KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, November 30, 2011

Shakur aipiga jeki Uhuru SC



MFANYABIASHARA Shakur Sanya ameipatia klabu ya michezo ya Uhuru vifaa vya michezo kwa ajili ya timu yake ya soka.
Shakur, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Mipango, Uchumi na Fedha ya CCM Kata ya Jangwani, alikabidhi vifaa hivyo juzi kwa Katibu wa klabu ya Uhuru, Rashid Zahor.
Vifaa vilivyotolewa na Shakur kwa klabu ya Uhuru ni seti moja ya jezi na mipira mitatu, vyote vikiwa na thamani ya sh. 500,000.
Hafla ya kukabidhi vifaa hivyo, ambayo ilifanyika kwenye ofisi za Shakur, mtaa wa Mafia, Dar es Salaam, pia ilihudhuriwa na nahodha wa timu ya soka ya Uhuru, Mussa Hassan.
Akizungumza wakati wa kukabidhi vifaa hivyo, Shakur alisema ameamua kutoa msaada huo kwa lengo la kuiimarisha timu ya Uhuru.
“Msaada huu pia ni utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, ambayo inasisitiza umuhimu wa kuibua vipaji vya michezo na kuviendeleza,”alisema.
Shakur alisema msaada huo ni wa mwanzo kwake kwa Uhuru, lakini hautakuwa wa mwisho, hivyo ameahidi kuendelea kuisaidia kila itakapohitaji msaada kutoka kwake.
“Ninayo taarifa kwamba timu yenu imekuwa ikisafiri mara kwa mara mikoani kucheza mechi za kirafiki na hivi karibuni mnatarajia kwenda Arusha, nitajitahidi katika siku zijazo kuendelea kuwasaidia,”alisema.
Kwa upande wake, Zahor alimshukuru Shakur kwa kuwapatia msaada huo wa vifaa vya michezo na kuahidi kuwa, watautumia kwa malengo yaliyokusudiwa.
Alisema msaada huo umekuja wakati mwafaka kwa timu yake kwa vile wamepanga kucheza mechi kadhaa za kirafiki kwa ajili ya kujiandaa na michuano ya Kombe la NSSF.
Uhuru ilitwaa kombe hilo mara mbili mfululizo mwaka 2007 na 2008 na mwaka 2009 ilishika nafasi ya pili wakati mwaka jana ilishika nafasi ya tatu. Timu ya netiboli nayo ilitwaa kombe hilo mwaka 2007.
Klabu ya michezo ya Uhuru pia imewahi kutwaa ubingwa wa jumla wa bonanza la vyombo vya habari mwaka 2010 na 2009.
Klabu ya Uhuru inaundwa na wafanyakazi wa Kampuni ya Uhuru Publications Ltd, wachapishaji wa magazeti ya Uhuru, Mzalendo na Burudani, kituo cha Radio cha Uhuru FM na ofisi ndogo ya CCM.

No comments:

Post a Comment