KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, December 11, 2017

PAPII KOCHA AANGUA KILIO BAADA YA KUPATA TAARIFA ZA KUACHIWA HURU



MWANAMUZIKI Johnson Nguza (Papii Kocha), jana, aliangua kilio cha furaha, baada ya kupata taarifa za kuachiwa huru kutokana na agizo la Rais Dk. John Magufuli.
Papii na baba yake, Nguza Vicking (Babu Seya), ni miongoni mwa wafungwa walionufaika na msamaha wa Rais Magufuli, alioutangaza jana, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 56 ya uhuru wa Tanzania Bara.
Rais Magufuli alitangaza kutoa msamaha kwa wafungwa 61, waliohukumiwa adhabu ya kifo na kuwaachilia huru Babu Seya na mwanawe, Papii Kocha.
Wanamuziki hao walihukumiwa kifungo cha maisha gerezani na Mahakama Kuu, mwaka 2004, baada ya kupatikana na hatia ya kubaka na kulawiti wasichana 10, wa shule ya Msingi Mashujaa, iliyoko wilayani Kinondoni, Dar es Salaam.
Hukumu hiyo ilizua hisia tofauti miongoni mwa Watanzania huku idadi kubwa ya wananchi wakiamini kuwa, wanamuziki hao hawakuhusika na tukio hilo.
Kufuatia kupewa hukumu hiyo, wanamuziki hao waliamua kukata rufani, lakini Novemba 21, mwaka 2013, Mahakama ya Rufaa ilitupilia mbali ombi lao la kuitaka ifanye marejeo ya uamuzi wake wa awali wa kuwapata na hatia, kama ambavyo hukumu dhidi yao ilivyotolewa.
Mahakama hiyo baada ya kufanya mapitio, ikiwa imeketi chini ya majaji watatu, iliamua warufani hao wawili wana hatia, hivyo waendelee kutumikia adhabu yao.
Akitumia Ibara ya 45 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inayotoa mamlaka kwa Rais kutoa msamaha kwa wafungwa, Rais Dk. Magufuli alitangaza kutoa msamaha kwa Babu Seya na mwanaye, kwenye sherehe za miaka 56 ya uhuru wa Tanzania Bara, zilizofanyika katika Uwanja wa Jamhuri mjini hapa.
“Sisi sote ni binadamu na hata mimi huwa namuomba Mungu anisamehe, ingawa sisi wanadamu ni wagumu kusamehe. Hivyo natangaza msamaha kwa familia ya Nguza Viking, maarufu kama Babu Seya na watoke leo,” alisisitiza Rais Magufuli huku akishangiliwa na umati wa watu waliohudhuria sherehe hizo.
Kuhusu wafungwa 61, waliohukumiwa adhabu ya kifo, Rais Magufuli alitangaza kuwasamehe kutokana na kukaa gerezani kwa miaka mingi.
Alisema baada ya kufanyika uchunguzi, imegundulika wafungwa hao wamejutia makosa yao kwa kiasi kikubwa na wamejirekebisha.
“Yupo mtu alifungwa akiwa na miaka 18. Sasa ana umri wa miaka 60, akiwa gerezani. Mwingine Mganga Matonya mwenye umri wa miaka 87, ambaye amekaa gerezani kwa miaka 44.
“Nitamkabidhi Waziri Mkuu orodha ya wafungwa wote ili ahakikishe utaratibu unafanyika wa kuachiwa huru leo au kesho. Na hii document (nyaraka) naisaini hapa hapa. Lisiongezwe jina lingine au kupunguzwa,” alibainisha.
Alisema wafungwa hao 61, hawakuua watu wenye ulemavu wa ngozi (albino) wala kuhusika na vitendo vya ujambazi, lakini alisisitiza serikali kuendelea kusimamia sheria kwani uwepo wa ibara hiyo ya kikatiba haina maana sheria haitofuata mkondo.
Rais alitaja idadi ya wafungwa waliosamehewa, kwenye gereza la Uyui (2), Butimba (5), Ukonga (19), Isanga (15), Maweni (11) Kinguwila (5) na gereza la Ruanda wapo wafungwa wanne.
Vilevile, Rais Magufuli alitoa msamaha kwa wafungwa 8,157, ambao kati yao, 1,828 walitakiwa kutoka tangu jana na wengine 6,329, walipunguziwa muda wa kukaa gerezani.
Jijini Dar es Salaam, mwanamuziki Papii alipata taarifa za kuachiwa kwao huru wakati akiwa anashiriki kucheza mechi ya soka ya wafungwa wanaozishabikia Simba na Yanga, kwenye gereza la Ukonga.
Wakati wafungwa wengine wakishiriki katika mechi hiyo, baadhi yao walikuwa wakitazama moja kwa moja matangazo ya maadhimisho ya miaka 56 ya uhuru kupitia kwenye runinga iliyokuwepo ndani ya gereza hilo.
Wakati Rais Magufuli akitangaza kuwaachia huru Nguza na Papii, wafungwa waliokuwa wakifuatilia matangazo hayo walilipuka mayowe ya kushangilia na kukimbilia uwanjani, ambako walianza kumkimbiza Papii na hatimaye kumzingira.
Mmoja wa wanamuziki wakongwe nchini, King Kikii, alisimulia mkasa huo jana, kwa waandishi wa Mzalendo, baada ya kwenda kuwatembelea Babu Seya na Papii kwenye gereza la Ukonga.
Kikii alisema alifika kwenye gereza hilo baada ya kumsikia Rais Magufuli akitangaza msamaha huo kwa Babu Seya na Papii, kupitia kwenye runinga, akiwa nyumbani kwake, Ubungo, Dar es Salaam.
“Kwanza namshukuru sana Rais Magufuli. Uamuzi alioufanya ni wa kihistoria. Nimefurahi sana. Siwezi kusema lolote kwa sasa, isipokuwa  namshukuru Mungu na rais wetu. Mdogo wangu na mwanawe wamekaa gerezani kwa miaka 10 na sasa wako huru,” alisema.
Akisimulia jinsi Babu Seya na Papii walivyopokea taarifa hizo, Kikii alisema Papii ndiye aliyeonekana kuwa na furaha kubwa, kutokana na kuzunguka gereza zima, akiwaaga wenzake kwa furaha.
“Papii anasema alipita kila chumba kuwaaga wenzake huku akiwashukuru kwa ushirikiano wao kwa muda wote waliokuwa pamoja gerezani,” alisema Kikii.
Aliongeza kuwa, kitendo cha wafungwa wenzake kumkimbiza na kumzingira, kilimshtua hivyo alilazimika kuwahoji kulikoni, ndipo wakamjulisha kwamba, yeye na baba yake wameachiwa huru na Rais Magufuli.
“Kuanzia hapo Papii anasema alikuwa kama amepagawa kwa furaha. Mwanzoni aliangua kilio kwa kuwa hakuamini, lakini baadaye alianza kufurahia kwa kuzunguka gereza lote akishangilia na kuwaaga wenzake,”alisema.
Akimzungumzia Babu Seya, alisema baada ya kupokea taarifa hizo, hakuwa na mengi ya kusema zaidi ya kumshukuru Mungu na Rais Magufuli kwa uamuzi wake huo.
“Nguza (Babu Seya) alikuwa akifuatilia matangazo hayo na wenzake gerezani, lakini hakuwa akitarajia kitu kama hicho kutokea. Alichosema ni kwamba, anamshukuru Mungu na Rais Magufuli kwa kuwaonea huruma,”alisema.
Mmoja wa askari wa Magereza, aliyekuwepo kazini kwenye gereza la Ukonga, jana, alisema licha ya Rais Magufuli kutoa agizo hilo, isingewezekana kwa Babu Seya na mwanawe kutolewa siku hiyo kwa kuwa kuna taratibu za kisheria, zinazopaswa kukamilishwa.
“Ni kweli mheshimiwa rais ametoa agizo hilo, lakini kwa jinsi ninavyofahamu, kuna taratibu ambazo lazima zifuatwe kabla ya kuwaachia huru. Inawezekana wakaachiwa kesho (leo),” alisema askari huyo, ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini.
Mapema wakati akitoa takwimu za idadi ya wafungwa waliopo magerezani, Rais Magufuli alisema hadi juzi, kulikuwa na wafungwa 39,000, kati yao wafungwa 37,000, ni wanaume na wanawake ni 2,000.
Dk. Magufuli alieleza kuwa wafungwa waliohukumiwa kunyongwa ni 522, kati yao wanaume 503 na wanawake 19.
Alisema wafungwa waliohukumiwa kifungo cha maisha ni 666, kati yao wanaume 655 na wanawake 11.
“Kwa maana hiyo wafungwa wengi waliopo magerezani ni wanaume, hivyo tuanze kujitambua ni kwanini wanaume wanaongoza kwenye vitendo vya uhalifu,”alisema.

No comments:

Post a Comment