KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, May 30, 2013

MNIGERIA AFUNIKA SIMBA



KIUNGO mkabaji Izdore Modebe kutoka Nigeria jana alikuwa kivutio kikubwa kwa makocha Abdalla Kibadeni na Jamhuri Kihwelo wa Simba wakati wa mazoezi yaliyofanyika kwenye uwanja wa Kinesi, Ubungo, Dar es Salaam.

Katika mazoezi hayo yaliyofanyika asubuhi na kushuhudiwa na mashabiki wachache wa Simba, Modebe alikuwa kivutio kikubwa kutokana na kuonyesha uwezo wa hali ya juu wa kumiliki mpira, kutoa pasi na kukaba.

Modebe amekuja nchini kufanya majaribio ya kusajiliwa na Simba, akitokea klabu ya Udense FC ya Benin. Kabla ya kwenda Benin, alikuwa akichezea klabu ya Kwao ya Nigeria.

Akizungumza wakati wa mazoezi hayo, Kocha Msaidizi wa Simba,Kihwelo alisema wametenga muda wa wiki moja kwa ajili ya kuwajaribu wachezaji wapya.

Kocha huyo, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Julio alisema, wachezaji waliojitokeza ni wazuri na wapo katika kiwango kizuri, lakini alimmwagia sifa zaidi Modebe.

Alisema mchezaji huyo yuko katika kiwango kizuri na kama ataendelea hivyo katika kipindi chote cha majaribio, anaweza kulamba karata dume na kusajiliwa.

Hata hivyo, Julio alisema benchi la ufundi la Simba haliwezi kukurupuka katika kufanya usajili wa wachezaji wapya kwa vile baadhi yao hufanya vizuri wakati wa majaribio na kuvurunda baada ya kusajiliwa.

Julio alisema mazoezi hayo ni sehemu ya maandalizi ya Simba kabla ya kushiriki katika michuano ya Kombe la Kagame, inayotarajiwa kuanza Juni 18 hadi Julai 2 mwaka huu nchini Sudan.

Wachezaji wengine wanaofanyiwa majaribio na Simba ni Joe Fils, Fabian Tsshiyaz, Fabrice Baloko kutoka klabu ya Vita ya Lubumbashi na Patrick Milambo kutoka Nguena FC ya Lumbumbashi nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.

Wengine ni Mohamed Abdallah (Ferreviariode Nampula,Msumbiji), Adeyun Saleh (Miembeni), Shaaban Kondo (Mbagala Jack Sports Academy), Rashid Salum (New Boko ya Zanzibar), Ramadhan Kipiala (Buza), Shaaban Saidi (Boom FC) na Samuel Ngassa mchezaji wa zamani wa African Lyon.

Mbali na wachezaji hao, kuna habari pia kuwa, Simba imekamilisha mipango ya kumsajili mwanasoka wa kimataifa wa Uganda, Samuel Ssenkoomi anayechezea timu ya URA.

Habari za uhakika kutoka ndani ya Simba zimeeleza kuwa, Ssenkoomi ametia saini mkataba wa miaka miwili wa kuichezea klabu hiyo.

Beki huyo anakuwa mchezaji wa tano mpya kusajiliwa na Simba kwa ajili ya msimu ujao, baada ya awali kusajiliwa wachezaji wanne wazawa, kipa Andrew Ntalla kutoka Kagera Sugar, beki Issa Rashid ‘Baba Ubaya’ kutoka Mtibwa Sugar, kiungo Twaha Shekuwe ‘Messi’ kutoka Coastal Union na mshambuliaji Zahor Pazi kutoka Azam FC aliyekuwa anacheza kwa mkopo JKT Ruvu.

No comments:

Post a Comment