KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, October 27, 2010

K-One, msanii mwenye ndoto ya kufika mbali kimuziki


WASWAHILI wana msemo usemao, ‘Avumaye baharini papa, kumbe wengi wapo’. Hivyo ndivyo ilivyojidhihirisha kwa msanii chipukizi wa muziki wa kizazi kipya, Karim Othman, maarufu kwa jina la K-One.
Japokuwa jina lake si maarufu miongoni mwa wasanii wa muziki wa kizazi kipya nchini, lakini umahiri wake wa kuimba na kutunga nyimbo zenye mashairi yenye mvuto umedhihirisha kwamba naye wamo.
K-One amedhihirisha ukali wake huo katika vibao vyake kadhaa, vikiwemo ‘Bila wewe’, ‘Sema baby’ , alivyowashirikisha wasanii nyota kama vile Ney wa Mitego na Pasha. Vibao hivyo viwili vimekuwa vikipigwa mara kwa mara kwenye vituo vya radio vya Times FM na Radio Uhuru.
Msanii huyo chipukizi amerekodi vibao hivyo katika studio za Brain Trust, zilizopo Temeke, Dar es Salaam kwa udhamini wa dada yake, ambaye hakupenda kumtaja jina.
Kwa mujibu wa K-One, amekuwa akipata sapoti kubwa ya kiusanii kutoka kwa familia yake, wakiwemo dada zake, ambao ndio wadhamini wake wakuu.
“Sio siri, naishukuru sana familia yangu, hasa bi mkubwa wangu (mama yangu) na dada zangu kwani wamekuwa wakinipa sapoti kubwa kiusanii. Japokuwa bado sijatoka kama ilivyo kwa wasanii wengine, lakini wamekuwa wakinipa moyo,”alisema msanii huyo.
Mbali na kurekodi vibao vyake, K-One pia amekuwa akishirikishwa kuimba viitikio katika nyimbo za wasanii mbalimbali maarufu wa muziki hao. Baadhi ya wasanii hao ni JB wa kundi la Mabaga Fresh na Mood Kibra.
Hivi sasa, K-One yupo katika hatua za mwisho za kukamilisha kibao chake kipya kinachokwenda kwa jina la ‘Valentine’. Amerekodi kibao hicho katika studio za Baucha Records.
Vibao vingine vilivyorekodiwa na msanii huyo, anayependa kutengeneza nywele zake kwa mtindo wa rasta ni ‘Kwa nini’, ‘Mpenzi sasa why’ na ‘Fau’. Amerekodi vibao hivyo kwenye studio za Brain Trust.
“Lengo langu ni kuwa na albamu moja ya nyimbo zangu zote. Naamini baada ya muda si mrefu, nitakuwa nimekamilisha albamu yenye nyimbo nane,”alisema msanii huyo.
Aliongeza kuwa, hadi sasa amekuwa akirekodi nyimbo zake kwa kutegemea msaada wa fedha kutoka kwa dada zake kwa vile bado hajapata wadhamini.
Ametoa mwito kwa wakuzaji wa vipaji vya wasanii nchini, kujitokeza kumsaidia kurekodi albamu yake na kusisitiza kuwa, hawatajutia uamuzi wao huo ama kupoteza fedha zao.
“Kipaji cha muziki ninacho na nimedhihirisha ukweli huo kupitia nyimbo zangu zilizofanikiwa kuzirekodi hadi sasa. Lakini ningependa kufika mbali zaidi, hivyo nawaomba mapromota wa muziki wa kizazi kipya wajitokeze kunidhamini,”alisema.
K-One alisema, muziki kwa sasa hapa nchini ni biashara na iwapo msanii atajiamini na kufanyakazi zake kwa umakini, ni rahisi kufaidi matunda ya jasho lake.
Kwa mujibu wa K-One, amepanga kukamilisha kazi ya kurekodi albamu yake kabla ya mwisho huu wa mwaka kumalizika. Alisema mambo yakienda vizuri, albamu yake hiyo itakuwa sokoni mwishoni mwa mwaka huu.
Je, ni kwa nini K-Onea aliamua kujitosa kwenye fani ya muziki wa kizazi kipya?
“Tangu nikiwa mdogo, nilipenda sana kushiriki katika maigizo na shughuli zozote zilizohusu mambo ya muziki. Ndipo nilipojigundua kwamba ninacho kipaji cha muziki kwani tangu nikiwa shule, niliweza kutunga mashairi ya wimbo,”alisema.
Kwa mujibu wa K-One, katika familia yake, hakuna ndugu yoyote aliyewahi kujihusisha na muziki huo. Ni yeye pekee, aliyejitosa kwenye fani hiyo baada ya kubaini kuwa, ana uwezo nayo.
“Lengo langu ni kuwaonyesha watanzania kwamba nina kipaji cha muziki. Pia nataka niutumie muziki kama ajira yangu kwa sababu ni biashara inayolipa,”alisema.
K-One ametoa wito kwa wasanii wa muziki wa kizazi kipya nchini, wapendane, kusaidiana na kuaminiana ili waweze kupiga hatua za juu zaidi kimaendeleo.
Alisema miongoni mwa sababu zinazochangia kuwakwamisha wasanii chipukizi wa muziki huo, ni kutokuwepo kwa umoja miongoni mwao, kuchukiana na kutosaidiana.
“Wasanii walio juu wanapaswa kukumbuka kuwa, kabla ya kufika huko waliko hivi sasa, nao walianzia chini, hivyo wasikwepe kuwasaidia wenzao wanaohitaji msaada kutoka kwao, hata kama wa kurekodi pamoja,”alisema.





No comments:

Post a Comment