KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, May 24, 2013

KIKWETE AWAPA CHANGAMOTO WACHEZAJI TAIFA STARS

RAIS Jakaya Kikwete amesema ataweka historia ya kukumbukwa na wachezaji wa timu ya Taifa, Taifa Stars iwapo itafuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia 2014.
Rais Kikwete pia amesema atatoa zawadi nono kwa timu hiyo iwapo itashinda mchezo wake wa kufuzu kucheza fainali za kombe hilo dhidi ya Morocco.

Kikwete alisema hayo jana Ikulu mjini Dar es Salaam alipokutana na wachezaji wa timu hiyo pamoja na viongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Taifa Stars inatarajiwa kurudiana na Morocco, Juni 8 mwaka huu katika mechi itakayopigwa mjini Marrakech. Katika mechi ya awali iliyochezwa mjini Dar es Salaam, Taifa Stars iliichapa Morocco mabao 4-1.

Timu hiyo imepangwa kundi C pamoja na timu za Morocco, Ivory Coast na Gambia. Inashika nafasi ya pili katika kundi hilo ikiwa na pointi sita nyuma ya Ivory Coast inayoongoza kwa kuwa na pointi saba.

Kikwete alisema kufuzu kwa Taifa Stars kucheza fainali za kombe hilo litakuwa tukio la kihistoria katika uongozi wake, hivyo atawapa zawadi nzito.

Alisema hatua iliyofikia sasa Taifa Stars ni nzuri hivyo wachezaji wanapaswa kucheza kufa na kupona ili kuandika historia mpya kwa Tanzania.

Kikwete alisema serikali itakuwa tayari kutoa msaada wa kila aina kwa timu hiyo ili iweze kufanikisha azma hiyo na kuongeza kuwa, jukumu la wachezaji ni kucheza mpira.

Alisema jambo la msingi kwa wachezaji ni kuhakikisha mawazo na akili zao wanazielekeza katika mechi zijazo za michuano hiyo.

"Sasa hivi elekezeni nguvu zenu katika michezo yenu na mhakikishe mnashinda, hayo mambo mengine niachieni mimi na Kamati ya Saidia Stars Ishinde,"alisema.

Rais Kikwete alisema mechi zilizobaki kwa Taifa Stars ni ngumu, lakini iwapo wachezaJi watajiamini na kujijenga kisaikolojia, haitakuwa migumu.

No comments:

Post a Comment