KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 23, 2013

YANGA YAITESA SIMBA



KAMATI ya Usajili ya klabu ya Simba imepanga kufanya usajili wa wachezaji wake wapya msimu ujao kwa siri ili kuepuka kuingiliwa na wapinzani wao.

Mwenyekiti wa kamati ya usajili ya Simba, Zacharia Hanspope alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, wamepania kufanya usajili wa nguvu msimu ujao kwa lengo la kurejesha taji la ligi kuu.

Hanspope alisema uamuzi huo ulifikiwa katika kikao cha kamati ya utendaji ya Simba kilichofanyika mjini Dar es Salaam juzi.

Alisema usajili huo utafanyika kwa kuzingatia vigezo muhimu, ambavyo vitawekwa na kamati hiyo.

"Tulikutana jana (juzi) na kuamua kufanya usajili kwa staili ya pekee ili kukwepa hujuma kutoka kwa wapinzani wetu,"alisema.

Alisema Simba ilifanya usajili usiokuwa na viwango msimu uliopita baada ya kufanyiwa hujuma nyingi na kujikuta ikisajili wachezaji ambao hawakuwa chaguo lao.

Katika msimu huo, Simba ilizidiwa kete na Yanga kwa mchezaji wa zamani wa APR ya Rwanda, Mbuyu Twite, ambaye alikula fedha za Msimbazi, lakini akatua Jangwani.

Hanspope alisema kwa kuwa msimu uliopita walifanya makosa, hawaoni sababu ya kuyaduria msimu ujao na kusisitiza kuwa, kila kitu kitafanyika kwa kuzingatia viwango vitakavyowekwa.

"Napenda niwaambie kuwa, msimu uliopita tulifanya usajili, lakini umetugharimu na kutufikisha hapa tulipo, hivyo hatupaswi kurudia makosa," alisema Hanspope.

Mbali na kuzungumzia usajili, Hanspope alisema kikao hicho pia kilijadili masuala mengine mbalimbali, ikiwemo tathmini ya wachezaji wote wanaounda timu hiyo.

Aliongeza kuwa, mambo mengine waliyoyajadili yatabaki kuwa siri hadi utekelezaji wake utakapokamilika ili taarifa zisivuje na kuwafikia wapinzani wao.

Kamati ya usajili ya Simba inaundwa na Hanspope (mwenyekiti), Kasim Dewji (makamu mwenyekiti), Francis Waya, Crencesious Magori, Salim Abdallah, Collins Frisch na Gerald Lukumaya (wajumbe).

No comments:

Post a Comment