KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 23, 2013

REHEMA, SHILOLE WAJA NA MDUARA


MWANAMUZIKI mkongwe wa muziki wa dansi nchini, Rehema Tajiri anatarajia kurekodi wimbo mpya wa mduara kwa kushirikiana na msanii wa muziki wa kizazi kipya, Zuwena Mohamed 'Shilole'.

Akizungumza mjini Dar es Salaam juzi, Rehema alisema ameshaanza kufanya mazoezi na Shilole kwa ajili ya kurekodi wimbo huo.

Rehema alisema lengo la kurekodi wimbo huo ni kuwapa ladha tofauti ya muziki mashabiki wake.

"Bado hatujaupa jina wimbo huo, lakini nawahakikishia mashabiki wangu kwamba utakuwa moto wa kuotea mbali,"alisema Rehema.

"Kwa vile nimeamua kurudi kwenye fani kwa nguvu zote, nawahakikishia mashabiki wangu kwamba nyimbo zote mpya nitakazozitoa, zitakuwa hatari. Lengo langu ni kuwapa burudani ya uhakika,"alisema.

Wakati huo huo, Rehema amesema video ya wimbo wake mpya wa Msikilize Mama imekamilika na inatarajiwa kuanza kuonekana kwenye vituo vya televisheni wakati wowote.

Rehema alisema juzi kuwa, video hiyo imerekodiwa kwa ubora wa kiwango cha juu na itakuwa na mvuto wa aina yake kwa watazamaji wa luninga.

Mwanamuziki huyo mkongwe aliyewahi kurekodi nyimbo zake nyingi kwa kushirikiana na baadhi ya wanamuziki wa Msondo Ngoma, amerekodi kibao hicho kwa kutumia miondoko ya zouk.

Katika wimbo huo, Rehema amemshirikisha msanii chipukizi wa muziki wa kizazi kipya, Dogo Sama kwa lengo la kuutia nakshi.

Wimbo huo unazungumzia masuala ya mapenzi kati yake mwanamke na mpenzi wake, huku kikwazo kikubwa kikiwa kwa mama mkwe.

"Nimesimulia jinsi mimi na mpenzi wangu tunavyopendana, lakini mkwe wangu (mama wa mpenzi wake) hanipendi, anataka niachane na mwanawe,"alisema.

Rehema amewataka mashabiki wake wakae mkao wa kula kwa vile amejipanga upya kuhakikisha anateka tena soko la muziki nchini.

Alisema ukimya wake wa muda mrefu ulitokana na kutingwa na matatizo ya kifamilia na pia kujipanga upya.

No comments:

Post a Comment