KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 23, 2013

KAMPUNI MBILI ZAIDI KUDHAMINI LIGI KUU



KAMPUNI mbili zinazomiliki vituo vya televisheni zimeanza kufanya mazungumzo na kamati ya ligi kuu ya Tanzania Bara kwa ajili ya kudhamini ligi hiyo msimu ujao.

Hayo yalisemwa jana na Mwenyekiti wa kamati hiyo, Wallace Karia alipokuwa akizungumza na gazeti hili mjini Dar es Salaam.

Wallace alisema katika makubaliano hayo, kampuni hizo zinataka kuonyesha mechi za ligi hiyo moja kwa moja kwenye luninga ili mashabiki wengi zaidi waweze kuzishuhudia.

Kwa mujibu wa Karia, katika makubaliano hayo, klabu za ligi kuu zitakuwa zikilipwa kutokana na mechi zao kuonyeshwa moja kwa moja kwenye luninga.

Hata hivyo, Karia hakuwa tayari kutaja majina ya kampuni hizo kwa madai kuwa ni mapema kufanya hivyo. Lakini alidokeza kuwa, kituo kimoja ni cha nje na kingine cha hapa nyumbani.

"Lengo la kamati yetu ni kuhakikisha kuwa, msimu ujao timu zote zitakazoshiriki katika ligi, zinapata udhamini wa uhakika kwa lengo la kuongeza ushindani,"alisema Karia.

Mbali na kampuni hizo, Karia alisema lengo la kamati yake ni kuhakikisha kuwa, ligi hiyo inakuwa na wadhamini wengi ili timu ziweze kunufaika.

Timu zinazotarajiwa kushiriki katika ligi kuu msimu ujao ni Yanga, Azam, Simba, Mtibwa, Ruvu Shooting, JKT Ruvu, Prisons, Coastal Union, JKT Mgambo, JKT Oljoro, Kagera Sugar, Ashanti,Rhino Rangers na Mbeya City.

Wakati huo huo, Kampuni ya Simu za Mkononi ya Vodacom imeomba kusogeza mbele tarehe ya utoaji wa zawadi kwa washindi wa ligi kuu ya Tanzania Bara msimu huu.

Mwenyekiti wa kamati ya ligi, Wallace Karia alisema jana kuwa, tarehe mpya ya utoaji wa zawadi hizo itatangazwa baadaye.

Awali, Vodacom ilipanga kukabidhi zawadi hizo kwa washindi mwishoni mwa wiki hii. Bingwa wa ligi hiyo atapata sh. milioni 70, wa pili sh. milioni 35, wa tatu sh. milioni 25 na wa nne sh. milioni 20.

Zawadi zingine ni ya kipa bora wa mwaka na mfungaji bora, ambao watazawadiwa sh. milioni tano kila mmoja wakati mwamuzi bora na kocha bora watapata sh. milioni 7.5 kila mmoja.

No comments:

Post a Comment