KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 30, 2013

MUUMIN MWINJUMA: NAJUTA KUTUNGA WIMBO WA CALL BOX



MWANAMUZIKI nyota nchini, Muumin Mwinjuma amesema hakuna kitu anachokijutia katika maisha yake kimuziki kama kutunga wimbo wa Call Box.

Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Muumin alisema wimbo huo ulipoteza heshima yake kimuziki na kumfanya achukiwe na wanawake wengi kwa kuhisi alimtungia mkewe wa pili.

Muumin alisema hadi sasa bado anakuna kichwa ili kurejesha heshima yake kimuziki, hasa kwa wanawake, ambao alikiri kuwa ndiyo mashabiki wake wakubwa.

Alikanusha madai kuwa, alitunga wimbo huo kwa lengo la kusimulia mkasa uliomfanya aachane na mkewe wa pili baada ya kumfumania mara mbili.

"Huu wimbo nilipewa na rafiki yangu mmoja, ambaye ni mganga wa kienyeji, aliniomba niuimbe. Bahati mbaya sana, nilirekodi wimbo huu muda mfupi baada ya kuachana na mke wangu, ndio sababu mashabiki wengi walidhani nimemwimbia yeye,"alisema.

Muumin alisema mashabiki wake wengi ni wanawake kutokana na kuzipokea vizuri nyimbo zake za Mgumba namba moja na namba mbili pamoja na Kilio cha Yatima, hivyo kumchukulia kama mtetezi wao.

Mwimbaji huyo mkongwe alisema amekuwa akitunga nyimbo zake nyingi kutokana na hisia, lakini wakati mwingine hufanya hivyo kutokana na kushuhudia ama kusikia mikasa mbalimbali.

Akisimulia mkasa uliosababisha atengane na mkewe wa pili, Muumin alisema aliwahi kumfumania mara mbili akifanya mapenzi na rafiki zake wawili.

"Ni matukio yaliyonisikitisha na kuhuzunisha sana kwa sababu watu niliomkuta nao ni rafiki zangu wa karibu wa kufa na kuzikana. Ni watu, ambao wamekuwa wakinisaidia na hadi leo ni rafiki zangu,"alisema mwanamuziki huyo.

Aliongeza kuwa, hakutaka kugombana na rafiki zake hao kwa sababu alichobaini ni kwamba, mkosaji mkubwa alikuwa mkewe.

"Alikuwa akiwafahamu vizuri watu hawa kwamba ni rafiki zangu, hivyo hakuwa na sababu ya kuhusiana nao kimapenzi. Hiyo ndiyo sababu kubwa iliyonifanya niachane naye,"alisema.

Muumin alikiri kuwa, kwa sasa amefunga ndoa na mwanamke mwingine, ikiwa ni ndoa yake ya tatu, lakini hapendi ijulikane kwa hofu ya kusukamwa kwa maneno.

Mwimbaji huyo mwenye sauti yenye mvuto alisema, mara nyingi baadhi ya watu wamekuwa wakimsakama kila anapofanya jambo fulani, hivyo ameona ni vyema afanye mambo yake kimya kimya.

Kwa sasa, Muumin ni kiongozi wa bendi ya Victoria Sound, aliyoianzisha mwaka jana baada ya kujiengua katika bendi ya Twanga Pepeta International.

Muumin alisema bendi ya Victoria Sound sio mpya kwa sababu ilianzishwa miaka sita iliyopita. Alisema kilichofanyika ni kuisuka upya.

Kwa mujibu wa Muumin, tayari wameshatunga vibao vipya vinne na wameshaanza kuvipiga kwenye kumbi mbalimbali wanazofanya maonyesho.

Alivitaja vibao hivyo kuwa ni Shamba la Bibi na Utafiti wa mapenzi, alivyovitunga yeye mwenyewe. Aliviita vibao hivyo kuwa ni moto wa kuotea mbali.

Vibao vingine ni Mama Bahati, kilichotungwa na mpiga gita la rythim, Yohana Mbatizaji na Mwisho wa siku, kilichotungwa na Waziri Sonyo.

Muumin alitamba kuwa, baada ya kuisuka upya bendi hiyo, wapinzani wao wakubwa kwa sasa watakuwa Twanga Pepeta na FM Academia.

Mbali na Muumin, Sonyo na Yohana, wanamuziki wengine wanaounda bendi hiyo ni Selemani Mumba, anayepiga gita la solo na Moshi Hamisi, anayepiga kinanda.

Wengine ni George Gama, anayepiga magita yote matatu, Januari Joseph, Ciana Jordan, Ramso Bushoke, Jonas Mlembuka na Mussa Kalenga, ambao ni waimbaji.

Wanamuziki wengine wanaounda bendi hiyo ni Kassim Mumba, anayepiga gita la besi, Abdalla Hussein anayepiga kinanda na Vaninga Swalehe,anayepiga tumba.

Bendi hiyo inakamilishwa na wacheza shoo, Omari Mussa 'Bokilo', Joha Juma, Mariam Othaman, Farida Omari, Lilian Wayanga, Nadia Benjamin na Sophia Ramadhani.

No comments:

Post a Comment