KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Saturday, October 26, 2013

YAHYA MWENYEKITI MPYA BODI YA LIGI, SAIDI MAKAMU MWENYEKITI



Bodi ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara, imepata viongozi wapya kufuatia uchaguzi mkuu uliofanyika jana kwenye ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Golden Jubilee Towers, Dar es Salaam.

Katika uchaguzi huo, Hamad Yahya Juma wa Mtibwa Sugar alichaguliwa kuwa mwenyekiti wakati Saidi Mohamed wa Azam alichaguliwa kuwa makamu mwenyekiti.

Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo, mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Hamidu Mbwelezeni alisema Hamad alishinda nafasi hiyo kwa kupata asilimia 100 ya kura zilizopigwa.

Mbwelezeni alisema Said naye alishinda nafasi ya makamu mwenyekiti kwa kupata asilimia 100 ya kura zilizopigwa.

Kwa mujibu wa Mbwelezeni, katika uchaguzi huo, baadhi ya wapiga kura waliondolewa kutokana na kushindwa kutimiza masharti yanayotakiwa.

Walioshinda ujumbe wa kamati ya utendaji ya bodi hiyo ni Kazimoto Miraji Muzo wa Pamba ya Mwanza na Omary Khatib Mwindadi wa Mwadui.

Akizungumza baada ya uchaguzi huo, Hamad alisema atahakikisha anakomesha vitendo vya rushwa katika michuano ya ligi kuu na ligi daraja la kwanza.

"Siwezi kuahidi kwamba tutacheza fainali za Kombe la Dunia, lengo hasa ni kuhakikisha tunakuza kiwango cha soka nchini,"alisema.

No comments:

Post a Comment