KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, May 30, 2010

Twiga Stars njia nyeupe kucheza fainali za Afrika



TIMU ya soka ya taifa ya wanawake, Twiga Stars mwishoni mwa wiki iliyopita ilijiweka kwenye nafasi nzuri ya kufuzu kucheza fainali za Mataifa ya Afrika baada ya kuibugiza Eritrea mabao 8-1 katika mechi ya awali ya raundi ya pili iliyochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam. Katika makala hii, Mwandishi Wetu RASHID ZAHOR anaelezea kiwango kilichoonyeshwa na Twiga Stars katika mechi hiyo.

Kutokana na ushindi huo, ili ifuzu kucheza fainali hizo kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, Twiga Stars sasa inahitaji sare ya aina yoyote timu mbili hizo zitakaporudiana wiki mbili zijazo mjini Asmara.

Kwa ushindi huo, hakuna kinachoweza kuizuia Twiga Stars isifuzu kucheza fainali hizo zitakazofanyika mwishoni mwa mwaka huu nchini Afrika Kusini. Labda itokee miujiza kwa Eritrea kuifunga Twiga mabao 8-0.

Lakini iwapo Eritrea itaishinda Twiga mabao yasiyozidi saba katika mechi hiyo, njia itakuwa nyeupe kwa akina dada hao kuweka rekodi ya kuwa timu ya pili ya taifa kufuzu kucheza fainali za Afrika, baada ya Taifa Stars kufanya hivyo mwaka 1980.

Ushindi huo mkubwa kwa Twiga Stars haukupatikana kirahisi ama kwa njia ya mteremko. Ulitokana na kiwango cha juu cha soka kilichoonyeshwa na wachezaji wa timu hiyo na pia kucheza kwa malengo.

Tofauti na walivyocheza katika mechi yao ya marudiano ya raundi ya kwanza dhidi ya Ethiopia na kulazimishwa kutoka nayo sare ya bao
1-1, katika mechi dhidi ya Eritrea, Twiga ilionekana kuwa na mabadiliko makubwa na kuimarika kila idara.

Wachezaji wake walicheza kwa nguvu muda wote wa mchezo bila ya kuonekana kuchoka, walikuwa na stamina na walipeana pasi za uhakika, japokuwa baadhi ya wakati hazikuwa na malengo.

Akina dada hao walicheza mechi hiyo wakiwa chini ya kocha wa muda, Rogasian Kaijage, ambaye alikabidhiwa jukumu hilo baada ya makocha waliopewa dhamana ya kuinoa timu hiyo, Charles Boniface na Mohamed Rishard Adolph kwenda mafunzoni Brazil.

Baadhi ya wadau waliozungumza baada ya mechi hiyo walikiri kuwa, Kaijage ameleta mabadiliko makubwa katika timu hiyo kutokana na wachezaji wake kucheza kwa mfumo unaoeleweka.

“Huyu jamaa bwana (Kaijage) anastahili kukabidhiwa hii timu moja kwa moja kwa sababu ameleta mabadiliko makubwa. Vijana wamecheza mpira unaoeleweka, tofauti na walivyocheza dhidi ya Ethiopia,” alisema Fadhili Hilali, mkazi wa Temeke, Dar es Salaam.

Mwanadada Justina James, mkazi wa Magomeni alisema ilikuwa mara yake ya kwanza kuiona Twiga ikicheza, lakini imemfurahisha kwa sababu ilicheza soka nzuri na kupata ushindi mkubwa.

Katika mechi hiyo, viungo Mwanaidi Abdalla, Fadhila Hamadi na washambuliaji Fatuma Bushiri, Asha Rashid, Eto Mlenzi na Esther Chabruna ndio waliotia fora kwa kugongeana vizuri na kufunga mabao ya kuvutia.

Kwa mfano, bao la pili la Mwanaidi alilifunga kwa shuti la mbali, akiwa amempima kipa Semhar Bekitr wa Eritrea, ambaye alishindwa kulidaka kwa vile alishatoka langoni.

Bao la tatu lililofungwa na Asha nalo lilikuwa la aina yake kwa vile kabla ya kufunga, aliwalamba chenga mabeki wawili pembeni ya uwanja, akaingia na mpira ndani ya mita 18 na kuwalamba tena chenga mabeki wengine wawili kabla ya kuukwamisha mpira wavuni.

Mabeki Sophia Mwasikili, Fatma Khatibu, Pulkeria Charaji na Helen Peter nao walicheza kwa umakini mkubwa, japokuwa baadhi ya wakati walifanya makosa ya kizembe yaliyowawezesha washambuliaji Rahwa Solomon na Tuta Mender kuingia na mpira mara kadhaa kwenye eneo la hatari.

Kilichovutia zaidi, hata wachezaji wa akiba, Fadhila Hamadi na Fatma Mustafa waliongia kipindi cha pili kuchukua nafasi za Mwanahamisi na Esther, walionyesha soka ya kiwango cha juu na hakukuwa na tofauti kati yao na walioanza mchezo huo tangu mwanzo.

Uamuzi wa Kocha Kaijage kufanya mabadiliko ya wachezaji kipindi cha pili ulipokewa kwa furaha kubwa na mashabiki waliohudhuria mechi hiyo, ambao walikuwa na kiu kubwa ya kuona uwezo wa wachezaji wa akiba, ambao hawakupata nafasi katika mechi dhidi ya Ethiopia.

“Hawa watoto waliongia sasa hivi kumbe nao ni wazuri! Mbona hawakucheza katika mechi na Ethiopia,” baadhi ya mashabiki waliohudhuria mechi hiyo walisikika wakisema mara kadhaa.

Kwa jumla, uwezo ulioonyeshwa na Twiga katika mechi hiyo umedhihirisha wazi kwamba, wakipata mafunzo zaidi ya kuwaunganisha vyema, wana uwezo wa kufika mbali zaidi katika michuano hiyo. Kocha Kaijage amedhihirisha kwamba anao uwezo huo.

Pengine ni vyema kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), lifikirie kumwongeza Kocha Kaijage katika benchi la ufundi la timu hiyo
kwa sababu inaonekana wachezaji wanamwelewa zaidi na kushika mafunzo yake.

Hii ni kwa sababu, tayari Adolph ni kocha msaidizi wa timu ya taifa ya vijana wa chini ya miaka 19, Ngorongoro Heroes, hivyo si vyema awe na majukumu mawili kwa wakati mmoja. Nafasi yake ndani ya Twiga apewe Kaijage.

Pamoja na Twiga kujisafishia njia ya kusonga mbele, haipaswi kudharau mechi yao ya marudiano dhidi ya Eritrea kwa sababu hali ya hewa ya nchi hiyo ni baridi kali na inaweza kuwaathiri wachezaji na kuwafanya washindwe kufanya vizuri.

TFF inapaswa kuzingatia ushauri uliotolewa na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, George Mkuchika wa kuipeleka timu hiyo kuweka kambi kwenye mkoa wenye hali ya hewa inayolingana na Eritrea ili wachezaji wasiathirike.

Lakini kubwa kuliko yote ni kwamba, bado Twiga inahitaji mafunzo zaidi ya kitaalam na pengine ziara waliyoahidiwa ya kwenda Marekani kwa mafunzo ya wiki mbili baada ya kuitoa Eritrea, inaweza kuwa na manufaa zaidi kwa wachezaji.

Ahadi hiyo ya kuipeleka Twiga nchini Marekani, ilitolewa na Mkurugenzi wa Kampuni ya RBP Oil Industrial Technology Limited, Rahma Al Kharoos, ambaye pia aliipatia timu hiyo sh. milioni 10 kabla ya kupambana na Eritrea kwa lengo la kuwaongezea motisha wachezaji.

Manji kumrejesha Ngasa Yanga

Na Emmanuel Ndege

MFADHILI Mkuu wa klabu ya Yanga, Yussuf Manji ameapa kuwa, atamrejesha mshambuliaji nyota wa timu hiyo, Mrisho Ngasa aliyejiunga na klabu ya Azam hivi karibuni.

Akizungumza mjini Dar es Salaam jana, Manji alisema atafanya hivyo wakati wa usajili wa dirisha dogo.

Manji alisema amefikia uamuzi wa kumrejesha Ngassa kwenye klabu hiyo kutokana na uongozi kutomshirikisha wakati wa kumuuza.

Mfadhili huyo alisema ameshangazwa na kitendo cha Mwenyekiti wa Yanga, Iman Madega kufanya mazungumzo na viongozi wa Azam kuhusu Ngasa bila kumshirikisha.

Alisema kuuzwa kwa Ngasa kumemfedhehesha yeye binafsi kwa sababu baadhi ya wanachama wameanza kumuona kama vile ameishiwa kifedha.

“Mimi ndiye niliyekuwa nikimlipa Ngasa fedha zote za usajili pamoja na mshahara, nilikuwa na haki ya kufahamishwa kuhusu mipango ya kumuuza Azam,”alisema.

“Matokeo yake ni kwamba, sasa nachekwa na baadhi ya wanachama pamoja na watani wetu Simba kwamba nimefulia. Siwezi kukubali kitu hiki kitokee, nitamrejesha Ngasa kwa gharama zozote,”aliongeza.

Mfadhili huyo alisema kama aliweza kununua mechi ya Yanga na Etoile Sahel ya Tunisia miaka minne iliyopita kwa kulilipa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), sh. milioni 100 na kuruhusu mashabiki waingie uwanjani bure, haoni kwa nini ashindwe kumrejesha Ngasa.

Ngasa amenunuliwa na Azam kwa kitita cha sh. milioni 98. Kati ya fedha hizo, Ngasa alilipwa sh. milioni 40 wakati klabu ya Yanga ilipata sh. milioni 58.

“Nimekuwa nikitumia fedha nyingi kuigharamia Yanga, siwezi kushindwa kuirejeshea Azam fedha ilizotumia kumnunua na nitafanya hivyo wakati wa usajili wa dirisha dogo,” alisisitiza.

Alipoulizwa jana iwapo yupo tayari kurejea Yanga, Ngasa alisema hakuna tatizo kwa vile suala la msingi ni fedha.

“Kama Manji amesema atairejeshea Azam fedha ilizoilipa Yanga wakati wa usajili wa dirisha dogo, mimi sina kinyongo nipo tayari kurudi,”alisema Ngasa.

Wakati huo huo, Manji ameahidi kugharamia uchaguzi mkuu wa klabu ya Yanga unaotarajiwa kufanyika hivi karibuni mjini Dar es Salaam.

Manji alisema jana kuwa, atawaandalia chakula na usafiri wanachama wote wa Yanga wakati wa uchaguzi huo ili uweze kufanyika kwa ufanisi.

“Nimesikia wenzetu Simba walifanya uchaguzi, lakini hakukuwa na chakula kwa wanachama waliopiga kura, mimi nawaahidi wanachama kwamba watapata chakula safi siku hiyo,”alisema.

Uchaguzi mkuu wa Yanga, utatanguliwa na mkutano mkuu wa kujadili katiba mpya ya klabu hiyo, unaotarajiwa kufanyika Juni 6 mwaka huu.

GERRARD: Zitakuwa fainali za mwisho kwangu



LONDON, England

KIUNGO wa kimataifa wa England, Steven Gerrard amesema, fainali za mwaka huu za Kombe la Dunia zitakazofanyika nchini Afrika Kusini, huenda zikawa za mwisho kwake.

Akizungumza wiki hii mjini hapa, Gerrard alisema anafikiria kustaafu soka ya kimataifa mara baada ya kumalizika kwa fainali hizo, zinazotarajiwa kuanza Juni 11 mwaka huu.

Gerrard (29) alisema hana hakika iwapo atakuwa na uwezo wa kucheza fainali za mwaka 2014, zilizopangwa kufanyika nchini Brazil, akiwa na umri wa miaka 33.

Kiungo huyo anayechezea klabu ya Liverpool ya England amesema, hatarajii iwapo ataweza kutwaa tuzo yoyote akiwa na timu ya taifa ya nchi hiyo baada ya kumalizika kwa fainali za mwaka huu.

“Nafikiria kuzifanya fainali za mwaka huu kuwa za aina yake kwa England kwa sababu huenda zikawa za mwisho kwangu. Natarajia kutimiza miaka 30 wiki hii na kamwe huwezi kuelewa nini kitatokea baadaye,”alisema kiungo huyo.

Gerrard ameshindwa kutwaa tuzo yoyote akiwa na kikosi cha Liverpool, hivyo amepania kufanya kila linalowezekana ili kuweka rekodi ya kutwaa ubingwa wa dunia akiwa na England.

“Kamwe sikuwahi kufikiria kustaafu kuichezea England, lakini wachezaji wengi wana umri mkubwa hivi sasa na watakuwa na wiki tatu au nne za mapumziko baada ya Kombe la Dunia kabla ya kufikiria mustakabali wao,”alisema.

Hata hivyo, Gerrard alisema hayo yote yatategemea jinsi England itakavyofanya vizuri katika fainali hizo na jinsi Kocha Fabio Capello atakavyokuwa akifikiria.

“Unapofikisha umri wa miaka 30, ni wakati ambao napaswa kufikiria soka ya kimataifa, nini nitakachokifanya ili kusonga mbele na pia mafanikio niliyoyapata,”alisema Gerrard.

“Sitaki kujiondoa katika soka ya kimataifa kama sijapata mafanikio yoyote. Kama tutafanya vizuri, huenda itasaidia kubadilisha fikra zangu, lakini sijalipa sana uzito hilo,” aliongeza.

Gerrard alisema kutokana na viwango vya wachezaji walio nyuma yake, hana hakika iwapo atakuwemo kwenye kikosi cha mwisho cha wachezaji 23 kitakachoteuliwa na Capello kucheza fainali za
mwaka huu.

“Napaswa kulifikiria hilo, lakini nashukuru kwamba nipo fiti na mwenye uwezo wa kuwemo kwenye kikosi hicho. Nataka kutoa mchango mkubwa katika fainali hizi , hasa ikizingatiwa huenda zitakuwa za mwisho kwangu,”alisema.

Kiungo huyo wa England alikataa kuzungumzia mustakabali wake ndani ya Liverpool, aliyoichezea kwa miaka 11 sasa, lakini alisema hana wasiwasi wa kuihama klabu hiyo.

Alisema ataamua kuhusu hatma yake ndani ya klabu hiyo mara baada ya kumalizika kwa fainali za Kombe la Dunia.

Gerrard amekuwa akihusishwa na mipango ya kujiunga na klabu ya Real Madrid ya Hispania, lakini amekuwa akikanusha mara kadhaa kuwepo kwa mipango hiyo.

Mara baada ya kumalizika kwa fainali za Mataifa ya Ulaya mwaka 2004 na fainali za Kombe la Dunia mwaka 2006, Gerrard pia alihusishwa na mipango ya kujiunga na Chelsea.

Mbali na Real Madrid, klabu nyingine iliyoonyesha nia ya kumsajili kiungo huyo ni Manchester City, ambayo imesema ipo tayari kuilipa Liverpool dau lolote inalotaka ili imwachie mchezaji huyo.

Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya soka wameeleza kuwa, upo uwezekano mkubwa kwa Gerrard kuihama Liverpool msimu ujao kutokana na klabu hiyo kukabiliwa na hali ngumu kifedha.

Sababu nyingine iliyotajwa na wachambuzi hao kwamba huenda ikamlazimisha Gerrard kuhama ni hali ya kutokuelewana kati ya mchezaji huyo na Kocha Rafael Benitez.

“Kwa sasa sifikirii kuhusu mustakabali wangu au nini kitanitokea Liverpool hadi baada ya kumalizika kwa fainali za Kombe la Dunia,”alisema.

Alisema hataki kujiingiza kwenye mtego wa fainali zilizopita za kombe hilo, ambapo nusura awe chizi kwa kufikiria hatma yake ya baadaye. Alisema safari hii, hataki kufanya kosa kama hilo.

“Kumekuwa na tetesi nyingi kuhusu hatma yangu katika kipindi cha miezi miwili au mitatu, lakini imekuwa hivyo kwa miaka mingi sasa.

“Natumaini kuna vitu huenda vikatokea nitakapokuwa sipo. Huenda kukawa na wachezaji watakaojiunga na Liverpool ili kuiongezea nguvu timu.

“Napaswa kusubiri na kuona, lakini kwa sasa sifurahishwi na mambo yanavyokwenda Liverpool. Naelekeza akili yangu katika fainali za Kombe la Dunia,”alisema.

Van Vicker afanya kioja cha mwaka Nollywood



LAGOS, Nigeria

MWIGIZAJI filamu nyota wa Ghana, Joseph Van Vicker amefanya kioja cha mwaka baada ya ‘kuingia mitini kiaina’ wakati yeye na waigizaji wenzake wa Nigeria walipokuwa wakipiga picha za filamu katika mji wa Asaba.

Habari kutoka katika mji huo zimeeleza kuwa, Vicker alifikia uamuzi huo bila kutoa taarifa, hali iliyowachanganya na kuwaweka kwenye wakati mgumu watayarishaji wa filamu hiyo.

Kwa mujibu wa habari hizo, Vicker alikutwa baadaye akiwa kwenye uwanja wa ndege wa mjini Lagos, akijiandaa kurejea nyumbani Ghana.

Baada ya kumsubiri kwa saa kadhaa bila ya kujua mahali alipo, mtayarishaji wa filamu hiyo aliamua kwenda hotelini kwake kumuulizia.

Kwa kuhofia kuwa, huenda mwigizaji huyo ametokewa na kitu chochote kibaya, uongozi wa hoteli hiyo uliamua kuvunja mlango wa chumba chake ili kujua kulikoni.

Lakini kwa mshangao mkubwa, maofisa wa hoteli pamoja na mtayarishaji wa filamu hiyo, walikikuta chumba kikiwa kitupu, hali iliyozidi kuwapa wasiwasi.

Mbali na kukikuta chumba kikiwa kitupu, mwigizaji huyo aliamua kuchukua kila kilichokuwa chake. Juhudi za kumtafuta kwa njia za mkononi hazikuzaa matunda kwa sababu simu yake ilikuwa imezimwa.

Baada ya kumkosa hotelini, mtayarishaji wa filamu hiyo aliamua kupiga simu kwa mkewe, lakini naye hakuwa na taarifa zozote kuhusu mahali alipokuwa. Aliahidi kumtumia ujumbe iwapo angempata.

Baadaye, mtayarishaji huyo wa filamu alifanikiwa kumpata Vicker kwenye simu yake ya mkononi, ambapo alimweleza kwamba, alikuwa mjini Lagos akijiandaa kupanda ndege kurejea nyumbani.

Katika mazungumzo yao, Vicker alimweleza mtayarishaji huyo wa filamu kwamba, alikuwa na ahadi ya kufika kwenye ubalozi wa Marekani nchini Ghana asubuhi ya siku iliyofuata.

Majibu hayo yalimkera mtayarishaji huyo wa filamu, ambaye alimshutumu Vicker kwa kutokuwa mwaminifu na kuishindwa kuiheshimu kazi yake, ikiwa ni pamoja na kutomweleza mapema kwamba alikuwa na mipango ya kuondoka.

Vicker alimjibu ‘kibosile’ huyo kwa kumweleza kwamba, alitarajia upigaji wa picha za filamu hiyo ungemalizika kabla ya yeye kuondoka kurejea Ghana.

Lakini Vicker alikuwa amesahau kwamba, upigaji wa picha za filamu hiyo ulichelewa kuanza kutokana na yeye kuwa na mkataba wa kupiga picha za filamu nyingine katika mji mwingine tofauti kwa wakati mmoja.

Kutokamilika kwa filamu hiyo mapema pia kulichangiwa na tabia ya Vicker kufika eneo la kupiga picha akiwa amechelewa.

Mbali na Vicker, mwigizaji mwingine aliyedaiwa kuchelewesha upigaji wa picha za filamu hiyo ni Mercy Jonhnson, ambaye aliomba ruhusa ya kuhudhuria sherehe za harusi ya Mike Ezuruonye mjini Enugu.

Kitendo cha Vicker kuingia mitini kabla ya filamu hiyo kukamilika, kimemkera mtayarishaji wake kwa sababu alishalipwa Naira 600,000 kwa ajili ya kazi hiyo na alitaka alipwe kwanza kabla ya kuanza kazi.

Vicker ni mmoja wa waigizaji nyota wa Ghana waliojipatia sifa kubwa barani Afrika kutokana na kushiriki kucheza filamu nyingi zilizotayarishwa nchini Nigeria.

Mwigizaji huyo aliyezaliwa Agosti Mosi, 1977, amewahi kushinda tuzo mbili za mwigizaji bora na ya mwigizaji bora anayechipukia za African Movie Academy Awards mwaka 2008.

Mama wa mwigizaji huyo asili yake ni nchini Liberia na baba yake ni raia wa Uholanzi. Baba yake alifariki wakati Vicker akiwa na umri wa miaka sita.

Vicker amekuwa akikakariwa mara kadhaa kwenye vyombo vya habari akisema kuwa, amelelewa zaidi na mama yake. Kutokana na kifo cha baba yake, Vicker amekuwa karibu zaidi na mama yake na amekuwa akimwelezea kama mtu shujaa.

Kabla ya kuwa mwigizaji, Vicker alikuwa mtangazaji wa kituo cha televisheni cha Metropolitan. Mwaka 2003, alionekana kwa mara ya kwanza kwenye kipindi cha televisheni cha Suncity, kikielezea maisha yake.

Filamu yake ya kwanza inajulikana kwa jina la Divine Love, akiwa mwigizaji msaidizi. Filamu hiyo pia iliwashirikisha waigizaji wenzake wa Ghana, Jackie Aygemang na Majid Michel, ambaye walisoma pamoja shule ya sekondari.

Vicker amekuwa akipewa nafasi zaidi ya kucheza filamu zinazohusu mapenzi, akiwa na waigizaji wengine nyota wa Ghana kama vile Nadia Buari na Jackie. Mashabiki wengi wa filamu wa Ghana na Nigeria wamekuwa wakimfananisha na Ramsey Nouah.

Mwigizaji huyo ameoa na ana watoto wawili. Kwa sasa anamiliki kampuni ya wakala wa matangazo, inayojulikana kwa jina la Sky & Orange na kampuni ya matukio, inayoitwa Babetown. Pia anamiliki taasisi ya Van Vicker Foundation.

APR bingwa Kombe la Kagame



WACHEZAJI wa timu ya APR ya Rwanda wakiwa na kombe la ubingwa wa michuano ya soka ya Kombe la Kagame walilolitwaa juzi baada ya kuichapa St George ya Ethiopia mabao 2-0 katika mechi ya fainali iliyochezwa kwenye uwanja wa Amahoro mjini Kigali. (Picha ya CECAFA).

Na Mwandishi Wetu, Kigali

APR ya Rwanda juzi ilitawazwa kuwa mabingwa wapya wa michuano ya soka ya Kombe la Kagame baada ya kuichapa St George ya Ethiopia mabao 2-0 katika mechi ya fainali iliyochezwa kwenye uwanja wa Amahoro mjini hapa.

Mshindi wa pambano hilo ilibidi apatikane katika muda wa nyongeza wa dakika 30 baada ya timu hizo kumaliza dakika 90 zikiwa suluhu.

APR ilihesabu bao lake la kwanza dakika ya 93 kupitia kwa Chiukepo Msowoya kabla ya Victor Nyirenda kuongeza la pili dakika ya 95.

Kwa ushindi huo, APR ilizawadiwa kitita cha dola 30,000 za Marekani, zilizotolewa na mdhamini wa michuano hiyo, Rais Paule Kagame wa Rwanda. St George ilizawadiwa dola 20,000.

Mabingwa wa mwaka jana, Atraco ya Rwanda walimaliza michuano hiyo wakiwa wa nne baada ya kupata kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Sofapaka ya Kenya.

Ushindi huo uliiwezesha Sofapaka kuzawadiwa kitita cha dola 10,000 kwa kushika nafasi ya tatu. Rais Kagame hudhamini michuano hiyo kila mwaka kwa kutoa dola 60,000 za Marekani kwa ajili ya washindi watatu wa kwanza.

Sofapaka ilitawala sehemu kubwa ya pambano hilo na kupata bao la kuongoza dakika ya 19 lililofungwa na Akinyemi Abass. Alifunga bao hilo baada ya kupokea pasi kutoka kwa Bob Mugalia.

Atraco ilisawazisha dakika ya 37 kwa bao lililofungwa na Birory Dady kabla ya Laurent Tumba kuiongezea Sofapaka bao la pili na la ushindi dakika ya 40.

Mechi ya fainali ilihudhuriwa na watazamaji wapatao 40,000 wakiongozwa na Rais Kagame. Mechi hiyo pia ilishuhudiwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Kenya, anayechezea klabu ya Inter Milan ya Italia, MacDonald Mariga.

Katika michuano ya mwaka huu, mshambuliaji Msowoya wa APR aliibuka kuwa mfungaji bora baada ya kupachika wavuni mabao saba.

Jumla ya timu 11 kutoka nchi wanachama wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), zilishiriki katika michuano ya mwaka huu.

Friday, May 21, 2010

Milioni 94 zamng'oa Ngasa Yanga



HATIMAYE timu ya Azam FC imefanikiwa kumng'oa mchezaji Mrisho Ngasa wa Yanga baada ya mazungumzo yaliyofanyika kwa siku mbli kati ya viongozi wa klabu hizo mbili.

Chanzo cha habari kutoka ndani ya Yanga kimeeleza kuwa, klabu hizo mbili zilikubaliana uhamisho wa mchezaji huyo ugharimu sh. milioni 94 na malipo hayo yalifanyika jana kwenye benki moja iliyopo barabara ya Lumumba, Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa habari hizo, kati ya malipo hayo, Ngasa amepata sh. milioni 40 wakati klabu ya Yanga imelipwa sh. milioni 54.

Mwenyekiti wa Yanga, Iman Madega amekiri kufanyika kwa mazungumzo hayo, lakini alikataa kutaja kiasi cha fedha walichokubaliana kwa ajili ya uhamisho wa Ngasa.

Naye Ngasa alipoulizwa alisema, hafahamu lolote kuhusu makubaliano yaliyofikiwa kati ya viongozi wa klabu hizo mbili kwa vile hakuwepo kwenye kikao hicho.

Mchezaji huyo jana mchana alionekana akiwa na Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako na kiongozi mmoja wa Azam wakiingia katika benki moja jijini Dar es Salaam, ambako inasemekana walikwenda kukamilisha malipo hayo.

Taarifa za kuondoka kwa Ngasa zimepokelewa kwa mshutuko mkubwa na mashabiki wa Yanga, kutokana na ukweli kuwa, mchezaji huyo alikuwa tegemeo kubwa la timu hiyo katika safu ya ushambuliaji.

Ngasa, ambaye ni mtoto wa mchezaji wa zamani wa Pamba ya Mwanza na Simba, Khalfan Ngasa, alijiunga na Yanga mwaka 2006 akitokea Kagera Sugar. Aliitwa kwenye kikosi cha timu ya taifa, Taifa Stars kwa mara ya kwanza mwaka 2007.

Thursday, May 20, 2010

Hatuwezi kumzuia Yondani kwenda Yanga-Rage

MWENYEKITI wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage amesema hawawezi kumzuia beki wao nyota, Kelvin Yondani kujiunga na wapinzani wao wa jadi, Yanga.

Akizungumza mjini Dar es Salaam juzi, Rage alisema timu yake inaundwa na wachezaji wengi wenye vipaji vya kucheza soka hivyo kuondoka kwa Yondani hakuwezi kuwa pigo kwao.

Rage alisema cha msingi kinachotakiwa kufanywa na mchezaji huyo ni kuheshimu na kufuata taratibu zote za usajili, ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa za kuaga kwa uongozi.

“Sina hakina kama ni kweli Yondani anataka kujiunga na Yanga, nimekuwa nikizisikia taarifa hizo kupitia kwenye vyombo vya habari, lakini kama ni za kweli, sisi hatuna kipingamizi chochote kwake,”alisema.

Ameutaka uongozi wa Yanga kufuata taratibu katika kumsajili mchezaji huyo kwa vile bado ana mkataba wa kuichezea Simba. Hakusema mkataba huo ni wa muda gani.

“Si busara hata kidogo kumzuia mchezaji kwenda kutafuta maslahi mazuri zaidi kwa sababu soka ndiyo kazi yake. Tunachosisitiza ni taratibu za usajili kufuatwa na kuheshimiwa,”aliongeza.

“Kama Yanga wamemuahidi mshahara mkubwa zaidi, ambao sisi hatuwezi kumpa, tupo tayari kumruhusu kwenda huko kwa moyo mweupe kabisa,” aliongeza.

Msimamo huo wa Simba umekuja siku chache baada ya vyombo vya habari kumnukuu Yondani hivi karibuni akisema kuwa, hivi sasa yupo huru baada ya mkataba wake na klabu hiyo kumalizika.

Vyombo hivyo vya habari vilimkariri Yondani akisema kuwa, atakuwa tayari kujiunga na Yanga iwapo klabu hiyo itampatia kitita cha sh. milioni 30.

Mbali na Yondani, imedaiwa pia kuwa, klabu ya Yanga inafanya mipango ya kumsajili mshambuliaji Emmanuel Okwi, aliyesajiliwa na Simba msimu uliopita akitokea Uganda.

KHADIJA KOPA: Hakuna anayeweza kunifikia kwa uimbaji taarab



Na Mohammed Issa

KWA umbo, Khadija Omar Kopa ni mnene. Rangi yake ni nyeusi yenye mng’ao. Uso wake hujawa na tabasamu muda wote utadhani hajui kitu kinachoitwa kukasirika.

Licha ya kuwa na umbile hilo, Khadija ni mwepesi wa kuunyonganyonga mwili wake atakavyo awapo stejini, akiimba nyimbo za muziki wa taarab. Sauti yake nayo ni maridhawa na yenye mvuto wa pekee.

Sifa hizo ndizo zilizomfanya mwanamama huyo apachikwe jina la ‘Malkia wa Mipasho’ nchini. Waliompa jina hilo hawakubahatisha, walitambua vyema kwamba uwezo wake katika fani hiyo ni mkubwa.

Mwanamama huyo alianza kuvuma kimuziki miaka 20 iliyopita alipokuwa katika kikundi cha taarab cha Culture cha Zanzibar, ambako aling’ara kwa vibao vyake kama vile ‘Kadandie’, ‘Wahoi’ na ‘Daktari’.

Anakiri kwamba, akiwa katika kundi hilo, aliweza kujifunza mambo mengi kuhusu muziki wa taarab ikiwa ni pamoja na utunzi wa nyimbo, uimbaji bora na upangiliaji wa muziki.

"Culture ni chuo, ambacho nilianza kujifunza uimbaji na utungaji wa mashairi, nilipata uzoefu wa kutosha na mashabiki walinikubali," alisema Khadija alipokuwa akizungumza na mwandishi wa makala hii hivi karibuni mjini Dar es Salaam.

Baada ya kutoka Culture, mwimbaji huyo alitua katika kundi la TOT mwaka 1992 akiwa mmoja wa waanzilishi wake, ambapo alianza kung’ara kwa kibao cha ‘Tx mpenzi’, ‘Ngwinji’, ‘Wrong number’, ‘Mtie kamba mumeo’ na nyinginezo.

“Kule Culture ni kama vile nilikuwa nasafisha nyota yangu, lakini baada ya kujiunga na TOT ndipo hasa mambo yangu yalipoanza kuwa mazuri,”alisema.

Khadija alikorofishana na uongozi wa TOT mwaka 1993 baada ya yeye na mwimbaji mwenzake, Othman Soud kuamua kuondoka kinyemela na kwenda Dubai, ambako walishiriki kuanzisha kundi la East African Melody.

Mara baada ya kurejea nchini kutoka Dubai, mwanamama huyo alilazimika kujiunga na kikundi cha Muungano Cultural Troupe kwa vile uongozi wa TOT uligoma kumpokea.

Kujiunga kwa Khadija na Othman katika kikundi cha Muungano kulisababisha kuwepo kwa ushindani mkali kati ya vikundi hivyo viwili, ambavyo vilifanya maonyesho kadhaa kwa ajili ya kuonyeshana nani mkali.

Akiwa Muungano, Khadija aling’ara kwa vibao vyake murua kama vile ‘Homa ya Jiji’, ‘Kiduhushi’ na ‘Umeishiwa’. Pia kulizuka ushindani mkali kati yake na marehemu Nasma Khamis ‘Kidogo’, ambaye alichukuliwa na TOT kutoka Culture kwa lengo la kuziba pengo lake.

"Nilipojiunga na Muungano nililiwezesha kundi hilo kuwa juu na tuliwapa wakati ngumu kweli wapinzani wetu TOT,”alisema mwimbaji huyo.

Mwaka 1998, mwanamama huyo aliamua kurejea TOT, akibadilishana na Nasma, ambaye aliamua kuhamia Muungano, hali iliyoongeza ushindani mkali kati ya vikundi hivyo.

Khadija anasema alikuwa akihama mara kwa mara kutoka kundi moja hadi jingine kutokana na matatizo ya uongozi na maslahi duni. Alisema msanii siku zote hufurahia kazi yake pale anapopata maslahi mazuri.

Mwimbaji huyo alisema kwa sasa anajivunia umaarufu aliojijengea nchini kutokana na uimbaji wake maridhawa na kuongeza kuwa, muziki huo umemwezesha kutembelea mikoa yote ya Tanzania.

"Usifanye mchezo, taarab hivi sasa inalipa, lakini ukiwa unamiliki kundi lako. Amini usiamini, taarab ipo juu kuliko muziki mwingine wowote ule," anasema mwanamama huyo.

Khadija alisema kwa sasa anajiandaa kuzindua wimbo wake mpya, utakaojulikana kwa jina la 'Top in Town'. Alisema amechelewa kuuzindua wimbo huo kutokana na kukosa wadhamini.

Mwimbaji mwenye sura yenye mvuto na mwili tipwatipwa alisema, wimbo huo umeshakamilika na kuanza kupigwa kwenye vituo mbalimbali vya radio na televisheni nchini.

"Ninachokifanya hivi sasa ni kuutambulisha wimbo huu kwa mashabiki wangu. Nikipata mdhamini nitauzindua rasmi kwa onyesho maalumu," alisema.

Gwiji huyo wa mipasho alisema, licha ya kuwepo kwa ushindani mkubwa katika muziki wa taarab hivi sasa, bado anaamini yeye ndiye malkia wa muziki huo na hakuna mwimbaji anayeweza kumfikia.

"Ninachowaambia wapinzani wangu ni kwamba, waparamie miti yote, lakini wajihadhari na mbuyu. Hawawezi kunifikia hata kwa bahati mbaya," alijigamba Gwiji huyo anayependwa na mashabiki wengi kutokana na uchangamfu wake awapo stejini.

Khadija alilielezea soko la muziki wa taarab hivi sasa kuwa ni kubwa, tofauti na miaka ya nyuma na kuongeza kuwa, muziki huo umekuwa na manufaa makubwa kwa wasanii.

Mwimbaji huyo mahiri alisema kwa sasa hana mpango wa kuhama katika kikundi cha sanaa za maonyesho cha Tanzania One Theatre (TOT) na ameahidi kuwapa raha zaidi ya muziki huo mashabiki wake.

Mbali na kutembelea mikoa yote nchini, Khadija alisema muziki huo umemwezesha kusafiri katika nchi kadhaa za Ulaya, Arabuni na Afrika. Alizitaja nchi hizo kuwa ni Marekani, Ufaransa, Ureno, India, Comoro, Kenya, Zimbabwe na Oman.

Mwimbaji huyo alisema pia kuwa, muziki wa taarab umemwezesha kujenga nyumba mbili katika kisiwa cha Unguja na pia kuendesha maisha yake bila matatizo.

Khadija, ambaye alizaliwa miaka 47 iliyopita katika kisiwa cha Unguja,
amebahatika kupata watoto wanne, lakini mmoja, ambaye alikuwa amerithi kipaji chake, Omar Kopa alifariki dunia mwaka juzi.

Anakiri kwamba kifo cha Omar kilikuwa pigo kubwa kwake na familia yake kwa sababu alikuwa na kipaji cha hali ya juu cha muziki. Anasema alikuwa akisaidiana naye katika utunzi wa nyimbo.

Simba yadundwa Rwanda

Na Charles Mganga, Kigali

SIMBA jana ilijiweka kwenye nafasi ngumu ya kusonga mbele katika michuano ya Kombe la Kagame baada ya kuchapwa bao 1-0 na Sofapaka katika mechi ya kundi C iliyochezwa kwenye uwanja wa Nyamirongo mjini hapa.

Kwa matokeo hayo, Sofapaka imefuzu kucheza robo fainali kwa kuongoza kundi hilo, ikiwa na pointi sita baada ya kucheza mechi mbili, ikifuatiwa na Simba yenye pointi tatu. Mechi nyingine ya kundi hili ilitarajiwa kuchezwa jana jioni kati ya URA ya Uganda na Atraco ya Rwanda.

Kwa mujibu wa ratiba ya michuano hiyo, Simba itacheza mechi yake ya mwisho kesho mchana kwa kumenyana na URA. Iwapo itashinda, itakuwa na nafasi kubwa ya kusonga mbele, lakini kwa kutegemea matokeo ya mechi kati ya Sofapaka na Atraco.

Mchezaji wa zamani wa Yanga, anayechezea Sofapaka, John Barasa
ndiye aliyeiua Simba baada ya kufunga bao hilo na la pekee dakika ya 32 kwa shuti kali lililomshinda kipa Juma Kaseja.

Barasa pia alizitikisa nyavu za Simba dakika ya 16 baada ya kuitoka ngome yake na kufumua shuti lililotinga wavuni, lakini mwamuzi
Mohamed Farah alilikataa kwa madai kuwa mfungaji aliotea.

Sofapaka iliendeleza mshambulizi langoni mwa Simba na kuifanya ngome ya timu hiyo, iliyokuwa chini ya beki Joseph Owino kufanya kazi ya ziada kuokoa mipira ya hatari. Kipa Juma Kaseja mara kadhaa alilazimika kuokoa mashuti ya washambuliaji wa timu pinzani.

Katika dakika 45 za mwanzo, Simba ilizidiwa maarifa na Sofapaka kutokana na sehemu ya kiungo, iliyokuwa chini ya Abdulrahim Humoud na Jerry Santo kuruhusu wapinzani wao kutawala eneo la katikati ya uwanja.

Licha ya kufungwa bao hilo, Simba ilionyesha uhai katika safu ya ushambuliaji, ambapo Mussa Hassan 'Mgosi', Robert Ssentongo na Uhuru Selemani walikuwa tishio kwa kipa, Obungu Wilson.

Kipindi cha pili kilitawaliwa zaidi na Sofapaka, ambayo ilionyesha kiwango cha juu na kuipa wakati mgumu Simba, iliyoshindwa kusawazisha.

Simba: Juma Kaseja, Juma Jabu, Kelvin Yondani, Juma Nyoso, Joseph Owino, Abdulhalim Humoud, Jerry Santo, Uhuru Selemani/Nico Nyagawa, Ramadhani Chombo, Robert Ssentongo na Mussa Mgosi.

Sofapaka: Obungu Wilson, Edger Ochieng, Rashid Idrisa, Anthony Kimani, Hussein Abdulrazak, John Barasa, Hugo Nzoka, Humphrey Ochieng, Bob Mugalia, Thomas Wanyama na James Situma.

Rage ampasha Kaduguda

MWENYEKITI mpya wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage amesema ajira za watendaji watatu wakuu wa klabu hiyo zitafanyika kwa kufuata taratibu zilizowekwa.

Rage alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, uongozi wake utakutana hivi karibuni kwa ajili ya kupanga taratibu za ajira ya viongozi hao.

Kwa mujibu wa katiba mpya ya Simba, klabu hiyo inapaswa kuajiri katibu mkuu, mhasibu na ofisa habari wa klabu.

Ajira za viongozi hao ni utekelezaji wa maelekezo ya Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA), ambalo limezitaka nchi wanachama kuzitaka klabu za ligi kuu ziajiri viongozi hao watatu.

Rage alielezea msimamo huo wa uongozi wake, kufuatia Katibu Mkuu wa zamani wa Simba, Mwina Kaduguda kuomba yeye na viongozi wenzake wa kuajiriwa waliomaliza muda wao, wafikirie kupewa tena ajira hizo.

Mbali na Kaduguda, ambaye kabla ya kupewa ajira hiyo alikuwa katibu mkuu wa kuchaguliwa, wengine ni aliyekuwa mhasibu, Chano Almasi na ofisa habari wa klabu, Clifford Ndimbo.

Rage alisema hata kama ajira hizo zitatolewa tena, ni vigumu kusema iwapo watawarejesha tena viongozi hao wa zamani kwa sababu taratibu za ajira zinafanywa na kamati ya utendaji.

Ngasa: Nipo tayari kwa lolote

MSHAMBULIAJI Mrisho Ngasa wa Yanga amesema yupo tayari kwa uamuzi wowote utakaochukuliwa katika kikao cha pamoja kati ya viongozi wa klabu hiyo na Azam.

Ngasa amesema kwa sasa anasubiri hatma ya kikao hicho kilichotarajiwa kufanyika jana kwenye hoteli ya Movenpick mjini Dar es Salaam.

“Mimi nipo tayari kuichezea timu yoyote, itakayokuwa tayari kunilipa dau ninalolitaka,”alisema Ngasa alipozungumza na Burudani kwa njia ya simu mjini Dar es Salaam.

“Kwa sasa siwezi kufahami ni timu ipi nitakayoichezea msimu ujao. Kikao cha pamoja kati ya viongozi wa Yanga na Azam ndicho kitakachotoa hatma yangu,”aliongeza.

Ngasa ameelezea msimamo wake huo siku moja baada ya uongozi wa Yanga kusema, hautakuwa tayari kumruhusu ajiunge na Azam kwa vile bado ana mkataba na klabu hiyo hadi mwaka 2010.

Mbali na kutakiwa na Azam, mshambuliaji huyo mwenye kasi na chenga za maudhi, pia anawindwa kwa udi na uvumba na klabu ya APR ya Rwanda, alikokwenda kufanya majaribio wiki iliyopita.

Wakati huo huo, Mwandishi Wetu Charles Mganga ameripoti kutoka Rwanda kuwa, timu ya APR imesema bado haijakata tamaa ya kumsajili Ngasa.

Kocha Msaidizi wa APR, Nshimiyimana Eric alisema juzi mjini hapa kuwa, wameshamalizana na Ngasa kwa ajili ya kumsajili msimu ujao.

Eric alisema hakuna kilichowakwamisha kumsajili mchezaji huyo ambaye tangu atue Jangwani, amekuwa mwiba mchungu kwa timu pinzani kwenye ligi kuu soka Tanzania Bara.

“Tulishakutana na Ngasa mjini hapa na kufanyanaye mazungumzo, ambayo yalifikia hatua nzuri. Alitueleza anachotaka nasi tukakubali na kumwambia ofa zetu. Mpaka anaondoka, mambo yetu na yeye yalikuwa yameshamalizika," alisema kocha huyo.

Eric alisema kilichobaki kwao ni uongozi wa APR kukutana na viongozi wa Yanga ili kukubaliana kuhusu malipo ya ada ya uhamisho wa mchezaji huyo.

"Siwezi kusema kwamba tumekwama, tunachofanya kwa sasa ni kutafuta muda ili tuweze kwenda Tanzania kuongea na viongozi wa mchezaji huyo," aliongeza Eric.

Kocha huyo alisema, wana nia ya dhati ya kumnasa mchezaji huyo na kamwe wasingependa kumkosa kutokana na uwezo wake na kipaji alichonacho cha kusakata kabumbu.

Awali, APR ilikuwa tayari kumlipa Ngasa dau la sh. milioni 20 kwa ajili ya kukamilisha uhamisho wake, lakini mchezaji huyo aligoma na kutaka alipwe sh. milioni 40 na mshahara wa sh. milioni 1.5 kila mwezi.

Wednesday, May 19, 2010

DALALI AKABIDHI OFISI KWA RAGE



Mwenyekiti wa zamani wa klabu ya Simba, Hassan Dalali akikabidhi kombe la ubingwa wa ligi kuu ya Vodacom kwa Mwenyekiti mpya wa klabu hiyo, Ismail Aden Rage wakati wa makabidhiano ya ofisini yaliyofanyika makao makuu ya klabu hiyo mtaa wa Msimbazi mjini Dar es Salaam jana.

Tuesday, May 18, 2010

SIMBA YAUNGURUMA RWANDA



MABINGWA wa soka wa Tanzania Bara, Simba jana walianza vyema michuano ya Kombe la Kagame baada ya kuichapa Atraco ya Rwanda mabao 2-1 katika mechi ya kundi C iliyochezwa kwenye Uwanja wa Amahoro mjini Kigali.

Mabao ya Simba yalifungwa na washambuliaji Robert Ssentongo na Mussa Hassan 'Mgosi', moja katika kila kipindi.

Simba inatarajiwa kuteremka tena dimbani kesho kupambana na Sofapaka ya Kenya, ambayo katika mechi ya ufunguzi iliicharaza URA ya Uganda mabao 3-0.

HII NDIO YANGA BWANA!



Wana-Yanga wa zamani wanakwambia kwamba hii ndiyo Yanga Original, iliyokuwa imesheheni wachezaji mbalimbali wenye uwezo wa kufanya maajabu uwanjani. Je, unawakumbuka wachezaji hawa? Yoyote anayewakumbuka tunaomba atusaidie majina yao.

UNAWAKUMBUKA WACHEZAJI HAWA?



HIKI ni kikosi cha wachezaji wa Simba kilichotamba miaka ya 1970 kwa kufanya vizuri katika michuano ya ligi na ya kimataifa. Je, unawakumbuka wachezaji hawa? Anayewakumbuka tunaomba atusaidie majina yao.

Monday, May 17, 2010

Rekodi na matukio muhimu Kombe la Dunia

BAO la mapema zaidi kufungwa katika fainali za Kombe la Dunia ni lile la Vaclav Masek wa Czechoslovakia, ambalo alilifunga sekunde la 16 wakati timu hiyo ilipomenyana na Mexico mwaka 1962.

Bao lililochukua dakika nyingi ni lile lililofungwa na David Pllatt wa England. Alifunga bao hilo dakika ya 119 wakati timu hiyo ilipomenyana na Ubelgiji katika fainali za mwaka 1990.

Mabao mengi yaliyofungwa haraka na kwa muda mfupi ni yale ya mwaka 1982. Mabao hayo yalifungwa na Laszlo Kiss wa Hungary. Alifunga mabao hayo dakika ya 70, 74 na 77.

Mchezaji mwenye umri mkubwa kufunga bao katika fainali za michuano hiyo ni Roger Milla wa Cameroon. Alifunga bao hilo katika fainali za mwaka 1994 dhidi ya Russia akiwa na umri wa miaka 42 na siku 39.

Mchezaji pekee aliyefunga bao na kujifunga katika mechi moja ni Ernie Brandts wa Uholanzi. Alijifunga na baadaye kufunga bao wakati Uholanzi ilipomenyana na Italia mwaka 1978. Katika mechi hiyo, Uholanzi iliibuka na ushindi wa mabao 2-1.

Goli la kwanza la kujifunga lilikuwa la Ramon Gonzalez wa Paraguay katika fainali za mwaka 1930. Alijifunga bao hilo wakati Paraguay ilipochapwa mabao 3-0 na Marekani.

Mchezaji aliyezifungia mabao nchi mbili tofauti katika fainali za kombe hilo ni Robert Prosineck. Aliichezea Yugoslavia mwaka 1990 na kuipachikia bao dhidi ya Falme za Kiarabu. Pia aliichezea Croatia katika fainali za mwaka 1998 na kuifungia bao dhidi ya Jamaica.

Wachezaji waliofunga mabao katika fainali mbili tofauti za kombe hilo ni Vava wa Brazil (1958 na 1962), Pele wa Brazil (1958 na 1970) na Paul Breitner wa iliyokuwa Ujerumani Magharibi (1974-1982).

Mchezaji mwenye umri mdogo kufunga bao katika fainali hizo alikuwa Pele wa Brazil. Alifunga bao hilo katika fainali za mwaka 1958 timu hiyo ilipomenyana na Wales, akiwa na umri wa miaka 17.

Mchezaji aliyefunga bao katika kila mechi alizocheza katika fainali hizo ni Jairzinho wa Brazil mwaka 1970 na Alcide Ghiggia wa Uruguay mwaka 1950.

Je Wajua?

Miji 23 imewahi kutumika mara mbili kwa fainali za Kombe la Dunia. Miji hiyo ni Berlin, Dortmund, Frankfurt, Gelsenkirchen, Hamburg, Hanover, Munich, Stuttgart na miji mingine minane katika nchi za Mexico na Ufaransa na miji saba ya Italia.

Miji saba iliyoandaa fainali za mwaka 1974 pia ilitumika tena katika fainali za mwaka 2006 zilizofanyika Ujerumani. Mji pekee ulioachwa ni Dusseldorf. Miji mipya ilikuwa Cologne, Kaiserslautern, Leipzig na Nuremberg.

Kombe la mwanzo la dunia lililoitwa Jules Rimet, lilizawadiwa moja kwa moja kwa Brazil mwaka 1970 baada ya kushinda fainali hizo mara tatu. Kombe hilo lililotengenezwa kwa madini ya dhahabu, liliibwa nchini humo na kuyeyushwa.

Kombe la pili liliibwa mwaka 1966 nchini England, lakini liligunduliwa baadaye likiwa limefukiwa ardhini chini ya mti. Aliyeligundua alikuwa mbwa mdogo aliyejulikana kwa jina la Pickles.

Licha ya kuwa majirani, vyama vya soka vya Argentina na Uruguay vilikuwa vikitumia mipira tofauti na kusababisha ubishani mkali katika mechi ya fainali kati ya timu hizo mwaka 1930 kuhusu mpira upi utumike. Mwamuzi Jean Langenus kutoka Ubelgiji aliamua mpira mwepesi wa Argentina utumike kipindi cha kwanza na mpira mzito wa Uruguay utumike kipindi cha pili.

Nchi zilizofuzu kucheza mara nyingi mechi ya fainali ya Kombe la Dunia ni Brazil, Ujerumani, Italia na Argentina. Brazil imemcheza fainali mara saba na kushinda mara tano. Ujerumani imecheza fainali mara saba na kushinda mara tatu. Italia imecheza fainali mara tano na kushinda mara nne. Argentina imecheza fainali mara tatu na kushinda mara mbili.

Brazil ndiyo nchi pekee iliyofuzu kucheza fainali zote 18 za kombe la dunia, ikifuatiwa na Italia na Ujerumani, zilizofuzu kucheza fainali 16 na Argentina iliyofuzu kucheza fainali 14.

Haijawahi kutokea kwa bingwa mtetezi kufanya vibaya katika fainali za kombe la dunia kama ilivyokuwa kwa Ufaransa mwaka 2002. Si tu kwamba ilishindwa kuvuka raundi ya kwanza, bali pia haikushinda hata mechi moja.

Wachezaji waliocheza mechi nyingi za fainali za Kombe la Dunia ni kipa Antonio carbajal wa Mexico (1950-66) na Lothar Matthaus wa Ujerumani (1982-98). Wachezaji hao walicheza fainali tano za kombe la dunia kila mmoja.

Norman Whiteside wa Ireland Kaskazini alikuwa mchezaji wa kwanza mwenye umri mdogo kucheza fainali za Kombe la Dunia mwaka 1982. Alicheza fainali hizo akiwa na umri wa miaka 17 na siku 41 wakati timu hiyo ilipomenyana na Yugoslavia.

Wanasoka wawili waliweka rekodi ya kutwaa Kombe la Dunia wakiwa wachezaji na makocha. Mario Zagallo wa Brazil alitwaa kombe la dunia akiwa mchezaji mwaka 1958 na 1962 na pia akiwa kocha 1970. Franz Beckenbauer wa Ujerumani alitwaa kombe hilo akiwa mchezaji mwaka 1974 na akiwa kocha 1990.

Oliver Kahn wa Ujerumani alikuwa kipa wa kwanza kupewa tuzo ya ya mpira wa dhahabu akiwa mchezaji katika fainali za mwaka 2002 zilizofanyika Japan na Korea Kusini.

Pele wa Brazil ni mchezaji pekee aliyecheza fainali tatu za kombe hilo na nchi hiyo kutwaa ubingwa. Alicheza fainali za mwaka 1958, 1962 na 1970. Hakucheza fainali za mwaka 1966 kutokana na kuwa majeruhi. Cafu wa Brazil pia alicheza fainali tatu mfululizo za mwaka 1994, 1998 na 2002.

Bora Milutinovic wa Serbia ndiye kocha pekee aliyeziongoza nchi tano katika fainali tano tofauti za kombe la dunia kati ya mwaka 1986 hadi 2002. Alizifundisha nchi za Mexico, Costa Rica, Marekani, Nigeria na China.

Carlos Alberto Parreira wa Brazil ameziongoza nchi nne katika fainali nne tofauti za kombe hilo. Nchi hizo ni Brazil, Saudi Arabia, Muungano wa Falme za Kiarabu na Kuwait.

Makocha watano waliziwezesha nchi zao kucheza fainali za kombe hilo mara mbili. Makocha hao ni Pozzo wa Italia (1934 na 1938), Schon wa iliyokuwa Ujerumani Magharibi (1966-1970), Zagallo wa Brazil (1970-1998), Beckenabauer wa iliyokuwa Ujerumani Magharibi (1986-1990) na Bilardo wa Argentina (1986-1990).

Mechi 16 ziliamuliwa kwa penalti kuanzia mwaka 1982 wakati Ujerumani ilipoishinda Ufaransa katika mechi ya nusu fainali. Mechi maarufu ilikuwa ya fainali ya mwaka 1994wakati Brazil ilipoichapa Italia kwa penalti 3-2 baada ya timu hizo kumaliza dakika 120 zikiwa suluhu. Italia pia ilifungwa mara mbili kwa njia ya penalti na Argentina na Ufaransa katika fainali za 1990 na 1998.

Kombe la Dunia lilianzishwa na Jules Rimet





HAKUNA michuano mingine yenye msisimko na inayovuta watu wengi duniani kama fainali za soka za Kombe la Dunia, zinazoandaliwa kila baada ya miaka minne na Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA).

Tangu fainali hizo zilipofanyika kwa mara ya kwanza mwaka 1930 nchini Uruguay,, FIFA imezidi kukua, kupata umaarufu na mafanikio makubwa kutokana na mchezo wa soka.

Wazo la kuandishwa kwa fainali za Kombe la Dunia lilianza nchini Ufaransa mwaka 1920 kutoka kundi moja la Wafaransa, likiongozwa na Jules Rimet.

Kombe la kwanza la dunia lililotengenezwa kwa kutumia madini ya dhahabu, lililopewa jina la Jules Rimet, lilishindaniwa mara tatu miaka ya 1930 kabla ya vita ya pili ya dunia, iliyosababisha fainali hizo zisifanyike kwa miaka 12.

Fainali hizo ziliporejea tena mwaka 1950, zilizidi kupata umaarufu mkubwa na kuwa pekee zenye msisimko na mvuto duniani.

Ziliingia doa mwaka 1966 baada ya kombe la awali la dunia kutoweka katika mazingira ya kutatanisha nchini England, lakini baadaye liligunduliwa likiwa limezikwa ardhini chini ya mti na mbwa mdogo, aliyekuwa akiitwa Pickles.

Kombe hilo lilitoweka tena mwaka 1983 baada ya kuibwa na wezi, safari hii mjini Rio de Janeiro na baadaye kuyeyushwa. Shirikisho la Soka la Brazil, ambalo lilipewa haki ya kulitunza kombe hilo, kufuatia timu ya taifa ya nchi hiyo kulitwaa mara tatu, liliamua kutengeneza kombe lingine.

Kombe la mwanza la dunia lilikuwa na urefu wa sentimita 3.8. Kombe hilo lilitengenezwa kwa kutumia mchanganyiko wa madini ya fedha na dhahabu na jiwe la ‘semi-precious’.

Kati ya mwaka 1930 na 1970, kombe hilo liliwekwa sahani ya dhahabu katika pande zote nne za chini, ambako yaliandikwa majina ya nchi zilizowahi kulitwaa.

Tangu kuanzishwa kwake, fainali hizo zilikuwa zikifanyika katika nchi moja za Ulaya na Amerika hadi mwaka 1996 wakati Kamati ya Utendaji ya FIFA ilipoziteua Japan na Korea Kusini kuandaa fainali hizo kwa pamoja mwaka 2002 na kufanyika kwa ufanisi mkubwa.

Kwa kipindi cha miaka 16 tangu fainali hizo zilipoanzishwa mwaka 1930, nchi saba zimetwaa ubingwa wa dunia. Nchi hizo ni Uruguay, Italia, Ujerumani, Brazil, England, Argentina na Ufaransa.

Brazil ndiyo inayoongoza kwa kutwaa ubingwa mara tano kuanzia mwaka 1958, 1962, 1970, 1994 na 2002. Inafuatiwa na Italia, iliyotwaa ubingwa mara nne, kuanzia mwaka 1934, 1938, 1982 na 2006.

Ujerumani imetwaa kombe hilo mara tatu, mwaka 1954, 1974 na 1990 wakati Uruguay imelitwaa mara mbili, 1930 na 1950 sawa na Argentina, iliyolitwaa 1978 na 1986 England na Ufaransa zimetwaa kombe hilo mara moja kila moja, 1966 na 1998.

Awali, nchi nyingi kutoka Ulaya na Amerika ya Kusini ndizo zilizokuwa zikishiriki kwenye fainali hizo. Lakini kukua kwa soka katika kanda zingine za Ulaya, Asia na CONCACAF kuliifanya FIFA iongeze idadi ya timu kutoka kanda hizo.

Maajabu yaliyoifanya FIFA ikubali kuongeza idadi ya timu ni pamoja na kipigo ilichokipata England kutoka kwa Marekani mwaka 1950, kipigo ilichokipata Italia kutoka kwa Korea Kusini mwaka 1966 na kufuzu kwa Cameroon kucheza robo fainali mwaka 1990.

Hivi sasa, fainali za Kombe la Dunia zimekuwa zikitazamwa na watu wengi duniani kupitia kwenye televisheni. Kwa mfano, inakadiriwa kuwa, watu bilioni 37 walitazama fainali za mwaka 1998 zilizofanyika Ufaransa, ikiwa ni pamoja na watu bilioni 1.3 waliotazama mechi ya fainali pekee wakati zaidi ya watu milioni 2.7 walifika kwenye viwanja mbalimbali kutazama mechi 64 zilizochezwa mwaka huo kwenye viwanja vya Ufaransa.

Hata hivyo, baada ya miaka yote hiyo na mabadiliko mengine, mwelekeo wa fainali hizo umebaki kuwa ni ule ule wa timu zinazoshiriki kuwania kombe la dunia, lililotengenezwa kwa madini ya dhahabu.

FIFA ilianzishwa 1904 na nchi saba










SHIRIKISHO la Soka la Dunia (FIFA) lilianzishwa Mei 21 mwaka 1904 mjini Paris, Ufaransa. FIFA ilianzishwa kwenye makao makuu ya Muungano wa Vyama vya Michezo vya Ufaransa.

Makubaliano ya kuanzishwa kwa FIFA yalitiwa saini na wawakilishi wa viongozi wa vyama vya soka vya nchi saba. Vyama hivyo ni vya Ufaransa, Ubelgiji, Denmark, Uholanzi, Hispania, Sweden na Uswisi.

Mkutano mkuu wa kwanza wa FIFA ulifanyika siku mbili baadaye, Mei 23, 1904 na kumchagua Robert Guerin wa Ufaransa kuwa raia wake wa kwanza.

Victor Schneider wa Uswisi na Carl Anton Wilhelm Hirschmann wa Uholanzi walichaguliwa kuwa makamu wawili wa rais wakati Louis Muhlinghaus aliteuliwa kuwa katibu mku na mhasibu, akisaidiwa na Ludvig Sylow wa Denmark.

Viongozi hawa walikabiliwa na kazi ngumu kwa sababu FIFA haikuwa na fedha na wala muundo wa wanachama. Changamoto yao ya kwanza ilikuwa ni kubuni muundo mzuri, uundaji wa vyama vya soka vya kitaifa ili view wawakilishi wa uhakika na upatikanaji wa wanachama wapya.

Kazi ya kwanza ya uongozi huo ilikuwa kuishawishi Uingereza kwamba, uanachama wake katika shirikisho hilo ulikuwa wa muhimu. Uingereza ilikubali ombi hilo.

Katika miaka mitano ya kwanza, wanachama wa FIFA walitoka barani Ulaya pekee hadi mwaka 1909. Wanachama wa kwanza kutoka nje ya bara hilo walikuwa Afrika Kusini, Chile na Marekani.

Afrika Kusini ilijiunga na FIFA mwaka 1910, ikifuatiwa na Argentina na Chile zilizojiunga mwaka 1912. Marekani ilijiunga na shirikisho hilo mwaka 1913. Huu ulikuwa mwanzo wa FIFA kuwa na mtazamo wa kimataifa.

Kuzuka kwa vita ya kwanza ya dunia mwaka 1914 kulizusha tafrani kubwa miongoni mwa nchi wanachama. Hata hivyo, mahusiano ya kimataifa katika nchi hizo hayakuvunjika, japokuwa yaliendeshwa kwa tabu.

Jules Rimet alikuwa rais wa tatu wa FIFA mwaka 1921. Licha ya kuzuka kwa vita ya pili ya dunia chini yake, FIFA iliongeza wanachama wake na kufika 20. Wakati huo, Uingereza iliamua kujitoa FIFA. Katika kipindi chote hicho, si Brazil ama Uruguay iliyojiunge na FIFA.

Katika kipindi cha miaka 33 ya uongozi wake, Rimet aliweza kutimiza ndoto aliyokuwa nayo kwa miaka mingi ya kuanzisha fainali za Kombe la Dunia. Na wakati FIFA ilipoandaa fainali hizo kwa mara ya tano mwaka 1954 nchini Uswisi, wanachama wa shirikisho hilo waliongezeka na kufika 85.

Uamuzi wa FIFA wa kuandaa fainali za kombe la dunia ulifikiwa katika mkutano wake mkuu wa mwaka uliofanyika nchini Ufaransa mwaka 1928. Nchi zilizotuma maombi ya kuandaa fainali hizo zilizofanyika mwaka 1930, zilikuwa Hungary, Italia, Uholanzi, Hispania, Sweden na Uruguay.

Uruguay ndiyo iliyoteuliwa kuandaa fainali hizo kwa sababu moja muhimu. Nchi hiyo, ambayo ilitwaa ushindi wa jumla wa michezo ya Olimpiki mwaka 1924 na 1928, ilikuwa ikisherehekea kutimiza miaka 100 tangu kupata uhuru wake.

Fainali hizo zilianza Julai 18 mwaka 1930 kwenye uwanja wa Cenetary wa mjini Montevideo. Miaka minne baadaye, ‘Baba wa Kombe la Dunia’, Rimet alihitimisha ndoto yake ya muda mrefu baada ya fainali hizo kufanyika Ufaransa, nchi alikozaliwa.

Fainali za nne ilikuwa zifanyike mwaka 1942. Lakini uteuzi wa mwenyeji wa fainali hizo ulichelewa kutangazwa. Ulitangazwa mwaka 1938 katika mkutano uliofanyika mjini Paris. Zikaja kufanyika mwaka 1950 wakati Brazil ilipoteuliwa kuwa mwenyeji kutokana na kuwa nchi pekee iliyotuma maombi ya kuandaa fainali hizo.

Ungereza ilirejea FIFA mwaka 1946. Kulirejea kwa Uingereza kulitokana na jitihada kubwa zilizofanywa na Rimet kwa kushirikiana na Arthur Drewry na Sir Stanley Rous.

Miaka minne baadaye, wakati wa fainali za kombe hilo zilizofanyika nchini Uswisi, Rimet wakati huo akiwa na umri wa miaka 80, aliamua kustaafu. Kwa mara ya mwisho, alikabidhi kombe la ubingwa wa dunia, wakati huo likijulikana kama ‘Kombe la Jules Rimet’ kwa nahodha wa Ujerumani.

Wakati wa uhai wake, Rimet aliteuliwa kuwa rais wa heshima wa FIFA kutokana na mchango mkubwa alioutoa kwa shirikisho hilo kabla ya kustaafu.

Rodolphe William Seeldrayers wa Ubelgiji alikuwa rais wa nne wa FIFA. Wakati wa uongozi wake, FIFA ilisherehekea kutimiza miaka 50. Wakati huo, idadi ya wanachama wake iliendelea kuongezeka na kufika 85.

Baada ya kuiongoza FIFA kwa miaka mitano na pia kuwa makamu wa rais chini ya Rimet kwa miaka 25, Seeldrayer alifariki dunia Oktoba mwaka 1955. Nafasi yake ilichukuliwa na Arthur Drewry, aliyechagulikuwa kuliongoza shirikisho hilo Juni mwaka 1956.

Kabla ya kuteuliwa kushika wadhifa huo, Arthur alikuwa mwenyekiti wa kamati iliyosimamia mabadiliko ya katiba na alikuwa msimamizi wa fainali za Kombe la Dunia za mwaka 1958 zilizofanyika Stockholm, Sweden. Arthur alifariki dunia mwaka 1961 akiwa na umri wa miaka 70.

Kufuatia kifo hicho cha Arthur, shughuli za FIFA zilikuwa chini ya Ernst B Thommen wa Uswisi hadi Septemba 1961 wakati mkutano mkuu wa shirikisho hilo ulipomchagua Sir Stanley Rous kuwa rais wake wa sita. Thommen pia alikuwa msimamizi wa fainali za mwaka 1954, 1958 na 1962.

Chini ya uongozi wa Sir Stanley, idadi ya wanachama wa FIFA iliongezeka maradufu. Pia alianzisha utaratibu wa fainali hizo kuonyeshwa moja kwa moja kupitia kwenye televisheni katika nchi mbalimbali duniani.

Ikiwa kama taasisi binafsi, FIFA haikuwa ikipata misaada yoyote kutoka kwa serikali za nchi zilizo wanachama wake ama kutoka kwingineko. Mapato yake yalitokana na fainali za Kombe la Dunia.

Dk. Joao Havelange alichaguliwa kuwa rais wa saba wa FIFA mwaka 1974. Siku hiyo hiyo, Sir Stanley alitunukiwa hadhi ya kuwa rais wa heshima wa shirikisho hilo kutokana na mchango wake.

Dk. Havelange ndiye rais pekee wa FIFA aliyekaa madarakani kwa kipindi kirefu na kufanya mabadiliko makubwa ya mfumo wa uendeshaji wa shirikisho hilo na pia muundo wake.

Kiongozi huyo anakumbukwa kutokana na jitihada zake kubwa zilizoliwezesha shirikisho hilo kuwa na mapato makubwa yatokanayo na fainali za Kombe la Dunia na pia kuwa na jengo lake la makao makuu lililopo mjini Zurich, Uswisi. Hivi sasa, FIFA ina wafanyakazi zaidi ya 120.

Dk.Havelange aliiongoza FIFA hadi Juni 8, 1998 na kumwachia kiti hicho rais wa sasa, Sepp Blatter wa Uswisi. Blatter ni rais wa nane wa FIFA.

Kabla ya uteuzi huo, Blatter aliitumikia FIFA kwa miaka 23, akiwa kwenye nyadhifa mbalimbali, ikiwa ni pamoja na katibu mkuu. Hivi sasa, FIFA inao wanachama 204.

Kwa sasa, uchaguzi mkuu wa FIFA unafanyika kila baada ya miaka minne na anachaguliwa na wajumbe kutoka nchi wanachama wa shirikisho hilo.

Friday, May 14, 2010

Yanga, Azam kubadilishana Boko na Cannavaro

KLABU ya Yanga imeutaka uongozi wa Azam uwe tayari kubadilishana wachezaji, iwapo inamtaka kwa dhati beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’.

Ofisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, klabu yake ipo tayari kumruhusu Cannavaro ajiunge na Azam, lakini kwa masharti ya kubadilishana na mshambuliaji John Boko ‘Adebayor’.

Msimamo huo wa Yanga umekuja baada ya kuwepo na taarifa kwamba, Azam inataka kumsajili Cannavaro kwa ajili ya msimu ujao wa ligi na tayari imeshafanya naye mazungumzo ya awali.

Beki huyo kutoka Zanzibar naye ameshauandikia barua uongozi wa Yanga, akiutaka umruhusu aihame klabu hiyo msimu ujao na kujiunga na Azam.

Wakati Azam ikimtaka Cannavaro, Yanga nayo imeshaeleza wazi kuwa, inataka kumsajili Boko, kufuatia mapendekezo yaliyowasilishwa kwa uongozi na Kocha Mkuu wa timu hiyo, Kostadin Papic.

“Sisi hatuna tatizo kumruhusu Cannavaro ajiunge na Azam, lakini sharti letu kubwa ni kwamba na wao waturuhusu kumsajili Boko, vinginevyo tubadilishane wachezaji,”alisema Sendeu.

Ofisa Habari huyo ameutaka uongozi wa Azam uwe tayari kukutana na wenzao wa Yanga ili kuzungumzia kwa undani usajili wa wachezaji hao wawili na kufikia mwafaka.

Katika hatua nyingine, Yanga imesema haitakuwa tayari kumruhusu mshambuliaji wake, Mrisho Ngasa ajiunge na Azam kwa malipo kidogo ya uhamisho.

Sendeu alisema jana kuwa, wamepata taarifa kwamba Ngasa amerejea nchini baada ya Azam kuahidi kumsajili kwa malipo makubwa.

Kwa mujibu wa Sendeu, Ngasa alirejea nchini juzi akitokea Rwanda, alikokwenda kufanya majaribio ya kucheza soka ya kulipwa katika klabu ya APR.

APR ilikuwa tayari kumlipa mchezaji huyo sh. milioni 20, lakini Ngasa alikataa na kutaka aliwe sh. milioni 40 na mshahara wa sh. milioni 1.5 kwa mwezi. Pande hizo mbili zilishindwa kufikia mwafaka.

“Hatuwezi kumfanyia Ngasa mtimanyongo. Tunaikaribisha klabu yoyote ije Jangwani kufanya mazungumzo ya kumnunua, lakini ijiandae kulipa dau kubwa,”alisema.

Hata hivyo, Sendeu hakuwa tayari kutaja kiwango cha fedha, ambacho Yanga inahitaji kulipwa kwa ajili ya mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Tanzania.

"Ni vyema viongozi wa Azam wakaacha kuzungumza na wachezaji wetu pembeni, klabu yetu inafahamika mahali ilipo, waje tuzungumze nao,"alisema Sendeu.

Sendeu alisema wanataka kulipwa dau kubwa kwa ajili ya uhamisho wa Ngasa kwa sababu uwezo wake ni mkubwa na ana uwezo wa kucheza soka ya kulipwa popote duniani.

Makocha wa Ilala, Temeke watambiana

MAKOCHA wa timu za mikoa ya Ilala na Temeke wametamba kuwa, watahakikisha timu zao zinafuzu kucheza fainali ya michuano ya Kombe la Taifa mwaka huu.

Makocha hao, Jamhuri Kihwelo wa Ilala na Habibu Kondo wa Temeke walitoa majigambo hayo Jumatano iliyopita mara baada ya timu zao kufuzu kucheza robo fainali ya michuano hiyo.

Ilala ilitinga robo fainali baada ya kushinda mechi zake mbili dhidi ya Mtwara na Lindi na kulazimishwa sare ya mabao 3-3 na Ruvuma katika mechi ya mwisho. Ilala ilipangwa kituo cha Mtwara.

“Tunamshukuru Mungu kwamba tumefuzu kucheza robo fainali, kilichobaki sasa ni kuhakikisha tunatoa kichapo kwa kila timu tutakayokutana nayo na kutwaa ubingwa,”alijigamba Kihwelo.

Aliwapongeza wachezaji wake kwa kucheza kwa kujituma na kuiwezesha timu hiyo kusonga mbele, licha ya kupata upinzani mkali kutoka kwa timu walizocheza nazo.

Kihwelo aliiwezesha Ilala kutwaa kombe hilo mara mbili mfululizo na mwaka huu inashiriki tema mashindano hayo kama bingwa mtetezi.

Naye Kondo alisema baada ya kutinga robo fainali, haoni kipi kitakachoikwamisha timu yake kutwaa ubingwa wa mashindano hayo.

Beki huyo wa zamani wa timu ya Sigara alisema, wasiwasi wake mkubwa ulikuwa kwenye mechi za hatua ya makundi kutokana na timu yake kutofanya maandalizi mazuri.

"Hatuiogopi timu yoyote tutakayopangwa nayo katika robo fainali, yoyote atakayekuja mbele yetu, tutahakikisha tunamchinja na kusonga mbele hadi fainali,”alisema.

Twiga Stars yapewa milioni 10/-

TIMU ya soka ya taifa ya wanawake, Twiga Stars imekabidhiwa kitita cha sh. milioni 10taslimu kutoka kwa mlezi wake, Rahma Al - Kharoosi.

Makabidhiano hayo yalifanyika jana kwenye ukumbi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), ambapo fedha hizo zilipokelewa kwa niaba ya Twiga Stars na meneja wake, Furaha Francis.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Rahma pia aliahidi kuipeleka Twiga Stars nchini Marekani iwapo itaitoa Eritrea na kufuzu kucheza fainali za michuano ya Afrika. Rahma anamiliki Kampuni ya RBP Oil & Industrial Technology (T) Limited.

Alisema kampuni yake imeguswa na kibarua kizito kinachoikabili Twiga Stars, ambayo ili iweze kufuzu kucheza fainali hizo kwa mara ya kwanza, italazimika kushinda mechi zote mbili. Fainali za michuano hiyo zimepangwa kufanyika baadaye mwaka huu nchini Afrika Kusini.

"Mabinti wa Twiga tayari wameonyesha nia ya kutaka kucheza fainali hizo, hasa ni baada ya kuwang'oa kinadada wa Ethiopia. Nikiwa mlezi wa vijana hao, nimeguswa ndio sababu nimeamua kutoa kiasi hicho cha fedha ili kiwe changamoto ya ushindi kwao," alisema.

Rahma alisema pia kuwa, kampuni yake imepokea mwaliko kutoka kwa timu ya wanawake ya Washington Freedom ya Washington DC nchini Marekani kwa ajili ya Twiga Stars kwenda huko kwa mazoezi ya wiki mbili.

Hata hivyo, alisema safari hiyo itafanyika iwapo tu Twiga Stars itaitoa Eritrea na kusonga mbele. Alizitaja timu, ambazo Twiga itacheza nazo itakapokuwa Marekani kuwa ni pamoja na wenyeji wao, Washington Freedom.

Zingine ni Seattle Woman, White Caps Woman na mechi ya mwisho watapangiwa na wenyeji wao.

Akipokea fedha hizo, Furaha alimshukuru mlezi huyo wa Twiga Stars na kuongeza kuwa, wamezipata kwa wakati mwafaka kwa vile zitawasaidia katika maandalizi yao dhidi ya Eritrea.

Pambano la awali kati ya timu hizo limepangwa kufanyika Mei 23 mwaka huu mjini Dar es Salaam na la marudiano wiki mbili baadaye mjini Asmara.

KISS KURASINI KUSAKWA LEO


SHINDANO la kumsaka mrembo wa kitongoji cha Kurasini, linatarajiwa kufanyika leo kwenye ukumbi wa Equatorial Grill, uliopo Mtoni kwa Azizi Ali mjini Dar es Salaam. Shindano hilo linatarajiwa kuwashirikisha warembo saba. Pichani, warembo hao wakiwa na mratibu wa shindano hilo, Yason Mashaka (katikati), Sam Mshana (kulia) wa Mwasu Fashion na Zuwena Mohamed, mratibu mkuu. (Na mpiga picha wetu).

Utafiti kubaini umri wa wachezaji wakamilika

MCHAKATO wa kutafiti umri sahihi wa wachezaji, unaosimamiwa na Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), umepangwa kumalizika kesho.

Akizungumza mjini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Kamati ya Tiba ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Dk. Sylvester Faya alisema, utafiti huo ulioanza mwanzoni Mei mwaka huu, uliwashirikisha wachezaji wa kike.

Alizitaja shule mbili, ambazo wachezaji wake walifanyiwa utafiti huo, wilaya zilipo zikiwa kwenye mabano ni sekondari ya Benjamini Mkapa (Ilala) na sekondari ya Kibasila (Temeke).

Dk. Faya alisema lengo la utafiti huo ni kubaini udanganyifu wa umri wa wachezaji, ambao hufanywa na viongozi klabu ama timu za vijana, hasa wa umri wa chini ya miaka 17.

"Tunakaribia kumaliza utafiti wetu wa kuhakiki umri sahihi wa wachezaji vijana kwa kutumia kipimo cha MRI, ambacho licha ya ughali wake, lakini kina uwezo mkubwa wa kung'amua umri sahihi wa mchezaji," alisema.

Akifafanua zaidi, Dk. Faya alisema FIFA imeamua kutumia kipimo hicho, kutokana na urahisi na ubora wake kwa mtumiaji ikilinganishwa na aina zingine za vipimo hivyo.

Alisema kupitia mifupa ya mwanasoka kijana na kulingana na umri wake, MRI inaweza kubaini umri sahihi bila ya kumuathiri mpimwaji hata kama atapimwa zaidi ya mara moja.

"Tunashukuru TFF kwa kutusaidia kwa namna moja au nyingine hadi kukamilika kwa mchakato wetu, ambapo Tanzania ni miongoni mwa nchi tano duniani zilizoendesha utafiti huo," alisema.

Faya amesema ni sifa kubwa kwa nchi kuteuliwa na FIFA kuwa miongoni mwa nchi zilizofanyiwa utafiti huo.

Mbali ya Dk. Faya kutoka TFF, utafiti huo pia ulimshirikisha Mjumbe wa Kamati ya Tiba ya FIFA, Yacine Zerguin, ambaye anatoka Algeria. Mbali na Tanzania, nchi zingine zilizofanya utafiti huo ni
Thailand (Asia), Brazil (Amerika Kusini), Canada (Amerika Kaskazini) na Ubelgiji (Ulaya).

Rodrigo: Kombe la Taifa limetusaidia kupata uzoefu

KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya taifa ya vijana wa chini ya miaka 20, Ngorongoro Heroes, Rodrigo Stockler amesema, mashindano ya Kombe la Taifa yamewasaidia vijana wake kuongeza uzoefu.

Rodrigo alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, ushiriki wao katika mashindano hayo utawaweka katika mazingira mazuri zaidi ya kukabiliana na Ivory Coast.

Ngorongoro ilialikwa kushiriki kwenye mashindano ya Kombe la Taifa mwaka huu kwa lengo la kuipa mazoezi, lakini imeshindwa kusonga mbele baada ya kutolewa hatua ya makundi.

Vijana hao walimaliza mechi za kituo cha Dodoma wakiwa nafasi ya tatu baada ya kuambulia pointi mbili, kufuatia kutoka sare na timu za mikoa ya Kigoma na Singida na kufungwa na Dodoma.

Kwa sasa, Ngorongoro inajiandaa kumenyana na Ivory Coast katika mechi ya raundi ya pili ya michuano ya kuwania ubingwa wa Afrika. Ilifuzu kucheza hatua hiyo baada ya kuitoa Malawi kwa jumla ya mabao 5-3.

“Haya mashindano yametusaidia sana, wachezaji wangu hawajaonyesha kwamba wao ni wadogo, walijitahidi kwenda sambamba na wachezaji wa mikoa mingine, ambao ni wakubwa kiumri na wazoefu wa michuano mbalimbali,”alisema Rodrigo.

Kocha huyo kutoka Brazil alisema mechi tatu walizocheza katika mashindano hayo zimewaongezea mbinu mbalimbali vijana wake, ambazo zitawasaidie kukabiliana na Ivory Coast.

Alisema tatizo kubwa lililokuwa likiwasumbua vijana wake ni ubovu wa Uwanja wa Jamhuri na uamuzi mbaya wa waamuzi waliochezesha mechi za kituo hicho.

Rodrigo aliwashutumu waamuzi hao kwa kushindwa kuwalinda vijana wake, ambao ni wadogo kiumri na kuruhusu wachezewe rafu zisizokuwa na ulazima.

Kocha huyo ameamua kuwapumzisha wachezaji wake hadi Julai Mosi mwaka huu watakapoingia kambini kujiandaa kwa pambano lao dhidi ya Ivory Coast.

Ngorongoro na Ivory Coast zinatarajiwa kucheza mechi ya kwanza kati ya Julai 24 na 25 mjini Abidjan na kurudiana kati ya Agosti 7 na 8 mwaka huu mjini Dar es Salaam.

England yataka uenyeji Kombe la Dunia 2018



ZURICH, Uswisi

MWANASOKA wa kimataifa wa England, David Beckham amekabidhi kitabu chenye kurasa 1,752, ambacho anaamini kitalishawishi Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA), kuizawadia England uenyeji wa fainali za Kombe la Dunia mwaka 2018.

Mwenyeji wa fainali hizo mwaka 2018 na 2022 anatarajiwa kutangazwa Desemba 2 mwaka huu.

Mbali na England, nchi nyingine zilizowasilisha maombi ya kuandaa fainali hizo ni Russia na Australia.

“Tuna furaha kubwa; soka ni kitu ambacho kinapita akilini mwetu,”alisema Beckham, ambaye alikabidhi kitabu hicho kwa Rais wa FIFA, Sepp Blatter jana mjini hapa.

Mara baada ya kupokea kitabu hicho, Blatter alidokeza kuwa, alipokea simu kutoka kwa Waziri Mkuu mpya wa Uingereza, David Cameron.

Nchi tisa, zikiwemo Uholanzi na Ubelgiji, zilizoomba kuandaa fainali hizo kwa pamoja, nazo ziliwasilisha maombi yao kwa Blatter jana asubuhi.

Ujumbe wa England ulitambulishwa na Blatter kama unaowakilisha ‘Mama wa soka’.

Beckham aliungana stejini na Makamu wa Pili wa Rais wa FIFA, Geoff Thompson, Msimamizi mkuu wa maombi ya England katika fainali hizo, Andy Anson na Mwenyekiti wa Chama cha Soka cha England, Lord Trieman, ambaye alimthibitishia Blatter kwamba, England pia ingependa kufikiriwa kuandaa fainali za mwaka 2022.

Katika hotuba yake fupi, Beckham alisema England ina kiu kubwa ya kuandaa fainali hizo kwa sababu soka ina mvuto mkubwa katika nchi hiyo na imejikita akilini mwao.

“Kila timu (itakayoshiriki fainali hizo), itakuwa katika mji wake na kuwa pamoja na mashabiki wake,”alisema Beckham.

Blatter aliushukuru ujumbe wa England kwa kuunga mkono mchezo wa soka, ambao umepata umaarufu mkubwa duniani kabla ya kudokeza kile alichozungumza na Cameron.

“Si tu kwamba alieleza kuunga kwake mkono maombi haya, lakini pia fainali za Kombe la Dunia za mwaka 2010 zitakazofanyika Afrika Kusini,”alisema.

FIFA inatarajia kupata pauni bilioni 2.1 kutokana na matangazo ya televisheni na udhamini katika fainali za Kombe la Dunia za mwaka 2010 wakati England inakadiria kuongeza mapato hayo kwa robo tatu, kufikia pauni bilioni tatu.


MCHEZAJI Alphonce Donald (mbele) wa Shinyanga akimdhibiti John Boscow wa Mwanza Heroes timu hizo zilipomenyana juzi katika mechi ya mashindano ya Kombe la Taifa iliyochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza. Wenyeji Mwanza walishinda mabao 2-1.(Picha na Executive Solutions)

Makocha wapya Taifa Stars wafanyiwa usaili kwa siri

MAKOCHA watano waliopitishwa kuwania nafasi ya kuinoa timu ya soka ya Taifa, Taifa Stars wamewasili nchini kwa ajili ya kufanyiwa usaili.

Habari zilizonaswa na Burudani jana zimeeleza kuwa, makocha hao waliwasili nchini juzi tayari kwa ajili ya kufanyiwa usaili huo kabla ya kuteuliwa kocha atakayerithi mikoba ya kocha wa sasa, Marcio Maximo.

Usaili wa makocha hao ulianza kufanyika juzi katika hoteli ya New Africa, chini ya usimamizi wa viongozi wa sekretariati ya Shirikikisho la Soka Tanzania (TFF), ikiongozwa na Mkurugenzi wa Ufundi,
Sunday Kayuni.

Makocha waliofanyiwa usaili huo wanatoka katika nchi za Bulgaria, Serbia, Denmark, Poland na Ureno.

Juhudi za gazeti hili kupata majina ya makocha hao zilishindwa kufanikiwa kwa vile usaili huo ulifanyika kwa siri kubwa na chini ya ulinzi na haikuruhusiwa kwa waandishi wa habari kuingia kwenye ukumbi wa hoteli hiyo.

Hata hivyo, habari kutoka ndani ya TFF zimeeleza kuwa, makocha hao watafanyiwa usaili kwa muda wa siku tatu kabla ya kutangazwa kwa mshindi.

Chanzo chetu cha habari kilidokeza kuwa, usaili wa makocha hao umefanywa kuwa siri kubwa ili kuepuka kuvuja kwa majina yao kabla ya kuchaguliwa mmoja wao, atakayefaulu usaili huo.

Imeelezwa kuwa, mara baada ya usaili huo, jina la kocha atakayepitishwa litatangazwa kwa ajili ya kuchukua nafasi ya Maximo, ambaye anamaliza mkataba wake Julai 28 mwaka huu.

Katika hatua nyingine, timu ya soka ya taifa ya wanawake, Twiga Stars inatarajiwa kuingia kambini leo kujiandaa kwa pambano lake dhidi ya Eritrea.

Katibu Mkuu wa TFF, Fredrick Mwakalebela alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, Twiga Stars itaweka kambi kwenye hoteli ya FNG Annex iliyopo Msasani.

Twiga Stars inatarajiwa kuvaana na Eritrea katika pambano la awali la raundi ya pili ya michuano ya Afrika, litakalochezwa Mei 22 mwaka huu mjini Dar es Salaam kabla ya kurudiana wiki mbili baadaye mjini Asmara.

Giggs: Hatupaswi kumtegemea Rooney pekee



LONDON, England

MSHAMBULIAJI mkongwe wa klabu ya Manchester United, Ryan Giggs amekiri kuwa, timu hiyo imeshindwa kutwaa taji la ligi kuu ya England msimu huu kwa sababu ya kumtegemea zaidi Wayne Rooney.

Giggs ni mchezaji anayeheshimika katika historia ya Manchester United, akiwa ameshinda mataji 11 ya ligi kuu ya England katika kipindi cha miongo miwili alichoichezea klabu hiyo, hivyo anapozungumza, watu humsikiliza.

Mshambuliaji huyo raia wa Wales alikiri kuwa, wachezaji wa Manchester United hawakutaka kutoka nje ya vyumba vya kubadili mavazi wakati wa mapumziko ya mechi yao dhidi ya Stoke City mwishoni mwa wiki iliyopita baada ya kubaini kuwa, Chelsea ilikuwa mbele kwa mabao 2-0 dhidi ya Wigan na kuelekea kutwaa ubingwa.

Lakini saa 24 baada ya Chelsea kutwaa taji hilo, Giggs alielezea kile kilichosababisha vijana wa Kocha Sir Alex Ferguson washindwe kung’ara msimu huu.

“Kama ulipaswa kusema kitu kimoja, pengine ungesema hatupaswi kumtegemea zaidi Rooney msimu ujao kama tulivyofanya msimu huu,”alisema Giggs.

“Tunahitaji kufunga mabao mengi zaidi kutoka maeneo tofauti na kutoka kwa wachezaji tofauti, japokuwa kama timu, tulifunga mabao mengi zaidi kuliko msimu uliopita,”aliongeza.

Giggs alisema safu ya ulinzi ya timu hiyo pia ilikuwa bora zaidi msimu huu kuliko msimu uliopita, lakini hawapaswi kumtegemea zaidi Rooney katika ufungaji mabao kama ilivyokuwa msimu huu.

Alisema katika mechi yao dhidi ya Stoke City, walianza kwa matumaini, lakini wakati wa mapumziko, walibaini kwamba Chelsea ilikuwa mbele kwa mabao 2-0 na Wigan ilisaliwa na wachezaji 10 uwanjani.

“Tulielewa kwamba huo ulikuwa mwisho na kuwa wazi, hatukutaka kurejea uwanjani kwa ajili ya kipindi cha pili. Katika hali kama hiyo, unatamani kwenda nyumbani,”alisema.

Rooney ameifungia Manchester United mabao 34 msimu huu na kuumia kwake katika mechi ya awali ya robo fainali ya ligi ya mabingwa wa Ulaya dhidi ya Bayern Munich ya Ujerumani kuliashiria mwisho wa vijana hao wa Ferguson.

Baada ya hapo, Rooney hakuweza kufunga bao na Manchester United ikapoteza mwelekeo. Giggs anakiri kuwa, lilikuwa pigo kubwa kwa vijana wa Ferguson, ambao kamwe hawakuweza kuzinduka.

“Ilikuwa bahati nzuri kwetu kwamba Rooney aliumia katika kipindi muhimu cha msimu kwa sababu tungeendelea kutegemea magoli zaidi kutoka kwake na tusingeyapata,”alisema.

Giggs alisema hata kama kocha alisajili ama hakusajili washambuliaji wengine msimu huu, wachezaji walielewa kwamba walihitajika kufunga mabao zaidi.

“Hata kama mabeki walipanda mbele wakati wa kona au viungo walishambulia, sote tulihitajika kuchangia ushindi,”alisema.

Katika ligi ya msimu huu, Manchester United ilipata vipigo kutoka kwa Burnley, Aston Villa, Liverpool, Everton na Fulham, lakini Giggs amevitaja vipigo viwili kutoka kwa Chelsea kuwa ndivyo vilivyoamua mshindi wa ligi.

“Unaweza kusema tulipoteza mwelekeo kutokana na vipigo hivyo viwili kutoka kwa Chelsea. Kama tungetoka sare katika mchezo mmoja, tungeweza kutwaa ubingwa,”alisema.

Giggs alisema siku zote timu inapopoteza mechi mbili dhidi ya wapinzani wao wakubwa, hali inakuwa ngumu. Alisema siyo siku zote mechi hizo huamua mshindi, lakini ndivyo ilivyokuwa msimu huu.

“Na ukitazama ukweli kwamba Chelsea walitufunga sisi, Arsenal na Liverpool, nyumbani na ugenini, unapaswa kusema kuwa walistahili kutwaa ubingwa,”alisema.

Giggs alisema walivunjika nguvu kutokana na kupoteza baadhi ya pointi kwa sababu walipaswa kushinda mechi hizo na ingekuwa rahisi kwao kutwaa ubingwa msimu huu.

Pamoja na kuukosa ubingwa, Giggs alisema Manchester United inapaswa kupongezwa kwa vile imezidiwa kwa pointi moja na mabingwa wapya, Chelsea.

“Hakuna timu iliyoweza kufanya jambo hilo, hivyo wachezaji wanastahili pongezi kwa jitihada hizo. Lakini hivyo sivyo ilivyopaswa kuwa,”alisema.

Giggs (36), ambaye anatarajiwa kumaliza mkataba wa kuichezea Manchester United mwaka 2011, kabla ya kutundika daruga ukutani alisema, machungu ya kupoteza ubingwa msimu huu yataisaidia klabu hiyo katika mipango yake ya baadaye.

Alisema akiwa na umri wa miaka 17, walipoteza ubingwa kwa Leeds msimu wa 1991-92, tukio ambalo lilimwezesha kupata uzoefu na kuwa mchezaji wa kutumainiwa na Manchester United.

“Wachezaji hawa chipukizi, ambao hawaelewi lolote zaidi ya kushinda mataji katika kipindi cha misimu mitatu iliyopita, sasa watakabiliwa na changamoto niliyokutana nayo msimu wangu wa kwanza Manchester United,”alisema Giggs.

“Tulikaribia sana kutwaa ubingwa, lakini tuliupoteza kwa Leeds na hilo linakatisha tamaa kwa sababu, hisia za kushindwa kamwe hazitatoka kichwani mwako kwa msimu mzima,”aliongeza.

“Unapaswa kuhakikisha unakuja kwa nguvu na ukiwa mwenye kiu kubwa ya ubingwa msimu unaofuata, na hiyo ni alama ya timu bora na wachezaji wazuri,”alisema.

Giggs alisema kupoteza ubingwa kwa Leeds kulimsaidia kwa sababu hakutaka hisia hizo zimjie tena msimu uliofuata.

“Ushindi huleta hisia za ajabu, lakini hazidumu kwa muda mefu. Hisia za kufungwa zinadumu kwa muda mrefu na zinaumiza,”alisema.

Mshambuliaji huyo alisema ni rahisi kwa mchezaji kukabiliana na hisia za aina hiyo anapokuwa mtu mzima, lakini zinauma. Alisema mara nyingi wamekuwa wakijitahidi kuzisahau wanapokwenda mapumziko na familia zao.

Giggs alisema ana hakika kushindwa kwa timu yake kutwaa taji hilo msimu huu na kwa jinsi wachezaji walivyoonekana kukata tamaa, ana hakika watakuja na nguvu mpya msimu ujao.

“Kocha ametutaka tufurahie mapumziko yetu, iwe kwenye mapumziko maalumu ama kwenye fainali za Kombe la Dunia na kurejea msimu ujao tukiwa na nguvu mpya,”alisema.

“Tutakuwa tayari msimu ujao. Kocha ametutaka tukumbuke hisia za kupoteza ubingwa na kuhakikisha hatutarudia kosa hilo msimu ujao,”alisema.

Okwi, Naftali nje Kagame

KIKOSI cha timu ya soka ya Simba kinatarajiwa kuondoka nchini leo kwenda Rwanda kushiriki katika michuano ya Kombe la Kagame huku wachezaji Emmanuel Okwi na David Naftali wakiachwa katika safari hiyo.

Mbali ya wachezaji hao kuachwa, timu hiyo inakabiliwa na majeruhi wawili, ambao ni washambuliaji Uhuru Selemani na Ramadhani Chombo.

Akizungumza mjini Dar es Salaam jana, Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Phiri alisema, licha ya kuwa majeruhi, Uhuru na Chombo wataambatana na timu hiyo nchini Rwanda.

Phiri alisema timu yake imeajiandaa vizuri kwa ajili ya mashindano hayo licha ya kupangwa kwenye kundi gumu. Simba imepangwa kundi moja na timu za Sofapaka ya Kenya, URA ya Uganda na Atraco ya Rwanda.

Kocha huyo raia wa Zambia alisema, kikosi chake kinakwenda kwenye mashindano hayo kikiwa na dhamira ya kupigana kufa au kupona ili kitwae ushindi.

Phiri alikiri ushiriki wa timu yake katika mashindano ya Kombe la Shirikisho, umeipa maandalizi mazuri kwa ajili ya michuano hiyo, inayotarajiwa kuanza keshokutwa, ikizishirikisha timu bingwa kutoka nchi za mataifa ya ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

"Kwa kweli tumejipanga vizuri na tunatarajia kufanya vizuri katika mashindano hayo, japokuwa mwaka huu yatakuwa magumu kuliko ilivyokuwa miaka iliyopita," alisema Phiri.

Katibu Mkuu wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Nicholaus Musonye, alisema maandalizi yote muhimu kwa ajili ya mashindano hayo yamekamilika.

Musonye alisema timu shiriki zimeshaanza kuwasili nchini Rwanda kwa ajili ya mashindano hayo, zikiwemo timu za Heart Land ya Nigeria na TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, ambazo zitakuwa waalikwa.

Timu zingine zinazotarajiwa kushiriki michuano hiyo, nchi zinazotoka zikiwa kwenye mabano ni Sofapaka (Kenya), Mafunzo (Zanzibar), URA (Uganda), Vital’ O (Burundi), St. George (Ethiopia), Telecom (Somalia), Atraco na APR za Rwanda.

Manji amvuruga Papic




HALI imeendelea kuwa si shwari ndani ya klabu ya Yanga baada ya kuzuka tena tafrani kubwa kati ya mfadhili mkuu wa klabu hiyo, Yussuf Manji na Kocha Mkuu, Kostadin Papic.

Habari za uhakika kutoka ndani ya Yanga zimeeleza kuwa, Papic sasa amefikia uamuzi wa kufungasha virago kurejea kwao Serbia huku akiapa kwamba hatarejea tena katika klabu hiyo.

Chanzo cha habari kutoka ndani ya klabu hiyo kimeeleza kuwa, Papic amekerwa na tabia ya Manji kuwa kigeugeu katika masuala yanayohusu usajili wa wachezaji kwa ajili ya msimu ujao wa ligi.

Kwa mujibu wa chanzo hicho, Manji amekubali kutoa fedha za usajili kwa wachezaji wote wazalendo, lakini amekataa kufanya hivyo kwa wachezaji wa kigeni waliotafutwa na Papic.

“Imefika hatua sasa Papic haelewi nini la kufanya kwa sababu Manji ndiye aliyemwambia atafuta wachezaji na kumpelekea ripoti, lakini ameikataa,” alisema mtoa habari wetu.

“Wachezaji wote wazalendo ameshawasainisha mikataba mipya na kuwalipa haki zao na wengine amewaongeza mishahara, lakini ajabu ni kwamba ameyakataa majina yote ya wachezaji wa kigeni yaliyopendekezwa na Papic,” aliongeza.

Chanzo hicho cha habari kiliongeza kuwa, Manji amemtaka Papic ayapeleke majina ya wachezaji hao wa kigeni kwa uongozi wa Yanga ili watafute fedha za kuwasajili.

Uchunguzi zaidi umebainisha kuwa, viongozi wa Yanga nao wapo njia panda kwa vile hawaelewi lengo la mfadhili huyo kwa vile kauli zake zimekuwa zikiwachanganya.

“Kwa kweli hata sisi sasa hatumuelewi na hatujui tufanye nini kwa sababu amekuwa akitoa kauli tofauti kwa Papic,” alisema kiongozi mmoja wa Yanga, ambaye hakupenda jina lake litajwe gazetini.

“Kama hataki kuendelea kuifadhili Yanga ni bora aweke mambo wazi kwa wanachama kuliko kuendelea kutuweka njia panda. Hivi anavyofanya, anatuchanganya,” aliongeza.

“Kama ni kocha, yeye ndiye aliyemtafuta na kuingia naye mkataba, sasa iweje hawaelewani? Hapa kuna kitu kinajificha, tunamuomba Manji aweke mambo hadharani,” alisema kiongozi huyo.

Kiongozi huyo alisema hawaelewi kwa nini Manji alimtaka Papic awapelekee orodha ya usajili wa wachezaji viongozi wa klabu hiyo wakati ambapo sio wanaotoa fedha hizo.

“Kwa hali ilivyo, Papic anaweza kuondoka nchini wakati wowote na ameshaanza kuwaaga watu wake wa karibu kwa kuwaeleza kwamba, huenda asirudi tena nchini,”alisema.

Kwa mujibu wa kiongozi huyo, upo uwezekano mkubwa kikao cha kamati kuu ya Yanga kilichopangwa kufanyika leo kikaahirishwa kutokana na viongozi wengi kutokuwepo Dar es Salaam.

“Hivi ninavyozungumza na wewe, Mwenyekiti (Iman) Madega yupo Dodoma kwa shughuli zake binafsi, (Emmanuel) Mpangala amefiwa kwao Mbeya na (Patrick) Fatah hatakuwepo,”alisema.

Kikao hicho kilipanga kujadili mambo mbalimbali yanayoihusu Yanga, ikiwa ni pamoja na marekebisho ya katiba na tarehe za kuitishwa kwa mkutano mkuu wa wanachama na uchaguzi wa viongozi wapya.

TENGA: RAGE NI MPIGANAJI

SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limempongeza Mwenyekiti mpya wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage kwa kumuelezea kuwa ni mpiganaji halisi katika masuala yanayohusu michezo.

Rais wa TFF, Leodegar Tenga aliwaambia waandishi wa habari mjini Dar es Salaam jana kuwa, Rage ni mmoja wa wadau, ambaye amepigana kwa hali na mali kulinda na kutetea katiba ya Simba, TFF na Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA).

“Kwa kweli nawapongeza wadau wa klabu ya Simba na hasa Rage, aliyechaguliwa kuwa mwenyekiti,”alisema Tenga.

Alisema kimsingi katiba zote zinapinga kitendo cha mgombea kupeleka suala la michezo kwenye mahakama za kawaida na kusisitiza kuwa, kufanya hivyo ni kosa kikatiba.

Tenga alisema inapotokea migogoro ya aina hiyo, muhusika anapaswa kufuata taratibu zilizowekwa kikatiba katika kutafuta haki yake badala ya kukimbilia mahakamani.

"Tayari soka yetu imekuwa ikikua kila kukicha na tulishaanza kusahau masuala ya watu kwenda mahakamani, lakini nashakuru kwa wadau ambao wameongozwa na Rage kuhakikisha wamesimamia matakwa ya katiba na uchaguzi umefanyika kama ilivyopangwa," alisema.

Rais huyo wa TFF alisema kitendo cha baadhi ya wanachama wa Simba kwenda mahakamani kuzuia kufanyika kwa uchaguzi huo, kungeiweka Simba kwenye hatari ya kufungiwa na FIFA.

Alisema kufanyika kwa uchaguzi wa Simba, siyo mafanikio pekee ya klabu hiyo bali soka ya Tanzania kwa ujumla.

"Maamuzi ya kufanyika kwa uchahuzi wa Simba yalitolewa usiku wa Ijumaa iliyopita, binafsi sikutarajia wanachama 1,500 wangejitokeza kwenda kupiga kura," alisema.

Ametoa wito kwa wanachama wa klabu zingine, kuiga mfano wa Simba na kuchagua viongozi wenye uwezo mkubwa wa kutafsiri na kutekeleza katiba zao kama alivyofanya Rage.

Katika uchaguzi huo uliofanyika Jumapili iliyopita, Rage alichaguliwa kuwa mwenyekiti baada ya kumshinda Hassan Othman Hassanoo. Uchaguzi huo ulifanyika kwenye ukumbi wa Bwalo la Maofisa wa Polisi Oysterbay, Dar es Salaam.

Papic: Ngasa APR si saizi yako

KOCHA Mkuu wa Yanga, Kostadin Papic amesema timu ya APR ya Rwanda haimfai Mrisho Ngasa kwa sababu kiwango chake hakina tofauti na timu za Tanzania.

Papic alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, Ngasa anapaswa kwenda kucheza soka ya kulipwa katika klabu zenye kiwango cha juu zaidi.

Kocha huyo alitoa kauli hiyo baada ya kuwepo na taarifa kwamba, Ngasa amekwenda Rwanda kufanya majaribio ya kuichezea APR.

Kuna habari kuwa, APR ilitaka kumsajili Ngasa kwa kitita cha sh. milioni 20, lakini mchezaji huyo aligoma na kutaka alipwe sh. milioni 35.

Papic alisema kama Ngasa ana kiu ya kwenda nje kucheza soka ya kulipwa, ni vyema aende katika klabu kubwa kama za Afrika Kusini na za Ulaya.

"Pale Rwanda sifahamu vizuri soka yao, lakini kwa ushauri wangu, naona ni vyema mchezaji huyo angefanya mipango ya kwenda Afrika Kusini au Ulaya,"alisema kocha huyo, ambaye ni raia wa Serbia.

Katika hatua nyingine, uongozi wa klabu ya Azam umesema kuwa, hauna mpango wa kumsajili mshambuliaji Mrisho Ngasa kutoka Yanga.

Mmoja wa viongozi wa Azam, Mohamed King alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, watasajili washambuliaji wapya kutoka klabu zingine na siyo Yanga.

King alisema hawajawahi kufanya mazungumzo na Ngasa kwa ajili ya kumsajili msimu ujao na kuongeza kuwa, taarifa hizo wamekuwa wakizisoma kupitia kwenye vyombo vya habari.

Hata hivyo, kiongozi huyo wa Azam alikiri kuwa, wamefanya mazungumzo ya awali na beki Nadir Haroub ‘Canavaro’ wa Yanga kwa ajili ya kumsajili msimu ujao.

"Ninachoweza kukuhakikishia ni kwamba, ni kweli tumefanya mazungumzo na Canavaro, lakini kwa upande wa Ngasa, hilo jambo halipo,"alisema King.

Tayari uongozi wa Yanga umekaririwa ukisema kuwa, milango ipo wazi kwa Canavaro kujiunga na Azam, lakini anapaswa kufuata taratibu za usajili.

Rooney atoa changamoto kwa Ferguson



LONDON, England

MSHAMBULIAJI Wayne Rooney wa Manchester United amesema anaamini, klabu hiyo inahitaji wachezaji wawili zaidi wa kiwango cha juu katika ligi ya msimu ujao.

Rooney alisema mjini hapa juzi kuwa, mmoja wa wachezaji hao anapaswa kuwa mshambuliaji, ili kukiongezea nguvu kikosi hicho baada ya kupokonywa taji la ligi kuu ya England msimu huu na Chelsea.

Mshambuliaji huyo ameonyesha kiwango cha juu msimu huu, ambapo ameifungia Manchester United mabao 34.

Hata hivyo, Rooney alipatwa na mkosi mwishoni mwa ligi hiyo baada ya kuumia kifundo cha mguu na kukaa benchi kwenye mechi kadhaa.

Rooney ndiye aliyekuwa tegemeo kubwa la Manchester United katika ufungaji magoli msimu huu, kufuatia kuondoka kwa Cristiano Ronaldo na Carlos Tevez msimu uliopita.

Licha ya Manchester United kushika nafasi ya pili msimu huu, nyuma ya Chelsea kwa tofauti ya pointi moja, Rooney alisema bado kuna umuhimu wa Kocha Sir Alex Ferguson kuongeza nyota wawili msimu ujao.

“Kama tutaweza kuongeza wachezaji wawili wenye majina makubwa, itatupa nafasi kubwa ya kurejesha taji la ligi kuu,”alisema Rooney.

“Kama utatazama timu ya mwaka 1999 iliyoshinda mataji matatu, tulikuwa na washambuliaji wanne na wote walikuwa na uwezo wa kufunga mabao,”aliongeza.

“Kwa sasa nipo mimi, Berbatov na Owen. Yupo pia Macheda, lakini kama tunaweza kumpata mwingine zaidi, itatuongezea nguvu zaidi,”alisema.

Mbali na Rooney, wachezaji wengine wanaounda safu ya ushambuliaji ya Manchester United kwa sasa ni Dimitar Berbatov, Michael Owen na chipukizi Federico Macheda na Mame Biram Diouf.

Mourinho aikana Real Madrid



MILAN, Italia

KOCHA Mkuu wa Inter Milan ya Italia, Jose Mourinho amekanusha madai kuwa, amekuwa akifanya mazungumzo kwa ajili ya kuwa kocha mkuu wa Real Madrid ya Hispania msimu ujao.

Mourinho alisema mjini hapa juzi kuwa, kwa sasa hana mpango huo na kusisitiza kuwa, ameelekeza nguvu zake katika kukabiliana na changamoto zote zinazoikabili Inter Milan.

Inter Milan inachuana vikali na AS Roma katika kuwania taji la ligi ya Serie A ya Italia na inatarajiwa kuteremka dimbani keshokutwa kumenyana na Siena. Mechi hiyo ndiyo itakayoamua bingwa wa ligi hiyo.

Mbali na kibarua hicho, Inter Milan pia inakabiliwa na mtihani mwingine mgumu wa kupambana na Bayern Munich ya Ujerumani katika mechi ya fainali ya ligi ya mabingwa wa Ulaya, itakayocheza Mei 22 mwaka huu.

“Sijafanya mazungumzo na klabu nyingine yoyote, na kama ilivyo kwa mashabiki wote wa Inter Milan, nafikiria mechi zetu mbili muhimu dhidi ya Siena na Bayern Munich,”alisema kocha huyo, ambaye amebatizwa jina la ‘Special One’.

“Hizi ni siku za ajabu, tumeelekeza akili na nguvu zetu katika mechi hizi mbili na hakuna yeyote ndani ya Inter Milan, anayefikiria kuhusu nini watakachokifanya baada ya mechi ya fainali ya ligi ya mabingwa. Huo ndio ukweli wenyewe,”aliongeza.

Mourinho alisema ameshamweleza wakala wake, Jorge Mendez kwamba hatajadili suala hilo hadi Mei 23 baada ya mechi ya fainali ya ligi ya mabingwa.

Hata hivyo, Mourinho alikiri kwamba bado ana mambo muhimu ya kufanya katika soka na kuongeza kuwa, moja ya mipango yake ya baadaye ni kufundisha kabumbu nchini Hispania ama kuwa kocha wa timu ya taifa ya Ureno.

“Lakini hayo nitaweza kuyafanya nitakapokuwa mtu mzima zaidi, inawezekana katika miaka 15 ama 20 ijayo,”alisema.

Alipoulizwa iwapo siku moja angependa kuwa kocha wa mshambuliaji Cristiano Ronaldo wa Real Madrid, kocha huyo alisema: “Vema, Nimesema nataka kuwa kocha wa Ureno katika kipindi cha miaka 15 au 20 ijayo.”

Mapema wiki hii, Rais wa Inter Milan, Massimo Moratti alitoa taarifa kwa vyombo vya habari ikikanusha madai kuwa, anamsaka mrithi wa Mourinho.

Drogba amtamani Torres


Drogba

LONDON, England

MSHAMBULIAJI Didier Drogba wa Chelsea amesema anamkaribisha kwa mikono miwili Fernando Torres wa Liverpool iwapo atasajiliwa na klabu yake.

Kauli hiyo ya Drogba imekuja siku chache baada ya kuwepo na taarifa kwamba, Chelsea imetenga pauni milioni 70 za Uingereza (sh. bilioni 140) kwa ajili ya kumsajili Torres.

Gazeti la Daily Mail la Uingereza liliripoti wiki iliyopita kuwa, mmiliki wa Chelsea, Roman Abramovich amepania kuvunja rekodi ya uhamisho wa wachezaji katika ligi kuu ya England kwa kusajili kifaa kipya kwa bei kali.

Kwa sasa, rekodi hiyo inashikiliwa na beki Rio Ferdinand, aliyesajiliwa na Manchester United kwa uhamisho wa pauni milioni 29.1 kutoka klabu ya Leeds miaka minane iliyopita.

Mtendaji Mkuu wa Chelsea, Ron Gourlay alithibitisha mapema wiki hii kuwa, Kocha Carlo Ancelotti atapatiwa fedha anazotaka ili kusajili mchezaji mmoja au wawili na kwamba lengo lao kubwa ni kumnasa Torres.

Akizungumza mjini hapa juzi usiku, Drogba alisema atakuwa na furaha kubwa iwapo Torres ataungana naye katika safu ya ushambuliaji ya Chelsea.

Alisema kujiunga kwa Torres kutaifanya safu ya ushambuliaji ya Chelsea iwe tishio kwa mabeki wa klabu za timu pinzani kokote duniani.

“Bila shaka nitamkaribisha Torres kwa mikono miwili,”alisema Drogba, ambaye ameibuka kuwa mfungaji bora wa ligi kuu ya England baada ya kupachika wavuni mabao 36 msimu huu.

“Kila wakati mchezaji mpya anakuja hapa, hilo linaifanya klabu iwe kubwa zaidi na kutuongezea nguvu,” alisema Drogba.

“Kama kuna nafasi ya yeye kuja hapa, anakaribishwa kwa sababu msaada wowote unahitajika,”aliongeza.

Mbali na Chelsea, klabu nyingine iliyoonyesha dhamira ya kumsajili Torres ni Manchester City, ambayo ipo tayari kutoa dau lolote ili kumnasa mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Hispania.

Torres (26) ameonyesha nia ya kutaka kuihama Liverpool baada ya kushindwa kutwaa taji lolote tangu alipojiunga na klabu hiyo miaka mitatu iliyopita.