KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 10, 2011

Simba yaikodia ndege TP Mazembe



KIKOSI cha wachezaji 20 wa Simba kinatarajiwa kutua nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo wiki jayo kwa ajili ya pambano lao dhidi ya TP Mazembe.
Simba na TP Mazembe zinatarajiwa kumenyana mwishoni mwa wiki ijayo, katika mechi ya awali ya raundi ya pili ya michuano ya klabu bingwa Afrika kabla ya kurudiana wiki mbili baadaye mjini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, msafara huo utawajumuisha mashabiki 25 pamoja na wabunge na baadhi ya wafanyabiashara maarufu nchini.
Rage alisema mipango yote kwa ajili ya safari hiyo inaendelea vizuri na kuongeza kuwa, wana imani kubwa ya kufanya vizuri katika mchezo huo.
Mwenyekiti huyo alisema kamati ya utendaji ya Simba inatarajiwa kukutana mwishoni mwa wiki hii kwa ajili ya kupanga mikakati zaidi ya kushinda pambano hilo.
Kwa mujibu wa Rage, uongozi umewaandalia wachezaji zawadi murua iwapo watashinda mechi hiyo. Hata hivyo, Rage hakuwa tayari kutaja zawadi hizo.
Habari zaidi zimeeleza kuwa, benchi la ufundi la Simba limeshapata kanda za video za mechi mbalimbali za TP Mazembe kwa ajili ya kusoma mbinu za wapinzani wao.
Simba itakwenda Congo baada ya mechi mbili za ligi kati yake na Ruvu Shooting na AFC ya Arusha. Ilitarajiwa kucheza na Ruvu Shooting jana mjini Morogoro kabla ya kuvaana na AFC keshokutwa mjini Arusha. Naye Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ alijigamba jana kuwa, wamejiandaa vyema kuwashinda wapinzani wao na kusisitiza kuwa, ushindi ni lazima.

No comments:

Post a Comment