KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, April 30, 2010

Capello is the richest managers in British

Fabio Capello not only heads the England team but also leads the list of the richest managers in British and Irish football, it was revealed today.
With an estimated fortune of £34 million, Capello emerged as the wealthiest manager in the The Sunday Times Sport Rich List 2010.
Capello, 63, is believed to be the highest paid England manager in history with a reported £6.5million-a-year contract.
The Italian was wealthy before he took over the England job following successful stints as manager of AC Milan, Roma, Juventus and Real Madrid.
Ipswich boss and former Manchester United midfielder Roy Keane is in second place with £30million.Keane heads a list of wealthy managers with Manchester United connections.
His riches outstrip those of his former boss Sir Alex Ferguson, the long-standing United manager, who, with a fortune of £24 million occupies third spot.
Elsewhere the top 10 is dominated by foreign coaches, and in particular Italians.
Chelsea's Carlo Ancelotti holds fourth spot with £21 million, followed by Republic of Ireland boss Giovanni Trapattoni with £18 million.
Roberto Mancini, manager of Manchester City, is in eighth position with £13million while under-pressure West Ham boss Gianfranco Zola is in joint 10th place with a fortune of £10million.The Sunday Times Sport Rich List Football Managers
1. Fabio Capello (England - wealth estimated at £34 million)
2. Roy Keane (Ipswich Town - £30 million)
3. Sir Alex Ferguson (Manchester United - £24 million)
Lure of the lira: Ireland boss Giovanni Trapattoni
4. Carlo Ancelotti (Chelsea - £21 million)
5. Giovanni Trapattoni (Republic of Ireland - £18 million)
6. Arsene Wenger (Arsenal - £17 million)
7. Sven-Goran Eriksson (Ivory Coast - £16 million)
8. Roberto Mancini (Manchester City, £13 million)
9. Rafa Benitez (Liverpool, £11 million)
10. Steve Bruce (Sunderland), Mark Hughes (Manchester City 2008-09), MartinO'Neill (Aston Villa), Ole Gunnar Solskjaer (Manchester United reserves),Gianfranco Zola (West Ham United) - with estimated £10 million.

WAMBURA: Nitapigania haki yangu hadi mwisho

MGOMBEA nafasi ya mwenyekiti katika uchaguzi mkuu wa Simba, Michael Wambura ambaye ameenguliwa kwenye kinyang'anyiro hicho, ameapa kupigana kufa na kupona kutetea haki yake.
Akizungumza muda mfupi baada ya Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka (TFF), Deogratias Lyatto, kutangaza matokeo ya pingamizi zilizowekwa kwa wagombea.
Wambura alisema anasubiri kupatiwa nakala ya uamuzi wa kuenguliwa kwake, na baada ya hapo atachukua hatua.
"Binafsi sishangazwi na taarifa ambazo zimetolewa leo (jana) na Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF, Lyatto. Kwani kilichokuwa kikiandikwa na vyombo vya habari ndicho hicho kilichotokea," alisema.
Alisema anawasiliana na wanacheria wake kuona nini cha kufanya, ili kumwezesha kuitetea haki yake ambayo inaonekana dhahiri kupokwa na baadhi ya watu kwa maslahi yao binafsi.
Wambura ambaye aliwahi kuwa Katibu Mkuu wa kilichokuwa Chama cha Soka Tanzania (FAT) (sasa Shirikisho la Soka nchini (TFF), alisema tangu mchakato wa upitiaji wa majina ya wagombea ulipoanza katika kamati ya uchaguzi ya Simba alijua kuweko mizengwe.
Alisema kuna watu (hakuwataja majina) ambao walikuwa wakifanya mbinu chafu, ikiwa pamoja na kutumia kiasi kubwa cha fedha ili kumchafua, asipate tiketi ya kuingia kwenye uchaguzi huo.
"Pamoja na kuwa kanuni za uchaguzi zineelekeza tunaweza kukata rufani kwa Kamati ya Rufani ya TFF, sitasema hivyo kwanza. Nasubiri nipate hiyo nakala na kisha nitazungumza na wanasheria wangu," alisema.
Wambura alisema wanasheria wake ndio watakuwa na jukumu la kumweleza nini anapaswa kukifanya, baada ya kutangazwa kuengeliwa kwenye mchakato huo.
"Kuna kipengele cha 'Integrity' (kukosa uaminifu) ambacho mara kwa mara wamekuwa wakikitumia juu yangu, lakini nataka wanielezee zaidi kuhusiana na kitu hicho ambacho kinanichafua mara zote," alisema.
Akijibu swali kama ana mpango wa kulipeleka suala hilo mahakamani, alisema ni mapema mno kwake kuzungumzia jambo hilo.
"Siwezi kuzungumzia suala la kwenda mahakamanin sasa, kwani kulingana na kanuni ya uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ibara ya 12, inaelekeza mgombea kufuata taratibu na kukata rufani kwa Kamati ya Rufaa, kama ikishindikana baadaye Kamati ya Nidhamu ya shirikisho hilo," alisema.
Kuenguliwa kwa Wambura, Zacharia Hans Poppe na Hassan Dalali kwenye nafasi hiyo kumeifanya nafasi hiyo isaliwe na wagombea watatu, ambao ni Hassan Othman'Hassanoo', Andrew Tupa na Ismail Aden Rage.

Wambura, Kaduguda watemwa kugombea Simba


YAMETIMIA. Hatimaye wanachama wawili mashuhuri katika klabu ya Simba, Michael Wambura na Mwina Kaduguda, wametupwa nje ya kinyang'anyiro cha kugombea uongozi katika uchaguzi mkuu ujao.
Kuenguliwa kwa wagombea hao pamoja na wengine wawili, kulitangazwa jana na Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka nchini (TFF), Deogratias Lyatto.
Wambura alikuwa akigombea uenyekiti wa klabu hiyo, wakati Kaduguda alikuwa akiwania nafasi ya Makamu Mwenyekiti.
Kuenguliwa kwa Wambura kunaifanya nafasi ya mwenyekiti sasa kugombewa na watu watatu, Aden Rage ambaye pia aliwekewa pingamizi lakini ameshinda, Hassan Othman 'Hassanoo' na Andrew Tupa, wakati nafasi ya Makamu Mwenyekiti inabaki na mgombea mmoja tu, Geoffrey Nyange 'Kaburu'.
Mgombea mwingine wa nafasi ya mwenyekiti ambaye ameondolewa na kamati ya Lyatto, ni Zacharia Hanspope, na Chano Almasi aliyekuwa akitaka kuwania ujumbe wa Kamati ya Utendaji.
Uchaguzi wa klabu ya Simba utafanyika Mei 9 mwaka huu, katika ukumbi wa Bwalo la Maofisa wa Polisi, Oysterbay.
Akifafanua kuondolewa kwa Wambura, Lyatto alisema kamati yake ilikubaliana na uamuzi uliyotolewa na kamati za uchaguzi na rufani za TFF wa mwaka 2008,ambao ulionyesha mgombea huyo hakukidhi matakwa ya ibara ya 29 (7) ya katiba ya TFF na ibara ya 9 ya kanuni za uchaguzi wa wanachama wa shirikisho hilo, wakati alipowania nafasi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa TFF.
"Hivyo kulingana na uamuzi uliotolewa na kamati hizo za rufani na uchaguzi za TFF, kamati yangu imemwondoa mgombea huyo," alisema.
Wakati huo Wambura aliondolewa kwa kigezo cha kutokidhi kipengele kinachohusiana na uaminifu.
Akimzungumzia Kaduguda, aliyewekewa pingamizi na mwanachama Asha Kigundula, alisema kamati imebaini hakutimiza wajibu kulingana na katiba ya Simba, ibara ya 19, kifungu namba 3,4,5,6,7,8 na ibara ya 21 kifungu f,g,h,i na ibara ya 38 kifungu namba 4,5,6 na 7.
"Baada ya kupitia pingamizi hiyo ya Asha, kamati imeridhika kuwa Kaduguda ameshindwa kukidhi matakwa ya kanuni za uchaguzi za wanachama wa TFF, ibara ya 9. Hivyo kamati imemwondoa mgombea kwenye mchakato," alisema.
Lyatto alisema Chano Almasi ambaye pia aliwekewa pingamizi na Asha, kamati yake imebaini na kuridhika kuwa mgombea huyo hakutimiza wajibu wake kulingana na katiba ya Simba ibara ya 19 kifungu namba 3,4,6,7 na 8 na ibara ya 21 kifungu g na i.
Alisema kamati pia imebaini mkanganyiko wa majina ya mwombaji huyo katika vyeti vyake vya elimu na hati zingine, na alitoa mfano kuwa katika maelezo yake binafsi ametumia jina la Karaha Hassani Almasi Chano, wakati kwenye kadi ya uanachama wa Simba imeandikwa Chano K.H. Almasi.
"Hivyo kwa kutotimiza wajibu wake kulingana na matakwa ya katiba ya Simba na mkanganyiko huo wa majina, hakika umeitia dosari fomu ya mgombea na amekosa sifa ya kuwa mmoja wa wagombea," alisema.
Lyatto alisema kuenguliwa kwa Hanspope, ambaye alikuwa amewekewa pingamizi na Issa Ruchaki, baada ya kubaini kanuni za uchaguzi za wanachama wa TFF ibara ya 25(2).
Alisema kamati yake imebaini kamati ya uchaguzi ya Simba ilifanya makosa kutumia ibara ya 45 ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, bila ya kuzingatia katiba ya klabu hiyo ibara ya 26(5) kwa kumpitisha mwombaji asiyekidhi matakwa ya kifungu hicho.
Lyatto alisema uamuzi huo umefanywa baada ya kuridhika kuwa wagombea hao wana upungufu unaowanyima nafasi ya kuwania uongozi, na si kwa lengo la kumuharibia yeyote ila kwa kuzingatia kanuni na taratibu kuhusiana na pingamizi zilizowekwa.
"Huo ni uamuzi wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF, ambayo kulingana na katiba ya shirikisho, bado wagombea wana haki ya kupinga uamuzi huo kwa Kamati ya Rufani ya TFF, endapo aliyeenguliwa haridhiki na uamuzi uliotolewa," alisema.
Hata hivyo, imedaiwa kuwa kitendo cha kuenguliwa wagombea hao kimezua minong'ono kwa baadhi ya walioenguliwa, na wanachama, na kuzusha tetesi kuwa kuna uwezekano wa wanachama au waliongeliwa wakalipeleka suala hilo mahakakamani.

BOB RAMOZA NA MREMBO WA TZ

BOB Ramoza (kushoto) akimuhoji mrembo wa Tanzania wa mwaka 2009, Miriam Gerard siku chache baada ya kuvishwa taji hilo katika shindano lililofanyika kwenye ukumbi wa Mlimani City mjini Dar es Salaam. Miriam alishindwa kung'ara katika shindano la dunia lililofanyika Afrika Kusini baada ya kutolewa hatua za awali.

Thursday, April 29, 2010

BOB RAMOZA NDANI YA DISCO DENMARK

BOB Ramoza (kushoto) akisakata muziki kwenye ukumbi wa Disco wa Huset uliopo mjini Copenhagen nchini Denmark mwaka 1989. Kwa kawaida, ukumbi huu huwa ukifurika vijana wengi wa Kiafrika na wanawake wa kizungu, ambao huenda hapo kutafuta mabwana weusi wenye sifa za nanihii....

BOB RAMOZA NA WADAU WA DISCO


MMILIKI wa blogu hii, Bob Ramoza (wa nne kulia) akiwa na wacheza disco mahiri wa miaka ya 1990. Hapa wapo Banza Stone, Ras De, Super Mamuu, Elvis Danger, Black Moses na Kelly John. Ilikuwa ni kwenye ukumbi mmoja wa Magomeni, Dar es Salaam.

Simba kuongeza wapiga mabao wawili


KOCHA Mkuu wa Simba, Patrick Phiri amesema anafanya mipango ya kusajili washambuliaji wapya wawili na kiungo mmoja kwa ajili ya msimu ujao wa ligi kuu na michuano ya kimataifa.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Phiri alisema amepanga kusajili wachezaji hao kwa lengo la kukiimarisha zaidi kikosi chake.
Hata hivyo, Phiri hakuwa tayari kutaja majina ya wachezaji hao, lakini kuna habari kuwa, miongoni mwao ni kiungo Abdulrahim Humoud kutoka Mtibwa Sugar ya Morogoro.
Phiri alikiri kuwa, baadhi ya wachezaji walioichezea Simba msimu huu, kiwango chao kimeshuka na hatarajii kuwa nao msimu ujao, ndio sababu ameanza mapema mipango ya kuziba mapengo yao.
Mbali na Humuod, mchezaji mwingine, ambaye ametajwa kuwa huenda akasajiliwa na Simba msimu ujao ni mshambuliaji Mumba Felix Sunzu kutoka FC Lupopo ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.
Chanzo cha habari kimelidokeza gazeti hili kuwa, Sunzu anatarajiwa kuwasili nchini wakati wowote kwa ajili ya kufanya mazungumzo na viongozi wa klabu hiyo.
Hata hivyo, Simba huenda ikakumbana na kizingiti kikubwa cha kumsajili mchezaji huyo baada ya klabu ya FC Lupopo kusema inataka ilipwe sh. milioni 195 kwa ajili ya ada ya uhamisho.
Wachezaji wengine, ambao Simba imepanga kuwasajili kwa ajili ya msimu ujao wanatarajiwa kutoka katika klabu za Dynamo na Lengthens za Zimbabwe.
“Lengo langu ni kuongeza nguvu sehemu zenye mapungufu na kuimarisha zaidi safu ya ushambuliaji kwani kama unavyojua, timu inakabiliwa na michuano migumu ya Afrika,”alisema.
Wachezaji wa kigeni walioichezea Simba msimu huu ni beki Joseph Owino na mshambuliaji Emmanuel Okwi kutoka Uganda, viungo Hillary Echessa, Jerry Santo na mshambuliaji Mike Baraza kutoka Kenya.

Usajili Yanga utatisha!

Papic akabidhi majina kwa Manji
Wachezaji wapya hadharani Juni
Watakaotemwa kupewa barua Mei 15
MFADHILI mkuu wa klabu ya Yanga, Yusuf Manji amekutana na Kocha Mkuu wa timu hiyo, Kostadin Papic na kuzungumzia usajili wa wachezaji wapya kwa ajili ya msimu ujao.
Uchunguzi uliofanywa na Burudani umebaini kuwa, Manji na Papic wamekutana zaidi ya mara nne kuanzia Jumamosi iliyopita na jana walikuwa na kikao kizito cha kupanga mikakati ya usajili.
Mbali na kikao hicho kujadili masuala ya usajili, pia kililenga kumaliza tofauti zilizozuka kati yao na kusababisha Papic atishie kubwaga manyanga baada ya mkataba wake kumalizika.
Hali ya kutokuelewana kati ya Manji na Papic, ilizuka baada ya mfadhili huyo kumpigia simu kocha huyo kutoka Serbia na kumweleza kuwa, angeacha kumlipa mshahara kuanzia jana.
Manji alimweleza Papic kuhusu uamuzi wake huo siku moja kabla ya Yanga kumenyana na Simba katika mechi ya marudiano ya ligi kuu ya Vodacom na kupata kipigo cha mabao 4-3.
Kauli hiyo ya Manji ilimweka Papic kwenye wakati mgumu, hasa ikizingatiwa kuwa, aliwaleta wachezaji wane kutoka nje kwa ajili ya kufanyiwa majaribio, sambamba na msaidizi wake kutoka Serbia.
Kocha huyo msaidizi, Medic Momcilo ‘Moma’ alitua nchini wiki mbili zilizopita na jana alikutana na Manji kwenye ofisi za mfadhili huyo zilizopo barabara ya Nyerere, Dar es Salaam kwa lengo la kuzungumzia mkataba wake. Wachezaji walioletwa na Papic kwa ajili ya kufanyiwa majaribio ni Issack Boakye, anayechezea timu ya New Aedubase United ya Ghana anacheza nafasi ya ulinzi na Kenneth Asamoah, anayechezea klabu ya FK Jagodina ya Serbia.
Wengine ni Sylivester Selaph Mokaine kutoka klabu ya Back Aces ya Afrika Kusini na Osai Boakye kutoka klabu ya Aduna ya Ghana. Tayari wachezaji hao wamesharejea kwao.
Akizungumza na gazeti hili jana, Manji alikiri kukutana na Papic mara kadhaa na kuongeza kuwa, amemuagiza atumie kipindi cha likizo yake kusaka wachezaji wengine zaidi wenye vipaji.
Alipoulizwa iwapo ni kweli amemaliza tofauti zilizojitokeza kati yake na Papic, mfadhili huyo alisema kwa sasa hana tatizo na kocha huyo na wataendelea kufanyakazi pamoja kwa lengo la kuipatia mafanikio klabu hiyo. Tayari Manji ameshaingia mkataba na wachezaji wanne waliofanyiwa majaribio na Papic. Wachezaji hao waliondoka nchini jana na juzi kurejea kwao kwa ajili ya kushughulikia taratibuza uhamisho wa kimataifa kabla ya kurudi nchini Juni mwaka huu.
Kuna habari pia kuwa, baadhi ya wachezaji wa hapa nchini walioichezea Yanga msimu huu, wameshakutana na Manji na kutia saini mikataba mipya.
“Mchakato wa usajili Jangwani umeshaanza kwa tahadhari na siri kubwa. Manji amekutana na Papic na kuzungumza kwa kirefu kuhusu suala hilo na kimsingi amewakubali wachezaji wote waliopendekezwa na kocha huyo,” alisema mmoja wa wajumbe wa kamati ya utendaji ya Yanga.
Kuna habari kuwa, kipa Yaw Berko kutoka Ghana ametia saini mkataba mpya wa kuichezea Yanga kwa miaka miwili. Awali, Yaw alikuwa na mkataba na klabu hiyo wa miezi mitatu.

Dully Sykes ajitoa tuzo za Kili


MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya, Dully Sykes ametangaza kujitoa katika shindano la mwaka huu la kuwania tuzo za muziki za Kilimanjaro.
Dully, maarufu kwa jina la Mr. Misifa alitangaza uamuzi wake huo mwishoni mwa wiki iliyopita kwa madai kuwa, haoni faida ya tuzo hizo.
“Nilishasema sitaki kuwekwa kwenye katagori yoyote ile ya Kili Music Award, sioni faida ya tuzo hizo,”alisema Dully, ambaye kwa sasa anatamba kwa kibao chake cha ‘Shekidee’.
“Sijawahi kupata tuzo hizo tangu nianze muziki. Nimetoa singo 36 mpaka sasa kama vile Salome, Hunifahamu na nyinginezo kibao, lakini ajabu ni kwamba hakuna hata moja iliyopata tuzo,”alisema.
Msanii huyo machachari na mwenye mvuto kwa mabinti wa kike alisema, ni bora aendelee kurekodi singo kwa vile zinalipa kuliko kurekodi albamu nzima.
Dully amekuwa msanii wa pili kujitoa kwenye tuzo za mwaka huu. Wa kwanza alikuwa Khaleed Mohamed, maarufu kwa jina la TID, aliyetangaza kujitoa wiki mbili zilizopita.
TID alifikia uamuzi huo kwa madai ya kutoridhishwa na uteuzi uliofanywa na majaji wa shindano hilo kuhusu nyimbo zake na tuzo alizoingizwa kuziwania.
Kiongozi huyo wa bendi ya Top alisema, amekuwa akitengeneza nyimbo nyingi zinazopendwa na kukubalika na mashabiki, lakini hajawahi kupewa tuzo, hivyo haoni sababu ya kuendelea kushindanishwa katika kuziwania.
Sababu nyingine iliyotajwa na TID ni kushindanishwa kuwania tuzo hizo na wasanii wasiokuwa na sifa, hivyo anaona ni bora aendelee kutumia muda wake mwingi kufanyakazi zake binafsi.

AY, Ali Kiba waongoza tuzo za Museke


KWAMBA muziki wa kizazi kipya nchini unazidi kuchukua chati kimataifa, hilo halina ubishi. Hii imetokana na wasanii wengi wa muziki za Bongo Fleva nchini kuteuliwa kuwania tuzo za muziki za Museke.
Taarifa iliyotolewa na waandaaji wa tuzo hizo wiki hii imeonyesha kuwa, katika kila tuzo, yupo msanii mmoja ama wawili wa Tanzania walioteuliwa kuziwania.
Katika tuzo ya mwanamuziki bora wa mwaka, yupo msanii Ambwene Yesaya, maarufu kwa jina la AY. Ameteuliwa kuwania tuzo hiyo na Barbara Kanam na Fally Ipupa wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, Darey na Wande Coal wa Nigeria, HHP wa Afrika Kusini na Lizha James wa Msumbini.
AY pia ameteuliwa kuwania tuzo ya mwanamuziki bora wa kiume wa mwaka akiwa na Ali Kiba. Wasanii wengine walioteuliwa kuwania tuzo hiyo ni Sarey, Ipupa, HHP, Wande na Ralph Anselmo wa Angola.
Kiba pia ameteuliwa kuwania tuzo ya albamu bora kupitia albamu yake ya Ali K 4 Real, sanjari na Blu3 wa Uganda, Samini wa Ghana, Sauti Sol wa Kenya, Anselmo na Wande Coal.
Mtayarishaji nyota wa muziki, Hermy B ameteuliwa kuwania tuzo ya mtengenezaji midundo bora sanjari na Bue d beats wa Angola, Culoe de Song wa Afrika Kusini, Don Jazzy wa Nigeria, Ogopa DJs wa Kenya na Richie wa Uganda.
AY yumo pia kwenye tuzo ya wimbo bora wa Hip Hop kupitia kibao chake cha Leo. Anawania tuzo hiyo na Sarkodie wa Ghana, Dama do Bling wa Msumbiji, STL wa Kenya, HHP wa Afrika Kusini, Navio wa Uganda na MI wa Nigeria.
Mkali wa nyimbo za Injili nchini, Rose Muhando, ameteuliwa kuwania tuzo ya wimbo bora wa miondoko hiyo, kupitia kibao chake cha Nibebe, sanjari na Noelie wa Togo, Midnight Crew wa Nigeria, Wilson Bugembe wa Uganda, Kefee wa Nigeria, Joyous Celebration wa Afrika Kusini na Makoma wa Congo.
Kiba na Lady JayDee pia wameteuliwa kuwania tuzo ya wimbo bora wa miondoko ya Afro kupitia vibao vyao vya Msiniseme na Natamani kuwa Malaika wakati AY na Marlaw wameteuliwa kuwania tuzo ya wimbo bora wa mwaka wa Afrika Mashariki kupitia vibao vyao vya Leo na Piiii Piiii.

Kutana na Preta wa Shades of Sin


KWA mashabiki wa tamthilia hapa nchini, jina la Preta de Souza si geni kwao. Ni mmoja wa waigizaji wenye mvuto na walioipamba vyema tamthilia ya Shades of Sin, inayoendelea kuonyeshwa kupitia kituo cha televisheni cha ITV.
Ni msichana mwenye sura na umbo lenye mvuto, aliyezaliwa Maranhao. Ni msichana mwenye tabia nzuri, anayejiamini na mwenye msimamo wa aina wa pekee katika maisha yake.
Preta, ambaye jina lake halisi ni Taís Bianca Gama de Araújo, alizaliwa na kulelewa na mama yake, Dona Lita. Kamwe hakuwahi kukutana na baba yake.
Licha ya kumbukumbu ya maisha duni, aliyoishi na mama yake, siku zote amekuwa ni mtu mwenye njozi njema katika maisha yake na amekuwa akifanyakazi kwa bidii kwa lengo la kufanikisha azma yake.
Tangu akiwa mdodo, Preta amekuwa akimsaidia mama yake kuuza dawa mbalimbali zitokanazo na mitishamba katika mji mdogo wa Sao Luis uliopo Maranhao.
Kila alipokuwa hana kazi ya kufanya, Preta alipendelea sana kucheza muziki wa dansi wa miondoko ya tambor de crioula, ambao asili yake ni nchini Brazil, akiwa na rafiki zake. Wakati mwingine alipendelea kwenda matembezini akiwa na rafiki yake, Helinho.
Kama ilivyokuwa kwa Paco, Preta hakuwahi kujitosa kimapenzi kwa mwanaume yeyote. Alikuwa na urafiki wa kawaida na Dodo, kijana mwenye kipaji cha fani ya muziki.
Wakati Paco alipofika Sao Luis, ndipo Preta alipojihisi na kuwa na uhakika kwamba ndiye mwanaume pekee aliyemuingia moyoni mwake. Alimuona kuwa ndiye mwanaume pekee anayemfaa maishani mwake.
Binti huyo mwenye haiba yenye mvuto, alilazimika kwenda kinyume na usia wa mama yake, ambaye hakuwa akimwamini kijana huyo. Aliamua kuliamini penzi la Paco. Hata hivyo, Preta anahujumiwa na Barbara, mwanamke mwenye tabia chafu na ambaye alikuwa anataka kumtumia Paco ili kuchuma utajiri wa baba yake, Afonso. Barabara anatumia kila njia kumtenganisha Preta na Paco.
Njama hizo za Barbara zinafanikiwa. Na wakati Paco akitengana na Preta, binti huyo alikuwa tayari na uja uzito kabla ya kujifungua mtoto wa kiume, Rai.
Preta anapata taarifa za kifo cha Paco akiwa kwenye gari, anarejea Maranhao kutoka mjini Rio de Janeiro. Anapatwa na huzuni kubwa.
Anaamua kumtunza Rai kwa msaada mkubwa wa mama yake pamoja na swahiba wake mkubwa, Helinho bila kufanya jitihada zozote za kuitafuta familia ya Paco.
Ni pale anapoamua kwenda mjini kuisaka familia ya Paco, ndipo Preta anapokutana na masahibu mazito, yanayomfanya aishi maisha yaliyojaa woga na mashaka mazito.
Barbara, mchumba wa zamani wa Paco, aliyejifanya kuzaa na kijana huyo, ndiye anayeongoza mashambulizi hayo dhidi ya Preta kwa kushirikiana na Tony, mmoja wa wafanyakazi katika kampuni ya Afonso.
Tony na Barbara wanafanikiwa kumfanya Rai aonekane kuwa si mjukuu wa Afonso kwa kubadili vipimo vya DNA. Pia wanamuhusisha Preta na utapeli wa kuuza fomula, inayomilikiwa na Afonso kwa kumtumia mmoja wa wafanyakazi waaminifu wa mzee huyo.
Mbaya zaidi, Afonso anamuasili Rai kwa kutumia nguvu kutokana na kumpenda sana kijana huyo. Siku zote Afonso amekuwa akimlinganisha Rai na Paco alipokuwa mdogo.
Hata hivyo, mbinu hiyo chafu ya kuuza fomula inakuja kubainika baada ya mfanyakazi huyo wa Afonso kukiri kosa hilo mbele ya Preta na kwa mzee huyo. Ni kuanzia wakati huo, Afonso anaanza kurejesha imani kwa Preta. Kujitokeza kwa Paco baada ya kugundua kwamba Rai ni mtoto wake halali, aliyezaa na Preta, ndiko kunakohitimisha tamthilia hii. Paco anagundua kwamba Preta si laghai kama alivyokuwa akimfikiria. Safari hii anajitokeza kama Paco na si Apollo.
Preta alizaliwa Novemba 25, 1978 mjini Rio de Janeiro. Ni mmoja wa waigizaji filamu wenye mvuto nchini Brazil, akiwa Mbrazil wa kwanza mweusi kuigiza tamthilia ya Xica da Silva mwaka 1996. Pia alishiriki kucheza tamthilia ya Da Cor do Pecado mwaka 2004. Binti huyo pia alikuwa mwigizaji mkuu katika tamthilia ya Viver a Vida.
“Nilipokuwa mdogo, sikuwa na kitu chochote kilicholinganishwa na mimi. Sasa msichana mweusi anavyo vitu vingi vya kulinganishwa naye kwenye TV, yakiwemo masuala ya urembo,”alisema Preta alipohojiwa na kituo kimoja cha televisheni cha Brazil.
Mbali na kushiriki kucheza tamthilia na filamu nyingi, mwigizaji huyo wa kike pia ameshinda tuzo nyingi kutokana na uigizaji wake maridhawa.
Baadhi ya filamu alizoshiriki kuzicheza ni pamoja na A Guerra dos Rocha, O Maior Amor do Mundo, Nzinga, As Filhas do Vento, Cida, Garrincha, Caminho dos Sonhos na Drama Urbano.

CAPELLO: Enzi za klabu za England kutamba Ulaya zimekwisha

LONDON, England
KOCHA Mkuu wa timu ya taifa ya England, Fabio capello amezionya klabu kubwa za England kuwa zitashindwa kuendelea kutamba barani Ulaya iwapo zitashindwa kuwekeza kwa kusajili wachezaji nyota.
Onyo hilo la Capello limekuja siku chache baada ya miamba ya soka nchini humo, Chelsea, Manchester United na Arsenal kutolewa mapema katika michuano ya ligi ya mabingwa wa Ulaya.
Kutolewa mapema kwa miamba hiyo ya soka kunamaanisha kwamba, kwa mara ya kwanza katika historia ya ligi ya mabingwa wa Ulaya tangu mwaka 2003, mechi za robo fainali zitafanyika bila ya kuwepo wawakilishi wa England.
Capello alizisikitikia Chelsea na Manchester United kwa kufungashwa virago mapema na timu za Inter Milan ya Italia na Bayern Munich ya Ujerumani katika hatua ya robo fainali.
Kocha huyo alisema: “Ikilinganishwa na msimu uliopita, klabu zote za England ziliuza wachezaji wake muhimu. Baadhi walikwenda nje ya nchi, wengine walihamia klabu mpya, ikiwemo Manchester City. Ni wazi kwamba zilidhoofika.”
“Kwa uzoefu wangu, kama klabu ipo juu, inapaswa kununua mchezaji mmoja au wawili wenye kiwango cha juu kila mwaka ili iweze kubaki nafasi za juu, ikizingatiwa kuwa, upinzani unazidi kuwa mkali,” aliongeza.
“Haishangazi kuona kwamba, klabu zilizotumia fedha nyingi kusajili wachezaji wapya msimu huu kama vile, Barcelona, Inter Milan na Bayern ndizo zilizofuzu kucheza nusu fainali msimu huu,”alisema kocha huyo.
Capello alisema ni wazi kwamba mtikisiko wa kiuchumi duniani umeziathiri klabu nyingi barani Ulaya, baada ya kuwa zimetingisha kisoka kwa miaka kadhaa.
Alisema mbali na Manchester City, klabu zilizopewa nafasi kubwa ya kufanya vizuri msimu huu, zilikuwa Real Madrid na Inter Milan, ambazo zilitumia mamilioni ya pesa kwa ajili ya kujiimarisha.
Kocha huyo alisema, Rais wa Real Madrid, Florentino Perez alifanya kila aliloweza kuirejesha kwenye chati klabu hiyo wakati Inter Milan ilinunua wachezaji wapya sita.
“Uwekezaji ni muhimu, lakini unapaswa kufanywa kwa umakini. Unapaswa kusajili wachezaji wenye uwezo wa kuelewana na wenzao kwa haraka na kupata mafanikio,”alisema.
“Hata hivyo, jambo hili si la lazima, baadhi ya wachezaji hupata wakati mgumu kufiti kwenye klabu mpya, hata kama ni kutoka klabu ndogo kwenda klabu kubwa,”aliongeza.
Licha ya kuondoka kwa Cristiano Ronaldo na Carlos Tevez katika klabu ya Manchester United na usajili mdogo uliofanywa na Carlo Ancelotti ndani ya Chelsea, Capello alisema timu hizo mbili zilipaswa kuendelea kuwemo kwenye michuano hiyo hadi sasa.
Lakini alikiri kuwa, uamuzi wa Arsenal kuwauza Emmanuel Adebayor na Kolo Toure kwa klabu ya Manchester City, kulichangia kuidhoofisha na kuifanya itolewe na Barcelona.
Kocha huyo alisema, Manchester United haikuwa na bahati kwa sababu ililipa kutokana na makosa iliyoyafanya, kama ilivyoizawadia Bayerm Munich bao la pili mjini Munich na kuiruhusu kupata bao la kwanza baada ya kuwa mbele kwa mabao 3-0 ziliporudiana kwenye uwanja wa Old Trafford.
“Kilichofanya kuwepo na tofauti ni kutolewa kwa kadi nyekundu beki Rafael na kuumia kwa Wayne Rooney. Huwezi kuendelea mbele katika michuano hii ukiwa na matatizo ya aina hii,”alisema.
Capello alisema Chelsea ilicheza vizuri mjini Milan na ingeweza kupata matokeo mazuri na kwamba Inter Milan ingepaswa kucheza mchezo tofauti kwenye uwanja wa Stamford Bridge.
“Kama ilivyotokea, Inter Milan ilicheza vizuri mechi ya marudiano,”alisema.
Akiizungumzia Arsenal, kocha huyo alisema haikuwa na bahati kutokana na kuwapoteza wachezaji wake nyota watano, ambao ni majeruhi. Wachezaji hao ni Van Persie, Cesc Fabregas, Arshavin, William Galas na Ramsey. Alisema Arsenal iliwahitaji wachezaji hao ili iweze kusonga mbele.
Kocha huyo aliwaeleza Rooney na Lionel Messi wa Barcelona kuwa ni wachezaji tofauti, lakini wenye uweo mkubwa. Alisema ni jambo linalofurahisha kuwazungumzia wachezaji hao pamoja na Ronaldo.
Capello alikataa kumlaumu Kocha Mkuu wa Manchester United, Sir Alex Ferguson kwa uamuzi wake wa kumchezesha Rooney katika mechi dhidi ya Bayern ya kupona sawasawa maumivu ya kifundo cha mguu.
Alisema kuumia kwa wachezaji hao na wengineo wa England, huenda kukatia doa mipango yake katika michuano ya mwaka huu ya fainali za Kombe la Dunia, zinazotarajiwa kufanyika nchini Afrika Kusini.
“Naelewa wazi uamuzi wa Sir Alex wa kumchezesha Rooney kwa sababu anaelewa umuhimu wake kwa timu nzima,”alisema Capello. “Sifikirii kama alifanya kosa. Kama Sir Alex alimchezesha Rooney, bila shaka hali yake ilimruhusu kufanya hivyo.”
“Bahati pekee ni kwamba wachezaji wote wa England watapatikana mwanzoni mwa maandalizi yetu nchini Austria. Wakati wachezaji wanaposhinda mataji, wanakuwa na furaha kubwa na naamini hilo litakuwa na mafanikio kwetu,”alisema.
“Kitu muhimu kitakuwa ni kwa wachezaji wote wa England kupona na kuwa kwenye kiwango chao cha kawaida, mambo ambayo yalitusaidia kufanya vizuri katika mechi za kufuzu kombe la dunia,”alisema.
Capello alisema amekuwa akiwafuatilia kwa makini wachezaji wake wote na kwamba, daktari wa England amekuwa akiwasiliana mara kwa mara na madaktari wa klabu ili kujua maendeleo ya hali zao.
Kocha huyo alisema haitakuwa na maana kwake kuzungumza na madaktari wa klabu au wachezaji kwa vile hawawezi kupata picha kamili. Alisema anazungumza na wachezaji anapokutana nao kwenye mechi, lakini si kwa lengo la kufuatilia hali zao.
00000

Stars yaivutia pumzi Amavubi

WACHEZAJI wa timu ya soka ya taifa, Taifa Stars wamepania kuifunga Rwanda katika mechi ya awali ya raundi ya pili ya michuano ya Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ligi za ndani, itakayochezwa Jumamosi.
Wakizungumza na Burudani kwenye kambi yao iliyopo hoteli ya Atrium, Sinza, Dar es Salaam, wachezaji hao walisema lazima waifunge Rwanda ili wajiweke kwenye nafasi nzuri ya kufuzu kucheza fainali za michuano hiyo.
Mmoja wa wachezaji hao, Kigi Makasi alisema wanaendelea vizuri na mazoezi yao chini ya Kocha Marcio Maximo huku kila mchezaji akiwa na ari kubwa ya kushinda mechi hiyo.
“Kwa kweli sote tuna ari kubwa sana ya kuishinda Rwanda kwa sababu tumepania kufuzu kucheza fainali za michuano hiyo kwa mara ya pili mfululizo,”alisema.
Kipa Shaaban Kado alisema, mbinu wanazofundishwa na Maximo ni za kiwango cha juu na zimewafanya wawe na matumaini makubwa ya kushinda mechi hiyo.
Mshambuliaji Mussa Hassan ‘Mgosi’ alisema, Stars ina nafasi kubwa ya kuitoa Rwanda kwa vile imeshakutana nayo mara kadhaa katika mechi za kimataifa na kirafiki na kuishinda.
“Dawa pekee ni kuishinda Rwanda kwa mabao mengi hapa nyumbani ili kujiweka kwenye mazingira mazuri ya kusonga mbele,”alisema.
Stars ilifuzu kucheza raundi ya pili ya michuano hiyo baada ya kuibugiza Somalia mabao 6-0 katika mechi iliyochezwa mwezi uliopita kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Simba yapania kuwang'oa Wamisri

KLABU ya Simba imetamba kuwa, inao uwezo wa kuing’oa Haras El-Hadood ya Misri katika michuano ya Kombe la Shirikisho.
Kocha Msaidizi wa Simba, Amri Said alisema mjini Dar es Salaam juzi kuwa, ushindi walioupata katika mechi ya awali, ni kichocheo kikubwa kwao kusonga mbele.
Katika mechi hiyo iliyochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Simba iliichapa El-Hadood mabao 2-1.
Kufuatia ushindi huo, ili isonge mbele katika michuano hiyo, Simba sasa itahitaji sare ya aina yoyote wakati timu hizo zitakaporudiana wiki mbili baadaye mjini Alexandria.
Amri, ambaye ni maarufu kwa jina la ‘Jaap Stam’ alisema, kikosi chake kimepania kuweka rekodi ya kuzitoa klabu za Misri katika michuano ya Afrika kwa mara ya pili.
Simba iliweka rekodi hiyo kwa mara ya kwanza mwaka 2003 wakati ilipoishinda Zamalek kwa penalti 3-2 mjini Cairo baada ya matokeo ya jumla kati ya timu hizo kuwa sare ya bao 1-1.
Mabingwa hao wa Tanzania Bara pia wanajivunia rekodi ya kuwa timu pekee nchini kuzishinda timu za Misri katika michuano hiyo. Iliwahi kuifunga Al Ahly mabao 2-1 mjini Mwanza mwaka 1984 kabla ya kuzifunga Ismailia bao 1-0 na Arab Contractors mabao 3-1 mjini Dar es Salaam.
Amri alisema Kocha Patrick Phiri amepanga kutumia muda wa siku 10 kurekebisha kasoro zote zilizojitokeza katika mechi ya awali. Timu hiyo ilitarajiwa kuondoka nchini jana kwenda Oman kuweka kambi kwa ajili ya kujiandaa na mechi hiyo.
"Tulichokigundua ni kwamba, wapinzani wetu wanatumia mchezo wa pasi fupi na kupiga mipira ya kushtukiza, kwa hiyo tutahakikisha tunawapa mafunzo maalumu wachezaji wetu ili kuwadhibiti,”alisema.
Katika mechi ya awali, Simba iliwakosa viungo wake mahiri, Hillary Echessa, aliyekuwa na kadi mbili za njano na Mohamed Banka, ambaye alikuwa mgonjwa.
Kwa mujibu wa Amri, wachezaji hao wataichezea Simba kwenye mechi ya marudiano na hivyo kuiongezea nguvu kwa vile wapinzani wao hawawafahamu vyema.

Miss Utalii Vyuo Vikuu leo Arusha

MWANAMUZIKI machachari nchini, Ndanda Kosovo anatarajiwa kutoa burudani wakati wa shindano la Miss Utalii Vyuo Vikuu Kanda ya Kaskazini, linalotarajiwa kufanyika leo.
Mratibu wa shindano hilo, Upendo Simwita alisema juzi kuwa, warembo 12 kutoka vyuo mbalimbali vya elimu ya juu katika kanda hiyo, wanatarajiwa kuwania taji hilo.
Upendo alisema shindano hilo limepangwa kufanyika kwenye ukumbi wa hoteli ya Naura Springs ya mjini Arusha.
Mbali na Kosovo, mratibu huyo alisema, shindano hilo pia litapambwa kwa burudani ya muziki wa kizazi kipya kutoka kwa msanii Belle 9 kutoka mjini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Upendo, washindi watatu wa kwanza wa shindano hilo watashiriki katika fainali ya Taifa iliyopangwa kufanyika Julai mwaka huu mjini Dar es Salaam.
Alisema washiriki katika shindano hilo watachuana katika mavazi ya ubunifu, utalii na kutokea matembezini nyakati za jioni. Pia alisema watachuana katika shindano la vipaji, ambapo watashindanishwa kuimba na kucheza ngoma za kiasili.
Upendo amewataka wakazi wa mji wa Arusha kujitokeza kwa wingi kushuhudia shindani hilo, ambalo lengo lake kubwa ni kutangaza vivutio vya kitalii vilivyopo nchini.

Ngorongoro kuivaa Malawi leo

TIMU ya soka ya Taifa ya vijana wa chini ya miaka 20, Ngorongoro Heroes leo itajitupa dimbani kumenyana na Malawi katika mechi ya marudiano ya raundi ya kwanza ya michuano ya kuwania ubingwa wa Afrika.
Pambano hilo linalotarajiwa kuwa la vuta nikuvute, litapigwa kuanzia saa 9.30 alasiri kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Florian Kaijage alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, pambano hilo limepangwa kuanza mapema, ili kama matokeo yatakuwa sare, kuwepo na muda wa nyongeza na wa kupigiana penalti tano tano.
Katika pambano la awali, lililochezwa wiki mbili zilizopita mjini Lilongwe, timu hizo zilitoka sare ya mabao 2-2.
Ili ifuzu kucheza raundi ya pili ya michuano hiyo, Ngorongoro italazimika kuifunga Malawi kwa idadi yoyote ya mabao na kutowaruhusu wapinzani wao kupata bao la ugenini.
Malawi ilitarajiwa kuwasili nchini jana mchana, ikiwa na msafara wa wachezaji 20 na viongozi watano.
Kwa mujibu wa Kaijage, baadhi ya mashabiki watakaohudhuria pambano hilo na kukaa kwenye eneo la mzunguko, hawatatozwa kiingilio. Eneo hilo ndilo linalochukua mashabiki wengi ikilinganishwa na kwenye majukwaa.
Kaijage alisema ofa ya kuruhusu mashabiki waingie uwanjani bure, itatoa hamasa kwao kuishangilia Ngorongoro muda wote wa mchezo na hivyo kuwapa ari wachezaji ya kushinda pambano hilo.
Ofisa huyo wa TFF alisema, mashabiki wengine watakaokaa jukwaa kubwa na la kijani watalipa kiingilio. Alivitaja viingilio hivyo kuwa ni sh. 10,000 kwa VIP, sh. 5,000 kwa jukwaa kubwa na sh. 3,000 kwa jukwaa la kijani.
Alisema mechi hiyo itachezeshwa na waamuzi kutoka Eritrea. Aliwataja waamuzi hao kuwa ni Gebremichael Luelsged, Mohamed Berhane na Tesfagiorghis O’Michael wakati mwamuzi wa akiba atakuwa Ibada Ramadhani wa Tanzania.
Iwapo Ngorongoro itaitoa Malawi, itakutana na Ivory Coast katika raundi ya pili. Fainali za michuano hiyo zimepangwa kufanyika mwaka 2011 nchini Libya.

Thursday, April 22, 2010

Humuod atupwa nje Stars

Na Deusdedit Undole
KIUNGO mahiri wa timu ya soka ya Taifa, Taifa Stars, Abdulhalim Humuod ametemwa kwenye kikosi kilichotangazwa na kocha Marcio Maximo.
Akizungumza kwenye ukumbi wa Shirikisho la Soka nchini (TFF) uliopo Ilala, Dar es Salaam jana, Maximo alisema amemuacha mchezaji huyo kutokana na kutokuwepo kambini kwenye timu yake ya Mtibwa takriban siku 10.
"Kamwe huwezi kumuita mchezaji aliyekimbia kambi ya klabu yake kwa zaidi ya siku 10. Tumebakiwa na siku chache za kujiandaa kwa mechi ngumu dhidi ya Rwanda," alisema Maximo.
Alisema licha ya uwezo na kipaji cha hali ya juu alichonacho mchezaji huyo, kiufundi hastahili kuwemo kwenye timu ya taifa kwa sababu wanahitajika wachezaji waliokaa kambini pamoja kwa muda mrefu katika klabu zao.
Maximo alisema kuwa amemrejesha mchezaji mwingine wa Mtibwa Sugar, Dickson Daud baada ya kubaini kiwango chake kimepanda.
"Timu ya taifa ina orodha ya wachezaji wengi na kila mmoja ana nafasi yake kulingana na uwezo anaokuwa nao wakati huo. Hivyo nimemrejesha Dickson Daudi kikosini, baada ya kuridhika na kiwango chake," alisema kocha huyo.
Maximo alisema kambi ya Stars itaanza kesho jioni jijini Dar es Salaam na amewataka wachezaji wote kuripoti isipokuwa wa timu ya Simba, ambao watajumuika na wenzao Jumapili.
Stars itaingia kambini kwa ajili ya maandalizi ya mechi ya mzunguko wa pili wa kusaka tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa Afrika kwa wachezaji wa ligi za ndani (CHAN) dhidi ya Rwanda.
Mechi hiyo itachezwa Mei Mosi mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa.Wachezaji wanaounda kikosi hicho ni;
Makipa: Shabani Kado (Mtibwa Sugar) na Jackson Chove (Ruvu JKT).
Mabeki: Shadrack Nsajigwa, Nadir Haroub 'Cannavaro' (wote Yanga), Salum Kanoni, Juma Jabu, Kelvin Yondani na David Naftali (wote Simba). Pia wamo Stephano Mwasika (Moro United), Aggrey Morris (Azam FC) na Dickson Daudi (Mtibwa Sugar).
Viungo: Erasto Nyoni, Ibrahim Mwaipopo, Seleman Kassim (wote Azam FC), Nurdin Bakari, Abdi Kassim 'Babi', Kigi Makasi (wote Yanga), Shaban Nditi (Mtibwa Sugar), Jabir Aziz na Uhuru Seleman (Simba).
Washambuliaji: Mrisho Ngasa, Jerson Tegete (Yanga), John Bocco (Azam FC), Mussa Hassan 'Mgosi' (Simba), Michael Mgimwa (Moro United na U20), Yussuf Soka na Jonas Kajuna (African Lyon na U20).
000

Maftah, Ndhlovu, Nurdin wakalia kuti kavu

WISDOM Ndhlovu
NURDIN Bakari

AMIR Maftah
Na Emmanuel Ndege
UONGOZI wa klabu ya Yanga umeanza uchunguzi wa kina kujua chanzo kilichosababisha kikosi chao kupokea kipigo cha mabao 4-3 kutoka kwa Simba katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom iliyochezwa Jumapili iliyopita.
Kwa mujibu wa taarifa iliyopatikana jana kutoka ndani ya klabu hiyo, uchunguzi huo unafanywa na viongozi kwa kuwaita baadhi ya wachezaji na kuwahoji, ambapo wachezaji wanaohusishwa na sakata hilo ni Amir Maftah, Wisdom Ndhlovu, Boniface Ambani, Obren Cirkovic na Nurdin Bakari.
Kocha wa Yanga Kostadin Papic, Jumatatu ya wiki hii alitoa maelezo kwa uongozi juu ya kilichosababisha timu hiyo kubugizwa mabao hayo katika mchezo huo wa wapinzani wa jadi nchini, na inadaiwa kwenye ripoti hiyo ametaja baadhi ya wachezaji waliocheza chini ya kiwango.
Habari zinadai kuwa viongozi wanaoongoza mchakato huo ni Katibu Mkuu, Lawrence Mwalusako, Katibu wa Kamati ya Mashindano, Emmanuel Mpangala, ambao walikutana na Papic siku ya pili baada ya mechi hiyo na kumwangushia maswali, ili kujua sababu ya Yanga kupata kibano hicho.
Taarifa hizo zimedai viongozi hao baada ya kupata maelezo ya kina watawasilisha ripoti kamili kwa wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo, ambayo inatarajiwa kukutana leo au kesho mara wachezaji watakaporejea Dar es Salaam kutoka Mbeya.
Kikosi hicho juzi kilikwenda jijini Mbeya kuikabili Prisons jana katika mechi ya kufunga pazia la ligi kuu msimu huu.
Mwalusako alipoulizwa kwa njia ya simu juzi kuhusu uchunguzi huo, alikiri kuwepo suala hilo na kufafanua kuwa wanataka kujua kwa nini Maftah alimtandika kichwa Juma Nyoso wa Simba wakati alifahamu timu hiyo ilikuwa na pengo la Ndhlovu aliyetolewa kwa kadi nyekundu.
“Ni kweli tunataka kujua kwa nini Maftah na Ndhlovu walifanya vile, lakini tutakuwa makini kabla ya kutoa uamuzi,” alisema Mwalusako.

Simba yaelekeza makombora yake Misri

Na Athanas Kazige
WAKATI kikosi cha timu ya soka ya Haras El-Hodood ya Misri kinatarajiwa kuwasili nchini kesho, benchi la ufundi la klabu ya Simba limefanikiwa kunasa siri kadhaa za timu hiyo.
Mwenyekiti wa kamati ya mashindano ya Simba, Kassim Dewji alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, El-Hodood inatarajiwa kuja nchini ikiwa na kikosi cha wachezaji 20 na viongozi watano.
Hata hivyo, Kassim hakueleza timu hiyo itakuja kwa ndege ipi na itafikia hoteli gani. Lakini kwa kawaida, timu za Misri huja nchini kwa ndege za Shirika la Ndege la Misri.
Simba na El-Hodood zinatarajiwa kumenyana Jumapili katika mechi ya awali ya raundi ya pili ya michuano ya Kombe la Shirikisho, itakayochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam kabla ya kurudiana wiki mbili baadaye mjini Cairo.
Wakati Wamisri wakitarajiwa kutua kesho, benchi la ufundi la Simba limesema, limeshanasa siri kadhaa za timu hiyo na limejiandaa kuwawezesha mabingwa hao wa soka Tanzania Bara kuibuka na ushindi mnono. Mmoja wa viongozi wa benchi la ufundi la Simba, amelieleza Burudani jana kuwa, wamefanikiwa kupata siri hizo kutoka kwa ofisa mmoja wa ubalozi wa Tanzania nchini Misri.
Kiongozi huyo alisema, mara baada ya kuzinasa siri hizo, walianza kuzifanyiakazi ili kuwawezesha wachezaji wa idara zote tatu kukabiliana vyema na wapinzani wao.
Imeelezwa kuwa, El-Hodood, inayotumia uwanja wa El-Max uliopo mjini Alexandria, imekuwa ikiwategemea zaidi wachezaji wake wane nyota kupata ushindi.
Wakali hao, ambao ni tegemeo kubwa la Kocha Tarek El-Ashry nipamoja na nahodha, Ahmed Eid Abdel Malek, ambaye yumo kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Misri.
Wengine ni mshambuliaji Fofo Wisdom, anayetoka Ghana, kiungo Abdoulaye Sidibé anayetoka Mali na kiungo mwingine, Abdelrahman Mohie, rais wa Misri, ambaye ni mahiri kwa kufunga mabao ya mashuti ya mbali.
Kwa upande wa makipa, timu hiyo imewasajili Wael Khalifa, Mohamed Said na Mathurin Kameni kutoka Cameroon, ambao mmojawapo atakuwa na kazi kubwa ya kuzuia mashuti ya Mussa Hassan ‘Mgosi’, Mohamed Banka, Emmanuel Okwi na Uhuru Selemani.
Ofisa Habari wa Simba, Clifford Ndimbo alisema jana kuwa, wameshachukua tahadhari zote kabla ya kukabiliana na timu hiyo ya Misri, ambayo inashika nafasi ya sita katika msimamo wa ligi ya nchi hiyo.
Ndimbo alisema Simba inatarajiwa kuondoka Morogoro leo asubuhi kurudi Dar es Salaam, ambako itapanda boti kwenda Zanzibar kwa ajili ya kuweka kambi ya kujiandaa kukabiliana na wapinzani wao.
Simba ilifuzu kucheza raundi ya pili ya michuano hiyo baada ya kuichapa Lengthens ya Zimbabwe kwa jumla ya mabao 5-1. Ilishinda mechi ya awali mjini Zimbabwe kwa mabao 3-0 kabla ya kushinda mechi ya marudiano mjini Dar es Salaam mabao 2-1.
Katika hatua nyingine, wagombea wa nafasi ya uenyekiti katika uchaguzi mkuu wa klabu ya Simba, Michael Wambura na Ismail Rage wamekatiwa rufani.
Wambura na Rage wamekuwa wagombea wengine wawili kukatiwa rufani baada ya kupitishwa na kamati ya usajili ya Simba. Mgombea mwingine ni Zacharia Hanspope.

SIMBA YAFUNGA KAZI; Mgosi awazika Ngasa na Boko; Kaseja kuibuka kipa bora

Na Latifa Ganzel, Morogoro
MABINGWA wa soka wa Tanzania Bara, Simba jana walimaliza michuano ya ligi kuu kwa kishindo baada ya kuichapa Mtibwa Sugar mabao 4-0 katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.
Matokeo hayo yaliiwezesha Simba kuweka rekodi ya kumaliza ligi hiyo bila kupoteza mchezo, ikiwa imeshinda mechi 20 na kutoka sare mbili. Inazo pointi 61 baada ya kucheza mechi 22.
Mbali na rekodi hiyo, mshambuliaji Mussa Hassan ‘Mgosi’ ameibuka kuwa mfungaji bora wa ligi kuu msimu huu baada ya kuifungia Simba mabao mawili kati ya manne.
Mgosi amemaliza ligi hiyo akiwa na mabao 18, akifuatiwa na Mrisho Ngasa wa Yanga na John Boko wa Azam waliofunga mabao 14 kila mmoja.
Kipa Juma Kaseja wa Simba huenda akaibuka kuwa kipa bora msimu huu baada ya kudaka mechi 21 kati ya 22 na kuruhusu timu yake kufungwa mabao 12.
Iliwachukua Simba dakika 15 kuhesabu bao la kwanza lililofungwa na Mgosi kwa shuti kali baada ya kupokea pasi kutoka pembeni ya uwanja.
Mohamed Kijuso aliiongezea Simba bao la pili dakika ya 34 baada ya kumalizia kazi nzuri iliyofanywa na Mike Baraza aliyeambaa na mpira pembeni ya uwanja na kumimina krosi. Mabao hayo yalidumu hadi mapumziko.
Bao la tatu la Simba lilifungwa na kiungo mshambuliaji, Ramadhani Chombo ‘Redondo’ baada ya gonga safi kati yake, Mgosi na beki Salum Kanoni, aliyepanda na mpira mbele kutoka nyuma ya uwanja.
Simba ilihitimisha karamu ya magoli dakika ya 80 kwa bao lililofungwa na Mgosi baada ya kuunganisha wavuni krosi iliyopigwa na Jabir Azizi.
Mtibwa ililazimika kumaliza mchezo huo ikiwa na wachezaji 10 baada ya beki wake, Geofrey Magori kutolewa nje kwa kadi nyekundu dakika ya 89 kwa kosa la kumkwatua kwa nyuma Kelvin Yondani akiwa ndani ya eneo la hatari.

Papic amwaga cheche Yanga


KOCHA Mkuu wa Yanga, Kostadin Papic amesema ni vigumu kuwafundisha nidhamu wachezaji wa timu hiyo kwa sababu wameshakomaa.
Akizungumza mjini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita, Papic alisema wachezaji wakishakuwa na umri mkubwa, haiwezekani kuwafundisha nidhamu.
Papic alitoa kauli hiyo muda mfupi baada ya Yanga kuchapwa mabao 4-3 na Simba katika mechi ya ligi kuu ya Vodacom, iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Papic alisema nidhamu inaanza utotoni na kazi anayoifanya Yanga ni kufundisha kucheza soka kwa kutumia mbinu mbalimbali.
“Haiwezekani kufundisha nidhamu kwa watu wakubwa,” alisema kocha huyo baada ya kuulizwa ana maoni gani kuhusu vitendo vya wachezaji wake, baada ya Amir Maftah na Wisdom Ndhlovu kuonyeshwa kadi nyekundu katika mechi hiyo ya watani wa jadi nchini.
Papic alikataa kumtupia lawama mwamuzi wa mchezo huo, Mathew Akram kwa kutoa kadi hizo na kusisitiza kuwa, anachoangalia ni matokeo.
“Nakubali nimebugizwa mabao manne na huu ndiyo mchezo wa soka,” alisema.
Kocha huyo alitoa onyo kali kwa wachezaji wa timu hiyo wenye tabia ya utovu wa nidhamu na kusema hawezi kuwavumilia kwa vile wanachangia kushuka kwa maendeleo ya timu hiyo.
Papic alisema hakufurahishwa na vitendo vilivyoonyeshwa na wachezaji hao na wengine katika mechi hiyo, hivyo hawezi kuvifumbia macho.
Alisema angependa kuona kila mchezaji anaonyesha juhudi uwanjani, ikiwa ni pamoja na kuepuka makosa ya utovu wa nidhamu yasiyokuwa na maana.
Alisema kwa kipindi cha miezi mitano alichokuwepo Yanga, amegundua kuwa baadhi ya wachezaji wana kiburi na dharau kutokana na kujiona wao ni bora kuliko wenzao.
“Huu ndio msimamo wangu, siwezi kuendelea kuwa na wachezaji wa aina hii na wanaoshindwa kutimiza majukumu yao. Yanga ni timu ya ushindi, wachezaji wanapaswa kutambua hilo,”alisema.

DALILI ZA UBINGWA SIMBA ZILIANZA MAPEMA

NAHODHA wa Simba, Nico Nyagawa (kushoto) na beki Juma Jabu wakifurahia kombe la ubingwa wa ligi kuu ya Bara
WACHEZAJI wa Simba wakishangilia baada ya kuifunga Yanga

TIMU kongwe ya soka nchini, Simba msimu huu imeweka rekodi ya kutwaa ubingwa wa ligi kuu ya Vodacom kabla haijamalizika baada ya kuwa na idadi kubwa ya pointi, ambazo haziwezi kufikiwa na timu zingine.
Simba iliweka rekodi hiyo baada ya kuichapa Azam FC mabao 2-0 katika mechi iliyochezwa Machi 14 mwaka huu kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Ushindi huo uliiwezesha Simba kufikisha pointi 56, ambazo hakuna timu nyingine inayoweza kuzifikia katika ligi hiyo. Jumla ya timu 12 zinashiriki katika ligi ya msimu huu.
Mbali na kutwaa ubingwa mapema, Simba pia iliweka rekodi ya kutofungwa hata mechi moja katika mechi 21 ilizocheza hadi sasa. Mabingwa hao wa soka Tanzania Bara, walitarajiwa kucheza mechi ya mwisho jana dhidi ya Mtibwa Sugar mjini Morogoro.
Mafanikio ya Simba msimu huu yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na mafunzo mazuri kutoka kwa Kocha Mkuu wa timu hiyo, Patrick Phiri kutoka Zambia. Phiri pia aliiwezesha Simba kutwaa taji hilo mwaka 2006 na 2007.
Dalili za mafanikio kwa Simba zilianza kujionyesha katika mechi zake za mwanzo, ambapo iliichapa Majimaji mabao 2-0 mjini Songea kabla ya kuilaza Prisons bao 1-0 mjini Mbeya.
Simba iliendeleza wimbi la ushindi kwa kuichapa Toto African mabao 3-1 mjini Dar es Salaam, iliilaza Kagera Sugar mabao 2-0 mjini Dar es Salaam kabla ya kuishindilia Manyema mabao 2-0 kwenye uwanja huo.
Miamba hiyo ya soka nchini iliendelea kuwapa raha mashabiki wake baada ya kuichapa Moro United mabao 2-1 mjini Dar es Salaam, iliichapa African Lyon bao 1-0 mjini Dar es Salaam kabla ya kuipa kipigo cha mwaka JKT Ruvu kwa kuicharaza mabao 4-1 kwenye uwanja huo.
Simba pia iliichapa Azam FC bao 1-0, ikaichapa Yanga idadi hiyo ya bao kabla ya kuibamiza Mtibwa Sugar mabao 3-1. Mechi hizo zote tatu zilichezwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam na kuiwezesha Simba kumaliza mzunguko wa kwanza kwa kushinda mechi zote 11.
Katika mechi za mzunguko wa pili, Simba iliichapa Majimaji mabao 2-0, iliicharaza Prisons mabao 3-1, iliilaza Toto African mabao 2-0 lakini ikakwaa kisiki kwa Kagera Sugar baada ya kulazimishwa kutoka nayo sare ya bao 1-1 mjini Bukoba.
Mabingwa hao wa Bara waliichapa Manyema mabao 2-0, waliibamiza Moro United mabao 4-1 lakini wakakwaa kisiki kwa African Lyon baada ya kulazimishwa kutoka nayo sare ya bao 1-1.
Simba iliendeleza tena ubabe kwa kuichapa JKT Ruvu mabao 3-1, iliichapa Azam FC mabao 2-0 kabla ya kuwapa kichapo kingine watani wao wa jadi Yanga cha mabao 4-3.
Mbali na mafanikio hayo ya Simba kuchangiwa kwa kiasi kikubwa na mafunzo ya Phiri, pia yametokana na kujituma kwa wachezaji wake na kucheza kwa ushirikiano.
Baadhi ya wachezaji waliochangia mafanikio hayo ni kipa Juma Kaseja, aliyecheza mechi zote 21 na kuruhusu kufungwa mabao 12 na kiungo Mohamed Banka, ambaye alicheza mechi zote 11 za mzunguko wa kwanza.
Wachezaji wengine ni nahodha Nico Nyagawa, ambaye Phiri amekuwa akimpanga mara kwa mara kutokana na uwezo wake wa kukaba wachezaji wa timu pinzani na mabeki Salum Kanoni, Juma Jabu, Kelvin Yondani na Juma Nyosso.
Kwa upande wa safu ya ushambuliaji, wachezaji waliochangia mafanikio hayo ya Simba ni Mussa Hassan ‘Mgosi’, Uhuru Selemani, Ulimboka Mwakingwe, Mohamed Kijuso.
Lakini si rahisi kuzungumzia mafanikio hayo ya Simba bila ya kuwataja nyota wake kutoka nje ya nchi. Nyota hao ni beki Joseph Owino na mshambuliaji Emmanuel Okwi kutoka Uganda na kiungo Hillaly Echessa kutoka Kenya.
Kama kuna timu inayoweza kujivunia usajili wake wa wachezaji wa kigeni basi ni Simba. Wachezaji hao wamekuwa wakicheza kwa kujituma na kuthibitisha maana halisi ya soka ya kulipwa, tofauti na wageni waliosajiliwa na timu zingine zinazoshiriki ligi hiyo.
Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Leodegar Tenga aliwahi kutamka bayana baada ya mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo kumalizika kuwa, kama kuna timu iliyosajili wachezaji halisi wa kulipwa, basi ni Simba.
Tenga alisema kujituma kwa wachezaji hao uwanjani, staili zao za uchezaji na ushirikiano waliouonyesha kwa wachezaji wenzao wa Simba ni baadhi tu ya mambo yaliyoiwezesha timu hiyo kufanya vizuri msimu huu.
Akizungumzia mafanikio ya timu hiyo msimu huu, Phiri alisema yametokana na wachezaji kuyashika vyema mafunzo yake na kuyafanyiakazi wanapokuwa uwanjani.
Phiri alisema amefurahi kuiwezesha timu hiyo kutwaa ubingwa kabla ya ligi kumalizika na pia kuwa timu pekee, ambayo haijapoteza mechi hata moja.

YANGA ILISAHAU BIASHARA ASUBUHI, JIONI MAHESABU

JERRY Tegete wa Yanga (kulia) akibadilishana jezi na Ulimboka Mwakingwe wa Simba
BEKI Shadrack Nsajigwa wa Yanga akiangushwa na beki mwenzake, Juma Jabu wa Simba katika mechi kati ya timu hizo iliyochezwa Jumapili iliyopita.

MUSSA Hassan 'Mgosi' (kulia) wa Simba akichuana na Athumani Iddi 'Chuji' wa Yanga timu hizo zilipokutana katika mechi ya marudiano ya ligi kuu ya Vodacom kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Simba ilishinda mabao 4-3.

KABLA ya kuanza kwa michuano ya soka ya ligi kuu ya Vodacom msimu huu, mashabiki wengi wa klabu ya Yanga walikuwa na matumaini makubwa ya kuiona timu hiyo ikitwaa ubingwa kwa mara ya tatu mfululizo.
Walikuwa na matumaini hayo kutokana na usajili mzuri na wa gharama kubwa uliofanywa na mfadhili mkuu wa klabu hiyo, Yusuf Manji kwa wachezaji 10 wa kimataifa kutoka nchi mbalimbali.
Wachezaji hao, nchi wanazotoka zikiwa kwenye mabano ni Obren Curkovic (Serbia), Yaw Berko (Ghana), Robert Jama Mba (Cameroon), Wisdom Ndhlovu (Malawi), George Owino, Moses Odhiambo, Boniface Ambani, John Njoroge (Kenya) na Steven Bengo (Uganda).
Matumaini mengine kwa wana-Yanga yalitokana na ukweli kwamba, tmu hiyo ilikuwa ikiendelea kufundishwa na Kocha Dusan Kondic kutoka Serbia, aliyeiwezesha kutwaa ubingwa kwa misimu miwili mfululizo.
Hata hivyo, wakati Yanga ikijiandaa kwa ligi hiyo, kulizuka mvutano kati ya Kocha Kondic na uongozi kuhusu mahali, ambako timu hiyo ingeweka kambi.
Kondic alikuwa akitaka timu hiyo iende kuweka kambi nchini Afrika Kusini kama ilivyofanya msimu uliopita, lakini Mwenyekiti wa klabu hiyo, Iman Madega alitaka kambi iwe Mwanza.
Kwa bahati mbaya, Kondic na Madega walikwaa kisiki baada ya Manji kuamuru timu ikaweke kambi makao makuu ya klabu hiyo, yaliyopo mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam.
Mbali ya kutaka timu ikaweke kambi Jangwani, Manji aliamua kumuhamisha Kondic kutoka kwenye hoteli ya New Africa, iliyopo katikati ya Jiji hadi Valley View iliyopo Jangwani, Dar es Salaam.
Kadhalika ulizuka mvutano miongoni mwa wachezaji kuhusu timu kuhamishia kambi Jangwani. Baadhi ya wachezaji walikubali kwenda kuishi klabuni, lakini wengine walipinga kwa madai kuwa, vyumba vyake ni vya hadhi ya chini.
Yanga ilianza ligi hiyo kwa kusuasua. Katika mechi yake ya kwanza, ililazimishwa kutoka sare ya bao 1-1 na African Lyon kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kabla ya kuinyuka Manyema mabao 3-0 kwenye uwanja huo.
Hata hivyo, Yanga ilikwaa kisiki katika mechi yake ya tatu baada ya kukubali kipigo cha bao 1-0 kutoka kwa Majimaji mjini Songea, ikalazimishwa sare ya mabao 2-2 na JKT Ruvu kabla ya kuzinduka na kuichapa Mtibwa Sugar mabao 2-1.
Yanga iliendeleza wimbi la ushindi kwa kuichapa Kagera Sugar mabao 2-1, lakini ikalazimishwa kutoka sare ya bao 1-1 na Azam, ikaichapa Moro United bao 1-0 kabla ya kucharazwa bao 1-0 na watani wao wa jadi Simba na kuhitimisha mzunguko wa kwanza kwa kuicharaza Prisons mabao 4-2.
Baada ya kumalizika kwa mzunguko wa kwanza, Yanga ilijikuta ikiwa nyuma ya Simba kwa tofauti ya pointi tano. Pia kocha wake, Kondic aliondolewa na nafasi yake ikachukuliwa na kocha wa sasa, Kostadin Papic.
Mabadiliko hayo yaliisaidia Yanga kwani kiwango chake kisoka kiliongezeka na iliweza kushinda mechi nyingi za mzunguko wa pili, lakini ilishachelewa na kukosea mahesabu. Waswahili wanasema walikumbuka shuka, wakati kumekucha.
Ni katika mechi hizo za mzunguko wa pili, Papic aliweza kugundua kuwa, baadhi ya wanasoka wa kigeni waliosajiliwa na timu hiyo walikuwa bomu na hawakuwa na msaada wowote kwenye kikosi chake.
Miongoni mwa wachezaji hao ni Jama Mba, ambaye alisajiliwa kwa fedha nyingi kuliko wachezaji wote, Kabongo, Owino, Bengo, Odhiambo na Njoroge. Tayari kocha huyo ameshasema kuwa, hatarajii kuwasajili wachezaji hao katika msimu ujao wa ligi.
Pamoja na wachezaji hao kuonekana kuwa mzigo kwa klabu, Yanga iliweza kuifunga African Lyon mabao 2-0, ikaicharaza Manyema mabao 3-1, iliichapa Majimaji mabao 3-0, iliibwaga JKT Ruvu kwa bao 1-0 kabla ya kuipiga Mtibwa Sugar mabao 3-1.
Katika mechi zingine za mzunguko wa pili, Yanga iliichapa Kagera Sugar mabao 2-1, iliitandika Toto African mabao 6-0, ikaichapa Azam mabao 2-1, iliibamiza Moro United 3-0 kabla ya kukubali kipigo cha mabao 4-3 kutoka kwa watani wao wa jadi Simba.
Kipigo kutoka kwa Simba kimeshaanza kuwagawa viongozi na wanachama wa klabu hiyo, huku kukiwepo na tuhuma kwamba abadhi ya wachezaji walicheza chini ya kiwango kwa lengo la kuihujumu timu.
Yanga ilitarajiwa kuhitimisha ligi hiyo jana kwa kumenyana na Prisons mjini Mbeya huku mshambuliaji wake, Mrisho Ngassa akiwa na matumaini ya kuwapiku Mussa Hassan ‘Mgosi’ wa Simba na John Boko wa Azam katika kuwania tuzo ya mfungaji bora.
Kabla ya mechi za jana, Mgosi alikuwa akiongoza kwa kufunga mabao 16, akifuatiwa na Boko na Ngassa waliofunga mabao 14 kila mmoja.




NI LIGI ILIYOJAA WANASOKA WENGI WA KIGENI

JOSEPH Owino
HILLARY Echessa

EMMANUEL Okwi

MICHUANO ya soka ya ligi kuu ya Vodacom ilitarajiwa kufikia tamati jana kwa mechi sita zilizotarajiwa kuchezwa kwenye viwanja sita tofauti.
Katika mechi hizo, mabingwa Simba walitarajiwa kumenyana na Mtibwa Sugar mjini Morogoro, washindi wa pili Yanga walitarajiwa kucheza na Prisons mjini Mbeya wakati African Lyon ilitarajiwa kucheza na JKT Ruvu mjini Dodoma.
Katika mechi zingine, Manyema ilitarajiwa kuvaana na Azam mjini Dar es Salaam, Majimaji ilitarajiwa kucheza na Moro United mjini Songea wakati Toto African ilitarajiwa kukipiga na Kagera Sugar mjini Mwanza.
Kabla ya mechi za jana, Moro United ndiyo timu pekee, iliyokuwa imeshapata tiketi ya kushuka daraja msimu huu na kusubiri kucheza ligi daraja la kwanza msimu ujao. Moro ilikuwa na pointi 15 baada ya kucheza mechi 21.
Timu zingine zilizokuwa hatarini kushuka daraja ni Prisons na Toto African, zilizokuwa na pointi 20 kila moja baada ya kucheza mechi 21 na Manyema iliyokuwa na pointi 22 baada ya kucheza idadi hiyo ya mechi.
Katika ligi ya msimu huu, timu saba kati ya 12 ziliweka maskani yake mjini Dar es Salaam na kucheza mechi zake kwenye Uwanja wa Uhuru. Timu hizo ni mabingwa Simba, Yanga, Azam, African Lyon, Moro United, JKT Ruvu na Manyema.
Timu zilizoshiriki ligi hiyo kutoka mikoani ni Kagera Sugar, Mtibwa Sugar, Majimaji, Prisons na Toto African.
Timu za Simba, Yanga na Azam, ambazo zinafundishwa na makocha wa kigeni, ndizo pekee zilizofanya vizuri na kushika nafasi tatu za kwanza. Simba inanolewa na Patrick Phiri kutoka Zambia, Yanga inanolewa na Kostadin Papic kutoka Serbia wakati Azam inanolewa na Itamar Amorin kutoka Brazil.
Kadhalika, timu zilizokuwa na wachezaji wengi wa kigeni ndizo zilizofanya vizuri katika ligi hiyo msimu huu. Simba iliwatumia Emmanuel Okwi na Joseph Owino kutoka Uganda, Hillary Echessa, Mike Baraza na Jerry Santo kutoka Kenya.
Wachezaji wa kigeni walioichezea Yanga msimu huu ni makipa Obren Curkovic (Serbia), Yaw Berko (Ghana), Robert Jama Mba (Cameroon), Wisdom Ndhlovu (Malawi), George Owino, Boniface Ambani, John Njoroge, Moses Odhiambo (Kenya), Steven Bengo (Uganda) na Honore Kabongo (DRC).
Wageni wengine waliocheza ligi ya msimu huu ni Vladimir Niyonkuru (Burundi), Ben Karama, Danny Wagaruka na Ibrahim Shikanda kutoka Uganda, waliosajiliwa na Azam FC, Mike Katende na Robert Ssentongo kutoka Uganda waliosajiliwa na African Lyon.
Pamoja na kuwepo kwa wanasoka wengi wa kigeni, ni wachache walioweza kuziletea mafanikio timu zao. Hao ni Okwi, Echessa na Owino wa Simba, makipa Curkovic wa Yanga na Niyonkuru wa Azam.
Baadhi ya wachezaji kama vile Robert Mba, Owino, Bengo, Kabongo, Njoroge, Ambani na Ndhlovu, ambao walisajiliwa kwa fedha nyingi na Yanga, walionekana kuwa mzigo kwa klabu hiyo na tayari Kocha Papic ameshatamka wazi kuwa, atawaacha kwenye usajili wa msimu ujao.
Japokuwa ligi ya msimu huu ilikuwa na ushindani mkali kutokana na timu nyingi kupania kutwaa ubingwa, zilijitokeza dosari kadhaa, ikiwa ni pamoja na uamuzi mbovu.
Katika baadhi ya mechi, waamuzi na wasaidizi wao walishindwa kutafsiri vyema sheria 17 za mchezo huo na wengine walichezesha kwa upendeleo, hatua iliyosababisha wafungiwe na kuondolewa kwenye orodha ya waamuzi wa ligi hiyo.
Baadhi ya timu zililazimika kutimua makocha wake kutokana na mwenendo mbovu katika ligi. Makocha walioonja adha hiyo ni pamoja na Abdalla Kibadeni wa Manyema, George Ssemogerere wa Kagera Sugar, Kenny Mwaisabula wa Majimaji, Dusan Kondic wa Yanga, Mbwana Makata wa Toto African, Fred Felix Minziro wa Moro United na Eduardo Almeider wa African Lyon.
Kwa mara ya kwanza katika historia ya ligi hiyo, kanuni za mashindano za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) zilikuwa zikijikanganya na kusababisha kutofautiana kwa maamuzi kati ya kamati ya mashindano na kamati ya nidhamu.
Kila kamati ya mashindano ilipotoa adhabu kwa timu ama wachezaji walioonyesha vitendo vya utovu wa nidhamu, kamati ya nidhamu ilitengua maamuzi hayo baada ya kupokea rufani na kuifanya kamati ya mashindano ionekane kama vile haitambui majukumu yake.
Msuguano kati ya kamati hizo mbili ulisababisha Makamu wa Pili wa Rais wa TFF, Nassib Ramadhani, ambaye ndiye mwenyekiti wa kamati ya mashindano, atoe malalamiko dhidi ya kamati ya nidhamuakidai kwamba maamuzi yake yamekuwa yakiidhalilisha kamati anayoiongoza.
Dosari nyingine iliyojitokeza katika ligi hiyo msimu huu ni kuuzwa kwa wachezaji katikati ya ligi. Hali hii ilisababisha timu nyingi kudhoofika kutokana na wachezaji wake nyota kuuzwa nje.
Kusimama kwa ligi kwa muda mrefu baada ya kumalizika kwa mechi za mzunguko wa kwanza na pia ligi kusimama ili kupisha mechi za timu ya taifa, Taifa Stars nako kulipunguza ushindani na msisimko wa ligi hiyo.
Mzunguko wa kwanza ulimalizika Novemba 15 mwaka jana wakati mzunguko wa pili ulianza Januari 16 mwaka huu. Hali hii ilisababisha baadhi ya wachezaji wajisahau kwamba wapo kwenye mashindano na ushindani kwa timu kupungua, tofauti na mzunguko wa kwanza.
Dosari nyingine iliyojitokeza katika ligi hiyo ni wizi wa mapato ya mechi za ligi. Kutokana na kukithiri kwa wizi huo, tayari baadhi ya watendaji wa TFF na viongozi wa klabu kubwa wameshakamatwa na polisi na kufikishwa mahakamani kwa tuhuma hizo.

PHIRI AWAFUNIKA MAKOCHA WENZAKE LIGI KUU

KOSTADIN Papic
PATRICH Phiri

Na Fred Majaliwa
SAFARI ndefu ya kusakwa timu bingwa katika Ligi Kuu ya Vodacom msimu wa 2009/2010 ilifika tamati jana, huku Simba ikitwaa kombe ikisaliwa na mechi mbili mkononi.
Mabingwa hao walikabidhiwa kombe hilo Jumapili iliyopita katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, kwa shangwe nyingi baada ya kufanikiwa kuisambaratisha Yanga kwa mabao 4-3 katika mechi iliyokuwa ya kuelekea kukamilisha ratiba.
Timu zote zilimaliza mechi za ligi kuu jana kwa kushuka katika viwanja tofauti, lakini hadi kufika hatua hiyo kuna makocha walioonyesha kiwango kupitia timu zao na wengine walidorora na kujikuta wamefukuzwa.
PATRICK PHIRI


Ni kocha wa Simba aliyepata mafanikio yasiyo na mfano kutokana na kuipa ubingwa timu hiyo bila ya kupoteza mechi hata moja.


Simba hadi inatwaa kombe la Vodacom, ilishinda mechi 18 na kutoka sare mara mbili.Ilisaliwa na mechi mbili ambazo ni dhidi ya Yanga na Mtibwa iliyochezwa jana, na japokuwa Phiri katika michezo hiyo hakuwepo kutokana na kwenda kwao Zambia kuzungumza na Chama cha Soka cha huko (FAZ) kuhusu kukabidhiwa mikoba ya timu ya taifa ‘Chipolopolo’, pasipo pingamizi anastahili kuwa kocha bora.


Kuiongoza Simba kushinda mechi 11 za mzunguko wa kwanza bila ya kufungwa, kigezo kimojawapo cha kuleta ushawishi kocha huyo alambe tuzo hiyo, pia kutwaa ubingwa timu ikibakiwa na mechi mbili za kumaliza ligi, kunatosha kumfanya Phiri kuwa kocha bora.


Mshambuliaji Mussa Hassan ‘Mgosi’ wa timu hiyo amekuwa anaongoza kwa ufungaji mabao katika ligi kuu ya msimu huu akichuana na nyota wa Yanga Mrisho Ngasa na John Boko ‘Adebayor’ wa Azam, ni ushawishi mwingine wa kutazama mafanikio yake katika timu za ligi kuu.


Mgosi ana mabao 16, Ngasa na Adebayor wana magoli 14 kila mmoja. Pia Kaseja ndiye golikipa pekee aliyecheza mechi nyingi za Simba na kufungwa mabao machache. Ametunguliwa mara 12.Ingawa hayo ni mafanikio ya wachezaji binafsi, Phiri hawezi kuwekwa kando kwa kuwa ndiye kocha wa Simba aliyefundisha kikosi kizima ambacho kilitandaza soka ya uhakika uwanjani.


Ni wazi akiondoka kwenye timu hiyo ataacha pigo kubwa kwa sababu hata mashindano ya Kombe la Shirikisho wanayocheza Simba mwaka huu na kung’ara baada ya kuitoa Lengthens ya Zimbabwe katika raundi ya kwanza yamechangiwa na ufundi wake, ambapo alikuja msimu wa 2008/2009 timu ikiwa nafasi ya sita na aliikwamua hadi ya pili, nyuma ya Yanga.
KOSTADIN PAPIC


Inawezekana alikubalika haraka kwa wachezaji au walishika vyema mafunzo yake baada ya kikosi cha Yanga kuonyesha mabadiliko makubwa uwanjani katika muda mfupi kinyume ilivyotarajiwa na wengi.


Baada ya kukabidhiwa mikoba na Dusan Kondic aliyefukuzwa kutokana na kuvurunda baadhi ya mechi za mwanzoni mwa ligi kuu, mtihani wake wa kwanza ulikuwa katika mechi ngumu ya watani wa jadi, Simba na Yanga Oktoba 31 mwaka jana.


Licha ya kulazwa bao 1-0, wachezaji wote walisakata kandanda vizuri hali iliyoleta matumaini mapya kwa mashabiki na wanachama wa klabu hiyo ya Jangwani kuwa timu imeiva.Chini ya Kondic Yanga haikuwa na ‘jeuri’ ya kupiga migongeo hata sita mfululizo, wachezaji walikuwa wanakimbiza mpira na kutumia nguvu kubwa kusaka ushindi, lakini Papic alipofika alikataa uchezaji huo na kufundisha upigaji pasi ili kumiliki mpira na kufunga mabao ya malengo.


Mechi za mzunguko wa kwanza si kipimo sahihi cha kutosheleza kupima uwezo wake katika makocha walioongoza timu za ligi kuu msimu huu kutokana na kufika wakati timu ilikuwa chini Kondic na ilishaanza kupoteza mwelekeo mapema, lakini anastahili kupimwa raundi ya pili.


Katika hatua hiyo ameng’ara kwa kuigandisha Yanga katika nafasi ya pili iliyokuwa inawaniwa pia na Azam kwa nyakati tofauti. Katika mechi 10 za raundi ya pili, ameiongoza timu hiyo kushinda mechi 10 na kufungwa moja dhidi ya Simba.


Alimaliza jukumu lake jana kwa kucheza na Prisons Mbeya.Yanga kubadilishana na Simba katika mashindano ya kimataifa mwakani kwa maana yenyewe kucheza Kombe la Shirikisho na mabingwa hao kucheza Ligi ya Mabingwa Afrika, ambayo mwaka huu walicheza watoto wa Jangwani na kutolewa na Lupopo, bado kunamfanya asitoke kwenye orodha ya makocha waliofanya vizuri msimu huu, japokuwa alikuja wakati ligi imeshaanza kutimua vumbi.


Papic kama atakuwepo Yanga katika msimu ujao timu hiyo inaweza kufanya makubwa zaidi kwa kuwa atapata muda wa kutosha kusajili wachezaji anaowataka na kuwaondoa wasiokuwa na mchango kwa timu hiyo.


Mara nyingi kocha huyo amekuwa anasema nyota wa kulipwa kama Robert Mba, Kabongo Honore na Steven Bengo, Obren Circovic, Wisdom Ndhlovu na wengineo wasiokuwa na manufaa kwa timu waondoke. Kama uongozi utampa ushirikiano katika kufanya mabadiliko mbalimbali kwenye timu ana nafasi ya kufanya maajabu msimu ujao.
SALUM MAYANGA


Si vibaya kumuita kocha kijana aliyemudu kutoa upinzani katika ligi kuu ya msimu huu licha ya kushindwa kutimiza malengo aliyokusudia ya kutwaa ubingwa.


Akisaidiwa na aliyekuwa mlinzi wa kulia wa timu hiyo Mecky Maxime katika kuliongoza benchi la ufundi la Mtibwa baada ya mchezaji huyo kustaafu mwaka juzi, Mayanga amehimili purukushani za ligi hiyo hadi kushika nafasi ya tatu.


Mtibwa ya Turiani, Morogoro, katika mechi 21 ilizocheza imevuna pointi 33 baada ya kushinda mechi tisa, sare sita na kufungwa michezo ya idadi hiyo.


Kocha huyo kama ataachwa aendelee kushusha programu zake za kufundisha katika timu hiyo anaweza kuivika Mtibwa Sugar taji la Vodacom, lakini atafanikiwa hilo endapo atapewa ‘fuko’ la fedha za kutosha kufanya usajili wa nguvu.


Mayanga anakabiliwa na changamoto ya kusajili wachezaji wapya na wenye ari ya soka na kuwapumzisha baadhi ya wakongwe ambao hawaendani na kasi ya mchezo wa mpira wa miguu kwa sasa.


Zuberi Katwila na Moja Liseki ni miongoni mwa wachezaji wanaotakiwa kukaa kando kupisha vijana wa kumsaidia kocha huyo kuwapa uhondo wa furaha wakata miwa wa Manungu, Mayanga aliyecheza mpira Mtibwa Sugar hadi kusomea ukocha akiwa hapo, akipewa nafasi atashangaza timu nyingi za ligi kuu na mashindano mengine.
ITAMAR AMORIN


Kocha mwingine wa kigeni aliyeonyesha akiwezeshwa anaweza kama alivyodhihirisha hivyo katika timu ya Azam FC, ambayo licha ya kupungua makali katika mzunguko wa pili ameifikisha nafasi ya nne msimu huu.


Azam ilimaliza ligi kwa kuchuana na Manyema Rangers jana, lakini kusua sua katika baadhi ya mechi za raundi ya pili hakutokani na wachezaji kucheza chini ya kiwango bali ugumu wa ligi hiyo, ambayo kila timu ilikuwa inakwepa kushuka daraja.


Kocha huyo aliiweka Yanga roho juu katika mbio ya nafasi ya pili kufuatia Azam kuing’ang’ania na kumaliza ligi wakiwa nyuma ya vinara Simba na Jangwani wakibaki nyuma ya lamba lamba hao.


Amorin alionyesha kila dalili kuwa ataipa Azam tiketi ya kucheza mashindano ya kimataifa mwakani, lakini kukwama katika baadhi ya mechi kwenye mzunguko wa pili kulimwangusha na kutoa mwanya kwa Yanga kuchukua nafasi hiyo kutokana na kurudi na kasi mpya ya kushinda kila mechi.


Ana wachezaji wazuri na kama timu hiyo itamaliza ligi ikiwa ya tatu au ya nne atapaswa kupongezwa kutokana na Azam kuwa na wachezaji mahiri na waliong’ara kwenye ligi hiyo kama John Boko aliyekuwa anachuana na kina Mgosi na Ngasa katika vita ya kuwania kiatu cha mfungaji bora msimu huu.


Mabao 14 aliyofunga Boko ni heshima kwa timu na kocha huyo na mbinu anazopewa mchezaji huyo mrefu na Amaron zimechangia awe mali hata machoni mwa kocha wa timu ya taifa, Taifa Stars, Marcio Maximo na kumuita katika baadhi ya mechi.


Timu yake ilikuwa inacheza mpira wa kuvutia uwanjani na kuzipa hofu timu vigogo za Simba na Yanga, ambapo kocha huyo kijana kama alivyo Mayanga msimu ujao akipewa nafasi ya kuongeza mabadiliko kikosini mwake, haitashangaza kuona Azam wanawalamba wapinzani wao katika kila mechi.


Tangu alipokabidhiwa timu hiyo msimu wa 2008/2009 alionyesha mabadiliko makubwa katika timu kutofautisha na Mbrazil mwenzake Neider dos Santos pamoja na msaidizi wake mzalendo Sylvester Marsh ambao walishindwa kuipa mafanikio timu hiyo kiasi cha kunusurika kushuka daraja.Bado ana nuru ya kuifikisha Azam kwenye kilele cha mafanikio kwa siku za usoni.
CHARLES KILINDA


Msimu huu wachezaji wake wameendelea kuchechemea kama ilivyokuwa katika mzunguko wa kwanza ambao JKT Ruvu walimaliza wakiwa nafasi ya sita, japokuwa kabla ya mechi ya jana dhidi ya African Lyon walikuwa wa tano katika msimamo.


Sifa na heshima ya timu hiyo imeporomoka katika msimu huu kufuatia kubebeshwa mabao mengi katika mechi tisa walizopoteza na kabla ya mechi ya mwisho ya jana, JKT ilikuwa imebamizwa jumla ya mabao 28 huku ikishinda 26.


Ladha ya soka ya maafande hao waliocheza vyema msimu wa 2008/2009 chini ya Kilinda msimu huu haikuonekana kabisa, lakini tatizo la majeruhi linaweza kuwa kikwazo kwa kocha huyo aliyewahi kucheza katika timu ya Yanga miaka ya nyuma.


Katika baadhi ya mechi za mzunguko wa kwanza Kilinda alisema majeruhi waliharibu malengo yake na katika mzunguko wa pili walikuwa nyanya zaidi kwa kupoteza mechi nyingi.Huenda mazoea ya kukaa miaka mingi na wachezaji bila ya kuwaondoa au kuongeza damu changa nyingine kama walivyofanya kwa Kazimoto, imechangia kikosi hicho kuyumba katika ligi hiyo iliyokuwa na ushindani mkubwa.


Kilinda hajafanya vibaya sana kiasi cha kutajwa hafai isipokuwa anatakiwa kufanya mabadiliko makubwa ya wachezaji kwa nia ya kuleta nguvu mpya, lakini itapendeza naye akitazama programu zake kwa nini hazikuzaa matunda kama ilivyokuwa msimu uliopita?
CHARLES MKWASA


Amefanya kazi nzuri ya kuinusuru African Lyon kushuka daraja baada ya kukabidhiwa timu ikiwa katika hali ngumu. Ilimaliza mechi za mzunguko wa kwanza ikiwa na pointi saba na ilikuwa ya pili kutoka mkiani.


Mkwasa japokuwa kuna kipindi alikuwa na jukumu la kuinoa timu ya taifa ya wanawake ‘Twiga Stars’, chini ya kocha msaidizi Seleman Matola timu hiyo iliendelea kusaka pointi za kuibakisha ligi huu na kufanikiwa katika hilo.


Kwa sasa ina pointi 24 ambazo zimewahakikishia kutoshuka daraja na kama Mkwasa atabaki au ataondoka kama mwenyewe alivyowahi kunukuliwa kuwa alisaini mkataba wa muda mfupi ambao utafika tamati baada ya ligi kumalizika, msimu ujao timu hiyo inatakiwa kufanya marekebisho kikosini.


Japokuwa uwepo wa kipa Ivo Mapunda aliyesajiliwa wakati wa dirisha dogo na kuwepo Vicent Barnabas, Meshack Abel na Anthony Matangalu waliotua kwa mkopo kutoka Simba na Yanga, kumeipa timu hiyo uhai katika mzunguko wa pili, suala la kupatikana kocha bora linapaswa kutazamwa kwa umakini.
MRAGE KABANGE


Sifa zake hazipishani na Mkwasa baada ya kukabidhiwa timu ya Kagera Sugar ikiwa taabani katika raundi ya kwanza, lakini alitumia ujuzi wake wote kuipa pointi na hatimaye kuiokoa kushuka daraja.


Wapenda soka wengi walitarajia Kagera ingeshuka kutokana na kupoteza mechi nyingi katika mzunguko wa kwanza na ilizinduka katika michezo ya raundi ya pili baada ya kufukuzwa kocha George Semogerere raia wa Uganda na jahazi lote kukabidhiwa Kabange.


Akizungumzia sababu ya kufukuzwa baadhi ya makocha katika timu hiyo, Kabange anasema si suala la kushangaza kwa kuwa kipimo cha mwalimu wa timu ya mpira wa miguu ni timu kufanya vizuri.Amesema hata yeye haitakuwa ajabu kuondolewa Kagera aliyopewa ubosi baada ya kupigwa chini Semogerere aliyewahi kucheza soka kwa mafanikio katika timu ya Sports Club Villa na timu ya taifa ya Uganda ‘The Cranes’.


Kocha huyo ameonyesha ana uwezo wa kuiongoza tena timu hiyo kwa msimu ujao kama atafanya usajili wa kurekebisha baadhi ya mapengo katika kikosi hicho na kwa kuibakisha ligi kuu anastahili sifa.
JUMA MWAMBUSI


Ujiko aliojipatia wakati alipokuwa Prisons ya Mbeya msimu wa 2007/2008 umepotea akiwa katika Moro United kutokana na timu hiyo kushuka daraja.Kocha huyo alishuhudia jahazi hilo likishuka daraja kwa kufungwa katika mechi nyingi na chache kuambulia sare. Ingawa, inasemekana aliondoka wakati timu hiyo ikibakiwa na michezo michache, hakwepi matokeo mabaya yaliyoikumba Moro United.Japokuwa kushuka kwa Moro kunaweza kusichafue sifa yake moja kwa moja, katika historia yake kamwe hatasahau kama kuna timu ilishuka ikiwa mikononi mwake na baadaye ataweza kufanya vizuri akiwa na timu hiyo au nyingine.
MAKOCHA WALIOFUKUZWA
EDUARDO ALMEIDA


Baada ya kuahidi kufanya mambo makubwa katika timu hiyo alipozungumza na waandishi wa habari pembeni yake akiwepo mmiliki wa klabu hiyo, Mohamed Dewji ‘Mo’, kocha huyo alifukuzwa baada ya mechi tano tu za raundi ya kwanza kutokana na ‘kuijaza maji’ boti ya Lyon.Kabla ya kufukuzwa Mreno huyo alishushwa cheo kwa kuwa kocha msaidizi wa mzawa Jumanne Chale, ambaye naye alitupiwa virago na kazi hiyo kupewa Mkwasa na Matola.Pamoja na Almeida kutoswa kabla meli haijazama, Lyon ilikosa mafanikio katika ligi na kujikuta ipo nafasi ya pili kutoka mkiani ikiwa na pointi saba katika mechi 11 ilizocheza.
AHMED MUMBA/ DAVID MWAMAJA


Mumba ndiye alikuwa kocha mkuu wa Majimaji ilipopanda Ligi Kuu msimu huu, lakini baada ya timu hiyo kupigwa mawimbi makali kwa kupoteza baadhi ya mechi mapema, alijikuta katika wakati mgumu.Licha ya kuitoa Yanga machozi kwa kuitandika bao 1-0 katika mechi ya pili ya Ligi Kuu na kupoza machungu ya kulizwa na Simba nyumbani kwao, mashabiki wa timu hiyo mjini Songea walisahau mazuri yake.Walimbeza kuwa hana uwezo kutokana na kufungwa mechi kadhaa nyumbani na ugenini, ambapo kelele hizo zilimnyima raha Mumba na kuahidi kushinda mechi zilizokuwa mbele yake, lakini mwisho wa siku aliwekwa kando katika ukocha na nafasi yake kupewa David Mwamaja.Mwamaja naye ametimuliwa Majimaji katika mzunguko wa pili kutokana na sababu ambazo hazikuwekwa wazi, lakini vipigo kutoka kwa Azam na Yanga huenda vilichangia aonyeshwe mlango wa kutokea na timu kubaki kwa kocha msaidizi Peter Mhina.
HASSANI MLILWO


Ni ofisa wa Jeshi la Magereza aliyepewa ukocha mkuu wa Tanzania Prisons ili kumuongezea nguvu James Nestory.Uwepo wake katika timu hiyo ulishindwa kufua dafu hasa katika michuano ya klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati iliyochezwa nchini Sudan mwaka jana na kujikuta wanaaga mapema.Chini ya Mlwilo na Nestory aliyewahi kuichezea Prisons kabla ya kustaafu, Prisons pia imekuwa nyanya katika ligi kuu ya Vodacom.Uongozi wa Prisons ulimtema Mlwilo na kukabidhi kikosi kwa Danny Koroso, lakini naye inadaiwa aling’olewa na timu kubaki kwa Nestory. Ilimaliza ligi jana kwa kucheza na Yanga ushujaa wa ‘kaimu’ huyo utatokana na timu kunusurika kushuka daraja na vinginevyo atakuwa ameshindwa kuonyesha cheche katika kazi ya ukocha kwa vile timu itashuka akishuhudia. Kabla ya kucheza na Yanga Prisons ilikuwa na pointi 20 na iligota kwenye nafasi ya 11 katika msimamo wa ligi kuu.
MBWANA MAKATA


Alikuwa kocha wa Toto African ya Mwanza, ambayo huenda kushindwa kwa timu hiyo kupiga makasia yao vyema kwenye ligi kuu kulichangia atoweke kabla ya kuambiwa aondoke.Makata alisikika katika vyombo vya habari akisema kuwa alirudi Dar es Salaam kujiuguza kwa kuwa afya yake si nzuri na hakuonekana tena kwenye jiji la Mwanza kuendelea na kazi yake hivyo kuwa amekimbia balaa mapema. Kocha msaidizi Choki Abeid ndiye aliyebaki na Toto.
DUSAN KONDIC


Mserbia huyo alifunga dimba katika orodha ya makocha waliong’olewa katika mzunguko wa kwanza wa ligi kuu, lakini katika raundi ya pili alipata wenzake wa kuondoka nao. Kocha huyo licha ya kuipa Yanga ubingwa wa ligi kuu mara mbili mfululizo, alitupiwa virago baada ya mzunguko wa kwanza wa ligi ya msimu huu kuanza kwa kusuasua hali iliyosababisha hata ipote taji kabisa ambalo limechukuliwa na Simba.Nafasi ya Kondic ilichukuliwa na Mserbia mwenzake Kostadin Papic.
ABDALLAH KIBADENI


Uongozi wa Manyema Rangers ulimtimua baada ya kushindwa kuipa timu ushindi katika mechi tatu alizokuwa masharti kuwa lazima ashinde ili kuiepusha timu na janga la kushuka daraja.Aliwaongoza vizuri Manyema katika mzunguko wa kwanza na hatua ya pili akajikuta anashindwa kazi na hivyo kuwekwa pembeni kwa kipimo cha mafanikio aliyoshindwa kutimiza kama ilivyokuwa inatarajiwa na uongozi wa klabu hiyo.
GEORGE SEMOGERERE


Mchezaji huyo wa zamani wa timu ya taifa ya Uganda ‘The Cranes’ alifukuzwa baada ya duru la kwanza kumalizika kutokana na kuiweka Kagera Sugar katika kona hatari ya kung’oka ligi kuu msimu huu.Timu hiyo ilimaliza mzunguko wa kwanza ikiwa na pointi 12 tu na ndipo wamiliki wa Kagera wakamwambia akae kando na nafasi hiyo kupewa msaidizi wake Mrage Kabange aliyejitahidi kurejesha uhai wa timu hadi kufanikiwa kubaki ligi kuu ya msimu ujao.

TFF: Ligi Kuu Bara imetufundisha mengi


RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Leodegar Tenga (kushoto) akiwa na Katibu Mkuu wake, Fredrick Mwakalebela.

Na Athanas Kazige
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limesema michuano ya ligi kuu ya Vodacom msimu huu ilikuwa mizuri na yenye ushindani, ikilinganishwa na ligi za miaka mitatu iliyopita.
Akizungumza na Burudani mjini Dar es Salaam juzi, Katibu Mkuu wa TFF, Fredrick Mwakalebela alisema ligi hiyo imetoa mafunzo mengi kwa shirikisho lake kuhusu namna ya kuiboresha zaidi.
"Hii ligi ilikuwa nzuri na timu nyingi zilipania kufanya vizuri na tumejifunza mambo mengi, ikiwemo kubaini kasoro mbalimbali na tutahakikisha tunawabana waamuzi ili waweze kutenda haki katika michuano ya msimu ujao," alisema Mwakalebela.
Katibu Mkuu huyo wa TFF alisema moja ya kasoro kubwa zilizojitokeza katika ligi hiyo msimu huu ni kushindwa kwa waamuzi kuzitafsiri vyema sheria 17 za soka.
Alisema waamuzi wa aina hiyo wamekuwa kikwazo kwa maendeleo ya soka nchini kutokana na kuchezesha mechi kwa upendeleo au kwa kutojua sheria za mchezo huo.
“Ni kweli wapo baadhi ya waamuzi ambao kwa makusudi wamekuwa wakichezesha mechi kwa upendeleo na wengine wanashindwa kuzitafsiri vyema sheria za soka. Hili ni jambo baya katika soka na tutakuwa makini sana msimu ujao,”alisema.
Mwakalebela alisema katika kupambana na tatizo hilo, shirikisho lake limeamua kuanzisha kitengo maalumu cha kufuatilia nyendo za waamuzi pamoja na uchezeshaji wao ili kuwabaini wenye tabia hiyo chafu.
“Hatuwezi kukaa tu na kulalamikia uchezeshaji mbovu wa waamuzi wetu. Tumeamua kuchukua hatua na kwanza kuanzia, tumeanzisha kitengo hiki kwa ajili ya kudhibiti tabia hiyo,”alisema.
Alisema kitengo hicho kinaundwa na baadhi ya maofisa wa TFF, ambao watakuwa wakienda mikoani kutazama mechi za ligi bila kufahamika na waamuzi, makamisaa na klabu husika.
Mbali na kuunda kitengo hicho, Mwakalebela alisema wamekuwa wakizifanyia kazi kwa umakini ripoti za makamisaa kuhusu mechi mbalimbali na kuwachukulia hatua wahusika pale inapobainika kwamba hawakutenda haki.
Hata hivyo, Mwakalebela alikiri kuwa utekezaji wa kazi hizo ulikuwa mgumu msimu huu kutokana na baadhi ya watendaji kushindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo. Alisema ana imani kutakuwa na mabadiliko makubwa msimu ujao.
“Lengo letu ni kuhakikisha kuwa, kazi ya kuwabaini waamuzi wabovu inafanyika bila kikwazo ili ligi iweze kuendeshwa kwa haki na washindi wapatikane kutokana na uwezo wao,”alisema.
Mwakalebela alisema umakini wa baadhi ya watendaji wao uliiwezesha TFF kuwafungia waamuzi kadhaa kwa makosa ya kupokea rushwa na kukiuka sheria za mchezo huo.
“Kama utakumbuka, tuliwafungia waamuzi wengi kwa makosa hayo na wengine waliondolewa kabisa kwenye ligi na hilo litaendelea hadi tutakapobaki na waamuzi wanaoheshimu na kufuata sheria,”alisema.
Mwakalebela alisema pia kuwa, shirikisho lake bado linaendelea na jitihada za kuzitafutia wadhamini timu zote zinazoshiriki kwenye ligi kuu ili ziweze kujiendesha bila matatizo.
Alisema kwa sasa, zipo baadhi ya timu, ambazo zinashiriki ligi hiyo katika mazingira magumu kutokana na kukabiliwa na ukata kwa vile fedha za udhamini zinazotolewa na Kampuni ya Simu za Mkononi ya Vodacom, hazitoshi.
Timu pekee zenye udhamini katika ligi hiyo ni Simba na Yanga zinazodhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), ambayo imekuwa ikiwalipa mishahara wachezaji, makocha na watendaji wakuu.
Zingine ni Azam FC, inayodhaminiwa na Kampuni ya SSB na African Lyon, inayodhaminiwa na Kampuni ya Mohammed Enterprises Tanzania Limited.
"Lengo letu ni kuhakikisha tunashirikiana vyema na viongozi wa klabu za ligi kuu kusaka wadhamini ili waweze kuwalipa mishahara wachezaji na makocha na kupunguza gharama. Tunafahamu timu nyingi zina hali mbaya kifedha,"alisema kiongozi huyo.
Amewataka viongozi wa klabu za ligi kuu wasibweteke na kuitegemea TFF ifanye kazi hiyo, badala yake, wajitahidi kuzishawishi kampuni mbalimbali zizidhamini timu zao ili zipate nafasi ya kujitangaza kibiashara.
Hata hivyo, Mwakalebela amewaonya viongozi wa klabu hizo kuwa, wawe makini na udhamini watakaoupata na waweke wazi ripoti za mapato na matumizi ya klabu kila mwaka.
"Unajua hakuna mtu ambaye anapenda kutoa pesa yake bila ya kunufaika, lakini hapa jambo la msingi ni kwamba inabidi viongozi wa klabu waweke mazingira ya uwazi ili kuwavutia wafadhili,"alisema Katibu huyo ambaye anakaribia kumaliza mkataba wake ndani ya TFF.
Alisema kuwa viongozi wa klabu za ligi kuu wamekuwa wakipatwa na wakati mgumu kutokana na baadhi ya pesa wanazopewa na Vodacom kutokidhi mahitaji yao.
"Baadhi ya timu zina madeni mengi, hiyo yote ni kutokana na pesa zinazotolewa na Vodacom kushindwa kutosheleza mahitaji ya klabu kwa vile kuna gharama za usafiri na posho, hivyo tutajaribu kuwaomba wadhamini wafikirie jambo hilo,"alisema.
Kiongozi huyo wa TFF alisema pia kuwa, wamewaomba makocha wa timu za ligi kuu kuwatumia zaidi wachezaji wazalendo badala ya kusajili idadi kubwa ya wanasoka wa kigeni.
Alisema tabia ya baadhi ya timu kubwa kusajili wageni wengi, inawachukiza wanasoka wazalendo kwa sababu idadi kubwa ya wageni hao ni ‘bomu’ kutokana na uwezo wao kisoka kuwa mdogo.
Mwakalebela alisema Tanzania ina hazina kubwa ya wanasoka chipukizi wenye vipaji, lakini wanakosa nafasi ya kuonyesha uwezo wao kutokana na kutokuwepo utaratibu wa kusaka na kuibua vipaji vipya.
"Tunawaomba makocha wa ligi kuu, wajaribu kutumia mfumo wa zamani wa kusaka wachezaji kwenye michezo ya mitaani, wilayani na mikoani. Huko kuna wachezaji wengi wazuri na wenye uwezo,"alisisitiza.
Alisema binafsi amefurahishwa kuona kuwa, wanasoka wa Tanzania ndio wanaoongoza katika kuwania tuzo ya mfungaji bora wa ligi kuu msimu huu, tofauti na misimu miwili iliyopita.
Wachezaji wanaowania tuzo hiyo ni Mussa Hassan 'Mgosi' wa Simba, anayeongoza kwa kufunga mabao 16, akifuatiwa na Mrisho Ngasa wa Yanga na John Boko wa Azam waliofunga mabao 14 kila mmoja.
Amezipongeza timu za Ruvu Shooting, Polisi Dodoma na AFC Arusha kwa kufuzu kucheza ligi kuu msimu ujao na kuzitaka zifanye usajili mzuri zaidi ili ziweze kutoa ushindani.
Alisema ana imani kubwa kwamba ligi ya msimu ujao itakuwa na msisimko na ushindani mkali kwa vile kila timu imejifunza mengi kutokana na ligi ya msimu huu.
Mwakalebela alisema hawatarajii iwapo mechi za ligi ya msimu ujao zitakuwa zikipanguliwa mara kwa mara kutokana na kuingiliana na michuano ya kimataifa. Alisema watahakikisha wanapanga ratiba kulingana na michuano hiyo ili kuepuka malalamiko.
000000

Tuesday, April 20, 2010

Simba ilipoiadhiri Yanga

HIVI tutashinda kweli leo! Ni Meneja wa Simba, Innocent Njovu (kushoto) na Kocha Msaidizi, Amri Saidi walipokuwa wakijadiliana jambo kabla ya mechi kati yao na Yanga
TWENDE ukakabidhi kombe. Ndivyo inavyoelekea Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Leodegar Tenga (kushoto) akimueleza Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya.

MASHABIKI wa Simba wakifuatilia kwa makini pambano kati yao na Yanga. Simba ilishinda mabao 4-3.
WACHEZAJI Shadrack Nsajigwa (kushoto) wa Yanga na Juma Jabu (kulia) wa Simba wakigombea mpira timu hizo zilipomenyana katika mechi ya ligi kuu ya Vodacom iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

MSHAMBULIAJI Mussa Hassan 'Mgosi' (kulia) akitafuta mbinu za kumtoka kiungo Athumani Idd 'Chuji' wa Yanga timu hizo zilipomenyana katika mechi ya ligi kuu ya Vodacom iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

WACHEZAJI wa Simba wakifurahia kombe walilokabidhiwa baada ya timu hiyo kuibamiza Yanga mabao 4-3 katika mechi ya ligi kuu ya Vodacom iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

WACHEZAJI wa Simba wakipongezana baada ya timu yao kuicharaza Yanga mabao 4-3 katika mechi ya ligi kuu ya soka ya Vodacom iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam
WACHEZAJI wa Simba wakiwa wamembeba kocha wao msaidizi, Amri Saidi baada ya timu hiyo kuichapa Yanga mabao 4-3 katika mechi ya ligi kuu ya Vodacom iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Monday, April 19, 2010

Omotola akana kuwa na uhusiano na Jim Iyke



LAGOS, Nigeria

OMOTOLA Jalade ni mmoja wa waigizaji nyota na maarufu wa filamu nchini Nigeria. Baada ya kuwemo kwenye fani hiyo kwa zaidi ya miaka 13, bado nyota yake inang’ara, kama ambavyo sura yake imekuwa kivutia kikubwa kwa mashabiki wa fani hiyo.

Kila anaposhiriki kuigiza filamu yoyote, lazima iwe na mvuto. Uigizaji wake, umbile lake, sura yake ya kitoto na miondoko yake ni baadhi ya vitu vilivyomfanya awe kivutio kikubwa kwa mashabiki wa fani hiyo.

Omotola pia ni mwanamuziki. Kibao chake cha ‘Gba’, alichokirekodi miaka mitatu iliyopita kilishika chati za juu kwenye vituo vya radio na televisheni nchini Nigeria, kama ilivyokuwa kwa albamu yake ya kwanza, ambayo iliuzwa nakala nyingi kuliko za wanamuziki nyota wa nchi hiyo.

Mwigizaji huyo pia amekuwa akijihusisha na kazi mbalimbali za kujitolea. Pia ni balozi wa Umoja wa Mataifa katika masuala yanayohusu wakimbizi.

Akihojiwa na waandishi wa habari mjini Lagos hivi karibuni, Omotola alisema uamuzi wake wa kujitosa katika fani ya muziki hauna maana kwamba fani ya filamu hailipi.

“Sifanyikazi zangu kutokana na shinikizo la watu. Si kwa sababu watu wengine wanapiga muziki kama ninavyofanya mimi. Watu walio karibu na mimi watakueleza kwamba, sifanyi vitu kwa sababu watu wengine wanavifanya. Nilichogundua ni kwamba, baadhi ya watu wamekuwa wakipenda kufanya vitu vinavyofanana na nilivyovifanya. Inawezekana ni kwa sababu watu wamekuwa wakiniunga mkono,”alisema.

Omotola alisema muziki si kitu ambacho mtu anaweza kuamka na kusema anataka kukifanya. Alisema anapiga muziki kwa lengo la kueleza hisia zake. Alisema anafurahia kupiga muziki.

Hata hivyo, Omotola alisema anazipenda fani zote mbili kwa vile zinamwezesha kuwasilisha hisia zake kwa jamii. Alisema katika filamu, anaigiza kutokana na maelezo ya hadithi, lakini hadithi si yake. Lakini katika muziki, ni kitu anachopenda kukifanya, ni hadithi yake na anaandika nyimbo zake.

“Katika albamu yangu ijayo, nimeandika asilimia 50 ya nyimbo zilizomo ndani yake. Zingine,
nilihakikisha ni nyimbo ninazoweza kuelezea hadithi yangu, zikielezea hisia zangu,”alisema.

Omotola alisema ameamua kupiga zaidi muziki wa miondoko ya rock kwa sababu ni rahisi kuelezea hisia zake kuliko muziki wa miondoko ya R&B ambao ni wa taratibu zaidi.

“Nahisi kama hatua ifuatayo ya maisha yangu imeshaanza. Najiamini sasa. Siku zote nimekuwa
nikijiamini, lakini najiamini zaidi kwa sasa,”alisema.

“Kuna vitu ambavyo ningependa kuvizungumzia, lakini inaniwia vigumu kuelezea hisia zangu katika miondoko ya R&B,”aliongeza mwanadada huyo, ambaye ni mama wa watoto wane.

Omotola alisema haikuwa vigumu kwake kujitosa kwenye fani ya uigizaji filamu kwa sababu siku ya kwanza aliyofanyiwa majaribio, alifuzu na kupewa nafasi ya kuigiza.Alisema siku hiyo, alimsindikiza rafiki yake kwenda kufanya majaribio, lakini hakufaulu. Alisema wakati
wakitaka kuondoka, rafiki yake huyo alimtaka ajaribu bahati hiyo na kujikuta akifanikiwa.

Pamoja na kufaulu kwake, Omotola alisema familia yake haikuvutiwa na fani hiyo kutokana na
kuheshimika kanisani. Alisema mama yake hakumruhusu kirahisi kujitosa kwenye fani hiyo. Wakati huo, Omotola alikuwa na umri wa miaka 16.

“Mmoja wa majirani zetu ndiye aliyekwenda kwa mama na kumshawishi aniruhusu nijitose kwenye fani hiyo na kumuahidi atahakikisha hakuna kibaya kitakachonitokea,”alisema.

Omotola alisema msimamo wake kwa sasa ni kutocheza filamu holela kwa sababu inapotokea kuwa mbaya, mashabiki hawamtazami mtayarishaji, mhariri au muongozaji. Macho yao huwa kwa waigizaji.

Alisema hali hiyo ndiyo iliyomfanya awe mwangalifu na watayarishaji wa filamu na kujaribu kucheza zile ambazo kiwango chake ni cha juu. Alisema kama nzuri, hayuko tayari kuicheza.

“Wapo baadhi ya waigizaji wenzangu waliochukua uamuzi huo pia na naona fahari juu yao. Ni vigumu, lakini tunapaswa kufanya hivyo, kuongeza kiwango cha filamu zetu,”alisema.

Mwanadada huyo amekanusha madai kuwa, ana uhusiano wa kimapenzi na mwigizaji Jim Iyke na kwamba wamekuwa wakisafiri mara kwa mara nje ya nchi. Alisema tuhuma hizo hazina ukweli wowote.

Alisema binafsi hazipi uzito tuhuma za aina hiyo kwa sababu zimelenga kumwangusha kiusanii.
Alisema haelewi ni faida zipi wanazozipata watu wa aina hiyo.Lakini alikiri kuwa, tuhuma za ana hiyo zinawachafua kwa vile baadhi ya mashabiki huziamini.

Alisema inauma kuona mtu anafanyakazi kwa bidii, lakini mtu mwingine anatokea kusikojulikana na kutaka kumwangusha.

Omotola alikiri pia kuwa, ni kawaida ya wanaume kumtongoza kutokana na mwonekano wake, lakini mara wanapogundua yeye ni mtu wa aina gani, hushindwa kuendelea kufanya hivyo.

Mwigizaji huyo alisema kutingwa kwake na kazi hakumkoseshi nafasi ya kuwa pamoja na familia yake. Alisema yeye na mumewe wameifanya siku ya Jumapili kuwa maalumu kwa familia na kila mwaka wametenga siku maalumu za mapumziko, ambapo huzima simu zao na kutumia muda mwingi kuwa na watoto wao.

Alikiri pia kuwa, mafanikio yake kiusanii yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na uamuzi wake wa kuolewa mapema. Alisema kwa wengine, ndoa ni kikwazo kikubwa kwao, lakini kwake ndoa ni uhuru.

“Mama yangu ananiunga mkono kwa kila ninachokifanya. Nina uhuru wa kufanya chochote
ninachochagua,”alisema.

Omotola ni mtoto wa kwanza katika familia ya watoto watatu. Alizaliwa Lagos. Baba yake anatoka katika Jimbo la Ondo wakati mama yake anatoka Abeokuta Jimbo la Ogun.Baba yake alikuwa meneja wa klabu ya Country Ikeja ya mjini Lagos wakati mama yake alikuwa
mfanyabiashara. Baba yake alifariki mwaka 1999 wakati Omotola alipokuwa akisoma shule ya
sekondari. Mama yake alifariki mwaka 2001.