KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, March 29, 2016

SERENGETI BOYS KUVAANA NA MISRI



Timu ya Taifa ya Vijana wenye umri chini ya miaka 17 (Serengeti Boys) inatarajiwa kucheza michezo miwili ya kirafiki na timu ya Taifa ya Misri Vijana wenye umri chini ya miaka 17 (The Pharaohs) jijini Dar es salaam.

Mchezo wa kwanza kati ya Serengeti Boys dhidi ya The Pharaohs utachezwa siku ya Jumamosi, Aprili 2 katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, huku mchezo wa pili ukichezwa Jumanne Aprili 5 katika uwanja wa Azam Complex Chamazi.

Msafara wa The Pharaohs unatarajiwa kuwasili Alhamis tarehe 31, Machi ukiwa na watu 33, wakiwemo wachezaji 25 pamoja na viongozi 8, na wataondoka nchini tarehe 6 Aprili kurudi kwao nchini Misri.

Kikosi cha Serengeti Boys kinachonolewa na makocha Bakari Shime na Sebastian Mkomwa wakishauriwa na Jan Poulsen, kimeendelea na mazoezi katika uwanja wa Karume, zilipo ofisi za Makao za Makuu ya TFF.

Serengeti Boys ilingia kambini takribani wiki mbili zilizopita katika hosteli za TFF zilizopo Karume, kujiandaa na michezo hiyo miwili ya kirafiki ya kujipima nguvu kujiandaa kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa ya Afrika kwa Vijana wenye umri chini ya miaka 17 zitakazofanyika mwaka 2017 nchini Madagascar.

Tanzania itaanza kuwania kufuzu kwa fainali hizo mwishoni mwa mwezi Juni, kwa kucheza dhidi ya timu ya Taifa ya Vijana ya Shelisheli.

YANGA, AZAM DIMBANI KESHOKUTWA KOMBE LA SHIRIKISHO



Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup) linatarajiwa kuendelea Alhamisi kwa michezo miwili kuchezwa katika hatua ya robo fainali ya michuano hiyo.

Azam FC watakua kwenye uwanja wa Azam Complex kuwakaribisha maafande wa Tanzania Prisons siku ya Alhamis saa 10 jioni kwa saa za Afrika Mashariki.

Young Africans watakua wenyeji wa Ndanda FC katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, huku kila timu ikihitaji ushindi katika michezo hiyo ili kuweza kufuzu kwa hatua ya nusu fainali.

Aprili 11, Simba SC watakamilisha hatua ya robo kwa fainali kwa kucheza na wagosi wa kaya Coastal Union katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Mwadui FC ndio timu pekee mpaka sasa ambayo imeshafuzu kwa hatua ya nusu fainali, baada ya kuwachapa Geita Gold kwa mabao 3 -0.

Bingwa wa michuano ya Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup) atawakilisha Tanzania mwakani kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika (CAF CC) mwaka 2017.

Monday, March 28, 2016

TFF KUWAREJESHEA MASHABIKI PESA ZA VIINGILIO VYA STARS NA CHAD



SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limetangaza kuwarudishia fedha zao kesho Jumanne, wapenzi wa mpira wa miguu waliokuwa wameshakata tiketi za kushuhudia mchezo wa kundi G kati ya Tanzania v Chad jijini Dar es salaam.
 

TFF inawaomba washabiki wa mpira wa miguu waliokua wamekata tiketi za mchezo huo, kufika kesho Jumanne saa 5 kamili asubuhi katika vituo walivyonunulia wakiwa na tiketi zao ili waweze kurudishiwa fedha zao.

Zoezi la kuwarudishia fedha washabiki waliokuwa wameshakata tiketi za mchezo kati ya Tanzania v Chad litafanyika katika vituo vinne vilivyokua vikiuza tiketi siku ya Jumapili, hivyo wenye tiketi za mchezo huo wanaombwa kufika na tiketi zao ili waweza kurudishiwa fedha zao.


Aidha TFF inawaomba radhi watanzania na wapenzi wa mpira wa miguu kwa usumbufu uliojitokeza na kuwataka kuwa watulivu na wavumilivu katika kipindi hiki ambacho wanasubiria taarifa zaidi kutoka CAF.
 

Chad imejiondoa jana katika kinyanganyiro cha kuwania kufuzu kwa Fainali za Kombe la Mataifa Afrika (AFCON) nchini Gabon mwaka 2017, ambapo iliku kundi G na timu za Misri, Nigeria pamoja na Tanzania.

CHAD YAIFANYIA KITU MBAYA TAIFA STARS



Timu ya Taifa ya Chad  ‘Les Sao’ imejiondoa katika michuano ya kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa Afrika (AFCON) itakayofanyika mwaka 2017 nchini Gabon.

Taarifa ya kujitoa kwa Chad imetolewa na Shirikisho la Mpira wa miguu barani Afrika (CAF) jana baada ya Les Sao kuandika barua ya kujitoka katika mashindano hayo ikiwa katika kundi G pamoja na timu za Tanzania, Nigeria na Misri.

Chad ilitarajiwa kucheza leo (Jumatatu) dhidi ya Tanzania katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, ikiwa ni mchezo wa marudiano wa kundi G baada ya kucheza mchezo wa awali jijini N’Djamena katika ya wiki.

Katika mchezo wa awali uliochezwa uwanja wa Idriss Mahamat Ouya, Taifa Stars iliibuka na ushindi wa bao 1- 0 , bao lililofungwa na nahodha Mbwana Samatta dakika ya 30 ya mchezo.

Kufuatia kujitoa kwa Chad, matokeo ya michezo yote iliyoihusisha timu hiyo yanafutwa, na msimamo wa kundi G kwa sasa unaongozwa na Misri yenye pointi 4, Nigeria pointi 2 na Tanzania pointi 1.

Kwa mujibu wa ibara ya 61 ya kanuni za mashindano kinasomeka kwamba: “kama timu itajitoa kwenye hatua ya kufuzu kwenye hatua ya makundi, matokeo yake yote yatafutwa (pointi, magoli ya kufunga na magoli ya kufungwa)”.

Maamuzi ya kamati ya utendaji ya CAF yaliyofanywa January 15, 2015 yalikuwa kwamba, kundi lolote litakalosalia na timu tatu kufuatia kujitoa kwa moja ya timu kwenye kundi hilo, timu itakayoongoza kundi hilo itafuzu moja kwa moja kwenye michuano hiyo.

Kutokana na timu ya Chad kujiondoa kwenye mashindano, Shirikisho la Mpira wa Miguu la Chad limepigwa faini ya dola za kimarekani 20,000 pamoja na kufungiwa kushiriki michuano ijayo ya AFCON kwa mujibu wa ibara ya 59 ya kanuni za mashindano ambacho kinaeleza kwamba: “Shirikisho lolote likithibitisha kujiondoa baada ya mechi kuanza kuchezwa litawajibika kulipa faini ya dola za kimarekani 20,000. Pia haitaruhusiwa kushiriki mashindano yanayofuata.

Wakati huohuo, Misri watachuana dhidi ya Nigeria Jumanne  March 29, 2016 Alexandria, Misri.

Sunday, March 27, 2016

TAIFA STARS, CHAD KAZI IPO KESHO


Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ inayodhaminiwa na bia ya Kilimanjaro Premium Lager kesho inashuka dimba la uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam kuwakabili Chad katika mchezo wa marudiano wa kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) mwaka 2017.

Taifa Stars itaingia uwanjani ikiwa na kumbukumbu nzuri ya ushindi wa bao 1-0 ilioupata katikati ya wiki jijini N’Djamena katika uwanja wa Idriss Mahamat Ouya, bao lililofungwa na nahodha Mbwana Samatta dakika ya 30 ya mchezo.

Kocha wa Taifa Stars, Charles Mkwasa amesema maandalizi kwa kikosi chake yamekalimika, vijana wote wapo katika hali nzuri ya kusaka ushindi ushindi kesho, kikubwa amewaomba watanzania kujitokeza kwa wingi katika uwanja wa Taifa kujwa kuwapa sapoti vijana watakapokuwa wakiwakilisha Tanzania.

Kuelekea katika mchezo huo, tiketi za mchezo zimeanza kuuzwa leo katika vituo vya Ubungo Oilcom, Buguruni kituo cha mafuta, Mbagala Darlive na Karume ofisi za TFF. Viingilio vya mchezo huo ni Shilingi 25,000 kwa VIP A, Shilingi 20,000 kwa VIP B na Shilingi 5,000 kwa viti vya rangi ya Blu, Kijani na rangi ya Machungwa.

TFF YAIAGIZA KRFA KUCHUNGUZA MATOKEO LIGI YA KATAVI


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limekiagiza Chama cha Mpira wa Miguu mkoa wa Katavi (KRFA) kufanya uchunguzi juu ya matokeo ya kumpata bingwa wa ligi ya mkoa huo iliyomalizika wikiendi hii kabla ya kutangaza Bingwa wa Mkoa wa Katavi.

TFF imeagiza KRFA kuziagiza kamati zake kufanya uchunguzi juu ya matokeo ya mwisho katika mchezo kati ya Stand FC dhidi ya Kazima FC, ambapo Stand FC iliibuka na ushindi wa mabao 16 - 0.

Kabla ya mchezo huo wa mwisho, klabu ya Nyundo FC ilikua inangoza kwa kuwa na pointi 21 na magoli 24 ya kufunga, na klabu ya Stand FC ilihitajia ushindi wa mabao 13 ili kuweza kuwa bingwa wa mkoa wa Katavi, hali inayopelea kuwepo kwa dalili za kupanga matokeo kwa ushindi wa Stand FC wa mabao 16 – 0 dhidi ya Kazima FC.

KRFA haitaruhusiwa kutangaza bingwa wa mkoa hadi uchunguzi ukamilke na TFF ijiridhishe na uchunguzi huo.

MWADUI YATINGA NUSU FAINALI KOMBE LA SHIRIKISHO

Michuano ya Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup) ngazi ya robo fainali imeendelea leo kwa mchezo mmoja, ambapo Mwadui FC wameibuka na ushindi wa mabao 3- 0 dhidi ya wneyeji Geita Gold FC.

Mchezo huo wa kwanza hatua ya robo fainali umechezwa katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza, na Mwadui FC kujipatia magoli yake kupitia kwa Joram Mgeveke, Jeryson Tegete pamoja na Jabir Aziz ‘Stima’.

Baada ya ushindi huo Mwadui FC inasuburi kuungana na timu zingine tatu katika hatua ya Nusu Fainali ambayo michezo yake itachezwa mwishoni mwa mwezi Aprili mwaka huu.

Michuano hiyo ya Kombe la Shirikisho inatarajiwa kuendelea tarehe 31 Machi kwa michezo miwili, Young Africans watakua wenyeji wa Ndanda FC uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, huku Azam FC wakiwakaribisha Tanzania Prisons katika uwanja wa Azam Complex Chamazi.

Mchezo wa mwisho hatua ya nusu fainali utachezwa tarehe 7 April, ambapo Simba SC watakua wenyeji wa Coastal Union katika uwanja wa Taifa jijini Dar ess alaam.

Bingwa wa Kombe la Shirikisho atawakilisha Tanzania kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika (CAF CC) mwaka 2017.

TFF YATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KNVB



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeomboleza kifo cha gwiji wa soka duniani Johann Cruffy aliyefariki hivi karibuni kwa ugonjwa wa Saratani.

Katika taarifa aliyoituma kwa Rais wa Chama cha Soka cha Uholanzi, Rais wa TFF Jamal Malinzi amemwelezea Marehemu Cruyff kama gwiji aliyetoa mchango mkubwa kama mchezaji na kocha katika timu ya Taifa ya nchi yake na klabu za Barcelona, Ajax, Lavanet mwaka 1964 – 1977.

Tanzania tulikuwa na bahati ya kutembelewa na Cruyff ikiwa ni sehemu ya kuitangaza klabu yake ya Barcelona na kuendeleza mpira wa Vijana na maendeleo ya walimu wa soka nchini.

TFF inaungana nawe, familia ya marehemu na wapenda soka ndani ya Uholanzi na duniani kote katika kuomboleza na kusheherekea maisha ya Marehemu Johann Cruyff. Mwenyezi Mungu aiweke roho ya marehemu mahali pema peponi, Amen.

Johann Cruyff alizaliwa Uholanzi tarehe 25 Aprili, 1947 na kuchezea klabu za Ajax, Feyenoord, Lavante, Los Angeles, Washington Diplomats na timu ya Taifa ya Uholanzi kati ya mwaka 1966 – 1977 na baadae alizifundisha kalbu za Ajax, Barcelona na Catalonia.

IMETOLEWA NA SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA (TFF)

KIINGILIO TANZANIA NA CHAD 5,000/- TU



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) leo limetangaza viingilio vya mchezo wa kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa Afrika (AFCON) kundi G siku ya Jumatatu kati ya Tanzania dhidi ya Chad, bei ya chini ikiwa ni shilingi elfu tano (5,000) tu.

Viingilio vya mchezo huo vimegawanyika katika makundi matatu, ambapo kiingilio cha juu kitakua shilingi elfu ishirini na tano (25,000) kwa VIP A, na shilingi elfu ishirini (20,000) kwa VIP B, na kwa viti vya rangi ya bluu, kijani na orange itakua shiligi elfu tano (5,000).

Tiketi za mchezo huo zitaanza kuuzwa kesho Jumapili saa 2 asubuhi katika vituo vinne ambavyo ni kituo cha mafuta Buguruni (Buguruni), Ubungo Oilcom (Ubungo) na Dar Live (Mbagala), na Jumatatu tiketi zitauzwa katika viunga vya uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Wakati huo huo Rais wa TFF, Jamal Malinzi amemshukuru Waziri Mkuu wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Majaliwa Kassim Majaliwa kwa kubali kuwa mgeni rasmi katika mchezo kati ya Tanzania v Chad utakaochezwa siku ya Jumatatu jijini Dar es salaam.

TFF pia inamshukuru Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye kwa kufanikisha ujio wa Waziri Mkuu kwa kufuatilia kwa karibu maombi ya TFF ya tarehe 21/03/2016 ya kumuomba Waziri Mkuu awe mgeni rasmi katika mchezo huo.

Kwa upande wa Taifa Stars iliyoweka kambi katika hoteli ya Urban Rose inaendelea na mazoezi katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, kujiandaa na mchezo wa marudiano dhidi ya Chad.

Waamuzi wa mchezo huo kutoka nchini Djibouti wanatarajiwa kuwaisli leo jioni ambao ni mwamuzi wa kati Djamel Aden Abdi, Abdilahi Mahamoud, Farhan Bogoreh Salim, Farah Aden Ali, huku kamisaa wa mchezo akiwa Andrea Abdallah Dimbiti kutoka nchini Sudani Kusini.

TASWA YAPATA WADAU WATAKAOSAIDIA KUDHAMINI MAFUNZO KWA WAANDISHI WA HABARI ZA MICHEZO



KAMATI ya Utendaji ya Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) ilikutana hivi karibuni na kujadili masuala mbalimbali.

A; Mafunzo

TASWA imepata wadau watakaosaidia kudhamini mafunzo kwa waandishi wa habari za michezo 60 chipukizi na wale wa kada ya kati.

Mada mbalimbali zitatolewa zikihusisha wataalamu wa uandishi wa habari za michezo, wahariri wazoefu na baadhi ya wataalamu wa michezo mbalimbali.

Pia itatolewa mada ya masuala ya ukuaji wa teknolojia ya habari na mawasiliano na namna ya kuripoti habari za michezo.

Mafunzo haya yatafanyika Mei 21-23 mwaka huu jijini Dar es Salaam, ambapo TASWA inaendelea na juhudi za kusaka wadau wengine ili mafunzo hayo yatatanguliwe na mkutano wa siku moja kwa wahariri wa habari za michezo na baadhi ya waandishi wazoefu wa habari za michezo.

Utaratibu wa kupata washiriki hao utafanyika kwa kutumia wahariri wa habari za michezo wa vyombo mbalimbali kwa kadri mahitaji yatakavyoruhusu.

TASWA inawashukuru wadau hao ambao tutawatangaza baada ya taratibu za udhamini wao kukamilika na tunaomba wengine waendelee kutuunga mkono katika hili.

B: Media Day

Kwa miaka miwili sasa, bonanza la wanahabari ‘Media Day’ limeshindwa kufanyika kutokana na sababu mbalimbali, hivyo imeundwa kamati ndogo kwa ajili ya jambo hilo na inaendelea vyema na maandalizi na muda si mrefu majibu mazuri yatatangazwa.

C: Vitambulisho

Tulisitisha kwa muda kutoa vitambulisho kwa wanachama ili kuboresha utaratibu na kutoa vyenye ubora zaidi, hilo tayari limekamilika na mtatangaziwa utaratibu mzuri na wale wote ambao hawana watapata vitambulisho vyao.

Nawasilisha,

Amir Mhando
Katibu Mkuu TASWA
26/03/2016

Thursday, March 24, 2016

TAIFA STARS KUREJEA NCHINI LEO USIKU




Kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kinachodhaminiwa na bia ya Kilimanjaro Premium Lager, kinatarajiwa kuwasili leo saa 8 usiku katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwl. JK Nyerere kikitokea nchini Chad kilipokuwa na mchezo dhidi ya wenyeji jana jioni.

Msafara wa Taifa Stars unaongozwa na mkuu wa msafara ambaye pia ni Rais wa Chama cha Soka Zanzibar (ZFA), Ravia Idarus Faina utaondoka uwanja wa ndege wa kimataifa wa N’Djamena saa 8 mchana kuelekea Addis Ababa nchini Ethiopia, kabla ya kuunganisha ndege saa 4 usiku tayari kwa safari ya kurejea nyumbani Tanzania.

Stars inarejea nyumbani baada ya kuibuka na ushindi wa bao 1–0 dhidi ya wenyeji Chad, bao lililofungwa na nahodha Mbwana Samatta katika mchezo uliochezwa uwanja wa Omnisport Idriss Mahaymat Ouya jijini N’Djamena katika mchezo wa kundi G kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa Afrika (AFCON) mwaka 2017.

Mara baada ya kuwasili jijini Dar es salaam, kikosi cha Taifa Stars kitaingia moja kwa kwa moja kambini katika hoteli ya Urban Rose iliyopo eneo la Kisutu kujiandaa na mchezo wa marudano utakaochezwa siku ya Jumatatu ya Pasaka katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.


RATIBA YA LIGI KUU YAFANYIWA MAREKEBISHO



Pokea marekebisho ya ratiba ya Ligi Kuu ya Vodacom msimu wa 2015/2016 yaliyoambatanishwa (attached).

Utangulizi;

-Marekebisho ya ratiba ya Ligi Kuu ya Vodacom yamezingatia mechi za viporo za timu za Azam na Yanga zinazoshiriki mashindano ya kimataifa (Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho).

-Pia ushiriki wa Azam na Yanga katika mechi zijazo za mtoano (play offs) zinazokutanisha timu zitakazotolewa kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika, na zile zilizosonga mbele kwenye Kombe la Shirikisho.

-Iwapo Azam itasonga mbele itacheza mechi hizo za mtoano, wakati Yanga yenyewe itacheza tu mechi hizo za mtoano iwapo itatolewa katika raundi inayofuata ya Ligi ya Mabingwa. Hivi sasa Azam na Yanga zinashiriki hatua ya 16 bora ambayo itachezwa kati ya Aprili 8-10 kwa mechi za nyumbani, na Aprili 19 na 20 kwa mechi za ugenini.

-Mechi za kwanza za raundi ya mtoano (play offs) zitachezwa kati ya Mei 6-8 wakati za marudiano zitafanyika Mei 17-18. Yanga ikiitoa Al Ahly maana yake haitacheza hatua ya mtoano (play offs), na badala yake itasubiri moja kwa moja hatua ya makundi ambayo mechi zake za kwanza zitafanyika kati ya Juni 17-19.

-Marekebisho mengine yanaweza kufanyika kwa kuzingatia matokeo ya scenario hizo hapo juu.
 

Wasalaam,
Boniface Wambura
Ofisa Mtendaji Mkuu
Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB)

STARS YAITUNGUA CHAD 1- 0 N'DJAMENA



Timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ inayodhaminiwa na bia ya Kilimanjaro Premium Lager leo imeibuka na ushindi wa bao 1- 0 dhidi ya wenyeji Chad katika mchezo uliomalizika jioni hii katika uwanja wa Omnisport Idriss Mahamat Ouya uliopo jijini N’Djamena.

Kikosi cha Stars kilicheza vizuri kwa maelewano kwa lengo la kusaka bao la mapema, safu ya ushambuliaji ilikuwa mwiba kwa walinzi wa Chad katika dakika 30 za kipindi cha kwanza na kukosa nafasi zaidi ya nne za wazi kupitia kwa Ulimwengu, Farid, Samatta na Kazimoto.

Nahodha Mbwana Samatta ambaye leo alikua akikiongoza kikosi cha Taifa Stars kwa mara ya kwanza tangu kuteuliwa katika nafasi hiyo, aliipatia Tanzania bao la kwanza dakika ya 30 akimalizia pasi ya Farid Mussa aliyewatoka walinzi wa Chad kabla ya kumpasia mfungaji.

Mara baada ya bao hilo wenyeji walikuja juu kusaka bao la kusawazisha, lakini ukuta wa Stars uliokuwa chini ya Kelvin Yondani, Erasto Nyoni, Shomari Kapombe, Haji Mwinyi na mlinda mlango Aishi Manula walikua imara kuokoa michomo hiyo.

Kipindi cha pili Stars ilianza kwa kufanya mabadiliko, Mwinyi Kazimoto aliyeumia alimpisha John Bocco na kuongeza nguvu katika sehemu ya ushambuliaji, na kuwapa wakati mgumu walinzi wa Chad.

Dakika ya 73, David Mwantika aliingia kuchukua nafasi ya Farid Mussa, huku Ibrahim Ajibu akiingia dakika ya 80 kuchukua nafasi ya Thomas Ulimwengu, mabadiliko ambayo yaliongeza nguvu kwa stars na kujilinda mpaka mwisho wa mchezo.

Mpaka dakika 90 za mchezo zinamalizika, Chad 0 –1 Tanzania.
 

Kocha wa Taifa Stars, Charles Boniface Mkwasa mara baada ya mchezo wa leo amewapongeza wachezaji wake kwa kupambana ugenini na kuibuka na ushindi huo japo mazingira ya joto yalikuwa tatizo kwa vijana wake katika muda wote wa mchezo.

Mkwasa amesema leo vijana wake wamecheza dakika 90 za kipindi cha kwanza na kuweza kupata ushindo, hivyo akili yao sasa ni katika mchezo wa marudiano utakaocheza Jumatatu ya Pasaka jijini Dar es salaa, ambapo amewaomba watanzania kujitokeza kwa wingi kuja kuwapa sapoti.

Taifa Stars inatarajiwa kurejea nyumbani kesho usiku kwa usafiri wa shirika la ndege la Ethiopia, ikitoka N’Djamena Chad saa 8 mchana kupitia Addis Ababa na kisha kuwasili uwanja JNIA Nyerere majira ya saa 7 usiku.

Stars iliwakilishwa na Aishi Manula, Shomari Kapombe, Mwinyi Haji, Erasto Nyoni, Kelvin Yondani, Himid Mao, Jonas Mkude, Mwinyi Kazimoto/John Bocco, Mbwana Samatta, Thomas Ulimwengu/Ibrahim Ajibu, Farid Mussa/David Mwantika.

Chad: Diara Gerrad, Asselmoun Massam, Nadjim Haroun, Abaya Cesar, Kelvine Nicaise, Ndoumnan Herman, Beadoum Monde/Altama Saana, Mahama Azarack, Djimenan Leger/Aldo Mathew, Ndouassel Ezekliel, Ninga Casimin

BASATA LAONYA KUMBI, LAPIGA MARUFUKU DISKO TOTO

Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) ambalo ni msimamizi wa sekta ya Sanaa na burudani nchini linawakumbusha wamiliki na waendeshaji wa kumbi za burudani kufuata sheria, kanuni na taratibu walizopewa kwenye vibali vyao vya uendeshaji wa kumbi.
 

Wanaelekezwa kuhakikisha wanakuwa na vibali halali vya uendeshaji wa kumbi zao, kuzingatia muda wa utumizi wa kumbi, kuepuka kelele zinazosumbua kwenye maeneo maalum hasa makazi ya watu na kuhakikisha ulinzi na usalama wa maisha ya watu na mali zao.
 

Aidha, BASATA linawakumbusha wamiliki wote wa kumbi za sherehe na burudani kwamba ni marufuku kukusanya watoto katika kumbi zao kupitia kile kinachoitwa ‘Disko Toto’ katika msimu huu wa Sikukuu ya Pasaka ili kuepuka maafa yanayoweza kujitokeza.
 

Uzoefu unaonesha kwamba, nyakati za sikukuu kama hizi wamiliki wa kumbi wamekuwa wakijisahau na kuendekeza faida katika biashara zao kiasi cha kuandaa madisko ya watoto hali mbayo imekuwa ikisababisha maafa ambayo yangeepukika kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu.
 

Aidha, baadhi ya wamiliki na waendeshaji wa kumbi kwa msingi huohuo wa kuendekeza faida pasi na kujali maelekezo ya vibali vyao wamekuwa wakijaza watu kupita viwango vya madaraja waliyopangiwa na BASATA.
 

BASATA kama mtoaji wa vibali vya kumbi za sherehe na burudani linasisistiza kwamba halitafumbia macho ukumbi wowote utakaokiuka maelekezo haya sambamba na kuruhusu maonesho machafu yenye kudhalilisha utu wa binadamu hasa yale yanayoonesha maungo ya ndani. Hatua kali na za kisheria zitachukuliwa kwa yeyote atakayekiuka maagizo haya.
 

BASATA linawatakia wasanii na wadau wote wa Sanaa Pasaka njema na yenye furaha tele.

SANAA NI KAZI TUIKUZE, TUILINDE NA KUITHAMINI

Godfrey L. Mngereza
KATIBU MTENDAJI, BASATA.

Tuesday, March 22, 2016

RAIS ZFA KUONGOZA MSAFARA WA STARS CHAD

 Rais wa Chama cha Soka Zanzibar (ZFA), Ravia Idarus Faina ndiye mkuu wa msafara wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, anatarajiwa kuondoka Dar es salaam kesho Jumanne alfajiri pamoja na wachezaji wengine kuelekea nchini Chad kwa ajili ya mchezo wa kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) mwaka 2017.

Kundi hilo la pili lenye wachezaji 8, linatarajiwa kuungana na mshambuliaji wa klabu ya TP Mazembe Thomas Ulimwengu kesho Jumanne asubuhi Addis Ababa kisha kuunganisha safari ya kuelekea nchini Chad wanapotarajiwa kufika saa 6 mchana.

Wachezaji wanaotarajiwa kusafiri kesho Jumanne alfajiri kuelekea Chad kwa shirika la ndege la Ethiopia ni Aishi Manula, Shomari Kapombe, Erasto Nyoni, David Mwantika, Himid Mao, Farid Mussa na John Bocco.

Kesho Jumanne wachezaji wote watafanya mazoezi mepesi ya mwisho ya pamoja katika uwanja wa Omnisport Idriss Mahamat Ouya saa 9 mchana, kabla ya kuwavaa wenyeji siku ya Jumatano katika uwanja huo huo.

TAIFA STARS YAIPIGIA ZOEZI KALI CHAD


Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ inayodhaminiwa na bia ya Kilimanjaro Premium Lager leo imefanya mazoezi katika uwanja wa Omnisports Idriss Mahamat Ouya ulipo katika jiji la D’jamena ikiwa ni maandalizi ya mchezo dhidi ya wenyeji Chad siku ya Jumatano.

Taifa Stars imefanya mazoezi kuanzia majira ya saa 9 alasiri, ikiwa ni sawa na muda utakaochezwa mchezo siku ya Jumatano sawa na saa 11 kwa saa za nyumbani Tanzania na Afrika Mashariki.

Akiongelea maandalizi ya mchezo huo, Kocha Mkuu wa Taif Stars Charles Boniface Mkwasa amesema anashukuru vijana wake waliotangulia wamefika salama, hakuna majeruhi na wote wameweza kufanya mazoezi aliyoyapangilia.

“Hapa D’jamena hali ya hewa ni joto kali tofauti na nyumbani, kwa hizi siku mbili tutakazofanya mazoezi hapa, naimani vijana wataweza kuzoea hali ya hewa na kufanya vizuri katika mchezo wa Jumatano” alisema Mkwasa.

Mkwasa amesema wachezaji wake wametoka katika vilabu vyao ambavyo vilikua na michezo mwishoni mwa wiki, wote bado wako fit kikubwa wanafanya maandalizi ya mwisho kwa ajili ya mchezo huo.

“Hatujapata muda mrefu wa kufanya mazoezi kwa pamoja, wachezaji walikua na majukumu katika vilabu vyao, nashukuru wote wamewasili wakiwa salama na kesho wataungana na wachezaji wenzao wanaokuja katika kundi la pili kwa ajili ya mazoezi ya mwisho na mchezo wenyewe” aliongeza Mkwasa.

Monday, March 21, 2016

AFRICANS SPORTS YATUNGULIWA 1-0 NA PRISONS


 AFRICAN Sports imezidi kujiweka katika mazingira ya kushuka daraja baada ya kufungwa 1-0 nyumbani na Prisons ya Mbeya jioni ya leo katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.
Bao pekee la Prisons leo limefungwa na beki James Mwasote sekunde ya 46 dakika ya kwanza aliyepiga kona iliyoingia moja kwa moja nyavuni, ingawa ilisindikizwa na Jumanne Elfadhil wakati tayari imekwishaingia langoni.
Kwa ushindi huo, Prisons inafikisha pointi 39 baada ya kucheza mechi 24 ingawa inaendelea kukamata nafasi ya tano, nyuma ya Mtibwa Sugar yenye pointi 39 pia na wastani mzuri wa mabao.
Kwa African Sports, inabaki na pointi zake 20 za mechi 24 na kuendelea kushika nafasi ya 15 katika ligi ya timu 16, mbele ya ndugu zao, Coastal Union wenye pointi 19 za mechi 24 pia.
Sports iliyopanda Ligi Kuu msimu huu baada ya zaidi ya miaka 20, sasa inahitaji kufanya kazi ya ziaba ili kubaki kwenye ligi hiyo, sawa na ndugu zao, Coastal na JKT Mgambo – ambao kwa pamoja wanashika nafasi tatu za mwisho.
Ligi Kuu inatarajiwa kuendelea kesho Uwanja wa Mkwakwani, kwa timu nyingine ya Tanga, JKT Mgambo kuikaribisha Toto Africans ya Mwanza.
Mgambo inashika nafasi ya 14 kwa pointi zake 20 za mechi 23, wakati Toto ni ya 12 ikiwa na pointi 23 za mechi 22.

FUNGU LA KWANZA LA TAIFA STARS LATUA SALAMA CHAD



Kikosi cha Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kinachodhaminiwa na bia ya Kilimanjaro Premium Lager kundi la kwanza limewasili salama jijini D’jamena nchini Chad tayari kwa mchezo wa kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa Afrika (AFCON) mwaka 2017.

Taifa Stars inayonolewa na kocha mkuu Charles Boniface Mkwasa akisaidiwa na Hemed Morocco kimewasili D’jamena leo majira ya saa 7 mchana kwa saa za huku kwa shirika la ndege la Ethiopia, sawa na saa saa 9 alasiri kwa saa za nyumbani na Afrika Mashariki na kufikia katika hoteli ya Legder Plaza.

Msafara wa 20 wa kundi la kwanza uliowasili umejumuisha viongozi pamoja na wachezaji 12, huku kundi la pili likitarajiwa kuondoka Tanzania Jumatatu usiku na kuwasili Jumanne kuungana kwa mazoezi ya mwisho nchini humu.

Stars inatarajiwa kufanya mazoezi kesho Jumatatu na Jumanne katika uwanja wa Omnisports Idrissm Mahamat Ouya kujiandaa na mchezo huo wa Jumatano katika dimba hilo hilo jijini D’jamena.

Wachezaji waliowasili nchini ni Chad ni Ally Mustafa, Juma Abdul, Haji Mwinyi, Kelvin Yondani, Deus Kaseke, Mohamed Hussein, Jonas Mkude, Mwinyi Kazimoto, Ibrahim Ajibu, Shiza Kichuya, Mohamed Ibrahim na nahodha Mbwana Samatta.

Mchezo kati ya Chad dhidi ya Tanzania unatarajiwa kuchezwa siku ya Jumatano Alasiri kwa saa za huku, sawa na saa 11 jioni kwa saa za nyumbani Tanzania.

NB: Namba ya simu ya Mawasiliano ya Afisa Habari wa TFF aliyeko nchini CHAD ni +235 65 21 9414

AZAM YASONGA MBELE KOMBE LA SHIRIKISHO



AZAM FC imefanikiwa kuingia Raundi ya Pili ya Kombe la Shirikisho Afrika baada ya kuitoa Bidvest Wits ya Afrika Kusini kwa ushindi wa jumla wa mabao 7-3.
Azam FC leo imeifunga Bidvest 4-3 Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam katika mchezo wa marudiano ikitoka kushinda 3-0 katika mchezo wa kwanza, ugenini mjini Johannesburg, Afrika Kusini.
Sasa timu hiyo ya Alhaj Sheikh Said Salim Awadh Bakhresa na family yake itakutana na Esperance ya Tunisia katika Raundi ya Pili mwezi ujao.
Azam FC ndiyo waliokuwa wa kwanza kupata bao, mfungaji mshambuliaji wa Ivory Coast, Kipre Herman Tchetche dakika ya 22 akimalizia kwa kichwa krosi ya kiungo Ramadhani Singano ‘Messi’.
Kipre Tchetche akamtoka beki wa kulia wa Bidvest na kuingia ndani kumpasia Nahodha John Raphael Bocco ‘Adebayor’ aliyefunga bao pili dakika ya 42.
Mcheaji wa kikosi cha kwanza cha Bidvest, Jabulani Shongwe aliyeingia dakika ya 43 kuchukua nafasi ya Pule Maliele, akaifungia timu yake sekunde chache baadaye dakika hiyo kwa shuti kali akiwa amezungukwa na mabeki wa Azam.
Bao hilo liliwafanya wachezaji wa Azam FC watulie kidogo na kuanza kucheza kwa uwiano mzuri wa kushambulia na kujilinda.
Kipindi cha pili, Azam FC wakaendelea kung’ara baada ya Kipre Tchetche kufunga bao la tatu dakika ya 56, akimlamba chenga kipa wa Bidvest, Barr Jethren na kufunga akiwa amebaki na nyavu, kufuatia pasi ya kiungo Salum Abubakar ‘Sure Boy’.
Hata hivyo, Bidvest wakatumia makosa ya safu ya ulinzi kupooza kupata bao la pili lililofungwa na Mosiatlhaga Koiekantse dakika ya 58, akimalizia pasi ya Botes Henrico.
Kipre Tchetche akakamilisha hat trick yake dakika ya 88 kwa kufunga bao zuri la tatu, baada ya pasi ya Sure Boy na kumchambua kipa Barr Jethren.
Botes Henrico akaruka juu peke yake kuifungia Bidvest bao la tatu dakika ya 90, akiunganisha kwa kichwa krosi ya Lecki Markus.
Bidvest ilitumia wachezaji wengi wa kikosi cha wachezaji wa akiba katika mechi zote mbili, ingawa leo kidogo walionekana wachezaji kama watano wa kikosi cha kwanza – na hiyo ni kwa sababu hawana malengo na michuano hiyo. 

IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA BINZUBEIRY

TWIGA STARS YATOLEWA KISHUJAA NA WAZIMBABWE


Timu ya Taifa ya Wanawake Tanzania ya Mpira wa Miguu ‘Twiga Stars’ imetoka sare ya bao 1-1 dhidi ya wenyeji Zimbabwe ‘Mighty Warriors’ katika mchezo uliochezwa jioni ya leo katika uwanja wa Rufaro jijini Harare.

Twiga katika mchezo wa leo imecheza vizuri na kuweza kuwabana wenyeji katika uwanja wao wa nyumbani kwa kuwalazimisha sare, na weyeji kupata nafasi ya kusonga mbele katika hatua inayofuata kwa jumla ya mabao 3-2.

Kwa matokeo hayo Twiga Stars imetolewa kwenye michuano ya kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa ya Afrika kwa Wanawake zitakazofanyika mwishoni mwa mwaka huu nchini Cameroon.

Kikosi cha Twiga Stars kinatarajiwa kurejea nyumbani kesho Jumatatu mchana kwa usafiri wa shirika la ndege la Fastjet.

Sunday, March 20, 2016

TWIGA STARS KULIPA KISASI KWA WAZIMBABWE LEO?


Timu ya soka ya Taifa ya Wanawake, Twiga Stars inatarajiwa kuwakabili wenyeji wao Zimbabwe (Mighty Warriors) katika mchezo wa marudiano wa kusaka tiketi ya kushiriki fainali zijazo za Kombe la Mataifa ya Afrika (AWC) utakaofanyika leo kwenye Uwanja wa Rufalo jijini Harare.
Katika mchezo wa kwanza uliofanyika Machi 4 kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi jijini Dar es Salaam, Twiga Stars ililala mabao 2-1 dhidi ya wapinzani wao hao na leo inahitaji ushindi wa kuanzia 2-0 ili iweze kusonga mbele.
Kocha mkuu wa Twiga Stars, Nasra Juma, alisema kwamba kikosi chake kiko tayari kwa mapambano na wanataka kurudia mafanikio waliyopata 2010 kwa kushiriki fainali hizo zilizofanyika jijini Johannesburg, Afrika Kusini.
Nasra alisema kuwa sasa wanaingia mchezo wakiwa wanawafahamu wapinzani wao tofauti na ilivyokuwa katika mechi ya kwanza ambayo walikubali kichapo.
"Tunajua aina ya wachezaji na mfumo wanaocheza, tumejipanga kufanya vizuri kwa sababu nia, sababu na uwezo wa kuwaondoa Zimbabwe wakiwa kwao tunao," alisema Nasra.
Mkuu wa msafara wa timu hiyo na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Amina Karuma, aliliambia gazeti hili kwa njia ya simu kwamba wachezaji wote wako katika hali nzuri na wanasubiri muda wa mchezo ufike.

TAIFA STARS YAENDA CHAD KWA MAFUNGU


KUNDI la kwanza la wachezaji wa timu ya soka ya Taifa (Taifa Stars) linaondoka leo kuelekea N'Djamena nchini Chad kwa ajili ya mechi ya kwanza ya kuwania tiketi ya kucheza fainali zijazo za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON).
Mechi kati ya Chad na Taifa Stars itafanyika Jumatano Machi 23 mwaka huu na marudiano itacheza Machi 28 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na gazeti hili jana, kocha mkuu wa Taifa Stars, Boniface Mkwasa, alisema kuwa uamuzi wa kuondoka kwa 'mafungu' umetokana na baadhi ya wachezaji walioitwa kwenye timu hiyo kuwa na majukumu ya klabu nje ya Dar es Salaam.
Mkwasa alisema kuwa wachezaji wanaocheza nje ya nchi nahodha Mbwana Samatta wa KRC Genk ya Ubelgiji na Thomas Ulimwengu wa TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) wataungana na timu hiyo huko huko N'Djamena.
"Tumefanya hivi ili kupata nafasi angalau ya kufanya mazoezi kwa siku tatu tukiwa huko huko Chad, ratiba ya Ligi Kuu na mashindano ya kimataifa ya Klabu Bingwa Afrika na Kombe la Shirikisho imetubana makocha wa timu za taifa safari hii, tutakutana na wachezaji muda mfupi kabla ya mechi," alisema Mkwasa.
Kocha huyo aliongeza kwamba licha ya changamoto hiyo, bado Taifa Stars ina nafasi ya kuanza vyema kampeni hizo kwa sababu alikuwa akifanya mawasiliano na wachezaji kwa ajili ya kuwaandaa na mchezo huo wa ushindani.
Stars itafanyika Jumatano Machi 23 mwaka huu na marudiano itacheza Machi 28 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

CHANZO CHA HABARI: NIPASHE

SIMBA KANYAGA TWENDE LIGI KUU BARA


SIMBA SC imepaa kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kwa pointi saba zaidi ya wapinzani Azam na Yanga katika mbio za ubingwa, kufuatia ushindi wa 2-0 dhidi ya Coastal Union Uwanja wa Mkwakwani, Tanga jioni ya leo.
Simba SC sasa inafikisha pointi 57, baada ya kucheza mechi 24, wakifuatiwa na mabingwa watetezi, Yanga wenye pointi 50 sawa na Azam FC baada ya timu zote hizo kucheza mechi 21. 
Coastal Union iliyozifunga Yanga 2-0 na Azam 1-0 Uwanja wa Mkwakwani, kipigo cha leo kinawafanya wabaki na pointi zao 19 baada ya kucheza mechi 24 na kuendelea kuburuza mkia katika Ligi Kuu ya timu 16
Mshambuliaji Daniel Lyanga aliifunga timu yake zamani dakika ya 39 kuipatia Simba bao la kwanza kwa kichwa akimalizia krosi ya beki wa kushoto, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’.
Hamisi Kiiza ‘Diego’ akaifungia Simba SC bao la pili dakika ya 52 akimalizia krosi ya beki wa kulia, Emery Nimubona.
Simba SC ingeweza kuondoka na ushindi mnono zaidi kama washambuliaji wake Kiiza na Lyanga wangetumia vizuri nafasi zaidi walizopata.

YANGA YAITOA APR, SASA KUKUTANA NA AL AHLY YA MISRI RAUNDI YA PILI YA KLABU BINGWA AFRIKA


WAWAKILISHI wa Tanzania katika michuano ya klabu bingwa Afrika, Yanga wamefuzu kucheza raundi ya pili ya michuano hiyo baada ya kulazimishwa kutoka sare ya bao 1-1 na APR ya Rwanda.

Sare hiyo iliyopatikana jana kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, imeiwezesha Yanga kusonga mbele kwa jumla ya mabao 3-2, kufuatia kushinda mechi ya awali mjini Bujumbura kwa mabao 2-1.

Kwa ushindi huo, Yanga sasa itakutana na Al Ahly ya Misri katika mechi ya raundi ya tatu.
Al Ahly imetinga hatua hiyo baada ya kuitoa Recreativo do Libolo ya Angola kwa jumla ya mabao 2-0. Katika mechi ya awali, timu hizo zilitoka suluhu mjini Luanda.

APR ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya tatu lililofungwa na Fiston Nkinzingabo aliyefumua shuti kali akimalizia pasi ya Jean Claude Iranzi.

Yanga walifanikiwa kusawazisha bao hilo dakika ya 28 kupitia kwa mshambuliaji wake, Donald Dombo Ngoma, aliyefumua shuti la kitaalamu baada ya pasi nzuri ya kiungo Mzimbabwe mwenzake, Thabani Scara Kamusoko.

Pambano kati ya Yanga na Al Ahly linatarajiwa kuvuta hisia za mashabiki wengi wa soka nchini, kutoka na timu hiyo ya Tanzania kuwa na rekodi ya kufungwa kila inapokutana na timu za Misri.

Mara ya mwisho timu hizo zilikutana mwaka 2014, katika raundi ya kwanza na Yanga ikatolewa kwa penalti 4-3, baada ya sare ya jumla ya 1-1, kila timu ikishinda 1-0 nyumbani kwake.

Kwa mujibu wa ratiba, mechi ya kwanza itachezwa Aprili 9, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati marudiano yatakuwa Aprili 19 mjini Cairo.

Saturday, March 19, 2016

TFF YAZITAKIA HERI YANGA, AZAM NA JKU


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limezitakia kila la kheri vilabu wawakilishi wa Tanzania kwenye michuano ya kimataifa, timu za Azam FC, JKU na Yanga SC katika michezo yao watakayocheza wikiendi hii.

Katika salamu hizo, TFF imezitakia kila la kheri timu hizo kuhakikisha zinafanya vizuri katika michezo yao ili ziweze kusonga mbele katika hatua inayofuata, na kuwapa furaha washabiki wa mpira wa miguu pamoja na watanzania wote.

Timu ya JKU ya visiwani Zanzibara leo Ijumaa watakua kibaruani kuchuana na SC Villa ya Uganda, mchezo utakaochezwa katika uwanja wa Amani mjini Zanzibar.

Kesho Jumamosi, Yanga SC watakua wenyeji wa APR ya kutoka nchini Rwanda katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa (CAF CL) kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, mchezo utakaochezeshwa na mwamuzi Bernard Camille, akisaidiwa na Eldrick Adelai, Gerard Pool na Allister Bara kutoka nchini Shelisheli.

Jumapili Azam FC watakua wakicheza dhidi ya Bidvest FC kutoka nchini Afrika Kusini katika mchezo wa Kombe la Shirikisho (CAF CC) kwenye uwanja wa Azam Complex Chamazi, mwamuzi wa mchezo huo ni Gait Oting akisaidiwa na Abdallah Gassim, Casim Dehiya, mwamuzi wa akiba Ariel James wote kutoka Sudan Kusini.


WAAMUZI WA TANZANIA WAULA CAF



Shirikisho la Mpira wa Miguu barani Afrika (CAF) limetoa orodha ya waamuzi watakaochezesha na kusimamia michezo ya Kombe la Shirikisho Afrika (CC), kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa Afrika (AFCON) pamoja na kuwania kufuzu kwa Fainali za Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20 (U20) mwaka 2017.

Michael Richard Wambura ameteuliwa kuwa Kamisaa wa Mchezo Kombe la Shirikisho Barani Afrika (CAF CC) kati ya Al Shandy ya Sudan dhidi ya FC Lupopo mchezo utakaochezwa siku ya Jumapili nchini Sudan.

Mwamuzi Israel Mujuni akisaidiwa Frank Komba na Soud Lila, mwamuzi wa akiba akiwa ni Mfaume Ali Nassoro katika mchezo kati ya Renaissance Football Club (Chad) v E.S.T. (Tunisia) wa Kombe la Shirikisho Afrika (CAF CC) nchini Chad.

Mchezo namba 97 wa kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa Afrika (AFCON) kati ya Lesotho v Shelisheli Machi 29, 2016 utachezeshwa na Israel Mujuni akisaidiwa na Ferdinand Chacha, Samuel Mpenzu huku mwamuzi wa akiba akiwa Waziri Sheha.

Mwamuzi Mfaume Ali Nassoro atachezesha mchezo kati ya Burundi v Congo DR kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa Afrika kwa Vijana wenye umri chini ya miaka 20 (U20), Aprili 4, 2016 mjini Bunjumbura akisaidiwa na Frank John Komba, Ali Kinduli, huku Martin Eliphas Saanya akiwa mwamuzi wa akiba.

TWIGA STARS WAIFUATA ZIMBABWE


Msafara wa watu 25 wa timu ya Taifa ya Wanawake ya mpira wa miguu “Twiga Stars” unatarajiwa kuondoka leo majira ya saa 4 usiku kuelekea nchini Zimbabwe kwa ajili ya mchezo wa marudiano kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa Afrika kwa Wanawake utakaochezwa siku ya Jumapili mjini Harare.

Twiga Stars inayonolewa na kocha mkuu, Nasra Juma inaondoka ikiwa na matumaini ya kufanya vizuri katika mchezo huo wa marudiano, baaada ya kuwa kambini kwa takribani wiki mbili kwa maandalizi ya mchezo huo.

Nasra amesema makosa yaliyojitokeza katika mchezo uliopita nyumbani, wameyafanyia kazi na sasa wana imani ya kufanya vizuri siku ya Jumapili katika uwanja wa Rufaro mjini Harare na kuweza kusonga mbele katika hatua ya pili.

Mkuu wa msafara ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji na Mwenyekiti wa Kamati ya Soka la Wanawake TFF, Amina Karuma, benchi la ufundi litaongozwa na kocha mkuu Nasra Juma, kocha msaidizie Elyutery Muholery, kocha msaidizi Edina Lema, daktari wa timu Anange Lwila, mtunza vifaa Esther Chaburuma na meneja wa timu Furaha Francis.

Wachezaji wanaosafiri leo ni Fatuma Omary, Stumai Abdallah, Maimuna Khamis, Fatuma Issa, Anastazia Katunzi, Donisia Minja, Happyness Mwaipaja, Wema Richard na Amina Bilal.

Wengine ni Asha Rashid, Mwanahamis Omary, Belina Julius, Fatuma Bashiri, Fatuma Khatibu, Mwajuma Abdallah, Amina Ramadhani, Fatuma Mustafapha na Neema Kiniga.

TFF YATOA TAMKO ZITO



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limesikitishwa na taarifa za upotoshaji za chombo kimoja cha habari ambacho mmoja wa watendaji alipata fursa ya kuhudhuria mkutano mkuu kama mgeni mwalikwa uliomalizika mwishoni mwa wiki jijini Tanga.

Katika hali inayotia mashaka, siku mbili kabla ya mkutano huo, chombo hicho kiliripoti kuwa wajumbe walikuwa wanalalamika kwa kutopelekewa nyaraka zinazohusiana na mkutano, wakati ukweli ni kuwa nyaraka hizo zilitumwa tangu mwezi Novemba 2015 zikiwa ni sehemu ya barua ya mwaliko wa kikao. Hivyo isingewezekana mwaliko wa kikao ukapokelewa na nyaraka zisiwepo. TFF inao ushahidi wa nyaraka hizo kuwafikia wajumbe wa mkutano huo.

Katika toleo lake la leo chombo hicho kilidai TFF kupata hasara ya shilingi za kitanzania milioni 500.

TFF inaviomba vyombo vya habari kuacha kupotosha juu ya taarifa za mkutano mkuu kuwa shirikisho lilipata hasara (loss) , TFF haifanyi biashara yoyote mpaka kufikia kupata hasara, kilichotokea ni kuongezeka kwa nakisi (deficit) katika bajeti ya mwaka 2014.

Matumizi yaliongezeka kutokana na kulipa madeni ambayo uongozi wa sasa uliyakuta uliyosababisha hata basi la timu ya Taifa likamatwe, kuwepo kwa michezo mingi ya timu za Taifa (Taifa Stars, Twiga Stars, Serengeti Boys), gharama ambazo zilijumuisha kambi za maandalizi za timu pamoja na safari.

Kwa kuwa TFF haifanyi biashara yoyote, matumizi yaliongezeka zaidi ya bajeti iliyokuwa imeratajiwa na kufanya kuwepo na upungufu wa zaidi ya milioni 490.

Aidha TFF imesikitishwa na taarifa zilizotolewa na baadhi ya vyombo vya habari mwishoni mwa wiki iliyopita, kuhusiana na suala la tiketi za Elektroniki.

Ifahamike kwamba TFF ndiyo ilianzishwa matumumizi ya tiketi hizo kabla hazijasitishwa na Serikali mwaka jana kutokana na kubaini mapungufu katika utekelezaji.

TFF haijawahi kugomea kuwepo kwa mfumo huo wa ki elektorniki, na kwa kushirikiana na Serikali kupitia Wizara ya Habari Utamaduni, Sanaa na Michezo wanaendelea na mazungumzo juu ya mfumo huo.

Vikao vinaendelea kati ya Wizara na TFF ili kuona njia gani itaweza kutumika katika uendeshaji wa kuingia viwanjani kw aka kutumia mfumo wa ki elektroniki na kesho kutakuwepo na kikao Wizarani kujadili mradi huo.

TFF inatafakari juu ya hatua za kuchukua dhidi ya wanaotoa taarifa za upotoshaji huo.

SIMBA YAMVUA UNAHODHA ISIHAKA HASSAN, YAMFUNGIA KWA MWEZI MMOJA


Klabu ya Simba imemvua umakamu nahodha beki wake wa kati Hassan Isihaka kutokana na kitendo chake cha utovu wa nidhamu kwa kocha wa klabu hiyo Jackson Mayanja.

Afisa habari wa Simba Haji Manara amesema, mbali na Isihaka kuvuliwa unahodha kamati ya utendaji ya klabu hiyo imetangaza kumsimamisha mlinzi huyo wa kati kwa muda wa mwezi ujao tangu siku aliyopewa barua ya kusimamishwa kwa muda usiojulikana.

“Kamati ya utendaji ya klabu ya Simba imemsimamisha Hassan Isihaka kwa muda wa mwezi mmoja toka siku aliyopewa barua atajiunga na timu baada ya mwezi mmoja na katika kipindi hicho cha mwezi mmoja atakuwa akilipwa nusu mshahara”, amesema Haji Manara wakati wa mkutano na waandishi wa habari.

“Lakini kutokana na ukubwa wa klabu ya Simba na uzito wa kosa alilolifanya, amevuliwa unahodha, tarejea kama mchezaji wa kawaida”

Isihaka amesimamishwa kutokana na kumtolea kauli kali kocha wake Jackson Mayanja kwasababu ya kumuweka benchi katika mechi kadhaa hususan ya Simba na Yanga kisha kumpanga kwenye mchezo wa kombe la FA dhidi ya Singida United.

Sunday, March 13, 2016

SIMBA YAZIDI KUZITIMULIA VUMBI YANGA NA AZAM


SIMBA leo imeendelea kujidhatiti kileleni mwa ligi kuu ya soka ya Tanzania Bara baada ya kuichapa Prisons bao 1-0 katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Ushindi huo umeiwezesha Simba kuendelea kuongoza ligi hiyo, ikitofautiana na Yanga kwa pointi sita na Azam kwa pointi tisa.

Hata hivyo, Yanga na Azam, ambazo zimecheza mechi pugufu, zinaweza kupunguza tofauti hiyo ya pointi iwapo zitashinda mechi zake za vipo. Yanga inavyo viporo viwili wakati Azam inavyo viporo vitatu.

Bao pekee  na la ushindi la Simba lilifungwa na kiungo Awadh Juma, zikiwa zimesalia dakika tatu kabla ya mchezo huo kumalizika.

Simba itabidi kujiulaumu kwa kushindwa kutoka uwanjani na ushindi mkubwa wa mabao, kwani ilipata nafasi nyingi nzuri za kufunga mabao, lakini ilizipoteza


TFF YAMALIZA MKUTANO WAKE MKUU JIJINI TANGA


 

Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) jana limefanya Mkutano Mkuu wa Mwaka katika Ukumbi wa Hoteli ya Regal Naivera jijini Tanga ambapo mgeni Rasmi alikua ni Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mwantumu Mahiza.
 
Katika hotuba yake kwa wajumbe wa mkutano huo, Mahiza aliushukuru uongozi wa TFF nchini kwa kuweza kuandaa mkutano mkuu mzuri na wa kisasa ambao pia ulifanyikia katika mkoa wake wa Tanga.
 
Akiongea na wajumbe wa mkutano mkuu, Mahiza alisema, TFF ina changamoto ambazo inapaswa kuzifanyia kazi kwa na hasa katika kuendeleza soka la wanawake nchini ambalo bado mwamko wake uko chini sana.
 
Mahiza alisema, Mpira wa miguu kwa sasa ni ajira nzuri ambayo inasaidia kujikwamua kiuchumi kwa wachezaji pamoja na familia zao, nayaomba makamouni yajitokeze kuwekeza katika mpira wa miguu na hasa katika soka la wanawake.
 
“Mahitaji ya wanawake katika kushiriki/kucheza mpira wa miguu ni makubwa zaidi, tofauti na wanaume hivyo kuangalia jinsi gani wadhamini wanapatikana ili kuweza kuwasaidia wanawake” alisema Mahiza.
 
Mkutano ulijadili Ajenda za kawaida ambazo ni Kufungua Mkutano ni Uhakiki wa Wajumbe, Kuthibitisha Muhtsari wa Mkutano Mkuu uliopita, Yatokanayo na Mkutano uliopita, Hotuba ya Rais, Taarifa kutoka kwa Wanachama, Kuthibitisha ripoti ya utekelezaji wa Kamati ya Utendaji.
 
Zingine ni Kuthibitisha ripoti ya Ukaguzi wa Hesabu 2013, Kuthibitisha ripoti ya Kamati ya Ukaguzi wa Hesabu, Kupitisha bajeti ya 2015, Marekebisho ya Katiba, Mengineyo na Kufunga Mkutano.
 
Baada ya majadiliano ya kina mkutano mkuu pia uliazimia kuahirisha ajenda ya marekebisho ya Katiba hadi Mkutano Mkuu ujao utakaofanyika mwezi Disemba mwaka huuu.

Wakati huo huo Leo Jumapili asubuhi Mkuu wa Mkoa Tanga, Mwantumu Mahiza ameweka jiwe la msingi katika eneo la kituo cha michezo cha kukuzia vipaji lilipo eneo la Mikanjuni jijini Tanga.
 
Akiongea wakati wa uzinduzi wa uwekaji jiwe la msingi, Mahiza alisema wamejisikia faraja mkoa wa Tanga kupata nafasi hiyo kuwa mkoa wa kwanza kupata kituo cha kukuzia vipaji nchini.
 
Mahiza alisema uongozi wa Serikali mkoa wa Tanga utashirikiana na Chama cha Mpira wa Miguu mkoa wa Tanga (TRFA)/TFF katika kusaidia usimamizi wa uendeshaji wa kituo hicho.
 
Mahiza ameishukuru TFF kwa kuamua kuwekeza katika ujezi wa kituo hicho, ambacho baaade kitatoa nafasi kwa vijana kupata ajira kupitia mpira na shughuli nyingine za maendeleo ya kiuchumi ikiwemo utalii na watu kupata ajira katika kituo hicho.

YANGA, AZAM ZAWAONYESHA UBABE APR NA BIDVEST



WAWAKILISHI wa Tanzania katika michuano ya klabu za Afrika, Yanga na Azam jana walijiweka kwenye mazingira mazuri ya kusonga mbele baada ya kuibuka na ushindi dhidi ya APR ya Rwanda na Bidvest ya Afrika Kusini.

Wakati Yanga iliichapa APR mabao 2-1 katika mechi ya michuano ya klabu bingwa Afrika iliyochezwa mjini Kigali, Azam iliitandika Bidvest mabao 3-0 katika mechi ya michuano ya Kombe iliyochezwa mjini Johannesburg.

Timu hizo nne zinatarajiwa kurudiana wiki mbili zijazo mjini Dar es Salaam, huku Yanga na Azam zikiwa zinahitaji sare ya aina yoyote ili ziweze kusonga mbele.

Beki Juma Abdul na kiungo Thabani Kamusoko ndio walioiwezesha Yanga kutoka uwanjani wakiwa wababe baada ya kuifungia mabao hayo mawili.

Katika mechi hiyo iliyochezeshwa na Duncan Lengani, aliyesaidiwa na washika vibendera Clemence Kanduku na Jonizio Luwizi wote wa Malawi, hadi mapumziko Yanga walikuwa mbele kwa bao 1-0.

Bao hilo lilifungwa na Juma Abdul Jaffar dakika ya 20 kwa shuti la mpira wa adhabu ndogo umbali wa mita 30, baada ya Haruna Niyonzima kuangushwa.

Kamusoko aliifungia Yanga bao la pili dakika ya 74, akimalizia pasi ya mshambuliaji Donald Dombo Ngoma.

APR ilipata bao la kujifariji dakika ya tatu ya muda wa nyongeza baada ya kutimu dakika 90 za kawaida lililofungwa na Patrick Sibomana.

Nayo Azam ilijipatia mabao yake matatu kupitia kwa kiungo Salum Abubakar ‘Sure Boy’ dakika ya 51, beki Shomary Kapombe dakika ya 56 na mshambuliaji na Nahodha John Bocco ‘Adebayor’ dakika ya 59.

Wawakilishi wengine wa Tanzania, JKU ya Zanzibar wamefungwa mabao 4-0 na wenyeji SC Villa katika mchezo wa kwanza wa raundi ya kwanza Kombe la Shirikisho, uliochezwa kwenye Uwanja wa Mandela, Kampala, Uganda.
Mabao ya Villa yalifungwa na Mike Ndera, Mike Serumaga, Umar Kasumba na Godfrey Lwesibawa.

Saturday, March 12, 2016

SERIKALI YAWAPONGEZA RITCHIE NA LULU KWA KUTWAA TUZO ZA FILAMU ZA AFRIKA





Na Immaculate Makilika MAELEZO

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  amesema Serikali imefarijIka kwa ushindi wa wasanii wa filamu nchini walioshinda tuzo za  filamu Afrika za mwaka 2016 (African Magic Viewers Choice Award) ziliyofanyika jijini Lagos nchini Nigeria mwishoni wa wiki iliyopita.

Waziri Mkuu Majaliwa, amesema hayo leo katika ukumbi wa mikutano ulipo katika  Ofisi yake Jijini Dares Salaam, alipokutana na washindi wa tuzo za  filamu Afrika za mwaka 2016 (AMVCA)  ambao ni  Elizabeth Michael ‘Lulu’ aliyeshinda tuzo ya Filamu Bora ya Afrika Mashariki na Single  Mtambalike ‘Richie’ aliyeshinda tuzo ya Filamu Bora ya Kiswahili pamoja Naibu Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo, Mhe. Annastazia Wambura,Katibu Mkuu wa wizara Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo, Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Tanzania Bi Joyce Fisso na wasanii wa filamu.

 “Serikali imefarijika sana kwa nyie kwenda Nigeria na kushinda na mmetumia lugha ya Kiswahili, lazima tutumie nafasi hii kuwatangaza  pia  mmuendelee na fani hii ili kuvutia wengi zaidi” amesema Waziri Mkuu Majaliwa.

Aidha, Waziri Mkuu amewapongeza wasanii hao na kusema kuwa  Serikali itaendelea kushirikiana  na wasanii wakati wowote na amewataka kujipanga vizuri kutumia vyama vyao vya sanaa na kusisitiza kuwa  Mhe.  Rais John Pombe Magufuli ametoa matamko kadhaa kuhusu sanaa  na wasanii  na ameendelea kushughulikia malalamiko yao ikiwemo suala la COSOTA, na kusema kuwa  baada ya taratibu zote kukamilika  suala hilo litasimamiwa na Wizara inayohusika na kazi za Sanaa.

Waziri Mkuu Majaliwa, pia amewataka watanzania kuacha tabia ya kutojiamini  na kujidharau, na kuwataka watu waige mfano kwa wasanii hao, na kuwashauri wasanii wote kwa ujumla kutumia vyombo vya habari kujiimarisha na kujitangaza.

Kwa  upande wao, wasanii waliopata  tuzo hizo kwa filamu ya “mapenzi ya Mungu” ya Elizabeth Michael na filamu ya “Kitendawili” ya Single  Mtambalike, wameishukuru Serikali kwa kuwathamini na kuonesha  ushirikiano katika kazi zao za sanaa, na wameahidi kuendelea kutengeneza  kazi nzuri za sanaa ili ziweze kuitangaza Tanzania kimataifa.

Naye, Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania(TAFF) Saimon Mwakifamba ameishukuru Serikali kwa jitihada mbalimbali  inazofanya katika kusaidia tasnia ya sanaa kwa ujumla na ameahidi kuendelea kushirikiana na  Serikali katika kuendeleza tasnia hiyo kimataifa.

Friday, March 11, 2016

SIMBA YEREJEA KILELENI LIGI KUU

KAMA ilivyotarajiwa, Simba SC imerejea kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kufuatia ushindi wa mabao 3-0 jioni ya leo dhidi ya Ndanda FC ya Mtwara Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Shukrani kwao, wafungaji wa mabao hayo, kiungo Mwinyi Kazimoto Mwitula kipindi cha kwanza na mshambuliaji Mganda, Hamisi Friday Kiiza mawili kipindi cha pili.
Simba SC sasa inafikisha pointi 51 baada ya kucheza mechi 22 na kuwashushia nafasi ya pili, mabingwa watetezi, Yanga SC wenye pointi 50 za mechi 21.
Simba walipata bao lao la kwanza dakika ya 35, baada ya Kazimoto kutuliza vizuri krosi ya Ibrahim Hajib iliyowapita kipa wa Ndanda, Jeremiah Kisubi na mabeki wake na kufumua shuti la kiufundi la juu lililotinga nyavuni.
Mshambuliaji wa Uganda, Kiiza akaipatia Simba bao la pili dakika ya 57 kwa kichwa akimalizia kona ya Hajib, hilo likiwa bao lake la 17 msimu huu katika Ligi Kuu na kumfikia mshambuliaji wa Yanga, Mrundi Amissi Joselyn Tambwe aliyekuwa anaongoza.
Kiiza akafunga bao lake la 18 msimu huu wa Ligi Kuu dakika ya 73 na kumpiku Tambwe, akimalizia pasi ya mshambuliaji Danny Lyanga aliyeuwahi mpira uliotemwa na kipa Jeremiah Kisubi kufuatia shuti kali la mpira wa dhabu la kiungo Mzimbabwe, Justive Majabvi.
Mchezo mwingine wa Ligi Kuu leo, Mbeya City
Imeifunga 2-0 Stand United Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya, mabao ya Raphael Daudi na Haruna Shamte. 

CHANZO CHA HABARI: BLOGU YA BINZUBEIRY

Wednesday, March 9, 2016

MKUTANO MKUU TFF MACHI 12-13 JIJINI TANGA


Mkutano Mkuu wa mwaka wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) uliokuwa ufanyike mwezi Disemba mwaka jana sasa utafanyika wikiendi hii Jumamosi na Jumapili tar 12-13 March 2016 jijini Tanga.

Ajenda za mkutano huu ni kwa mujibu wa katiba ya TFF. Mkutano mkuu utahitimishwa kwa uwekaji wa jiwe la msingi la kituo cha kukuza na kuendeleza vipaji vya uchezaji mpira, kituo kitakachojengwa jijini Tanga.

Mkutano huo utafanyika katika ukumbi wa hoteli ya Regal Naivera.

MKOPI MCHEZAJI BORA WA LIGI KUU FEBRUARI


Mshambuliaji Mohamed Mkopi wa timu ya Tanzania Prisons amechaguliwa kuwa mchezaji bora wa Februari kwa Ligi Kuu ya Vodacom msimu huu wa 2015/2015.

Mkopi katika mwezi huo uliokuwa na raundi nne, alicheza mechi zote nne za timu yake dhidi ya Mbeya City, Yanga, Mwadui na Mgambo Shooting. 


Alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika mechi hizo ambapo zote ilitoka sare, hivyo kupata jumla ya pointi nne.

Katika mechi hizo ambapo Tanzania Prisons ilifunga mabao matatu, Mkopi alifunga bao moja na kusaidia kupatikana mabao mengine mawili.

Mshambuliaji huyo ambaye mpaka sasa amefunga mabao sita kwenye Ligi hiyo, aling’ara zaidi katika mechi mbili kati ya hizo nne ambapo alichaguliwa kuwa mchezaji bora.

Mkopi ambaye ni mshambuliaji wa kati alichaguliwa mchezaji bora kwenye mechi dhidi ya Mwadui iliyochezwa mkoani Shinyanga, na ile dhidi ya Yanga iliyofanyika Uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya.

Kwa kunyakua tuzo ya mchezaji bora kwa Februari, Mkopi atazawadiwa kitita cha sh. 1,000,000 (milioni moja) na wadhamini wa Ligi hiyo, kampuni ya Vodacom.

Wachezaji bora wa miezi miwili iliyopita ni kiungo Thaban Kamusoko wa Yanga (Desemba 2015), na beki Shomari Kapombe wa Azam FC (Januari 2016).

JONESIA RUKYAA KUCHEZESHA KOMBE LA DUNIA


Mwamuzi wa kike wa Kimataifa wa Tanzania mwenye beji ya FIFA, Jonesia Rukyaa ameteuliwa kuungana na waamuzi kutoka nchini Kenya kuchezesha mchezo wa kuwania kufuzu kwa Fainali za Kombe la Dunia kwa Wanawake  wenye umri chini ya miaka 17 (WWC-Q 17) mwishoni mwa mwezi huu.

Jonesia Rukyaa atakua mwamuzi wa akiba katika mchezo huo kati ya Misri dhidi ya Cameroon utakaochezwa jijini Cairo wikiendi ya tarehe 25,26,27 Machi, 2016.

Mwamuzi wa kati katika mchezo huo atakua ni Carolyne Wanjala (Kenya), akisaidiwa na Carolyne Kiles (Kenya), Mary Njoroge (Kenya), huku kamisaa wa mchezo huo akiwa ni Leah Annette Dabanga kutoka nchi ya Afrika ya Kati.

MKWASA ATANGAZA KIKOSI CHA STARS KITAKACHOIVAA CHAD



Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) inayodhaminiwa na bia ya Kilimanjaro Premieum Lager, Charles Boniface Mkwasa leo ametangza kikosi cha wa wachezaji 25 kwa ajili ya mchezo wa kuwania kufuzu kwa fainali za Mataifa Afrika (AFCON) dhidi ya Chad, Machi 23, 2016 mjini Djamena.

Akiongea na waandishi wa habari wakati akitangaza kikosi hicho, Mkwasa amewaomba wachezaji aliowaita katika kikosi hicho, kujiweka fit katika mazoezi wanayoyafanya katika vilabu vyao, kwani hakutakua na muda wa kufanya mazoezi kwa ajili ya mchezo huo wa ugenini.

“Ligi Kuu ya Vodacom, michuano ya CAF (CL, CC) inachezwa wikiendi ya tarehe 18-20 Machi, hivyo wachezaji wote watakua na majukumu katiak timu zao, muda wa kufanya mazoezi kwa pamoja kwa ajili ya mchezo huo hautakuwepo, ndio maana nasisitiza wachezaji niliowachagua wahakikishe wanajilinda wenyewe kwa kuwa fit wanapokuja kwenye safari ya mchezo huo wa machi 23, 2016” alisema Mkwasa

Wachezaji walioitwa Taifa Stars ni magolikipa Aishi Manula (Azam FC), Ally Mustapha (Young Africans) na Shaban Kado (Mwadui FC), walinzi ni Juma Abdul, Haji Mwinyi, Kelvin Yondani (Young Africans), Shomari Kapombe, Erasto Nyoni, David Mwantika (Azam FC) na Mohamed Hussein (Simba SC).

Viungo Himidi Mao (Azam FC), Ismail Juma (JKU), Jonas Mkude, Said Ndemla, Mwinyi Kazimoto (Simba SC), Mohamed Ibrahim, Shiza Kichuya (Mtibwa Sugar), Farid Mussa (Azam FC), Deus Kaseke (Young Africans).

Washambuliaji ni Nahodha Mbwana Samatta (KRC Genk), Thomas Ulimwengu (TP Mazembe), John Bocco (Azam FC), Elias Maguri (Stand United), Jeremia Mgunda (Tanzania Prisons) na Ibrahim Hajibu (Simba SC).

Monday, March 7, 2016

SIMBA YAREJEA KILELENI LIGI KUU


SIMBA jana ilirejea kileleni mwa ligi kuu ya soka ya Tanzania Bara baada ya kuichapa Mbeya City mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Washambuliaji Ibrahim Hajib na Daniel Lyanga ndio walioiwezesha Simba kutoka uwanjani na pointi zote tatu baada ya kuifungia mabao hayo mawili.

Kwa ushindi huo, Simba sasa imefikisha pointi  48 baada ya kucheza mechi 21 na kuziengua Yanga na Azam, zenye pointi 47 kila moja huku zikiwa na mechi moja mkononi kila moja.

Lyanga, aliyeingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Bryan Majwega, alifunga bao la kwanza dakika ya 75 baada ya kuuwahi mpira uliotemwa na kipa Hannington Kalyesebula.

Hajib aliiongezea Simba bao la pili dakika ya 90 baada ya kuwatoka mabeki wa Mbeya City na kufumua shuti kama krosi lililotinga moja kwa moja wavuni.

Sunday, March 6, 2016

LULU, RITCHIE WANG'ARA TUZO ZA FILAMU AFRIKA

WASANII wawili wa filamu wa Tanzania, Single Mtambalike 'Ritchie' na Elizabeth Michael 'Lulu', juzi walipeperusha vyema bendera ya Taifa baada ya kushinda tuzo mbili za 'Africa Magic Viewer's Choice Awards 2016.

Katika tuzo hizo zilizotolewa mjini Lagos, Nigeria na kuhudhuriwa na waigizaji wengi maarufu barani Afrika, Ritchie ameshinda tuzo ya Best Indigeous Language Movie/TV Series Swahili kupitia filamu ya Kitendawili.

Kwa upande wake, Lulu ambaye alikuwa kivutio kutokana na mwonekane wake usiku huo, alishinda tuzo ya Best Movie East Africa kupitia filamu yake ya Mapenzi.

Miongoni mwa watanzania waliohudhuria hafla ya utoaji wa tuzo hizo ni pamoja na msanii nyota wa muziki wa kizazi kipya, Ali Kiba, ambaye licha ya kumpongeza Lulu, walipiga picha ya pamoja.

Kiba, mmoja wa wasanii wa Tanzania wanaoheshimika barani Afrika, ni miongoni mwa wanamuziki waliotumbuiza katika sherehe hiyo.

Akizungumza baada ya kupokea tuzo yake, Ritchie aliwashukuru mashabiki wake walioko Tanzania na kwingineko barani Afrika kwa kumpigia kura na kumwezesha kuibuka mshindi katika kipengele hicho.

Naye Lulu, aliyekuwa akizungumza huku akibubujikwa na machozi, aliishukuru familia yake, hasa mama yake kwa kumuunga mkono katika kipindi chote cha matatizo, ikiwa ni pamoja na kukaa lupango kwa miaka kadhaa, kutokana na tuhuma za kumuua, mwigizaji nyota wa zamani nchini, Steven Kanumba.

Washindi wa tuzo zingine ni kama ifuatavyo:

BEST ART DIRECTOR (MOVIE/TV SERIES)
The refugees – Frank Raja Arase

BEST TELEVISION SERIES
Daddy’s Girls – Ariyike Oladipo

BEST MAKEUP ARTIST (MOVIE/TV SERIES)
Ayanda – Louiza Calore

BEST SHORT FILM
A day with death – Oluseyi Amuwa

BEST WRITER (MOVIE AND TV SERIES)
Ayanda – Trish Malone

BEST LIGHTING/DESIGN
Common Man- Stanley Ohikhuare

BEST CINEMATOGRAPHY
Tell me sweet something- Paul Michaelson

BEST SOUND EDITING
Marquex Jose Guillermo

BEST PICTURE EDITING
Rebecca- Shirley Frimpong-Manso

BEST COSTUMING
Uche Nancy- Dry

BEST INDIGENOUS LANGUAGE MOVIE (SWAHILI)
Kitendawali- Single Mtambalike

BEST INDIGENOUS LANGUAGE MOVIE (HAUSA)
Dadin Kowa- Salisu Balarabe

BEST INDIGENOUS LANGUAGE MOVIE (YORUBA)
Binta Ofege – Abiodun Jimoh and Jumoke Odetola

BEST INDIGENOUS LANGUAGE MOVIE (IGBO)
Usekwu Igbo- Paul Igwe

BEST DOCUMENTARY
Faaji Agba- Remi Vaughan Richards

BEST SUPPORTING ACTOR
A soldier’s story- Sambassa Nzeribe

BEST SUPPORTING ACTRESS
Before 30- Tunbosun Aiyedhin

BEST ACTOR IN A COMEDY
Jenifa’s Diary- Folarin Falana

BEST ACTRESS IN A COMEDY
Jenifa’s Diary- Funke Akindele

TRAILBLAZER AWARD
Kemi Lala-Akindoju

INDUSTRY MERIT AWARD
Sadiq Daba
Bukky Ajayi

BEST MOVIE- SOUTHERN AFRICA
JOYCE MHANGO CHAIGUALA

BEST MOVIE- EASTERN AFRICA
Mapenzi- Elizabeth Michael

BEST MOVIE- WESTERN AFRICA
Chinny Onwugbenu, Chichi Nwoko and Genevieve Nnaji – Road to Yesterday

BEST ACTRESS IN A DRAMA
Falling- Adesua Etomi

BEST ACTOR IN A DRAMA
A Soldier’s Story- Daniel K. Daniel

BEST DIRECTOR
Tell me Sweet Something- Akin Omotosho

BEST OVERALL MOVIE
Dry- Stephanie Linus