KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 31, 2013

KESHO NI YANGA NA JKT RUVU




Raundi ya 12 ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inaendelea kesho (Novemba 1 mwaka huu) kwa mechi kati ya JKT Ruvu na Yanga itakayochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni.

Viingilio katika mechi hiyo ni sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 kwa VIP A. Tiketi zitauzwa siku ya mechi uwanjani katika magari maalumu kuanzia saa 4 asubuhi.

Novemba 2 mwaka huu kutakuwa na mechi nne; Mgambo Shooting na Coastal Union (Uwanja wa Mkwakwani, Tanga), Tanzania Prisons na Oljoro JKT (Uwanja wa Sokoine, Mbeya), Azam na Ruvu Shooting (Azam Complex, Dar es Salaam), na Mtibwa Sugar na Rhino Rangers (Uwanja wa Manungu, Morogoro).

Raundi hiyo itakamilika Novemba 3 mwaka huu kwa mechi moja ambapo Mbeya City itakuwa mwenyeji wa Ashanti United kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Mechi za kukamilisha mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo zitachezwa Novemba 6 na 7 mwaka huu. Novemba 6 ni JKT Ruvu vs Coastal Union, Ashani United vs Simba, Kagera Sugar vs Mgambo Shooting, Rhino Rangers vs Tanzania Prisons na Ruvu Shooting vs Mtibwa Sugar.

Novemba 7 mwaka huu, Azam itacheza na Mbeya City wakati Yanga itacheza na Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

MABOMU YARINDIMA MECHI YA SIMBA NA KAGERA SUGAR, ZATOKA SARE




PENALTI iliyopigwa dakika za nyongeza katika mchezo wa Ligi Kuu ya Bara uliozikutanisha Simba na Kagera Sugar muda mfupi uliopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, ilibadili matokeo na kufanya mchezo huo kuisha kwa sare ya bao 1-1.


Huku mashabiki wengi wakidhani mechi hiyo ingemalizika kwa Simba kuibuka na ushindi wa bao 1-0, mwamuzi Mohamed Theofile wa Morogoro aliipa penalti Kagera wakati mwamuzi wa akiba akiwa ameshaonyesha dakika nne za nyongeza na mashabiki kutoamini kilichotokea.

Beki Joseph Owino ndiye aliyesababisha penalti hiyo baada ya kumchezea vibaya Daudi Jumanne wa Kagera ndani ya eneo la hatari ambapo, beki Salum Kanoni wa Kagera alifunga penalti hiyo na sekunde chache baadaye mwamuzi alimaliza pambano hilo.

Awali Simba ilipata bao la kuongoza dakika ya 45 lililofungwa na Amisi Tambwe baada ya mabeki wa Kagera kujichanganya katika kuokoa. Bao hilo lilidumu hadi timu hizo zilipoenda kupumzika.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi lakini hadi dakika ya 85, hakuna timu iliyoweza kupata bao kutokana na safu zote za ushambuliaji kutokuwa makini.

Mshambuliaji wa Kagera, Themi Felix pamoja na winga Paul Ngwai leo hawakuweza kufurukuta mbele ya mabeki wa Simba waliokuwa wakiongozwa na nahodha wao Nassor Masoud ‘Chollo’.

Nao washambuliaji wa Simba, Tambwe na Betram Mombeki hawakuweza kufuruka kutokana na mabeki wa Kagera kucheza kwa nguvu zaidi wakiongozwa na Maregesi Mwangwa ambaye ni nahodha wao.

Muda mfupi baada ya Kanoni kufunga bao, alienda kushangilia akiwa sambamba na wenzake mahala ambapo mashabiki wa Simba wamekaa na kuzua tafrani ya kurushiwa chupa za maji na viti vilivyovunjwa na mashabiki hao.

Kutokana na hali hiyo, askari wa Jeshi la Polisi waliokuwepo uwanjani hapo walilazimika kulipua mabomu matatu ya machozi ili kutawanya mashabiki hao, hali iliyozua hali ya taharuki uwanjani hapo.

Matokeo haya yanaifanya Simba kufikisha pointi 21 na kubaki katika nafasi ya nne baada ya kucheza mechi 12.Nayo Kagera imepanda hadi nafasi ya tano ikiwa na pointi 17.

BLATTER, HAYATOU WAMPONGEZA MALINZI


Rais mpya wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania, Jamal Malinzi ameendelea kupokea salamu za pongezi baada ya kushinda wadhifa huo katika uchaguzi uliofanyika Oktoba 27 mwaka huu.

Salamu nyingine za zimetoka kwa Rais wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), Sepp Blatter ambapo amempongeza Malinzi kwa kuchaguliwa na kumtakia kila la kheri katika majukumu yake ya kuongoza mchezo huo nchini.

Blatter amesema ana uhakika ufahamu wake na uwezo wake katika uongozi ni muhimu katika kuimarisha maendeleo ya mpira wa miguu nchini, na kuongeza kuwa milango ya FIFA iko wazi wakati wowote anapotaka kujadili masuala yanayohusu mchezo huo.

“Nakutakia wewe na kamati mpya ya Utendaji iliyochaguliwa kila la kheri, nguvu, na kila aina ya mafanikio kwa changamoto zilizo mbele yenu,” amesema Rais Blatter katika salamu zake.

Wengine waliomtumia Rais Malinzi salamu za pongezi ni Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu la Kenya (FKF), Sam Nyamweya, Rais wa Heshima wa Shirikisho la Vyama vya Mpira wa Miguu Uganda (FUFA), Lawrence Mulindwa, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Mwanza (MZFA) na Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Wilaya ya Arumeru (ADFA), Peter Temu.
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), Issa Hayatou amempongeza Jamal Malinzi kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) katika uchaguzi uliofanyika Oktoba 27 mwaka huu.

Katika salamu zake kwa niaba ya Kamati ya Utendaji ya CAF na familia ya mpira wa miguu Afrika, Rais Hayatou amesema uchaguzi huo unampa Rais Malinzi fursa ya kuupeleka mbele mpira wa miguu nchini Tanzania.

Amesema CAF ina imani uwezo wake katika uongozi, uzoefu na ujuzi katika mpira wa miguu havitausaidia mpira wa miguu Tanzania pekee bali Afrika kwa ujumla, na kuongeza kuwa ataendeleza ushirikiano uliopo ili kuwanufaisha zaidi vijana wa bara hili.

Rais Hayatou amemtakia Rais Malinzi kila la kheri katika kipindi chake cha uongozi na kumhakikishia kuwa CAF iko pamoja naye katika kusukuma mbele gurudumu la kuendeleza mpira wa miguu.

Monday, October 28, 2013

AZAM YAISHUSHA SIMBA KILELENI


AZAM jioni ya leo imeukwaa uongozi wa ligi kuu ya Tanzania Bara baada ya kuichapa Simba mabao 2-1 katika mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Ushindi huo umeiwezesha Azam kuwa na pointi 23 baada ya kucheza mechi 10 wakati Simba inashika nafasi ya pili ikiwa na pointi 20.

Hata hivyo, Azam inaweza kuenguliwa kileleni mwa ligi hiyo iwapo Mbeya City itawabwaga ndugu zao wa Prisons kesho katika mechi itakayochezwa kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.

Mabingwa watetezi Yanga wanaweza kuchupa nafasi ya pili iwapo kesho wataifunga Mgambo JKT kwenye Uwanja wa Taifa.

Kwa sasa, Yanga inashika nafasi ya nne ikiwa na pointi 19 baada ya kucheza mechi 10 na iwapo itashinda kesho, itafikisha pointi 22.

Simba ilikuwa ya kwanza kupata bao kupitia kwa Ramadhani Singano 'Messi' kabla ya John Bocco kuisawazishia Azam na Kipre Tchetche kuongeza la pili.

EL MAAMRY MWENYEKITI BODI YA TFF


Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) umemteua Said Hamad El Maamry kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ambayo kazi yake kubwa ni kusimamia mali za shirikisho.
El Maamry ambaye kitaaluma ni mwanasheria na Mwenyekiti wa zamani wa TFF wakati huo ikiwa Chama cha Mpira wa Miguu Tanzania (FAT) ataongoza bodi hiyo yenye jumla ya wajumbe watano.

Wajumbe wengine wa bodi hiyo ni Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera ambaye anakuwa Makamu Mwenyekiti, Dk. Ramadhan Dau, Mohamed Abdulaziz na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Stephen Mashishanga.

YANGA, MGAMBO JKT DIMBANI KESHO



Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inakamilisha raundi ya kumi na moja kesho (Oktoba 29 mwaka huu) kwa mechi tatu huku Yanga ikiwa mwenyeji wa Mgambo Shooting kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Mbeya City na Tanzania Prisons. Rhino Rangers na JKT Ruvu zitacheza katika Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora.

Raundi ya 12 ya ligi hiyo itaanza Oktoba 31 mwaka huu kwa mechi kati ya Simba na Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati Novemba Mosi mwaka huu kutakuwa na mechi kati ya Yanga na JKT Ruvu kwenye uwanja huo huo.

Novemba 2 mwaka huu kutakuwa na mechi nne; Mgambo Shooting na Coastal Union (Uwanja wa Mkwakwani, Tanga), Tanzania Prisons na Oljoro JKT (Uwanja wa Sokoine, Mbeya), Azam na Ruvu Shooting (Azam Complex, Dar es Salaam), na Mtibwa Sugar na Rhino Rangers (Uwanja wa Manungu, Morogoro).

Raundi hiyo itakamilika Novemba 3 mwaka huu kwa mechi moja ambapo Mbeya City itakuwa mwenyeji wa Ashanti United kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Mechi za kukamilisha mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo zitachezwa Novemba 6 na 7 mwaka huu. Novemba 6 ni JKT Ruvu vs Coastal Union, Ashani United vs Simba, Kagera Sugar vs Mgambo Shooting, Rhino Rangers vs Tanzania Prisons na Ruvu Shooting vs Mtibwa Sugar.

Novemba 7 mwaka huu, Azam itacheza na Mbeya City wakati Yanga itacheza na Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

TANZANITES, MSUMBIJI ZAINGIZA MIL 6



Pambano kati ya timu ya Taifa ya wanawake kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20 ya Tanzania (The Tanzanite) dhidi ya Msumbiji lililochezwa juzi (Oktoba 26 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam limeingiza sh. 6,190,000.

Washabiki waliohudhuria mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya kwanza ya Kombe la Dunia, Kanda ya Afrika iliyomalizika kwa The Tanzanite kuibuka na ushindi wa mabao 10-0 walikuwa 5,003. Viingilio vilikuwa sh. 1,000, sh. 2,000, sh. 5,000 na sh. 10,000.

Mgawo wa mapato hayo ulikuwa kama ifuatavyo; Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) sh. 944,237.29, gharama za kuchapa tiketi sh. 2,247,900, gharama za mchezo sh. 599,573 wakati wamiliki wa uwanja walipata sh. 449,679.

Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) lilipata sh. 149,893 huku Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) likipata sh. 1,798,718.

Mechi ya marudiano kati ya The Tanzanite na Msumbiji itachezwa kati ya Novemba 8 na 10 mwaka huu.

KIM ATEUA 30 FUTURE YOUNG TAIFA STARS


Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen ametaja kikosi cha wachezaji 30 wa timu ya pili (Future Young Taifa Stars) kitakachoingia kambini Novemba 9 mwaka huu ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya michuano ya Kombe la Chalenji.

Kipa Ivo Mapunda wa Gor Mahia ya Kenya ni miongoni mwa wachezaji walioitwa na Kim kwenye kikosi hicho ambacho hukitumia kuangalia uwezo wa wachezaji kabla ya kuwajumuisha kwenye timu ya wakubwa.

Kikosi hicho kamili ambacho Novemba 13 kitacheza mechi ya kirafiki na Taifa Stars kinaundwa na; makipa Aishi Manula (Azam), Hussein Shariff (Mtibwa Sugar) na Ivo Mapunda (Gor Mahia, Kenya).

Mabeki ni David Luhende (Yanga), Hassan Mwasapili (Mbeya City), Himid Mao (Azam), Issa Rashid (Simba), Ismail Gambo (Azam), John Kabanda (Mbeya City), Kessy Khamis (Mtibwa Sugar), Michael Pius (Ruvu Shooting), Miraji Adam (Simba), Mohamed Hussein (Kagera Sugar), Said Moradi (Azam) na Waziri Salum (Azam).

Viungo ni Amri Kiemba (Simba), Farid Mussa (Azam), Haruni Chanongo (Simba), Hassan Dilunga (Ruvu Shooting), Jonas Mkude (Simba), Khamis Mcha (Azam), Ramadhan Singano (Simba), Simon Msuva (Yanga), William Lucian (Simba).

Washambuliaji ni Elias Maguli (Ruvu Shooting), Hussein Javu (Yanga), Joseph Kimwaga (Azam), Juma Liuzio (Mtibwa Sugar), Mwagane Yeya (Mbeya City) na Paul Nonga (Mbeya City).
Kim amesema kikosi cha Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager chenyewe kitaingia kambini Novemba 12 jijini Dar es Salaam ambapo siku inayofuata ndipo kitakapocheza mechi na Future Young Taifa Stars.

Baada ya mechi hiyo, kambi ya Future Young Taifa Stars itavunjwa wakati Taifa Stars itaondoka Novemba 14 mwaka huu kwenda Arusha ambapo itaweka kambi na kucheza mechi ya kirafiki ya kimataifa kabla ya kwenda Nairobi, Kenya kwenye michuano ya Kombe la Chalenji itakayofanyika kuanzia Novemba 27 hadi Desemba 12 mwaka huu.

Wachezaji 16 wa kikosi cha Taifa Stars kitakachoingia kambini Novemba 12 mwaka huu kinaundwa na Ally Mustafa (Yanga), Mwadini Ali (Azam), Aggrey Morris (Azam), Kelvin Yondani (Yanga), Shomari Kapombe (AC Cannes, Ufaransa) na Nadir Haroub (Yanga).

Erasto Nyoni (Azam), Vincent Barnabas (Mtibwa Sugar), Salum Abubakar (Azam), Mwinyi Kazimoto (Markhiya, Qatar), Frank Domayo (Yanga), Athuman Idd (Yanga), Mrisho Ngasa (Yanga), Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, DRC), Mbwana Samata (TP Mazembe, DRC) na John Bocco (Azam).

Wachezaji wengine kumi kutoka Future Young Taifa Stars baadaye wataongezwa katika kikosi kitakachounda timu ya Tanzania Bara (Kilimanjaro Stars) kwa ajili ya michuano ya Kombe la Chalenji.

MALINZI AWASAMEHE WAFUNGWA WOTE WA SOKA, ISIPOKUWA WATOA RUSHWA NA WAPANGAJI WA MATOKEO



RAIS mpya wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ametoa msameha kwa wanachama wote wa shirikisho hilo waliofungiwa chini ya Utawala wa rais aliyemaliza muda wake, Leodegar Tenga, isipokuwa tu wale ambao adhabu zao zinatokana na makosa ya rushwa na kupanga matokeo.

Maana yake- Michael Richard Wambura aliyekwama kabisa kugombea nafasi yoyote chini ya utawala wa Tenga, sasa yuko huru kugombea au kuteuliwa kwa nafasi yoyote ya uongozi katika soka ya Tanzania.

Akizungumza mara baada ya kutangazwa mshindi katika uchaguzi uliomalizika usiku wa manane jana ukumbi wa NSSF Water Front, Dar es Salaam, Malinzi aliiagiza Sekretarieti ya TFF chini ya Katibu wake, Angetile Osiah mara moja kuandika barua za misamaha kwa wote wanaotumikia adhabu za utawala wa Tenga.
“Hata rais wa nchi anapoingia madarakani huwa anatoa misamaha, nami nachukua fursa hii kuomba ridhaa yenu Wajumbe, kwa kuwa huu ni uongozi mpya, basi tufungue ukurasa mpya, nipeni ridhaa yenu, watu wote waliofungiwa chini ya utawala uliomaliza muda wake, wasamehewe tuanze upya. Isipokuwa wale tu ambao adhabu zao zinatokana na rushwa na upangaji matokeo,”alisema Malinzi.
Malinzi alisema muda si mrefu atakutana na Kamati yake ya Utendaji kujipanga na amewataka wajumbe wote kujiandaa kwa hilo.
Kwa upande wake, Tenga pamoja na kumpongeza Malinzi, aliahidi kumkabidhi ofisi Jumamosi ijayo.
Malinzi ameshinda Urais wa TFF baada ya kupata kura 72, dhidi ya 52 za mpinzani wake Athumani Jumanne Nyamlani.
Katika uchaguzi huo uliofanyika kwenye ukumbi wa NSSF Water Front, Dar es Salaam, Walace Karia alifanikiwa kushinda nafasi ya Makamu wa Rais kwa kupata kura 67 akiwashinda Nassib Ramadhani kura 52 na Imani Madega sita.

IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA BIN ZUBEIRY.

THE TANZANITES YADHIHIRISHA KAIJAGE BONGE LA KOCHA



 TIMU ya soka ya Taifa ya Wanawake ya vijana wa chini ya umri wa miaka 20, The
Tanzanites mwishoni mwa wiki iliyopita ilijiweka kwenye nafasi nzuri ya kufuzu kucheza
fainali za Kombe la Dunia baada ya kuichapa Msumbiji mabao 10-0.

 Katika mechi hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, The Tanzanites,
inayofundishwa na Kocha Rogasiun Kaijage, ilikwenda mapumziko ikiwa mbele kwa mabao
5-0.

Kutokana na ushindi huo, The Tanzanites sasa inahitaji sare ya aina yoyote wakati timu hizo
zitakaporudiana wiki mbili zijazo mjini Maputo. Msumbiji itaweza kusonga mbele iwapo tu
itashinda mechi hiyo mabao 11-0, kitu ambacho hakuna anayeamini kwamba kinaweza
kutokea.

Licha ya kuibuka na ushindi huo mkubwa wa mabao, vijana wa Tanzanites walionyesha soka
ya kiwango cha juu na kuwafanya wapinzani wao wachanganyikiwe mapema. Bila shaka
walicheza kwa kufuata maelekezo ya kocha wao.

Safu ya ulinzi ya timu hiyo ilicheza kwa utulivu mkubwa, huku mabeki wa kati,Fatuma Issa na
Anastazia Anthony wakitumia akili zaidi katika kuokoa mashambulizi na kumfanya kipa wao,
Celina Julius asipate misukosuko mingi.

Safu ya kiungo, iliyokuwa ikiundwa na Deonisia Daniel na Amina Ali na ile ya ushambuliaji
iliyokuwa ikiundwa na Vumilia Maarifa, Neema Paul, Shelder Boniface na Theresa Yona nazo
zilicheza kwa uelewano mkubwa, hasa kipindi cha pili.

Vijana wa The Tanzanites walionekana kukosa uelewano katika dakika za mwanzo za
mchezo huo, lakini hilo lilitokana na ugeni wao katika mashindano makubwa kama hayo na pia
kutozoea kucheza mbele ya idadi kubwa ya mashabiki.

Walianza kubadilika baada ya Neema Paul kufunga bao la kuongoza dakika ya sita na
mfungaji bora wa michuano ya kimataifa ya Airtel Rising Stars, Shelder Boniface kuongeza
la pili dakika ya 24.

Kuanzia wakati huo, The Tanzanites ilianza kutawala mchezo huku viungo wake, Deonisia na
Amina wakitawala dimba la kati na kuwafanya mashabiki waliofika uwanjani kushuhudia
mechi hiyo kuweweseka kwa furaha muda wote.

Deonisia na Amina waliongeza mabao mengine mawili dakika ya 32 na 41. Bao la Deonisia
lilikuwa tamu zaidi kwani alifunga kwa mpira wa adhabu uliotinga moja kwa moja wavuni.

Cheche za The Tanzanites zilidhihirika zaidi kipindi cha pili wakati Neema Paul, Shelder,
Amina na Stumai kufunga mabao mengine matano na kuweza rekodi ya kuwa timu ya kwanza
ya wanawake kuibuka na ushindi mkubwa wa mabao.

Kiwango kilichoonyeshwa na mabinti hao kimedhihirisha wazi kuwa, Kaijage ni kocha
aliyepaswa kupewa timu hiyo mapema zaidi kutokana na ukweli kwamba, anatumia mbinu
tofauti na zilizokuwa zikitumiwa na makocha wa zamani wa Twiga Stars, Charles Boniface
na Mohammed Rishard Adolph.

Kuna wakati Boniface na Adolph walipokwenda kuhudhuria mafunzo ya ukocha nje ya nchi,
Kaijage alikabidhiwa kwa muda jukumu la kuinoa Twiga Stars na akaiwezesha kuibuka na
ushindi mnono wa mabao 6-1 dhidi ya Eritrea.

Katika mechi hiyo, wachezaji wa Twiga Stars walionyesha soka ya kufundishwa. Kila
aliyeshuhudia mechi hiyo, alirejea nyumbani moyo wake ukiwa umeridhika si tu kutokana na
ushindi huo mkubwa, bali pia kiwango kilichoonyeshwa na timu hiyo.

Hilo lilijirudia tena katika mechi kati ya The Tanzanites na Msumbiji. Kila aliyekuwepo
uwanjani, alionekana kufurahia aina ya mchezo ulioonyeshwa na mabinti wa Kitanzania na
uwezo walioonyesha wa kufunga mabao.

Kutokana na kiwango kilichoonyeshwa na The Tanzanites katika mechi dhidi ya Msumbiji, ni
wazi kwamba mabinti hao wameanza kuwiva, wanafundishika na wana uwezo mkubwa wa
kuichezea Twiga Stars katika siku zijazo.

Jambo la msingi ni kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) pamoja na wadau wa soka,
kuiunga mkono timu hiyo kwa nguvu zote ili iweze kufanya vizuri katika mashindano hayo.

Kilichojidhihirisha ni kwamba, Twiga Stars na The Tanzanites zinahitaji changamoto mpya,
ari mpya na mbinu mpya hivyo mabadiliko ya uendeshaji wake ni muhimu kwa wakati huu.

Pamoja na mwanzo mzuri wa The Tanzanites, inasikitisha kuona kuwa, TFF haikutoa hamasa
ya kutosha kwa mashabiki kufika uwanjani kwa wingi kuishangilia. Vilevile ilishangaza kuona
kuwa, TFF ilipanga viingilio vya juu wakati inafahamu wazi kwamba, timu za wanawake
hazina mvuto mkubwa kwa mashabiki wa soka nchini.

Pengine lingekuwa jambo la muhimu kwa TFF kuweka viingilio vya chini kwenye maeneo yote
ya uwanja ili mashabiki wengi zaidi wahamasike kwenda kuishangilia. Ingekuwa vyema zaidi
iwapo TFF ingeweza kiingilio maalumu kwa wanawake ili kuwavutia waipende timu yao.

Ikumbukwe kuwa, wakati Mkwasa alipotangaza kujiuzulu kuifundisha Twiga Stars,
malalamiko yake makubwa yalikuwa ni timu hiyo kutothaminiwa na TFF na kutopata
maandalizi mazuri kama ilivyo kwa timu ya wanaume, Taifa Stars.

Uamuzi uliochukuliwa na Mkwasa ulikuwa wa kijasiri na ulistahili kupongezwa kwa sababu
ulionyesha wazi jinsi alivyokuwa tayari kuwajibika kutokana na matokeo mabaya ya timu hiyo
bila kujali kiini cha tatizo kipo wapi.

Ukweli ni kwamba, Mkwasa atakumbukwa kwa kuifikisha juu timu hiyo, akiiwezesha kushiriki
fainali za Afrika miaka mitatu iliyopita nchini Afrika Kusini, ikiwa ni mara ya kwanza katika
historia ya timu hiyo.

Safari ya Twiga Stars kisoka ilianza mbali, miaka ya mwishoni mwa miaka ya 1990, wakati
huo ikiwa inaundwa na wachezaji wengi kutoka timu ya Sayari, iliyokuwa na maskani yake
Magomeni, Dar es Salaam.

Twiga Stars ilipitia mikononi kwa makocha wengi. Alikuwepo marehemu Suleiman Gwaje,
akaja marehemu Iddi Machuppa na baadaye ikawa chini ya Mkwasa na Adolph. Kabla ya
Mkwasa kujiuzulu, alikuwa akiinoa timu hiyo kwa kushirikiana na Nasra Juma kutoka
Zanzibar.

Mafanikio ya Twiga Stars kimataifa yalianza kuonekana chini ya Mkwasa, ambaye ndiye
aliyeiongoza katika fainali za Afrika, fainali za All Africa Games na fainali za COSAFA. Kwa
jumla, kocha huyo ndiye aliyeiingiza Twiga Stars kwenye ramani ya kimataifa kisoka.

Hata hivyo, kushindwa kwa Twiga Stars kufanya vizuri katika michuano ya mwaka jana
kuliacha maswali mengi, hasa kutokana na kiwango cha chini ilichoonyesha katika mechi za
kirafiki dhidi ya Zimbabwe, Afrika Kusini na Ethiopia.

Katika mechi hizo tatu, wachezaji wa Twiga Stars walishindwa kucheza kwa uelewano na
ilikuwa haieleweki aina ya mfumo wanaocheza. Pia hawakuwa na stamina ya kutosha. Ilikuwa
kama vile ni timu iliyofanya mazoezi kwa kipindi kifupi.

Ni dhahiri kwamba uwezo wa Mkwasa kuinoa timu hiyo ulikuwa umepungua na alihitajika
 mtu mwingine kuchukua nafasi yake. Hii ni kwa sababu alikaa na wachezaji wa timu hiyo kwa
miaka mingi hivyo inawezekana walimzoea kupita kiasi na pengine heshima yao kwake ilianza
kupungua.

Ieleweke kuwa, kocha anapozoeana na kuwa karibu na wachezaji kwa miaka mingi, ni rahisi
heshima na nidhamu kuanza kushuka kwa vile watamuona na kumchukuluia kama mwenzao.

Bravo TFF kwa kumteua Kaijage kuwa mrithi wa Mkwasa na ni jukumu la viongozi wapya wa
TFF kuipatia timu hiyo huduma zote muhimu na ikiwezekana kuitafutia wadhamini ili iweze
kufika mbali zaidi.

MALINZI RAIS MPYA TFF, KARIA MAKAMU WA RAIS



RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) anayemaliza muda wake, Leodegar Tenga usiku wa kuamkia leo amemtangaza rasmi Jamal Malinzi kuwa rais mpya wa Shirikisho hilo baada ya kushinda uchaguzi wa rais wa TFF kwenye Ukumbi wa NSSF Waterfront, Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa, Malinzi alipata kura 73, huku mpinzani wake pekee Athuman Nyamlani akiambulia kura 52. Hii ni tofauti ya kura 21 kati ya mshindi Malinzi na Nyamlani.

Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Hamidu Mbwezeleni ndiye aliyetangaza matokeo hayo na kuamsha shangwe ukumbini hapo huku wapambe wa wagombe wengine wakitoka vichwa chini.

Awali kabla ya uchaguzi huo, Nyamlani ndiye aliyekuwa Makamu wa rais wa TFF.

Kwa upande wa makamu wa rais wa TFF, aliyeshinda ni Wallace Karia aliyepata kura 67, akifuatiwa na Ramadhan Nasib aliyepata kura 52 na Iman Madega aliyepata kura 6 tu.

Kabla ya uchaguzi huo, Karia amewahi kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi inayoendesha Ligi Kuu ya Bara na Ligi Daraja la Kwanza.

KIDAU, MGOYI, KABURU, NYENZI WASHINDA UJUMBE

Katika uchaguzi wa wajumbe wa kamati ya utendaji, Wilfred Kidau alishinda kwa upande wa kanda ya Dar es Salaam akiwabwaga Alex Crispine Kamuzelya, Muhsin Said Balhabou na Omary Isack Abdulkadir. Aliyeshinda kanda ya Pwani na Morogoro ni Geofrey Nyange ‘Kaburu’ aliyewabwaga Farid Nahdi, Juma Abbas Pinto, Riziki Juma Majala na Twahil Twaha Njoki.

Khalid Mohamed ameshinda ujumbe kanda ya Tanga, Kilimanjaro akimshinda Davis Elisa Mosha. Naye Msafiri Mgoyi ameshinda kanda ya Tabora na Kigoma akimshinda Yusuf Hamis Kitumbo. Ayoub Nyenzi ameshinda kwa upande wa Iringa na Mbeya akiwashinda David Lugenge, John Exavery Kiteve, na Elias Mwanjala.

Kwa upande wa Ruvuma na Njombe aliyeshinda ni James Mhagama aliyemshinda Stanley William Lugenge. Naye Athuman Kambi ameshinda kanda ya Lindi na Mtwara akiwashinda Francis Kumba Ndulane na Zafarani Mzee Damoder. Na Blassy Kiondo ameshinda kanda ya Katavi, Rukwa akimbwaga Ayubu Nyaulingo.
 
IMETOLEWA KWENYE BLOGU YA SHAFFIH DAUDA

Saturday, October 26, 2013

NYAMLANI, MALINZI NANI KUMRITHI TENGA LEO?


UCHAGUZI mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), unatarajiwa kufanyika leo kwenye ukumbi wa NSSF Water Front ulioko Gerezani, Dar es Salaam.

Katika uchaguzi huo, nafasi inayotolewa macho zaidi ni ya rais, ambayo inagombewa na makamu wa kwanza wa rais, anayemaliza muda wake, Athumani Nyamlani na Jamil Malinzi. Mshindi wa nafasi hiyo ndiye atakayerithi mikoba ya rais anayemaliza muda wake, Leodegar Tenga, ambaye ameliongoza shirikisho hilo kwa miaka minane.

Wagombea kwenye uchaguzi wa TFF ni Athuman Jumanne Nyamlani na Jamal Emily Malinzi (Rais), Imani Omari Madega, Ramadhan Omar Nassib na Wallace Karia (Makamu wa Rais).


Kwa upande wa wajumbe wa Kamati ya Utendaji ni Kalilo Samson (Kanda namba 1- Geita na Kagera), Jumbe Odessa Magati, Mugisha Galibona, Samwel Nyalla na Vedastus Lufano (Kanda namba 2- Mara na Mwanza), Epaphra Swai na Mbasha Matutu (Kanda namba 3- Shinyanga na Simiyu).

Ali Mtumwa, Elley Simon Mbise na Omar Walii Ali (Kanda namba 4- Arusha na Manyara), Ahmed Idd Mgoyi na Yusuf Hamis Kitumbo (Kanda namba 5- Kigoma na Tabora), Ayubu Nyaulingo na Blassy Mghube Kiondo (Kanda namba 6- Katavi na Rukwa), Ayoub Shaibu Nyenzi, David Samson Lugenge, John Exavery Kiteve, Lusekelo Elias Mwanjala (Kanda namba 7- Iringa na Mbeya).

James Patrick Mhagama na Stanley William Lugenge (Kanda namba 8- Njombe na Ruvuma), Athuman Kingombe Kambi, Francis Kumba Ndulane na Zafarani Mzee Damoder (Kanda namba 9- Lindi na Mtwara), Hussein Zuberi Mwamba, Stewart Ernest Masima, Charles Komba (Kanda namba 10- Dodoma na Singida), Farid Nahdi, Geofrey Irick Nyange, Juma Abbas Pinto, Riziki Juma Majala) na Twahil Twaha Njoki (Kanda namba 11- Morogoro na Pwani).

Davis Elisa Mosha, Khalid Abdallah Mohamed (Kanda namba 12- Kilimanjaro na Pwani), Alex Crispine Kamuzelya, Kidao Wilfred Mzigama, Muhsin Said Balhabou na Omary Isack Abdulkadir (Kanda namba 13- Dar es Salaam).

MABINTI WA KIBONGO WAWAFANYIA MAUAJI WENZAO WA MSUMBIJI





Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam

TIMU ya soka ya taifa ya wanawake kwa vijana chini ya umri wa miaka 20, The Tanzanites imeifunga Msumbiji mabao 10-0 katika mechi ya kwanza ya raundi ya Kwanza ya Kombe la Dunia kwa mabinti wa umri huo, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam jioni ya leo.

Katika mchezo huo uliohudhuria na mashabiki wachache mno, hadi mapumziko, tayari Tanzanites walikuwa mbele kwa mabao 5-0

Bao la kwanza lilifungwa dakika ya sita na Neema Paul aliyeunganisha pasi ya Theresa Yona, kutoka wingi ya kushoto, wakati mfungaji bora wa michuano ya kimataifa ya Airtel Rising Stars iliyofanyika mwaka huu Nigeria, Shelder Boniface alifunga la pili dakika ya 24 baada ya kupangua ngome na kumpiga chenga hadi kipa.

Deonesia Daniel akafunga bao la tatu kwa shuti kali la mpira wa adhabu lililotinga moja kwa moja nyavuni dakika ya 32 na dakika ya 41, Amina Ali akafunga la nne kwa shuti kali kutoka nje ya eneo la mita 18

Shelider Boniface alifunga bao ambalo lingekuwa la tano dakika ya 45, lakini refa Ines Niyonsara wa Burundi akakataa.

Kipindi cha pili The Tanzanites inayofundishwa na Rogasian Kaijage ilirudi na moto wake na kufanikiwa kupata bao tano, mfungaji Neema Paul aliyeunganisha krosi ya Theresa Yona.

Hatimaye Shelder alifunga bao la sita dakika ya 80 akimalizia mpira uliotemwa na kipa kufuatia shuti la Stumai Abdallah.

Dakika ya 82 Tanzania ikapata bao saba kupitia kwa Amina Ali aliyefumua shuti kutoka katikati ya Uwanja.

Tanzanites walipata bao la nane dakika ya 86 kupitia kwa Deonesia Daniel aliyefunga kwa mkwaju wa penalti, baada ya Shelder Boniface kuangushwa kwenye eneo la hatari.

Dakika ya 89 Tanzania ilipata bao tisa kupitia kwa Amina Ali tena, ambaye alikuwa nyota wa mchezo huo. Stumai Abdallah akaifungia Tanzania bao la 10 dakika ya 90.

Kikosi cha Tanzania kilikuwa; Celina Julius, Stumai Abdallah, Maimuna Said/Amina Hebron dk60, Fatuma Issa, Anastazia Anthony, Deonisia Daniel, Vumilia Maarifa, Amina Ali, Neema Paul, Shlder Boniface na Theresa Yona.

Msumbiji; Paulina Jambo/Catarina Francue dk50, Esperanca Malaita/Delice Assane dk52, Felismisa Moiane, Emma Paulino, Gilda Macamo, Deolinda Gove, Jessica Zunguene, Cidalia Cuta, Nelia Magate, LonicaTsanwane na Onesema David.

IMETOLEWA KUTOKA BLOGU YA BINZUBEIRY

YAHYA MWENYEKITI MPYA BODI YA LIGI, SAIDI MAKAMU MWENYEKITI



Bodi ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara, imepata viongozi wapya kufuatia uchaguzi mkuu uliofanyika jana kwenye ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Golden Jubilee Towers, Dar es Salaam.

Katika uchaguzi huo, Hamad Yahya Juma wa Mtibwa Sugar alichaguliwa kuwa mwenyekiti wakati Saidi Mohamed wa Azam alichaguliwa kuwa makamu mwenyekiti.

Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo, mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Hamidu Mbwelezeni alisema Hamad alishinda nafasi hiyo kwa kupata asilimia 100 ya kura zilizopigwa.

Mbwelezeni alisema Said naye alishinda nafasi ya makamu mwenyekiti kwa kupata asilimia 100 ya kura zilizopigwa.

Kwa mujibu wa Mbwelezeni, katika uchaguzi huo, baadhi ya wapiga kura waliondolewa kutokana na kushindwa kutimiza masharti yanayotakiwa.

Walioshinda ujumbe wa kamati ya utendaji ya bodi hiyo ni Kazimoto Miraji Muzo wa Pamba ya Mwanza na Omary Khatib Mwindadi wa Mwadui.

Akizungumza baada ya uchaguzi huo, Hamad alisema atahakikisha anakomesha vitendo vya rushwa katika michuano ya ligi kuu na ligi daraja la kwanza.

"Siwezi kuahidi kwamba tutacheza fainali za Kombe la Dunia, lengo hasa ni kuhakikisha tunakuza kiwango cha soka nchini,"alisema.

TENGA: TUNAFURAHI KUSIKIA AJENDA KATIKA KAMPENI




Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) anayemaliza muda wake, Leodegar Tenga amesema amefurahishwa na jinsi kampeni za uchaguzi zinazokwenda kutoka na ukweli kuwa wagombea wamekuwa wakielezea kile wanachotaka kuufanyia mpira wa miguu.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye ofisi za TFF leo mchana, Rais Tenga ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) amesema Watanzania wanataka kusikia ajenda za wagombea.

“Ombi langu ni kwamba kampeni zimeanza vizuri, watu wanazungumza hoja zaidi. Ni jukumu la wajumbe kupima na kufanya uamuzi. Kwangu mimi nimejitayarisha kumkabidhi Katiba, Rais mpya wa TFF,” amesema.

Tenga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) amesema kazi kubwa iliyofanywa na uongozi wake ni kujenga taasisi (TFF) pamoja na kuweka mifumo (structure) inayoainisha majukumu ya kila mmoja.

“Ajenda yetu wakati tunaingia madarakani mwaka 2005 ilikuwa ni kujenga taasisi. Tayari taasisi ipo, sasa mtazamo uwe kuushughulia mpira wa miguu wenyewe,” amesema.

Mkutano Mkuu wa TFF unafanyika kesho kwenye ukumbi wa mikutano wa NSSF Waterfront, na tayari wajumbe wa mkutano huo ambao pia utakuwa na ajenda ya uchaguzi siku inayofuata wameshawasili jijini Dar es Salaam.

Wawakilishi kutoka Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), Ashford Mamelodi ambaye ni Ofisa Maendeleo wa kanda hii, Magdi Shams El Din ambaye ni mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya CAF na Rais wa Chama cha Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFA) ni miongoni mwa wageni watakaohudhuria mkutano huo.

NYAMLANI AANZA KAMPENI KWA AHADI TISA


MGOMBEA nafasi ya U-Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Athuman Jumanne Nyamlani amezindua kampeni zake za kuwania ukuu wa shirikisho hilo akipambana na Jamal Malinzi.

Akizindua kampeni zake jana jijini Dar es Salaam, Nyamlani aliweka wazi jinsi atakavyoendeleza mipango ya sasa ya TFF kwa kuwa alishiriki katika kuiandaa na kuipanga chini ya uongozi wa sasa wa Leodegar Tenga.
Nyamlani anaenda mbali zaidi kwa kuweka pia ahadi zake tisa za kutekeleza endapo atapewa ridhaa ya kuliongoza shirikisho hilo. Miongoni mwa ahadi hizo za Nyamlani ni pamoja na;
Moja:
KUIMARISHA USIMAMIZI NA MENEJIMENTI YA SOKA KATIKA NGAZI ZOTE.
Nyamlani anasema akiwa rais wa TFF, kwa kushirikiana na viongozi wa klabu na vyama vya soka vya wilaya na mikoa pamoja na serikali ataimarisha usimamiaji na menejimenti ya soka katika ngazi zote kwa kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa viongozi pamoja na kusimamia sheria na taratibu za uendeshaji wa soka Tanzania.
Mbili: RUSHWA KATIKA SOKA NCHINI.
Nyamlani anakiri kwamba kumekuwa na malalamiko na vitendo vya rushwa ambavyo vinawahusisha viongozi wa soka. Anasema kwa kushirikiana na serikali na viongozi wa soka katika ngazi zote atahakikisha anaendeleza mapambano dhidi ya rushwa katika soka nchini.
Tatu: KUKUZA SOKA LA WATOTO, VIJANA NA WATOTO.
Endapo Nyamlani atachaguliwa kuwa rais mpya wa TFF amesema atalipa uzito wa kipekee soka la watoto wenye umri chini ya miaka 16 na soka la vijana na kukuza vipaji (miaka 9-12, miaka, miaka 13-14, miaka 15-17 na miaka 18-21) pamoja na soka la wanawake. Kazi hii Nyamlani ataitekeleza kwa kuanzisha program mbalimbali za mashindano za kukuza vipaji kwa makundi haya ya vijana kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa soka.
Nne: KUIMARISHA UWEZO WA RASILIMALI FEDHA WA TFF.
Nyamlani anasema akishinda nafasi ya U-Rais wa TFF atahakikisha shirikisho hilo linapata vyanzo endelevu na vya kuaminika vya fedha ili kujenga uwezo wa TFF katika kutekeleza mipango yake na kufikia malengo kikamilifu. Vilevile ataimarisha idara ya masoko ili kuweza kupata wadhamini zaidi na kuweza kuuza nembo za shirikisho hilo.
Tano: KUONGEZA IDADI NA UBORA WA WAAMUZI, MAKOCHA NA WATAALAM WA AFYA YA MICHEZO.
Nyamlani anasema atahakikisha kunakuwa na program endelevu ya mafunzo ya makocha, waamuzi na wataalam wa afya ya michezo ili kuongeza ufanisi wao katika kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa sheria na taratibu zinazoongoza mchezo wa soka nchini na pia waweze kufikia viwango vya kimataifa vilivyowekwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF) na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA).
Pia Nyamlani anasema atahakikisha anaweka msisitizo katika kuhamasisha watu wanaopenda soka na wenye uwezo wajiunge na katika fani hizo jambo ambalo litaongeza idadi ya wataalam hao.
Sita: KUONGEZA UBORA WA LIGI KUU, LIGI DARAJA LA KWANZA, LIGI ZA WILAYA NA MIKOA.
Anasema michuano ya Ligi Daraja la Kwanza, Ligi za Wilaya, Mikoa na Ligi Kuu ni ngazi muhimu ya kukuza soka katika nchi yoyote. Ni imani yake kwamba ligi hizo zikiimarishwa kwa kushirikiana na viongozi wa soka wa wilaya, mikoa na bodi ya kusimamia uendeshwaji wa ligi kuu Tanzania itaweza itaweza kuinua ubora wa soka na kufikia viwango vya kimataifa na kuweza kuhimili ushindani wakati wote.
Nyamlani anasema atashirikiana na viongozi wa soka na vyama vya kitaalam ili kuweza kuboresha kanuni mbalimbali zitakazowawezesha wachezaji vijana kuwa wachezaji wa kulipwa. Vile vile Nyamlani anasema atasimamia ipasavyo suala la malipo kwa klabu na vituo vya kukuzia vipaji pindi wachezaji wao wanapouzwa au kupanda viwango na kuwa wachezaji wa kulipwa.
Saba: KUONGEZA IDADI YA MAWAKALA.
Nyamlani ana imani kwamba ili mpira wa Tanzania ukue kwa kasi ni lazima tuongeze idadi ya wachezaji wanaocheza soka la kulipwa nje ya nchi kwa kufanya hivyo ni lazima kuwa na mawakala wanaozingatia weledi na siyo uwakala wa kupeana kiholela huku wakishindwa kuuza hata mchezaji mmoja tangu mtu alipopewa kazi hiyo.
Nane: KUIMARISHA USHIRIKIANO WA SERIKALI NA TFF.
Nyamlani anasema atahakikisha anasimamia, kukuza na kuendeleza uhusiano uliopo sasa kati ya TFF na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa imani kwamba jambo hili ni muhimu kwa ustawi wa soka Tanzania kwa sababu ni ukweli soka kwa sasa ni ajira rasmi kwa vijana ambao ndiyo nguzo ya taifa.
Tisa: KUIMARISHA USHIRIKIANO WA TFF, CAF NA FIFA.
Nyamlani anasema atahakikisha kuwa anakuza na kuendeleza uhusiano mzuri uliopo kati ya TFF na CAF na FIFA ili kuongeza kasi ya ukuaji wa soka nchini kufikia viwango vya kimataifa kwa kutumia misaada mbalimbali ya kitaalam na kifedha inayotolewa na taasisi hizo kubwa Afrika na duniani.
NAAM, HIZO NDIZO SERA ZA NYAMLANI KAZI KWENU WAPIGA KURA!

Friday, October 25, 2013

MSUMBIJI U20 KUTUA DAR LEO, KUKIPIGA NA TWIGA JUNIORS KESHO


Timu ya Taifa ya wanawake kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20 inawasili nchini kesho (Ijumaa, Oktoba 25 mwaka huu) saa 8.30 mchana tayari kwa mechi ya kwanza ya raundi ya kwanza ya Kombe la Dunia dhidi ya Tanzania itakayofanyika Jumamosi (Oktoba 26 mwaka huu).

Msumbiji itatua Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) kwa ndege ya LAM ikiwa na msafara wa watu 25 wakiwemo wachezaji, benchi la ufundi na viongozi. Timu hiyo itafikia kwenye hoteli ya Sapphire iliyopo maeneo ya Gerezani, Dar es Salaam.

Mara baada ya kuwasili JNIA, kocha na nahodha wa timu hiyo watazungumza na waandishi wa habari juu ya mechi hiyo itakayochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni.

Kwa upande wa U20 chini ya Kocha Rogasian Kaijage imejiandaa vizuri kwa ajili ya mechi hiyo, na kesho saa 10 jioni itafanya mazoezi yake ya mwisho Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Viingilio kwa mechi hiyo ni sh. 1,000 kwa viti vya rangi ya kijani, bluu na rangi ya chungwa. Viingilio vingine ni sh. 2,000 kwa VIP C, sh. 5,000 kwa VIP B wakati VIP A itakuwa sh. 10,000.

Kamishna wa mechi hiyo Evelyn Awuor kutoka Kenya tayari amewasili nchini wakati waamuzi kutoka Burundi wanatarajia kuwasili leo saa 1 usiku kwa ndege ya Kenya Airways wakiunganishia safari yao Nairobi, Kenya. Maofisa wote wa mechi hiyo wanafikia hoteli ya New Africa.

UCHAGUZI MKUU BODI YA LIGI LEO



Uchaguzi wa Bodi ya Ligi Tanzania (Tanzania Professional League- TPL Board) unafanyika kesho (Oktoba 25 mwaka huu) kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Golden Jubilee Tower kuanzia saa 3 asubuhi.

Mgeni rasmi katika mkutano huo wa Bodi ya TPL ambao unafanyika kwa mara ya kwanza atakuwa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga.

Kwa mujibu wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF, wajumbe wanaounda Mkutano wa Uchaguzi ni wenyeviti kutoka klabu 24 za Ligi Daraja la Kwanza (FDL), na 14 wa klabu za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL).

Viongozi wa klabu za FDL wamefikia hoteli ya Royal Valentino iliyoko Barabara ya Uhuru wakati wale wa VPL ambao pia watashiriki Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wamefikia hoteli ya Landmark iliyopo Ubungo.

Wagombea kwenye uchaguzi huo ni Hamad Yahya Juma (Mwenyekiti), Said Muhammad Said Abeid (Makamu Mwenyekiti) wakati wanaoumba ujumbe wa Kamati ya Uendeshaji ni Khatib Omari Mwindadi na Kazimoto Muzo.

Thursday, October 24, 2013

MALINZI ATANGAZA NEEMA TFF



MGOMBEA wa nafasi ya urais katika uchaguzi mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi, amesema itamchukua siku 100 kuleta mabadiliko ya uendeshaji wa mchezo huo.

Malinzi alisema hayo mjini Dar es Salaam jana, alipokuwa akizindua kampeni za uchaguzi huo, unaotarajiwa kufanyika Jumapili.

Alisema iwapo atachaguliwa kushika wadhifa huo, atahakikisha vipaumbele vyote alivyoviweka, vinafanyiwa kazi ili kuleta mageuzi katika mchezo huo.

Alivitaja vipaumbele hivyo kuwa ni kuendeleza soka kwa vijana, makocha, vifaa vya michezo na uboreshaji wa viwanja.

Malinzi alivitaja vipaumbele vingine kuwa ni kuendeleza utulivu ndani ya TFF, kubuni na kuboresha ustawi wa soka nchini na kuunda upya idara ya ufundi iliyoko ndani ya shirikisho hilo.

Alisema anataka idara hiyo iwe kichocheo kikubwa katika maendeleo ya soka nchini na itatengewa fedha nyingi kuliko idara zingine kutokana na umuhimu wake.

Kwa mujibu wa Malinzi, vipaumbele vyake vingine ni kujenga kituo kipya cha soka, kitakachokuwa na uwanja wa kisasa, vituo vya tiba, maabara za utafiti na hosteli za wanamichezo.

Malinzi alisema pia kuwa, atahakikisha ligi kuu ya Tanzania Bara, inakuwa na timu nyingi, tofauti na ilivyo sasa na waamuzi wanapatiwa mafunzo ya mara kwa mara ili waweze kwenda na wakati.

RAGE AMKINGIA KIFUA KIBADENI



MWENYEKITI wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage amesema atawachukulia hatua za kinidhamu, viongozi watakaobainika kuingililia kazi na majukumu ya benchi la ufundi la timu hiyo.

Akizungumza kwa njia ya simu kutoka Tabora jana, Rage alisema hakuna kiongozi anayeruhusiwa kumpangia timu Kocha Mkuu wa timu hiyo, Abdalla Kibadeni.

Rage ametoa tishio hilo baada ya Kibadeni kukaririwa wiki hii akisema kuwa, baadhi ya viongozi wa klabu hiyo wamekuwa wakimshinikiza kuwachezesha wachezaji wanaowapenda.

Kwa mujibu wa Kibadeni, viongozi hao walitaka kuingilia majukumu yake kabla ya mchezo wao wa ligi kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Simba, uliochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

"Kibaden ni kocha halali wa Simba,ana mkataba na amesomea fani hiyo, hivyo kama kuna kiongozi ameingilia kati majukumu yake, tutamshughulikia,"alionya Rage.

Wachezaji, ambao Kibadeni amelalamika kwamba, amekuwa akishinikizwa kuwachezesha ni pamoja na kiungo, Abdulharim Humud, ambaye alionyesha kiwango cha chini katika mechi dhidi ya Yanga.

Katika mechi hiyo, Simba na Yanga zilishindwa kutambiana baada ya kutoka sare ya mabao 3-3. Yanga ilikuwa mbele kwa mabao 3-0 baada ya dakika 45 za kwanza, lakini Simba ilizinduka kipindi cha pili na kusawazisha.

MANJI AMTOLEA UVIVU BRANDTS



KOCHA Mkuu wa Yanga, Ernie Brandts hataongezwa mkataba mpya baada ya mkataba wake wa sasa kumalizika, Juni mwakani.

Uamuzi huo ulifikiwa katika kikao cha pamoja kati ya uongozi wa Yanga na benchi la ufundi, kilichofanyika juzi usiku kwenye hoteli ya Protea mjini Dar es Salaam.

Katika kikao hicho, uongozi wa Yanga uliwakilishwa na Mwenyekiti, Yussuf Manji, makamu wake, Clement Sanga wakati benchi la ufundi liliwakilishwa na Brandts, msaidizi wake, Fred Felix Minziro na kocha wa makipa, Razak Siwa.

Katika kikao hicho kilichofanyika kuanzia saa moja hadi saa sita usiku, ilibainika kuwa, Brandts amekuwa na matatizo kutokana na kutokubali kusikiliza ushauri wa wasaidizi wake.

Habari kutoka ndani ya kikao hicho zimeeleza kuwa, Minziro aliamua kueleza bayana kuwa, Brandts amekuwa akimtolea majibu ya kijeuri kila anapompa ushauri na kukataa kumsikiliza.

"Viongozi walimweleza Brandts kwamba, makosa ambayo amekuwa akiyafanya katika kila mechi ni yale yale, hataki ushauri na amekuwa akitoa lugha chafu kwa Minziro na meneja wa timu," kimeeleza chanzo cha habari.

Imeelezwa kuwa, katika mechi ya ligi kuu dhidi ya Simba iliyochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Brandts alikataa kusikiliza ushauri wa meneja wa timu hiyo wa kumwacha Hamisi Kiiza aendelee na mchezo.

"Hafidhi alimshauri asimtoe Kiiza kwa sababu ameshafunga mabao matatu katika ligi na angeweza kuongeza mengine na alikuwa mwiba kwa mabeki wa Simba, lakini alimjibu kijeuri na kuukataa ushauri wake," kilieleza chanzo cha habari.

Katika mechi hiyo, timu hizo kongwe nchini zilishindwa kutambiana baada ya kutoka sare ya mabao 3-3. Yanga ilikuwa ya kwanza kupata mabao matatu hadi mapumziko, kabla ya Simba kusawazisha kipindi cha pili.

Chanzo hicho cha habari kiliongeza kuwa, kwa vile mkataba wa kocha huyo utamalizika mwishoni mwa ligi hii, uongozi umeamua kutomuongezea mkataba mpya. Pia umemtaka ajirekebishe katika mechi zilizosalia za ligi hiyo, vinginevyo atatimuliwa.

Katika kikao hicho, uongozi wa Yanga pia ulimuonya Siwa kutokana na kiwango cha kipa Ally Mustapha 'Barthez' kushuka, ambapo ameshafungwa mabao 12, tofauti na msimu uliopita, ambapo alimaliza ligi akiwa amefungwa mabao manne.

YANGA YACHINJA, SIMBA YABANWA


MSHAMBULIAJI Hamisi Kiiza jana aling'ara baada ya kuifungia Yanga mabao mawili, ilipoibwaga Rhino Rangers mabao 3-0 katika mechi ya ligi kuu ya soka ya Tanzania Bara, iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kiiza alifunga mabao hayo dakika ya 12 na 81 kutokana na kazi nzuri iliyofanywa na Mrisho Ngasa, ambaye pia alitengeneza bao la tatu lililofungwa na Frank Domayo dakika ya 73.

Ushindi huo umeifanya Yanga iendelee kushika nafasi ya nne katika msimamo wa ligi hiyo, ikiwa na pointi 19 baada ya kucheza mechi 10. Rhino Rangers inaendelea kushika nafasi ya 11 ikiwa na pointi saba.

Katika mechi hiyo, Yanga iliwapumzisha beki Nadir Haroub 'Cannavaro', kiungo Athumani Iddi 'Chuji' na mshambuliaji Didier Kavumbagu, waliocheza dhidi ya Simba mwishoni mwa wiki iliyopita na nafasi zao kuchukuliwa na Rajabu Zahir, Juma Abdul na Simon Msuva.

Iliwachukua Yanga dakika 12 kupata bao la kwanza lililofungwa na Hamisi Kiiza baada ya kazi nzuri iliyofanywa na Mrisho Ngasa, aliyetoa pasi kwa Simon Msuva, aliyemimina krosi, ambayo mabeki wa Rhino Rangers walishindwa kuiokoa, mpira ukamkuta mfungaji, aliyeukwamisha wavuni.

Rhino Rangers haikufanya shambulizi kubwa kwenye lango la Yanga katika kipindi cha kwanza, kutokana na safu yake ya ushambuliaji kushindwa kuelewana vyema na ile ya kiungo. Timu hizo zilikwenda mapumziko Yanga ikiwa mbele kwa bao 1-0.

Vijana hao wa JWTZ walipata nafasi nzuri ya kufunga bao dakika ya 55 wakati mshambuliaji wake, Victor Hangaya alipoingia na mpira ndani ya mita 18, lakini shuti lake lilikuwa mboga kwa kipa Deogratius Munishi 'Dida'.

Baada ya Kiiza kukosa bao lingine dakika ya 72, Frank Domayo alirekebisha makosa dakika moja baadaye kwa kuifungia Yanga bao la pili, kufuatia kazi nzuri iliyofanywa na Ngasa, aliyewahadaa mabeki wawili wa Rhino Rangers.

Bao la tatu la Yanga lilifungwa na Kiiza dakika ya 81, baada ya Ngasa kumtoka  Nurdin Bakari pembeni ya uwanja na kutoa pasi kwa mfungaji, aliyeukwamisha mpira wavuni.

Sophia Wakati ameripoti kutoka Tanga kuwa, Simba na Coastal zimeshindwa kutambiana baada ya kutoka suluhu katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani.

Sare hiyo iliiwezesha Simba kurejea kwenye uongozi wa ligi hiyo kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa kati yake na Azam na Mbeya City, kufuatia kila moja kuwa na pointi 20 baada ya kucheza mechi 10.

Timu zote mbili zilicheza kwa uangalifu kipindi cha kwanza na kufanya mashambulizi machache ya kushtukiza, lakini hakuna iliyoweza kupata bao.

Simba: Abel Dhaira/ Abuu Hashim, Nassoro Masoud 'Cholo'/Edward Christopher,  Haruna Shamte, Gilbert Kaze, Joseph Owino, Jonas Mkude, Ramadhani Singano, Saidi Ndemla, Hamisi Tambwe, Amri Kiemba/Zahoro Pazi, William Lucian 'Galas'.

Coastal Union: Shabani Kado,Mbwana Hamisi, Tamim Othman, Marcus Rafael, Juma Nyoso, Jerry Santo, Daniel Lianga/ Uhuru Selemani, Christopher Odula, Yaiyo Lituma, Haruna Moshi 'Boban', Kenneth Masumbuko.

IBRAHIMOVIC:OLE WAKO RONALDO



ZURICH, Uswisi
MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Sweden, Zlatan Ibrahimovic, amemchimbia mkwara nyota wa timu ya taifa ya Ureno, Cristiano Ronaldo.

Mkwara huo wa Ibrahimovic, unahusu pambano maalumu la michuano ya kuwania tiketi ya kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia kati ya Sweden na Ureno.

Ibrahimovic ameeleza kupitia waraka maalumu aliomwandikia Ronaldo kwamba, atahakikisha Sweden inashinda pambano hilo na kwenda Brazil kucheza fainali za michuano hiyo.

Mshambuliaji huyo wa Sweden amesema, hakutarajia iwapo Sweden ingepangwa kucheza na Ureno, hivyo ni jukumu la kila mmoja kati yao kuhakikisha anaisaidia timu yake.

"Naelewa kwamba watu wengi hawakupendi, lakini kamwe sijawahi kupatwa na hisia hizo kuhusu wewe. Siku zote nimekuwa nikikuona kama mtu dhaifu na haufanani na Zlatan kiuchezaji," ametamba nyota huyo wa Sweden.

Hata hivyo, Ibrahimovic amekiri kuwa, kwa vile hakutakuwa na wachezaji 11 wa Sweden wanaofanana na yeye kiuchezaji, hawezi kuwa na uhakika wa ushindi dhidi ya Ureno.

"Sweden haikufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia 2010. Haya hayakuwa mafanikio kwa Zlatan. Kama itatokea tena hivyo, nitalazimika kutumia njia nyingine ya kukufanya uonekane kama vile umehudhuria hafla, ambayo Lionel Messi alikushinda katika kila kipengele,"ameeleza kupitia waraka huo.

"Hili si tishio. Zlatan hatoi vitisho. Ninazungumzia vitu ambavyo huwa vinatokea. Fainali za Kombe la Dunia zinamuhitaji Zlatan,"amesisitiza Ibrahimovic.

"Nakutakia kila la heri Cristiano, lakini baada ya kusoma haya, sidhani kama utaihitaji. Kama unadhani Pepe anaweza kukulinda kwa Zlatan, umekosea na utalia," aliongeza nyota huyo wa Sweden.

"Huenda baada ya pambano hili kumalizika, tutakuwa marafiki. Nitakuona uwanjani na utaniona kwenye ndoto zako,"ameeleza nyota huyo.

KITABU CHA FERGIE CHAZUA BALAA


LONDON, England
KOCHA Mkuu wa zamani wa Manchester United, Sir Alex Ferguson, amesema Carlos Tevez na Anderson, waliikosesha timu hiyo ubingwa wa Ulaya 2009 katika mchezo wa fainali dhidi ya Barcelona.

Kauli hiyo ya Ferguson ni mwendelezo wa mashambulizi yake kwa wachezaji wa Man United, kupitia katika kitabu chake alichokizindua juzi.

Katika mechi hiyo, Manchester United ilichapwa mabao 2-0 na Barcelona
na Ferguson, ameweka bayana kuwa, chanzo cha kipigo ni Anderson kushindwa kucheza vyema nafasi ya kiungo.

Alisema Anderson alipiga pasi tatu katika dakika 45 za mwanzo, lakini Tevez alikuwa mchoyo na alicheza mechi hiyo kwa ubinafsi.

"Michael Carrick alipwaya, lakini tatizo kubwa lilikuwa kwa Anderson," alisema kocha huyo, ambaye kwa sasa amestaafu.

Katika kitabu hicho, Fergie pia alielezea sababu ya kumpiga bei nahodha wa zamani wa England, David Beckham. Alisema mchezaji huyo alianza kuwa na majivuno na
kujiona mtu mzito kuliko kocha.

Fergie alisema, alianza kukorofishana na Beckham baada ya kumshutumu kwa kucheza vibaya katika michuano ya Kombe la FA dhidi ya Arsenal mwaka 2003, ambapo Man United ilifungwa.

"Dakika moja, ambayo mchezaji wa Manchester United atafikiria ni mkubwa kuliko kocha, alipaswa kuondoka," ameandika Fergie katika kitabu hicho. "David alijiona mkubwa kuliki Alex Ferguson."

Fergie amesema pia kuwa, hakufurahishwa na maisha ya kifahari aliyokuwa akiishi Beckham, baada ya kufunga ndoa na Victoria Adams, mmoja wa wanamuziki waliokuwa wakiunda kundi la Spice Girls.

Katika kipindi cha miaka 26, alichokuwa akiifundisha Man United, Fergie aliiwezesha kutwaa mataji 38 na kuwaongoza wachezaji wengi nyota kama vile Beckham, Eric Cantona, Cristiano Ronaldo, Peter Schmeichel, Bryan Robson, Roy Keane, Jaap Stam na Ruud Van Nistelrooy.

Fergie pia ameelezea alivyoamua kumweka benchi Wayne Rooney na kuiacha hatma yake kwa kocha mpya, David Moyes, alivyokataa kuwa kocha mkuu wa England mara mbili na jinsi alivyogombana na Rafael Benitez.

Kocha huyo wa zamani wa Man United, pia amempamba mshambuliaji Cristiano Ronaldo, akimwelezea kuwa ni mchezaji aliyejaliwa kipaji cha aina yake cha kucheza soka.

KIM POULSEN KUIUNDA UPYA KILIMANJARO STARS


KOCHA Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen ameahidi kufanya mabadiliko makubwa katika kikosi cha Tanzania Bara, kitakachoshiriki michuano ya Kombe la Chalenji, itakayofanyika mwezi ujao nchini Kenya.

Kim alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, mabadiliko hayo yamelenga kuiwezesha timu hiyo kutwaa kombe hilo baada ya kulikosa kwa miaka mitatu.
 
Kocha huyo kutoka Denmark alisema, anataka kutengeneza kikosi imara na chenye wachezaji wengi chipukizi, aliowaona wakati wa michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara.

Kim alisema anatarajia kutangaza kikosi kitakachoshiriki michuano hiyo wakati wowote ili kiweze kuingia kambini mapema kwa ajili ya kujiandaa na michuano hiyo.

Michuano ya Kombe la Chalenji, inayoandaliwa na Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), itafanyika Kenya kuanzia Novemba 27 hadi Desemba 12 mwaka huu.

Nchi wanachama wa CECAFA, zilizothibitisha kushiriki katika michuano hiyo ni Burundi, Djibouti, Eritrea, Ethiopia, Kenya, Rwanda, Somalia, Sudan, Sudan Kusini, Tanzania Bara, Uganda na Zanzibar.

Michuano hiyo itatanguliwa na Mkutano Mkuu wa CECAFA, utakaofanyika Novemba 26 mwaka huu, ambao pamoja na mambo mengine, utakuwa na ajenda ya uchaguzi. Uchaguzi huo ni kwa ajili ya kujaza nafasi nne za wajumbe wa Kamati ya Utendaji.

Wajumbe wanaomaliza muda wao ni Sahilu Gebremarian wa Ethiopia, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa CECAFA, Abdigaani Saed Arab (Somalia), Tariq Atta (Sudan) na Raoul Gisanura (Rwanda).

TCHETCHE, BALOU MAPACHA WA IVORY COAST WANAOIBEBA AZAM


KIPRE Tchetche na Kipre Balou ni wanasoka wawili mapacha kutoka Ivory Coast wanaocheza soka ya kulipwa katika klabu ya Azam, inayoshiriki michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara.

Mapacha hao ni miongoni mwa wanasoka wa kigeni wanaolipwa fedha nyingi na klabu za Tanzania, wakiwemo wengine wanaotoka katika nchi za Kenya, Burundi na Uganda.

Tchetche na Balou walichangia kwa kiasi kikubwa kuiwezesha Azam kushika nafasi ya pili katika ligi kuu msimu uliopita na kupata tiketi ya kushiriki kwa mara ya kwanza katika michuano ya Kombe la Shirikisho na kuishia raundi ya tatu.

Tchetche alikuwa wa kwanza kutua nchini Januari 2011 baada ya kuivutia Azam wakati wa michuano ya Kombe la Chalenji, iliyofanyika Desemba 2010. Ivory Coast ni miongoni mwa timu zilizoalikwa kushiriki kwenye michuano hiyo.

Baada ya kuichezea Azam kwa msimu mmoja, Tchetche alivutiwa na michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara na kuamua kwenda nyumbani, ambapo aliporejea, alimchukua pacha wake Balou.
Akiwazungumzia wachezaji hao, Kocha Mkuu wa Azam, Stewart Hall alisema ni wa kiwango cha juu.

"Tumepata thamani halisi ya pesa. Tchetche na Balou wameongeza thamani katika timu yetu,"alisema Hall.

Tchetche aliifungia Azam mabao 20 msimu uliopita, 17 katika ligi kuu ya Tanzania Bara na mengine matatu katika michuano ya Kombe la Shirikisho.

Kwa upande wake, Balou ni kiungo mkabaji japokuwa wakati mwingine amekuwa akipanda mbele kusaidia mashambulizi.

Stewart hakuwa tayari kutaja kiwango cha fedha wanacholipwa wachezaji hao katika mikataba yao, lakini alisisitiza kuwa, klabu imefaidika kwa kiasi kikubwa kutokana na usajili wao.

"Hatukupata matatizo kuwapata na hawakutugharimu fedha nyingi,"alisema kocha huyo, ambaye ni raia wa Uingereza.

Kwa mujibu wa Stewart, machafuko yaliyotokea nchini Ivory Coast yalichangia kwa kiasi kikubwa kuwafanya wachezaji hao waje kutafuta pesa Tanzania kupitia mchezo wa soka.

"Kwa sababu kulikuwa na machafuko Ivory Coast na klabu za huko hazikuwa na fedha, hawakuwa na lingine la kufanya. Walihitaji pesa,"alisema Stewart.

Akizungumzia ligi kuu ya Tanzania Bara, Tchetche alisema ni ngumu ikilinganishwa na ile ya Ivory Coast, ina ushindani na wachezaji wanatumia nguvu.

"Ligi ina ushindani mkubwa na imetupa changamoto tofauti," alisema mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 26.

"Azam inatutunza vyema na tunayo mikataba mizuri. Siwezi kuzungumzia mshahara wangu, lakini tunajisikia tupo nyumbani,"alisema Tchetche.

Tchetche alisema aliporudi nyumbani Ivory Coast, alimweleza Balou kuhusu ligi ya Tanzania na klabu ya Azam na alikubali kuja naye nchini.

"Nilimweleza pacha wangu kwamba Azam ni klabu kubwa Tanzania na imekuwa ikifanya vizuri kadri siku zinavyosonga mbele na alikubali kuja nami,"alisema Tchetche.

Kabla ya kuja nchini, Tchetche alikuwa akichezea klabu ya JAC ya Ivory Coast wakati Balou alikuwa akichezea klabu ya Sewe Sport. Pia waliiwakilisha Ivory Coast katika michuano ya Kombe la CHAN kwa wachezaji wa ndani.

Tchetche na Balou wanaamini kuwa, Tanzania ni kama kituo cha muda katika harakati zao za kutaka kwenda kucheza soka ya kulipwa barani Ulaya.

"Ndoto zetu ni kucheza katika ngazi za juu zaidi, hatuelewi ni lini mipango hiyo itafanikiwa, lakini hatuna haraka kwa sababu tunafurahia kuwepo hapa,"alisema Balou.

Tayari mapacha hao wameshazoea mazingira ya Tanzania na wameshaanza kufanya jitihada za kujifunza lugha ya kiswahili. Kwa ujumla, wanafurahia maisha ya Tanzania.

Azam, inayomilikiwa na mfanyabiashara maarufu wa Tanzania, Salim Bakhresa, imekuwa ikifanya jitihada kubwa ya kuwekeza katika soka, ikiwa ni pamoja na kujenga uwanja wa kisasa eneo la Mbagala-Chamazi, Dar es Salaam.

Hivi karibuni, Azam ilianzisha kituo chake cha televisheni, ambacho kimeshapata idhini ya kuonyesha laivu mechi za ligi kuu ya Tanzania Bara, inayoendelea katika viwanja mbalimbali nchini.

RONALDO DE LIMA: HAKUNA ANAYEWEZA KUFUTA REKODI YANGU



ZURICH, Uswisi
MEI 25, 1993, Ronaldo Luis Nazario de Lima alianza kuandika ukurasa mpya katika maisha yake kisoka. Akiwa na umri wa miaka 16, aliichezea timu ya Cruzeiro dhidi ya Caldense katika michuano ya kuwania ubingwa wa Jimbo la Minas Gerais nchini Brazil, akiwa na wanasoka kadhaa maarufu wa kulipwa.

Kutokana na umahiri wake wa kusakata kabumbu, Ronaldo alipachikwa majina mengi ya utani kama vile 'O Fenomeno' na ni mmoja wa wachezaji wa aina yake kutokea duniani.

Hadi sasa, Ronaldo anashikilia rekodi ya kufunga mabao 15 katika fainali za Kombe la Dunia na amewahi kuzichezea klabu kadhaa maarufu duniani kama vile PSV Eindhoven ya Uholanzi, Barcelona ya Hispania, Inter Milan na AC Milan za Italia na Real Madrid ya Hispania.

Mwaka huu, Ronaldo ametimiza miaka 20 tangu alipoanza kucheza soka ya kulipwa. Anaikumbuka vyema siku alipopewa nafasi kwa mara ya kwanza ya kuichezea Cruzeiro, akiwa kinda mwenye umri wa miaka 16.

"Ni muda mrefu uliopita. Nakumbuka kila kitu kuhusu maisha yangu kisoka, kuanzia tangu mwanzo, kama vile ilikuwa jana. Nakumbuka jinsi nilivyojisikia nilipoanza kuicheza soka ya kulipwa Cruzeiro. Siku zote nilikuwa na ndoto ya kuwa mwanasoka na ilifurahisha nilipogundua ndoto hiyo ilianza kuwa kweli. Ilikuwa kama vile uchawi. Miguu, mikono na viganja vyangu vilikuwa vikitetemeka. Lakini baada ya mchezo kuanza, nilitulia,"alisema Ronaldo.

Mwanasoka huyo anasema, baada ya kuelezwa na kocha kwamba angecheza mechi hiyo, alichanganyikiwa na moyo wake ulianza kwenda mbio, lakini hicho ndicho alichokuwa akikitaka.

"Niliweza kutulia na kuwa katika hali ya kawaida. Kwa kawaida, wachezaji hupatwa na  kimuhemuhe kabla ya mchezo, lakini baadaye kinatoweka. Unasahau kila kitu unapokuwa kwenye mchezo,"alisema.

Kutokana na kutokuwepo kwa simu za mkononi wakati huo, Ronaldo hakuweza kuwapa taarifa rafiki zake waliokuwa wakiishi Bento Ribeiro, jirani na Rio de Janeiro. Pia hawakuwa na simu za kawaida katika nyumba walizokuwa wakiishi.

Aliwapa taarifa hizo wazazi na ndugu zake, nao wakazisambaza kwa rafiki zake na watu wengine. Kila mmoja alikuwa na hamu kubwa ya kumshuhudia kwa macho akisakata kabumbu katika moja ya klabu kubwa na maarufu nchini Brazil.

Kwa mujibu wa Ronaldo, mechi hiyo haikuonyeshwa kwenye televisheni. Baba yake alilazimika kwenda sehemu fulani ya mji aliokuwa akiishi na kupanda juu ya mlima, ambako aliwasha redio yake na kusikiliza mechi hiyo moja kwa moja. Cruzeiro ilishinda mechi hiyo.

Ronaldo anakumbuka vyema kwamba, mshahara wake wote wa kwanza alimpatia mama yake mzazi kwa vile ndiye aliyempatia sofa kwa ajili ya kulalia walipokuwa wakiishi Bento Ribeiro.

Mwanasoka huyo nyota wa zamani anasema, kutokana na nidhamu aliyokuwa nayo wakati akicheza soka, hakuweza kufanya vitendo, ambavyo vingeharibu maisha yake ama kuchafua jina lake.

"Kila kitu kilikwenda vizuri kama nilivyotaka. Kiukweli, mambo yalikuwa mazuri kuliko nilivyotarajia. Kamwe sikufikiria iwapo ningefika mbali. Siku zote nilikuwa na ndoto ya kuwa mwanasoka tu,"alisema Ronaldo.

Nyota huyo wa zamani wa Brazil anasema, hali ilianza kuwa ngumu kwake baada ya kuondoka Brazil akiwa na umri wa miaka 17 na kwenda Uholanzi kwa vile maisha yalikuwa tofauti. Tatizo kubwa aliloanza kukumbana nalo ni mabadiliko ya hali ya hewa.

Ronaldo anasema kila kitu mwilini mwake kilikuwa kama vile kimeganda, kuanzia miguu, mikono, shingo na masikio. Hali hiyo ilikuwa ikimtokea zaidi alipokuwa mazoezini. Kamwe hakuwaza kuishi katika nchi yenye baridi kali.

Tatizo lingine lilikuwa kwenye chakula na lugha. Hakuweza kuzungumza Kidachi. Ilikuwa vigumu kwake kuchagua aina ya chakula alichotaka kula kwenye 'menyu'. Ilikuwa vigumu kwake kujifunza lugha hiyo.

"Ilinichukua miaka miwili kujifunza lugha na kuielewa na sasa nimeshaisahau kwa vile sijaizungumza kwa muda mrefu. Lakini nilifurahia kuwepo uwanjani,"alisema Ronaldo.

Nyota huyo wa Brazil amewataja wanasoka waliokuwa wakimvutia kuwa ni pamoja na Zico na Marco van Basten wa Uholanzi. Anasema wanasoka hao wawili walikuwa miongoni mwa washambuliaji bora duniani.

Ronaldo anasema maamuzi yote aliyowahi kuyafanya wakati akicheza soka ya kulipwa yalikuwa mazuri na yaliweza kubadili maisha yake. Ameyataja maamuzi hayo kuwa ni kujiunga kwake na klabu za Cruzeiro, PSV Eindhoven, Barcelona, Inter Milan na zinginezo alizowahi kuzichezea.

Mwanasoka huyo anasema, hakuna timu aliyokuwa akipenda kuichezea, akashindwa kufanya hivyo. Anasema alitamani kwenda kucheza soka England, lakini haikuwezekana.

Licha ya kuchezea klabu kubwa kama vile Barcelona na Real Madrid, Ronaldo anasema hajali iwapo baadhi ya watu hawakufurahishwa na kiwango chake. Anasema anachotambua ni kwamba, mashabiki wengi walifurahishwa na staili yake ya uchezaji.

Ronaldo alikuwemo kwenye kikosi cha Brazil kilichotwaa Kombe la Dunia nchini Marekani, lakini hakucheza mechi hata moja. Aliitwa kwenye kikosi hicho kwa ajili ya kupata uzoefu kwa vile kilikuwa kikiundwa na washambuliaji wengi nyota kama vile Romario, Bebeto, Dunga, Rai na Leonardo.

Anasema alikuwa akifurahia kuwaona wachezaji hao kwenye TV, lakini baada ya kuwa nao kwenye kikosi kimoja, furaha yake iliongezeka. Anasema alipata nafasi nzuri ya kujifunza mengi kutoka kwao na pia kucheza nao pamoja.

"Nakumbuka wakati wa mazoezi, nilikuwa nikiwatazama Romario na Bebeto wanavyocheza. Ilikuwa sehemu nzuri ya kujifunza kucheza soka,"alisema.

Akizungumzia fainali zijazo za Kombe la Dunia, zitakazofanyika 2014 nchini Brazil, Ronaldo anasema kikosi cha sasa cha timu hiyo ni tofauti na vya miaka iliyopita. Lakini anakiri kwamba, kikosi hicho kimeonyesha mabadiliko makubwa wakati wa michuano ya Kombe la Mabara.

Ronaldo anasema ushindi wa Brazil katika michuano ya Kombe la Mabara, umewapa faraja kubwa mashabiki kwamba, huenda wakafanikiwa kutwaa Kombe la Dunia nyumbani.

"Tunayo nafasi kubwa,"alisisitiza nyota huyo, ambaye anamiliki vitega uchumi kadhaa, ikiwa ni pamoja na kununua hisa kwenye kampuni mbalimbali.

Ronaldo ametoa nafasi kubwa kwa timu za Hispania na Ujerumani kutwaa kombe hilo mwakani. Lakini pia ametoa nafasi hiyo kwa timu yake ya Brazil kwa vile itakuwa ikicheza nyumbani.

"Naweza kusema kwamba, timu zenye nafasi kubwa ni Brazil, Ujerumani na Hispania,"amesema nyota huyo.
 Ronaldo anatambua vyema kwamba, mshambuliaji Miroslav Klose wa Ujerumani anaweza kufikia rekodi yake iwapo atafunga bao katika fainali hizo. Klose ameweka rekodi ya kufunga mabao 14 katika fainali za kombe hilo.

"Sina wasiwasi wa kuvunjwa kwa rekodi yangu. Siku zote naamini kwamba, rekodi zinaweza kuvunjwa. Ipo siku atatokea mtu wa kuvunja rekodi hiyo,"alisema Ronaldo.

"Nilitengeneza jina langu kwa sababu ya kufunga magoli na hilo haliwezi kusahaulika. Historia yangu binafsi na mabao 15 niliyofunga katika Kombe la Dunia, kamwe haviwezi kufutika,"alisisitiza.

"Kama atafunga mabao zaidi yangu, nitampongeza na ni mwanasoka ninayevutiwa naye. Lakini kamwe hawezi kufuta historia yangu na mabao yangu," aliongeza.

Iwapo Klose atafanikiwa kuifikia ama kuvunja rekodi hiyo, itakuwa ni sawa na kulipiza kisasi kwa Wajerumani baada ya Ronaldo kuvunja rekodi ya Gerd Muller.

"Inawezekana rekodi ikarejea Ujerumani. Lakini ni rekodi inayoleta mafanikio binafsi, sio ushindi wa timu. Rekodi inaisaidia timu, lakini kitu muhimu ni kupata ushindi wa pamoja,"alisema Ronaldo.

Ronaldo amewataka wanasoka wanaochipukia kuwa na subira, malengo na nidhamu. Anasema binafsi hajabadilika kitu kwa vile bado anafanya mambo yale yale aliyokuwa akiyafanya wakati akicheza soka ya kulipwa.

WEMA: SIMFIKIRII DIAMOND, NAWAZA PESA



HATIMAYE mcheza filamu machachari, Wema Sepetu ameamua kuvunja ukimya kwa kusema, kamwe hamfikirii mpenzi wake wa zamani, Naseeb Abdul 'Diamond' katika akili yake.

Wema amesema siku zote kitu cha kwanza kinachomuijia akilini ni jinsi ya kutafuta pesa na kuzitumia.

"Watu wengi, hasa vyombo vya habari, vimekuwa vikidhani akili yangu siku zote ipo kwa Diamond, kwamba siku zote namuwaza Diamond," ameandika binti huyo kwenye mtandao wa twitter wiki hii.

"Diamond hayupo kwenye kichwa cha Wema, muda wote nafikiria pesa," amesisitiza  mrembo huyo wa zamani wa Tanzania.

Kauli hiyo ya Wema imekuja siku chache baada ya vyombo vya habari na mitandao ya kijamii nchini, kuchapisha picha alizopiga pamoja na Diamond walipokutana hivi karibuni barani Asia hivi karibuni.

Picha hizo zilikwenda sambamba na maelezo kuhusu Wema na Diamond, kwamba bado wapo kwenye mapenzi mazito, licha ya Diamond kutangaza kuwa wameachana na sasa yuko na mpenzi wake mpya, anayejulikana kwa jina la Penny.

Katika maelezo aliyoyatoa kwenye mtandao wa twitter, Wema ameweka picha zake mbili, moja ikiwa na picha ndogo ya Diamond pembeni yake, ikiwa na maneno yanayosema: ' Wanachofikiria namuwaza Diamond'.

Katika picha nyingine, Wema ameweka picha ndogo inayoonyesha maburungutu ya noti za dola za Marekani, ikiwa na maneno yanayosema: 'Ninachokifiria ni pesa'.

Wema ameelezea msimamo wake huo siku chache baada ya kuvitaka vyombo vya habari viache kumfuatafuata na kuchafua jina lake.

Mwanadada huyo alisema haelewi ni kwa nini vyombo vya habari vimekuwa vikimchafua mara kwa mara na ameiita tabia hiyo kuwa ni ya kionevu na iliyolenga kumkatisha tamaa ya maisha.

"Mara ya mwisho nililia wakati nilipoambiwa nina pepo la ngono. Leo hii nalia tena baada ya kuambiwa nimekamatwa na unga (dawa za kulevya) China na nitanyongwa," alieleza Wema kupitia akaunti yake ya mtandao wa intergram.

Wema aliamua kutoa dukuduku hilo, kufuatia taarifa zilizoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari nchini hivi karibuni kwamba, amekamtwa na dawa za kulevya China na amehukumiwa kunyongwa.

"Siwezi kusema kwamba nina furaha, sina furaha kabisa na sikuwahi kufikiria kwamba magazeti yetu, ipo siku yatakuwa na nguvu ya kuandika uongo wa namna hii," alieleza Wema kupitia mtandao huo.

"Kwa sababu huwa nakaa kimya, ndio muone kwamba mnaweza kunionea muda wote! Roho inaniuma sana. Naumia kwa sababu nimechoka kuchafuliwa jina langu bila sababu za msingi.

"Nimesema nitoke zangu kimya kimya kuja huku (China), kujihangaikia zangu kuhusu kazi zangu, lakini nimeonekana nimekuja kuuza unga na nitanyongwa hivi karibuni. Ni lini nyinyi watu mtaniacha niishi kwa amani? Sidhani kama nilishawahi kumkosea yeyote kati yenu.

"Maskini ya Mungu naishi maisha yangu mwenyewe, sina habari na mtu, sijawahi hata kufikiria kufanya upuuzi huo, nimeumia sana. Mungu nisaidie," alieleza Wema kupitia akaunti yake hiyo.

Tuesday, October 22, 2013

UCHAGUZI MKUU BODI YA LIGI IJUMAA



Uchaguzi wa Bodi ya Ligi Tanzania (TPL Board) utafanyika Oktoba 25 mwaka huu
kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Golden Jubilee Tower.

Kwa mujibu wa Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
wajumbe wanaounda Mkutano wa Uchaguzi ni wenyeviti kutoka klabu 24 za Ligi
Daraja la Kwanza (FDL), na 14 wa klabu za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL).

Wagombea kwenye uchaguzi huo ni Hamad Yahya Juma (Mwenyekiti), Said
Muhammad Said Abeid (Makamu Mwenyekiti) wakati wanaoumba ujumbe wa
Kamati ya Uendeshaji ni Khatib Omari Mwindadi na Kazimoto Muzo.

KIINGILIO MECHI YA TWIGA STARS NA MSUMBIJI BUKU


Kiingilio cha chini kwenye mechi ya wanawake chini ya miaka 20 katika ya Tanzania
na Msumbiji itakayochezwa Jumamosi (Oktoba 26 mwaka huu) kwenye Uwanja wa
Taifa, Dar es Salaam kitakuwa sh. 1,000.

Mechi hiyo itachezwa kuanzia saa 10 kamili jioni, na kiingilio hicho ni kwa ajili ya viti
vya rangi ya kijani, bluu na chungwa. Viingilio vingine ni sh. 2,000 kwa VIP C, sh.
5,000 kwa VIP B wakati VIP A itakuwa sh. 10,000.

Timu ya Msumbiji inatarajiwa kuwasili nchini kesho (Oktoba 23 mwaka huu) saa 8
kamili mchana kwa ndege ya LAM. Msumbiji yenye msafara wa watu 25 itafikia
kwenye hoteli ya Sapphire.

SERENGETI BOYS YAALIKWA MICHUANO YA ANOCA
Timu ya Taifa ya Tanzania kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20 (Serengeti
Boys) imealikwa kushiriki Olimpiki ya Afrika itakayofanyika Mei mwakani.

Mpira wa miguu ni kati ya michezo 22 itakayoshindaniwa katika mashindano
yatakayofanyika Gaborone, Botswana chini ya Kamati za Olimpiki za Afrika
(ANOCA).

Kwa mujibu wa Kamati ya Olimpiki ya Tanzania (TOC), Tanzania imepewa nafasi ya
kushiriki katika michezo hiyo ya Olimpiki kwa Afrika kutokana na kuwa na programu
nzuri za vijana hasa chini ya umri wa miaka 17.

Hiyo itakuwa ni michezo ya Pili ya Afrika kwa Olimpiki ambapo ya Kwanza ilifanyika
mwaka 2010 jijini Rabat, Morocco.

SIMBA, YANGA DIMBANI TENA KESHO


Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inaendelea kesho (Oktoba 23 mwaka huu) kwa mechi tatu; ambapo Yanga itaikaribisha Rhino Rangers katika mchezo utakaofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Coastal Union inaikaribisha Simba katika mechi itakayopigwa Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga na kuchezeshwa na mwamuzi Dominic Nyamisana kutoka Dodoma.

Tanzania Prisons ambayo imepoteza mechi mbili zilizopita ugenini dhidi ya Ashanti United na Simba inarejea uwanja wake wa Kumbukumbu ya Sokoine kwa kuikaribisha Kagera Sugar.

Nayo Ligi Daraja la Kwanza (FDL) inaendelea kesho (Oktoba 23 mwaka huu) kwa mechi moja ya kundi A itakayozikutanisha Tessema na Villa Squad kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume jijini Dar es Salaam.


RAMBIRAMBI MSIBA WA JIMMY MHANGO
Shrikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko taarifa za kifo
cha mjumbe wa Bodi ya klabu ya Ashanti United, Jimmy Mhango kilichotokea jana
(Oktoba 21 mwaka huu).

Msiba huo ni mkubwa kwa wadau wa mpira wa miguu kwani Mhango aliutumikia
mpira wa miguu kwa muda mrefu, tangu akiwa mchezaji, kocha na baadaye
kiongozi.

Kabla ya kuingia kwenye Bodi ya Ashanti United, enzi za uchezaji wake alichezea
timu za Mapinduzi ya Dodoma, Ushirika ya Moshi na Pan African ya Dar es Salaam.
Pia aliwahi kuwa Kocha Mkuu wa Ashanti United.

TFF inatoa pole kwa familia ya marehemu Mhango, klabu ya Ashanti United na
Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA), na kuwataka kuwa na
subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.

Maziko yamefanyika leo mchana katika makaburi ya Abeid (Mchikichini) Dar es
Salaam. Mungu aiweke roho ya marehemu Mhango mahali pema peponi. Amina

DRFA YAOMBOLEZA MSIBA WA JIMMY MHANGO



CHAMA Cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) kimetuma salamu za rambirambi kutokana na kifo cha Mjumbe wa Kamati ya Nidhamu na Usuluhishi, Jimmy Mhango aliyefariki juzi katika hospitali ya Muhimbili jijini Dar es Salaam kutokana na presha.

Katibu Mkuu wa DRFA Msanifu Kondo amesema leo (Oktoba 22) kwamba wamepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha Mjumbe huyo, ambaye pia aliwahi kuwa mchezaji mahiri katika timu ya Ushirika ya Moshi katika miaka ya tisini chini ya Kocha Dan Korosso.

Marehemu pia aliwahi kuzichezea timu za Pan Africans ya Dar es Salaa pamoja na timu ya Mkoa wa Kilimanjaro ‘Kilimanjaro Stars.

“DRFA imepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha Jimmy Mhango na inatoa pole kwa familia, ndugu jamaa na wanafamilia wote wa mpira wa miguu, tunawaomba wawe na subira katika kipindi hiki kigumu,” alisema.

Kamati ya Nidhamu na Usuluhishi ya DRFA ambayo marehemu alikuwa mjumbe, inaongozwa na Roman Masumbuko (Mwenyekiti), Fahadi Kayuga (Makamu Mwenyekiti), Mohamed Mpili (Mjumbe) na Peter Nkwera (Mjumbe).

Marehemu anatarajiwa kuzikwa leo (Jumanne)katika makaburi ya Ilala Mchikichini, Dar es Salaam saa kumi jioni.

Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema

Imetolewa na Mohamed Mharizo
Ofisa Habari
Chama Cha Mpira Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA)
Oktoba 22, 2013

NASSIB AWAZAWADIA WAAMUZI WA SIMBA NA YANGA



Makamu wa Pili wa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Ramadhan Nassib ametoa sh. milioni moja kwa waamuzi waliochezesha mechi ya Simba na Yanga iliyochezwa wikiendi iliyopita jijini Dar es Salaam.

Nassib, ambaye alichaguliwa katika nafasi hiyo akiwakilisha klabu, amesema ametoa fedha hizo ili kuwapongeza waamuzi hao kwa kuchezesha vizuri mechi hiyo iliyomalizika kwa sare ya mabao 3-3.

“Waamuzi wanapofanya vibaya tunawaadhibu, hivyo wakifanya vizuri wanastahili kupongezwa pia. Vilevile kuwapongeza ni kuwaongezea ari ya kuchezesha vizuri zaidi,” amesema.

Israel Nkongo, ndiye aliyeongoza jopo hilo ambapo mwamuzi msaidizi namba moja alikuwa Hamis Chang’walu wakati namba mbili alikuwa Ferdinand Chacha. Mwamuzi wa mezani alikuwa Oden Mbaga.

Waamuzi wote hao wana beji za Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), na watoka Dar es Salaam ukiondoa Chacha ambaye maskani yake ni Bukoba mkoani Kagera.

Monday, October 21, 2013

SIMBA, YANGA ZAINGIZA MIL 500/-


Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) ya watani wa jadi Simba na Yanga iliyochezwa jana (Oktoba 20 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kumalizika kwa sare ya mabao 3-3 imeingiza sh. 500,727,000.

Washabiki 57,422 ndiyo waliokata tiketi kushuhudia pambano hilo namba 63 kwa viingilio vya sh. 5,000, sh. 7,000, sh. 10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000.

Ni tiketi 131 tu ndizo hazikuuzwa ambazo ni 90 za VIP A, 40 za VIP B na moja ya VIP C. Tiketi zilizochapwa kwa ajili ya mechi hiyo ni 57,558 ambayo ndiyo idadi ya viti vilivyopo kwenye uwanja huo.

Kila klabu imepata mgawo wa sh. 123,025,564.32 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 76,382,084.75.

Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 62,555,371.69, tiketi sh. 7,309,104, gharama za mechi sh. 37,533,223.01, Kamati ya Ligi sh. 37,533,223.01, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 18,766,611.51 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 14,596,253.39.


VITAMBULISHO MICHUANO YA CHALENJI
Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) limefungua maombi ya vitambulisho (Accreditation) kwa ajili ya waandishi wa habari wanaotarajia kuripoti mashindano ya Kombe la Chalenji.

Mashindano ya Kombe la Chalenji yatafanyika nchini Kenya kuanzia Novemba 27 hadi Desemba 12 mwaka huu. Kwa waandishi wa habari wanaotaka kuripoti mashindano hayo wanatakiwa kutuma maombi yao kabla ya Oktoba 31 mwaka huu.

Mbali ya majina, katika maombi hayo mwandishi wa habari ni lazima aoneshe chombo anachofanyia kazi na kuambatanisha na picha moja ya pasipoti.

TFF YAPANGUA MECHI ZA LIGI KUU



Kamati ya Ligi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imefanya marekebisho ya ratiba ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) ili kupisha mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia kati ya Tanzania na Msumbiji.

Mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya kwanza kwa mashindano ya wanawake wenye umri chini ya miaka 20 itachezwa Jumamosi (Oktoba 26 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 jioni.

U20 tayari imehamishia kambi yake hosteli ya Msimbazi Center, Dar es Salaam kutoka JKT Ruvu mkoani Pwani tangu wiki iliyopita kujiandaa kwa mechi hiyo. Fainali za Kombe la Dunia kwa U20 wanawake zitafanyika mwakani nchini Canada.

Marekebisho ya ratiba ya VPL yamegusa raundi zote tatu zilizobaki kukamilisha mzunguko wa kwanza. Kutokana na marekebisho hayo mechi za raundi ya 11 zitakuwa ifuatavyo; Oktoba 28 mwaka huu ni Coastal Union vs Mtibwa Sugar, Oljoro JKT vs Ashanti United, Ruvu Shooting vs Kagera Sugar na Simba vs Azam. Oktoba 29 mwaka huu ni Tanzania Prisons vs Mbeya City, Yanga vs Mgambo Shooting na Rhino Rangers vs JKT Ruvu.

Raundi ya 12 ni kama ifuatavyo; Oktoba 31 mwaka huu ni Simba vs Kagera Sugar, Novemba 1 mwaka huu ni JKT Ruvu vs Yanga. Novemba 2 mwaka huu ni Mgambo Shooting vs Coastal Union, Tanzania Prisons vs Oljoro JKT, Azam vs Ruvu Shooting, Mtibwa Sugar vs Rhino Rangers na Mbeya City vs Ashanti United.

Raundi ya 13 ni kama ifuatavyo; Novemba 6 mwaka huu ni JKT Ruvu vs Coastal Union, Ashanti United vs Simba, Kagera Sugar vs Mgambo Shooting, Rhino Rangers vs Tanzania Prisons na Ruvu Shooting vs Mtibwa Sugar. Novemba 7 mwaka huu ni Azam vs Mbeya City.

Mechi za kufunga raundi ya 10 zitachezwa keshokutwa (Oktoba 23 mwaka huu) kama ratiba inayoonesha. Mechi hizo ni kati ya Coastal Union vs Simba, Tanzania Prisons vs Kagera Sugar na Yanga vs Rhino Rangers.

SIMBA YAFANYA MAAJABU, YARUDISHA BAO TATU NA KUTOKA SARE NA YANGA, MASHABIKI KADHAA WAZIMIA UWANJANI


Kikosi cha Yanga
Kikosi cha Simba

WACHEZAJI Betram Mwombeki, Joseph Owino na Gilbert Kaze jana walirejesha
heshima ya Simba baada ya kuifungia mabao ya kusawazisha katika mechi ya ligi
kuu ya Tanzania Bara dhidi ya watani wao wa jadi Yanga.
Katika mechi hiyo, iliyokuwa na ushindani mkali na msisimko wa aina yake,
iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, timu hizo kwenye nchini na
zenye utani wa jadi, zilishindwa kutambiana baada ya kutoka sare ya mabao 3-3.
Yanga itabidi ijilaumu kwa kushindwa kutoka uwanjani na ushindi baada ya kuwa
mbele kwa mabao 3-0 hadi mapumziko.
Bao la kwanza la Yanga lilifungwa na Mrisho Ngasa dakika ya 12 kwa mpira wa
kuparaza baada ya kupokea pasi kutoka kwa Didier Kavumbagu.
Hamisi Kiiza aliiongezea Yanga bao la pili dakika ya 36 baada ya mabeki wa Simba
kuzembea kuokoa mpira uliopigwa kwenye lango lao.
Dakika moja kabla ya mapumziko, Kiiza aliiongezea Yanga bao la tatu baada ya
gonga nzuri kati ya Kavumbagu na Ngasa.
Mmoja wa mashabiki waliozimia uwanjani akibebwa kwenye machela

Kipindi cha pili kilipoanza, wachezaji wa Yanga walionekana kuridhika na ushindi wa
mabao 3-0 walioupata na hivyo kucheza kwa kurilaksi.
Kuona hivyo, Kocha Abdalla Kibadeni aliamua kuwatoa Abdulrahim Humud na
Haruna Chanongo na kuwaingiza Saidi Ndemla na William Lucian, ambao waliongeza
uhai kwenye safu ya kiungo.
Mwombeki aliifungia Simba bao la kwanza dakika ya 53 baada ya kuwatoka mabeki
wa Yanga na kufumua kiki kali iliyotinga wavuni.
Owino aliiongezea Simba bao la pili dakika ya 56, kufuatia mpira wa adhabu uliopigwa
na Ramadhani Singano kabla ya Kaze kufunga la tatu dakika ya 75.
Simba: Abel Dhaira, Nassoro Masoud 'Cholo', Haruna Shamte, Gilbert Kaze, Joseph
Owino, Jonas Mkude, Ramadhani Singano, Abdulrahim Humud/William Lucian,
Betram Mwombeki, Amisi Tambwe, Haruna Chanongo/Saidi Ndemla.
Yanga: Ali Mustafa 'Barthez', Mbuyu Twite, David Luhende, Nadir Haroub
'Cannavaro', Kelvin Yondan, Athumani Iddi 'Chuji', Haruna Niyonzima, Frank
Domayo, Didier Kavumbagu, Mrisho Ngasa, Hamisi Kiiza.
Wakati huo huo, mashabiki wapatao 20 jana walizimia uwanjani wakati Simba na
Yanga zilipokuwa zikimenyana.
Mashabiki hao walianza kuzimia baada ya Yanga kufunga bao la pili na wengine
baada ya Simba kufunga bao la pili na hatimaye kusawazisha.
Furaha ya ushindi. Wachezaji wa Yanga wakifurahia baada ya kupata bao la tatu
Shabiki huyu mwanamke akiwa amezimia

Sunday, October 20, 2013

KING MAJUTO; NATAKA UBUNGE NIWASAIDIE WANANCHI, ASEMA HANA NJAA, ANAZO FEDHA ZA KUTOSHA KUISHI VIZURI


MSANII nyota wa vichekesho na filamu nchini, Amri Athumani 'King Majuto' amesema, atagombea ubunge katika jimbo la Tanga Mjini katika uchaguzi mkuu ujao wa rais na wabunge, unaotarajiwa kufanyika 2015.

Akihojiwa na kituo cha redio cha Clouds FM wiki hii, Majuto alisema amepanga kuwania ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CCM.

Mkongwe huyo wa sanaa nchini alisema, yeye ni muumini mzuri wa CCM na kwamba anakipenda na kukiheshimu kutokana na mfumo wake mzuri wa uongozi.

Majuto (60) alisema ameamua kujitosa kwenye siasa ili kuendeleza mafanikio, ambayo wasanii wa fani mbalimbali nchini wameyapata baada ya kuwania nafasi mbalimbali za uongozi.

Msanii huyo mkongwe alisema, anaamini kuwa, uzoefu alioupata kutokana na kuishi Tanga kwa miaka mingi, utamwezesha kutatua matatizo na kero mbalimbali zinazowakabili wakazi wa jimbo hilo.

"Lengo langu ni kuwaletea maendeleo ya kweli wananchi wenzangu iwapo Mungu atanisaidia katika kusudio langu hili,"alisema.

Majuto alisema hali ya sasa ya Tanga na ugumu wa maisha ni miongoni mwa mambo yaliyomfanya aamue kujitosa kwenye ulingo wa siasa kwa kuwania ubunge katika jimbo hilo.

Kwa sasa, mbunge wa jimbo la Tanga Mjini  ni Omar Nundu, ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Uchukuzi.

"Wakazi wengi wa Tanga wamekuwa wakiishi maisha magumu na ya kukatisha tamaa, hivyo wakati umefika wa kujitosa kwenye siasa ili kuwasaidia wawe na maisha mazuri,"alisema.

Alipoulizwa iwapo haoni umri na elimu vinaweza kuwa kikwazo kwake kuwania ubunge, Majuto alisema umri si tatizo kwa sababu wapo wabunge wenye umri mkubwa kuliko wa kwake.

Mkongwe huyo alisema pia kuwa, elimu si tatizo kwa sababu elimu aliyonayo inamruhusu kuwania nafasi hiyo kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa na CCM. Majuto ni muhitimu wa elimu ya msingi.

“Kuna watu wanaweza kusema labda njaa ndio inayonifanya niingie kwenye siasa na kutaka kuwania nafasi kubwa ya ubunge, lakini lazima wajue kuwa sina njaa kwa kuwa kazi ninayoifanya inanipatia fedha za kutosha na maisha yangu ni mazuri,"alisema msanii huyo.

“Nina mpangilio mzuri wa kazi zangu, bado naheshimika kwa kiasi kikubwa na kazi zangu zinapendwa, ila kuingia kwenye siasa ni kwa sababu nina malengo mazuri na wanananchi wa Tanga Mjini na Tanzania kwa ujumla, hivyo hakuna wa kunizuia,” alisisitiza Majuto.

Majuto alisema hana hofu na majina ya wanasiasa maarufu, atakaopambana nao katika harakati zake hizo, kuanzia ndani ya CCM na kutoka vyama vya upinzani.

Iwapo Majuto atatekeleza mkakati wake huo kwa vitendo, atakuwa amefuata nyayo za baadhi ya wasanii waliojitosa kwenye ulingo wa siasa na kupata ubunge. Miongoni mwa wasanii hao ni Joseph Mbilinyi 'Sugu', mbunge wa Mbeya Mjini kwa tiketi ya CHADEMA, Kepteni John Komba, mbunge wa jimbo la Mbinga Magharibi kwa tiketi ya CCM.

Majuto ni miongoni mwa wasanii wenye mashabiki wengi nchini kutokana na umahiri wake wa kucheza filamu za vichekesho na za kawaida. Ni msanii aliyetokea mbali katika fani hiyo, ikilinganishwa na wasanii wengi waliopo sasa.

King Majuto amekuwa mwigizaji wa vichekesho kwa miaka 55 sasa, akijivunia mafanikio makubwa na kutambuliwa hata kimataifa.
Alianza kuigiza 1958 akiwa na umri wa miaka 10. Wakati huo alikuwa darasa la pili katika shule ya msingi ya Msembweni mjini Tanga.

Baada ya kumaliza darasa la saba 1966, alijiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na kudumu nalo hadi 1970, alipoamua kuachana nalo kutokana na kukosa nafasi ya kufanya sanaa kama ndoto zake zilivyokuwa zikimwelekeza. 
     
Kabla ya kujitosa kwenye sanaa, Majuto aliwahi kufanyakazi katika kikosi cha Zimamoto, Kiwanda cha Mablanketi na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), akiwa mlinzi.

Majuto alianza sanaa kwa kuigiza sauti za makabila mbalimbali. Alitengeneza kanda za kaseti za sauti yake na kuziuza, ambapo anakiri kwamba alipata pesa nyingi.

Kikundi chake cha kwanza kilikuwa DDC Kibisa, alichojiunga nacho 1982. Ni katika kikundi hicho, ndipo akapachikwa jina la King Majuto kwa maana ya Mfalme wa Kulia. Maigizo yake mengi yalikuwa ya kuhuzunisha na kuwatoa machozi mashabiki.

Hata hivyo, Majuto alianza kunufaika na kazi zake baada ya kuanzishwa kwa vituo vya televisheni nchini, ambapo alipata nafasi ya kucheza filamu za vichekesho na kulipwa fedha nyingi.

Kwa sasa, Majuto anamiliki nyumba kadhaa pamoja na magari ya biashara mjini Tanga. Ni msanii pekee wa vichekesho, anayelipwa fedha nyingi kuliko wasanii wengine wa fani hiyo.