KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 6, 2010

NI VITA YA CHELSEA NA MAN UTD

SIR Alex Ferguson

CARLO Ancelotti

Ancelloti atamba hakuna wa kuwazuia kutwaa ubingwa
Ferguson mambo mazito, ategemea mbeleko ya Wigan
Newcastle, West Bromwich zafuzu kucheza ligi kuu
LONDON, England
UNAWEZA kuielezea ligi kuu ya soka ya England msimu huu kuwa ni yenye ushindani mkali na wa aina yake kuliko ligi zilizopita kutokana na ukweli kwamba bingwa atajulikana siku ya mechi za mwisho zitakazochezwa Jumapili.
Kitendawili juu ya timu ipi itakuwa bingwa kimekuwa kigumu kuteguliwa, kufuatia vinara wa ligi hiyo, Chelsea na Manchester United kushinda mechi zake za mwishoni mwa wiki iliyopita.
Katika mechi hizo, Chelsea iliichapa Liverpool mabao 2-0 wakati mabingwa watetezi, Manchester United waliilaza Sunderland bao 1-0.
Matokeo hayo yaliiwezesha Chelsea kuendelea kuongoza ligi hiyo kwa tofauti ya pointi moja kati yake na Manchester United, inayoshika nafasi ya pili.
Chelsea inaongoza kwa kuwa na pointi 83 baada ya kucheza mechi 37, ikifuatiwa na Manchester United yenye pointi 82 kutokana na idadi hiyo ya michezo. Arsenal ni ya tatu kwa kuwa na pointi 72 baada ya kucheza mechi 36.
Je, ni timu ipi itakayovikwa taji la ligi hiyo msimu huu? Swali hilo ndilo lililotawala kwenye vichwa vya mashabiki wa soka nchini England.
Matokeo ya mechi za Jumapili ndiyo yatakayojibu swali hilo. Katika mechi hizo, Chelsea itamenyana na Wigan kwenye uwanja wa Stamford Bridge wakati Manchester United itavaana na Stoke City kwenye uwanja wa Old Trafford.
Hata hivyo, wachambuzi wa masuala ya soka wanaipa Chelsea nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa kutokana na kuwa na idadi kubwa ya magoli ya kufunga. Hii ina maana kwamba, hata kama Chelsea itatoka sare na Wigan na Manchester United kuishinda Stoke City, inaweza kuwa bingwa kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa.
Hadi sasa, Chelsea imefunga mabao 95 na kufungwa 32 wakati Manchester United imefunga mabao 82 na kufungwa 28.
Lakini iwapo Chelsea itafungwa na Wigan na Manchester United kuibwaga Stoke City, taji la ligi hiyo litarejea tena kwa Mashetani Wekundu, ambao wataweka rekodi ya kulitwaa kwa mara ya tatu mfululizo.
Chelsea itaingia uwanjani Jumapili huku ikiwa na kumbukumbu ya kichapo cha mabao 3-1 ilichokipata kutoka kwa Wigan katika mechi ya mzunguko wa kwanza.
Lakini wachambuzi wa soka wanaamini kuwa, kutokana na makali ya Chelsea hivi sasa, si rahisi kwa Wigan kuhimili vishindo vya vijana hao wa mfanyabiashara bilionea, Roman Abramovich.
Wachambuzi hao wamesema, pambano hilo lingekuwa gumu kutabirika iwapo Wigan ingekuwa kwenye janga la kushuka daraja. Kwa sasa, Wigan inashika nafasi ya 16 katika msimamo wa ligi hiyo.
Kocha Mkuu wa Chelsea, Carlo Ancelotti alijigamba baada ya kuibwaga Liverpool kwamba, hakuna kitakachowazuia kutwaa taji hilomsimu huu.
Ancelotti alisema japokuwa bingwa atajulikana baada ya mechi za mwisho, kimahesabu, hakuna wasiwasi kwamba Chelsea ndiyo itakayolinyakua taji hilo.
“Huenda bado tunayo kazi ya kufanya, lakini huu ulikuwa mchezo muhimu katika kuwania ubingwa,”alisema. “Ulikuwa mchezo muhimu, na tulionyesha kiwango cha hali ya juu na kupata matokeo mazuri. Nina furaha kubwa.”
“Siku zote nimekuwa nikisema, ubingwa utapatikana katika mechi za mwisho, na hilo ndilo lililotokea,”aliongeza kocha huyo.
Ancellotti hakuwa tayari kueleza mustakabali wake katika klabu hiyo kwa madai kuwa, hana haraka ya kufanya hivyo. Alisema anatarajia kukutana na mwenyekiti wa klabu hiyo hivi karibuni kujadili juu ya suala hilo.
Alikiri kuwa, ligi ya msimu huu haikuwa bora kwa Chelsea kufuatia kufungwa mechi 11 na pia kujitokeza kwa matatizo mbalimbali. “Inaonekana, kocha amekuwa akibebeshwa lawama zote kwa kila kilichotokea miaka miwili iliyopita,”alisema.
Kocha Mkuu wa Manchester United, Sir Alex Ferguson hakuwa tayari kuzungumzia kiundani ushindani wa taji hilo. Lakini alikiri kuwa, Chelsea inayo nafasi kubwa zaidi ya kuwa bingwa.
Hata hivyo, Ferguson alisema bado wanayo matumaini ya kutwaa tena taji hilo na kuongeza kuwa, watategemea zaidi kubebwa na Wigan.
Wakati Chelsea na Manchester United zikipigana vikumbo kuwania ubingwa, ushindani wa nafasi ya nne upo kwa timu za Tottenham na Manchester City, ambazo zinatofautiana kwa pointi moja.
Kabla ya mechi za jana, Tottenham ilikuwa ikishika nafasi ya tatu kwa kuwa na pointi 67 baada ya kucheza mechi 36 wakati Man City ni ya nne kwa kuwa na pointi 66 baada ya kucheza idadi hiyo ya mechi.
Hatma juu ya timu ipi itakayoshika nafasi ya nne, ilitarajiwa kujulikana jana usiku baada ya mechi kati ya timu hizo, iliyotarajiwa kuchezwa kwenye uwanja wa Light.
Iwapo Tottenham itashinda mechi hiyo, itajiweka kwenye nafasi nzuri zaidi ya kushika nafasi hiyo na kusubiri mechi yake ya mwisho dhidi ya Burnley, ambapo itahitaji sare ya aina yoyote.
Wakati huo huo, Hull City wiki hii iliungana na Portsmouth na Burnley kushuka daraja la kwanza baada ya kulazimishwa kutoka sare ya mabao 2-2 na Wigan.
Matokeo hayo yaliifanya Hull City iwe na pointi 29 baada ya kucheza mechi 37 na hivyo kutokuwa na uwezo wa kufikisha pointi 34 ilizonazo West Ham, hata kama itashinda mechi yake ya mwisho dhidi ya Liverpool.
Portsmouth ilikuwa ya kwanza kupata tiketi ya kushuka daraja kutokana na kuwa na idadi ndogo ya pointi kuliko timu zingine zinazoshiriki ligi hiyo. Timu hiyo inayofundishwa na Kocha Avram Grant, inazo pointi 19 baada ya kucheza mechi 37 ikifuatiwa na Burnley yenye pointi 27.
Katika hatua nyingine, timu za Newcastle na West Bromwich zimefuzu kucheza ligi kuu ya England msimu ujao, baada ya kushika nafasi ya kwanza na ya pili katika ligi daraja la kwanza msimu huu.
Nafasi ya tatu ya kupanda daraja bado inawaniwa na timu za Nottingham Forest, Cardiff, Leicester City na Blackpool, ambazo zitalazimika kucheza mechi za mtoano ili kupata bingwa.
MECHI ZA MWISHO ZA
LIGI KUU JUMAPILI
Arsenal v Fulham
Aston Villa v Blackburn
Bolton v Birmingham
Burnley v Tottenham
Chelsea v Wigan
Everton v Portsmouth
Hull v Liverpool
Man Utd v Stoke
West Ham v Man City
Wolverhampton v Sunderland







No comments:

Post a Comment