KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 23, 2013

WACHEZAJI JANGWANI KUJAZWA MAMILIONI

KLABU ya Yanga imepanga kuwajaza mamilioni ya pesa wachezaji wake kutokana na timu hiyo kutwaa ubingwa wa ligi kuu ya Tanzania Bara msimu huu.

Pesa hizo ni zile zinazotokana na zawadi ya ubingwa wa ligi hiyo kutoka kwa wadhamini, Kampuni ya Simu za Mkononi ya Vodacom na zilizoahidiwa na Mwenyekiti wa klabu hiyo, Yussuf Manji.

Yanga itazawadiwa kitita cha sh. milioni 70 kutokana na kutwaa ubingwa wa ligi hiyo, ambao mwaka jana ulinyakuliwa na watani wao wa jadi Simba.

Naye Manji aliahidi kuwazawadia wachezaji wa timu hiyo sh. milioni 20 kwa kila mechi watakayoshinda katika mechi tano zilizokuwa zimesalia kabla ya ligi hiyo kumalizika kwa lengo la kuwaongezea hamasa.

Katika mechi hizo, Yanga ilishinda nne na kutoka sare moja, lakini uongozi umeamua kuwapa sh. milioni 50 bila kujali mechi moja waliyopata sare.

Uongozi wa Yanga pia uliahidi kuwapa wachezaji zawadi ya sh. milioni 50 iwapo wangeifunga Simba katika mechi ya mwisho ya ligi hiyo.

Katika mechi hiyo iliyochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Yanga iliichapa Simba mabao 2-0 na kunogesha sherehe za ubingwa.

Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako alikiri jana kufanyika kwa kikao cha kujadili mgawo huo wa wachezaji, lakini hakuwa tayari kutaja kiwango watakachowapa kwa madai kuwa hiyo ni siri ya klabu.

No comments:

Post a Comment