KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 30, 2013

NEYMAR DA SILVA SANTOS: NIMEACHA PESA BRAZIL, NAFUATA SOKA HISPANIA



SAO PAULO, Brazil
MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Brazil, Neymar da Silva Santos amesema uamuzi wake wa kujiunga na klabu ya Barcelona ya Hispania umelenga kukuza zaidi kipaji chake cha soka.

Neymar alisema wiki hii mjini hapa kuwa, ameacha pesa nyingi katika klabu yake ya Santos na kufuata soka Hispania.

"Nakwenda Barcelona kukuza kiwango changu cha soka, sifuati pesa,"alisema Neymar, ambaye kwa sasa ni mwanasoka anayelipwa pesa nyingi nchini Brazil.

Mbali na malipo ya mshahara na posho katika klabu yake ya Santos, picha za Neymar zimekuwa zikitumika kwenye matangazo mbalimbali na hivyo kumwingizia mamilioni ya pesa.

Neymar alitangaza rasmi kujiunga na Barcelona mwishoni mwa wiki iliyopita kabla ya kumwaga wino Jumatatu wiki hii. Chipukizi huyo mwenye umri wa miaka 21 ameingia mkataba wa kuichezea Barcelona kwa miaka mitano.

Mbrazil huyo alikuwa akiwindwa na klabu mbalimbali za Ulaya, wakiwemo mahasimu wakubwa wa Barcelona, Real Madrid na Chelsea ya England.

"Nina masikitiko makubwa kuondoka Santos, lakini ni heshima kubwa kuingia mkataba na klabu kama Barcelona na kupata nafasi ya kucheza na baadhi ya wachezaji nyota duniani,"alisema Neymar.

Neymar ataungana na nyota kadhaa wa dunia, akiwemo mwanasoka bora wa dunia wa Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA), Lionel Messi, Xavi Hernandez na Andres Iniesta.

Hata hivyo, klabu za Barcelona na Santos hazijatangaza kiwango cha malipo ya ada ya uhamisho wa mchezaji huyo, lakini baadhi ya vyombo vya habari vya Brazil vimeripoti kuwa, uhamisho wake umeigharimu klabu hiyo ya Hispania pauni milioni 38.7.

Kwa mujibu wa vyombo hivyo vya habari, Santos ilikuwa imepokea ofa za kumsajili mchezaji huyo kutoka Barcelona na Real Madrid na lilikuwa jukumu la mchezaji kuamua wapi anapotaka kwenda kucheza.

Neymar aliandika ujumbe kupitia kwenye Twitter akielezea uamuzi wake wa kuondoka Santos, ambayo alianza kuichezea tangu 2009 alipokuwa mdogo kiumri.

"Asante kwa kila kitu. Nitatunza kumbukumbu hii katika maisha yangu yote,"alisema.

Neymar aliipatia Santos umaarufu mkubwa tangu mwanasoka nyota wa zamani wa dunia, Pele alipoichezea klabu hiyo miaka ya 1970. Aliiwezesha Santos kutwaa Komeb la Brazil 2010, Copa Libertadores 2011 na ubingwa wa Jimbo la Sao Paulo mara tatu mfululizo.

Mchezaji huyo kipenzi wa Pele, ameweka rekodi ya kuwa mfungaji bora wa Santos kwa kufunga mabao 138 katika mechi 230.

Baba wa mwanasoka huyo, Silva Santos alisema waliingia mkataba na Barcelona, Jumatatu wiki hii ukihusisha malipo ya mshahara na ada ya uhamisho wake.

Mzee huyo alisema pia kuwa, Neymar ameamua kujiunga Barcelona badala ya Real Madrid kwa sababu staili yake ya uchezaji inafanana na ya klabu hiyo.

Neymar alitarajiwa kujiunga na kikosi cha Brazil, Jumanne iliyopita kwa ajili ya maandalizi ya michuano ya Kombe la Mabara kabla ya kwenda Hispania kwa ajili ya utambulisho kwa mashabiki wa Barcelona, unaotarajiwa kufanyika Juni 2 mwaka huu.

Mwanasoka huyo anatarajiwa kuwemo katika kikosi cha Brazil kitakachocheza mechi ya kirafiki dhidi ya England, itakayopigwa kwenye uwanja wa Maracana.

Alipoulizwa kuhusu namba ya jezi anayotarajiwa kuivaa atakapokuwa Barcelona, mwanasoka huyo wa Brazil alisema hatajali iwapo atapewa namba yoyote.

Neymar amekuwa akivaa jezi namba 11 katika klabu yake ya Santos na timu ya taifa ya Brazil.

"Acha tuone namba itakayopatikana, hilo halitakuwa tatizo kwangu,"alisema Neymar.

Mwanasoka huyo alisema pia kuwa, hana hakika iwapo familia yake itahamia Barcelona au la.

Mtandao wa Barcelona umemwelezea Neymar kuwa ni mshambuliaji na mfungaji mabao wa aina yake, anayetumia mbinu za uchezaji zenye mvuto.

"Wengi wanaamini kuwa ndiye mrithi wa Pele,"ulieleza mtandao huo wiki hii.

Gazeti la Marca la Hispania liliripoti wiki hii kuwa, muunganiko wa Messi na Neymar utaunda safu tishio ya ushambuliaji. Neymar na Messi wanatarajiwa kucheza pamoja katika safu ya ushambuliaji.

Kwa mujibu wa gazeti hilo, Barcelona ilikuwa ikihitaji kwa muda mrefu kuwa na mshambuliaji mwenye staili ya uchezaji kama ya Messi ili kuifanya safu ya ushambuliaji ya timu hiyo iwe tishio zaidi.

Hata hivyo, baadhi ya wachambuzi wa masuala ya soka wanahoji iwapo Neymar, aliyeifungia Brazil mabao 32, ataweza kuimudu staili ya uchezaji soka ya Ulaya.

No comments:

Post a Comment