KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 23, 2013

LUIZ AZIGONGANISHA BARCA NA REAL MADRID


MADRID, Hispania
KLABU za Real Madrid na Barcelona za Hispania zimeanza kupigana vikumbo kwa ajili ya kumwania beki David Luiz wa Chelsea ya England.

Luiz huenda akawa mchezaji wa kwanza kuondoka Chelsea baada ya kutua kwa kocha mpya, Jose Mourinho, ambaye havutiwi na uchezaji wa beki huyo.

Beki huyo kutoka Brazil aliigharimu Chelsea pauni milioni 12 za Uingereza (sh. bilioni 19) na klabu hiyo inataka kumuuza kwa faida iwapo itapata ofa kutoka kwa klabu zingine.

Mourinho anataka kusajili beki mpya wa kati, kiungo mkabaji na mshambuliaji mmoja baada ya kurejea Stamford Bridge.

Luiz amekuwa akicheza nafasi ya kiungo mkabaji chini ya kocha Rafael Benitez, ambaye amefungashiwa virago baada ya ligi kuu ya England kumalizika.

Barcelona imepanga kumsajili Luiz kwa ajili ya kuimarisha safu yake ya ulinzi na huenda ikatumia kitita cha pauni milioni 25 (sh. bilioni 40) kumnyakua beki huyo.

Mabingwa hao wa Hispania pia walipanga kumsajili Thiago Silva kutoka Paris St Germain, lakini wameamua kubwaga manyanga kutokana na malipo ya ada ya uhamisho kuwa makubwa.

Barcelona pia imekuwa ikimuwinda beki chipukizi, Marquinhos kutoka AS Roma ya Italia, lakini ameamua kubaki nchini humo kwa msimu mmoja zaidi.

Mchezaji mwingine, ambaye Chelsea imeonyesha dhamira ya kumsajili ni beki Krygiakos Papadopoulos wa klabu ya Schalke ya Ujerumani, ambaye pia anawaniwa na Liverpool ya England.

Mourinho pia ni shabiki mkubwa wa mchezaji Raphael Varane wa Real Madrid ya Hispania, lakini huenda akakumbana na kikwazo katika kumsajili kutokana na uondokaji wake katika klabu hiyo kutawaliwa na mizengwe.

Real Madrid imepanga kukipangua kikosi chake kilichokuwa kikinolewa na Mourinho kwa kumuuza beki Pepe na kumbakisha Varane. Tayari Manchester City imeonyesha dhamira ya kumsajili Pepe.

No comments:

Post a Comment