KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor@hotmail.com '

Monday, June 17, 2013

STARS, IVORY COAST ZAINGIZA MIL 500/-

Mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia, Kundi C, Kanda ya Afrika kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Ivory Coast (The Elephants) iliyochezwa jana (Juni 16 mwaka huu) imeingiza sh. 502,131,000 kutokana na watazamaji 57,203.

Tiketi za kushuhudia mechi hiyo ziliuzwa kwa sh. 5,000, sh. 7,000, sh. 10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000.

Mgawanyo wa mapato hayo ulikuwa kama ifuatavyo; asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ni sh. 76,596,254.24 wakati wa gharama za uchapaji tiketi ni sh. 7,809,104.

Asilimia 15 ya uwanja sh. 62,658,846.26, asilimia 20 ya gharama za mechi sh. 83,545,128.35 na asilimia 5 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh. 20,886,282.09.

Asilimia 60 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) sh. 250,635,385.06 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 12,531,769.25 ambayo ni asilimia 5 kutoka kwenye mgawo wa TFF.

Mechi iliyopita ya Stars dhidi ya Morocco (Lions of the Atlas) kwenye uwanja huo iliingiza sh. 226,546,000.

TAIFA STARS KAMBINI TENA JULAI 4


Kocha wa Taifa Stars, Kim Poulsen ameiita tena kambini timu hiyo Julai 4 mwaka huu kujiandaa kwa mechi ya kutafuta tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) zitakazofanyika mwakani nchini Afrika Kusini.

Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager inavunja kambi leo (Juni 17 mwaka huu) baada ya mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia, kundi C Kanda ya Africa dhidi ya Ivory Coast iliyochezwa jana (Juni 16 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kim amesema wachezaji watakaoitwa kambin ni wote walioko kwenye timu hivi sasa isipokuwa Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu wanaocheza mpira nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) katika klabu ya TP Mazembe Englebert.

Wachezaji hao ni Juma Kaseja, Aishi Manula, Aggrey Morris, Mwadini Ally, Ally Mustafa, Shomari Kapombe, Kevin Yondani, Erasto Nyoni, Haroub Nadir, Mwinyi Kazimoto, Frank Domayo, Mrisho Ngasa, Khamis Mchana, Amri Kiemba, Salum Abubakar, Simon Msuva, John Bocco, Vicent Barnabas, Mudathiri Yahya, Athuman Idd, Haruni Chanongo na Zahoro Pazi.

Mechi hiyo namba 37 dhidi ya Uganda (The Cranes) itachezwa jijini Dar es Salaa kati ya Julai 12 na 14 mwaka huu wakati ile ya marudiano itafanyika wiki mbili baadaye katika Uwanja wa Mandela ulioko Namboole nje kidogo ya Jiji la Kampala.

President Kikwete Tours Sunderland Football Club

President Dr.Jakaya Mrisho Kikwete and Chairman and owner of Sunderland Football Club Mr.Ellis Short pose with some students who study football skills at the club’s Academy of Light in Sunderland yestarday afternoon. The Club in collaboration with Symbion Power Tanzania Limited have agreed to build a state of the art football academy in Dar es Salaam at the request of President Kikwete. President Kikwete is London for a three days working visit.
President Dr.Jakaya Mrisho Kikwete talks to pupils attending  some lessons on football skills AND HEALTH  at Sunderland’s Association Football Club Academy of Light in Sunderland yestarday afternoon.
President Dr.Jakaya Mrisho Kikwete in conversation with Sunderland’s Association Football Club  Chairman and owner Mr.Ellis Short at the Club’s Stadium of Light in Sunderland yestarday afternoon.
President Dr.Jakaya Mrisho Kikwete and his delegation pose with some students who attend football training at Sunderland’s  Association Football Club Stadium of Light Academy yestarday afternoon. Others in picture from left are Symbion’s Power Limited CEO Mr.Paul Hinks(left), Ilala member of parliament Hon. Musa Zungu(Second left), Minister for Information,Youth ,Culture and Sports Dr.Fenella Mukangara(fourth left) and Minister for Land and Human Settlement Prof.Anna Tibaijuka(right).
President  Dr.Jakaya Mrisho Kikwete unveils Sunderland’s Association Football plaque at the club’s Academy of Light yestarday afternoon when the President and his delegation toured the club. On the left, looking on, is the Club’s Chairman and Owner Ellis Short.(photo by Freddy Maro).

LUCY NDIYE MREMBO WA MWANZA


SHINDANO la kumsaka mrembo wa mkoa wa Mwanza kwa mwaka 2013, kiliteguliwa mwishoni mwa wiki iliyopita baada ya Lucy Charles, msomi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino kuwabwaga warembo wengine 13 waliojitokeza kuwania taji hilo.


Nyota ya mrembo huyo ilianza kuonekana mapema katika mavazi yote aliyovaa, lakini zaidi aliwapagawisha mashabiki wa urembo waliofurika katika ukumbi wa Yatch club baada ya kujibu swali kwa ustadi lililouliza ni changamoto ipi kubwa walionayo vijana wa leo.

Mshindi wa pili katika shindano hilo alikuwa Judith Josephat na mshindi wa tatu ni Suzan Ikombe.
Washindi hao watauwakilisha mkoa wa Mwanza katika shindano la kanda ya ziwa litakalofanyika mwishoni mwa mwezi huu.

Sunday, June 16, 2013

TAIFA STARS YACHAPWA 4-2 NA IVORY COAST


MATUMAINI ya timu ya soka ya Taifa, Taifa Stars kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za 2014 leo yameyeyuka baada ya kuchapwa mabao 4-2 na Ivory Coast katika mechi ya kundi C iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kipigo hicho kimeifanya Taifa Stars iporomoke nafasi ya tatu katika msimamo wa kundi hilo ikiwa na pointi sita baada ya kucheza mechi tano, ikiwa nyuma ya Ivory Coast inayoongoza kwa kuwa na pointi 13, ikifuatiwa na Morocco yenye pointi nane. Gambia inashika mkia kwa kuambulia pointi moja.

Licha ya kufungwa, Taifa Stars ilionyesha kiwango cha juu cha soka na magoli yake yalikuwa ya kifundi zaidi ikilinganishwa na wapinzani wao, ambao mabao yao yalitokana na makosa ya kizembe ya mabeki wa Tanzania.

Mshambuliaji Yaya Toure anayechezea klabu ya Manchester City ya England ndiye aliyeibeba Ivory Coast baada ya kuifungia mabao mawili kati ya manne.

Taifa Stars ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya kwanza mfungaji akiwa Amri Kiemba baada ya kupokea pasi kutoka kwa Mbwana Samatta kufuatia mpira wa kurushwa na Erasto Edward Nyoni kusababisha kizazaa langoni mwa Tembo wa Abidjan.

Ivory Coast ilisawazisha bao hilo dakika ya 15 kupitia kwa Lacina Traore baada ya mabeki wa Stars kuzembea kuokoa na Yaya Toure akafunga la pili kwa mpira wa adhabu dakika ya 23, nje kidogo ya eneo la hatari.

Stars ilirudi mchezoni na kufanikiwa kusawazisha bao hilo dakika ya 35 mfungaji Ulimwengu aliyeunganisha krosi maridadi ya Shomary Kapombe. Hata hivyo, Ivory Coast wakapata penalti rahisi baada ya Gervinho kujiangusha wakati anakabiliana na Nadir Haroub ‘Cannavaro’ . Bao hilo lilifungwa na Yaya Toure dakika ya 43.

Mabadiliko yaliyofanywa na kocha Mdenmark, Kim Poulsen dakika ya 87 kumtoa kiungo Mwinyi Kazimoto na kumuingiza mshambuliaji Vincent Barnabas yaliigharimu Tanzania kwa kufungwa bao la nne na kupotea kabisa mchezoni.

Baada ya kutoka Kazimoto, aliyetekeleza majukumu yake vizuri leo, Ivory Coast wakatawala sehemu ya kiungo na kutengeneza bao la nne lililofungwa na Bonny Wilfred dakika ya 88.

Taifa Stars: Juma Kaseja, Erasto Nyoni, Shomary Kapombe/Khamis Mcha dk 85, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Frank Domayo, Mwinyi Kazimoto/Vincent Barnabas dk 87, Salum Abubakar, Thomas Ulimwengu, Mbwana Samatta na Amri Kiemba.

Ivory Coast: Boubakar Barry, Arthur Boca, Didier Zakora, Solomon Kalou/Sio Giovanni, Gervais Yao, Jean Jarques Gosso Gosso, Alain Aurier, Lacina Traore/Bonny Wilfred, Yaya Toure, Geoffrey Serey na Suleiman Bamba/Nori Koffi Christian.

Friday, June 14, 2013

KAISHANGILIENI TAIFA STARS KESHO-KAVISHE



WADHAMINI wa timu ya Taifa (Taifa Stars), Kilimanjaro Premium Lager wamewaomba watanzania washikane na kuungana pamoja wakati wa mechi dhidi ya Ivory Coast kutafuta tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia kwani kuna watanzania ambao tayari wamekata tamaa.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo, Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, George Kavishe alisema Taifa Stars inatakiwa kuungwa mkono na kushangiliwa kwa nguvu kwani wachezaji wameonesha kuwa wana uwezo.

“Hawa ni wanajeshi wetu…nawaomba watanzania wajitokeze kwa wingi…tuwape sapoti na tuoneshe uzalendo kwani kwenye mpira lolote linawezekana,” alisema. Kavishe alisema watanzania lazima welewa timu hii bado ni changa na ina wachezaji wapya wenye umri mdogo ambao wameonesha uwezo mkubwa.

“Hata ikitokea tusifuzu kwenda Kombe la Dunia, vijana wameshaonesha dalili nzuri na tuna imani tutafanya vizuri katika mashindano mengine kama AFCON na CHAN,” alisema.

Aliwataka wachezaji kutulia uwanjani na kutobabaishwa na ukubwa wa timu ya Ivory Coast kwani wana uwezo wa kuwafunga na kushangaza dunia nzima Jumapili.

“Hii ni kama fainali kwa Ivory Coast na wao pia wamebabaika na kuitilia maanani kabisa mechi hii kwa sababu tukiwafunga ina maana hawatakuwa na uhakika wa kufuzu katika hatua inayofuata,” alisema Kavishe.

Bia ya Kilimanjaro Premium Lager imetimiza mwaka mmoja tangu ianze kuidhamini Taifa Stars na wadau mbalimbali wamesifia udhamini huu kwani umeleta mabadiliko makubwa katika timu ya Taifa.

Timu ya Ivory Coast iliwasili nchini Alhamisi usiku na imeweka kambi katika hoteli ya Bahari Beach, Kunduchi tayari kwa mechi itakayopigwa katika Uwanja wa Taifa JUmapili hii saa tisa kamili.

Kwa mujibu wa TFF maandalizi yote yamekamilika na mechi hii inatarajiwa kuangaliwa na maelfu ya watanzania watakaojitokeza uwanjani na kupitia runinga pia. Ivory Coast inaongoza katika kundi C ikiwa na pointi 10, Tanzania ya tatu na pointi 6, Morocco ya tatu na pointi 5 na Gambia ni ya nne na pointi 1.

Wakati timu ya Ivory Coast imewasili nchini jana usiku (Juni 13 mwaka huu) kwa ndege maalum, kocha wa timu hiyo Sabri Lamouchi na mwenzake wa Taifa Stars, Kim Poulsen watakutana na waandishi wa habari kuzungumzia mechi yao kesho.

Mkutano huo utafanyika kesho (Juni 15 mwaka huu) saa 4 kamili asubuhi kwenye ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Mkutano huo pia utajumuisha makocha wa timu zote mbili. Ivory Coast inafanya mazoezi yake ya kwanza leo (Juni 14 mwaka huu) saa 9 alasiri kwenye viwanja vya Gymkhana.

Timu zote kesho (Juni 15 mwaka huu) zitafanya mazoezi ya mwisho kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Ivory Coast watafanya mazoezi saa 9 kabla ya kuwapisha Stars saa 10 kamili. Maandalizi yanaendelea vizuri ikiwemo kuwasili kwa maofisa wote wa mechi itakayochezwa Jumapili saa 9 kamili alasiri.

Wakati huo huo, mauzo ya tiketi kwa ajili ya mechi hiyo yameanza leo mchana (Juni 14 mwaka huu) katika vituo vya Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, City Sports Lounge iliyoko Mtaa wa Samora na Azikiwe, Dar Live Mbagala, BMM Salon iliyoko Sinza Madukani na Uwanja wa Taifa.

Mauzo yataendelea kesho katika vituo hivyo, wakati siku ya mchezo yatafanyika Uwanja wa Taifa. Viingilio katika mechi hiyo ya mchujo ya Kombe la Dunia, Kanda ya Afrika katika kundi C ni sh. 5,000, sh. 7,000, sh. 10,000, sh. 15,000 VIP C, sh. 20,000 VIP B na VIP A sh. 30,000. Pia kuna kadi maalumu 100 kwa viti vya Wageni Maalumu (VVIP) zinazopatikana kwa sh. 50,000 katika ofisi za TFF.

SIMBA, YANGA RUKSA KWENDA DARFUR, LAKINI CECAFA YAZIPIGA CHINI



WAZIRI wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara

SERIKALI imeziruhusu klabu za Simba SC, Yanga SC za Dar es Salaam na Super Falcons ya Zanzibar kwenda Sudan kushiriki michuano ya Klabu Buingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame.

 Naibu Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo, Amos Makalla amefanya Mkutano na Waandishi wa Habari mjini Dodoma asubuhi ya leo kusema wameruhusu klabu hizo ziende Sudan baada ya kuhakikishiwa na Serikali ya nchi hiyo kwamba itatoa ulinzi wa kutosha dhidi ya timu za Tanzania.

Makalla amesema wameandikiwa barua na Serikali ya Sudan ikiwahakikishia kwamba timu za Tanzania zitapewa ulinzi mkubwa zisiathirike na machafuko yanayoedelea Sudan.

 Kufuatia tamko la Serikali kuziruhusu klabu hizo sasa ziende Sudan, sasa ni juu yao ya klabu hizo kuamua kwenda au kutokwenda.

Lakini Katibu wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Mkenya Nicholas Musonye amekwshatishia atazichukulia hatua kali klabu hizo zisipokwenda.

Juzi Serikali kupitia Makalla ilitoa tamko la kuzuia klabu za Tanzania kutokwenda Sudan kutokana na machafuko yanayoendelea nchini humo.

 Kufuatia tamko hilo, jana Yanga, ambao ni mabingwa watetezi kwa miaka miwili mfululizo, walitangaza kuvunja kambi yao hadi wiki mbili baadaye, wakati Kombe la Kagame linaanza kutimua vumbi Juni 18, mwaka huu.

 Yanga wamepangwa Kundi C katika michuano hiyo pamoja na Ports ya Djibouti, Express ya Uganda na Vital 'O' ya Burundi, wakati wapinzani wao wa jadi, Simba SC wamepangwa Kundi A pamoja na wenyeji El-Mereikh, Elman ya Somalia na APR ya Rwanda.

Katika michuano hiyo inayotarajiwa kufikia tamati Julai 2, mwaka huu mjini Khartoum, Sudan, mabingwa wa Kenya, Tusker wamepangwa Kundi B pamoja na wenyeji wengine, Al-Hilal, Falcons ya Zanzibar, Al Ahly Shandy ya Sudan na Al-Nasir Juba ya Sudan Kusini.

Yanga wataanza kampeni zao za kutetea taji hilo Juni 20 kwa kumenyana na Express, wakati Simba SC itashuka dimbani Juni 21 kufungua dimba na El-Mereikh, na mechi zote zitachezwa Elfashar.

TFF YATOA NOTISI YA MKUTANO MKUU



Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga ametoa notisi kwa wajumbe wa Mkutano Mkuu Maalumu wa Shirikisho utakaofanyika Julai 13 mwaka huu kwenye ukumbi wa NSSF Waterfront jijini Dar es Salaam ukiwa na ajenda moja ya marekebisho ya Katiba.

Notisi hiyo imetolewa juzi (Juni 12 mwaka huu). Rais ameitisha Mkutano huo kwa mujibu wa Ibara ya 25(1) ya Katiba ya TFF baada ya kupata maagizo kutoka Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kwa barua yake ya Aprili 29 mwaka huu.

Ajenda rasmi na taarifa nyingine zitatumwa kwa wajumbe siku 15 kabla ya Mkutano huo kwa mujibu wa Ibara ya 25(4) ya Katiba ya TFF.

Wanachama wa TFF ambao ni vyama vya mikoa, vyama shiriki na klabu za Ligi Kuu wanatakiwa kutuma majina ya wajumbe halali. TFF inapenda kuwakumbusha wanachama wake kutuma majina ya wajumbe halali ili kufanikisha maandalizi ya Mkutano huo.

Ni vizuri kuhakikisha kuwa jina linalotumwa ni la mjumbe halali wa Mkutano Mkuu kwa mujibu wa Katiba ya TFF.

RAMBIRAMBI KIFO CHA ABDALLA MSAMBA



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha mchezaji wa zamani wa timu za Pan Africans, Simba na Taifa Stars, Abdallah Msamba kilichotokea juzi usiku (Juni 12 mwaka huu) jijini Dar es Salaam.

Msiba huo ni mkubwa kwa wadau wa mpira wa miguu kwani kwa nyakati tofauti Msamba akiwa mchezaji, na baadaye kocha wa timu kadhaa alitoa mchango mkubwa kwa timu mbalimbali alizochezea na kufundisha ikiwemo Villa Squad, hivyo mchango wake tutaukumbuka daima.

TFF inatoa pole kwa familia ya marehemu Msamba, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA), Chama cha Mpira wa Miguu Wilaya ya Kinondoni (KIFA) na klabu ya Villa Squad na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.

Maziko ya mchezaji huyo yamefanyika leo (Juni 14 mwaka huu) katika makaburi ya Ndugumbi mkoani Dar es Salaam na kuhudhuriwa na mamia ya waombolezaji wakiwemo wachezaji wa zamani na viongozi mpira wa miguu nchini. Mungu aiweke roho ya marehemu Msamba mahali pema peponi. Amina

TENGA AMPONGEZA RAIS MPYA WA ZFA


Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga amempongeza Rais mpya wa Chama cha Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFA), Ravia Idarous Faina aliyechaguliwa katika uchaguzo mdogo uliofanyika hivi karibuni.

Amesema ushindi aliopata Faina unaonyesha jinsi wajumbe wa Mkutano Mkuu wa ZFA walivyo na imani naye katika kuhakikisha maendeleo ya mpira wa miguu visiwani humo.

Rais Tenga amesema ni imani yake kuwa Rais Faina ataendeleza ushirikiano uliopo kati ya TFF na ZFA kwa ajili ya ustawi wa mpira wa miguu katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na kumtakiwa kila kheri katika wadhifa wake huo mpya.

WAAMUZI WATATU WAFUNGIWA



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limefungia miezi mitatu waamuzi watatu walioshindwa kuchezesha mechi namba 32 ya Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) kati ya Mpwapwa Stars ya Dodoma na Machava FC ya Kilimanjaro iliyokuwa ichezwe Juni 2 mwaka huu Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.

 TFF kupitia Kamati yake ya Waamuzi iliyokutana katika kikao chake cha Juni 12 mwaka huu kupitia taarifa mbalimbali za waamuzi wa RCL ilibaini makosa yaliyofanywa na baadhi ya waamuzi na kuyatolea uamuzi.

Waamuzi hao waliofungiwa ambao wanatoka mkoani Singida ni Jilili Abdallah, Amani Mwaipaja na Theofil Tegamisho. Wamefungiwa kwa kutoripoti katika kituo walichopangiwa (Uwanja wa Jamhuri, Dodoma) na kutoa taarifa ya uongo kwa kushirikiana na Kamishna wa mechi hiyo.

Kanuni iliyotumika kuwafungia ni ya 28 kifungu (d) na (g) ya Ligi za TFF, na adhabu hiyo imeanza Juni 13 mwaka huu.

Waamuzi hao pamoja na kamishna badala ya kwenda Uwanja wa Jamhuri, wao walikwenda kwenye Uwanja wa Mgambo ulioko Mpwapwa na kuandika ripoti iliyoonesha kuwa timu ya Machava FC haikufika uwanjani wakati wakijua kuwa mechi hiyo ilitakiwa kuchezwa katika Uwanja wa Jamhuri

MR. NICE ATOSWA, CHAMELEONE ANG'ARA MAREKANI



NAIROBI, Kenya
KAMPUNI ya Grandpa Records ya Kenya imevunja mkataba wake na mwanamuziki Lucas Nkenda 'Mr. Nice'.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Refigah Slams amelieleza gazeti la Daily Nation la Kenya wiki hii kuwa, amefikia uamuzi huo baada ya Mr. Nice kukiuka makubaliano kati yao.

Mr. Nice, ambaye amehamishia makazi yake nchini Kenya, aliingia mkataba na kampuni hiyo miezi miwili iliyopita kwa ajili ya kusimamia kazi zake.

"Tumeamua kumwondoa Mr. Nice katika udhamini wa Grandpa Records kutokana na kukiuka makubaliano yetu," alisema Slams.

Slams amemwelezea Mr. Nice kuwa ni mtu asiye na ushirikiano na ni mgumu kufanya naye kazi.

Alisema tangu walipoingia naye mkataba, mwanamuziki huyo wa kitanzania amesababisha matatizo mengi katika kampuni yake, ambayo hakuwa tayari kuyataja.

"Kwa kifupi, Mr. Nice alikuwa ameingia mikataba na Sallam Sharaf na Lamar wa Tanzania na hakutueleza wakati anaingia mkataba na Grandpa Records,"alisema.

Mr. Nice alitarajiwa kufanya uzinduzi wa albamu yake mpya ya Chali wa Kibera hivi karibuni chini ya udhamini wa kampuni hiyo.

Katika hatua nyingine, mwanamuziki nyota wa Uganda, Jose Chameleone amezindua albamu yake mpya inayojulikana kwa jina la Badilisha nchini Marekani.

Chameleone alifanya uzinduzi wa albamu hiyo mwishoni mwa wiki iliyopita, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya wiki mbili nchini Marekani.

Mtandao wa Msn uliripoti juzi kuwa, tayari mwanamuziki huyo tajiri wa Kiganda ameshafanya maonyesho katika miji ya Seattle na Los Angeles.

Kwa mujibu wa mtandao huo, Chameleone anatarajiwa kufanya maonyesho mengine katika miji ya Dallas na Texas kabla ya kurejea Uganda mwezi ujao.

SIJAACHWA, NAIFURAHIA NDOA YANGU-INI EDO


LAGOS, Nigeria
MWIGIZAJI mwenye mvuto wa Nigeria, Ini Edo amesema si kweli kwamba ndoa yake na mumewe, Philip Ehigwina imevunjika.

Ini aliueleza mtandao wa Nigeriafilms wiki hii kuwa, hana matatizo yoyote na mumewe na kwamba anaifurahia ndoa yake.

Baadhi ya vyombo vya habari vya Nigeria viliripoti hivi karibuni kuwa, Ini hana furaha kwa sasa kutokana na ndugu wa mume wake kushinikiza aachwe.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, ndugu wa Philip hawafurahii kuona kuwa, mcheza filamu huyo ameshindwa kumzalia mtoto ndugu yao baada ya kuolewa miaka minne iliyopita.

"Mashemeji na wakwe wa Ini Edo wamemweleza Philip amuache kama hawezi kumzalia mtoto," zilieleza taarifa hizo.

Hata hivyo, Ini amekanusha vikali taarifa hizo kwa kusema kuwa, hana matatizo na mumewe wala ndugu zake.

"Sitajali mtakachoandika kama kitabadili ukweli kwamba naifurahia ndoa yangu. Nadhani mnapaswa kuachana na uzushi huu,"alisema In.

"Tangu siku ya kwanza nilipoolewa, mmekuwa mkizusha mambo mengi ya kishetani kwangu. Sielewi ni kwa nini hamtaki kuachana na upuuzi huu. Kamwe haitatokea,"alisisitiza.

NIMERITHI FIGA YA MAMA YANGU-OMOTOLA



LAGOS, Nigeria
MCHEZA filamu machachari wa Nigeria, Omotola Jalade amesema hajawahi kufanya operesheni ya aina yoyote kwa ajili ya kuupendezesha mwili wake.

Akihojiwa na gazeti la Encomium la Nigeria wiki hii, Omotola alisema amerithi umbile alilonalo kutoka kwa mama yake mzazi.

Mwanamama huyo mwenye sura na umbile lenye mvuto alisema amekuwa akifanya shughuli mbalimbali ili aweze kubaki kama alivyo.

"Hakuna siri katika mwonekano wangu, huo ndiyo ukweli ulivyo. Ukitazama picha ya mama yangu, anaonekana kama msichana. Hadi anafariki, tulizoea kumwita msichana,"alisema.

"Mama yangu alikuwa na umbile la kisichana hata alipokaribia kufikisha umri wa miaka 50. Alikuwa na umbile la kike hasa. Amenirithisha umbile hilo," aliongeza.

Omotola alisema ni kazi ngumu kulifanya umbile lake libaki kama lilivyo kutokana na mazingira ya kazi yake.

Mcheza filamu huyo aliyeolewa na rubani wa ndege na kuzaa naye watoto wanne, alisema pia kuwa hajawahi kutumia dawa za aina yoyote ili kunenepesha 'hips' zake.

"Hata mimi nimekuwa nikizisikia habari hizo, lakini hakuna kitu kama hicho. Kamwe sijawahi kutumia dawa ama kufanyiwa upasuaji kwa ajili ya kunenepesha hips zangu,"alisema.

"Ni suala tu la kuwa mwangalifu na makini katika mwili wangu, kazi na kila kitu,"alisisitiza mwanamama huyo, ambaye pia ni mwanamuziki.

MTIBWA YAITEGA YANGA



UONGOZI wa klabu ya Mtibwa Sugar ya Morogoro umesema hauna mpango kupokea mchezaji yoyote kutoka Yanga kwa ajili ya kumsajili kwa mkopo.

Mratibu wa Mtibwa Sugar, Jamal Bayser alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, hawako tayari kufanya makubaliano ya aina hiyo na Yanga kwa sababu viongozi wake vigeugeu.

Bayser alisema wamefikia uamuzi huo kutokana na viongozi wa Yanga kuwageuka msimu uliopita kwa kumuuza kipa Shaaban Kado kwa klabu nyingine bila ridhaa yao.

"Hivi sasa tuko makini sana na Yanga. Msimu uliopita walikuja kwetu na kumtaka Said Bahanuzi, tukawapa kwa masharti kwamba watupatie Shaaban Kado kwa mkopo, lakini wakaja kumuuza bila ya kutupatia taarifa,"alisema.

Kutokana na kufanyiwa kitendo hicho, Bayser alisema hawako tayari kuingia makubaliano yoyote na viongozi wa Yanga kuhusu usajili wa wachezaji wao.

"Kuanzia msimu ujao, hatutamsajili mchezaji yoyote kutoka Yanga kwa mkopo kwa vile viongozi wake vigeugeu na tumekuwa tukishindwa kuwaelewa,"alisisitiza.

Akizungumzia usajili wa kikosi chake, Bayser alisema kazi hiyo inaendelea vizuri na imekuwa ikifanyika kwa umakini mkubwa ili kuepuka kufanya makosa.

Bayser alisema usajili wao utalenga zaidi kuziba mapengo ya wachezaji waliohama na wale, ambao kiwango chao kimeshuka.

Hadi sasa, Mtibwa Sugar imewapoteza mabeki wake wa kati, Issa Rashid, alisajiliwa na Simba na Rajab Zahir, aliyesajiliwa na Yanga.

Hata hivyo, Bayser amesema hawana taarifa yoyote kuhusu klabu za Simba na Yanga kuwasajili wachezaji hao wawili kwa vile hazijafuata taratibu za kuwahamisha.

KIFO CHA MANGWEA KIWE DIRA KUPAMBANA NA MANYANG'AU



NA STEPHEN BALIGEYA
NIMEFARIJIKA sana, nimefurahishwa sana na nimepata nguvu sana. Watanzania wamenifanya nijisikie hivyo, wamenipa ujasiri wa kugeuza mlima kuwa tambarare. Kweli nawashukuru sana.

Hali hiyo inatokana na kile nilichokiandika wiki iliyopita juu ya kifo cha Albert Mangweha. Kifo ambacho niliuliza kwa nini watu wanamlilia na kumsifu kwa maneno matamu baada ya kufa na wakati walishindwa kufanya hivyo akiwa hai?

Nikauliza tena, kwa nini baadhi ya redio zilishiriki kumuua Mangweha kisanii wakati wa uhai wake kwa kukataa kupiga nyimbo zake lakini baada ya kuaga dunia zikajifanya zilimpenda sana na kusifu uwezo wake kiusanii?

Niliuliza, kama redio hizo zingepiga nyimbo za Mangweha kama zilivyopiga wakati wa msiba wake, msanii huyo angekuwa tajiri kiasi gani kwa kupata matamasha na kuuza kazi zake ambazo zimetangazwa sana baada ya kufa?

Katikati ya dimbwi la kufikiria juu ya kifo hicho, nimepata simu nyingi na ujumbe wa maandishi kiasi cha kutisha. Kumbe Watanzania wana dukuduku lakini watasemea wapi?

Taaluma ya habari ni kazi ya jamii. Unafanya kazi kwa maslahi ya jamii pana na si kulitumikia kundi dogo, ambalo linanenepa kwa damu za walio wengi. Kazi ya taaluma hii ni kuwa msemaji na mtetezi wa jamii.

Leo napenda kutoa somo kwa wasanii, ambao kwa kuchukua kifo cha Mangweha kama darasa, wanatakiwa sasa kuamka.

Kuamka huko kuwe na mtazamo mpana miongoni mwao, kwa kutambua kwamba leo mwenzao amefariki kama ngao ya ukombozi wao. Kifo cha Mangweha kiwe kama sadaka ya ukombozi kwao.

Lazima wafikirie namna wenye mabavu watakavyowatumia baada ya kuaga dunia na namna watu hao watakavyonufaika baada ya kuwekwa kaburini.

Kifo cha Mangweha kimeonyesha usanii na unyang’au wa wenye redio, ambao walimtumia Mangweha kama njia ya kuongeza umaarufu wa vituo vyao, lakini pia kujitafutia maslahi zaidi.

Wale walioshiriki kumuua Mangweha kiusanii kiasi cha kumfanya aishi maisha magumu na ya shida, wakafikia hatua ya kusafiri hadi Afrika Kusini ili kuwapasha namna Mangweha alivyofariki.

Wakadiriki kwa mbinu za kimafia kukanusha hata taarifa ya daktari juu ya mwili wa msanii huyo kukutwa na chembe za dawa za kulevya. Kwa nini walikanusha habari za namna hiyo?

Jibu ni rahisi. Kwa sababu msanii huyo alipata msongo wa mawazo kutokana na kazi zake kutupiliwa mbali na hao, ambao wamejifanya ndugu zake.

Msongo huo wa mawazo ulimfanya msanii huyo kujifariji kwa kutumia dawa za kulevya. Lazima Watanzania watambue kwamba kama mtu anakosa mshauri wa haraka wakati anapata msongo wa mawazo, anaweza kutumia njia yoyote iwe halali au haramu kujifariji.

Mangweha alikuwa mhanga wa tatizo hilo. Akajifariji kwa kile kinachoelezwa dawa za kulevya. Marafiki wake wa karibu wanalieleza hili kwa ufasaha. Ripoti ya uchunguzi inaeleza haya kwa ufasaha.

Wale walioshiriki kumuua kwa msongo wa mawazo wakajitosa kupotosha ukweli huu kwa vile walijua fika kwamba kitendo hicho kitawatia fedheha.

Lakini kwa vile hawana soni katika nyuso zao na mioyo yao, wakajifanya wasemaji wa familia ya Mangweha. Wakawateka baadhi ya ndugu wawe wasemaji kupitia redio zao. Huku kote ni kuzidi kuonyesha uibilisi wao uliokamaa.

Tabia hii ya kishetani haikuishia hapo. Bado wakajifanya watalaamu wa kualika wasanii katika redio zao ili wawe wanaeleza uzuri wa Mangweha, lakini nadiriki kusema kwamba wamefanikiwa kidogo maana Watanzania walio wengi wamenasua usanii huo.

Kifo cha Mangweha kiwe funzo kwa wasanii, ambao wamekuwa wakitumikishwa na watu hao, ambao wanasubiri wafe ili waweze kuwasimulia na kuwaeleza kwa uzuri, ambao hawawezi kuelezwa wakiwa hai.

Wananyimwa matamasha, wananyimwa nyimbo zao kupigwa kwenye redio za manyang’au hao, lakini wanasubiri wasanii, ambao wanatumia nafasi hiyo kama ajira badala ya kuiba wafe ili waeleze uzuri wa marehemu.

Marehemu alikuwa mtu mzuri sana, marehemu alikuwa msanii wa kisasa, marehemu alikuwa na malengo makubwa, marehemu alikuwa mtu wa watu, marehemu alikuwa na singo aliyotaka kuachia na ujinga mwingine mwingi tu juu ya sifa za marehemu.

Leo wasanii wanapeleka nyimbo zao zinakaliwa kama hawatakubali masharti ya kinyonyaji. Msanii anatumiwa kwenye matamasha kwa sh. 100,000 na akidai malipo mazuri, anafungiwa duniani na kuzimu.

Matokeo yake wasanii wamekuwa vijibwa vya watu hao. Wasanii wamekuwa watumwa, wanatumikishwa kwa stahili zote, hata zile ambazo hawazitaki.

Wanavumilia upuuzi wote ambao unaua utu wao, lakini fadhila zao watazipata wakifa, pale watakaposifiwa na kunakishiwa kwa rangi zote. Huu ni ujinga ambao Watanzania wanatakiwa kuupinga.

Wasanii sasa waungane, waache kujiona kwamba kwa vile baadhi yao mambo yanawaendea vizuri, basi hawana haja ya kuungana na wenzao wanaouawa kisanii na magabachori hao.

Umoja wao utakuwa nguzo yao kuu kujikomboa, utengano wao utashuhudia sifa zao baada ya kufa, sifa ambazo zitakuwa mithili za malaika aliyeishia duniani.

Lazima wapiganie sifa hizo wapewe wangali hai, hali itakayowasaidia kuinua vipato vyao, kwa maslahi yao, familia na taifa kwa jumla.

Lazima wajiulize ni wasanii wangapi wamekufa kisanii kwa sababu ya uhuni wa watu hao, ambao bado wanaendeleza mapambano kwa wasanii wenye fikra hai?

Kama mgogoro unaofukuta leo na baadhi ya wasanii ungekuwa unahusu wasanii wadogo, kifo cha wasanii hao kingekuwa karibu lakini kazi bado imekuwa ngumu kwao.

Naandika haya si kwa maslahi ya wasanii na umma wa Watanzania kwa jumla, kwani watoto wenye vipaji wanatoka katika jamii zetu, hawana ajira na wanategemea vipaji vyao kujiajiri.

Taifa haliwezi kuendelea kwa watu wote kufanyakazi ofisini. Kazi ya sanaa itaajiri watu wengi kama kutakuwa na fursa sawa kwa vijana hao kufanya kazi zao na kunufaika na kazi zao.

Kwa msingi huo, wasanii na jamii nzima lazima kuungana kupambana na watu hawa ambao wanadhani wako juu ya sayari nyingine katika kuua vipaji vya vijana na kisha wawatumie katika vifo vyao.

Kwa maoni na ushauri, 0752646838,0713976894.

WASOMAJI WA LIWAZOZITO WALIVYOMLILIA MANGWEA


Much respect kwa makala yako. Media zimekuwa na unafiki baada ya msanii kufariki dunia. 0759928344

Uko sawa kaka, yaani wanakera sana.0774401918.

Ni ukweli usiopingika kipindi cha uhai wa Mangweha nyimbo zake hazikusikika redioni wala kwenye televisheni, ila kila siku ya kifo kuna redio zilishinda zinapiga nyimbo zake. Enzi za uhai wake hatukuweza kusikia wimbo wa Mangweha hata mara moja kwa mwaka. Ni ukweli kuwa wasanii wa Tanzania wananyonywa sana na yakitokea mambo kama haya wanaanza kumsifia ujinga, alikuwa mtu wa watu, alikuwa mpole, jamani tumuogope Mungu, uwezo uliopewa na Mungu kisiwe kigezo cha kuwakandamiza wenzako, chonde chonde. 0752752132 Katoro-Geita.

Ipo siku moja watajuta kwa dhambi waliyomfanyia mangweha. 0774629813

Pole na kazi, nakupongeza kwa kuandika makala ya kifo cha mangweha, tunamlilia mangweha baada ya kufa. Safi sana, unajua kazi.Bukoba. 0754648041.

Ebwana kaka Baligeya, mi naitwa Seif Omary, nipo UDOM mwaka wa kwanza Kiswahili Fasihi, yaani uliyoandika ni ukweli kabisa, lakini ni vyema yasiishie hapa, uendelee kuandika makala kama hizi ili kuwaamsha wasanii mazuzu wasiojitambua.0769867781.

Mambo vipi mkubwa, nimelisoma gazeti la Burudani na kusoma makala yako inayohusu kifo cha mangweha. Kiukweli hata mimi ilikuwa inaniboa kila stesheni kupiga nyimbo zake tena na kutoa wasifu wake. Kama kweli wapo karibu naye, mbona hawakutangaza anakwenda Afrika Kusini wakati alipokuwa hai. Hizi stesheni za redio ni za kinafiki. 0719522328.

Ni kweli ndugu vyombo vya habari baadhi ni wanafiki. Mungu huwa analipa hapa hapa duniani, leo kwa huyu, kesho kwao.0764157865

Bwana Stephen Baligeya, umeongea yaliyokuwa moyoni mwangu (Tunamlilia mangweha baada ya kufa). Ni kweli kabisa kwamba vipo vyombo vya habari vinavyoua masoko ya wasanii na kuwafanya waishi kwa shida. Vyombo hivyo tunavijua mpaka majina. By Mzaile Bokilo, nipo Misungiwi-Mwanza 0757283585.

Kaka nakupa pongezi kwa kutowaonea haya waliomnyonya Mangweha mpaka kabaki mifupa mitupu. Matatizo yote wamesababisha wao. Hili ni fundisho kwa wasanii wa bongo, ningependa wamuunge mkono P Funk.

Tatizo la wasanii wa Tanzania hawana kauli moja.0752805090.

Habari kaka, naitwa Paskacaly Mbasha. Kiukweli mi mwenyewe sikuamini kile kilichosemwa na vyombo vya habari kwamba Mangweha ametoweka duniani. Lakini nimekuja kuamini katika kuaga mwili wake.

Machozi yalinitoka bila mwenyewe kujielewa. Inauma sana brother. Kiukweli umimi ndio unaangamiza au unashusha maendeleo ya wasanii wetu. Kumpaisha mwenzako sidhani kama wewe unaweza ukabaki chini, tumekuwa mbele na kujionyesha tunawajali pale wanapopatwa na mauti, tunawasahau pale wanapokuwa na matatizo. Kama kukusanya michango na kuweka majukwaa inawezekana, inashindikana vipi kufanya hivyo wakiwa hai? Naungana na wewe kuwa ni wanafiki na wazandiki, kuweka majukwaa na kupigwa nyimbo zake utadhani wanasherehekea badala ya kuomboleza. Big up brother.0768839171.

Ebwana kaka unatisha. Nimependa makala yako kuhusu kifo cha Mangweha. Umesema mambo ambayo hata mimi yamenikera kabisa. Big up. Kutoka Mwanza.0769096013

Kaka makala yako imenigusa, lakini ungefanya kudokeza kidogo hizo stesheni za radio ili tuwajue waliojifanya wanampenda Mangweha wakati wa mauti kuliko kutuacha na mafumbo.0766915346.

Naomba hizo stesheni zianikwe ili nyingine ziogope. Haiwezekani msanii afe ndio apate umaarufu. Wengine leo ndio wanamjua Mangweha. Naitwa Joseph Sanga kutoka Igunga Tabora.0768603090.

Nakupongeza sana kwa kulijua hili na kupata ujasiri wa kulizungumzia. Itakuwa fundisho kwa vyombo vya habari.0714136226.

Kaka makala hii ya Mangweha umesema ukweli na mimi sina zaidi ya kuunga mkono juu ya jambo hili. Uko sahihi na kuna wasanii wangelitambua hili mpaka leo hii Mangweha angekua hai.0659380040.

Mbona kwenye makala yako unakandamiza chombo kimoja tu cha habari? Kama kweli wewe umekereka, ungetaja media zote sio kuponda sehemu moja tu. Hata sisi wananchi tuna makosa kwa sababu hatutoi support kwa wasanii wetu, hatupaswi kulaumiana.0653936885.

Salute mkuu Baligeya! Nimesoma makala yako, umewachana ndani na nje hawa wanafiki wanaochukulia msiba wa Mangweha kujipatia sifa za kijinga, hasa hawa wanaojiita masupa staa. Naamini walikuwa hata hawajui safari yake ya Afrika Kusini.0764920545.

Umeandika ambacho mimi pia kimeniuma sana, lakini nilikuwa sina pa kusemea. Nafikiri umewakilisha Watanzania wengi walio werevu wa fikra! Najua itakujengea maadui wengi sana kwa ukurasa huo mmoja tu ambao umeelimisha watu wengi kwa wakati mmoja. ‘Only God knows’. 0752809939.

Ukweli kabisa Mangweha alishasahaulika kwenye gemu la muziki wa kizazi kipya. Sasa kafariki amevuma, amekuwa gumzo kila kona bila faida kwake.0652316053.

Hilo hata mimi nakubaliana nalo maana leo hii Mangweha angekuwa tajiri sana, lakini maskini ya Mungu wako wanaokula vizuri , kulala vizuri kupitia mgongo wake. Wasanii wanatakaiwa wafikirie sana juu ya hili, angalau wamuone hata yule Mama Mangweha. I love you bro RIP Mangweha. Husna wa Arusha.0767189858.

Nashangaa hawana chembe ya aibu. Msanii akirekodi kwa P Funk inakuwa shida. Tazama Jay Mo na Mangweha wamezimwa na ndo wamebadili ngoma kali. Kwa kifo hiki, wabadilike. Kutoka Kiteto.0782501774.

Ni vibaya kumfanyia uovu mtu halafu akifa uwe mstari wa mblele kumzika. Nafsi zao zinawasuta. Watanzania tunasikia hayo na ipo siku yatafika mwisho. Haipendekezi wewe mwenyewe uwe stari wa mbele bila kushirikisha wenzio mwanzo hadi mwisho wakati nyimbo za marehemu Mangweha zinapigwa na stesheni zote na kusikika na rika lolote. Zaidi msanii ni nguzo imara kufikisha ujumbe kwa vijana wote kiurahisi. Tumepoteza askari mshauri. Wasanii wawe na chama chao chenye kuratibu mambo yao.089575789.

Nimemaliza kusoma makala yako kuhusu kifo cha msanii Mangweha bila shaka ujumbe utakuwa umewafikia wahusika. Asante.0717796037.

Hawa makupe ni wajinga na watu wasiofaa hata kidogo. Sielewi kwa nini wakati alipokuwa hai, hawakutaka kupiga nyimbo zake. Walimchukulia Mangweha kama mtu asiyekuwa na maana. Leo hii amekufa, wanampamba sifa kibao na kujiweka kimbelembele. Kinachokera zaidi ni kwamba wanajisifu kwamba walimsaidia alipokuwa hai. Nawachukia sana watu hawa kwa unyonyaji wao kwa wasanii. 0713941101.

Habari ya asubuhi! Nimesoma makala yako ya 'Tunamlilia Mangweha baada ya kufa! Kwa kweli upo sahihi kabisa. Nakutakia mafanikio mema katika kazi yako ya uandishi wa habari. Naitwa Bahati Kiula mkazi wa Mikocheni B, Dar es Salaam.

Yaani makala yako imenigusa na kuniumiza moyo wangu sana na hapa nilipo mazungumzo ni hayo ya Mangweha na hizo redio. Kama ulinikataa nilipokuwa hai, hata nikifa usinikubali. 0717353370

Habari brother. Mimi ni mtanzania, naishi Kilimanjaro. Nimeguswa sana na mada yako kuhusu kifo cha Mangweha. Ushauri wangu naomba hivyo vyombo vya habari, ambavyo vina tabia hiyo, muwaweke hadharani watanzania wote watambue kwani huo ni unyama uliokithiri. Inauma sana kuona vijana wetu wanajituma sana, lakini kuna watu wanawamaliza. Iwapo itadhihirika ni kweli, sheria ichukue mkondo wake wafungwe. 0753616171.

Mambo vipi kaka? Uko poa? Mimi mzima wa afya. Nakupongeza sana kaka kwa kuitoa nakala yako kwenye gazeti la Burudani. Baligeya wewe ni mwandishi wa habari, ambaye una mtazamo wa mbali sana. Hawa watu wanaojiona bora katika mambo ya habari ni wabaya sana.

Wanawaua wasanii na muziki huu kwa jumla. Leo Albert Mangweha anaonekana ana thamani wakati tayari amekuwa marehemu. Kipindi alipokuwa hai walikuwa hawamthamini na nyinbo zake hawazichezi. Mungu atamlipia Mangweha kwa unafiki waliomtendea. Endelea hivyo kaka, kusema maneno yaliyo ya kweli na Mungu atakuongoza na kubariki kazi za mikono yako—RIP ALBERT MANGWEHA-ailaze roho yako mahali pema peponi amina. Mangole.0714057304.

Safi sana kaka Stephen Baligeya kwa makala hii ya Mangweha. Tatizo letu watanzania linabaki palepale, unafiki. Hata wewe unawajua waziwazi wanaowaua wasanii na watakaoua wengine pia kwa kuwachanganya kiakili, lakini kama hautawataja moja kwa moja kuwa ndio chanzo cha yote haya, sote tutabaki pale pale na wao wataendelea kufanya yale yale. Atakufa mwingine na wengine mpaka Tanzania tutakapoamua kuambiana ukweli bila kupepesa.0717340184.

KIEMBA: NIMEFUNGA MJADALA



MSHAMBULIAJI Amri Kiemba amesema kwa sasa ameamua kufunga mjadala kuhusu mustakabali wake kisoka baada ya kutia saini mkataba mpya wa kuichezea Simba kwa miaka miwili.

Akizungumza mjini Dar es Salaam jana, Kiemba alisema si kweli kwamba alikuwa katika harakati za kurejea katika klabu yake ya zamani ya Yanga.

"Unajua mimi si muongeaji sana. Wakati magazeti yanaandika mimi nimesaini mkataba na Yanga, nilikuwa nashangaa sana, lakini sikutaka kujibu. Sasa ukweli ni huu, nimeingia mkataba na Simba kwa miaka miwili zaidi,"alisema.

Kiemba alisema kwa sasa anaelekeza nguvu zake katika timu ya Taifa, Taifa Stars, ambayo inajiandaa kumenyana na Ivory Coast katika mechi ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za 2014.

"Naamini mjadala wa Kiemba umekwisha salama, sasa ni zamu ya wengine,"alisema.

Kiemba alimwaga wino Simba juzi mbele ya Kaimu Makamu Mwenyekiti wa Simba, Joseph Itang'are, maarufu kwa jina la Mzee Kinesi.

Kiungo huyo alimwaga wino Simba siku moja baada ya kurejea kutoka Morocco, ambako alikwenda kuichezea Taifa Stars katika mechi dhidi ya timu ya taifa ya nchi hiyo.

Kiemba alikuwa kivutio kikubwa kwa mashabiki wa Morocco kutokana na kuifungia Taifa Stars bao la kujifariji kwa shuti kali la umbali wa mita zipatazo 25. Katika mechi hiyo, Taifa Stars ilichapwa mabao 2-1.

Baada ya mchezo huo, mashabiki wa soka wa Morocco walianza kumfuatafuata Kiemba wakiomba kupiga naye picha na walimtambua kwa urahisi kutokana na rasta zake.