KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, March 30, 2011

Yanga yanusa ubingwa

TIMU ya Yanga imeongeza kasi ya kuwania kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom msimu huu, baada jana kuibanjua Azam FC mabao 2-1 katika mechi iliyokuwa na upinzani mkubwa iliyochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam. Matokeo hayo yamezidisha presha kwa Simba inayoshika usukani wa ligi hiyo kwani, Yanga sasa imefikisha pointi 43 ikibaki nafasi ya pili kwa kupitwa alama mbili na Simba. Timu hizo zote zimecheza mechi 20 na imebaki michezo miwili ligi kumalizika. Mshambuliaji John Bocco 'Adebayor' wa Azam FC alianza kutikisa nyavu za Yanga katika dakika ya nne ya mchezo huo baada ya kuunasa mpira kutoka kwa beki Chacha Marwa na kufunga bao kwa kumchambua kipa Ivan Knezevic.Kufungwa bao hilo kuliwaamsha Yanga ambao walilisakama lango la Azam kama nyuki na katika dakika ya 12 Jerry Tegete alikosa goli kutokana na shuti alilopiga kugonga mwamba na mpira kuokolewa na mabeki baada ya kurudi uwanjani. Tegete alifanya shambulizi hilo baada ya kupokea mpira wa krosi iliyopigwa na Davis Mwape, huku mchezaji huyo akikosa tena goli dakika ya 38 kufuatia shuti lake la mpira uliorushwa na Fred Mbuna, kupanguliwa na kipa wa Azam Vladimir Niyonkuru na kuwa kona butu.Dakika tatu kabla ya mapumziko Tegete aliisawazishia Yanga kwa mpira wa shuti kali baada ya kuunganisha krosi ya Shadrack Nsajigwa, huku mchezaji huyo akiwa shujaa kwa wana Jangwani baada ya kuongeza bao la pili dakika ya 60 kwa kuunganisha wavuni mpira uliotemwa na kipa Niyonkuru kufuatia kutema shuti kali la Davis Mwape.Kuingizwa kwa Kally Ongala kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Suleiman Kassim kulisaidia kuiimarisha Azam FC upande wa kiungo, lakini washambuliaji walishindwa kukwamisha mipira wavuni ikiwemo dakika ya 83, ambayo Boko apiga kichwa mpira na kutoka nje.Mrisho Ngasa, Tegete, na Nurdin Bakari walionyeshwa kadi za njano kwa utovu wa nidhamu.Akizungumzia matokeo hayo kocha wa Yanga, Sam Timbe, alisema kuwa wataendelea kupigana mpaka mechi ya mwisho kuwania ubingwa, huku kocha wa Azam, Stewart Hall akisema wamepoteza mchezo huo kwa sababu baadhi ya wachezaji wake tegemeo majeruhi na wengine wanasumbuliwa na uchovu wa safari ya timu ya taifa ya vijana iliyokwenda jijini Yaounde wiki iliyopita kucheza na Cameroon.Yanga: Ivan Knezevic, Shadrack Nsajigwa, Stephano Mwasika, Nadir Haroub 'Cannavaro', Chacha Marwa, Juma Seif/ Omega Seme, Fred Mbuna, Nurdin Bakari, Davis Mwape, Jerry Tegete, Kigi Makasi.Azam FC: Vladimir Niyonkuru, Ibrahim Shikanda, Malika Ndeule/Himid Mao, Erasto Nyoni, Aggrey Morris, Mutesa Mafisango, Mrisho Ngasa, Jabir Aziz, John Boko 'Adebayor', Ramadhani Chombo, Suleiman Kassim/Kally Ongala.

Dede achomoza na vibao viwili vipya


MWIMBAJI nyota wa bendi ya muziki wa dansi ya Msondo Ngoma, Shaabani Dede ameibuka na vibao viwili vipya, vitakavyojumuishwa kwenye albamu mpya ya bendi hiyo. Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Dede alivitaja vibao hivyo kuwa ni ‘Vita dhidi ya dawa za kulevya’ na ‘Suluhu’. Dede alisema vibao hivyo ni zawadi aliyowaandalia mashabiki wa Msondo Ngoma baada ya kurejea kwenye bendi hiyo wiki mbili zilizopita. Mwimbaji huyo mkongwe alirejea Msondo Ngoma akitokea bendi ya Mlimani Park Orchestra, ambayo alidumu nayo kwa zaidi ya miaka 20. Wakati huo huo, Meneja wa Msondo Ngoma, Saidi Kibiriti amesema wameamua kuiimarisha zaidi bendi hiyo kwa kumsaka mpuliza saxaphone mpya. Kibiriti alisema tangu Shabani Lendi alipoamua kurejea kwenye bendi yake ya zamani ya Mlimani Park, wamekuwa wakipiga nyimbo zao bila kutumia ala hiyo. Alisema kwa sasa wamepanga kufanya maonyesho ya kumtambulisha Dede mikoani ili kuwadhihirishia mashabiki wao kwamba bendi hiyo bado ipo imara. Kibiriti alisema tayari wameshafanya ziara mkoani Tanga na mwishoni mwa wiki hii watatembelea Ikwiriri mkoani Pwani. “Kama nilivyosema awali, lengo letu kubwa ni kumtambulisha Dede pamoja na vibao vyetu vipya, vilivyomo kwenye albamu yetu mpya, tutakayoizindua baadaye mwaka huu,”alisema.

Studio hii ni ya wote-JK

RAIS Jakaya Kikwete amewataka wasanii wa muziki wa kizazi kipya nchini kuacha malumbano kuhusu umiliki wa studio aliyowafungulia kwa ajili ya kuendeleza vipaji vyao. Kauli hiyo ilitolewa wiki hii na Mkurugenzi wa Idara ya Utamaduni wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Angela Ngowi katika Jukwaa la Sanaa lililofanyika kwenye ofisi za Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) mjini Dar es Salaam. Akizungumza kwa niaba ya Rais Kikwete, Angela alisema ni wajibu wa kila msanii kuelewa kuwa, wote wanaruhusiwa kuitumia studio hiyo kwa kuwasilisha maombi mapema. Angela alisema Rais Kikwete ametoa tamko hilo kwa maandishi, kufuatia kuzuka kwa malumbano miongoni mwa wasanii kuhusu ni nani anayestahili kuisimamia studio hiyo. Akinukuu tamko hilo la Rais Kikwete, Angela alisema: “Nimetoa vifaa vya mastering studio kwa ajili ya wasanii walioomba kwangu kupitia risala, hata hivyo wasanii wote wanaruhusiwa kuitumia na ikiwa kuna yeyote anahitaji, anapaswa kuleta maombi yake.” Tamko hilo lilisababisha mtafaruku kwa baadhi ya wasanii katika jukwaa hilo, akiwemo Mbunge wa Mbeya Mjini (CHADEMA), Joseph Mbilinyi, ambaye alisema wasanii wananyonywa na kutumiwa kisiasa. Mbilinyi alisema ni vyema studio hiyo ingekabidhiwa kwa Kampuni ya Tanzania Fleva Unit bila kupitia BASATA ili iweze kutumiwa na wasanii wote. "Hili suala limeendeshwa kisiasa zaidi, hatutaki kutumika kisiasa, ninashindwa kuelewa ni kwa sababu gani vyombo hivyo visingefikishwa BASATA au vingepitia wizarani," alisema Mbilinyi. "Katika hotuba yake bungeni, Rais Kikwete alisema kuwa kilio cha wasanii amekisikia na sasa tunaambiwa, eti amewapa wale walichokihitaji, sasa mbona hiyo studio hatuioni na tunaambiwa leo amewapa walioomba?" alihoji mbunge huyo. Katibu Mtendaji wa Basata, Ghonche Materego alisema anaheshimu tamko la Rais Kikwete na kuongeza kuwa malumbano kwa wasanii hayana tija. "Nadhani suala ambalo lilikuwa likituchanganya kwa muda mrefu limepatiwa ufumbuzi, hivyo tamko limetolewa tayari na sidhani kama kuna haja ya kuendeleza malumbano," alisema. Msemaji wa Tanzania Fleva Unit, Said Fella, ambaye ndiye aliyewakilisha umoja huo, unaomiliki vyombo hivyo mpaka sasa, alisema waliamua kumuengua Ruge Mutahaba katika usimamizi wa vifaa hivyo kutokana na migogoro iliyokuwa ikiendelea. "Ni muda mrefu tangu tukabidhiwe vifaa hivyo, lakini migogoro ilikuwa haiishi, tuliamua kumuengua Ruge katika usimamizi ili tuweze kufungua studio hii na hivi sasa tumeshasajili kampuni hii Basata" alisema Fela.

SIMBA: Lazima tuivue ubingwa TP Mazembe

WACHEZAJI wa timu ya soka ya Simba wamejigamba kuwa, lazima waifunge TP Mazembe kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na kusonga mbele katika michuano ya klabu bingwa Afrika. Wakizungumza na Burudani mjini Dar es Salaam juzi, wachezaji hao walisema wamepania kuishinda TP Mazembe na kuweka rekodi ya kuivua ubingwa wa Afrika. Majigambo hayo ya Simba yamekuja siku chache baada ya timu hiyo kubanwa mbavu na Kagera Sugar kwa kulazimishwa kutoka nayo suluhu katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara, iliyochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam. Simba na TP Mazembe zinatarajiwa kurudiana Jumapili katika mechi ya raundi ya pili, itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Katika mechi ya awali, iliyochezwa wiki iliyopita mjini Lubumbashi, TP Mazembe iliichapa Simba mabao 3-1. Ili isonge mbele, Simba italazimika kushinda mechi hiyo kwa mabao 2-0. Akizungumzia mechi hiyo, kiungo Mohamed Banka alisema wamedhamiria kupambana kufa au kupona ili kushinda mechi hiyo na kusonga mbele. Banka alisema iwapo Simba iliweze kuivua ubingwa Zamalek mwanzoni mwa miaka ya 1990, haoni kwa nini washindwe kufanya hivyo kwa TP Mazembe. “Ni kweli tumeshindwa kucheza vizuri dhidi ya Kagera Sugar leo (juzi), lakini ni kwa sababu ya mazoezi magumu tuliyopata kutoka kwa makocha wetu. Tuna hakika Jumapili tutakuwa fiti kabisa,”alisema. Beki Amir Maftah alisema, wameshazifahamu vyema mbinu zote za wapinzani wao, hivyo ushindi katika mechi hiyo ni kitu cha lazima. Maftah alisema wana imani kubwa ya kushinda mechi hiyo kwa vile watakuwa wakicheza kwenye uwanja wao wa nyumbani na mbele ya mashabiki wao. “TP Mazembe waje tu, lakini wajue wazi kwamba lazima wafe,”alijigamba beki huyo wa zamani wa Yanga. Kiungo Patrick Ochan kutoka Uganda aliisifu TP Mazembe kwamba ni timu nzuri, lakini alijigamba kuwa, haina nafasi ya kushinda tena mechi ya marudiano. Alisema moja ya mapungufu waliyoyabaini katika kikosi cha TP Mazembe ni ubutu wa safu yake ya ulinzi, hivyo wamejiandaa vyema kuutumia ili kupata ushindi. Ochan alisema watajihidi kuingia eneo la wapinzani wao mara kwa mara ili kuwachosha mabeki wao na hatimaye kufunga mabao ya kushtukiza. Kipa Juma Kaseja alisema, licha ya kufungwa katika mechi ya awali, bado hawajakata tamaa kwa vile nafasi ya ushindi kwao ni kubwa. Amewataka mashabiki wa Simba kujitokeza kwa wingi kushuhudia mechi hiyo kwa vile watapata burudani, ambayo hawataisahau kwa muda mrefu. Alisema uzuri wa TP Mazembe hauwezi kuwakwaza kwa vile katika soka lolote linaweza kutokea, lakini cha msingi ni wachezaji kucheza kwa ari na kujituma. Mshambuliaji Emmanuel Okwi alisema wamepania kuifunga TP Mazembe kwa sababu ni timu ya kawaida na wana uwezo wa kuimudu. Hata hivyo, Okwi alisema ili waweze kufanikisha azma yao hiyo, wanapaswa kucheza kwa kujituma na kutambua majukumu yao uwanjani. “TP Mazembe ni timu ya kawaida tu, tuliwakimbiza sana kipindi cha pili kule kwao, kama tukifanya hivyo Jumapili, sioni kwa nini tushindwe kuwafunga,”alisema.

Gurumo alazwa tena Muhimbili


KIONGOZI wa bendi ya muziki wa dansi ya Msondo Ngoma, Muhidin Gurumo amelazwa tena kwenye Hopitali ya Taifa ya Muhimbili mjini Dar es Salaam baada ya hali yake kuwa mbaya. Gurumo alifikishwa kwenye hospitali hiyo jana saa moja asubuhi akiwa mahututi na kuna habari kuwa, alilazwa kwa muda kwenye chumba cha wagonjwa mahututi. Meneja wa bendi hiyo, Saidi Kibiriti alithibitisha jana kulazwa kwa mwanamuziki huyo kwenye hospitali hiyo, lakini hakuwa tayari kuzungumzia afya yake kiundani. “Ni kweli Mzee Gurumo amelazwa tena hapa Muhimbili na mimi ndio kwanza nafika hapa, sijapata nafasi ya kumuona, hivyo siwezi kujua nini kinamsumbua,”alisema. Kibiriti alisema alipata taarifa za kupelekwa kwa Gurumo kwenye hospitali hiyo kutoka kwa ndugu zake wa karibu, lakini hawakumweleza kilichomsibu. Hii ni mara ya pili kwa Gurumo kulazwa hospitali ya Muhimbili. Mara ya kwanza ilikuwa Februari mwaka huu, alipokuwa akisumbuliwa na homa ya kwenye mapafu. Licha ya kuruhusiwa kutoka hospitali, Gurumo alikuwa akikabiliwa na tatizo la kutembea, ambapo alikuwa akisaidiwa kufanya hivyo na mkewe. Mwanamuziki huyo mkongwe alikuwepo kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee mjini Dar es Salaam wakati Msondo Ngoma ilipofanya onyesho la pamoja na Mlimani Park Orchestra wiki mbili zilizopita.

Friday, March 25, 2011

SERIKALI KUISAIDIA FIVE STARS MODERN TAARAB


SERIKALI imetoa tamko la kusaidia kupatikana kwa wanamuziki wengine watakaounda kundi la taarabu la Five Stars Modern Taarab baada ya wanamuziki 13 wa kundi hilo kupoteza maisha katika ajali iliyotokea hivi karibuni mkoani Morogoro.

Akizungumza katika dua ya kuwaombea wanamuziki hao juzio katika hoteli ya Starlight, Naibu Waziri wa Habari, Vijana Utamaduni na Michezo Dr Fenela Mukangara alisema vijana wasikate tamaa baada ya vijana hao kupoteza maisha katika ajali hiyo.

Mukangara alisema serikali katika jitihada za kufanikisha azma hiyo, watajitahidi kuwasiliana na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kuzipiga nyimbo za kundi hilo na kusaidia kuuza kazi zilizofanywa na kundi hilo.

Alisema Serikali itaendelea kuwapa ushirikiano kwa muda wote viongozi na familia za marehemu waliokumbwa na msiba huo hapa nchini na pia watajipanga kuwasaidia vyombo kundi hilo kwa kushirikiana na wadau wa muziki.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Henry Clemence alitoa wito kwa wasanii kutunga tungo za kupigia kelele madereva wazembe kwa sababu ajali ndio mojawapo ya matukio yanayomaliza Watanzania wengi.

Clemence ambaye pia ni mwenyeji wa wanachama wa Taasisi ya Wasanii Tanzania (SHIWATA), Wilayani Mkuranga alisema pengo la wanamuziki hao halitozibika.

Mwenyekiti wa Shiwata, Taalib Cassim alitoa shukrani kwa viongozi wa Serikali kwa kuonyesha kuwajali wasanii ambapo asilimia kubwa ya viongozi wa serikali kupitia Wizara walihudhuria katika dua ya kuwaombea marehemu waliofariki katika ajali hiyo.

Cassim alisema Shiwata inawapenda viongozi wa Serikali kwa kuonyesha kuguswa na tukio hilo ambalo limetingisha Taifa.Viongozi waliohudhuria katika dua hiyo ni pamoja na Mkurugenzi wa Utamaduni, Profesa Hermas Mwansoko, Msaidizi wake Anjela Ngowi, Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) Ghonche Materego na wadau mbalimbali wa sanaa.

UCHEZAJI GANI HUU YARABII!


LICHA ya Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) kupiga marufuku wacheza shoo wa bendi za muziki wa dansi kucheza nusu uchi, amri hiyo inaelekea kukiukwa ama kutokuwa na makali yoyote. Pichani mcheza shoo wa bendi ya Msondo Ngoma akiselebuka stejini wakati bendi hiyo ilipokuwa ikipambana na Mlimani Park kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam wiki iliyopita. Viongozi wa BASATA mpo? Kazi kwenu. (Picha na Mohamed Issa wa Uhuru)

KWA NINI WAIMBAJI WA KIKE BONGO HAWADUMU?

LUIZA Mbutu
NYOTA Kinguti

LADY JayDee


Janet Isinike

Amina Remy


Amina Ngaluma

MUZIKI wa dansi una historia ndefu hapa nchini. Ulianza kupigwa tangu miaka ya 1950, lakini idadi kubwa ya wanamuziki katika miaka hiyo ilikuwa ni wanaume. Ni wanawake wachache sana waliojitokeza katika fani hiyo wakati huo.
Mabadiliko yalianza kujitokeza mwanzoni mwa miaka ya 1980, ambapo walijitokeza waimbaji wengi wa kike, ambao waliongezea ladha na utamu wa muziki, hasa kutokana na sauti zao maridhawa na miondoko yao stejini.
Kujitokeza kwao kuliwafanya mashabiki wengi wa muziki waanze kuamini kwamba, mambo yangeanza kuwa murua kwenye kumbi za burudani. Hiyo ilitokana na ukweli kwamba, sauti za waimbaji wa kike ni kachumbari tosha katika muziki wa aina yoyote.
Huenda pia waliamini hivyo kutokana na ukweli kwamba kwa miaka kadhaa iliyopita, kabla ya miaka hiyo ya 1980, muziki huo, hasa kwenye uimbaji, ulikuwa umetawaliwa zaidi na wanaume, hata kama nafasi ya uimbaji ilipendeza zaidi kuwakilishwa na mwanamke.
Ni kuanzia hapo ndipo walipoanza kujitokeza baadhi ya waimbaji wa kike waliong’ara na kujipatia sifa na umaarufu katika kila pembe ya Tanzania. Miongoni mwao alikuwepo Tabia Mwanjelwa, aliyeng’ara katika bendi ya Maquiz Original.
Waimbaji wengine wa kike waliojitokeza wakati huo ni pamoja na Nana Njige, aliyekuwa bendi ya Magereza, Rukia Mtama, aliyekuwa akimiliki bendi ya Ram Choc, Emma Mkelo, aliyekuwa bendi ya Super Rainbow na Kida Waziri , aliyekuwa Vijana Jazz.
Vilevile walikuwepo Nyota Kinguti, aliyekuwa Bicco Stars na sasa yupo The Kilimanjaro, Betty Enock, ambaye alipotelea Arabuni na Titty Shang, ambaye aling’ara kwa muda mfupi katika bendi ya Lulu Orchestra.
Pamoja na kujitokeza kwa waimbaji wengi wa kike, matarajio waliyokuwa nayo mashabiki wa muziki wa dansi yalianza kufifia kutokana na baadhi yao kushindwa kudumu muda mrefu katika bendi walizokuwa wakiimbia na wakati mwingine kushindwa kuimba katika hali ya kuvutia.
Baadhi yao baada ya kung’ara kwa kipindi kifupi, walitoweka wasijulikane mahali walipo. Na kwa wale walioendelea na muziki, walishindwa kung’ara na kufikia viwango vya waimbaji wenzao waliong’ara barani Afrika kama vile Mbilia Bel, Tshala Muana, Yvonne Chakachaka na wengineo.
Katika nyimbo nyingi za muziki wa dansi zilizoimbwa na waimbaji wa kike, baadhi yao walishindwa kuimba kwa sauti kike hasa. Sauti zao zilikuwa hazina utamu na mvuto wowote masikioni mwa mashabiki.
Zipo sababu nyingi zilizowafanya waimbaji hao wa kike kushindwa kudumu katika bendi zao kwa muda mrefu ama kutokuwa na maendeleo ya kuridhisha. Na mara nyingi walikuwa wakizua sokomoko kubwa katika bendi zao kiasi cha kuzifanya baadhi kudiriki kutamka bayana kwamba hazihitaji tena wanamuziki wa kike.
Dosari moja kubwa, ambayo ilionekana kujitokeza sana kwa waimbaji wa kike ni kujihusisha zaidi kimapenzi na wanamuziki wenzao, hasa viongozi. Tabia hiyo ilikuwa ikizua matukio mengi, si kwa waimbaji wa kike tu, bali hata wenzao wa kiume.
Mara nyingi iliwahi kutokea mwanamuziki wa kike alipojihusisha kimapenzi na kiongozi wa bendi, alijiona yupo matawi ya juu na kuwadharau wenzake. Aliweza kufanya anavyotaka, kutozingatia mazoezi na pia ilikuwa si ajabu kwake kufika mazoezini wakati anaotaka.
Hata hivyo, uzuri wa wanamuziki hao wa kike nao ulichangia kuwaponza, kwani mara nyingi ilipotokea baadhi yao kung’ara kimuziki, kila mwanaume alitaka kumtongoza. Awe mwanamuziki, mfanyabiashara au mtu wa kawaida, kila mmoja alitaka ampate kimapenzi.
Wakati mwingine, baadhi ya wanamuziki hao wa kike waliamua kuacha kabisa muziki na kuamua kuolewa pale ilipotokea mwanaume wake kumkataza kuendelea kujihusisha na fani hiyo. Matokeo yake ni kwamba wengi wa wanamuziki hao wa kike walikuwa hawadumu katika bendi zao.
Pamoja na hayo, sio siri kwamba waimbaji wengi wa kike wakati huo hawakuwa wakitilia maanani kazi ya muziki. Wengi walikuwa wakiuchukulia muziki kuwa ni kazi ya kihuni, hivyo mara nyingi kusababisha hata wao wenyewe wasijiheshimu.
Hali hiyo ilisababisha wanawake wengi wenye vipaji vya uimbaji kuhofikia kujitokeza hadharani ama kukatishwa tamaa kutokana na falsafa kwamba muziki ni uhuni.
Pengine ni vyema kwa wakati huu tulionao, wanamuziki wa kike waanze kubadilika kwa kuelewa wajibu wao katika suala zima linalohusu muziki. Wasiichukulie fani hiyo kuwa ni ya kihuni. Hizo dosari zilizokuwa zikijitokeza mara kwa mara juu yao inafaa ziepukwe.
Mwanamuziki pekee wa kike, ambaye hadi sasa anastahili kupongezwa kutokana na kudumu kwenye fani kwa miaka mingi ni Nyota Kinguti. Tangu alipoanza muziki akiwa Bicco Stars na sasa The Kilimanjaro, Nyota hajawahi kutetereka na uwezo wake kimuziki umekuwa ukiongezeka badala ya kushuka.
Waimbaji wengine wa kike, ambao angalau wamejitahidi kudumu kwenye fani hiyo kwa kipindi kirefu ni Luiza Mbutu, Khadija Mnoga na Janet Isinike wa Twanga Pepeta na Amina Ngaluma, ambaye kwa sasa yupo Arabuni na Judith Wambura ‘Lady JayDee’ anayemiliki bendi ya Machozi.
Wapo wanamuziki wengine wa kike wanaopiga muziki wa kizazi kipya, lakini hawapaswi kulinganishwa na wenzao wa dansi kwa vile muziki wao unatengenezwa zaidi kwa kutumia njia ya kompyuta. Hawapigi muziki wa dansi ambao ni laivu kwenye steji.
Ni vyema wanamuziki wa kike nchini kutambua kuwa, wanapaswa kuwa na moyo wa uvumilivu na kutokata tamaa mapema kwani hakuna maendeleo ya ghafla na ya haraka.Wanapaswa kutilia maanani mazoezi na kujifunza mbinu za muziki zitakazowawezesha kutunga na kuimba kwa sauti tamu kama wanavyofanya wenzao wanaong’ara hapa Afrika.
Inafaa pia kwa wanamuziki wetu wa kike kuithamini kazi hiyo kwa kuiona kuwa sawa na zingine, tena isiyopaswa kuchezewa. Isiwe tu wanapotoka stejini, basi wanajiona na kazi ndio imekwisha.
Ni vyema pia kwa wanamuziki wetu wa kike kujiheshimu wakati wote. Iwapo watajiheshimu wawapo kwenye bendi zao, ni rahisi pia kwao kuheshimika kwa mashabiki.
Ieleweke kuwa, maendeleo ya wanamuziki wa kike na kung’ara kwao kimuziki, kutaamsha hamasa kwa wanawake wengi wenye vipaji kujitokeza, badala ya ilivyo hivi sasa, ambapo wengi wanasita kwa kuiona fani hiyo ni ya kihuni.

MWIMBAJI wa bendi ya muziki wa dansi ya Mlimani Park Orchestra, Hussein Jumbe akiserebuka na mcheza shoo wa bendi hiyo wakati wa onyesho dhidi ya Msondo Ngoma lililofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam. (Picha na Emmanuel Ndege).

Simba, TP Mazembe kurudiana mchana


MWENYEKITI wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage amesema mchezo kati yao na TP Mazembe utafanyika saa tisa mchana ili kuwachosha wapinzani wao.
Akizungumza na Burudani mwanzoni mwa wiki hii mjini Dar es Salaam, Rage alisema wameandaa mikakati kabambe ili kuhakikisha wanashinda mchezo huo na kusonga mbele.
Simba na TP Mazembe zinatarajiwa kurudiana wiki mbili zijazo katika mechi ya raundi ya pili ya michuano ya klabu bingwa Afrika. Katika mechi ya awali iliyochezwa wiki iliyopita mjini Lubumbashi, Simba ilichapwa mabao 3-1.
Ili iweze kusonga mbele katika michuano hiyo, Simba italazimika kuishinda TP Mazembe mabao 2-0 na kutowaruhusu wapinzani wao kupata bao la ugenini.
“Tuna hakika tukiwachezesha TP Mazembe katika muda huo, watachoka haraka na hiyo itatupa nafasi ya kushinda mechi hiyo kirahisi,”alisema Rage.
Mwenyekiti huyo wa Simba alisema hali ya hewa ya mji wa Lubumbashi ni ya baridi kali na ndio sababu waliamua kwenda kuweka kambi Arusha kujiandaa na pambano la awali.
Mbali na kutumia mbinu hiyo, Rage alisema wamepanga kuiandaa timu yao kikamilifu ili waweze kushinda mechi hiyo, ikiwa ni pamoja na kuwaongezea hamasa wachezaji.
“Tunawaomba mashabiki wetu wajitokeze kwa wingi katika mechi hiyo ili kuwaongezea hamasa wachezaji kwa sababu uwezo wa kushinda ni mkubwa,”alisema.
Rage alisema Simba inatarajiwa kuanza kambi kati ya leo na kesho kwa ajili ya kujiandaa na mchezo huo. Jana, mabingwa hao wa Tanzania Bara walitarajiwa kucheza mechi ya kirafiki dhidi ya Vijana Stars.

DAISY MUSHUMBUSI, Mrembo wa Utalii mwenye vipaji lukuki


KWA umri na umbo, Daisy Mushumbuzi anaonekana kuwa mdogo. Urefu wake hauzidi futi tano. Pia ni mwembamba na rangi yake ni nyeusi, ile ya asilimia. Ni mwenyeji wa mkoa wa Bukoba.
Daisy (24) ndiye aliyeibuka kuwa mshindi wa taji la kipaji katika shindano la Miss Utalii 2011 lililofanyika mwanzoni mwa mwezi huu kwenye hoteli ya Kiromo iliyopo Bagamoyo mkoani Pwani.
Isingekuwa kigezo cha urefu, pengine Daisy ndiye angeibuka mshindi wa taji hilo kwani ana uelewa wa hali ya juu kuhusu masuala mbalimbali duniani. Pia ana uelewa mkubwa wa masuala ya utalii kwa vile ni fani aliyoisomea.
Hata Mkurugenzi wa Kamati ya Miss Utalii, Gideon Chipungahelo anakiri juu ya ukweli huo kwa kusema, binti huyo ana akili za kipekee na kwamba kilichomwangusha ni umbo lake.
Daisy ana shahada ya usimamizi wa utalii aliyoipata katika Chuo Kikuu cha Moi kilichopo mjini Nairobi, Kenya. Ni mtoto wa nne katika familia ya watoto watano wa Mzee Mushumbuzi.
Akizungumza na Burudani mjini Dar es Salaam wiki hii, Daisy alisema alishawishika kushiriki kwenye mashindano hayo kwa vile fani hiyo ipo kwenye damu yake. Alisema alikuwa akipenda mambo ya utamaduni, hasa uchezaji ngoma tangu akiwa shule ya msingi.
“Binafsi nimesomea fani ya utalii, ni taaluma yangu na nimekuwa nikiipenda tangu nikiwa mdogo ndio sababu nilianza kushiriki kwenye shindano hili kuanzia ngazi ya mkoa wa Kagera,”alisema.
Daisy alisema amejifunza mengi kutokana na ushiriki wake katika mashindano hayo, ikiwa ni pamoja na kuufahamu vyema utalii wa ndani na kutembelea vivutio vinane vya utalii kati ya 16 vilivyopo nchini.
Mrembo huyo mwenye haiba ya kuvutia pia alisema ushiriki wake kwenye mashindano hayo umemwezesha kujifunza jinsi lugha ya Kiswahili ilivyoweza kuwaunganisha pamoja watanzania licha ya kuwepo na makabila zaidi ya 120.
Alisema amepanga kutumia taji lake la mrembo mwenye kipaji kuutangaza vyema utalii wa ndani ya nchi na pia kuwashawishi vijana wenzake wa kike kujitosa kwenye fani ya urembo na kuondokana na dhana kwamba ni ya kihuni.
Mrembo huyo anayependa kuogelea, kuimba na kucheza ngoma za kiasili alisema, ana hakika binadamu yoyote mwenye kipaji akikitumia vyema, ana uwezo mkubwa wa kufanikiwa katika maisha yake hivyo amewataka vijana wenzake wenye vipaji kujitokeza hadharani.
Aliyataja baadhi ya malengo yake ya baadaye kuwa ni pamoja na kuanzisha kikundi cha utamaduni na kuwafundisha vijana wenzake kucheza ngoma.
“Nitafanya mipango ili nishirikiane na BASATA kuimarisha sekta ya utamaduni kwa kuzifanya ngoma za na nyimbo za asili ziwe miradi tegemezi kwa kurekodiwa kwenye CD na kanda za video,”alisema.
Alisema pia kuwa, amepania kuendeleza kipaji chake cha ubunifu wa mavazi ili aweze kuwa mjasiliamali na kujiingizia kipato. Mbali na kubuni mavazi, ana uwezo mkubwa wa kutengeneza heleni za kiasili.
“Mungu akipenda nimepanga kuanzia kampuni ya utalii na nitaitumia kuendeleza sekta hii nchini. Pia nitashirikiana vyema na waandishi wa habari katika kuutangaza utalii wa ndani,”alisema.
Akimzungumzia mshindi wa shindano la mwaka huu la Miss Utalii, Adelqueen Njozi, mrembo huyo alisema alistahili kuvikwa taji hilo kutokana na kuwa na vigezo vyote vinavyotakiwa.
“Kwa kweli mshindi wa taji hilo ana sifa zote zinazotakiwa hivyo alistahili. Ana heshima, muelewa na ana uwezo mkubwa wa kuishawishi jamii,”alisema Daisy.
Aliongeza kuwa, ana hakika Adelqueen ana uwezo mkubwa wa kufanya vizuri katika shindano la dunia la Miss Utalii, linalotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu.
Ametoa mwito kwa wanawake wenye vipaji kujiamini na kujitokeza hadharani ili waweze kuvitumia kujipatia kipato cha kuendesha maisha yao.

WAREMBO WA UTALII WALIPOTINGA OFISI ZA UHURU

WAREMBO wa Miss Utalii wakiwa katika picha ya pamoja na Ofisa Utawala wa Kampuni ya Uhuru Publications Ltd, Rhoda Kangero walipotembelea ofisi za Uhuru mjini Dar es Salaam juzui

WAREMBO wa Miss Utalii wakisoma gazeti la Burudani walipotembelea katika ofisi za Uhuru juzi. Kushoto ni Mhariri wa Burudani, Rashid Zahor. Aliyeketi kulia ni mshindi wa taji la kipaji, Daisy Mushumbusi.



MWANDISHI wa habari wa gazeti la Burudani, Fred Majaliwa (kulia) akiwatambulisha warembo wa Miss Utalii kwa Mhariri wa Habari za Kimataifa wa gazeti la Uhuru, Noor Shija (aliyeketi).


MHARIRI wa Michezo wa gazeti la Uhuru, Mwadin Hassan (aliyeketi) akitoa maelekezo kwa warembo wa Miss Utalii.


MHARIRI Mtendaji wa Kampuni ya Uhuru Publications Ltd, Josiah Mufungo (kulia) akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na washindi watano wa kwanza wa shindano la kumsaka mrembo wa Utalii 2011 walipotembelea ofisi za Uhuru zilizopo barabara ya Lumumba mjini Dar es Salaam juzi
MHARIRI wa Habari wa gazeti la Uhuru, Ramadhani Mkoma (aliyeketi) akiwaonyesha warembo wa Miss Utalii jinsi habari zinavyopatikana kutoka mikoani kupitia mtandao wa kompyuta.

MENEJA Raslimali Watu wa Kampuni ya Uhuru Publications Ltd, Lucas Kisasa (kulia) akipeana mkono na mmoja wa washindi watano wa kwanza wa shindano la kumsaka mrembo wa Utalii walipotembelea ofisi za Uhuru mjini Dar es Salaam juzi.


WAREMBO wa Miss Utalii wakifuatilia kwa makini maelekezo waliyokuwa wakipewa na Msanifu Mkuu wa gazeti la Uhuru, Esta Mvungi (aliyeketi).

MHARIRI wa Makala wa gazeti la Uhuru, Epson Luhwago akitoa maelekezo kwa warembo wa Miss Utalii jinsi gazeti hilo linavyotengenezwa kwenye chumba cha kompyuta.

















Thursday, March 24, 2011

Sam Timbe awazulia balaa mastaa Yanga

KOCHA Mkuu wa Yanga, Sam Timbe amezua hofu miongoni mwa wachezaji mastaa wa timu hiyo baada ya kueleza kwamba atawatimua wale wote walio wazembe na watovu wa nidhamu.
Kufuatia kauli na msimamo huo wa Timbe, baadhi ya wachezaji wanaojiona kuwa ni nyota katika klabu hiyo wameanza kupatwa na mchecheto na kusaka timu za kuchezea msimu ujao.
Uchunguzi uliofanywa na Burudani wiki hii umebaini kuwa, uamuzi huo wa Timbe umekuja baada ya kubaini kuwa, baadhi ya wachezaji hawazingatiaa ratiba ya mazoezi na kujiona ni bora kuliko wenzao.
Msimamo huo wa Timbe umewafanya wachezaji kama vile Ernest Boakye kuonekana mara kwa mara kwenye ofisi za Azam na African Lyon kwa lengo la kusaka usajili msimu ujao.
Kwa mujibu wa uchunguzi wa Burudani, Boakye ni mmoja wa wachezaji, ambao wamekuwa wakionyesha vitendo vya utovu wa nidhamu na hivyo kumtibua Timbe.
Hivi karibuni, Boakye alidaiwa kugoma kufanya mazoezi wakati Yanga ilipokuwa ikijiandaa kumenyana na Azam mjini Tanga na kusababisha aondolewe kambini.
Boakye pia alidaiwa kutaka kuihujumu Yanga ilipokuwa ikijiandaa kumenyana na Simba katika mechi ya ligi kuu, hali iliyosababisha asichezeshwe.
Mchezaji mwingine, ambaye amedaiwa kuanza kusuka mipango ya kuihama na timu hiyo ni Yaw Berko. Kipa huyo anadaiwa kutaka kujiunga na mojawapo kati ya timu za Simba na Azam.
Wachezaji wengine wanaodaiwa kufanya mipango hiyo ni viungo Athuman Idd 'Chuji' na Nurdin Bakari na beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’. Mikataba ya wachezaji hao inatarajiwa kumalizika msimu ujao.

Yanga vululuvululu

BAADHI ya wanachama wa klabu ya Yanga, Jumanne iliyopita walinusurika kuchapana makonde kwenye makao makuu ya klabu hiyo, kufuatia baadhi yao kuandaa mkutano wa matawi bila ya kuwashirikisha viongozi wa klabu hiyo.
Tukio hilo lilitokea saa tisa alasiri baada ya baadhi ya viongozi wa matawi kupanga kumuondoa madarakani Mwenyekiti wa matawi ya klabu hiyo nchini, Mohamed Msumi.
Kundi la wanachama la Yanga Bomba lilifika kwenye makao makuu ya klabu hiyo yaliyopo mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam kwa ajili ya kufanya mkutano huo wa kumjadili Msumi.
Mara baada ya kufika kwenye klabu hiyo, kundi hilo likiwa na baadhi ya viongozi wa matawi, lilishindwa kufanya mkutano wake baada ya kuwakuta wanachama wengine wanaomuunga mkono Msumi wakilinda usalama wa klabu.
Kufuatia hali hiyo, yalitokea mabishano makali kati yao na kusababisha baadhi ya wanachama kutaka kupigana, kufuatia kila ipande kudai kuwa, una haki. Hali hiyo ilisababisha Kaimu Katibu Mkuu wa klabu hiyo ,Mwesingwa Joas Selestin kueleza kuwa hakuwa na taarifa ya mkutano huo.
Mwesingwa alilazimika kuondoka haraka kwenye majengo ya klabu hiyo kwa kutumia mlango wa nyuma ili kukwepa vurugu hizo huku baadhi ya wanachama wakisikika wakieleza kuwa, wataharibu vifaa vya jengo hilo.
Uchunguzi uliofanywa na Burudani umebaini kuwa, fujo hizo zilitokea baada ya baadhi ya wanachama kutaka Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Davis Mosha arejeshwe madarakani huku wengine wakipinga.
Mosha aliandika barua ya kujiuzulu uongozi wa klabu hiyo hivi karibuni na kusababisha hali ndani ya klabu hiyo kuchafuka baada ya kutishiwa kuuawa huku gari lake likivunjwa kioo cha nyuma.
Gari la kiongozi huyo lilivunjwa kioo hicho mara baada ya mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara kati ya Yanga na Polisi ya Dodoma uliofanyika kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Hali imezidi kuchafuka ndani ya Yanga kufuatia baadhi ya wanachama kudai kwamba, klabu hiyo imekuwa ikikosa mapato makubwa ya mauzo ya jezi na vitu vyenye nembo ya Yanga.
Wanachama hao wanawashutumu baadhi ya viongozi wao kuwa wanahusika na uchapishaji wa fulana, kalenda na vitu vingine kwa kutumia nembo ya klabu na kisha kuviuza.
Alipoulizwa kuhusu vurugu zilizotokea Jumanne iliyopita, Mwenyekiti wa matawi ya klabu hiyo, Msumi alikiri kutokea kwake, lakini alisema hakuwa na taarifa za kuwepo kwa mkutano wa wanachama.

Ochan, Okwi wamlipua Rage

MWENYEKITI wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage amesema wachezaji Patrick Ochan na Emmanuel Okwi wanamlipua moyo wake kutokana na kucheza soka ya kiwango cha juu.
Akizungumza mjini Dar es Salaam juzi, Rage alisema wachezaji hao wawili kutoka Uganda wamekuwa wakiupa raha moyo wake kila wanapokuwa uwanjani wakisakata kabumbu.
Rage alisema katika mchezo wa awali wa michuano ya klabu bingwa Afrika kati yao na TP Mazembe uliochezwa mjini Lubumbashi nchini Congo mwishoni mwa wiki iliyopita, wachezaji hao waliwaduwaza mashabiki wengi waliohudhuria mechi yao.
Alisema baadhi ya watu walioduwazwa na kiwango kilichoonyeshwa na timu hiyo ni pamoja na viongozi wa TP Mazembe, ambao walikuwa wakiwaulizia mara kwa mara.
"Nilikuwa nimeketi kwenye jukwaa kuu pale uwanjani, kutokana na soka waliyoionyesha, hasa kipindi cha pili, viongozi wa TP Mazembe waliniulizia majina yao,”alisema Rage.
Mwenyekiti huyo wa Simba alisema, Ochan alikuwa akiwasumbua mara kwa mara mabeki wa timu pinzani kutokana na chenga zake za maudhi, kutoa pasi za uhakika na kuutumia vyema mwili wake, hivyo kuwawia vigumu kumpokonya mpira.
Kwa upande wa Okwi alisema, aliwasumbua sana walinzi wa TP Mazembe na mara nyingi walikuwa wakimchezea rafu kwa lengo la kupunguza kasi yake.
Aliongeza kuwa, ana imani kubwa kwamba Simba ilipoteza mechi ya awali kwa kufungwa mabao 3-1 kwa bahati mbaya kutokana na makosa madogo madogo, ambayo wameshaanza kuyafanyiakazi.
Akizungumzia mechi ya marudiano, Rage alisema tayari maandalizi yameshaanza na kujigamba kuwa, iwe isiwe, lazima TP Mazembe wafungwe kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
"Tumepanga mechi hiyo ianze saa tisa mchana, lengo likiwa ni kuwachosha wachezaji wa TP Mazembe kwa vile jua litakuwa kali. Kule kwao wamezoea hali ya hewa ya baridi,” alisema. Wakati huo huo, baadhi ya wanachama wa klabu ya Simba wa mjini Dar es Salaam wamejigamba kuwa, wameandaa jeneza maalumu kwa ajili ya TP Mazembe kwa vile wana uhakika mkubwa wa kuifunga.
Wanachama hao walisema mjini Dar es Salaam wiki hii kuwa, wameshaanza kuandaa mbinu za ushindi za nje ya uwanja ili kuhakikisha Simba inaishinda TP Mazembe na kuivua ubingwa wa Afrika.
Kamati ya utendaji ya Simba ilitarajiwa kukutana mwanzoni mwa wiki hii kwa ajili ya kuandaa mikakati ya ushindi. Kikao hicho pia kilitarajiwa kuwahusisha wanachama wa kundi la Friends of Simba.

MOLA WALAZE PEPONI WASANII WA FIVE STARS MODERN TAARAB


KWA kawaida, hakuna binadamu anayependa kifo. Ni kwa sababu kinaogopesha. Kila binadamu anapenda aishi kwa muda mrefu ili ayafurahie maisha hata kama anaishi kwa dhiki na mashaka.
Lakini hakuna mwenye uwezo wa kukipwepa kifo kwani hata vitabu vyote viwili vya Quraan na Biblia vinatamka wazi kwamba, sisi sote ni waja wa Mwenyezi Mungu na kwake ni lazima tutarejea. Kwamba kila chenye roho lazima kionje mauti.
Ishi utakavyoishi, uwe tajiri, masikini, mwanamichezo, mwanamuziki, jambazi atoaye roho za watu ama vyovyote vile, lazima ukumbane na kifo kwa sababu hakikwepeki.
Enzi za uhai wake, rafiki yangu marehemu Remmy Ongala aliwahi kutunga nyimbo nyingi zinazozungumzia kifo, akikilalamikia kwa kuwatenganisha waliopendana, kuwatoa duniani vipofu na walemavu na mengineyo mengi.
Alitamani kila mtu angekuwa akipewa taarifa ya siku yake ya kufa ili aandae sherehe na kuwaaga ndugu na jamaa zake na ikiwezekana kujipeleka mwenyewe kaburini, lakini hilo haliwezekani. Ni siri kubwa iliyofichwa na Mola wetu.
Hivyo ndivyo ilivyotokea kwa wasanii 13 wa kikundi cha taarab cha Five Stars cha mjini Dar es Salaam, waliofariki dunia katika ajali ya gari iliyotokea usiku wa kuamzia juzi maeneo ya Mikumi mkoani Morogoro.
Katika ajali hiyo, iliyowahuzunisha watanzania wengi, hasa mashabiki wa muziki wa taarab, watu saba walijeruhiwa, mmoja kati yao hali yake ikiwa mbaya.
Ajali hiyo ilitokea saa mbili usiku wakati wasanii wa kikundi hicho walipokuwa wakirejea mjini Dar es Salaam kwa basi aina ya Toyota Coaster, wakitokea katika ziara ya maonyesho kadhaa katika miji ya Ruvuma, Morogoro na Mbeya. Basi hilo lilipata ajali baada ya kuacha njia na kugonga lori la mbao lililokuwa limeegeshwa kando ya barabara baada ya dereva wake kukwepa kukutana uso kwa uso na lori lingine lililokuwa likija upande wake.
Miongoni mwa wasanii waliopoteza maisha yao kutokana na ajali hiyo ni pamoja na mwimbaji nyota wa kundi hilo, Issa Kijoti na kiongozi wake, Nassoro Madenge.
Wengine ni waimbaji Husna Mapande na Hamisa Omary, ambaye ni mke wa msanii Mussa Mipango, mpiga solo Sheba Juma, mpiga gita la besi Omary Hashim, mbeba vyombo Omary maarufu kama Tall, mfanyakazi wa kundi hilo, Ngereza Hassan, wapiga kinanda Tizzo Mgunda na Hamma Kinyoya, mwingine aliyetambuliwa kwa jina moja la Maimuna, mcheza shoo wa kundi hilo, ambaye jina lake halijaweza kujulikana mara moja na mbeba vyombo Haji Mzaniwa.
Waliojeruhiwa katika ajali hiyo na ambao wamelazwa katika hospitali ya mkoa wa Morogoro ni mwimbaji mkongwe na mgeni aliyekuwa amefanya onyesho moja na kundi hilo, Mwanahawa Ally, Suzana Benedict , Zena Mohamed, Samila Rajab, Ally Juma, Rajab Kondo,Mwanahawa Hamis, Shaban Hamis na Msafiri Mussa.
Kwa sababu kifo kimeumbwa na hakuna binadamu anayeweza kukikwepa, napenda kuchukua fursa hii kuwaomba ndugu wa wasanii waliofariki dunia kuwa na moyo wa subira na ustahamilivu.
Ni kawaida unapotokea msiba mkubwa na wa kushtukiza kama huo, baadhi ya watu huzusha maneno mengi, ikiwa ni pamoja na kuvihusisha vifo vya aina hiyo na mambo ya ushirikina. Lakini napenda waamini kuwa huo ni msiba kama mingine na umepangwa na Mungu. Hakuna ambaye angeweza kuukwepa wala kuuzuia.
Ni vyema ndugu wa wasanii waliofariki dunia wakubali kwamba hiyo ni mipango ya Mungu, hakuna anayeweza kuipinga. Wanapaswa kuamini kuwa, duniani tunapita njia, makazi yetu ya kudumu ni ahera.
Wakumbuke kuwa, binadamu sote tunapita katika madaraja matatu. La kwanza ni kuzaliwa, la pili ni kuishi na la tatu ni kifo. Hivyo vyovyote iwavyo, binadamu sote lazima tuonje mauti.
Na kwa wale wasanii waliojeruhiwa, tunawaombea kwa Mola wapate nafuu ili watakapotoka hospitali waweze kuendelea na shughuli zao za kila siku zinazowaendeshea maisha yao. Nao waamini kuwa, ajali hiyo ni mipango ya Mungu kamwe si mkono wa mtu. Ndivyo maisha yalivyo.
Mungu awalaze pema peponi wasanii wote 13 wa Five Stars Modern Taarab waliofariki dunia katika ajali hiyo na awape ahueni wale waliojeruhiwa.

Tuesday, March 22, 2011

Majina ya wasanii wa Five Stars waliofariki

Na Latifa Ganzel Morogoro

WASANII 13 wa kundi la Muziki la Five Star’s Modern Taarab wamefariki dunia na wengine saba kujeruhiwa kati yake mmoja vibaya baada ya gari yao aina ya Toyota Coaster waliyokuwa wakisafiria kutoka Mbeya, kuelekea jijini Dar es salaam kuacha njia na kulivaa lori lililokuwa limesimama na kupinduka, wakikwepa kukutana uso kwa uso na lori lililokuwa likija mbele.
Ajali hiyo iliyothibitishwa na Mkuu wa Usalama Barabarani Mkoa wa Morogoro Ibrahim Mwamakula, zilibainisha ajali hiyo kutokea Machi 21, majira ya saa 2.30 usiku, ndani ya eneo la hifadhi ya taifa ya Mikumi, kilometa karibu sita kutoka lango kuu la kuingilia hifadhi hiyo kutoka upande wa Doma.
Mwamakula alisema kuwa watu 12 walikufa papo hapo na mwingine mmoja alifia njia wakati akipelekwa hospitali ambapo kati yao kumi ni wanaume na watatu wanawake.
Alisema chanzo cha ajali hiyo ni Mwendo kasi wa gari hiyo aina ya Costa iliyokuwa imewabeba wasanii ,yenye namba za usajili T 351 BGE iliyokuwa ikiendeshwa na Juma Hassan anayedaiwa kutoroka baada ya ajali, na uzembe wa dereva huyo kujaribu kulipita gari jingine bila kuwa na uangalifu.
Alisema ajali hiyo ilitokea baada ya Costa hiyo kujaribu kulipita lori aina ya scania lililokuwa limebeba mbao lililokuwa limesimama barabarani baada ya kuharibika lenye namba za usajili T848 APE na tela namba T 556 BDL mali ya Meshack Rajab Mvamba, na kukutana mbele yake na lori aina ya scania lenye namba T 182 BKB na tela namba T 530 BHY ambalo katika kuikwepa Costa hiyo na lenyewe lilipinduka
Kwa upande wake Rais wa bendi hiyo Ally Juma (25) maarufu kama “Ally J” ambaye ni miongoni mwa majeruhi walionusurika,alisema gari hiyo ilikuwa na watu 24 wakiwemo wasanii 21, madereva wawili na abiria mmoja, na walikuwa wakitokea Mkoani Mbeya kwenye maonesho ambapo Jumapili walifanya wilayani Kyela mkoani humo na kabla, siku ya Ijumaa walifanya maonesho Makambako, Mikumi siku ya alhamisi na Kilosa Mkoani Morogoro siku ya jumatano.
Miongoni mwa waliopoteza maisha yumo mwanamuziki Issa Kijoti na kiongozi wa bendi hiyo Nassoro Madenge , waimbaji wa bendi hiyo Husna Mapande na Hamisa Omary ambaye ni mke wa msanii Mussa Mipango, mpiga solo Shebe Juma, mpiga gitaa la base Omary Hashim, mbeba vyombo Omary maarufu kama Tolu,Mfanyakazi wa bendi hiyo Ngereza Hassan, wapiga kinanda Tizzo Mgunda na Hamma Kinyoya, mwingine aliyetambuliwa kwa jina moja la Maimuna na mcheza shoo wa kundi la “Kitu Tigo” la Ilala ambaye jina lake halijaweza kujulikana mara moja na hao wote walikufa papo hapo katika eneo la ajali.
Mwingine aliyekufa akipelekwa katika hospitali ya Mkoa wa Morogoro kwa matibabu ni Haji Mzaniwa (32) mkazi wa jijini Dar es salaam ambaye ni mbeba vyombo katika bendi hiyo.
Majeruhi katika ajali hiyo waliolazwa katika hospitali ya Mkoa wa Morogoro ni pamoja na mwimbaji Mkongwe na mgeni aliyekuwa amefanya onesho moja tu katika bendi hiyo, Mwanahawa Ally (55), Suzana Benedict (32),Zena Mohamed (27), Samila Rajab (22), Ally Juma (25), Rajab Kondo (25), Mwanahawa Hamis (38), Shaban Hamis (41) na Msafiri Mussa (22) wote wasanii na wakazi wa jijini Dar es salaam.
Hata hivyo baadhi ya mashuhuda wa ajali hiyo,Mohamed Hawanga ambaye ni mtumishi wa Hifadhi ya Mikumi, Justine Simon aliyekuwa safarini kuelekea Mafinga na Jatemi Lembilinyi aliyekuwa akielekea Iringa wakitokea Dar es salaam, walisema kama sio jitihada za dereva wa lori lililokuwa likija mbele kukwepesha gari hiyo na kuipeleka porini, huenda angekutana na Costa hiyo uso kwa uso, na watu wote wangeweza kupoteza maisha katika tukio hilo.
Maiti zote pamoja na majeruhi walipelekwa usiku wa manene katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Morogoro kwajili ya kuhifadhiwa huku majeruhi wakipatiwa matibabu.
Ndugu na jamaa wa marehemu hao walifurika katika chumba cha kuhifadhi maiti cha hospitali ya mkoa wa morogoro kwaajili ya kuzitambua maiti zao na kuchukua kwaajili ya mazishi.

Monday, March 21, 2011

WASANII 13 WA FIVE STARS WAFARIKI KATIKA AJALI

ISSA KIJOTI, mmoja wa waimbaji wa kikundi cha taarab cha Five Stars, anayedaiwa kufariki dunia katika ajali ya gari iliyotokea jana usiku mjini Morogoro.

BAADHI ya wasanii wa kikundi cha taarab cha Five Stars, ambao inadaiwa walifariki dunia katika ajali ya gari iliyotokea jana usiku mjini Morogoro.

Wanamuziki 13 wa kundi la Five Stars Modern Taarab, 'Watoto wa Bongo' wamefariki dunia katika ajali mbaya ya gari iliyotokea usiku wa kuamkia leo eneo la Mikumi mkoani Morogoro. Katika ajali hiyo, wasanii 12 walifariki papo hapo, akiwemo muimbaji maarufu wa kundi hilo Issa Kijoti.
Taarifa zinasema ajali hiyo imetokea baada ya gari lililokuwa limewabeba wanamuziki wa kundi la taarab la Five Stars kugongana uso kwa uso na roli la mbao, wakati wakitokea mikoani kurejea Dar es Salaam.
Waliotambuliwa kufariki dunia mpaka sasa ni pamoja na Issa Kijoti, Hamisa Omary, Husna Mapande, Omary Hashim, Nasor, Sheba Juma, Tizo Mkunda na Samir Maulid.
Taarifa zaidi kutoka eneo la tukio zinasema kuwa, tayari miili ya marehemu hao imeondolewa eneo la ajali na kupelekwa katika hospitali ya mkoa ya Morogoro.
Akizungumza kwa njia ya simu kutoka Morogoro jana, kiongozi wa kundi hilo, Ally J alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo.
Walionusurika katika ajali hiyo ya kusikitisha ni pamoja na muimbaji mkongwe, Mwanahawa Ally, ambaye alikuwa kama muimbaji mualikwa katika ziara hiyo.
Mbali na Mwanahawa, rais wa bendi hiyo Ally J naye amenusurika katika ajali hiyo wakati
waimbaji wengine nyota, Jokha Kassim na Issa Kamongi hawakusafiri na kundi hilo katika safari hiyo.
Kundi hilo lenye upinzani mkali na Jahazi, liliondoka Dar es Salaam wiki iliyopita kwenda katika
katika mikoa ya Morogoro, Singida na Mbeya kwa ajili ya kufanya maonyesho na kutambulisha albamu zao walizozizindua mwanzoni mwa mwaka huu.

Thursday, March 17, 2011

BASATA kuyasuka upya mashindano ya urembo


Baraza la Sanaa la Taifa litayafanyia mabadiliko makubwa mashindano yote ya urembo nchini ili yafanyike kwa kufuata taratibu na kanuni zilizopo lakini pia kufanyika katika misingi ya haki na uwazi kuliko ilivyo sasa ambapo kumekuwa na malalamiko mengi kutoka kwa baadhi ya washiriki na wadau mbalimbali.
Hayo yamesemwa na Katibu Mtendaji wa BASATA,Ghonche Materego kwenye Jukwaa la Sanaa linalofanyika kila Jumatatu barazani hapo wakati akihitimisha mada ya Mchango wa Mashindano ya Urembo na Mitindo katika Kukuza Ajira iliyokuwa ikiwasilishwa na Juliana Urio ambaye ni muandaaji wa Shindano la Kisura linalofanyika kila mwaka.
Alisema kwamba,Baraza linakusudia kuwaita waandaaji wote wa mashindano ya urembo na mitindo ili kuwakutanisha na wadau mbalimbali kwa ajili ya kueleza changamoto zilizopo na baadaye kuja na mapendekezo ambayo yatafanya mashindano hayo kuwa bora zaidi na yatakayofanyika katika misingi ya uwazi na haki zaidi.
“Tunatambua mchango wa mashindano haya lakini lazima yafanyike katika misingi iliyo wazi na bora zaidi ndiyo maana tunataka tuwaite waandaaji wote tuwakutanishe na wadau mbalimbali ili tupate changamoto na michango mbalimbali ya uboreshaji” alisema Materego.
Aliongeza kwamba, si nia ya Baraza kufuta shindano lolote lakini akasisitiza kwamba pale shindano linapokuwa na mapungufu mengi basi lazima lifutwe.Katika hili alisema kwamba, lazima waandaaji wazingatie masharti na taratibu zote wanazopewa ili kuepuka kufutwa kwa mashindano yao.
“Tunajua kwamba,ufutaji wa shindalo lolote utaathiri watu wengi hasa wasanii (warembo) sisi hatutaki kufika huko kwa sasa ndiyo maana tunasema mabadiliko katika uendeshaji wake ni ya msingi.Hatutaki mashindano ambayo washindi wanapatikana kwa misingi ya fedha na vigezo visivyostahili” alisisitiza Materego.
Kwa upande wake Juliana Urio alisema kwamba,washiriki wa shindano la kisura wamekuwa wakipatikana kutoka mikoa mbalimbali nchini na kusisitiza kwamba shindano lake limekuwa likifanyika katika misingi ya uwazi na haki kwani washindi wamekuwa wakipatikana kutokana na kura za wananchi na yeye kama muandaaji hajui kinachokuwa kinaendelea katika kumpata mshindi.

Rage: Lazima tuiue TP Mazembe


WAKATI kikosi cha Simba kinatarajiwa kuondoka nchini kesho kwenda Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kupambana na timu ya TP Mazembe, uongozi wa klabu hiyo umetaja mbinu watakazozitumia kuwaua wapinzani wao. Katika makala hii ya ana kwa ana,iliyoandikwa na Mwandishi Wetu ATHANAS KAZIGE, Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage anaelezea kuhusu mbinu hizo.

SWALI: Hongera kwa ushindi mnaoendelea kuupata katika michuano ya ligi kuu msimu huu. Nini siri ya mafanikio hayo?
JIBU: Siri ya mafanikio hayo ni juhudi zinazofanywa kwa pamoja na kila mmoja wetu na pia kutimiza malengo tuliyopangiana. Kuanzia wachezaji, makocha na viongozi sote tupo pamoja na tumekuwa tukifanyakazi kwa ushirikiano mkubwa.
Mbali na hayo, bado tuna imani kuwa tutaweza kufanya vizuri zaidi kwa vile wachezaji wetu wote wana ari ya kuhakikisha wanajenga heshima ya klabu yetu kwa mara ya pili mfululizo.
Ukweli ni kwamba ushindi wetu unaweza kuchangiwa na mshikamano uliopo kati ya wanachama, viongozi pamoja na mashabiki, ambao wamekuwa wakijitokeza kwa wingi uwanjani na kuwashangilia kwa nguvu wachezaji kitu, ambacho kimeongeza juhudi ya ushindi.
SWALI: Hivi karibuni ulisikika ukieleza kwamba mtaunda kamati ya kuhakikisha mnaivua ubingwa TP Mazembe. Je, kazi hiyo tayari mmeifanya? Ni kina nani wanaounda kamati hiyo?
JIBU: Simba ni klabu kubwa, imefanya maandalizi ya kutosha kuhakikisha tunashinda mchezo wetu dhidi ya TP Mazembe hapo Jumamosi.
Miongoni mwa mipango tuliyofanya ni pamoja na kuwepo baadhi ya watu ambao wameunda kamati ya kusaka ushindi dhidi ya mabingwa hao watetezi wa Afrika.
Lakini nasikitika kwamba siwezi kukutajia majina ya wajumbe wanaounda kamati hiyo kwa vile wameomba wasitajwe hadharani.Lakini kamati hiyo ipo na inaendelea na kazi na tayari imeweza kufanya mambo makubwa, ikiwa ni pamoja na kupata siri za ushindi wa wapinzani wetu hasa wanapokuwa nyumbani kwao Congo.
Miongoni mwa siri hizo ni pamoja na kuifahamu kwa undani timu hiyo wakiwemo wachezaji wao wapya, ambao wanacheza ligi kuu ya nchini humo na mfumo wao wa uchezaji.
SWALI: Ukiacha kamati hiyo kunasa siri za ushindi wa TP Mazembe huko kwao, je mmepata CD au kanda za video za michezo mbalimbali ya timu hiyo ya Congo?
JIBU: Ni kweli tumeweza kupata baadhi ya CD za michezo ya TP Mazembe na benchi letu la ufundi pamoja na wachezaji wamefanyia kazi kujua mbinu za kuweza kuwasambaratisha na kwa kweli tunaondoka Ijumaa kwenda Congo tukiwa tumechukua tahadhari zote.
Miongoni mwa tahadhari hizo ni pamoja na kuwashirikisha viongozi wa ubalozi wetu kule Congo ili kukwepa hujuma zozote za nje na ndani ya uwanja na pia kwenye makazi yetu, ambayo tutafikia ambako tayari tumetuma watu wetu kuweka mazingira sawa.
Pia tumeweza kuwatumia baadhi ya Watanzania, ambao wanaishi Congo kwa ajili ya kujua mambo mengi ya TP Mazembe. Kwa kweli tumejipanga vizuri kuhakikisha tunaweka rekodi ya kuivua ubingwa timu hiyo kama tulivyofanya kwa Zamalek.
SWALI: Mnatarajia kwenda Congo kwa usafiri gani na siku ipi?
JIBU: Tumepanga kuondoka nchini siku ya Ijumaa kwenda Congo na taratibu zote za kukodi ndege maalumu zinaendelea. Pia wanachama wetu wanaendelea kujiandikisha majina yao pale makao makuu ya klabu, mtaa wa Msimbazi.
Wapo baadhi ya viongozi wa serikali na wabunge, ambao wameonyesha nia ya kutaka kuongozana na sisi kwenda Congo ili kuwapa hamasa vijana wetu waweze kushinda mchezo huo.
Napenda kukuhakikishia kwamba tumepanga kuweka rekodi huko Congo, lazima tuwashangaze watu, hasa wale ambao wanatuponda na kutuombea mabaya.
SWALI: Watu gani ambao wanawaombea mabaya wakati nyinyi ni wawakilishi wa Tanzania katika michuano ya kimataifa? Au ni Yanga?
JIBU: Wapo watu wachache ambao wanataka sisi tutolewe katika mashindano haya, lakini tutakwenda na kupambana na hao TP Mazembe hadi hatua ya mwisho.
Siwezi kusema ni watu gani hao,lakini kwenye soka mambo hayo yapo na watafunga mdomo wenyewe baada ya kusikia habari za huko Congo.
SWALI: Unaweza kutupatia majina ya wachezaji, ambao mmepanga kwenda nao huko Congo?
JIBU: Sina orodha ya wachezaji ambao watakwenda Congo kwa vile kazi hiyo inafanywa na viongozi wa benchi la ufundi, lakini nategemea kuipata Jumatano au Alhamisi.
Hata hivyo,baadhi ya wachezaji ambao ni wagonjwa kama Uhuru Suleiman,Joseph Owino wao nina hakika hawawezi kwenda Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
SWALI:Je tokea mmeanza maandalizi ya mchezo dhidi ya TP Mazembe mnapata ushirikiano kutoka Shirikisho la soka nchini (TFF) na Serikalini?
JIBU:Hakika napenda kuwashukuru viongozi wa Serikali,TFF kwa vile tupo nao bega kwa bega kuhakikisha Simba inapeperusha vyema bendera ya nchi katika mashindano hayo ukumbuke sisi ndio wawakilishi pekee tulio bakia katika michuano ya kimataifa.
Tumeona wenzetu Yanga wametolewa katika mzunguko wa kwanza,Zanizbar Ocean View na KMKM zote zimetoka,nawaomba mashabiki wote wa soka nchini kuiombea dua Simba.

Banana azusha kasheshe na BASATA


KIONGOZI wa bendi ya muziki wa dansi ya B, Banana Zorro amezua mzozo kati yake na Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), baada ya kudai kuwa, studio iliyofunguliwa na Rais Jakaya Kikwete itakuwa chini ya Chama cha Tanzania Fleva Unit (CTFU).
Akizungumza na waandishi wa habari wiki iliyopita, Banana alisema vyombo hivyo vya studio vipo chini yao na hakuna msanii yeyote atakayezuiwa kujiunga na chama hicho.
Banana, ambaye ni Makamu Mwenyekiti CTFU alisema, vifaa hivyo vipo chini yao pamoja na mtambo wa kufyatulia CD na kwamba vimehifadhiwa sehemu maalum.
"Tumeshampata prodyuza kutoka Uingereza, ambaye ni mtaalamu wa studio ya kisasa (master studio), baada ya wiki moja studio itafunguliwa," alisema Banana.
Hata hivyo, kauli hiyo ya Banana imepingwa vikali na Katibu Mtendaji wa BASATA, Ghonche Materego, aliyesema chama hicho hakisajiliwa na baraza hilo.
Materego alisema Chama cha Tanzania Urban Music (TUMA) ndicho pekee kinachotambuliwa na baraza hilo na ndicho chenye idhini ya kusimamia vyombo hivyo.
Alisema lengo la kuundwa kwa TUMA ni kukuza muziki wa kizazi kipya kwa lengo moja tu, hivyo hakuna sababu ya kuwa na vyama viwili.
“Huu ni muziki, sio siasa, vyama vingi havina manufaa kwa wasanii zaidi ya kuwatenga kwani kiliundwa chama kimoja kwa lengo la kushauri, kuhamasisha na kujenga umoja,”alisema.

Marlaw, Besta sasa ni mume ne mke


HATIMAYE baada ya uchumba wa siri wa takribani miaka minne,mastaa wawili wa muziki wa kizazi kipya, Lawrence Marima ‘Marlaw’ na Besta Prosper Rugeiyamu wamefunga ndoa.
Marlaw na Besta walifunga ndoa mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye kanisa moja katoliki mjini Dar es Salaam na kufuatiwa na tafrija kabambe iliyofanyika kwa siri.
Habari kutoka kwa watu wa karibu na wanandoa hao zimeeleza kuwa, tafrija hiyo ilifanyika kwa siri kwa sababu hawakuwa wakitaka bughudha kutoka kwa watu.
Marlaw alikaririwa akiwaeleza baadhi ya rafiki zake kuwa, hakutaka harusi yao ipewe uzito kwenye vyombo vya habari kwa sababu ni suala la kifamilia zaidi.
Msanii huyo, anayetamba hivi sasa kwa kibao chake cha ‘Missing my baby’ alithibitisha kufanyika kwa harusi hiyo, lakini alikataa kuzungumza zaidi kwa kile alichodai ni mambo binafsi.
“Mahali tulipofungia ndoa ndipo hapo hapo tulipofanyia sherehe. Siwezi kuweka jambo hilo wazi kwenye vyombo vya habari kwa sababu ni suala la kifamilia zaidi,” alisema Marlaw.
Marlaw alisema ameamua kuachana na ‘ubachela’ na ameamua kumweka ndani Besta huku akimwomba Mungu awajalie maisha ya furaha.
Hata hivyo, Marlaw amewataka mashabiki wake wajiandae kusherehekea naye ndoa hiyo kwa utaratibu atakaowatangazia hapo baadaye.
Kabla ya kufunga pingu za maisha, familia ya Besta ilimwandalia tafrija kabambe ya kumuaga iliyofanyika wiki mbili zilizopita. Marlaw na Besta walikuwa wakificha uchumba wao kwa muda mrefu, lakini sasa wameamua kutimiza ndoto yao ya kuishi pamoja. Mungu awajalie maisha marefu.

Keisha awa mama


MSANII nyota wa kike wa muziki wa kizazi kipya nchini, Khadija Shaban ‘Keisha’ amejifungua mtoto wa kiume hivi karibuni.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Keisha alisema alijifungua mtoto huyo kwa njia ya upasuaji na ameamua kumpa jina la Jam Key.
Keisha alisema mtoto wake huyo ameshatimiza wiki tatu hapa duniani na anamshukuru Mungu kwa kujifungua salama.
“Kwanza namshukuru Mungu kwa kujifungua salama na kuweza kubeba dhamana ya kuitwa mama,”alisema msanii huyo huku uso wake ukiwa umepambwa kwa tabasamu mwanana.
“Hii itanifanya nizidi kujituma katika maisha yangu ili mwanangu aweze kuishi maisha mazuri hapo baadaye,” aliongeza.
Nyota huyo ambaye alifunika vilivyo kwenye wimbo wa ‘Bado tunapanda’ wa kundi la Tip Top Connection lenye maskani yake Manzese jijini Dar alisema alisema, pamoja na kupata kichanga hicho, bado ataendelea na kazi yake ya kukonga nyoyo za mashabiki.
Keisha alijiengua katika kundi hilo mwishoni mwa mwaka jana baada ya kutokea hali ya kutokuelewana kati yake na uongozi. Kwa sasa, Keisha anapiga muziki kwa kujitegemea.

DEDE: Nimerudi nyumbani


Asema hana kinyongo ama ugomvi na Sikinde
Aliitumikia kwa miaka 21 tangu alipojiunga nayo 1990

MTUNZI na mwimbaji mkongwe wa nyimbo za muziki wa dansi nchini, Shabani dede (54) ametangaza kuihama bendi ya Mlimani Park Orchestra ‘Sikinde’ na kujiunga na bendi nyingine kongwe ya Msondo Ngoma.
Dede alitangaza uamuzi wake huo juzi, ikiwa ni siku mbili kabla ya bendi hizo zenye mashabiki wengi nchini kufanya onyesho la pamoja kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.
Mwimbaji huyo mwenye sauti ya mvuto alijiunga na Mlimani Park mwaka 1990 akitokea Msondo Ngoma. Amerejea kwenye bendi hiyo baada ya kuitumikia Sikinde kwa miaka 21.
Akizungumza na Burudani nyumbani kwake Mbagala Rangitatu mjini Dar es Salaam jana, Dede alisema ameamua kurejea Msondo Ngoma baada ya kuikumbuka na kuwakosa mashabiki wake kwa muda mrefu.
Dede, ambaye pia aliwahi kuimbia bendi ya Bima Lee alisema hakushawishiwa na mtu yeyote katika kufikia uamuzi wake huo, ambao alisisitiza kuwa, ulitokana na mapenzi yake binafsi.
“Sikuondoka Sikinde kwa sababu ya kushawishiwa kwa pesa, mtu ama kiongozi yeyote wa Msondo Ngoma. Huu ni uamuzi wangu binafsi,”alisema mwimbaji huyo, ambaye kuna wakati alipachikwa jina la ‘Super Motisha’.
Akifafanua zaidi, alizitaja sababu zingine zilizomfanya afungashe virago Sikinde kuwa ni mapenzi makubwa aliyonayo kwa Msondo Ngoma, bendi ambayo ndiyo iliyomkuza na kumtangaza kimuziki.
Alisema anarudi Msondo Ngoma kwa kishindo hivyo amewataka mashabiki wake wajiandae kusikia nyimbo zake mpya na kali, ambazo tayari ameshazitunga.
Alipoulizwa iwapo ameamua kuondoka Sikinde kwa sababu ya kukosa uongozi, Dede alisema madai hayo si ya kweli kwa sababu hata huko Msondo anakokwenda hana lengo la kuwa kiongozi, bali anataka kuwatumikia mashabiki wake.
“Nimekuwa swahiba mkubwa wa Habibu Mgalusi (kiongozi wa Sikinde) kwa muda mrefu pamoja na wanamuziki wengine, hivyo sina kinyongo ama ugomvi na yeyote. Naitakia kila la heri pamoja na mafanikio mema bendi ya Sikinde,”alisema.
Dede amewataka mashabiki wake wauchukulie uamuzi wake huo kuwa ni wa kawaida kwa mwanamuziki kwa vile katika safari ya kutafuta maisha, lolote linaweza kutokea.
Alitoa mfano wa mwanasoka Mrisho Ngasa, ambaye alipotangaza kuihama Yanga na kujiunga na Azam FC, hakuna aliyepatwa na mshangao kwa sababu ilieleweka kwamba anatafuta maslahi bora zaidi.
Kabla ya kunyakuliwa na Mlimani Park mwaka 1990, Dede aliimbia Msondo Ngoma wakati ilipokuwa chini ya Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (JUWATA) na baadaye OTTU.
Akiwa katika bendi hiyo, Dede alijipatia umaarufu mkubwa kupitia vibao vyake vya ‘Fatuma’, ‘Jenny’, ‘Sauda’, ‘Mkono wa birika’ na nyinginezo. Aliimba nyimbo hizo kwa kushirikiana na marehemu Joseph Lusungu, Juma Akida, Moshi William na Suleiman Mbwembwe.
Dede alijiunga na Msondo Ngoma akitokea bendi ya Dodoma International. Alinyakuliwa kutoka kwenye bendi hiyo na mpiga solo maarufu nchini, Saidi Mabera baada ya kukunwa na kipaji chake cha uimbaji.
Licha ya kujipatia sifa na umaarufu kwa kipindi kifupi, Dede aliamua kuiacha solemba Msondo Ngoma na kujiunga na Sikinde, bendi ambayo ilizidi kumtambulisha zaidi kimuziki. Wakati huo, Sikinde ilikuwa ikimilikiwa na Shirika la Uchumi na Maendeleo la Dar es Salaam (DDC).
Akiwa Sikinde, Dede ambaye aliwahi kushikilia uongozi kwa vipindi vinne tofauti, alitunga nyimbo lukuki, ambazo ziliipatia umaarufu mkubwa bendi hiyo. Baadhi ya nyimbo hizo ni ‘Talaka rejea’, ‘Amua’, ‘Ndugu wagombanapo’, ‘Kumbuka fadhila’, ‘Binamu’, ‘Uchungu wa mwana’, ‘Chozi la huba’, ‘Fumanizi’, ‘Maneno maneno’ na nyinginezo.
Dede alisema ili kuonyesha uungwana na mapenzi kwa Sikinde, ameamua kuiachia zawadi ya nyimbo zake mbili alizozitunga hivi karibuni. Nyimbo hizo ni ‘Tunu ya upendo’ na ‘Mwanamke akiwezeshwa anaweza’, ambazo zitarekodiwa kwenye albamu mpya ya Sikinde.
Alipoulizwa kuhusu ujio wa Dede, Meneja wa Msondo Ngoma, Saidi Kibiriti alisema, wanamkaribisha kwa mikono miwili na kuongeza kuwa, watamtambulisha rasmi katika onyesho lao la Jumapili kwenye ukumbi wa Max Bar, Ilala, Dar es Salaam.
Naye Katibu wa Mlimani Park, Hamisi Milambo alisema hawababaiki kuondoka kwa Dede na kwamba wanajipanga upya kuwarejesha waimbaji wao wa zamani, Karama Regesu na Bennovilla Anthony.

UHURU SC KAZINI

Nahodha wa timu ya soka ya Uhuru, Mussa Hassan (kulia) akitoa mawaidha kwa wachezaji wa timu hiyo wakati wa mazoezi yaliyofanyika juzi kwenye uwanja wa shule ya msingi ya Mnazi Mmoja, Dar es Salaam. Uhuru inayoundwa na wafanyakazi wa Radio Uhuru na Uhuru Publications Ltd, inajiandaa kwa michuano ya Kombe la NSSF. (Picha na Emmanuel Ndege).

Sikinde, Msondo Ngoma kazi ipo kesho


BENDI kongwe za muziki wa dansi nchini, Msondo Ngoma na Mlimani Park Orchestra kesho zinatarajiwa kuonyeshana ubabe katika onyesho litakalofanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.
Onyesho hilo la kihistoria limeandaliwa na Kampuni ya Prime Time Promotions kwa lengo la kuonyesha uhai wa bendi hizo na pia kuwapa mashabiki burudani kabambe.
Taarifa iliyotolewa na kampuni hiyo jana imeeleza kuwa, onyesho hilo limepangwa kuanza saa nne usiku na kiingilio ni sh. 5,000 kwa mtu mmoja.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, bendi hizo zitapanda jukwaani kwa awamu na kupiga nyimbo zao mpya na za zamani kwa lengo la kuwapa mashabiki ladha tofauti ya muziki.
Hii ni mara ya pili katika kipindi cha miezi mitano kwa bendi hizo mbili kufanya onyesho la pamoja. Mara ya mwisho zilionyeshana kazi mwishoni mwa mwaka jana kwenye ukumbi wa Mzalendo Pub, Kijitonyama, Dar es Salaam.
Akizungumzia onyesho hilo, Katibu wa Mlimani Park, Hamisi Milambo alisema wamejiandaa vyema kuwadhihirishia mashabiki wao kwamba wao ni mabingwa halisi wa muziki nchini.
Alisema kukosekana kwa mwimbaji wao nyota, Shaban Dede aliyejiunga na Msondo Ngoma juzi hakuwezi kuwaathiri kwa vile bendi yao ina hazina ya waimbaji wengi wazuri.
“Tumekuwepo kambini kwa takriban wiki moja tukizifanyia mazoezi nyimbo zetu za zamani kwa lengo la kuwakumbusha mashabiki tulipotoka, tulipo na tunapokwenda,”alisema.
Aliwataja waimbaji wengine watakaopanda jukwaani siku hiyo kuwa ni Hassan Bitchuka, Hassan Kunyata, Abdalla Hemba na wapiga ala kama vile Ramadhani Mapesa, Karama Tony na Steven Maufi.
Naye Meneja wa Msondo Ngoma, Saidi Kibiriti alisema, hawana wasiwasi na onyesho hilo kwa vile wamefanya maandalizi ya kutosha kwa ajili ya kuwasambaratisha wapinzani wao.
Alisema kuongezeka kwa Dede kwenye kikosi chao kutaiongezea nguvu bendi hiyo kwa vile wamemchukua kwa lengo la kuziba mapengo ya waimbaji mbalimbali, ambao kwa sasa hawapo.
Kibiriti amewataka mashabiki wa Msondo Ngoma kujitokeza kwa wingi kuhudhuria onyesho hilo kwa lengo la kuwaongezea ari na nguvu ya kufanya vizuri.

Rose, Bahati wapigwa kumbo


WANAMUZIKI nyota wa Injili nchini, Rose Muhando, Bahati Bukuku na Flora Mbasha mwishoni mwa wiki iliyopita walishindwa kung’ara katika tuzo za muziki huo baada ya kupigwa kumbo na waimbaji chipukizi.
Licha ya majina ya waimbaji hao watatu kuwemo katika tuzo ya mwimbaji bora wa kike, walifunikwa na waimbaji chipukizi Martha Mwaipaja, Christina Shusho, Upendo Nkone na Upendo Kilahiro.
Mshindi wa tuzo hiyo alikuwa Christina, ambaye aliwafunika vibaya Rose na Bahati.
Boniface Mwaitege aliibuka mshindi wa tuzo ya mwimbaji bora wa kiume wakati tuzo ya kundi bora la mwaka ilinyakuliwa na Double E.
Tuzo ya wimbo bora ilinyakuliwa na mwimbaji mkongwe Upendo Nkone wakati tuzo ya video bora ya mwaka ilinyakuliwa na John Lisu kupitia wimbo wake wa Jehova yu hai.
Mwimbaji chipukizi Miriam Shilwa alitwaa tuzo ya balozi bora wa jamii baada ya kumshinda Flora.
Mratibu wa tuzo hizo kutoka Tanzania Gospel Music Award (TGMA), Harris Kapiga alisema washindi walipatikana kutokana na kupigiwa kura na mashabiki wa muziki huo.
Wanamuziki wengine wa kiume waliopigiwa kura ya kuwania tuzo ya mwimbaji bora wa kiume walikuwa Jackson Bent, Fanuel Sedekia, Ambwene Mwasongwe na John Lisu.
Waimbaji wengine waliokuwa wakiwania tuzo ya wimbo bora ni Christina Mbilinyi ‘Nasubiri baraka zangu’, Miriam Mauki ‘Double Double’, Upendo Kilahiro ‘Usifurahi mwenzako anapofanikiwa’ na Martha Mwaipaja ‘Usikate Tamaa’.
Tuzo ya wimbo bora kwa wanaume iliwaniwa na Thomas Bernard ‘Jehova ananipa kushinda’, Christopher Israel ‘Hosana’, Danford Sunday ‘Mwacheni Mungu’, Aaron Kyara ‘Juu Mbinguni’ na Charles Thobias ‘Akili zangu zimefika mwisho’.

Sunday, March 13, 2011

BONANZA LA WANAHABARI LILIVYOFANA DAR








Wadau kutoka vyombo mbalimbali vya habari, vikiwemo Uhuru Publications Ltd, wachapishaji wa magazeti ya Uhuru, Mzalendo na Burudani na Radio Uhuru wakijiburudisha wakati wa bonanza la vyombo vya habari lililofanyika jana kwenye ufukwe wa klabu ya Cine iliyopo Msasani, Dar es Salaam. Bonanza hilo liliandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo nchini (TASWA) na kudhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL).




Friday, March 11, 2011

MISS UTALII 2011 APATIKANA

HUYU ndiye Adelqueen Njozi, Miss Utalii 2011. Alishinda taji hilo mwishoni mwa wiki iliyopita katika shindano lililofanyika kwenye hoteli ya Kiromo iliyopo Bagamoyo mkoani Pwani. Hapa alikuwa akizungumza na waandishi wa habari juzi kwenye ukumbi wa Idara ya Habari (Maelezo), Dar es Salaam.

SURVIVALS SISTERS WAPEWA BAJAJ

RAIS Jakaya Kikwete juzi alitekeleza ahadi aliyotoa kwa wasanii wa kundi la muziki wa kizazi kipya la Survival Sisters baada ya kuwazawadia Bajaj kwa ajili ya kuwasaidia katika shughuli zao mbalimbali. Pichani, Kaimu Mnikulu Kassim Mtawa akikabidhi Bajaj hizo kwa wasanii hao, Irene Malekela (kushoto) na Ratifa Abdalla. (Picha ya Ikulu).


Thursday, March 10, 2011

Semsekwa: Nilitimuliwa Extra Bongo kimizengwe


MWIMBAJI na rapa machachari wa bendi ya muziki wa dansi ya Twanga Pepeta International, Greyson Semsekwa amedai kuwa, alitimuliwa katika bendi ya Extra Bongo Next Level kimizengwe na bila kujua tatizo lake.
Akihojiwa katika kipindi cha televisheni cha Nyumbani ni Nyumbani cha TBC 1 mwishoni mwa wiki iliyopita, Semsekwa alisema kiongozi wa Extra Bongo, Ally Choki alifikia uamuzi wa kumtimua bila kumueleza kosa lake.
“Kusema kweli Choki hakuwahi kuniita kunieleza kosa langu, nilisoma habari hizo kupitia kwenye vyombo vya habari,”alisema mwanamuziki huyo.
Semsekwa alisema katika bendi ya Extra Bongo, maamuzi yote yanafanywa na mtu mmoja (Choki) na kwamba hakuna uongozi wa pamoja.
“Mfukuze mtu kwa sababu maalumu, sio unalipuka tu. Huku ni kuvunjiana heshima,”alisema rapa huyo, ambaye alijizolea sifa kwa rapu yake inayosema ‘kichaa kapewa rungu’.
“Kabla ya kufikia uamuzi wa kumfukuza mtu kazi, unatakiwa umwite na kumweleza kosa lake na ikiwezekana unamwandikia barua na kama kuna madai yake unamlipa,”alisema.
“Yeye (Choki) baada ya kutoa taarifa hizo kwenye vyombo vya habari, akawa ananikimbia, simu anazima, kwa nini? Kiongozi wa bendi unakuwa mwoga?”aliongeza.
Semsekwa ametoa shutuma hizo kwa Choki siku chache baada ya Extra Bongo kuwatimua wanamuziki wake kadhaa na kuajiri wengine wapya saba.
Wanamuziki wapya waliochukuliwa na Extra Bongo ni pamoja na Rogert Hegga ‘Caterpilar’, Saulo John ‘Ferguson’, George Kanuti, Oseah, Isaack Buriani ‘Super Danger’, Otilia Boniface ‘Kandoro’ na Hassan Mussa ‘Super Nyamwela’
Akiwatambulisha wanamuziki hao kwa waandishi wa habari, Choki alijigamba kuwa, amepania kuifanya bendi yake iwe tishio kimuziki nchini.
Semsekwa alisema hana kinyongo na TOT na kwamba yote yaliyotokea kwake yamekwisha kwa vile ameshajipanga upya katika bendi ya Twanga Pepeta.
Alisema ameamua kujiunga na Twanga Pepeta kwamba sababu ni bendi kongwe na yenye mafanikio makubwa na pia ndiyo iliyomtambulisha kimuziki.
“Niliwahi kuimbia Twanga Pepeta kabla ya kwenda Extra Bongo. Hiki ni chuo cha mafunzo. Hata hao wanaoidharau, walipata sifa na umaarufu walipokuwa Twanga Pepeta, “ alisema.
“Nashangaa, mtu amejifunzia maisha hapa, halafu anapotoka anapadharau na kupakashifu. Huko ni kupotoka,”alisema.
Semsekwa alisema aliamua kwenda Twanga Pepeta yeye mwenyewe baada ya kupata taarifa za kutimuliwa kwake Extra Bongo na kusisitiza kuwa, hajapoteza kitu.
“Nitaibuka na mambo mapya na mazito. Nataka kule nilikitoka wajue kwamba wamepoteza chombo chenye thamani kubwa,”alisema.
“Ukiondoa Msondo Ngoma na Sikinde, hakuna tena bendi nyingine bora hapa nchini kama Twanga Pepeta. Hizi zingine ni sawa na raba za kichina. Ukitaja bendi tano bora nchini, huwezi kuikosa Twanga Pepeta. Nami niliamua nije kwenye bendi bora,”alisema.

K-One akamilisha albamu yake mpya

MSANII chipukizi wa muziki za kizazi kipya nchini, Karim Othman amekamilisha kazi ya kurekodi albamu yake ya kwanza, inayojulikana kwa jina la ‘Sina hakika’.
Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii, Karim, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la K-One alisema, albamu hiyo itakuwa na vibao sita, alivyovirekodi kwenye studio za Baucha Records.
K-One alisema amerekodi baadhi ya vibao vyake kwa kuwashirikisha wasanii mbalimbali nyota wa muziki huo kama vile Tundaman, Chegge, Ali Kiba, Madee na Baker.
Alisema ameamua kurekodi na wasanii hao kwa lengo la kuzipa nyimbo zake ladha tofauti na pia kuongeza ushirikiano kati ya wasanii wakongwe na chipukizi hapa nchini.
“Unajua hii ni albamu yangu ya kwanza, hivyo nitakapotoka lazima nitoke kiaina sio kiubabaishaji, ndio maana niliomba kampani ya wakali hawa watano,”alisema.
Alivitaja vibao vitakavyokuwemo kwenye albamu hiyo kuwa ni ‘Ngoja niseme’, ‘Dhahabu’, ‘Nielewe’, ‘Niwaambie’, ‘Weekend special’ na ‘Sina hakika’.
Kwa mujibu wa K-One, albamu hiyo inatarajiwa kuingia sokoni mwishoni mwa mwezi huu chini ya usimamizi wa Baucha Records.
Msanii huyo mwenye sura ya mvuto alisema pia, tayari ameshatengeneza video ya wimbo wa ‘Sina hakika’, ambao ndio utakaobeba albamu hiyo. Video hiyo imerekodiwa na kampuni ya Showbize.
“Nawaomba mashabiki wangu wakae tayari kunipokea kwa sababu ninakuja kwa mtindo wa aina yake. Nakuja kuwashika,”alisema msanii huyo mwenye maskani yake Kiwalani, Dar es Salaam.

BASATA kuboresha tuzo za muziki za Kili

BARAZA la Sanaa la Taifa (BASATA) linatarajia kuzipa taswira mpya tuzo za muziki za Tanzania, kuanzia zile zitakazofanyika mwaka 2012.
Katibu Mtendaji wa BASATA, Ghonche Materego alisema mjini Dar es Salaam mwanzoni mwa wiki hii kuwa, tayari bodi ya baraza hilo imeshapitisha uamuzi wa kuboresha tuzo hizo.
Materego alisema hayo wakati wa Jukwaa la Sanaa linalofanyika kila Jumatatu kwenye ukumbi za baraza hilo uliopo Ilala Sharrifu Shamba mjini Dar es Salaam.
Alisema lengo la uamuzi huo ni kuzifanya tuzo hizo ziwe na mvuto, ubora na kuwa maarufu katika ukanda mzima wa Afrika Mashariki kutokana na jinsi zitakavyoandaliwa na kufanyika.
“Baraza kila mara limekuwa likifanyiakazi mapendekezo na michango ya wadau, hivyo kuanzia tuzo za muziki za mwaka 2012, kutakuwa na marekebisho makubwa yatakayoshirikisha wadau wengi na lengo kuu ni kuzipa taswira mpya na kuzifanya zizidi kuwa na ubora,” alisisitiza.
Materego alisema wamekuwa wakizifanyia maboresho tuzo hizo kila mwaka, lakini baadhi ya wadau wamekuwa wakizilalamikia kwa madai kuwa, hazijakidhi ubora na hadhi inayotakiwa.
Alitoa mwito kwa wadau kujikita kwenye kutoa changamoto za kujenga, lakini huku wakielewa kwamba, tuzo hizo hazina muda mrefu kiasi cha kuweza kumaliza changamoto zote zilizopo.
“BASATA iko wazi muda wote kupokea changamoto na michango ya wadau, ndiyo maana kwenye mpango mkakati wa Baraza wa mwaka 2011-2014, tumebeba kwa kiwango kikubwa ushauri uliopatikana kwenye jukwaa hili la sanaa,” alisema Materego.
Awali, msanii Witness anayepiga muziki wa miondoko ya hip hop aliwasilisha mada kuhusu uzoefu wake kwenye tuzo mbalimbali za muziki barani Afrika.
Katika mada yake hiyo, Witness alieleza kukerwa kwake na tabia ya vyombo vya habari na kumbi za burudani nchini kupiga nyimbo za nje kwa kiwango kikubwa pasipo kuzipa nafasi zile za nyumbani.
“Ukienda Afrika Kusini radio na kumbi zao za burudani hupiga kwa asilimia kubwa muziki wao na hiki ndicho kinaufanya muziki na wanamuziki wa nchi hiyo kuvuma na kutambulika dunia nzima. Hapa kwetu ni tofauti, utakumbana na miziki ya akina 50 Cent na Ja Rule, kuna haja ya hili kusimamiwa kikamilifu,” alisema.

Mwalala ampibu Timbe

Na Emmanuel Ndege
MSHAMBULIAJI wa zamani wa klabu ya Yanga, Bernard Mwalala ametua nchini kwa ajili ya kufanya mazungumzo na Kocha Sam Timbe.
Mwalala alitua nchini wiki iliyopita kwa ajili ya kufanyiwa majaribio na Timbe ili aweze kuichezea tena Yanga msimu ujao.
Mshambuliaji huyo aliyeichezea Yanga kwa mafanikio makubwa, alikuwepo uwanjani wakati timu hiyo ilipomenyana na mahasimu wao Simba katika mechi ya ligi na kutoka sare ya bao 1-1.
Akizungumza na Burudani mjini Dar es Salaam wiki hii, Mwalala alisema amekuja nchini kwa ajili ya kukutana na Timbe ili kuangalia kama anaweza kumfanyia majaribio.
"Napenda kujiunga tena na Yanga. Nilikuwa Uganda kwa siku chake pale SC Villa, sasa nataka kurejea kuitumikia klabu hii, ambayo naipenda toka moyoni mwangu,"alisema mchezaji huyo ambaye ni raia wa Kenya.
Mmoja kati ya viongozi wa benchi la ufundi la timu hiyo, ambaye hakutaka kutajwa jina lake gazetini, alisema mchezaji huyo ameshafanya mazungumzo na Timbe.
Mchezaji huyo pia amekuwa akifika kwenye mazoezi ya Yanga mara kwa mara yanayofanyika katika uwanja wa Uhuru huku akionyesha kuvutiwa na wachezaji waliopo kwenye kikosi hicho.
Akizungumzia ujio wa mchezaji huyo, Timbe alisema anamfahamu vizuri Mwalala na ana imani ataweza kuisaidia timu hiyo katika msimu ujao wa ligi kuu.
Hata hivyo, Timbe alisema atalazimika kumfanyia majaribio mchezaji huyo kabla ya kuamua kumsajili au la.

Simba yaikodia ndege TP Mazembe



KIKOSI cha wachezaji 20 wa Simba kinatarajiwa kutua nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo wiki jayo kwa ajili ya pambano lao dhidi ya TP Mazembe.
Simba na TP Mazembe zinatarajiwa kumenyana mwishoni mwa wiki ijayo, katika mechi ya awali ya raundi ya pili ya michuano ya klabu bingwa Afrika kabla ya kurudiana wiki mbili baadaye mjini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, msafara huo utawajumuisha mashabiki 25 pamoja na wabunge na baadhi ya wafanyabiashara maarufu nchini.
Rage alisema mipango yote kwa ajili ya safari hiyo inaendelea vizuri na kuongeza kuwa, wana imani kubwa ya kufanya vizuri katika mchezo huo.
Mwenyekiti huyo alisema kamati ya utendaji ya Simba inatarajiwa kukutana mwishoni mwa wiki hii kwa ajili ya kupanga mikakati zaidi ya kushinda pambano hilo.
Kwa mujibu wa Rage, uongozi umewaandalia wachezaji zawadi murua iwapo watashinda mechi hiyo. Hata hivyo, Rage hakuwa tayari kutaja zawadi hizo.
Habari zaidi zimeeleza kuwa, benchi la ufundi la Simba limeshapata kanda za video za mechi mbalimbali za TP Mazembe kwa ajili ya kusoma mbinu za wapinzani wao.
Simba itakwenda Congo baada ya mechi mbili za ligi kati yake na Ruvu Shooting na AFC ya Arusha. Ilitarajiwa kucheza na Ruvu Shooting jana mjini Morogoro kabla ya kuvaana na AFC keshokutwa mjini Arusha. Naye Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ alijigamba jana kuwa, wamejiandaa vyema kuwashinda wapinzani wao na kusisitiza kuwa, ushindi ni lazima.

Mosha abwaga manyanga Yanga



HALI ndani ya klabu ya Yanga imeendelea kuchafuka baada ya Makamu Mwenyekiti, Davis Mosha kuandika barua ya kujiuzulu wadhifa huo.
Taarifa za kuaminika zilizopatikana jana na kuthibitishwa na kiongozi mmoja wa juu wa Yanga zimeeleza kuwa, Mosha aliwasilisha barua hiyo juzi.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, Mosha amefikia uamuzi huo kutokana na kuzuka tena kwa hali ya kutokuelewana kati yake na Mwenyekiti, Llyod Nchunga na mfadhili mkuu wa klabu hiyo, Yusuf Manji.
Mosha ametangaza uamuzi wake huo siku chache baada ya kurejea nchini kutoka Uingereza na kushirikiana na viongozi wenzake wa Yanga katika kuiandaa timu kwa ajili ya mechi yao dhidi ya Simba.
Makamu Mwenyekiti huyo, ambaye imeelezwa kuwa ana nguvu kubwa ya kulinyima raha kundi la Friends of Simba, amekuwa haelewani na Nchunga licha ya kukutanishwa mara kadhaa kwa lengo la kumaliza tofauti zao.
Habari zaidi zimeeleza kuwa, Mosha aliandika barua hiyo baada ya kupata shinikizo kubwa kutoka kwa wajumbe wa kamati, kufuatia uamuzi wao wa kubariki kujitoa kwa Manji kuifadhili klabu hiyo.
Imeelezwa kuwa katika kikao cha kumjadili Manji, Mosha alionekana kuwa na msimamo mkali wa kutaka uongozi usimpigie magoti mfadhili huyo, ambao ulipingwa vikali na Nchunga.
Yanga imejikuta ikiingia kwenye mzozo mwingine mkubwa baada ya Manji kuandika barua ya kujiuzulu kwa kile alichodai, kuandamwa na kashfa za kuihujumu timu hiyo.
Uamuzi huo wa Manji umeugawa uongozi wa klabu hiyo katika makundi mawili, ambapo moja linaupinga na kumtaka arejee wakati lingine limebariki kuondoka kwake na kutaka asinyenyekewe.
“Mosha ameamua kuachia ngazi ili kulinda heshima yake na kumwacha Nchunga afanye anavyotaka,” kimesema chanzo cha habari.
Kuna habari kuwa, huenda wajumbe wengine zaidi wa kamati ya utendaji ya Yanga wakatangaza kujiuzulu, kufuatia kubainika kuwepo kwa mipango ya kuwatimua kwenye uongozi watu wanaompinga Manji.
Juhudi za kumtafuta Nchunga ili athibitishe taarifa hizo, hazikufanikiwa jana kwa vile kila alipopigiwa simu yake ya mkononi, haikuwa na majibu.

BINGWA KOMBE LA NSSF KUPATA Mil 3.5/-

MKURUGENZI wa Uendeshaji wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Crescentius Magori (kushoto) akikabidhi vifaa vya michezo kwa Katibu wa klabu ya Uhuru, Rashid Zahor (kulia) katika hafla iliyofanyika jana makao makuu ya mfuko huo mjini Dar es Salaam. Katikati ni Mwenyekiti wa kamati ya mashindano ya Kombe la NSSF, Masoud Saanani. (Picha kwa hisani ya Francis Dande wa globu ya Jami).

BINGWA wa michuano ya soka ya Kombe la NSSF kwa mwaka 2011, atazawadiwa kitita cha sh. milioni 3.5 wakati mshindi wa netiboli atapata sh. milioni tatu.
Akitangaza zawadi hizo kwa waandishi wa habari mjini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Uendeshaji wa NSSF, Crescentius Magori alisema, mshindi wa pili katika soka atazawadiwa sh. milioni 2.5 na watatu sh. milioni 1.5.
Magori alisema mshindi wa pili wa netiboli atazawadiwa sh. milioni mbili wakati mshindi wa tatu atapata sh. milioni moja. Alizitaja zawadi zingine kuwa ni sh. milioni 2.5 kwa wafungaji wa michuano yote miwili.
Kwa mujibu wa Magori, wameamua kuiboresha zaidi michuano ya mwaka huu kwa kuongeza zawadi kwa washindi, ambapo jumla ya zawadi zote ni sh. milioni 14.
Mkurugenzi huyo alisema NSSF inaona fahari kuandaa michuano hiyo kwa vile imekuwa ikisaidia kutangaza shughuli zake na kuwataka washindi waheshimu kanuni walizojiwekea.
Alisema kamati ya mashindano imejitahidi kuzifanyiakazi dosari zote zilizojitokeza katika michuano iliyopita na kuongeza kuwa, katika siku zijazo, huenda ikazishirikisha timu zingine kutoka nchi za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano hayo, Masoud Saanani alisema, jumla ya timu 17 zinatarajiwa kuchuana katika mchezo wa soka na zingine 11 katika netiboli.
Masoud alivitaja vyombo vya habari vitakavyoshiriki katika michuano ya mwaka huu kuwa ni wenyeji NSSF, Mlimani Media, Changamoto, New Habari, IPP Limited, Global Publishers, Habari Zanzibar, Mwanahalisi na Radio Kheri.
Vingine ni Free Media, Uhuru Publications Ltd, Tumaini Media, Mwananchi, Jambo Leo, Sahara Communications, Business Times na TBC.
Mwenyekiti huyo alisema michuano ya mwaka huu itachezwa kwa mtindo wa ligi, ambapo timu za soka zimegawanywa katika makundi manne, moja likiwa na timu tano na matatu yakiwa na timu nne kila moja.
Alisema kundi A litakuwa na timu za Business Times, Changamoto, NSSF na Mlimani Media wakati kundi B litakuwa na timu za Habari Zanzibar, Global Publishers, New Habari na Radio Kheri.
Kundi C litakuwa na timu za Uhuru, Mwananchi, Mwanahalisi, Tumaini Media na Sahara Communications wakati kundi D litakuwa na timu za IPP, TBC, Jambo Leo na Freee Media.
Kwa upande wa netiboli, Masoud alisema kundi A litakuwa na timu za NSSF, Global Publishers na Tumaini Media, kundi B timu za Mwananchi, Uhuru, New Habari na Free Media wakati kundi C litakuwa na timu za Business Times, Habari Zanzibar, TBC na IPP.
Michuano ya mwaka huu imepangwa kuanza Machi 19 hadi Aprili 16 mwaka huu na itachezwa kwenye viwanja vya TCC na Chuo Kikuu Kishiriki cha Ualimu (DUCE) vilivyopo Chang’ombe, Dar es Salaam.
Katika mechi za ufunguji, mabingwa watetezi wa soka, Business watamenyana na wenyeji NSSF wakati katika netiboli, Global Publishers watamenyana na Tumaini Media.

Wednesday, March 9, 2011

Soka si uadui



WACHEZAJI Juma Kaseja (juu kushoto) wa Simba na Shadrack Nsajigwa wa Yanga wakipongezana mara baada ya pambano kati ya timu hizo kumalizika mwishoni mwa wiki iliyopita.

PICHA nyingine chini inamuonyesha mshambuliaji Emmanuel Okwi wa Simba na Isaack Boakye wa Yanga wakipozi katika picha ya pamoja

Marlaw, Besta kufunga ndoa keshokutwa


Wanamuziki wawili wa muziki wa bongo fleva hapa nchini, Marlaw na Besta Jumamosi hii wanatarajia kuwa mwili mmoja kwa kufunga pingu za maisha.
Mmiliki wa blogu hii anawatakia kila la heri katika maisha ya ndoa,mtangulizeni Mungu katika ndoa yenu na mpendane,mvumiliane na kuheshimiana. Pia mawasiliano yawe nguzo yenu katika kudumisha urafiki wenu na mapenzi yenu.

Friday, March 4, 2011

Simba, Yanga nani zaidi kesho?


Na Rashid Zahor
HAYAWI hayawi yamekuwa. Baada ya subira na majigambo ya muda mrefu, hatimaye miamba miwili ya soka nchini, Simba na Yanga leo inakutana katika mechi ya ligi kuu ya Vodacom, itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Pambano hilo linalogusa hisia za mashabiki wengi wa soka nchini, linatarajiwa kuwa kali na gumu kwa vile kila timu imepania kushinda ili kujiweka kwenye nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa.

Katika mechi ya mzunguko wa kwanza, iliyochezwa Oktoba 16 mwaka jana kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza, Yanga iliichapa Simba bao 1-0.

Je, Yanga itaendeleza ubabe wake kwa Simba ama vijana hao wa Msimbazi watalipiza kisasi kwa wenzao wa Jangwani?

Swali hilo na mengineyo kadhaa ndiyo yaliyotawala hisia za mashabiki wa klabu hizo mbili, ambao baadhi yao huangua kilio, kupatwa na huzuni au hata kushindwa kula kila timu yao inapofungwa.

Hadi sasa, Yanga inaongoza ligi hiyo kwa kuwa na pointi 38 baada ya kucheza mechi 17, ikifuatiwa na Simba yenye pointi 37 kutokana na michezo 16. Azam ni ya tatu kwa kuwa na pointi 36 katika mechi 18 ilizocheza.

Simba itaingia uwanjani ikitokea mafichoni Zanzibar, ilikokwenda kuweka kambi kwa ajili ya kujiandaa na mechi hiyo wakati Yanga itatokea kambini Bagamoyo mkoani Pwani.

Mechi hiyo itakuwa mtihani wa kwanza kwa Kocha Sam Timbe wa Yanga, aliyeanza kuinoa timu hiyo mwishoni mwa mwezi uliopita, lakini ni ya kawaida kwa Kocha Patrick Phiri wa Simba, ambaye ameshazoea mikikimikiki ya timu hizo mbili.

Timbe alikaririwa juzi akisema kuwa, amemkabidhi jukumu la kuiongoza timu hiyo, kiungo Athumani Iddi ‘Chuji’, ambaye amerejea kwenye kiwango chake cha kawaida baada ya kusimamishwa kwa miezi kadhaa na kocha wa zamani, Kostadin Papic.

Kocha huyo kutoka Uganda alisema, timu yake itawakabili wapinzani wao, ikiwa haina hofu kwa kuwa wanatambua vyema umuhimu wa mechi hiyo na wamejiandaa kwa kila hali kuibuka na ushindi.

Hata hivyo, Timbe alisema timu yake itamkosa kiungo mchezeshaji, Ernest Boakye kutokana na kuwa majeruhi. Alisema mchezaji huyo anasumbuliwa na maumivu ya goti la kushoto.

Kwa upande wa Simba, itawakosa kiungo Hillary Echessa na beki John Owino kutokana na kuwa majerehu. Pia itamkosa kiungo Mohamed Banka, aliyetimuliwa kambini kwa makosa ya utovu wa nidhamu. Lakini itakuwa na faraja kubwa baada ya mshambuliaji wake nyota, Emmanuel Okwi kupona maumivu ya kifundo cha mguu na kurejea uwanjani.

Ushindani mkali katika mechi ya leo unatarajiwa kuwa kwa washambuliaji, Jerry Tegete, Davis Mwape wa Yanga, Mbwana Samatta na Mussa Hassan ‘Mgosi’ wa Simba, ambao kila mmoja amepania kufunga mabao.

Pambano hilo litachezeshwa na mwamuzi Oden Mbaga kutoka Dar es Salaam, ambaye anatambuliwa na Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA). Atasaidiwa na Mohamed Mkono wa Tanga na Maxmillian Mkongolo wa Rukwa. Mwamuzi wa akiba atakuwa Army Sentimea wa Dar es Salaam.

Viingilio katika mechi hiyo ni sh. 30,000 kwa jukwaa la VIP A, sh. 20,000 jukwaa la VIP B, sh. 10,000 jukwaa la VIP C, sh. 7,000 na sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya chungwa na bluu na sh. 3,000 kwa viti vya rangi ya kijani mzunguko.

Timu zinatarajiwa kupangwa hivi:

Yanga: Yaw Berko, Shadrack Nsajigwa, Stephano Mwasika, Chacha Marwa, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Athumani Iddi, Ibrahim Job, Nsa Job, Kigi Makasi, Davis Mwape, Jerry Tegete.

Simba: Ally Mustapha, Haruna Shamte, Amir Maftah, Juma Nyoso, Kelvin Yondani, Jerry Santo, Rashid Gumbo, Mbwana Samatta, Patrick Ochan, Mussa Hassan ‘Mgosi’ na Nico Nyagawa.

Msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom hadi sasa ni kama ifuatavyo:

P W D L GF GA Pts
Yanga 17 11 5 1 23 4 38
Simba SC 16 12 1 3 31 14 37
Azam 18 11 3 4 33 12 36
Mtibwa Sugar 18 8 6 4 18 17 30
Kagera Sugar 18 8 5 5 18 15 29
JKT Ruvu 18 6 7 5 17 16 25
Toto African 18 5 5 8 16 21 20
African Lyon 18 4 7 7 14 23 19
Polisi Dodoma 18 4 5 9 8 16 17
Ruvu Shooting 17 3 6 8 12 19 15
Maji Maji 18 2 6 10 10 19 12
AFC 18 3 2 13 12 36 11