KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 30, 2013

PELLEGRINI ATALIWEZA FUPA LILILOMSHINDA MANCINI?



LONDON, England
KOCHA Mkuu wa Malaga ya Hispania, Manuel Pellegrini amethibitisha kuwa, Manchester City ya England ni miongoni mwa klabu zilizompa ofa nzuri na ambayo anaipa uzito mkubwa.

Pellegrini (59) amekuwa akipewa nafasi kubwa ya kuchukua nafasi ya Roberto Mancini, ambaye alitimuliwa Manchester City kabla ya msimu huu kumalizika.

Hata hivyo, kocha huyo raia wa Chile, pia amekuwa akiwindwa kwa udi na uvumba na klabu za AS Roma, Napoli za Italia na Paris St Germain (PSG) ya Ufaransa.

Pellegrini aliwaambia waandishi wa habari wiki hii kuwa, anaondoka Malaga ili kutimiza ndoto aliyonayo katika mchezo wa soka na kuongeza kuwa, tayari ameshaanza kufanya mazungumzo na viongozi wa Manchester City.

Kocha huyo alisema anapaswa kuwa makini katika kuamua wapi pa kwenda, lakini alisisitiza kuwa, anaipa uzito mkubwa ofa kutoka kwa Manchester City.

Pellegrini aliiongoza Malaga katika mechi ya mwisho Jumapili iliyopita wakati timu hiyo ilipomenyana na Deportivo la Coruna katika mechi ya ligi kuu ya Hispania na kuibuka na ushindi wa mabao 3-1.

Kocha huyo alisema anaona fahari kuondoka Malaga akiwa ameiacha timu hiyo katika hali nzuri. Malaga imemaliza ligi ya Hispania ikiwa nafasi ya sita.

"Hupaswi kuuliza sherehe nzuri ya kuagwa. Nilitaka kuondoka hapa na ushindi na hivyo ndivyo nilivyofanya. Naondoka hapa timu ikiwa inashiriki michuano ya Ulaya kwa mara ya pili mfululizo. Nitayakumbuka mafanikio haya kwa muda mrefu,"alisema kocha huyo.

"Lengo letu lilikuwa kucheza michuano ya Ulaya kwa sababu klabu hii inastahili. Miaka yangu miwili na nusu hapa imekuwa ya kihistoria. Kuna siku ambazo kamwe siwezi kuzisahau,"aliongeza.

Staili ya ufundishaji soka ya Pellegrini na uongozi wake ni miongoni mwa vitu vilivyotarajiwa kumwongezea thamani kocha huyo atakapoanza kibarua cha kuinoa Manchester City.

Manchester City iliamua kukatisha mkataba wake na Mancini, kufuatia timu hiyo kupokonywa taji la ubingwa wa ligi kuu ya England na mahasimu wao, Manchester United na pia kufungwa na Wigan katika fainali ya Kombe la FA.

Kuna habari kuwa, iwapo Pellegrini atatua Manchester City, huenda akamnyakua kiungo nyota wa Malaga, Isco.

Tayari uongozi wa Manchester City umeshampa mtihani mgumu Pellegrini kwa kumweleza kuwa, anatakiwa kuiongoza klabu hiyo kutwaa mataji matano katika misimu mitano.

Pellegrini anatarajiwa kutangazwa rasmi kuwa kocha wa Manchester City, Juni 3 mwaka huu.

Mtendaji Mkuu wa Manchester City,Ferran Soriano alisema licha ya Manchester City kutwaa taji la ligi kuu ya England msimu uliopita, haijapata mafanikio makubwa chini ya Mancini.

"Nadhani msimu ujao utakuwa bora zaidi kwetu. Nashawishika kuamini hivyo,"alisema Soriano.

"Haimaanishi kwamba tutashinda taji moja au mawili, lakini katika mpangilio wa vitu, tukitazama miaka mitano ijayo, na ninaweza kupanga hivyo, naweza kusema nataka kushinda mataji matano katika kipindi cha miaka mitano ijayo,"aliongeza.

Akifafanua, Soriano alisema iwapo watashindwa kutwaa taji lolote katika msimu mmoja, wanapaswa kutwaa mataji mawili katika msimu utakaofuata.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa lengo lao ni kushinda taji moja kila msimu, yakiwemo mataji ya ligi ya mabingwa wa Ulaya, ligi kuu ya Englandn na Kombe la FA.

"Kama mwaka ujao hatutashinda taji lolote, lakini tutaendelea vyema na mchezo wetu na kufuzu kucheza nusu fainali ya ligi ya mabingwa wa Ulaya, kushika nafasi ya pili katika ligi kuu ya England na kufungwa kwenye fainali ya Kombe la FA, haitakuwa mbaya,"alisema.

"Tunachotaka kocha wetu mpya akifanye ni kujenga kikosi, ambacho kinaweza kudumu na kufanya vizuri katika miaka 10 ijayo,"aliongeza kocha huyo.

Soriano alimpongeza Mancini kwa kazi nzuri aliyoifanya alipokuwa akiifundisha Manchester City, ambapo aliiwezesha kufuta ukame wa miaka 35 kwa kutwaa Kombe la FA, 2011 na taji la ligi kuu ya England msimu wa 2012.

Alisema Mancini alifanyakazi nzuri kwa kuibadili klabu hiyo kutoka isiyoshinda taji lolote na kuwa klabu ya ushindi. Alikiri kuwa kazi hiyo ilikuwa ngumu.

Mtendaji huyo wa Manchester City alisema uamuzi wa kumtimua Mancini ulifanywa kwa muda mrefu na umakini mkubwa ili kuepuka kuivuruga timu hiyo.

"Kamwe tusingeweza kumbadili kocha kutokana na matokeo ya mechi moja au mbili. Unapotaka kufanya mabadiliko, unapaswa kuwa na hakika na kile unachokifanya,"alisema Soriano.

Hata hivyo, alisema kikosi walichonacho sasa kina uwezo wa kushinda taji la ligi kuu ya England na siyo kikosi cha kutolewa hatua ya makundi katika michuano ya ligi ya mabingwa wa Ulaya.

Soriano, ambaye aliteuliwa kuwa mtendaji mkuu wa Manchester City, 2012, alisema bodi ya wakurugenzi wa klabu hiyo ilitafakari mambo mengi kabla ya kufikia uamuzi wa kumtimua Mancini, aliyedumu klabu hiyo kwa miaka mitatu na nusu.

Alitoa mfano wa tukio la kocha huyo kurushiana ngumi na mshambuliaji, Mario Balotelli, ambaye aliuzwa kwa klabu ya AC Milan mwanzoni mwa mwaka huu.

Alisema tukio hilo lilileta picha mbaya kwa Manchester City duniani na kuongeza kuwa, hawako tayari kuliona likitokea tena.

"Kutokana na kikosi tulichonacho, tunataka kuwa na kocha mtu mzima. Tunataka kuwa na kocha, anayefahamu kuhusu soka na uongozi. Haitawezekana kwetu kushinda ubingwa wa Ulaya kama hatutakuwa na kundi linalojiona kama familia moja,"alisema Soriano.

Mtendaji huyo alisema pia kuwa, wanataka kuwa na kikosi ambacho nusu ya wachezaji ni wazawa kama ilivyo kwa klabu za Manchester United na Barcelona ya Hispania.

WASIFU WA PELLEGRINI
KUZALIWA: Septemba 16, 1953
UMRI: Miaka 59
URAIA: Chile
NCHI ALIZOFUNDISHA SOKA: Hispania, Argentina na Chile

No comments:

Post a Comment