KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, April 19, 2010

ISHA MASHAUZI: Muziki wa taarab unalipa


‘MAMA nipe radhi, kuishi na watu kweli kazi, Mama nipe usia, nipe usia unifae katika dunia’.Hiyo ni baadhi ya mashairi yanayopatikana katika wimbo wa ‘Mama nipe radhi’ ulioimbwa na mwimbaji anayechipukia kwa kasi hapa nchini, Isha Ramadhani ‘Mashauzi’.
Wimbo huo wenye mashairi ya kuvutia, umelenga kutoa mafunzo mbalimbali kwa vijana kuhusumaisha na jinsi mtoto anavyotakiwa kuishi vizuri katika jamii iliyomzunguka.
Mwimbaji huyo hivi karibuni alizindua albamu yake ya kwanza, inayoitwa ‘Mama na Mwana’ katika onyesho lililofanyika kwenye ukumbi wa Travertine, Magomeni mjini Dar es Salaam.
Albamu hiyo inazo nyimbo nne,‘Maneno si mkuki’, ‘Mama nipe radhi’, ‘Kila mtu na mtuwe’ na
‘Tugawane ustarabu’.
Isha alifanya uzinduzi wa albamu hiyo, akisindikizwa na vikundi vya taarab vya Jahazi, Coast Modern Taarab, Baikoko kutoka Tanga , Hadija Kopa, Mc Babu Ayubu, Hassani Ally na Ahmed Mgeni kutoka Zanzibar Stars.

Katika onyesho hilo, mashabiki waliokuwa wamefurika ukumbini walilipuka mayowe ya kushangilia muda wote kutokana na kuguswa na mashairi ya nyimbo zilizoimbwa na mwanadada huyo.

Isha, ambaye ni mwimbaji wa kikundi cha Jahazi, alipanda jukwaani saa 7.05 usiku, akiwaamesindikizwa na mama yake mzazi, Rukia Juma na kuimba kibao cha ‘Mama nipe radhi’.

Utamu wa mashairi ya nyimbo zake, sauti yake nyororo na madoido yake anapokuwa stejini, nimiongoni mwa mambo yaliyompatia sifa kubwa mwanadada huyo na kumfanya aibuke kuwamwimbaji tishio.

Isha amekuwa mwimbaji wa kwanza chipukizi wa kike kutoa albamu yake binafsi, nje ya kundi lake la Jahazi kwa lengo la kujiongezea kipato.

Akizungumza na Burudani wakati wa onyesho hilo, Ishe alisema uamuzi wake wa kutoa albamu hiyo yenye nyimbo nne haumaanishi kwamba anataka kulipa kisogo kundi lake la Jahazi, bali anataka kujipima uwezo wake wa uimbaji.“Najua wengi wanaweza kuhisi kwamba nimehama Jahazi.

Lakini ukweli ni kwamba bado mimi ni mwimbaji wa Jahazi na sina mpango wa kuhama,”alisema.Isha alianza kujihusisha na muziki huo kutokana na kuvutiwa na uimbaji wa mama yake. Alijitosarasmi kwenye taarab mwaka 2007.

“Nilikuwa nikihusudu sana kuimba tangu nikiwa shule ya msingi ya Mnazi Mmoja. Naweza kusema kipaji changu kilianza kuonekana tangu nikiwa shule, ambako nilikuwa nikiimba kwaya,”alisema.

Kikundi chake cha kwanza kilikuwa Wazazi Culture Troupe, kilichokuwa na maskani yake Kariakoo, mjini Dar es Salaam. Anasema akiwa katika kikundi hicho, alikuwa akiimba nyimbo mbalimbali, lakini hakubahatika kurekodi nacho.

Mwishoni mwa mwaka 2007, alijiunga rasmi na kundi la Jahazi Modern Taarab ‘Wana wanakshinakshi’, linachoongozwa na mwimbaji mahiri nchini, Mzee Yusuf.

Anasema mara yake ya kwanza kupanda stejini na kuimba na kundi la Jahazi, ilikuwa kwenye onyesho lililofanyika kwenye ukumbi wa bwalo la maofisa wa polisi, Oysterbay, Dar es Salaam. Katika onyesho hilo, aliimba wimbo wa ‘Hayanifiki’.

“Kwa kweli nilijisikia faraja kubwa, sikuwa na hofu yoyote ile, mashabiki walinikubali vilivyo, si unajua mambo yangu,” alisema.

Isha anakiri kwamba, kibao cha ‘Hayanifiki’ ndicho kilichompandisha chati na kudhihirisha uwezo wake katika fani hiyo. Wimbo huo umetungwa na Mzee.

Miaka miwili baadaye, alifanikiwa kutunga wimbo wake mwenyewe, unaotambulika kwa jina la ‘Ya wenzenu midomo juu.’ Wimbo huo unapatikana kwenye albamu ya ‘VIP’, ambayo ni ya nne kwa Jahazi.

“Wimbo huo ulinifanya niwe juu, mashabiki waliupenda sana na hadi leo wanaupenda, namshukuru Mzee kwa kutunga wimbo ule, ambao ni guzo kwa mashabiki wengi,” anasema.

Mwimbaji huyo anakiri kwamba, muziki wa taarab una manufaa makubwa kwao hivi sasa, tofauti na miaka ya nyuma.

Alisema binafsi amekuwa akipata fedha za kumwezesha kuishi vizuri na kupata mahitaji menginemuhimu kutokana na muziki wa taarab.Alizitaja faida zingine alizozipata kutokana na muziki huo kuwa ni pamoja na kusafiri katika nchimbalimbali kama vile Uingereza na Arabuni.

“Hivi sasa nimenunua kiwanja kwa ajili ya kujenga nyumba na naendesha duka na kuuzavinywaji,”alisema.

Aliwataja waimbaji taarab wanaomvutia kuwa ni pamoja na mama yake, Rukia na Mzee kutokana na tungo zao maridhawa pamoja na sauti yenye mvuto.Amewataka wasanii wa muziki huo kupendana na kufanyakazi kwa ushirikiano ili waweze kupiga hatua zaidi kimaendeleo.

Mwimbaji huyo alizaliwa Februari 3, 1982 mkoani Mwanza na ni mtoto wa kwanza kati ya watoto watano katika familia yake.Alisoma shule ya msingi Mnazi Mmoja, Dar es Salaam kuanzia mwaka 1990 hadi 1996 alipomaliza darasa la saba.

Licha ya kuchaguliwa kuendelea na masomo ya sekondari, alijikuta akiishia kidato cha pili shuleni hapo kutokana na matatizo mbalimbali.Isha, ambaye ni mwenyeji wa mkoa wa Mara, hivi sasa ameolewa na ana watoto wawili. Anaishi na familia yake maeneo ya Tandale, Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment