KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, October 21, 2010

Genevieve aanza vibaya Miss World


SANYA, China
MREMBO wa Tanzania, Genevieve Emmanuel ameanza vibaya mashindano ya mwaka huu ya kuwania taji la dunia baada ya kutolewa mapema katika kinyang’anyiro cha vazi la ufukweni.
Genevieve hakuwa miongoni mwa warembo 40 waliovuka mchujo wa awali wa kuwania taji hilo. Alikuwa miongoni mwa warembo 79 waliotolewa mapema.
Taji hilo lilinyakuliwa na mrembo Yara Santiago kutoka Puerto Rico, ambaye sasa ataingia moja kwa moja katika hatua ya nusu fainali ya shindano hilo.
Katika shindano hilo lililofanyika juzi kwenye ufukwe wa mji wa Sanya, mrembo Alexandria Mills kutoka Marekani alishika nafasi ya pili akifuatiwa na Mariann Bincedal kutoka Norway.
Warembo 40 waliofuzu kuingia hatua ya nusu fainali ya shindani hilo walitoka katika nchi za Argentina, Australia, Bahamas, Barbados, Botswana, Bolivia, Bosnia & Herzegovina, Cape Verde, Cayman Islands, China PR, Jamhuri ya Czech, Ufaransa, French Polynesia, Ghana, Guadeloupe na Hong Kong China.
Wengine ni kutoka nchi za Hungary, India, Israel, Italia, Lithuania, Luxembourg, Martinique, Moldova, Mongolia, Uholanzi, New Zealand, Norway, Paraguay, Puerto Rico, Russia, St Lucia, Scotland, Sri Lanka, Thailand, Trinidad & Tobago, Uturuki, Ukraine, Marekani na Zimbabwe.
Kwa mujibu wa taratibu za shindano hilo, katika hatua za awali, washiriki huchuana katika kuwania taji la vazi la ufukweni, vipaji vya michezo na mrembo anayependeza kwenye picha (miss photogenic).
Fainali ya mashindano ya mwaka huu imepangwa kufanyika Oktoba 30, ambapo washiriki kutoka nchi 119 wanatarajiwa kupanda jukwaani kuwania taji hilo.
Katika mashindano hayo, bara la Afrika litawakilishwa na warembo kutoka nchi 18. Nchi hizo ni Angola, Botswana, Ivory Coast, Misri, Ethiopia, Ghana, Kenya, Lesotho na Malawi.
Zingine ni Mauritius, Namibia, Nigeria, Sierra Leone, Afrika Kusini, Uganda, Zambia, Zimbabwe na Tanzania.
Pamoja na kushindwa kufanya vizuri katika shindano la vazi la ufukweni, mrembo Emma Wareus kutoka Botswana ametajwa kuwa ni miongoni mwa wanaopewa nafasi kubwa ya kutwaa taji la dunia mwaka huu.
Shirika la Habari la OLBG limemwelezea Emma kuwa, ni mrembo mwenye sifa na vigezo vyote vinavyostahili kumfanya ashinde taji hilo, akifuatiwa na Kamilla Salgado kutoka Brazil na Laura Restrepo kutoka Colombia.
Emma amekuwa kivutio kikubwa tangu washiriki walipowasili mjini Sanya kutokana na uzuri wake wa sura na umbo na pia mambo mbalimbali, ambayo amekuwa akiyafanya.
Shirika hilo liliwataja warembo wengine wa Afrika wanaopewa nafasi ya kufanya vizuri kuwa ni Samantha Tshuma kutoka Zimbabwe, Ivaniltan Jones kutoka Angola na Zindaba Hanzala kutoka Zambia.

No comments:

Post a Comment