KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 23, 2013

HAYNCKES: HAKUNA KAMA BAYERN MUNICH


KOCHA Mkuu wa Bayern Munich, Jupp Heynckes wiki iliyopita alionekana kujawa na furaha kubwa wakati timu yake ilipoichapa Augsburg mabao 3-0 na kukabidhiwa kombe la ubingwa wa Bundesliga.

Bayern Munich ilitwaa kombe hilo tangu Aprili 6 mwaka huu huku ikiwa imesaliwa na mechi sita mkononi. Imetwaa taji hilo baada ya kulikosa kwa miaka mitatu na mechi ya wiki iliyopita ilikuwa ya kukamilisha ratiba.

"Hakuna timu katika historia ya Bundesliga, ambayo imewahi kuonyesha kiwango cha soka kama tulichoonyesha sisi msimu huu,"alisema kocha huyo, ambaye mikoba yake inatarajiwa kurithiwa na Pep Guardiola mwishoni mwa msimu huu.

Guardiola anatarajiwa kuanza rasmi kibarua cha kuinoa Bayern Munich, Juni 26 na kusafiri nayo hadi katika mji wa Trentino nchini Italia kwa ajili ya kambi ya mazoezi inayotarajiwa kuanza Julai 4 hadi 12 mwaka huu.

"Tulicheza kwa kiwango cha juu na hilo limenifanya nione fahari kubwa," aliongeza kocha huyo, ambaye aliagwa na mashabiki wapatao 20,000 waliohudhuria mechi hiyo.

Taji hilo lilikuwa na maana kubwa kwa Bayern Munich kwa vile haikuwa imetwaa taji lolote tangu 2010 ilipotwaa ubingwa wa ligi hiyo na kombe la ligi.

"Furaha yenu inanieleza kwamba, mlikuwa na kiu kubwa ya kubeba taji hili na mmekuwa mkilisubiri kwa muda mrefu," kocha huyo aliwaeleza mashabiki wa Bayern Munich.

Heynckes aliwaahidi mashabiki hao kwamba, wanayo nafasi nyingine kubwa ya kutwaa taji la ligi ya mabingwa wa Ulaya wakati watakapomenyana na mahasimu wao, Borussia Dortmund katika mechi ya fainali itakayopigwa Mei 25 mwaka huu kwenye uwanja wa Wembley nchini England.

"Tutafanya kila tunaloweza kuhakikisha kwamba tunakipata kile, ambacho tumekuwa tukikiota kwa miaka mingi,"alisema kocha huyo.

Bayern Munich ilishindwa kutwaa taji hilo 2010 baada ya kufungwa na Inter Milan ya Italia katika mechi ya fainali kabla ya kulikosa tena msimu uliopita baada ya kufungwa na Chelsea.

Mbali na taji hilo, Bayern Munich pia inatarajiwa kumenyana na Stuttgart katika mechi ya fainali ya DFB-Pokal itakayochezwa Juni Mosi mwaka huu kwenye uwanja wa Olimpiki mjini Berlin.

Kwa upande wake, nahodha wa Bayern Munich, Philipp Lahm alisema bado kazi waliyoianza haijamalizika kwa sababu wamepania kuongeza mataji mawili zaidi.

"Kombe hili limerejea Munich, ambako ndiko mahali pake. Ni ndoto kuona idadi kubwa ya mashabiki hapa uwanjani,"alisema nahodha huyo alipokuwa akizungumzia ubingwa wa Bundesliga.

Lahm ndiye aliyepokea kombe la ubingwa kutoka kwa Rais wa Ligi ya Soka ya Ujerumani (DFL), Reinhard Rauball kwenye uwanja wa Allianz Arena.

Nahodha huyo wa Bayern Munich alisema lengo lao kubwa ni kuweka rekodi ya kutwaa mataji matatu msimu huu na kuendelea hivyo kwa miaka michache ijayo.

Lahm alisema anaona fahari kubwa kuwa nahodha wa Bayern Munich iliyotwaa ubingwa wa Bundesliga msimu huu na pia kuendelea kuwa katika kiwango cha juu.

"Kutwaa ubingwa wa ligi siku zote ni kitu muhimu na ni mafanikio makubwa kwa sababu mnakuwa mmecheza kwa kiwango bora katika mechi 34. Na msimu huu tumevunja rekodi chache,"alisema nahodha huyo.

Lahm alilielezea benchi la ufundi la klabu hiyo kwamba limefanyakazi nzuri na kumfanya kila mchezaji ajione muhimu katika timu.

Alisema kufuzu kwa Bayern Munich na Dortmund kucheza fainali ya ligi ya mabingwa wa Ulaya ni mafanikio makubwa katika soka ya Ujerumani na kuongeza kuwa, hawatakuwa tayari kuipoteza nafasi hiyo.

"Ni mechi itakayozikutanisha timu zenye kiwango cha juu. Na siku zote, timu itakayocheza kwa kiwango cha chini ama kufanya makosa ndiyo itakayopoteza mchezo,"alisema.

"Tutalazimika kuwa makini katika safu yetu ya ulinzi, kama ambavyo tumekuwa tukifanya msimu wote. Na tunayo safu nzuri ya ushambuliaji na siku zote imekuwa ikitafuta magoli kwa bidii,"aliongeza nahodha huyo.

Kwa mujibu wa Lahm, Bayern Munich itaendelea kuwa na mafanikio makubwa katika kipindi cha miaka michache ijayo, ndani na nje ya nchi hiyo.

No comments:

Post a Comment