KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 23, 2013

MICHO KOCHA MPYA THE CRANES


KAMPALA, Uganda
SHIRIKISHO la Soka la Uganda limemteua Milutin 'Micho' Sredojevic kuwa kocha mkuu mpya wa timu ya taifa ya nchi hiyo, The Cranes.

Micho (43) anachukua nafasi ya kocha wa zamani wa timu hiyo, Bobby Williamson, ambaye mkataba wake ulikatishwa mwezi uliopita.

Habari kutoka ndani ya shirikisho hilo zimeeleza kuwa, Micho ametia saini mkataba wa kuifundisha timu hiyo kwa miaka miwili.

Micho, ambaye alitimuliwa kuifundisha timu ya taifa ya Rwanda mwezi uliopita, alilieleza Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) juzi kuwa, amefurahi kurejea katika nchi, ambayo alianza kufundisha soka kwa mara ya kwanza barani Afrika.

"Ndoto yangu ya kufundisha soka Afrika ilianzia 2001 nchini Uganda katika klabu ya Villa na nilikaa kule kwa miaka mitatu. Katika miaka minane iliyopita, nilifundisha soka Ethiopia, Sudan, Afrika Kusini, Tanzania na Rwanda. Na sasa nimerejea nyumbani nilikoanzia,"alisema.

Micho alisema amejipanga vizuri kufanya kila analoweza kuipatia mafanikio Uganda katika michuano mbalimbali itakayoshiriki.

"Nataka kuendelea kukuza kiwango cha soka cha Uganda na kuiwezesha kufuzu kucheza fainali za Afrika. Nahisi nakwenda nyumbani, ambako wachezaji wananielewa vyema na kwenye utamaduni ninaoufahamu,"alisema kocha huyo.

Micho alisema anawaelewa vyema wachezaji wa Uganda kutokana na kucheza soka ya kiwango, hivyo anachohitajika kukifanya ni kuongeza kiwango chao.

Alisema Uganda haijafuzu kucheza fainali za Afrika tangu 1978 hivyo jukumu lake kubwa litakuwa ni kuwashawishi wachezaji wawe na dhamira hiyo.

Micho alisema haendi Uganda kutafuta pesa bali kuwasaidia wachezaji na timu ya taifa ya nchi hiyo katika kupata mafanikio na anaamini mchango wake utafanikisha azma yake hiyo.

Rais wa Shirikisho la Soka la Uganda, Lawrence Mulindwa alisema makocha 37 walituma maombi ya kutaka kuifundisha timu hiyo na kusisitiza kuwa, Micho atapewa kila anachokihitaji katika kufanikisha kazi yake.

Kwa mujibu wa Mulindwa, Micho atasaidiwa na Sam Timbe na Kefa Kisala wakati Fred Kajoba atakuwa kocha wa makipa.

Micho aliiongoza Villa kutwaa mataji matatu ya ligi kuu ya Uganda, aliiongoza St George ya Ethiopia kutwaa ubingwa wa nchi hiyo mara moja na pia kuiongoza Orlando Pirates kutinga nusu fainali ya ligi ya mabingwa wa Afrika 2006.

Kocha huyo pia aliiwezesha Al Hilal ya Sudan kufuzu kucheza hatua ya makundi ya michuano ya ligi ya mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho kwa miaka minne mfululizo.

No comments:

Post a Comment