KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 21, 2010

ROONEY: Bye bye Man Utd


LONDON, England
HATIMAYE Kocha Mkuu wa Manchester United, Sir Alex Ferguson amefichua kuwa, mshambuliaji Wayne Rooney anataka kuondoka katika klabu hiyo.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa juzi, Ferguson alikiri kuwa alipatwa na mshtuko na kukatishwa tamaa kusikia habari hizo, lakini alikanusha kuwepo na hali ya kutokuelewana kati yake na mchezaji huyo.
“Tumechanganyikiwa kama inavyoweza kutokea kwa yeyote, lakini hatuwezi kuelewa kwa nini anataka kuondoka,”alisema kocha huyo raia wa Scotland. Hata hivyo, Ferguson alisema milango ipo wazi kwa Rooney iwapo atabadili uamuzi wake huo. Rooney alishindwa kuichezea Manchester United jana katika mechi ya ligi ya mabingwa wa Ulaya dhidi ya Bursaspor kutokana na kuwa majeruhi.
Hatima ya Rooney kuendelea kuwepo Manchester United ilikuwa shakani, kufuatia kuwepo na habari kwamba aligoma kutia saini mkataba mpya wa kuichezea klabu hiyo. Mkataba wa sasa wa Rooney unatarajiwa kumalizika mwishoni mwa msimu wa 2011/12.
Akihojiwa na kituo cha televisheni cha MUTV kabla ya kuzungumza na waandishi wa habari juzi, Ferguson alisema Mtendaji Mkuu wa klabu hiyo, David Gill alimweleza kuhusu uamuzi huo wa Rooney kutosaini mkataba mpya.
“Nilikuwa ofisini Agosti 14 na David alinipigia simu kunieleza kwamba Rooney hatasaini mkataba mwingine,”alisema Ferguson.
“Miezi michache iliyopita alisema yupo kwenye klabu kubwa dunia na anataka kubaki hapa maisha yake yote. Hatuelewi nini kimebadili msimamo wa kijana huyu,”aliongeza.
Mara baada ya kupata taarifa hizo, Ferguson alisema aliomba kuzungumza na mchezaji huyo, ambaye alimuhakikishia kuhusu uamuzi wake huo.
Ferguson alisema amesikitishwa na uamuzi huo wa Rooney kwa sababu alifanya kila analoweza kumsaidia tangu alipojiunga na klabu hiyo mwaka 2004 akitokea Everton.
“Hatuna tulichokifanya zaidi ya kumsaidia tangu alipowasili katika klabu hii,”alisema Ferguson, ambaye bado hajakata tamaa ya kumzuia mchezaji huyo asiondoke.
Wakati huo huo, Rooney amewadokeza wachezaji wenzake wa Manchester United kuwa, huenda akafikiria kujiunga na mahasimu wao, Manchester City.
Rooney alielezea msimamo wake huo siku chache baada ya kuieleza Manchester United kwamba, hatarajii kuongeza mkataba mpya na klabu hiyo.
Tayari Manchester City imeshaonyesha dhamira ya kumsajili mchezaji huyo wakati wa usajili wa dirisha dogo Januari mwakani na ipo tayari kumlipa mshahara wa pauni 230,000 (sh. milioni 529) kwa wiki.
Iwapo Manchester City itafanikiwa kumsajili Rooney, atakuwa ndiye mchezaji ghali kuliko wote wanaocheza katika ligi kuu ya England hivi sasa.
Baadhi ya wachezaji wa Manchester United wamelieleza gazeti la Daily Mail kuwa, uamuzi wa Rooney kuondoka klabu hiyo unatokana na masuala ya pesa na si kutokuelewana kwake na Kocha Sir Alex Ferguson.
Mke wa mwanasoka huyo, Coleen ameshamweleza wazi mumewe kuwa, hawezi kwenda nje ya England, hasa katika kipindi hiki, ambacho dada yake, Rosie ni mgonjwa.
Msimamo huo wa Coleen umemfanya Rooney akubali kubaki England na kujiunga na moja kati ya klabu za Manchester City na Chelsea, ambazo ndizo pekee zenye uwezo wa kumlipa mshahara mnono na kumudu ada ya uhamisho.
Rooney amewaeleza wazi wachezaji wenzake kuwa, hatafikiria mara mbili kujiunga na Manchester City iwapo klabu hiyo itawasilisha maombi ya kumsajili kabla ya Januari mwakani.
Kwa mujibu wa sheria za Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA), Rooney anaruhusiwa kulipa pauni milioni tano kwa ajili ya kuvunja mkataba wake, iwapo utakuwa umesalia mwaka mmoja kabla ya kumalizika.
Kipengele hicho ndicho kilichozua hofu kwa viongozi wa Manchester United, ambao wana wasiwasi kuwa, wasipomuuza Januari mwakani, huenda akavunja mkataba wake ama kuhama bila kulipiwa ada.
Kocha Mkuu wa Chelsea, Carlo Ancelotti alisema juzi kuwa, atafikiria kumsajili mshambuliaji huyo wakati Kocha Mkuu wa Manchester City, Roberto Mancini bado anafuatilia hatma ya mchezaji huyo katika klabu ya Manchester United.
“Kwa sasa, Chelsea haitarajii kumsajili Rooney kwa sababu bado ni mchezaji wa Manchester United na nafikiri bado wanaweza kumaliza tatizo lililojitokeza,”alisema Ancelotti.
“Kama Rooney atawekwa sokoni, si Chelsea pekee itakayotaka kumsajili, bali na klabu zingine kubwa duniani,”aliongeza.
Klabu nyingine iliyoonyesha nia ya kumsajili mshambuliaji huyo wa kimataifa wa England ni Real Madrid ya Hispania. Lakini kocha wake, Jose Mourinho alikuwa mwangalifu kuzungumzia suala hilo kwa hofu ya kumchefua Ferguson.
“Sifikirii iwapo atahama. Nafikiri kocha wake atamshawishi abaki,”aliongeza.
Mkurugenzi wa Real Madrid, Jorge Valdano alifichua juzi kuwa, anavutiwa na mchezaji huyo, lakini hana nafasi kwenye kikosi cha kwanza cha timu hiyo.
Real Madrid imekuwa ikihusishwa na mipango ya kumsajili Rooney tangu msimu uliopita, ambapo rais wake wa zamani, Ramon Calderano alidai mapema mwaka huu kuwa, mrithi wake, Florentino Perez naye anavutiwa na mchezaji huyo.
Valdano alilieleza gazeti la Telemadrid: "Navutiwa sana na Rooney, lakini swali la kujiuliza ni je, kama Rooney atakuja, nani tutamwondoa kwenye timu. Tunao wachezaji wazuri wa safu ya ushambuliaji, akina Ronaldo, Higuain, Ozil na Di Maria.”
Rais huyo wa zamani wa Real Madrid alisema pia kuwa, klabu hiyo ina hazina ya wachezaji wengi chipukizi, ambao wataifanya isiwe na tatizo la kusajili wachezaji nyota kutoka nje kwa kipindi cha miaka kumi ijayo.
Taarifa za Rooney kutaka kufuata nyayo za Carlos Tevez, aliyejiunga na Manchester City msimu uliopita akitokea Manchester United, huenda zikawashtua mashabiki wa klabu hiyo.
Uhusiano wa Rooney na Kocha Ferguson umekuwa mbovu tangu mchezaji huyo alipokumbwa na kashfa ya kufanya mapenzi na changudoa.
Kocha Ferguson amekuwa akimweka benchi Rooney katika mechi kadhaa za ligi kuu ya England huku akitoa taarifa kwamba, mchezaji huyo ni majeruhi.
Hata hivyo, Rooney amezikana taarifa hizo za Ferguson na kusisitiza kuwa, yupo fiti na hajawahi kuumia tangu msimu huu ulipoanza.
Tayari Manchester United imeshaeleza wazi kuwa, haina mpango wa kumuuza Rooney wakati wa dirisha dogo na imeziita taarifa hizo kuwa ni za uzushi.
Katika hatua nyingine, kiungo wa zamani wa Manchester United, Roy Keane amemwonya Rooney awe makini katika kufikia uamuzi wa kuihama klabu hiyo.
Keane alisema juzi kuwa, kutokuelewana kwa Rooney na Ferguson hakupaswi kuwa kigezo cha yeye kuhama kwa vile wachezaji na makocha kukorofishana mara kwa mara ni jambo la kawaida katika maisha ya soka.

No comments:

Post a Comment