KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, May 26, 2013

30 WAITWA KAMBINI TWIGA STARS



Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ya wanawake ya mpira wa miguu (Twiga Stars), Rogasian Kaijage amewaita kambini wachezaji 30 ikiwa ni mwendelezo wa kuijenga na kuiimarisha timu hiyo.

Twiga Stars itakuwa na kambi ya siku kumi kuanzia Jumapili (Mei 26 mwaka huu) ambapo baadaye inatarajia kucheza mechi moja ya kirafiki kabla ya wachezaji kurudi kwenye klabu zao.

Kambi hiyo ni mwendelezo wa programu iliyopendekezwa na kocha kuijenga na kuiimarisha timu hiyo kwa vile haina mashindano mwaka huu, na itakuwa kambi ya pili baada ya ile iliyofanyika Machi mwaka huu.

Wachezaji walioitwa na klabu zao kwenye mabano ni Asha Rashid (Mburahati Queens), Aziza Mwadini (Zanzibar), Belina Julius (Lord Barden), Ester Chabruma (Sayari), Ester Mayala (TSC Academy), Eto Mlenzi (JKT), Evelyn Sekikubo (Mburahati Queens) na Fatuma Bushiri (Mburahati Queens).

Fatuma Hassan (Mburahati Queens), Fatuma Omari (Sayari), Flora Kayanda (Tanzanite), Hamisa Athuman (Marsh Academy), Hellen Peter (JKT), Maimuna Said (JKT), Mwajuma Abdallah (Tanzanite), Mwanahamisi Omari (Mburahati Queens), Mwanaidi Tamba (Mburahati Queens) na Mwapewa Mtumwa (Sayari).

Nabila Ahmed (Marsh Academy), Pulkeria Charaji (Sayari), Rehema Abdul (Lord Barden), Rukia Khamis (Uzuri Queens), Semeni Abeid (Tanzanite), Sharida Boniface (Makongo Sekondari), Sophia Mwasikili (Sayari), Therese Yona (TSC Academy), Vumilia Maarifa (Evergreen) na Zena Khamis (Mburahati Queens).

RCL KUENDELEA KUTIMUA VUMBI KESHO
Raundi ya pili ya Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) inaendelea kesho (Mei 26 mwaka huu) kwa mechi sita za kwanza zitakazochezwa katika miji sita tofauti.

Abajalo ya Dar es Salaam na Kariakoo ya Lindi zitaumana kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam wakati Machava FC ya Kilimanjaro itakuwa mwenyeji wa Mpwapwa Stars ya Dodoma kwenye Uwanja wa Ushirika mjini Moshi.

Nayo Stand United FC ya Shinyanga itakuwa mgeni wa Magic Pressure ya Singida kwenye Uwanja wa Namfua mjini Singida huku Polisi Jamii ya Bunda mkoani Mara ikimenyana na Biharamulo FC ya Kagera kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma.

Mjini Kigoma kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika ni kati ya wenyeji Saigon FC na Katavi Warriors ya Katavi wakati Njombe Mji itaikaribisha Kimondo SC ya Mbeya kwenye Uwanja wa Sabasaba mjini Njombe.

Leo (Mei 25 mwaka huu) Friends Rangers ya Kinondoni, Dar es Salaam inacheza na African Sports ya Tanga kwenye Uwanja wa Azam Chamazi. Mechi za marudiano zitachezwa kati ya Juni 1 na 2 mwaka huu.

Timu zitakazofuzu kucheza raundi ya tatu zitacheza mechi za kwanza kati ya Juni 8 na 9 mwaka huu wakati mechi za marudiano zitakuwa kati ya Juni 15 na 16 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment