KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 30, 2013

KIFO CHA MANGWAIR SIMANZI TUPU


KWA mashabiki wengi wa muziki wa kizazi kipya, taarifa za kifo cha msanii nyota wa muziki huo nchini, Albert Mangwair zilionekana kama ni za uzushi.

Hakuna aliyependa kuzisikia wala kuamini. Ilionekana kama vile ni utamaduni uliozoeleka wa watu kutumiana meseji za uzushi kupitia simu za mkononi kwa lengo la kutiana vihoro.

Kadri muda ulivyokuwa ukisonga mbele, taarifa hizo ziliendelea kutapakaa nchi nzima kupitia matangazo ya redio na kwenye mitandao ya kijamii na hatimaye kuthibitika kwamba ni kweli Mangwair amefariki dunia.

Mangwair, ambaye alijipatia umaarufu mkubwa kutokana na umahiri wake katika kuimba nyimbo za muziki wa hip hop, alifariki dunia juzi nchini Afrika Kusini, ambako alikwenda mwezi mmoja uliopita.

Taarifa zilizopatikana kutoka Afrika Kusini zilieleza kuwa, Mangwair alifariki dunia kutokana na matatizo ya matumizi ya dawa za kulevya.

Kifo cha Mangwair kimezua simanzi kubwa miongoni mwa wasanii na mashabiki wa muziki wa kizazi kipya, ambao baadhi yao walijikuta wakiangua vilio hadharani kwa huzuni.

Mama mzazi wa msanii huyo alisema, alipata taarifa za kifo cha mwanawe kutoka kwa dada wa marehemu, ambaye alipigiwa simu na mtu wa karibu wa msanii huyo.

"Wakati anaondoka, hakuniaga, lakini baada ya kufika huko, alinipigia simu na kuniambia kuwa yupo huko na aliniuliza kama sijambo, nikamwambia sijambo na aliniomba nimuombee na alishukuru kusikia tunaendelea vizuri," alisema mama huyo alipohojiwa na kituo cha redio cha Clouds FM.

"Hapa tunasubiri baba zake wadogo walikwenda Songea, wakirudi tutajua taratibu za mazishi zitakuwaje," aliongeza mama huyo.

Baba mdogo wa msanii huyo, ambaye anaishi Mbinga, Songea alisema wamekubaliana na kaka yake mkubwa, David Mangweha kukutana Mbezi, Dar es Salaam kwa ajili ya kupanga mipango ya mazishi ya mtoto wao.

Japokuwa bado haujatolewa uamuzi wowote kuhusu wapi atakapozikwa msanii huyo, David alisema huenda mazishi yakafanyika Morogoro, ambako baba yake mzazi alizikwa.

Alisema taratibu za kuurejesha nyumbani mwili wa Mangwair zinafanywa na baadhi ya ndugu zake kwa kushirikiana na ubalozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini.

Akihojiwa na kituo cha redio cha East Africa jana asubuhi, mwanamuziki nyota wa muziki huo, Judith Wambura 'Lady Jaydee' alishindwa kuzungumza maneno mengi zaidi ya kuangua kilio.

Jaydee alisema amekuwa mtu wa karibu na Mangwair na kuongeza kuwa, taarifa za kifo chake zimemuhuzunisha.

Kutokana na kifo cha msanii huyo, JayDee aliamua kuahirisha onyesho lake la kutimiza miaka 13 katika muziki huo lililopangwa kufanyika kesho.

Onyesho hilo la Jaydee pia lilikuwa maalumu kwa ajili ya uzinduzi wa albamu yake mpya, uliotarajiwa kufanyika kwenye ukumbi wa Nyumbani Lounge.

JayDee alipanga kulitumia onyesho hilo kupiga nyimbo zake zote zilizowahi kutamba, ikiwa ni pamoja na zile alizowashirikisha wasanii mbalimbali nchini.

Naye Khamis Mwijuma (Mwana FA) alisema jana kuwa, amelazimika kusogeza mbele onyesho lake la kutimiza miaka 10 katika fani ya muziki lililopangwa kesho kutokana na kuguswa na kifo cha msanii huyo.

Mwana FA alipanga kufanya onyesho hilo kwenye ukumbi wa Makumbusho uliopo Kijitonyama, Dar es Salaam, akiwashirikisha wasanii mbalimbali maarufu nchini pamoja na bendi ya The Kilimanjaro 'Wana Njenje'.

Alisema kifo cha Mangwair ni pigo kubwa katika fani ya muziki wa kizazi kipya nchini kwa vile alikuwa na mchango mkubwa katika muziki huo.

"Siwezi kuendelea na onyesho langu siku mbili baada ya kifo cha mwenzetu na kaka yetu, naomba radhi kwa mashabiki wangu. Tutapanga tarehe nyingine ya kufanya onyesho hili,"alisema.

Mwana FA alisema alipata taarifa za kifo cha msanii huyo akiwa mazoezini na kujikuta akijawa na majonzi mengi kwa vile alikuwa mtu wake wa karibu.

"Nililazimika kuwaeleza wasanii wenzangu, ambao ningeshirikiana nao kufanya onyesho langu la Ijumaa (kesho) kwamba hatutaweza kuendelea nalo,"alisema Mwana FA.

Akielezea uhusiano wake na Mangwair, Mwana FA alisema walikuwa marafiki wa karibu, lakini walishindwa kuwa pamoja katika miaka ya hivi karibuni kutokana na kila mtu kutingwa na shughuli zake.

Kiongozi wa kikundi cha Kikosi cha Mizinga, Karama Kalapina alisema jana kuwa, kifo cha Mangwair kimewafanya waamue kuahirisha onyesho lao la kusherehekea kutimiza miaka 13 lililopangwa kufanyika kesho kwenye ukumbi wa Msasani Beach Dar es Salaam.

Mtangazaji wa kituo cha redio cha Clouds FM, Boniventura Kilosa 'DJ Venture' alisema aliwahi kuishi gheto na Mangwair na kuongeza kuwa, alikuwa mtu wake wa karibu.

Kwa upande wake, P Funky, ambaye ndiye aliyemtoa Mangwair alisema ameamua kukizuia kituo cha redio cha Clouds FM kupiga nyimbo zote za msanii huyo aliyezirekodi kwenye studio yake.

Wakati huo huo, msanii M to the P aliyekwenda Afrika Kusini pamoja na marehemu Albert Mangwair, amefariki dunia.

Taarifa zilizopatikana jana kutoka Afrika Kusini zilisema kuwa, msanii huyo alipelekwa katika hospitali ya St Hellen iliyopo chini humo kwa matibabu baada ya kukutwa amepoteza fahamu akiwa na Mangwair aliyefariki dunia juzi.

Miili ya marehemu hao bado iko katika hospitali hiyo na mipango ya kuisafirisha kuirejesha Tanzania inaendelea kufanywa na watanzania wanaoishi nchini humo.

No comments:

Post a Comment