KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 30, 2013

NAMPENDA PENNY KULIKO WEMA-DIAMOND



MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Naseeb Abdul 'Diamond' amekiri kuwa anampenda zaidi mpenzi wake mpya, Penny Mungilwa kuliko ilivyokuwa kwa mpenzi wake wa zamani, Wema Sepetu.

Diamond alisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, mapenzi yake kwa Penny yamemfanya ajione kama vile ameoza kwa binti huyo.

"Ni sawa na kusema treni imegonga mwamba maana kila ninapokuwa naye, nasikia raha ya ajabu, sijui ameniroga. Ananipenda mno,nami nampenda, kwake nimefika,"alisema Diamond.

Msanii huyo nyota wa bongo fleva alisema japokuwa udanganyifu katika mapenzi ni jambo la kawaida, lakini Penny hajawahi kuonyesha dalili hiyo kwake.

Alisema kwa kawaida, mwanamke anapofanya udanganyifu wa mapenzi, inakuwa aibu kwa mwanaume, lakini udanganyifu huo ukifanywa na mwanaume, inakuwa sifa kwake.

"Ni kweli Wema alinipenda, alinionyesha mapenzi ya dhati, lakini alifanya udanganyifu hadharani, alinivunjia heshima, alinivunja moyo, sikupenda kitendo alichokifanya,"alisema Diamond.

Diamond alikanusha madai kuwa, aliwahi kuhusiana kimapenzi na mcheza filamu nyota, Irene Uwoya lakini alikiri kuhusiana kimapenzi na Jokate Mwegelo na Jacqueline Wolper.

Alipoulizwa ni kwa nini amekuwa akipenda kuhusiana kimapenzi na wacheza filamu kuliko wasanii wa fani zingine, Diamond alisema ni kwa sababu amekuwa akikutana nao mara kwa mara sehemu mbalimbali.

"Huwezi kujitosa kimapenzi kwa mtu usiyemfahamu. Hawa ndio ambao nakutana nao mara kwa mara,"alisema.

Je, ni kwa nini wasichana wengi wamekuwa wakimpenda Diamond?

"Unajua mimi nampenda sana mama yangu. Huenda Mungu ananiona na ameamua kunirejeshea upendo huo kupitia kwa watoto wa kike kwa kuwajaza mapenzi kwangu,"alisema.

Diamond alisema yeye ni mstaarabu na amekuwa akijituma katika kazi zake ndiyo sababu hata anapogombana na mpenzi wake, atabaki kumpenda.

Hata hivyo, Diamond alikiri kuwa anajuta kukosana na mpenzi wake wa zamani, Jokate kwa vile ni mwanamke mstaarabu na asiyekuwa na doa.

"Kusema kweli, Jokate hakuwahi kunikosea. Ni mtoto asiye na kosa lolote. Nilimfuata mwenyewe, nikampenda, lakini nilimkosea,"alisema Diamond.

Aliitaja sababu kubwa iliyomfanya agombane na Jokate kuwa ni uamuzi wake wa kurudiana kimapenzi na Wema.

"Nilikuwa nimegombana na Wema, tukarudiana, Jokate hakuufurahia uamuzi huo, sijui nilirogwa, sijui ilikuwa ni utoto, maana ujana ukizidi sana ni matatizo! Hajawahi kunikosea. Ni mstaarabu na ana maisha mazuri,"alisema.

Diamond alisema hajawahi kumuomba msamaha Jokate kwa kosa hilo kwa sababu hadi sasa anajisikia aibu kufanya hivyo.

Wakati huo huo, Diamond amesema amekubali kucheza filamu na Wema kutokana na muandaaji wake kumlipa kiasi kikubwa cha pesa.

"Sidhani kama kuna mcheza filamu wa Tanzania aliyewahi kulipwa fedha nyingi kiasi hiki na tayari nimeshalipwa. Hata katika muziki, sijawahi kulipwa pesa nyingi kiasi hiki,"alisema.

Diamond alisema awali, alimueleza muandaaji wa filamu hiyo wasiwasi aliokuwa nao kuhusu kucheza filamu hiyo na Wema, lakini baadaye akagundua kwamba hiyo ni kazi.

"Kuna watu waliokuwa na uhusiano wa kimapenzi, wakatengana lakini baadaye wakaja kufanya shughuli nyingi pamoja,"alisema msanii huyo.

Katika hatua nyingine, Diamond amesema akaunti yake benki haijawahi kupungua sh. milioni 100.

Alisema akaunti yake inapopungua pesa, huwa anachanganyikiwa na kuongeza kuwa, alianza kuwa na kiasi hicho cha pesa benki tangu 2011.

"Ukipiga hesabu, huu sasa ni mwaka 2013. Hapa nazungumzia zaidi ya bilioni moja benki,"alisema.

No comments:

Post a Comment