KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 23, 2013

AZAM: HATUNA MPANGO WA KUMTOSA UHURU SELEMANI

UONGOZI wa klabu ya Azam umesema hauna mpango wa kumtupia virago mshambuliaji Uhuru Selemani baada ya msimu huu wa ligi kuu kumalizika.

Kocha Msaidizi wa Azam, Kally Ongara alisema mjini Dar es Salaam juzi kuwa, Uhuru ataendelea kuwemo kwenye kikosi cha timu hiyo katika msimu ujao wa ligi.

Ongara alisema kukaa benchi kwa Uhuru katika msimu huu wa ligi, kulitokana na mpangilio wa uchezaji wa Kocha Stewart Hall katika kikosi cha kwanza.

"Si kweli kwamba Uhuru alikuwa hapangwi kwa sababu ya kushuka kwa kiwango chake. Bado Uhuru ni mchezaji mzuri, isipokuwa ulikuwa uamuzi wa kocha anavyotaka kikosi chake kicheze,"alisema.

Ongara alisema Uhuru bado ni mchezaji mzuri na ana uwezo wa kuendelea kuwemo kwenye kikosi cha Azam kwa zaidi ya mwaka mmoja.

Alisisitiza kuwa, kwa vile kocha ndiye mwenye uamuzi wa mwisho kuhusu upangaji wa kikosi katika mechi, Uhuru anapaswa kuwa mvumilivu na kuongeza bidii katika mazoezi.

"Nimesikia watu wakilalamika kwa nini Uhuru hachezeshwi katika mechi za Azam. Ninachofahamu ni kwamba Uhuru ni mchezaji mwenye sifa zote za kucheza soka, lakini bado kuna mtu mwenye mamlaka ya kuamua nani acheze na nani asicheze,"alisema.

Kauli ya Ongara imekuja siku chache baada ya kuwepo na taarifa kwamba, Uhuru anataka kurejea Simba kutokana na kuchoshwa kukaa benchi.

Mshambuliaji huyo wa zamani wa Coastal Union, alijiunga na Azam kwa mkopo wakati wa usajili wa dirisha dogo akitokea Simba, aliyoichezea kwa misimu miwili.

Alipoulizwa iwapo ni kweli anataka kuondoka Azam, mshambuliaji huyo alisema: "Hakuna mchezaji anayefurahia kuwekwa benchi."

Hata hivyo, Uhuru alisema amepanga kukitumia kipindi hiki cha mapumziko kufanya mazoezi ya nguvu ili aweze kurejea katika kiwango chake.

No comments:

Post a Comment