KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 14, 2010

Vibopa Yanga watenga mil 40 kuiua Simba




WAKATI homa ya pambano la watani wa jadi wa soka nchini ikizidi kupamba moto, baadhi ya wafanyabiashara matajiri wa klabu ya Yanga wametenga sh. milioni 40 kwa ajili ya kuiua Simba.
Habari kutoka ndani ya Yanga zimeeleza kuwa, fedha hizo zitatolewa kwa wachezaji wa timu hiyo iwapo watashinda Simba katika mchezo wa ligi kuu ya Tanzania Bara kati yao utakaochezwa keshokutwa.
Mechi hiyo inayosubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa soka nchini, inatarajiwa kupigwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza, Simba wakiwa wenyeji.
Kwa mujibu wa habari hizo, wafanyabiashara hao walikutana na viongozi wa klabu hiyo pamoja na wachezaji wa Yanga Jumatatu iliyopita kwenye hoteli ya Kiromo Resort iliyopo Bagamoyo mkoani Pwani.
Katika mkutano huo, viongozi pamoja na wafanyabiashara hao, waliwaeleza wachezaji umuhimu wa kushinda mechi hiyo na pia kuwapatia kitita hicho cha fedha iwapo watawabwaga watani wao.
Ujumbe wa wafanyabiashara hao wenye mapenzi na Yanga, uliongozwa na Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Davis Mosha na mwanachama, aliyejulikana kwa jina la Majid Seif.
Kufuatia ahadi hiyo, wachezaji wa Yanga waliwahakikishia viongozi na wafanyabiashara hao kuwa, watapigana kufa au kupona uwanjani ili kuhakikisha wanashinda mechi hiyo na kupata pointi zote tatu.
Hata hivyo, hadi jana haikuweza kufahamika iwapo mfadhili mkuu wa klabu hiyo, Yusuf Manji atatoa zawadi yoyote ya pesa kwa wachezaji iwapo watashinda mechi hiyo.
Lakini habari za uhakika kutoka kwa mmoja wa viongozi wa klabu hiyo zimeeleza kuwa, Manji huenda akaenda Mwanza keshokutwa asubuhi kwa ajili ya kushuhudia mechi hiyo.
Kikosi cha Yanga kinatarajiwa kutua Mwanza kati ya kesho na keshokutwa asubuhi kwa ajili ya mechi hiyo, kikiwa chini ya ulinzi mkali wa wanachama wanaojulikana kwa jina la ‘makomandoo’.
Yanga imeweka kambi Bagamoyo kwa ajili ya kujiandaa na mechi hiyo na imekuwa ikifanya mazoezi asubuhi na jioni kwenye uwanja wa Mbegani.
Ofisa Habari wa klabu hiyo, Louis Sendeu alisema jana kuwa, kikosi chao chote kipo fiti na hakuna mchezaji majeruhi. Alitamba kuwa, ushindi katika mechi hiyo ni muhimu na wa lazima kwao.
Kufuatia wachezaji wote kuwa fiti, Sendeu alisema Kocha Mkuu wa timu hiyo, Kostadin Papic ameshindwa kikosi kipi kianze katika mechi hiyo kwa vile kila mchezaji ana uchu wa kucheza.
Sendeu alisema mashabiki kadhaa wa timu hiyo wanatarajiwa kuondoka Dar es Salaam kwa mabasi kati ya leo na kesho kwenda Mwanza kwa ajili ya kushuhudia pambano hilo.
Pambano hilo litakuwa la pili kuzikutanisha Simba na Yanga katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita. Zilipokutana Agosti mwaka huu katika mechi ya kuwania Ngao ya Hisani, Yanga iliichapa Simba kwa penalti 3-1.

No comments:

Post a Comment