii lakini pia michezo ikiwemo soka kupitia michuano ya vijana ya Airtel Rising Stars kwa kushiriki na klabu ya Manchester United,” alisema.

Mohamed Mharizo
Ofisa Habari wa DRFA
Februari 11, 2014

HIZI NDIZO KAMATI NDOGO ZA TFF


BOARD OF TRUSTEE; Said Hamad El-Maamry, Stephen Mashishanga, Dr Ramadhan Dau, Joel Bendera, Mohamed Abdul Aziz

Kamati ya Nidhamu; Tarimba Abbas (Mwenyekiti), Advocate Jerome Msemwa (Makamu Mwenyekiti), Kassim Dau, Nassoro Duduma, Kitwana Manara.

Kamati ya Rufani ya Nidhamu; Profesa Mgongo Fimbo (Mwenyekiti), Advocate Hamidu Mbwezeleni (Makamu Mwenyekiti), Titus Bandawe, Twaha Mtengera, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) mstaafu Boniface Mpaze.

Kamati ya Maadili; William Erio (Mwenyekiti), Advocate Ezekiel Maganja (Makamu Mwenyekiti), Advocate Victoria Mandari, Kanali mstaafu Enos Mfuru na Said Mtanda.

Kamati ya Rufani ya Maadili; Jaji mstaafu Stephen Ihema (Mwenyekiti), Wakili Alesia Mbuya (Makamu Mwenyekiti), Lilian Kitomari, Jabir Shekimweri na Chabanga Hassan Dyamwale.

Kamati ya Uchaguzi; Advocate Melchesedeck Lutema (Mwenyekiti), Advocate Walter Chipeta (Makamu Mwenyekiti), Hamidu Mahmoud Omar, Jeremiah John Wambura, Hassan Dalali.

Kamati ya Rufani ya Uchaguzi; Advocate Julius Lugaziya (Mwenyekiti), Advocate Mwita Waissaka (Makamu Mwenyekiti), Juma Abeid Khamis, Rashid Dilunga, Masoud Issangu.

Kamati ya Fedha na Mipango; Wallace Karia (Mwenyekiti), Francis Ndulane (Makamu Mwenyekiti), Omari Walii, Eliud Mvella, Said Muhammad, Geofrey Nyange, Kidao Wilfred, Ayoub Nyenzi, Lina Kessy, Cyprian Kuhyava.

Kamati ya Mashindano; Geofrey Nyange (Mwenyekiti), Clement Sanga (Makamu Mwenyekiti), Msafiri Mgoyi, James Mhagama, Mohamed Nassoro, Moses Katabaro, Seif Ahmed, Gerald Ambi, Davis Mosha, Said George, Nassoro Idrissa (Mshauri wa Rais Ufundi- Pelegrinius Rutayuga).

Kamati ya Ufundi; Kidao Wilfred (Mwenyekiti), Athumani Kambi (Makamu Mwenyekiti), Vedastus Lufano, Blassy Kiondo, Rahim Kangezi, Patrick Kahemele, Daud Yassin, Nicholas Mihayo, Dk. Cyprian Maro (Mshauri wa Rais Ufundi- Pelegrinius Rutayuga).

Kamati ya Mpira wa Miguu wa Vijana; Ayoub Nyenzi (Mwenyekiti), Khalid Abdallah (Makamu Mwenyekiti), Ali Mayay, Mulamu Ng’hambi, Apollo Kayungi, Said Tully, Luteni Kanali Charles Mbuge, Lameck Nyambaya, Ibrahim Masoud (Mshauri wa Ufundi wa Rais- Pelegrinius Rutayuga).

Kamati ya Mpira wa Miguu wa Wanawake; Lina Kessy (Mwenyekiti), Shyrose Bhanji (Makamu Mwenyekiti), Zena Chande, Amina Karuma, Dk. Cecilia Makafu, Zafarani Damoder, Beatrice Mgaya, Sofia Tigalyoma, Martin Mung’ong’o, Ingridy Kimaro.

Kamati ya Waamuzi; Saloum Umande Chama (Mwenyekiti), Nassoro Said (Makamu Mwenyekiti), Charles Ndagala (Katibu), Riziki Majala, Kanali Isaro Chacha, Paschal Chiganga, Victor Mwandike, Soud Abdi, Zahra Mohamed.

Kamati ya Habari na Masoko; Hamad Yahya Juma (Mwenyekiti), Naibu Waziri January Makamba (Makamu Mwenyekiti), Tido Mhando, Yusuf Manji, Yusuf Bakhresa, Samwel Nyalla, Jack Gotham, Fredrick Mwakalebela, Juma Pinto.

Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji; Advocate Richard Sinamtwa (Mwenyekiti), Advocate Moses Kaluwa (Makamu Mwenyekiti), Zacharia Hans Poppe, Hussein Mwamba, Philemon Ntahilaja, Abdul Sauko, Imani Madega.

Kamati ya Ukaguzi wa Fedha; Ramadhan Nassib (Mwenyekiti), Zitto Kabwe (Makamu Mwenyekiti), Nicholas Magarinza, Jackson Songora, Epaphra Swai, Kalilo Samson, Goodluck Moshi, Golden Sanga, Elias Mwanjala.

Kamati ya Tiba; Dk. Paul Marealle (Mwenyekiti), Dk. Fred Limbanga (Makamu Mwenyekiti), Dk. Mwanandi Mwankemwa, Dk. Nassoro Matuzya, Dk. Eliezer Ndelema, Asha Sadick.

Kamati ya Mpira wa Miguu wa Ufukweni; Ahmed Idd Mgoyi (Mwenyekiti), Shaffih Kajuna Dauda (Makamu Mwenyekiti), Boniface Pawasa, Deo Lucas, Juma Mgunda, John Kanakamfumu, John Mwansasu.

AD HOC COMMITTEES
Kamati ya Kutathimini Muundo wa Ligi; Dk. Mshindo Msolla (Mwenyekiti),Idd Mshangama (Katibu), Rahim Kangezi, Amri Said, Sunday Manara, Salim Bawazir, Lucas Kisasa.

Kamati ya Kutathimini Muundo wa Bodi ya Ligi; David Nchimbi (Mwenyekiti), Edwin Kidifu, Jones Paul Evans Aveva, John Jambele, Masoud Sanani, Pelegrinius Rutayuga.

Friday, February 7, 2014

TAMBWE AINUSURU SIMBA


KASI ya Simba kukwea kileleni mwa msimamo wa ligi kuu ya soka ya Tanzania Bara jana ilipunguzwa baada ya kulazimishwa kutoka sare ya bao 1-1 na Mtibwa Sugar katika mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Hata hivyo, sare hiyo imeiwezesha Simba kuchupa nafasi ya tatu ikiwa na pointi 31 baada ya kucheza mechi 16, sawa na Mbeya City, lakini ipo mbele kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa. Mtibwa inaendelea kushika nafasi ya tano ikiwa na pointi 22.

Mtibwa ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 10 lililofungwa na mshambuliaji wa zamani wa Simba, Mussa Hassan 'Mgosi' kutokana na uzembe wa kipa Ivo Mapunda.

Simba ilipata nafasi nzuri ya kufunga bao dakika ya 17 wakati Amri Kiemba alipounganisha kwa kichwa mpira wa adhabu uliopigwa na Issa Rashid, lakini ulitoka nje. Timu hizo zilikwenda mapumziko Mtibwa ikiwa mbele kwa bao 1-0.

Mtibwa ilicheza vizuri katika kipindi cha kwanza huku viungo wake Jamal Simba, Shabani Kisiga na Juma Luizio wakitawala dimba la kati. Katika kipindi hicho, Simba ilionekana kupoteza mawasiliano japokuwa uwanja uliwasumbua kwa kuwa mpira haukuwa ukitulia.

Kipindi cha pili kilianza kwa Simba kubadili staili ya mchezo, ambapo ilicheza pasi ndefu na kufanya mashambulizi kadhaa kwenye lango la Mtibwa na hatimaye kupata bao dakika ya 50 lililofungwa na Hamisi Tambwe.

Mtibwa ilipata pigo dakika ya 69 baada ya kiungo wake, Shaaban Nditi kuonyeshwa kadi ya pili ya njano na kutolewa nje kwa kadi nyekundu na kuifanya timu yake ibaki na wachezaji 10 uwanjani.

AZAM YAPANIA KUWEKA REKODI


WAWAKILISHI wa Tanzania katika mashindano ya Kombe la Shirikisho Afrika, Azam watawakosa nyota wao wanne katika mechi ya awali dhidi ya Ferroviario de Beira ya Msumbuji, itakayochezwa Jumapili kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam.

Nyota wa Azam watakaokosekana katika mechi hiyo ni pamoja na mshambuliaji hatari, John Bocco na beki Hajji Nuhu, ambao ni majeruhi. Wengine ni chipukizi Ismail Lugambo na Farid Musa.

Ofisa Habari wa Azam, Jaffari Iddi alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, Bocco bado majeruhi wakati Nuhu aliumia goti juzi baada ya kuanguka ghafla wakati wa mazoezi yaliyofanyika Chamazi.

Jaffari alisema Lugambo alivunjika mguu mwishoni mwa wiki iliyopita wakati wa mechi ya kirafiki kati ya Azam na Ashanti wakati Farid amekuwa akisumbuliwa na majeraha mara kwa mara na itabidi afanyiwe vipimo vikubwa.

"Farid itabidi afanyiwe vipimo vya MRY kwenye mgongo ili tujue sababu ya kuumia mara kwa mara na Bocco bado goti lake halijawa sawa. Alipewa mapumziko ya wiki mbili na tayari ameshamaliza wiki moja, hivyo hatacheza mchezo huo," alisema Jaffari.

Pamoja na kuwakosa nyota hao, Jaffari alisema wamejiandaa vizuri kwa ajili ya mechi hiyo dhidi ya Ferroviario na kusisitiza kuwa, wamepania kuweka rekodi ya kufika mbali zaidi kuliko ilivyokuwa mwaka jana.

Aliongeza kuwa, wamefurahi kupata ruhusa kutoka kwa Shirikisho la Soka Afrika (CAF) ya kucheza mechi hiyo kwenye uwanja wa Chamazi kwa vile wachezaji wao wameuzoea na watautumia vizuri kupata ushindi.

Msimu uliopita, Azam iliiwakikisha Tanzania katika mashindano hayo baada ya kumaliza ligi kuu ikiwa mshindi wa pili, lakini ilitolewa raundi ya tatu. Iwapo Azam itaitoa Ferroviario,  itamenyana na mshindi kati ya St. Michel ya Shelisheli na ASSM Elgeco Plus ya Madagacar

Wakati huo huo, timu za KMKM na Chuoni za Zanzibar, zinaondoka nchini kwenda Ethiopia na Zimbabwe kwa ajili ya mechi zao za michuano ya klabu za Afrika.

KMKM imepangwa kumenyana na Dedebit ya Ethiopia mwishoni mwa wiki hii katika mechi ya michuano ya klabu bingwa itakayochezwa mjini Addis Ababa wakati Chuoni itamenyana na How Mine ya Zimbabwe katika mechi ya Kombe la Shirikisho, itakayochezwa mjini Harare.

KMKM ilitarajiwa kuondoka jana jioni kwenda Ethiopia kwa ndege ya Shirika la Ndege la Ethiopia wakati Chuoni inatarajiwa kuondoka leo alfajiri kwenda Zimbabwe kwa ndege ya Shirika la Ndege la Zimbabwe.

OKWI, CHUJI KUWAKOSA WACOMORO


UONGOZI wa klabu ya Yanga, umesema hauna uwezo wa kumtumia mshambuliaji, Emmanuel Okwi, licha ya Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF), kutoa leseni ya kucheza michuano ya klabu bingwa mwaka huu.

Akizungumza jana na waandishi wa habari kwenye makao makuu ya klabu hiyo mjini Dar es Salaam, Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto, alisema hadi jana walikuwa wakifuatilia kwenye mtandao wa CAF kuona iwapo kuna pingamizi lolote kwa mchezaji huyo.

Yanga inatarajiwa kushuka dimbani keshokutwa kumenyana na Komorozine de Domoni kutoka Comoro katika mechi ya awali ya michuano ya klabu bingwa Afrika itakayopigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Kizuguto, alisema kwenye mfumo wa usajili wa Okwi, wamegundua hakuna dosari yoyote kwa vile walifuata taratibu zote, ikiwemo kuzungumza na mchezaji na kisha klabu ya Villa ya Uganda, ambayo imetoa ruhusa ya kusajiliwa kwa mchezaji huyo.

Hata hivyo, Kizuguto alisema wanaendelea kusubiri taarifa kutoka Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kama litatoa baraka zake kwa mchezaji huyo kuichezea Yanga katika michuano hiyo na ligi kuu msimu huu.

Okwi alisajiliwa na Yanga mwaka jana kutoka SC Villa baada ya kugoma kuendelea kuichezea Etoile du Sahel ya Tunisia, iliyomsajili kwa mkataba wa miaka minne kuanzia Januari mwaka juzi kutoka Simba SC ya Tanzania.

Nyota huyo wa Uganda, alifungua kesi Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), akilalamika kutolipwa mishahara ya miezi mitatu na Etoile, ndipo akaruhusiwa kujiunga na SC Villa ya Uganda, ambayo baadae ilimuuza kwa Yanga.

Hata hivyo, baada ya Villa kumuuza Yanga ikidai ina haki zote, TFF imeandika barua FIFA kutaka ufafanuzi kama inaweza kumuidhinisha Mganda huyo kucheza timu ya Jangwani na wakati huo huo imeizuia klabu hiyo kumtumia hadi majibu yapatikane.

Hadi sasa Etoile haijailipa Simba SC dola za Marekani 300,000 za manunuzi ya mchezaji huyo na Wekundu hao wa Msimbazi nao wamefungua kesi FIFA.    

"Sheria inasema kabla ya kumsajili mchezaji inabidi mkubaliane, tulifanya hivyo na kisha tukazungumza na viongozi wa Villa na kisha tukatuma jina na mambo muhimu CAF, usajili wake umekamilika, kama kungekuwa na pingamizi tusingeweza kupata system na password," alisema Kizuguto.

Amesema baada ya kipindi cha pingamizi kupita, Okwi aliwekewa pingamizi baada ya siku 37 kwenye Shirikisho la Soka nchini, kitu ambacho nina imani CAF hawana taarifa nacho.

Kauli ya kiongozi huyo, imekuja siku chache baada ya Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya TFF, kusimamisha usajili wa mshambuliaji huyo Yanga hadi FIFA itakapotoa ufafanuzi.

Shirikisho hilo, limechukua uamuzi huo, baada ya kubaini kuwa Okwi, aliruhusiwa kuichezea SC Villa ya Uganda kwa kibali maalumu cha miezi sita kutoka FIFA.

FIFA inazo kesi tatu mkononi za mchezaji huyo, ikiwemo ya kuishitaki Etoile  kwa kutomlipa mshahara wakati Etoile nayo imemshitaki mchezaji huyo kwa utoro.
Simba nayo imeishitaki Etoile wa kushindwa kuilipa ada ya mauzo ya mchezaji huyo ambayo ni dola za Marekani 300,000 (sh. milioni 480).

ATHUMAN IDD 'CHUJI'
Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto, amesema kiungo wao mahiri, Athuman Idd 'Chuji' ataukosa mchezo wa keshokutwa dhidi ya Wacomoro kutokana na kukabiliwa na adhabu ya kadi nyekundu aliyopewa katika mchezo kati ya Yanga na Zamalek ya Misri.

Kizuguto alisema jana kuwa, wamepokea taarifa kutoka Shirikisho la Soka Barani Afrika(CAF), likiwakumbusha kuacha kumtumia nyota huyo kwenye mchezo huo kwa vile alipewa kadi nyekundu.

Yanga ilishiriki na kutolewa raundi ya kwanza katika michuano ya klabu bingwa Afrika
mwaka 2012 baada ya kufungwa na Zamalek ya Misri. Katika mechi ya kwanza,
walilazimishwa sare ya 1-1 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na katika mechi ya marudiano walifungwa bao 1 – 0 mjini  Cairo.

SEIF AHMED'MAGARI'
Mwenyekiti wa mashindano ya kimataifa wa klabu ya Yanga, Seif Ahmed 'Magari', amesema wana imani na kikosi chao dhidi ya Komorozine de Domoni.

Magari alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, tayari wameshagawa kazi kwa kamati yake, ambapo wakimaliza mchezo wa marudiano, watahakikisha wanaanza kuifuatilia timu ya Al Ahly ya Misri ili kujua mbinu zao zote.

Kiongozi huyo alisema wamejipanga kuweka historia barani Afrika mwaka huu kwa vile kikosi chao kimekamilika kila idara baada ya kufanya usajili kwa umakini mkubwa.

Ameongeza kuwa, lengo lao ni kuona Yanga inavuka vikwazo vya timu za Misri na kusonga mbele katika michuano hiyo.

"Tunajua wazi kwamba waarabu wanajua mbinu za kusaka ushindi nje ya mchezo, lakini tutatuma watu kufahamu mbinu zao na mahali ambapo Yanga ikienda Misri itafikia,"alisema.

WAAMUZI
Shirikisho la Soka Barani Afrika( CAF), limeteua waamuzi kutoka Somalia kuchezesha mechi kati ya Yanga na Wacomoro itakayofanyika keshokutwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mwamuzi wa kati atakuwa Hassan Mohamed Hagi wakati wasaidizi wake ni Hamza Hagi Abdi, Bashir Abdi Suleiman na Bashir Olab Arab. Kamishna wa mechi hiyo atakuwa Eugene Musoke kutoka Uganda.

VIINGILIO
Uongozi wa Yanga umetangaza viingilio vya mechi ya klabu bingwa Afrika itakayoikutanisha Yanga na Comorozine de Domoni ya Comoro, ambapo kiingilio cha chini kitakuwa sh. 5,000.

Akizungumza mjini Dar es Salaam jana, Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto, alisema kiingilio cha juu katika mechi hiyo ni VIP A sh.30,000, VIP B na C Sh. 20,000, viti vya rangi ya chungwa sh. 10,000 na viti vya kijani sh.5,000.

Alisema Klabu ya Yanga imetengeneza tiketi 45,000 ambapo katika VIP A kuna tiketi 500, VIP B na C tiketi 4,500, viti vya rangi ya chungwa tiketi 7,000 na viti vya kijani tiketi 33,000.

Alisema tiketi hizo, zitapatikana katika vituo 10 ikiwemo makao makuu ya klabu hiyo Jangwani, Olicom Buguruni, Stears, Oilcom Ubungo, Kimara Mwisho, Uwanja wa Uhuru, Shule ya Benjamin Mkapa pamoja na Uwanja wa Taifa.
 
Tiketi hizo, zitaanza kuuzwa kesho asubuhi na siku ya mchezo, ambapo zitapatikana mpaka saa tano asubuhi.Kizuguto amewataka mashabiki wa Yanga kufika kwa wingi uwanjani kuishangilia timu hiyo ambayo mechi hiyo itakuwa muhimu kushinda.

Tuesday, February 4, 2014

MAKOCHA 40 KUSAKA VIPAJI VYA KUIBORESHA STARS



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeteua kikosi cha makocha 40 kutoka
sehemu mbalimbali, Tanzania Bara na Zanzibar ili kung’amua vipaji katika mpango wa
kuboresha timu ya Taifa (Taifa Stars).

Makocha hao ambao watafanya kazi hiyo katika michuano maalumu ya mikoa wanatakiwa
kuripoti katika ofisi za TFF siku ya Jumamosi (Februari 8 mwaka huu) saa 4 asubuhi kwa
ajili ya kupewa maelekezo zaidi.

Walioteuliwa ni Abdallah Hussein (Kilimanjaro), Abdul Mingange (Dar es Salaam), Ali
Bushiri (Zanzibar), Ali Mayay (Dar es Salaam), Ally Mtumwa (Arusha), Ayoub Selemani
(Zanzibar), Boniface Pawasa (Dar es Salaam), Dan Korosso (Mbeya), Dk. Mshindo Msolla
(Dar es Salaam) na Edward Hiza (Morogoro).

Elly Mzozo (Dar es Salaam), Fred Minziro (Dar es Salaam), George Komba (Dodoma),
Hafidh Badru (Zanzibar), Hamimu Mawazo (Mtwara), Idd Simba (Mwanza), Jabir
Seleman (Zanzibar), John Tegete (Mwanza), Juma Mgunda (Tanga) na Kanali mstaafu
Idd Kipingu (Dar es Salaam).

Kenny Mwaisabula (Dar es Salaam), Khalid Abeid (Dar es Salaam), Madaraka Bendera
(Arusha), Madaraka Selemani (Dar es Salaam), Mbarouk Nyenga (Pwani), Mohamed
Mwameja (Dar es Salaam), Musa Kissoki (Dar es Salaam), Nicholas Mihayo (Dar es
Salaam), Patrick Rweyemamu (Dar es Salaam) na Peter Magomba (Singida).

Peter Mhina (Songea), Salvatory Edward (Dar es Salaam), Salum Mayanga (Morogoro),
Sebastian Nkoma (Dar es Salaam), Sekilojo Chambua (Dar es Salaam), Shaban
Ramadhan (Zanzibar), Steven Nemes (Dar es Salaam), Sunday Manara (Dar es Salaam),
Tiborowa Jonas (Dar es Salaam), Yusuf Macho (Dar es Salaam), Zamoyoni Mogela (Dar
es Salaam),

QUALITY GROUP YAIPIGA JEKI TFF
Kampuni ya Quality Group Limited imetoa sh. milioni 10 kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu
Tanzania (TFF) kwa ajili ya kuunga mkono mikakati ya shirikisho la katika kuendeleza
mpira wa miguu nchini.

Mchango huo wa Quality Group utatumika katika programu mbalimbali za kuendeleza
mpira wa miguu nchini ambapo tunaishukuru kampuni hiyo kwa kuunga mkono mikakati
yetu.

TFF YASIMAMISHA MATUMIZI YA TIKETI ZA ELEKTRONIKI



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limesitisha matumizi ya tiketi za elektroniki kwenye viwanja vyote vyenye huduma hiyo ili kutoa fursa ya kufanyika tathmini ya kina kabla ya kuendelea tena.

Uamuzi huo umefikiwa kwa kuzingatia sababu mbalimbali baada ya kikao kati ya Sekretarieti ya TFF na maofisa wa benki ya CRDB kilichofanyika jana (Februari 3 mwaka huu) katika ofisi za Shirikisho.

Tathmini hiyo inafanyika ili kubaini changamoto zilizojitokeza na kuzitafutia ufumbuzi kabla ya kuendelea tena na matumizi hayo, kubwa ikiwa ni hadhari iliyotolewa na vyombo vya Usalama juu ya misongamano inayotokea uwanjani kutokana na kutokuwepo mtiririko mzuri wa uingiaji.

Tayari zipo changamoto za wazi ikiwemo uelewa wa washabiki wa jinsi ya kununua na kutumia tiketi hizo, milango michache ya kuingilia uwanjani na washabiki wengi kununua tiketi dakika za mwisho hivyo kuchangia misongamano.

YANGA YAWAJIA JUU WANAOIHUJUMU

       
 
Hivi karibuni kumekuwa na madai ya kutoridhishwa na mwenendo wa timu, taarifa za hujuma ndani ya timu yetu ya mpira, uongozi na baadhi ya wanachama.
Ni haki na ni kwa nia njema tu ya wanachama kuhoji mwenendo wa timu yao pale wanapoona-hairidhishi, Ni wajibu wa wanachama kuchanganua mawazo mema na mabaya. 
 
Ushindi au mwenendo mzuri wa timu unatokana na viwango vizuri, nidhamu na ushirikiano wa wahusika wote, Wachezaji, Walimu, Viongozi, Wanachama na wapenzi kwa ujumla.
 
Uongozi ulikutana na wachezaji, walimu, baadhi ya wanachama na wapenzi na kuyazungumzia na kukubaliana kuhusu mapungufu yaliyojitokeza kwa wahusika wote na kuchukua hatua ya kubadilisha technical bench yote na kutoa adhabu na onyo kali kwa baadhi ya wachezaji walionyesha utovu wa nidhamu kwa kipindi kilichopita.
 
Inasikitisha kuona kuwa baadhi ya wadau kwa kutumia vyombo vya habari wanachochea na kutengeneza uhasama ambao kwa kweli haupo ama kwa faida zao binafsi, au kwa kutumiwa na watu wa nje kutuvuruga na kuondoa amani klabuni.
 
Habari zilizoandikwa na moja ya gazeti maarufu za kusema Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Kimataifa Ndugu Seif Ahmed kuwa si mwanachama halali wa YANGA, eti anahujumu timu na yupo kwa maslahi yake binafsi ni za uzushi na hazina ukweli wowote.
 
Habari hizi zimelenga kuwakatisha tamaa na kuwavunja moyo viongozi wetu ambao wapo mstari wa mbele katika kujenga YANGA. Watu hawa ni hatari sana na hawaitakii merna YANGA na wanafanya hujuma hizi kwa malengo ya kuwapandikiza viongozi vibaraka wa kuidhoofisha timu yetu na kutimiza malengo yao binafsi.
 
Uongozi ungependa kutoa tahadhari kwa wanachama kuwa hizo ni mbinu chafu ambazo zimelenga kutudhoofisha na kutusambaratisha.
 
Wachochezi hawa kwa nyakati tofauti wamekuwa pia wakutuma ujumbe wa simu wenye vitisho na matusi kwa kiongozi huyu na baadhi ya viongozi wenzake.
 
Tunatoa onyo kwa wale wote wanaotuma ujumbe wa simu wenye uchochezi na matusi, kwamba hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao mara watakapofanya hivyo tena.
 
Tunawaomba wadau wote wanamichezo na hasa wahariri wa michezo kudhibiti matumizi mabaya ya watu au vyombo vya habari yanayochangia sana kuzorotesha michezo nchini.
 
Uongozi unawaomba Wana Yanga kutulia na kutoa ushirikiano katika kupambana na njama hizi ambazo zinawe a kutudhoofisha tusipokuwa waangalifu ili tushindwe kufikia malengo yetu.
 
YANGA DAIMA MBELE NYUMA MWIKO
 
Yusuf Manji
Mwenyekiti wa Yanga

RAIS WA TFF ATEMBELEA RUANGWA


Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi ametembelea Chama cha Mpira wa Miguu Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.

Katika ziara hiyo aliyoifanya jana (Februari 2 mwaka huu), pia alikuwa mgeni rasmi mechi ya kugombea Kombe la Majaliwa kati ya Hull City na Mbagala City, na kuahidi kuwa TFF itaandaa kozi za awali za ukocha na uamuzi kwa Wilaya ya Ruangwa.

RAMBIRAMBI MSIBA WA OMARI CHANGA
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha aliyekuwa mchezaji wa Vijana, Moro United na Yanga, Omari Changa kilichotokea juzi (Februari 1 mwaka huu) jijini Dar es Salaam.

Msiba huo ni mkubwa katika familia ya mpira wa miguu kwani Changa wakati wake uwanjani akichezea timu mbalimbali, alitoa mchango mkubwa ambao tutaukumbuka daima.

TFF tunatoa pole kwa familia ya marehemu Changa, klabu ya Moro United na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.

Katika maziko, TFF itawakilishwa na mjumbe wa Kamati ya Utendaji, Kidao Wilfred, na imetoa rambirambi ya sh. 200,000.

MASHABIKI MBARONI KWA TIKETI FEKI


Mshabiki mmoja anashikiliwa na Jeshi la Polisi akidaiwa kukutwa na tiketi bandia kwenye mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya Yanga na Simba iliyochezwa jana (Februari 2 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Matei Cosmas (28) ambaye ni mkazi wa Buza Njiapanda Kitunda, Dar es Salaam amefunguliwa jalada namba CHA/IR/900/2014 kwenye Kituo cha Polisi Chang’ombe akidaiwa kupatikana na tiketi bandia.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) leo asubuhi (Februari 3 mwaka huu) limeamkia Kituo cha Polisi Chang’ombe kusaini hati ya maelezo dhidi ya mtuhumiwa.

Ni imani ya Shirikisho kuwa mtuhumiwa atachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria za nchini.

Tunatoa mwito kwa washabiki wa mpira wa miguu kuepuka kununua tiketi kutoka mikononi mwa watu, kwani kufanya hivyo ni kosa. Tiketi zinauzwa kwenye sehemu maalumu zenye chapa ya TFF.

Monday, February 3, 2014

SIMBA YAPELEKA KIKOSI CHA MAUAJI MOROGORO, KUIVAA MTIBWA J'TANO


TIMU ya Soka ya Simba leo (Februari 3), imeondoka jijini kuelekea mjini Morogoro tayari kwa pambano lake la Ligi Kuu dhidi ya Mtibwa Sugar litakalofanyika keshokutwa (Februari 5) katika Uwanja wa Jamhruri, Morogoro.

Timu hiyo imeondoka ikiwa na kikosi cha wachezaji 22 na viongozi watano ambapo kitapiga kambi katika hoteli ya Mount Usambara kujiandaa na mchezo huo ambapo kitakuwa ikifanya mazoezi katika Uwanja wa Jamhuri.

Kwa mujibu wa Daktari wa timu hiyo, Yassin Gembe, wachezaji wote wako katika hali nzuri na hakuna majeruhi hata mmoja isipokuwa Nassor Chollo anaeendelea na matibabu ya nyonga ya kushoto pamoja na Gilbert Kaze anayesumbuliwa na goti na kutakiwa kupumzika kwa wiki moja. Pia mchezaji Haruna Shamte aliyekuwa akitumikia adhabu ya kadi tatu za njano atakuwemo katika msafara huo.

Akizungumza mda mfupi kabla ya kuondoka, Kocha Mkuu wa timu hiyo, Zdravko Logarusic alisema wanaelekea mjini Morogoro wakitarajia kupanda upinzani kutoka kwa Mtibwa kwa vile kila timu inazihitaji pointi ili kuweza kujiimarisha katika msimamo wa ligi hiyo.

Alisema licha ya kutarajia upinzani ana matarajio makubwa ya ushindi katika mchezo huo kwa vile amekiandaa kikosi chake kwa ajili ya kupambana katika kutafuta ushindi.

Wachezaji walioondoka jana ni Ivo Mapunda, Yaw Berko, Abuu Hashim, William Lucian, Issa Rashid, Joseph Owino, Donald Mosoti, Jonas Mkude, Haruna Chanongo, Awadh Juma, Amri Kiemba, Amisi Tambwe, Ramadhani Singano.

Wengine ni Henry Joseph, Abdulhalim Humud, Uhuru Selemani, Said Ndemla, Ramadhani Chombo, Gilbert Kaze, Haruna Shamte, Betram Mwombeki na Ali Badru.

Makocha ni Logarusic, Selemani Matola, Idd Pazi, Meneja Nicco Nyagawa, Daktari Yassin Gembe na Mkuu wa Msafara ambaye ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo, Said Pamba.

TFF YAADHIMISHA MIAKA 50 NDANI YA FIFA


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) litaadhimisha miaka 50 tangu lipate uanachama wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (TFF) kwa shughuli mbalimbili ikiwemo michezo na makongamano.

Kamati maalumu itaundwa kwa ajili ya kupanga na kuratibu shughuli hiyo ambayo TFF imepanga kuadhimisha nchini nzima kwa kutumia wanachama wake.

TFF wakati huo ikiitwa Chama cha Mpira wa Miguu Tanzania (FAT) ilijiunga na FIFA Oktoba 8, 1964.

TFF YAPATA HATI YA KIWANJA TANGA
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepata hati ya kiwanja chake kilichopo eneo la Mnyanjani katika Jiji la Tanga.

Hati hiyo ya miaka 99 ya kiwanja hicho namba 75 Block D chenye ukubwa wa ekari 7.6 ilikabidhiwa kwa TFF, Januari 13 mwaka huu.

Kiwanja hicho kitaendelezwa kwa matumizi mbalimbali, kubwa ikiwa ni uwanja wa mpira wa miguu.

YANGA, MBEYA CITY ZAINGIZA MIL 175/-


Pambano la Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya wenyeji Yanga na Mbeya City lililofanyika jana (Februari 2 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam limeingiza sh. 175,285,000.

Watazamaji 30,411 walikata tiketi kushuhudia mechi hiyo kwa viingilio sh. 5,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 kwa VIP A. Yanga ndiyo iliyoibuka na ushindi wa bao 1-0.

Mgawanyo wa mapato ulikuwa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) sh. 26,738,389.83, gharama za kuchapa tiketi sh. 2,919,200 wakati kila klabu ilipata sh. 42,960,086.50.

Uwanja sh. 21,844,111.53, gharama za mechi sh. 13,106,466.92, Bodi ya Ligi sh. 13,106,466.92, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 6,553,233.46 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 5,096,959.36.

Nayo mechi ya Simba na Oljoro JKT iliyochezwa Februari 1 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 47,705,000 ambapo kila timu imepata sh. 11,254,122 kutokana na watazamaji 8,267.

Mgawanyo mwingine katika mechi hiyo iliyomalizika kwa Simba kushinda mabao 4-0 ni Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) sh. 7,277,033.90 na gharama za kuchapa tiketi sh. 2,278,400.

Uwanja sh. 5,722,434.92, gharama za mechi sh. 3,433,460.95, Bodi ya Ligi sh. 3,433,460.95, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 1,716,730.47 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 1,335,234.81.

SIMBA WAANZA MKAKATI WA UJENZI WA UWANJA


Na Asha Muhaji, Bunju
VIONGOZI na wanachama wapatao 50 wa Klabu ya Simba jana walitembelea eneo la mradi wa uwanja wao ulioko Bunju ‘B’ jijini Dar es Salaam.

Katika ziara hiyo, wanachama hao walifanya kazi ya kulisafisha eneo hilo kwa kufyeka ikiwa ni hatua za awali za kutaka kuuendeleza, ambalo linakadiriwa kuwa na eka 25.

Lengo la kufanya ziara pamoja na kusafisha eneo hilo ni mkakati wa klabu hiyo, kutaka kuanza rasmi mipango ya uendelezaji wa eneo hilo.

Katibu mpya wa Simba SC, Ezekiel Kamwaga mwenye skafu akizungumza na wanachama wa klabu hiyo katika eneo la kiwanja cha klabu yao, Bunju B, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam jana.

Eneo hilo linatarajiwa kujengwa uwanja wa mpira utakaokuwa ukimilikiwa na klabu hiyo, pamoja na majengo mengine muhimu yatakayoendana na sura ya kimichezo.

Katika hatua za awali, klabu hiyo imepanga kufyeka pamoja na kupitisha greda lengo likiwa ni kusafisha eneo hilo tayari kwa ujezi wa uwanja utakaoweza kutumiwa na timu yake kwa ajili ya mazoezi na mechi nyingine za kirafiki.

Katibu Mkuu wa Simba, Ezekiel Kamwaga ameahidi mpaka kufikia Aprili mwaka huu eneo hilo litakuwa na sura ya kiwanja cha michezo huku jitihada zingine zikiendelea kufanywa na uongozi kwa ajili ya mradi mkubwa wa kituo hicho ambacho hapo baadaye utahusisha hosteli ya wachezaji, mgahawa, gym pamoja na bwawa la kuogelea.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu, mpango wa awali utahusisha kuzungusha uzio eneo lote pamoja na ujenzi wa uwanja wa kuchezea mpira.

Kamwaga alisisitiza mradi wa ujenzi mkubwa wa eneo hilo bado unafanyiwa kazi na uongozi wa klabu hiyo ili kumpata  mkandarasi atakayesimamia ujenzi huo na mipango itakapokuwa tayari basi itawekwa wazi isipokuwa kwa sasa wanachofanya ni hatua za awali za uendelezaji wa eneo hilo.

YANGA YAITOA NISHAI MBEYA CITY



YANGA jana ilivuna pointi zote tatu kutoka kwa Mbeya City baada ya kuichapa bao 1-0 katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Pamoja na ushindi huo, Yanga imebaki nafasi ya pili katika msimamo wa ligi hiyo ikiwa na pointi 35 baada ya kucheza mechi 16, ikiwa nyuma ya vinara Azam, wanaoongoza kwa kuwa na pointi 36.

Azam iliendelea kujikita kileleni mwa ligi hiyo baada ya jana kutoa kipigo kikali cha mabao 4-0 kwa Kagera Sugar katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam.

Bao pekee na la ushindi la Yanga lilifungwa na mshambuliaji, Mrisho Ngasa dakika ya 16 baada ya krosi ya David Luhende kuokolewa vibaya na beki mmoja wa Mbeya City na mpira kumkuta mfungaji.

Mbeya City ililazimika kumaliza mchezo huo ikiwa na wachezaji 10 baada ya kiungo Steven Mazanda kutolewa nje kwa kadi nyekundu kwa kosa la kutoa lugha chafu kwa mwamuzi.

Yanga: Deogratius Munishi ‘Dida’, Mbuyu Twite/Juma Abdul dk63, Oscar Joshua, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Frank Domayo, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Didier Kavumbangu/Hamisi Kiiza dk70, Mrisho Ngassa na David Luhende.

Mbeya City: David Burahn, John Kabanda, Hassan Mwasapili, Deogratius Julius, Yussuf Abdallah, Anthony Matogolo, Mwagane Yeya/Saad Kipanga dk75, Steven Mazanda, Paul Nonga/Richard Peter dk63, Peter Mapunda na Deus Kaseke/Joseph Willson dk70.

TARIMBA KUONGOZA KAMATI YA NIDHAMU TFF



KAMATI ya Utendaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imefanya uteuzi wa wajumbe kuunda kamati mbili za awali za haki, na kamati mbili za rufani za vyombo hivyo.

Rais wa zamani wa Yanga, Tarimba Abbas ambaye pia kitaaluma ni mwanasheria ataongoza Kamati ya Nidhamu. Wajumbe wanaounda kamati hiyo ni Wakili Jerome Msemwa (Makamu Mwenyekiti), Kassim Dau, Nassoro Duduma na Kitwana Manara.
 Kamati ya Rufani ya Nidhamu inaendelea kuongozwa na Profesa Mgongo Fimbo wakati makamu wake ni Wakili Hamidu Mbwezeleni. Wajumbe wengine wa kamati hiyo ni Titus Bandawe, Twaha Mtengera na Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) mstaafu Boniface Mpaze.

Mkurugenzi Mkuu wa PPF, William Erio ambaye pia kitaaluma ni mwanasheria anaongoza Kamati ya Maadili. Wajumbe ni Wakili Ezekiel Maganja, Wakili Victoria Mandari, Kanali mstaafu Enos Mfuru na Mbunge wa Jimbo la Mtama mkoani Lindi, Said Mtanda.

Kamati ya Rufani ya Maadili inaundwa na Jaji mstaafu Stephen Ihema (Mwenyekiti), Wakili Alesia Mbuya (Makamu Mwenyekiti), Lilian Kitomari, Jabir Shekimweri na Chabanga Hassan Dyamwale.

Wakati huo huo: TFF imeagiza kifanyike kikao cha dharura kati ya Sekretarieti ya TFF, Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) na benki ya CRDB ili kutathimini maendeleo ya matumizi ya tiketi za elektroniki.

Lengo la kikao hicho ni kutathimini maendeleo ya utekelezaji wa mfumo huo wa tiketi za elektroniki ni kutafuta ufumbuzi pamoja changamoto zake.

Viwanja vinane nchini vimefungwa mfumo huo wa tiketi za elektroniki. Viwanja hivyo ni Uwanja wa Azam uliopo Chamazi, Uwanja wa Kaitaba, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Uwanja wa Jamhuri, Morogoro, Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine, Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid, Uwanja wa Mkwakwani, na CCM Kirumba.

Katika hatua nyingine, TFF imeiagiza Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) ifanyie marejeo (review) uamuzi wake wa kuagiza mechi ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) irudiwe mkoani Tabora.

Maagizo hayo yametolewa na Kamati ya Utendaji iliyokutana jana (Februari 1 mwaka huu) baada ya kupokea vielelezo vipya kuhusiana na mechi hiyo iliyochezwa Novemba 22 mwaka jana mjini Shinyanga.

Mechi hiyo iliyochezwa Uwanja wa Kambarage ilivunjwa na mwamuzi dakika ya 87 baada ya kupigwa na wachezaji wa Kanembwa JKT.

Pia Kamati ya Nidhamu ya TFF inatarajiwa kukutana wiki ijayo kujadili tukio hilo la Shinyanga wakiwemo wachezaji wanane wa Kanembwa JKT waliripotiwa kumpiga mwamuzi wa mechi hiyo.

SIMBA YAIGAGADUA JKT OLJORO



SIMBA imefufua matumaini ya kutwaa ubingwa wa ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kuichapa JKT Oljoro katika mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Katika mechi hiyo, mshambuliaji Hamisi Tambwe aliweka rekodi ya kuifungia tena Simba mabao matatu katika mechi moja na kuzawadiwa mpira. Bao lingine lilifungwa na kiungo Jonas Mkude.

Matokeo hayo yaliiwezesha Simba kuwa na pointi 30 baada ya kucheza mechi 15, ikiwa nafasi ya nne nyuma ya Mbeya City yenye pointi 31, Yanga yenye pointi 32 na Azam yenye pointi 33.

Mshambuliaji machachari wa Simba, Ramadhani Singano 'Messi' aliendelea kudhihirisha makali yake baada ya kutoa pasi nne maridhawa zilizozaa mabao hayo manne.

Kikosi cha Simba SC leo kilikuwa; Ivo Mapunda, William Lucian ‘Gallas’, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Donald Mosoti, Joseph Owino, Jonas Mkude, Haroun Chanongo, Awadh Juma, Amri Kiemba/Uhuru Suleiman dk64, Amisi Tambwe/Abdulhalim Humud na Ramadhani Singano ‘Messi’/Said Ndemla dk55.

JKT Oljoro; Mohamed Ali, Paul Malipesa, Ali, Omar, Nurdin Mohamed, Sabri Makame, Babu Ally, Jacob Masawe, Amir Omar, Shijja Mkina na Majaliwa Mbaga/Shaibu Nayopa dk38

Saturday, February 1, 2014

AZAM KUCHEZA MECHI ZA KIMATAIFA CHAMAZI



Shirikisho la Mpira wa Miguu barani Afrika CAF leo tarehe 31 Januari 2014 limeupa kibali cha kuchezea mashindano ya kimataifa yanayoandaliwa na CAF uwanja wa Azam Complex Chamazi na kuufanya uwanja wa kwanza unaomilikiwa na klabu Afrika Mashariki  kuruhusiwa kuandaa (ku-host) mashindano makubwa ya vilabu

Kwa mujibu wa barua pepe iliyotumwa leo na CAF kupitia kwa naibu mkurugenzi wa mashindano,
Khaled Nassar, Uwanja wa Azam Compex Chamazi umepita vigezo vyote vinavyohitajika na CAF “ku-host” mashindano ya kimataifa hivyo kuanzia tarehe ya leo, uwanja huu unaruhusiwa “ku-host” mech za CAF

Bwana Khaled ameandika katika taarifa yake ya barua pepe kwenda TFF na Azam FC kuwa CAF ilimtuma mkaguzi wake toka nchini Zimbabwe, Wilfried Mukuna kuja kukagua uwanja huu.

Bwana Mukuna aliwasilisha ripoti CAF iliyopelekea shirikisho hilo kutoa kibali kwa Azam FC na TFF kuruhusiwa kuutumia uwanja huu kwa mechi zinazoandaliwa na CAF

Uongozi wa Azam FC unatoa shukrani kwa mkaguzi wa CAF, Mukuna, uongozi wa TFF chini ya Rais Jamal Malinzi, na uongozi wa CAF Cairo Misri hasa Khaled Nasser kwa kuwezesha zoezi hili kufanyika kwa uwazi na uweledi wa hali ya juu uliopelekea uwanja wetu kupata kibali cha kutumika kwenye michezo ya kimataifa.

Azam FC ingependa kuwataarifu wapenzi wake kuwa kuanzia msimu huu mechi zake za  CAF zitachezwa Azam Complex Chamazi

NIYONZIMA, CANNAVARO HAWAKUPIGANA-YANGA


Benchi la Ufundi la klabu ya Young Africans limesikitishwa na taarifa zilizoenea kwenye baadhi ya vyombo vya habari kwamba wachezaji wa Young Africans kiungo Haruna Niyonzima na nahodha Nadir Haroub "Cannavaro" walipigana katika mchezo dhidi ya Coastal Union siku ya jumatano jijini Tanga kuwa hazina ukweli wowote bali ni katika kutaka kuharibu twasira ya timu.

Akiongea na mtandao rasmi wa klabu www.youngafricans.co.tz , kocha msaidizi wa Young Africans Charles Boniface Mkwasa amesema wao benchi la ufundi wameshangazwa na taarifa hizo baada ya kuziona na kuzisoma leo na kusisitiza walioandika wamefanya hivyo kwa ajili ya maslahi yao tu.

Kila mtu alikuwepo uwanjani na aliweza kushuhudia mchezo huo, hakuna aliyeona Cannavaro na Niyonzima wakipigana katika kipindi chote cha dakika 90 za mchezo, nashikwa wasi wasi na waandishi waliokuwepo uwanjani kama walikua makini kufuatilia mchezo na kuandika kitu tofauti na walichokiona.

"Sheria za soka zipo wazi, mchezaji au wachezaji wapigana ndani ya uwanja mwamuzi anawatoa nje ya uwanja kwa kuwapa kadi nyekundu, sasa tumeshangazwa na taarifa hizo zilioripotiwa leo kuwa kuwa kuna wachezaji wetu walipigana ili wachezaji wote walicheza kwa dakika 90 "alisema Mkwasa.

Nadhani imefika wakati tuisaidie jamii kuelewa uhalisia wa jambo husika liliotokea, kwani kuandika tofauti na kilichotokea kunasababisha jamii kuamini/kuelewa jambo ambalo silo lililotokea.

Katika mchezo wowote wachezaji kuelekezana/kukumbushana majukumu ni jambo la kawaida na ndicho kilichotokea katika mchezo dhidi ya Coastal kati ya Cananavaro na Yondani na Niyonzima na Cannavaro na si kama ilivyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari.

"Hata mara baada ya mchezo wachezaji wote walikuwa pamoja na kupeana pole kutokana na ugumu wa mechi, kisha wote kuondoka kuelekea hotelini kupumzika, na sisi kama viongozi hatujaona wachezaji kutofautiana kitu chochote hata kufikia hatua ya kusuruhishwa kama ilivyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari "aliongeza Mkwasa .

Kuhusu maandalizi ya mchezo wa jumapili Mkwasa amesema vijana wake leo wamefanya mazoezi asubuhi kujiandaa na mchezo huo, na hakuna mchezaji majeruhi hata mmoja kwani Hamis Kiiza, Hassana Dilunga waliokuwa wagonjwa wameshaungana wenzao kambini na Athuman Idd "Chuji"  aliyekua amesimamishwa kurejeshwa kundini.

SIMBA, JKT OLJORO KAZI IPO LEO




Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania inaingia raundi ya 16 wikiendi hii kwa mechi nne ambapo leo (Februari 1 mwaka huu) Simba itakuwa mwenyeji wa Oljoro JKT katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Viingilio katika mechi hiyo itakayochezwa kuanzia saa 10 kamili jioni ni sh. 5,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 kwa VIP A. Refa atakuwa Nathan Lazaro kutoka mkoani Kilimanjaro wakati Kamishna ni Hakim Byemba wa Dodoma.

Uwanja wa Azam uliopo Mbagala siku hiyo kutakuwa na mechi kati ya wenyeji Ashanti United na Mgambo Shooting kutoka Handeni mkoani Tanga kwa viingilio vya sh. 3,000 kwa sh. 10,000.

Jumapili (Februari 2 mwaka huu) ni Yanga vs Mbeya City (Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, saa 10 kamili jioni), na Azam vs Kagera Sugar (Uwanja wa Azam Complex, Chamazi saa 10 kamili jioni).

Ligi hiyo itaendelea Jumatano (Februari 5 mwaka huu) kwa mechi kati ya Tanzania Prisons vs Coastal Union (Uwanja wa Sokoine, Mbeya), Mgambo Shooting vs Ruvu Shooting (Uwanja wa Mkwakwani, Tanga), Rhino Rangers vs Oljoro JKT (Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora), na JKT Ruvu vs Ashanti United (Uwanja wa Azam Complex, Chamazi).

SERENGETI BOYS KUKIPIGA NA AFRIKA KUSINI


Timu ya Taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 17 (Serengeti Boys) itacheza na Afrika Kusini katika mechi za mchujo kutafuta tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa umri huo zitakazofanyika mwakani nchini Niger.

Serengeti Boys ambayo pamoja na nchi nyingine 17 zimeingia moja kwa moja katika raundi ya pili itaanzia mechi hiyo nyumbani kati ya Julai 18-20 mwaka huu wakati ile ya marudiano itafanyika nchini Afrika Kusini kati ya Agosti 1-3 mwaka huu.

Ikifanikiwa kuitoa Afrika Kusini, Serengeti Boys itacheza mechi ya raundi ya tatu na ya mwisho na mshindi wa mechi kati ya Misri/Sudan vs Congo Brazzaville.

Nchi nyingine ambazo zimeingia moja kwa moja raundi ya pili ni Afrika Kusini, Angola, Benin, Botswana, Burkina Faso, Congo Brazzaville, Ethiopia, Gabon, Ghana, Ivory Coast, Mali, Morocco, Nigeria, Rwanda, Senegal, Tunisia na Zambia.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) inatarajia kutangaza benchi la ufundi litakaloiongoza Serengeti Boys hivi karibuni.

TFF YATIMIZA SIKU 100


Kamati mpya ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) chini ya Rais Jamal Malinzi, Februari 4 mwaka huu inatimiza siku 100 tangu iingie madarakani katika uchaguzi uliofanyika Oktoba 28 mwaka jana.

Hivyo, Rais Malinzi atazungumza na waandishi wa habari Februari 7 mwaka huu kuelezea utekelezaji wa Ilani yake ya uchaguzi. Muda na mahali utakapofanyika mkutano huo mtaarifiwa baadaye.

BODI YA LIGI YAZIPIGA JEKI KLABU ZA FDL

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imetoa sh. milioni 1.5 kwa kila klabu ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL).

Uamuzi wa kuzisaidia timu hizo ulifanywa katika kikao cha TPLB kilichofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam ambapo fedha hizo zitalipwa kupitia kwenye akaunti za klabu husika. Hivyo klabu ambazo hazijawasilisha akaunti zao TPLB zinatakiwa kuwasilisha haraka.

Klabu za FDL ni African Lyon, Burkina Moro, Friends Rangers, Green Warriors, Kanembwa JKT, Kimondo, Kurugenzi Mafinga, Lipuli, Majimaji, Mkamba Rangers, Mlale JKT na Mwadui.

Nyingine ni Ndanda, Pamba, Polisi Dar es Salaam, Polisi Dodoma, Polisi Mara, Polisi Morogoro, Polisi Tabora, Stand United, Tessema, Toto Africans, Trans Camp na Villa Squad.