KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, October 13, 2017

TFF YATAWATOA MAKOCHA KATIKA MABENCHI



Bodi ya Ligi (TPLB) ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania, limewapiga marufuku makocha watano wa timu za Ligi Daraja la Kwanza kukaa katika mabenchi ya timu hizo kwa sababu ya kukosa sifa.


Makocha hao ni Mathias Wandiba wa Pamba FC ya Mwanza, Salum Waziri wa JKT Mgambo ya Tanga, Adam Kipatacho wa African Lyon ya Dar es Salaam, Omba Thabit wa Mvuvumwa FC ya Kigoma na Ngelo Manjamba wa Polisi Dar.


Makocha hao wamekuwa kwenye mabenchi ya timu wakifanya kazi kama makocha wakuu katika mechi nne mfululizo za Ligi Daraja la Kwanza msimu wa 2017/2018 inayoendelea hivi sasa.


Kwa mujibu wa kanuni ya 72 (3) (5) ya Ligi Daraja la Kwanza, Kocha Mkuu anatakiwa kuwa na Leseni ya chini kuanzia daraja C ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) wakati Kocha Msaidizi anatakiwa kuwa na  sifa isiyopungua ngazi ya Kati cha Ukocha (Intermediate).


Tayari Idara ya Ufundi ya TFF imefafanua wazi kuwa makocha hao hawana Leseni C ya CAF hivyo hawastahili kukaa kwenye mabenchi ya timu zao kama makocha wakuu.


Vitendo vinavyofanywa na timu husika ni ukiukwaji wa kanuni, na ni matarajio ya TFF kuwa viongozi wa timu hizo watasitisha mara moja kwa makocha hao kukaa kwenye mabenchi ili kuepika adhabu.


TFF tunachukua nafasi hii kuzikumbusha klabu husika  kwamba kuanzia msimu ujao 2018/2019 kuwa sifa ya Kocha Mkuu wa kila timu ya Daraja la Kwanza ni Leseni B ya CAF.


PATASHIKA LIGI VPL, FDL, SDL WIKIENDI HII


Baada ya kupisha wiki ya FIFA kwa mchezo wa kirafiki wa kimataifa ukihusisha Taifa Stars ya Tanzania na Miale ya Moto kutoka Malawi iliyotoshana nguvu ya bao 1-1, uhondo wa mashindano ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Ligi Daraja la Kwanza na Ligi Daraja la Pili, umerejea.


Kwa upande wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inatarajiwa kuendelea wikiendi hii ambako kesho Oktoba 13, 2017 kutakuwa na mchezo mmoja tu utakaokutanisha timu za Mbao FC na Mbeya City kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Dar es Salaam.


Timu hizo ziko katika nafasi za katikati katika msimamo wa VPL, lakini ushindani unatarajiwa kuwa kwa timu za Simba SC, Mtibwa FC na Azam ambazo kila moja ina pointi 11 na ziko kileleni kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa tu.


Katika michezo ya Jumamosi Oktoba 14, 2017 Azam FC itakuwa mgeni wa Mwadui FC kwenye Uwanja wa Mwadui wakati Kagera Sugar itawaalika mabingwa watetezi, Young Africans kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.


Ndanda itakuwa nyumbani kucheza na majirani zao Majimaji ya Songea kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara wakati Singida United itasafiri hadi Uwanja wa Mabatini ulioko Mlandizi kucheza na wenyeji Ruvu Shooting ya Pwani.


Majirani wengine, Njombe Mji na Lipuli ya Iringa watacheza kwenye Uwanja wa Sabasaba mjini Njombe ilihali michezo mingine ya Ligi hiyo ikifanyika Jumapili Oktoba 15, ambako Simba itakuwa mwenyeji wa Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam wakati Tanzania Prisons itacheza na Stand United kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.


Ligi Daraja la Kwanza (FDL) nayo itaendelea ambako kesho kutakuwa na mchezo kati ya African Lyon na JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam. Timu hizo ni za Kundi A.


Mechi nyingine kwenye kundi hilo itafanyika Jumamosi ambako Ashanti United itacheza na Mvuvumwa ya Kigoma kwenye Uwanja wa Uhuru ilihali Jumatatu Oktoba 16, Kiluvya itacheza na Friends Rangers kwenye Uwanja wa Uhuru huku Mgambo JKT ikishikamana na Mshikamano kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.


Kundi B kwa mujibu wa ratiba ni kwamba kesho Ijumaa JKT Mlale itacheza na Polisi Dar kwenye Uwanja wa Majimaji mjini Songea huku michezo mingine katika kundi hilo ikicheza Jumapili kwa michezo mitatu.


Siku hiyo Mbeya Kwanza itacheza na Mawenzi Uwanja wa Mabatini ulioko Mlandizi mkoani Pwani, Coastal na Polisi Tanzania kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga huku Mufindi United itacheza na KMC Uwanja wa Samora mkoani Iringa.


Kundi C litakuwa na mchezo mmoja siku ya Jumamosi  Oktoba 14, 2017 ambako Toto African itakipiga na Pamba kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza na michezo mingine mitatu itafanyika siku ya Jumapili Oktoba 15, mwaka huu.


Michezo ya Jumapili itakuwa ni kati ya Dodoma FC dhidi ya JKT Oljoro ya Arusha kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma; Rhino Rangers itacheza Biashara United wakati mchezo wa Alliance Schools na Transit Camp utachezwa kwenye Uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza.


Ligi Daraja la Pili (SDL), Jumapili Oktoba 15, 2017 Kundi A kutakuwa mchezo kati ya Villa Squad na Abajalo FC Uwanja wa Kinesi, Dar es Salaam.


Jumamosi kutakuwa na michezo miwili ya Kundi B ambako African Sports itacheza na Pepsi kwenye Uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga huku Arusha FC itacheza na Kitayose kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha.


Jumapili Oktoba 15, 2017 katika kundi B hilo la B kutakuwa na mchezo mmoja kati ya Madini na Kilimanjaro Heroes kwenye Uwanja wa Nyerere mkoani Arusha.


Kundi C kutakuwa na michezo yote mitatu ya raundi ya tatu ambako Ihefu itacheza na Green Warriors kwenye Uwanja wa Highland; Mkamba Rangers itacheza na The Mighty Elephant kwenye Uwanja wa Mkamba huko Morogoro ilihali Boma FC dhidi ya Burkinafaso zitacheza Uwanja wa Mwakangale, Mbeya.


Kundi D pia kutakuwa na mechi zote tatu Oktoba 14, 2017 ambako Nyanza itacheza na Mashujaa kwenye Uwanja wa Nyerere; Area ‘C’ United itacheza na Milambo Uwanja wa Jamhuri Dodoma wakati JKT Msange itacheza na Bulyanhulu kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi.


NI ZAMU YA WAAMUZI DARAJA I NA II


Baada ya mtihani wa utimamu wa mwili kwa waamuzi wenye beji za FIFA na wale wa Daraja la Kwanza kufanyika Agosti, 2017, sasa ni zamu ya waamuzi wa madaraja ya Tatu na Pili.


Waamuzi wa madaraja ya Tatu na Pili kuanzia leo Alhamisi Oktoba 12, 2017 wameanza vipimo kabla ya  mitihani ya utimamu wa mwili katika vituo viwili vya Dar es Salaam na Mwanza. 


Kwa wale watakaopata matokeo mazuri, watapata fursa ya kupandisha madaraja kwa mujibu wa utaratibu.


Zoezi hilo litajumuisha pia wale waamuzi wa Daraja la Kwanza walioshindwa mitihani hiyo mwezi Agosti, mwaka huu. Hivyo nao wanaruhusiwa kwenda kufanya mitihani tena.


Kituo cha Dar es Salaam kitakuwa na waamuzi wa mikoa ya Dar es Salaam yenyewe, Pwani, Morogoro, Tanga, Kilimanjaro, Lindi, Mtwara, Ruvuma, Njombe, Iringa, Mbeya, Rukwa na Songwe.


Kituo cha Mwanza kitakuwa na waamuzi wa mikoa ya Mwanza yenyewe, Mara, Kagera, Simiyu, Geita, Kigoma, Arusha, Shinyanga, Tabora, Dodoma, Singida, Manyara na Katavi.


Waamuzi wote waende kwenye vituo vyao walivyopangiwa kama ilivyoelekezwa Oktoba 12, 2017 - ni siku ya kupima afya kabla ya kuanza kwa mitihani mingine ukiwamo wa utimamu wa mwili hapo kesho.

No comments:

Post a Comment