KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, May 21, 2013

NGASA ATUA YANGA KWA MIL 30/-




HATIMAYE mshambuliaji Mrisho Ngasa wa klabu ya Simba ametia saini
mkataba wa miaka miwili wa kuitumikia klabu yake ya zamani ya Yanga
kwa ajili ya michuano ya ligi kuu na kimataifa.

Japokuwa viongozi wa Yanga hawakuwa tayari kutaja kiwango cha pesa
walichomlipa mchezaji huyo, kuna habari kuwa, Ngasa amechota zaidi
ya sh. milioni 30 na atakuwa akilipwa mshahara wa sh. milioni tatu
kwa mwezi.

Mara baada ya kutambulishwa kwa waandishi wa habari jana makao
makuu ya klabu hiyo, mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam,
Ngasa alisema amefurahi kurudi nyumbani.

Ngasa alisema amekubali kutia saini mkataba na Yanga kwa sababu ana
mapenzi na klabu hiyo, aliyokuwa akiichezea kabla ya kujiunga na
Azam.

"Nimefurahi kurejea katika klabu, ambayo naipenda. Nilicheza Simba
kwa ajili ya kazi tu na nilicheza kwa nguvu zangu zote ili kupata
ushindi, lakini hawakuwa na imani na mimi,"alisema.

Ngasa aliwasili makao makuu ya Yanga akiwa amefutana na Mwenyekiti
wa Yanga, Yussuf Manji, Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano, Abdalla
Bin Kleb, mjumbe wa kamati ya usajili, Seif Ahmed 'Magari' na
mjumbe wa baraza la wadhamini, Francis Kifukwe.

Bin Kleb alisema ujio wa mchezaji huyo utaiongezea nguvu Yanga na
kwamba walimsaka mchezaji huyo kwa miezi sita kabla ya kufanikiwa
kumshawishi arejee nyumbani.

Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako alisema Ngasa ni
mchezaji mahiri nchini hivyo kurejea kwake Yanga ni faraja kubwa
kwa klabu hiyo.

Ngasa alijiunga na Yanga kwa mara ya kwanza 2006 akitokea Kagera
Sugar, ambayo ilimsajili kutoka Toto Africans. Mshambuliaji huyo
alikwenda kufanya majaribio ya kucheza soka ya kulipwa katika klabu
ya West Ham, 2009 kabla ya kwenda kujaribiwa Seattle Sounders ya
Marekani.

No comments:

Post a Comment